Jumamosi, 1 Julai 2023

Kufunguliwa mlango wa kufaa sana


1Wakorintho 16:7-9 “Maana sipendi kuonana nanyi sasa, katika kupita tu, kwa sababu nataraji kukaa kwenu muda kidogo, Bwana akinijalia. Lakini nitakaa Efeso hata Pentekoste; kwa maana nimefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana, na wako wengi wanipingao.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha yetu ya kila siku duniani, hatupaswi kuwa na huzuni pale tunapoona jambo moja katika maisha yetu limekwama, na ukajaribu na lingine likakwama, na lingine likakwama, hii haimaanishi kuwa unatakiwa kukata tamaa, na kama ulikuwa unamuomba Mungu au wewe ni mtu wa Mungu acha kufikiri kuwa ndio basi, Mungu katika mpango wake ameweka majira na nyakati mbalimbali kwa makusudi maalumu wakati mwingine tusiyoajua au tutakayoyajua baadaye kwa manufaa yetu

Muhubiri 3:1 “Kwa kila jambo kuna majira yake, Na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu

Kwa msingi huo kila changamoto unayoipitia katika maisha yako kumbuka kuwa wewe sio wa kwanza, wako na wenzako au na wengine waliopitia, alieleza dada mkoja ambaye aliwahi kufungwa gerezani kwa kosa la kusingiziwa na akaa gerezani mwaka mmoja tena akiwa ananyonyesha anasema kule gerezani hali aliyoiona alimsamehe hata mtu aliyemfikisha gerezani, kwani alikutana na watu wenye changamoto kubwa kuliko zake na waliofungwa miaka mingi Zaidi kuliko yake na walisingiziwa makossa makubwa Zaidi na kudhulumiwa hata kuliko yeye, Maandiko yamejaa mifano ya watu kadhaa wa kadhaa katika maandiko ambao walipitia changamoto za aina mbalimbali wengine wakisingiziwa n ahata kufungwa gerezani lakini hatimaye walitoka au Mungu alitafuta njia ya kuwatoa huko, Mungu atakutoa na wewe vilevile Haleluyaaa! Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Kufunguliwa mlango wa kufaa sana

·         Mifano ya watu waliofunguliwa milango ya kufaa

·         Jinsi ya kufunguliwa mlango wa kufaa

Kufunguliwa mlango wa kufaa sana

1Wakorintho 16:7-9 “Maana sipendi kuonana nanyi sasa, katika kupita tu, kwa sababu nataraji kukaa kwenu muda kidogo, Bwana akinijalia. Lakini nitakaa Efeso hata Pentekoste; kwa maana nimefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana, na wako wengi wanipingao.”

Paulo mtume anafunua mpango wake uliokuwa moyoni mwake kwaajili ya Kanisa lililokuwako Korintho, anaelezea mpango wake kuwa ilikuwa apate nafasi ya kwenda Korintho na kukaa nao kwa muda wa kutosha hususani wakati wa baridi, hata hivyo vilevile alikuwa na makusudi ya kukaa Efeso mpaka wakati wa Pentekoste, lakini hata hivyo ilikuwa ngumu pia kuwaaachaWaefeso kwa sababu huko alikuwa amefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana, ni kwa jinsi gani Paulo anaelezea kuchelewa kwenda Korintho na kuendelea kubaki Efeso sababu kubwa ni kuwa amefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana !

Paulo anatumia mfano wa mlango akimaanisha kuwa injili yake imepata kibali na watu wa Efeso wanalipokea neno la Mungu kwa kiwango kikubwa sana na cha hali ya juu , Kila wakati Paulo mtume alipopata nafasi na kibali cha kuihubiri injili mahali na mahali hapo pakawa na moyo mkubwa wa kuikubali injili aliitqa swala hilo kufunguliwa mlango ona

2Wakorintho 2:12 “Basi nilipofika Troa kwa ajili ya Injili ya Kristo, nikafunguliwa mlango katika Bwana”,

Hii ni kwa sababu ziko sehemu au maeneo mengine ambayo kuipokea kwao injili kulikuwa ni kwa ugumu sana na wakati mwingine kwa upinzani mkubwa sana, iko miji ambayo Paulo alitamani sana aihubiri injili lakini shetani akiwatumia watu alipinga vikali sana na huduma ya Paulo mtume, wakati mwingine alikimbia usiku kutoka mji mmoja kwenda mji mwingine

Matendo 17:1-10 “Wakiisha kupita kati ya Amfipoli na Apolonia wakafika Thesalonike, ambapo palikuwa na sinagogi la Wayahudi. Na Paulo, kama ilivyokuwa desturi yake, akaingia mle walimo, akahojiana nao kwa maneno ya maandiko sabato tatu, akiyafunua na kuwaeleza ya kwamba ilimpasa Kristo kuteswa, na kufufuka katika wafu; na ya kwamba, Yesu huyu ninayewapasha ninyi habari zake ndiye Kristo. Wengine miongoni mwao wakaamini, wakashikamana na Paulo na Sila; na Wayunani waliomcha Mungu, wengi sana, na wanawake wenye cheo si wachache. Na Wayahudi wakaona wivu, wakajitwalia watu kadha wa kadha katika watu ovyo wasio na sifa njema, nao wakakutanisha mkutano, wakafanya ghasia mjini, wakawaendea watu wa nyumba ya Yasoni, wakataka kuwapeleka mbele ya watu wa mji; na walipowakosa, wakamkokota Yasoni na baadhi ya ndugu mbele ya wakubwa wa mji, wakipiga kelele, wakisema, Watu hawa walioupindua ulimwengu wamefika huku nako, na Yasoni amewakaribisha; na hawa wote wanatenda mambo yaliyo kinyume cha amri za Kaisari, wakisema na kwamba yupo mfalme mwingine, aitwaye Yesu. Wakafadhaisha ule mkutano na wakubwa wa mji walipoyasikia hayo. Nao walipokwisha kumtoza dhamana Yasoni na wenziwe wakawaacha waende zao. Mara hao ndugu wakawapeleka Paulo na Sila usiku hata Beroya. Nao walipofika huko wakaingia katika sinagogi la Wayahudi.”      

Kutokana na upinzani huu wa mara kwa mara dhidi ya injili, Paulo mtume aliwaomba wakristo wa makanisa ya miji mingine kuwa na maombi rasmi ya kumuombea ili kwamba afunguliwe mlangowa injili,

Wakolosai 4:2-3 “Dumuni sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani; mkituombea na sisi pia, kwamba Mungu atufungulie mlango kwa lile neno lake, tuinene siri ya Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa,”

Katika mji wa Efeso mambo yalikuwa ni tofauti sana na maeneo mengine, watu wa Efeso walipomuona Paulo mtume kwa mara ya kwanza na kumsikia katika sinagogi hata wayahudi wa Efeso walimtaka Paulo akae kwao siku nyingi Zaidi, Paulo alikuwa na safari ya kwenda Syria (Shamu) na hivyo aliwaahidi kuwa angerejea tena ona

Matendo 18:18-19 “Baada ya hayo Paulo akazidi kukaa huko siku nyingi, kisha akaagana na ndugu akaabiri kwenda Shamu; na Prisila na Akila wakaenda pamoja naye, alipokwisha kunyoa kichwa chake huko Kenkrea; maana alikuwa ana nadhiri. Wakafika Efeso, akawaacha huko. Yeye mwenyewe akaingia katika sinagogi, akahojiana na Wayahudi. Walipomtaka akae wakati mwingi zaidi, hakukubali;

Paulo aliporejea Efeso baadaye mlango mkubwa sana wa injili ulifunguka, watu walilipokea neno la Mungu kwa furaha kubwa sana pamoja na kuwa injili huwa inapingwa lakini Pale Efeso alipata neema ya kukaa muda mrefu zaidi na hivyo kuwa na kanisa imara sana, Katika mji huu Paulo alitumiwa na Mungu kwa miujiza mikubwa sana na kupita kawaida, watu wengi walikuja kwa Bwana na sio hivyo tu waliokuwa wachawi na waaguzi waliacha uchawi na kuchoma moto vifaa vyao vya kiroho na vitabu vyao vya thamani kubwa sana na kushikamana na Paulo

Matendo 19:8-11 “Akaingia ndani ya sinagogi, akanena kwa ushujaa kwa muda wa miezi mitatu, akihojiana na watu, na kuwavuta katika mambo ya ufalme wa Mungu. Lakini wengine walikaidi, wakakataa kuamini, wakiitukana ile Njia mbele ya mkutano; basi, akaondoka akawaacha, akawatenga wanafunzi, akahojiana na watu kila siku katika darasa ya mtu mmoja, jina lake Tirano. Mambo haya yakaendelea kwa muda wa miaka miwili, hata wote waliokaa Asia wakalisikia neno la Bwana, Wayahudi kwa Wayunani. Mungu akafanya kwa mikono ya Paulo miujiza ya kupita kawaida;”

Matendo 19:18-20 “Na wengi wa wale walioamini wakaja wakaungama, wakidhihirisha matendo yao. Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu. Hivyo ndivyo neno la Bwana lilivyozidi na kushinda kwa nguvu.”  

Ni kutokana na mafanikio makubwa sana Paulo mtume anaelezea kuwa katika huduma yake ambayo kimsingi ilikuwa na upinzani mkubwa sana anaona kuwa amefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana Pale Efeso licha ya kuwepo kwa upinzani wa hapa na pale, Muda alioutumia Pale Efeso ulimkosesha Fursa ya kwenda Korintho kwa kusudi la kuwaimarisha huko nako na ndipo alipowaandikia kuwa anatamani kuwa nao lakini alikuwa amefunguliwa mlango mkubwa sana wa kufaa japo kuna upinzani mdogo

1Wakorintho 16:7-9 “Maana sipendi kuonana nanyi sasa, katika kupita tu, kwa sababu nataraji kukaa kwenu muda kidogo, Bwana akinijalia. Lakini nitakaa Efeso hata Pentekoste; kwa maana nimefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana, na wako wengi wanipingao.”

Mifano ya watu waliofunguliwa milango ya kufaa

Mungu alimfungulia mtume Paulo mlango mkubwa wa kufaa sana kwaajili ya injili, kama tunavyoweza kuona katika maandiko kwamba Upinzani dhidi ya injili ulimkabili Paulo mtume kila mahali kiasi cha kuhatarisha maisha yake japo watu wengi walikuja kwa Bwana, Ni muhimu kufahamu kuwa sio katika huduma tu watu hufungiwa mlango, lakini hata katika maisha yetu ya kawaida kuna milango inaweza kufungwa yako mambo ambayo ungetamani yakae sawa lakini yamefungwa, ni huduma yako bado haijapata nafasi ya kutulia na kuwafikia wale ambao ulikuwa unawafikiri, ni  tumbo lako na uzao wako umefungwa hushiki mimba, au huwezi kumpa mwanamke mimba, biashara haijapata mpenyo unaokusudiwa, Hata hivyo haupaswi kukata tamaa, Neno la Mungu linatukumbusha kuwa katika kila jaribu Mungu huweka mlango wa kutokea

 1Wakorintho 10:13 “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”

·        Yusufu alipitia katika mitihani ya namna mbalimbali katika maisha yake hata kufungwa gerezani kwa kusingiziwa tu lakini hatimaye Mungu alimfungulia mlango na akawa mtu mkubwa sana katika incho ya Misri

-          Mwanzo 37:12-36 “Ndugu zake wakaenda kuchunga kondoo za baba yao huko Shekemu. Israeli akamwambia Yusufu, Je! Ndugu zako hawachungi kondoo katika Shekemu? Njoo, nikutume kwao. Akamwambia, Mimi hapa.  Akamwambia, Enenda, basi, ukaone kama ndugu zako hawajambo, na kundi nalo li salama, ukaniletee habari. Basi akampeleka kutoka bonde la Hebroni, akafika Shekemu. Mtu mmoja akamkuta, naye alikuwa anazunguka-zunguka katika nyika; yule mtu akamwuliza, akisema, Unatafuta nini? Akasema, Nawatafuta ndugu zangu; tafadhali uniambie mahali wanakochunga. Yule mtu akasema, Wametoka hapa, maana niliwasikia wakisema, Twendeni Dothani. Basi Yusufu akawafuata ndugu zake akawakuta huko Dothani. Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake. Reubeni akasikia akamwokoa katika mikono yao, akasema, Tusimwue. Reubeni akawaambia, Msimwage damu; mtupeni katika birika hii iliyopo nyikani, wala msimguse; ili apate kumwokoa katika mikono yao, akamrudishe kwa baba yake. Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji. Nao wakakaa kitako kula chakula; wakainua macho yao, wakaona, msafara wa Waishmaeli wanakuja wakitoka Gileadi na ngamia zao, wakichukua ubani na zeri na manemane, wakisafiri kuvichukua mpaka Misri. Yuda akawaambia ndugu zake, Kwafaa nini kumwua ndugu yetu, na kuificha damu yake? Haya, na tumwuze kwa hawa Waishmaeli, wala mikono yetu isimdhuru, maana yeye ni ndugu yetu, na damu yetu. Ndugu zake wakakubali. Wakapita wafanya biashara Wamidiani; basi wakamtoa Yusufu, wakampandisha kumtoa katika birika, wakamwuza Yusufu kwa Waishmaeli kwa vipande vya fedha ishirini; nao wakamchukua Yusufu mpaka Misri. Akarudi Reubeni birikani, kumbe! Yusufu hayumo katika birika, akararua nguo zake. Akarudi kwa ndugu zake, akasema, Mtoto hayuko, nami niende wapi?  Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi. Wanawe wote, na binti zake wote, wakaondoka wamtulize, lakini akakataa kutulizwa, akasema, La! Nitamshukia mwanangu, nikisikitika, hata kuzimu. Baba yake akamlilia. Nao Wamidiani wakamwuza huko Misri, kwa Potifa, akida wa Farao, mkuu wa askari.”

·        Ayubu alipitia mitihani migumu sana kufiwa na watoto wote, kupoteza mali zake zote, kupata hasara ya mifugo yake yote na wafanyakazi wake wote waliuawa na kutekwa na kubakiwa na watoa taarifa tu, kama haitoshi yeye aliugua na kufilisika kwa kiwango kikubwa, hata hivyo Mungu alimfungulia mlango wa kufaa baadaye

-          Yakobo 5:10-11 “Ndugu, watwaeni manabii walionena kwa jina la Bwana, wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu. Angalieni, twawaita heri wao waliosubiri. Mmesikia habari ya subira yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”

Mpenzi haupaswi kukata tamaa na kudhani ya kuwa wewe una nuksi au balaa, kila changamoto unayoipitia kumbuka kuwa Mungu atafanya mlango wa kutokea, Mlango ambao Mungu atakufungulia utakuwa ni mkubwa na wa kufaa Zaidi, Mungu aliyewafungulia mlango watakatifu waliotutangulia na wale ambao wako leo na tnasikia shuhuda zao hatakosa kukufungulia mlango mkubwa wa kukufaa Zaidi wewe nawe katika maisha yako   

Jinsi ya kufunguliwa mlango wa kufaa

Ni muhimu kufahamu kuwa hata sasa Mungu anakuwazia mema, Paulo mtume hakukata tamaa kwa sababu ya magumu aliyokuwa akiyapitia, aliendelea kuhubiri injili, kila alikokuwa akikataliwa alikimbia katika mji mwingine na hatimaye kule Efeso Mungu alimfungulia mlango mkubwa wa kufaa Zaidi, ziko sababu nyingi kwako kwanini Mungu atakufungulia mlango

1.       Mungu tunayemwambudu na kumtumikia nidye mwenye funguo yeye anauwezo wa kufungua na hakuna wa kufunga na ana uwezo wa kufunga na hakuna afunguaye kwa msingi huo ni Mungu mwenyewe anayeweza kuingilia katika hali unayoipitia na kukufungulia mlango  na ni yeye anayeweza kukupa mlango uliofunguliwa mbele yako ona

 

Ufunuo 3:7-8 “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Filadelfia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye mtakatifu, aliye wa kweli, aliye na ufunguo wa Daudi, yeye mwenye kufungua wala hapana afungaye, naye afunga wala hapana afunguaye. Nayajua matendo yako. Tazama, nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga, kwa kuwa unazo nguvu kidogo, nawe umelitunza neno langu, wala hukulikana jina langu.”

 

2.       Mungu amelipa Kanisa mamlaka ya kushangaza sana wewe kama mtu uliyemwamini Bwana Yesu wewe ni kanisa na Mungu amekupa uwezo na mamlaka ya kufungua lolote kiasi hata mbinguni likafunguliwa na una uwezo wa kufunga lolote nahata mbinguni likafungwa, kwa msingi huo katika kila jambo ambalo unahisi limefungwa unaweza kumuomba Mungu na akakufungulia mlango  ona

 

Mathayo 18:18 “Amin, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni.”

3.       Washirikishe wale unaowaamini katika maombi yako, kuna nguvu kubwa sana kama watu wawili au zaidi wakipatana na kuomba Mungu huwafanyia, kile walichokiomba, Mungu huwa kati kati ya watu Zaidi ya wawili au watatu wakiungana katika maombi, hiki ndicho alichosema Kristo ona

 

Mathayo 18:19-20 “Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.”        

 

Na ndio maana Paulo mtume alipoona changamoto zilizokuwa zinamkabili aliwaomba kanisa wamuombee neema ili kwamba wamuombee ili afunguliwe mlango

Wakolosai 4:2-3 “Dumuni sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani; mkituombea na sisi pia, kwamba Mungu atufungulie mlango kwa lile neno lake, tuinene siri ya Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa,”

Daniel alipopata changamoto kazini wakati wenye hekima walipotakiwa kutafasiri na kumkumbusha mfalme Nebukadreza kuhusu Ndoto aliyoiota akaisahau na kuwataka wamkumbushe kwanza kisha wamuelezee maana vinginevyo angewaua Daniel aliamua kumuomba Mungu na kuwashirikisha na wenzake na wakamuomba Mungu, shirikisha watu muhimu unaowaamini ombeni pamoja kuhusu changamoto inayokukabili na Bwana atakufungulia mlango mkubwa wa kufaa Zaidi.

Daniel 2:17-19 “Ndipo Danieli akaenda nyumbani kwake, akawapasha habari kina Hanania, na Mishaeli, na Azaria wenzake; ili waombe rehema kwa Mungu wa mbinguni kwa habari ya siri hiyo, ili kwamba Danieli na wenzake wasiangamizwe pamoja na wenye hekima wa Babeli. Ndipo Danieli alipofunuliwa siri hiyo katika njozi ya usiku. Basi Danieli akamhimidi Mungu wa mbinguni.”


Bwana kupe neema na kukufungulia mlango mkubwa wa kufaa Zaidi katika kila jambo ambalo unakutana nalo katika maisha yako, Mungu ni mwema na ni mwingi wa huruma amejaa neema hakika hatakuacha ulie tu atakufungulia mlango wa kufaa na utafanikiwa sana katika maisha yako!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!


Hakuna maoni: