Jumatatu, 3 Oktoba 2022

Haki yako ya Mzaliwa wa Kwanza!

Waebrania 12:16-17 “Asiwepo mwasherati wala asiyemcha Mungu, kama Esau, aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya chakula kimoja. Maana mwajua ya kuwa hata alipotaka baadaye kuirithi baraka, alikataliwa (maana hakuona nafasi ya kutubu), ijapokuwa aliitafuta sana kwa machozi.”



Utangulizi

Haki ya Mzaliwa ni haki ya kimila, kitamaduni na kiroho anayoipata mtu kutokana na kuzaliwa au mfululizo wa kuzaliwa kwake, Haki hizi zinaweza kumpa mtu, kwa mfano uraia kutokana na mahali ulipozaliwa au walipozaliwa wazazi wake, au kupokea sehemu ya mali na heshima kutoka katika familia yake kufuatana na mpangilio wa kuzaliwa kwake. Haki hii inaweza pia kumpatia mtu urithi wa kifalme kama anatokea katika familia za kifalme!

Katika maandiko Haki ya mzaliwa ilihusiana moja kwa moja na kijana wa kiume aliyezaliwa kwanza katika familia kuwa na haki ya kurithi mali au heshima na mamlaka ya baba yake mara mbili zaidi kuliko watoto wengine, Katika Israel, Kwa mfano kila mtoto alipokea sehemu fulani ya urithi wa mali za baba yake lakini mtoto wa kwanza alipokea mara mbili zaidi kuliko wengine pamoja na uongozi wa Familia.

Mwanzo 48:21-22 “Israeli akamwambia Yusufu, Angalia, mimi ninakufa, lakini Mungu atakuwa pamoja nanyi, naye atawarudisha mpaka nchi ya baba zenu. Nami nimekupa wewe sehemu moja zaidi kuliko ndugu zako, niliyoitwaa katika mikono ya Waamori, kwa upanga wangu na upinde wangu.”

Haki ya kuzaliwa kwanza kwa kawaida ilipaswa kuwa ya Mzaliwa wa kwanza hata kama umezaa na mwanamke usiyempenda, mtoto wa kwanza alihesabika kama mwanzo wa nguvu zako yeye ni Malimbuko ya uzao wako  kwa hivyo maandiko yaliagiza kutazamwa kwa jicho la tofauti kwa mzaliwa wa kwanza katika familia ona  

Kumbukumbu la Torati 21:15-17 “Akiwa mtu yuna wake wawili, mmoja ampenda, mmoja hampendi, nao wamemzalia watoto, ampendaye na asiyempenda wote wawili; na yule mzaliwa wa kwanza akiwa ni wa mke asiyependwa; ndipo itakapokuwa ya kwamba siku atakayowarithisha wanawe alivyo navyo, asimweke mwana wa ampendaye kuwa mzaliwa wa kwanza mbele ya mwana wa asiyempenda, naye ndiye mzaliwa wa kwanza huyu; lakini amkubali mzaliwa wa kwanza mwana wa yule asiyempenda, kwa kumpa mafungu mawili katika vyote alivyo navyo; kwa maana ndiye mwanzo wa nguvu zake; haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake yeye.”

Neno Mzaliwa wa kwanza katika Lugha ya kiyunani ilihusiana zaidi na mfululizo wa kimamlaka kutoka juu kwenda chini mfululizo huu unaitwa itifaki, neno la kiyunani linalotumika kuelezea kuhusu mzaliwa wa kwanza ni “PROTOTOKOS”ambalo maana yake ni wa kwanza katika cheo, kwa hiyo mamlaka ya uzaliwa wa kwanza ingeweza kuhama hata kwa mtoto mwingine kama kijana wa kwanza hangekuwa na nidhamu, au angefanya mambo ya kipuuzi

Vita vya uzaliwa wa kwanza.

Katika ulimwengu wa kiroho shetani anapigana sana vita  na haki za mzaliwa wa kwanza kwa sababu Mzaliwa wa kwanza ndiye anayekuwa mlango wa Baraka kwa ndugu zake wote, kila mzaliwa wa kwanza alikuwa ni mali ya Mungu ona Hesabu 3:12-13 “Mimi, tazama, nimewatwaa Walawi na kuwatoa kati ya wana wa Israeli badala ya wazaliwa wa kwanza wote wafunguao tumbo katika wana wa Israeli; na hao Walawi watakuwa wangu; kwa kuwa hao wazaliwa wa kwanza wote ni wangu; katika siku ile niliyowapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri nikajiwekea wakfu wazaliwa wa kwanza wote wa Israeli, wa wanadamu na wa wanyama; watakuwa wangu; mimi ndimi Bwana.”

Kwa kuwa wazaliwa wa kwanza ni mali ya Mungu ni urithi wa Mungu, ni Makuhani, ni viongozi wa ibada, ni warithi wa Baraka za kifamilia, ni ishara ya mafanikio ya familia ni nguvu ya familia ni akiba, ni mtazamo wa baadaye wa familia nan i mali ya Mungu, kamwe shetani hangeweza kufurahia na kupenda kuona mpango wa Mungu unapitia kwa wazaliwa wa kwanza kwa hiyo kuna vita katika ulimwengu wa roho kwaajili ya wazaliwa wa kwanza, shetani angefurahia kuharibu kila mzaliwa wa kwanza kiadilifu, kitaaluma na kimafanikio ili kudhoofisha familia ambazo Mungu amekusudia kuzibarikia, kwa hiyo kila mzaliwa wa kwanza anapaswa kujua kuwa iko vita katika maisha yake.

Ni muhimu kufahamu kuwa kuupata urithi, kungehitaji uvumilivu mkubwa na mapambano ya hali ya juu, shetani anafahamu kuwa kuna urithi uolioko mbele yako na hivyo atahakikisha kuwa anapambana kwa kadiri awezavyo ili ikiwezekana upoteze, vita kati ya Mungu na Farao kule Misri kimsingi ilikuwa ni vita ya kugombea Mzaliwa wa Kwanza, Israel ni taifa ambalo lina haki ya mzaliwa wa Kwanza miongoni mwa mataifa ya dunia, lakini Farao hakutaka kuwaachia alitaka wawe watumwa wake awatumikishe hivyo kimsingi kulikuwa na vita kali kwaajili ya kumgombea mzaliwa wa kwanza  na ndio maana Mungu alimuonya Farao kumuachia Israel kwani vinginevyo angwewaadhibu wazaliwa wa kwanza wote wa mwanadamu na mnyama katika taifa la Misri ili Israel auweze kuwa huru ona

Kutoka 4:22-23 “Nawe umwambie Farao, BWANA asema hivi, Israeli ni mwanangu mimi, mzaliwa wa kwanza wangu; nami nimekuambia, Mpe mwanangu ruhusa aende, ili apate kunitumikia, nawe umekataa kumpa ruhusa aende; angalia basi, mimi nitamwua mwanao, mzaliwa wa kwanza wako.”  

Mzaliwa wa kwanza alikuwa ni mlinzi wa mali au urithi wa mali za wazee wao kizazi hata kizazi na walipaswa kuhakikisha kuwa haki ile inatunzwa kwa gharama yoyote ili isipotee Shetani angetamani wakati wote Mzaliwa wa kwanza apoteze,

1 Wafalme 21:1-3 “Ikawa baada ya hayo, Nabothi Myezreeli alikuwa na shamba la mizabibu katika Yezreeli, karibu na nyumba ya kifalme ya Ahabu mfalme wa Samaria. Ahabu akasema na Nabothi, akamwambia, Nipe shamba lako la mizabibu nilifanye shamba la mboga, maana ni karibu na nyumba yangu; nami nitakupa badala yake shamba la mizabibu lililo zuri zaidi; au ukipenda, nitakupa fedha sawasawa na thamani yake. Nabothi akamwambia Ahabu, Bwana apishe mbali nikupe wewe urithi wa baba zangu

 Kila mtu aliyemwamini Bwana Yesu kuwa bwana na Mwokozi ni mzaliwa wa kwanza, na una haki na Baraka zilezile zilizokusudiwa kwa Ibrahimu, Isaka na Yakobo, kwa msingi huo Mwandishi wa kitabu cha waebrania alikuwa akiwaasa Wakristo wa kiyahudi, kutokurudia nyuma na kuiacha imani kwani kufanya hivyo kungekuwa hakuna tofauti na mwesherati au mtu asiyemcha Mungu kama ilivyokuwa kwa Esau.

Jinsi ya kuilinda haki ya mzaliwa wa Kwanza.

Kwa kuwa haki ya mzaliwa wa kwanza ni jambo linaloweza kuponyoka kutoka katika mikono ya mtu mmoja kwenda kwa mwingine  na tumeona wazi kuwa shetani kama mpinzani hangependa kuona makusudi ya Mungu yakitimizwa kwa wazaliwa wa kwanza hatuna budi kuhakikisha ya kuwa unailinda haki hiyo kwa gharama yoyote, Maandiko yanatuonya kuwa asiwepo mweshatari, wala mtu asiyemcha Mungu kama Esau aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwaajili ya chakula kimoja hii ina maana gani? Maana yake ni kuwa Esau sio kuwa alifanya uasherati lakini lugha inayotumika hapo inamaanisha kubadilisha kitu kikubwa sana na cha thamani kwa kitu kidogo sana kisicho na tamani, tabia ya aina hii inafananishwa na uasherati, uashetari unaweza kumuharibia mtu thamani yake na heshima yake kwa muda mfupi sana, maandiko yanatutaka tulinde kila kitu ambacho tunakiweka katika idadi ya vitu vya thamani sana duniani. Mambo yanayohitaji kupewa kipaumbele yapewe kipaumbele, Mfano watu wanapokuja shuleni, wazazi wanakuwa wamewekeza fedha ambazo wanazitafuta kwa hali na mali, ili mwanafunzi asome, lakini inasikitisha sana kama mwanafunzi badala ya kusoma yeye akawa anapoteza Muda na kucheza huku anapoteza fedha ya wazazi wake na kuharibu maisha yake ya baadaye kwa njia za kiupuuzi, mtu anaweza kufanya jambo la kijinga tu na likamkosesha kazi,  wakati wote tuyape kipaumbele maswala ambayo ni ya muhimu katika maisha yetu na kujihami na mambo yasiyo ya msingi, majukumu yoyote unayopewa hapa dunaini hakikisha kuwa unayatimiza na kuyatetendea haki kwa kujituma kwa gharama kubwa, mwenendo wako na uadilifu wako na tahadhari ni za muhimu sana katika kuhakikisha kuwa unatunza sana kile ambacho Mungu anakitarajia katika maisha yako! Biblia imejaa mifano ya watu waliopoteza haki yao ya uzaliwa wa kwanza kwa njia za kipuuzi na za kusikitisha sana ona :-

-          Mwanzo 9:20-26 “Nuhu akaanza kuwa mkulima, akapanda mizabibu; akanywa divai, akalewa; akawa uchi katika hema yake. HAMU, baba wa Kanaani, akauona uchi wa baba yake, akawaeleza ndugu zake wawili waliokuwa nje. Shemu na Yafethi wakatwaa vazi, wakalitanda mabegani mwao wote wawili, wakaenda kinyumenyume, wakaufunika uchi wa baba yao; na nyuso zao zilielekea nyuma, wala hawakuuona uchi wa baba yao. Nuhu akalevuka katika ulevi wake, akajua mwana wake mdogo alivyomtendea. Akasema, Na alaaniwe Kaanani; Atakuwa mtumwa kabisa kwa ndugu zake. Akasema, Na atukuzwe BWANA, Mungu wa Shemu; Na Kaanani awe mtumwa wake.”

-           

-          Mwanzo 49:3-4 “REUBENI, u mzaliwa wangu wa kwanza, Nguvu zangu, na malimbuko ya uwezo wangu. Umewapita wengine kwa ukuu na kwa nguvu. Umeruka mpaka kama maji, basi usiwe na ukuu, Kwa sababu ulikipanda kitanda cha baba yako, Ukakitia unajisi; alikipandia kitanda changu.”

-           

-          Mwanzo 25:29-32 “Yakobo akapika chakula cha dengu. ESAU akaja kutoka nyikani, naye alikuwa amechoka sana. Esau akamwambia Yakobo, Tafadhali, unipe hicho chakula chekundu nile, kwa kuwa ninazimia mimi. Kwa hiyo walimwita jina lake Edomu.Yakobo akamwambia, Kwanza niuzie leo haki yako ya mzaliwa wa kwanza. Esau akasema, Tazama, mimi ni karibu kufa, itanifaa nini haki hii ya uzazi?

Pigania urithi wako !

Wako watu wanaotajwa kama Mashujaa walioishi wakati wa Daudi watu hawa walikuwa Hodari sana katika kuutetea urithi wa bwana na kuhakikisha kuwa watu wengine wanafaidiaka kwa ujasiri wao, ni imani yangu Kuwa Mungu atakusaidia wewe na mimi tuweze kupigania kile ambacho Mungu ametukabidhi kwa gharama yoyote

2Samuel 23:8-12 “Haya ndiyo majina ya mashujaa aliokuwa nao Daudi; Yashobeamu Mhakmoni,mkuu wa maakida ;huyo aliliinua shoka lake juu ya watu mia nane waliouawa pamoja.Na baada yake kulikuwa na Eleazari, mwana wa Dodai, Mwahohi, mmojawapo wa wale mashujaa watatu waliokuwa pamoja na Daudi; walipowatukana Wafilisti waliokuwa wamekusanyika huko ili kupigana, na watu wa Israeli walikuwa wamekwenda zao; huyo aliinuka, akawapiga Wafilisti hata mkono wake ukachoka, na mkono wake ukaambatana na upanga; naye Bwana akafanya wokovu mkuu siku ile; nao watu wakarudi nyuma yake ili kuteka nyara tu. Na baada yake kulikuwa na Shama, mwana wa Agee, Mharari; nao Wafilisti walikuwa wamekusanyika huko Lehi, palipokuwapo konde lililojaa midengu; nao watu wakawakimbia Wafilisti; ila huyo alisimama katikati ya konde lile, akalipigania, akawaua Wafilisti; naye Bwana akafanya wokovu mkuu.”

 

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa Wajenzi Mwenye Hekima!

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

mimi kama mzaliwa wa kwanza nimejifunza vyema sana na nitabadilika na kuwa shujaa zaidi kuisimamia nafasi hii ya baraka niliyopewa na Bwana.