Jumatano, 19 Julai 2023

Iliwapasa kunisikiliza mimi kwanza!


Matendo 27:20-25Jua wala nyota hazikuonekana kwa muda wa siku nyingi, na tufani kuu ikatushika, basi tukakata tamaa ya kuokoka. Na walipokuwa wamekaa wakati mwingi bila kula chakula, Paulo akasimama katikati yao, akasema, Wanaume, iliwapasa kunisikiliza mimi na kutokung'oa nanga huko Krete, na kupata madhara haya na hasara hii. Sasa nawapeni shauri, iweni na moyo mkuu, kwa maana hapana hata nafsi mmoja miongoni mwenu atakayepotea, ila merikebu tu. Kwa maana usiku huu wa leo malaika wa Mungu yule ambaye mimi ni wake, naye ndiye nimwabuduye, alisimama karibu nami,akaniambia, Usiogope, Paulo, huna budi kusimama mbele ya Kaisari; tena, tazama, Mungu amekupa watu wote wanaosafiri pamoja nawe. Basi, wanaume, changamkeni; kwa sababu namwamini Mungu, ya kwamba yatakuwa vile vile kama nilivyoambiwa.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu huwa anawatumia watumishi wake kwa namna mbalimbali katika kutuonya na kutushauri kwa maswala mbalimbali katika maisha, Maandiko matakatifu yanasisitiza kuwa tumwamini Mungu wetu, lakini vilevile tuwaamini manabii wake ndipo tutakapothibitika na kufanikiwa, Lakini tatizo kubwa sana la watu wengi tulionao katika kizazi hiki ni kuwa wanaamini katiika akili zao na uweza wao wa kibinadamu jambo ambalo linawaletea madhara na kuwafanya wajifunze katika njia ngumu sana, lakini kumbe njia rahisi ilikuwa ni kumsikiliza Mungu na kuwasikiliza watumishi wake na wakati mwingine ushauri wanaotupa kama watumishi wake ona  

2Nyakati 20:20 “Wakaamka asubuhi na mapema, wakaenda nje katika jangwa la Tekoa; nao walipokuwa wakitoka, Yehoshafati akasimama, akasema, Nisikieni, enyi Yuda nanyi wenyeji wa Yerusalemu; mwaminini Bwana, Mungu wenu, ndivyo mtakavyothibitika; waaminini manabii wake, ndivyo mtakavyofanikiwa

Hakuna jambo baya na linaloweza kuleta madhara duniani kama kutokuyajua mapenzi ya Mungu na kutokutaka ushauri kutoka kwa Bwana kisha tukazitumainia akili zetu wenyewe na uzoefu wetu wenyewe katika maisha yangu Mungu wangu alinifundisha kwamba nimtegemee yeye hata katika kiwango cha kutafuta sindano ya kushonea nguo inapokuwa imepotea au imeanguka na siioni.

Mithali 3:5-6 “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako.”

Kwa msingi huo kuna somo kubwa sana katika maisha yetu kuhusu kumsikiliza Mungu na kumuamini na kuwasikiliza watumishi wake katika kifungu cha msingi tulichokisoma hapo juu Paulo mtume aliwahi kutoa ushauri Fulani wakati wa safari yao iliyokuwa ngumu sana na yenye misuko suko mingi lakini hata hivyo ushauri wake ulipuuzwa na watu kutokana na kudhani ya kuwa wao wana ujuzi na utaalamu kuliko yule mtumishi wa Mungu aliyezungumza! Na matokeo yake walipata madhara makubwa sana kuliko madhara yaliyokuwa yamekusudiwa !

Kupuuzia ushauri wa mtumishi wa Mungu!

Paulo mtume alikuwa miongoni mwa wafungwa waliokuwa wanapelekwa Roma kwaajili ya kusimama mbele ya Kaisari kutokana na Kesi iliyosababishwa na kazi zake za injili, akiwa amehesabiwa kama wafungwa wengine tu Meli waliyokuwa wakiitumia kusafiria ilikutana na dhuruba kali sana hali ilikuwa ngumu na kulikuwa na hatari kubwa na madhara makubwa sana ambayo yangeweza kutokea wakati huu mtumishi wa Mungu ambaye kimsingi alikuwa mfungwa tu aliamua kuwapa maonyo na tahadhari kuhusu safari ile kwa Kamanda (Akida) wa kikosi cha safari ile lakini akida yule aliamua kumpuuzia Paulo na akawasikiliza manahodha  na wenye meli na wakapuuzia kile alichikisema Paulo mtume na mfungwa wa Yesu Kristo ona

Matendo 27: 6-13 “Na huko yule akida akakuta merikebu ya Iskanderia, tayari kusafiri kwenda Italia, akatupandisha humo. Tukasafiri polepole kwa muda wa siku nyingi, tukafika mpaka Nido kwa shida; na kwa sababu upepo ulikuwa ukituzuia tukapita chini ya Krete, tukaikabili Salmone. Tukaipita kwa shida, pwani kwa pwani, tukafika mahali paitwapo Bandari Nzuri. Karibu na hapo pana mji uitwao Lasea. Na wakati mwingi ulipokwisha kupita, na safari ikiwa ina hatari sasa, kwa sababu siku za kufunga zilikuwa zimekwisha kupita, Paulo akawaonya, akawaambia, Wanaume, naona kwamba safari hii itakuwa na madhara na hasara nyingi, si ya shehena na merikebu tu, ila na ya maisha yetu pia. Lakini yule akida akawasikiliza nahodha na mwenye merikebu zaidi ya yale aliyoyasema Paulo. Na kwa sababu bandari ile ilikuwa haifai kukaa wakati wa baridi, wengi wao wakatoa shauri la kutweka kutoka huko ili wapate kufika Foinike, kama ikiwezekana, na kukaa huko wakati wa baridi; nayo ni bandari ya Krete, inaelekea kaskazini-mashariki na kusini-mashariki.Na upepo wa kusi ulipoanza kuvuma kidogo, wakidhani ya kuwa wamepata waliyoazimu kupata, wakang'oa nanga, wakasafiri karibu na Krete pwani kwa pwani.

Unaona kuna kitu cha kujifunza hapo, Akida na manahodha na wenye chombo walipuuzia maneno ya Paulo Mtume walimuhesabu kuwa ni mfungwa tu na kuwa hana mawazo wala kitu cha kuchangia, yeye sio mjuzi wa bahari, yeye aliwaonya kuwa kila kitu kingekuwa salama mizigo, pamoja na shehena na abiria kama tu wangetweka nanga na kutokuendelea na safari, Lakini Nahodha alitumia ujuzi wake na utaalamu wake na uzoefu wake wa kuijua bandari na hali ya hewa na kuwa hapafai kupiga nanga wakati wa baridi, hivyo waliamua kuendelea na safari na kumpuuzia kusikiliza habari za mfungwa mmoja maarufu tu, hawakujua ya kuwa mfungwa huyo ni Mtume wa Yesu Kristo hawakujua ya kuwa alikuwa ni wakili wa Mungu, hawakujua ya kuwa alikuwa kinywa cha Mungu, hawakujua ya kuwa Yesu alikuwa anamtumia, hawakujua ya kuwa Roho wa Mungu alikuwa anasema naye, hawakujua ya kuwa malaika wa Bwana wako pamoja naye wao walidhani wako na mjinga mmoja tu mfungwa na mtuhumiwa na mtu asiyekuwa na ujuzi kuhusu bahari kumbe Paulo alikuwa ni mtume wa Mungu aliyeziumba mbingu na nchi na ardhi na bahari, wao walifikiri ya kuwa wana dira na ramani na ujuzi na uzoefu kumbe Mwenye dira ujuzi na uzoefu ni Mungu mwenyewe aliyeziumba mbingu na nchi na matokeo yake walipata hasara kubwa sana walipoteza kila kitu walichokuwa nacho na mizigo na shehena na hata meli yanyewe ni wao tu ambao Mungu aliyaponya maisha yao kwa sababu ya mtume wake aliyekuwa katika safari ile wote walikata tama na kufikia ngazi ya kufikiri kuwa watakufa ona        

Matendo 27:14-20 “Baada ya muda mchache ukavuma upepo wa nguvu wa namna ya tufani, uitwao Eurakilo, merikebu iliposhikwa, na kutoweza kushindana na upepo, tukaiacha tukachukuliwa. Na tukipita upesi karibu na kisiwa kidogo kiitwacho Kauda tukadiriki kuikweza mashua; lakini kwa shida. Walipokwisha kuikweza wakatumia misaada, wakaikaza merikebu kwa kupitisha kamba chini yake, nao wakiogopa wasije wakakwama katika fungu liitwalo Sirti, wakatua matanga wakachukuliwa vivi hivi. Na kwa maana tulikuwa tukipigwa sana na ile tufani, siku ya pili yake wakaanza kuitupa shehena baharini. Siku ya tatu wakatupa vyombo vya merikebu kwa mikono yao wenyewe. Jua wala nyota hazikuonekana kwa muda wa siku nyingi, na tufani kuu ikatushika, basi tukakata tamaa ya kuokoka.”

 Unaweza kuona ni muhimu kufahamu kuwa Licha ya kuwa na ujuzi na ufahamu katika maswala ya aina mbalimbali, Mungu ni Mungu na Mungu ni mwenye hekima na maarifa makubwa zaidi, yeye anajua yajayo sisi hatujui yatakayokuwako kesho kwa msingi huo ni vema kumsikiliza Mungu na watumishi wake na ni kweli tunaweza kufanikiwa sana kama tutamuhusisha Mungu na watumishi wake halisi katika kila Nyanja ya maisha yetu, Mungu yuko juu ya yote, hakuna kinachojitawala hapa duniani kila kitu kiko chini ya uweza wake hivyo hata kama tumesomea sayansi na jambo lolote lile bado kamwe tusiache kumuhusisha Mungu katika kila swala la maisha yetu ili tusiwe na majuto, wako watu wanaojifunza kutokana na makosa na wako watu wanaojifunza haraka kwa kutii ni vema kumtii Mungu na kuyafanya mapenzi yake ili tusijifunze kupitia mazingira magumu na yenye majuto, tunaposhauriwa na watu wa Mungu tusiwachukulie kama kwamba wao ni watu wapuuzi tu tukumbuke ya kuwa wao ni mawakili wa serikali na mamlaka iliyo juu ya mamlaka zote baada ya majuto mengi hatimaye sasa kila mmoja alimsikiliza Mtume na mtumishi wa Mungu ambaye aliwakumbusha hata kula sasa.

Iliwapasa kunisikiliza mimi kwanza!

Baada ya meli kupita katika madhara makubwa sana na kundi lile kupoteza kila walichokuwa nacho, wenye mali walipoteza shehena zote, lakini hata meli yenyewe ilivunjikia mbali, akida wa askari aliyekuwa na wafungwa alifikiri kuwaua wafungwa wote hakuna mtu aliweza kupika wala kula kila mmoja sasa alikuwa anajuta na kufikiri kuhusu uhai wake Ndipo Paulo mtume sasa anawakumbusha kuwa iliwapasa kumsikiliza, Yeye hakuwa mfungwa wa kawaida yeye alikuwa ni Mtumishi wa Mungu aliye hai wakati wao wanataabika huenda yeye alikuwa akiomba na alikuwa akipata mawasiliano na Mungu kuwa nini kinapaswa kufanyika, kwa hiyo ilikuwa sahihi wasingelipata hasara na taabu zile kama tu wangesikiliza kwanza lakini  baada ya taabu na dhuruba sasa ndio wanajua ya kuwa  kweli wangemsikiliza na sasa wanamsikiliza mtumishi wake ona  

Matendo 27:20-25Jua wala nyota hazikuonekana kwa muda wa siku nyingi, na tufani kuu ikatushika, basi tukakata tamaa ya kuokoka. Na walipokuwa wamekaa wakati mwingi bila kula chakula, Paulo akasimama katikati yao, akasema, Wanaume, iliwapasa kunisikiliza mimi na kutokung'oa nanga huko Krete, na kupata madhara haya na hasara hii. Sasa nawapeni shauri, iweni na moyo mkuu, kwa maana hapana hata nafsi mmoja miongoni mwenu atakayepotea, ila merikebu tu. Kwa maana usiku huu wa leo malaika wa Mungu yule ambaye mimi ni wake, naye ndiye nimwabuduye, alisimama karibu nami,akaniambia, Usiogope, Paulo, huna budi kusimama mbele ya Kaisari; tena, tazama, Mungu amekupa watu wote wanaosafiri pamoja nawe. Basi, wanaume, changamkeni; kwa sababu namwamini Mungu, ya kwamba yatakuwa vile vile kama nilivyoambiwa.”

Unaweza kuona, watu hawa ambao walikosa kula na kunywa kwa muda wa siku 14 kila mmoja akihofia uhai wake na usalama wake tu, hali yao ikiwa tete huku wakiwa wamepata hasara ya kila kitu ndipo sasa wanajirudi na kukaa kimya na kumsikiliza Mtumishi wa Mungu, walikuwa wamepoteza Muda wao, walikuwa wamepigika na kupata hasara, meli, shehena chakula na kila kitu lakini sasa wanasikiliza, ukweli ilikuwa wote wafe lakini ashukuriwe Mungu kulikuwa na mmoja aliyekuwa anaomba, aliomba kwaajili ya Mabaharia, aliwaombea wenye meli, aliwaombea manahodha, aliwaombea askari, aliwaombea wafungwa, aliwaombea na abiria wengine  na Mungu akamtuma malaika wake na kumhakikishia kuwa hataacha mtu afe isipokuwa watapoteza kila kitu, wakati wote hatuna budi kumshukuru Mungu na kuwatumia watumishi wake na waombaji na kukubali kuwa wao ni sehemu muhimu sana katika maisha yetu, ushauri wao na nafasi yao isitazamwe kama ni ya kiwango cha chini wakati mwingine maisha yetu yamefungwa katika mikono yao, ramani na dira ya kweli kuhusu maisha na mwelekeo ulionyoooka uko kwa Mungu na watumishi wake uongezewe neema unapolitendea kazi somo hili katika jina la Yesu Kristo amen

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!  



Hakuna maoni: