Jumatatu, 17 Oktoba 2022

Jinsi ya kukabiliana na mambo ya kutisha


1Samuel 17:4-11 Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. Na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana.”


Utangulizi:

Goliath ni moja ya watu wanaotajwa katika Biblia katika kitabu cha Samuel akielezewa kama jitu kubwa sana ambalo lilipigwa na kijana mdogo sana aitwaye Daudi, kwa silaha dhaifu sana, Kuja kwa Daudi ni matokeo ya Sauli pamoja na majeshi yake yote kufadhaika na kuogopa sana kupigana na askari huyo komandoo wa kikosi cha wafilisti, Leo hii stori ya Daudi na Goliath imekuwa ni moja ya mfano unaotumiwa sana katika kutia moyo watu wa kila aina kuondoa hofu na kukabiliana na tukio lolote gumu au linaloonekana lenye kutisha hata kama inaonekana kibinadamu kuwa tunakabiliana na kitu kigumu lakini tukiwa tuna Mungu aliye hai ndani yetu!

1Samuel 17:45 “Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.”

Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-

·         Mambo ya kutisha

·         Jinsi ya kukabiliana na mambo ya kutisha!

·         Siri ya kukabiliana na mambo ya kutisha.

Mambo ya kutisha.

Tunapozungumzia mambo ya kutisha katika nyakati za leo, tunaweza kuzungumzia hali yoyote ngumu na ambayo kwa akili za kibinadamu ni ngumu kuikabili katika hali ya kawaida, hali hizo zote ngumu leo, au zenye kutisha na kuogopesha zinaweza kufananishwa na ukubwa aliokuwa nao adui wa Israel yaani Goliath, Kwa mujibu wa maelezo ya Biblia tunaambiwa kuwa Goliath alikuwa na urefu wa mikono sita na shubiri moja kwa vipimo vya leo ni kama Goliath alikuwa na urefu wa futi tisa na nusu, wakati watu wengine wanakisiwa kuwa na futi kama tano na inchi tatu au sita kwa wale wenye sifa ya urefu Gioliath alikuwa ni mrefu sana kwenda juu kuliko wanadamu wa kawaida hivyo lilikuwa jitu kwelikweli, lakini pia tunaambiwa alikuwa na Kofia ya kivita Chepeo ya shaba yenye uzito wa Paundi 66, kumbuka Paundi moja ni sawa na kilo 0.454 hivyo Paundi 66 ni sawa na Kilo 29 au 30, Pia jamaa alikuwa na koti la kivita dirii ya shaba yenye uzito wa Shekel 5000 sawa na Paundi 175 ambayo ni sawa na kilo 79 au 80 hivi, hali kadhalika mkuki wake kile kicha tu pekee kilikuwa na uzito wa Paundi 20 yaani sawa na kilo 9-10 na kumbuka huo ulikuwa ni kishwa tu cha mkuki wake, kwa kifupi tu Goliathi lilikuwa ni jitu la kutisha kimsingi Goliath alikuwa ni kama mashine ya kifo ambaye kwa kumuona tu huwezi kurusha mguu wako vitani, lakini kwa cv uzoefu wake huyu alikuwa mzoefu wa vita tangu utoto wake

1Samuel 17:33 “Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake.”

 Unaweza kuona na licha ya kuwa na uzoefu wa vita Goliath alikuwa anajiamini na alikuwa na maneno ya hivyo na ya jeuri na kila aliyemsikia na kumuona aliyeyuka moyo! Haya ni mambo ya kutisha, Yawezekana katika maisha yetu tukawa tunakutana na mambo magumu ambayo kwa akili ya kibinadamu hayawezi kukabilika wala hayaonyeshi upenyo, hayo ni mambo ya kutisha na hatupaswi kuogopa kwani neno la Mungu linatupa matumaini kuwa iko njia ya kushinda!. Tunapomuangalia Daudi tunaweza kugundua kuwa yako mambo Muhimu yaliyopelekea akubali kupambana na lijitu na akaweza kufanikiwa!

Jinsi ya kukabiliana na mambo ya kutisha!

1.       Alifikiri juu ya kulinda Heshima yake.

 

Daudi alifikiri juu ya kulinda heshima yake na na ya Mungu wake, Mfalme alikuwa ameahidi kuwa mtu atakayetoka na kumpiga mfilisti huyu kwanza angefanywa kuwa tajiri sana, pili angeinuliwa kwa kuingia katika familia ya kifalme na kuketi katika meza kuu pamoja na mfalme kwa kuozwa binti wa kifalme jambo ambalo linempa haki hiyo na zaidi ya hayo Familia yake ingekuwa huru katika maswala ya kulipa Kodi. Unaweza kuona

 

1Samuel 17:25-27Watu wa Israeli wakasema, Je! Mmemwona mtu huyu aliyepanda huko? Hakika ametokea ili awatukane Israeli; basi, itakuwa, mtu yule atakayemwua, mfalme atamtajirisha kwa utajiri mwingi, naye atamwoza binti yake, na kuifanya mbari ya baba yake kuwa huru katika Israeli., Daudi akaongea na watu waliosimama karibu, akisema, Je! Atafanyiwaje yeye atakayemwua Mfilisti huyo, na kuwaondolea Israeli aibu hii? Maana Mfilisti huyu asiyetahiriwa ni nani hata awatukane majeshi ya Mungu aliye hai? Nao watu wakamjibu vivyo hivyo, wakisema, Ndivyo atakavyofanyiwa mtu yule atakayemwua.”

 

Katika kila niia ya mafanikio kwa kawaida kuna jambo gumu linalosimama ambalo ni lazima upambane kuliangusha ndipo uweze kutoboa, Israel wasingeliweza kuingia katika inchi ya mkanaani nchi ya maziwa na asali bila kuwapiga wakazi wake, wakati wote njia ya mafanikio yako haiwezi kuwa nyepesi, lakini kumbuka kuna utajiri kuna heshima kuna uhuru ambao utapatikana kama tu jitu litaanguka, hivyo ni lazima ujipe moyo na ukubali kukabiliana na giant nani ajuaye ya kuwa wewe ndie utakayeikomboa Familia yako na taifa lako pigana kwaajili ya kuweka heshima, haiwezekani ukubali kupuuzwa pigana na kila kinachosimama mbele yako na Mungu atakuwa pamoja nawe!

 

2.       Alifikiri juu ya kulinda Heshima ya Mungu.

 

Israel lilikuwa ni taifa ambalo Mungu amewachagua ili waweze kuwa Baraka kwa mataifa yote, kushindwa kwa Israel ilikuwa ni sawa na kushindwa kwa Mungu wao na Mungu wa baba zao, Mungu wa Ibrahimu na Isaka na Yakobo angetukanwa, Mtu huyu anayetisha lisha ya kuwatukana waisrael lakini pia alimtukana Mungu aliye hai, wakati mwingine kushindwa kwetu, kuanguka kwetu, umasikini wetu na kushindwa kwetu kufanikiwa kunafanya ionekane kuwa Mungu wetu ameshindwa na jina lake kutukanwa Hivyo Daudi alikuwa akipigana kwaajili ya utukufu wa Mungu pia

 

1Samuel 17: 45-47 “Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya Bwana, naye atawatia ninyi mikononi mwetu.”

 

Kwaajili ya jina la Mungu wetu, ili kuitunza heshima yake hatuna budi kumuomba Mungu atukuzwe hata kupitia changamoto zinazotukabili, ijulikane ya kuwa changamoto unayoipitia hata kama inatisha kiasi gani ikishughulikiwa jina la Mungu wetu litatukuzwa na kuinuliwa Daudi aliona hana budi kushinda kwaajili ya jina la Mungu ili wafilisti waelewe kuwa Israel hata kama haina silaha wala nguvu inashinda kwa jina la Mungu aliye hai.

 

3.       Alifikiri juu ya kupoteza uhuru na kuwa watumwa.

 

Hakuna kitu kinauma duniani kama kuwa mtumwa au kupoteza Uhuru, wazee wetu waliopigania uhuru, walikataa kila aina ya ugandamizaji  na uonevu na ndio maana walidai uhuru kwa nguvu zao zote, sababu kubwa ilikuwa ni kukataa uonevu na kudhalilishwa, wapigania uhuru wote walikuwa na roho inayofanana, Jomo Kenyatta, Julius Nyerere, Patrice Lumumba, Kwame Nkuruma, Haile Selasie, Robert Mugabe, Keneth Kaunda, Abeid Karume, Samora Machel, Nelson Mandela, Oliva Tambo, Na mwimbaji Bob Marley walikataa dhana ya utumwa na kuwa na roho moja yenye kuitaka Afrika iweze kuwa huru kujitawala na kujiamulia mambo yake  na ndio maana Mungu aliwaamsha nia na mioyo yao  ili wawe na uchungu na kuwatetea ndugu zao, Mungu aliamsha hari ya Daudi na kukubali kuwa Mwamuzi na mwokozi wa ndugu zake kwa sababu hakutakamkukubali wawe watumwa wa wafilisti, masharti ya vita hii ilikuwa kama Goliath akimshinda yule ambaye Israel wangemtoa wangekuwa watumwa wa wafilisti na kama yule ambaye wangemtoa angemshinda basi wafilsiti wangekuwa watumwa wa Israel ona

 

1Samuel 17:8 -9 “Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia.”

Siri ya kukabiliana na mambo ya kutisha.

-          Usikimbie vita na mambo ya kutisha – hakikisha kuwa unakabiliana na jitu lako lenye kutisha litokee kabiliaba nalo, jifunze kukabiliana na mambo ya kutisha na wakati mwingine sio lazima yakukabili bali unaweza hata kuyafuata 1Samuel 17:34-35 “Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua.” Uko wakati ambako lazima umfuatilie adui na uambane naye kule aliko anaweza kukuvamia na kuchukua kila kilicho chako, kuna wakati katika maisha unaweza kudhulumiwa, adui akachukua kila kilicho chako, akachukua kipato chako, nyumba yako, familia yako, muda wako na hata afya yako, lazima uwe mkali usikubali kudhalilika pambana bila kujali ukubwa wa tatizo pambana kwa jina la Bwana wa majeshi, hakuha kukimbia wengine wakikimbia we baki pambana mpaka senti ya mwisho! 1Samuel 17:24 “Na watu wote wa Israeli walipomwona yule mtu wakakimbia, wakaogopa sana.” Huwezi kuwa kiongozi wa Bendi asiyependa Muziki.

 

-          Usiogope – Hata kama adui yako anaoneana mwenye kutisha kiasi gani haupaswi kuogopa neno usiogope katika Biblia limeandikwa mara 366 sawa na siku zote za mwaka mzima hii maana yake hatupaswi kuogopa, kuwaogopa na badala yake ujae imani umtegemee Mungu tu jua ya kuwa Mungu yuko nawe na atakusaidia 2Wafalme 1:15 “Malaika wa Bwana akamwambia Eliya, Shuka pamoja naye; usimwogope. Akaondoka, akashuka pamoja naye hata kwa mfalme.” Kuna wakati maandiko yanatuambia USIMUOGOPE hii kama inahusu mtu na pia inatuambia USIWAOGOPE kama  ni kundi kubwa

 

-          Kumbukumbu 20:1 “Utokapo kwenda vitani kupigana na adui zako, na kuona farasi, na magari, na watu wengi kuliko wewe, usiwaogope; kwa kuwa Bwana Mungu wako, yu pamoja nawe, aliyekukweza kutoka nchi ya Misri.”

 

-          Maandiko hayatutaki tuwe na hofu kwa sababu vitani tutaonekana kuwa ni sisi tunaopigana lakini ndani ya mioyo yetu anayepigana ni Bwana mwenyewe vita sio yako ni vita ya Mungu tunayemuamini na kumtumikia ona

 

2Nyakati 20:15 “akasema, Sikieni, Yuda wote, nanyi mkaao Yerusalemu, na wewe mfalme Yehoshafati; Bwana awaambia hivi, Msiogope, wala msifadhaike kwa ajili ya jeshi kubwa hili; kwani vita si yenu bali ni ya Mungu.”

Hitimisho:-

Silaha zetu zina nguvu kubwa ya ajabu sana na hatupaswi kuogopa tunajifunza kutoka kwa Daudi ya kuwa hata iweje au adui aweje Mungu atatupa ushindi mkubwa sana, vita ni yake wala si yetu inawezekana unayakumbuka mamo haya yote lakini wakati mwingine tunapaswa kukumbushwa ili kibinadamu tusiogope, usiogope wakati vita vinakukabili kwa sababu zozote zile.Silaha alizochagua Daudi zilionakana kwa machio ya kibinadamu kuwa duni kwa kulinganisha na jitu alilokuwa anapigana nalo lakini Mungu alimpa ushindi

1Samuel 17: 49 “Daudi akatia mkono wake mfukoni, akatwaa humo jiwe moja, akalitupa kwa kombeo lake, akampiga Mfilisti katika kipaji cha uso; jiwe hilo likamwingilia kipajini, akaanguka chini kifudifudi.” Daudi alishinda kwa kutumia jiwe moja tu kati yam awe matano aliyokuwa nayo, silaha za vita vyetu zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome ona

2Wakoritho 10: 3-5 “Maana ingawa tunaenenda katika mwili, hatufanyi vita kwa jinsi ya mwili; (maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome;) tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo;”    

Na Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!



Hakuna maoni: