Jumatano, 19 Julai 2023

Msipoona Ishara na maajabu hamtaamini kabisa?


Yohana 4: 45-48 “Basi alipotoka Galilaya, Wagalilaya walimpokea; kwa kuwa wameyaona mambo yote aliyoyatenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu; maana hao nao waliiendea sikukuu.  Basi alifika tena Kana ya Galilaya, hapo alipoyafanya yale maji kuwa divai. Na palikuwa na diwani mmoja ambaye mwanawe hawezi huko Kapernaumu. Huyo aliposikia ya kwamba Yesu amekuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya, alimwendea, akamsihi ashuke na kumponya mwanawe; kwa maana alikuwa kufani. Basi Yesu akamwambia, Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa?”


Utangulizi:

Yesu alikuwa ni mtenda miujiza mkubwa Zaidi kupata kutokea Duniani, Mungu alimpa neema kubwa sana ya kufanya kazi ya uponyaji na kufundisha kwa uweza wa Roho Mtakatifu kila alikokwenda

Mathayo 4:23-25 “Naye alikuwa akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri Habari Njema ya ufalme, na kuponya ugonjwa na udhaifu wa kila namna katika watu. Na habari zake zikaenea katika Shamu yote; wakamletea wote waliokuwa hawawezi, walioshikwa na maradhi mbalimbali na mateso, wenye pepo, na wenye kifafa, na wenye kupooza; akawaponya. Na makutano mengi wakamfuata, kutoka Galilaya, na Dekapoli, na Yerusalemu, na Uyahudi, na ng'ambo ya Yordani

Sababu kubwa ya Yesu kusukumwa na Roho Mtakatifu kufanyahuduma hizi zote ni kwa sababu aliwahurumia watu na kusikitishwa na taabu zao na uonevu wa Shetani aliokuwa ameufanywa kwa wanadamu  hivyo alifanya kazi hiyo ya kuwaponya na kuwafundisha neno la Mungu

Mathayo 9:35-36 “Naye Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme, na kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.”

Kwa hiyo kazi zote alizozifanya Kristo alizifanya kwa sababu ya moyo wake wa upendo kwa wanadamu, alitumia karama zake na vipawa vyake kwa faida ya kuwajenga watu, kuwasaidia, kuwakwamua na kuwatoa katika shida na changamoto kubwa zilizokuwa zikiwakabili, Hata hivyo kwa upande wa watu waliokuwako nyakati zile wao walianza kumfuata Yesu kila alikokwenda wakifurahi na kushangilia kwaajili ya kuona miujiza na kufurahia ishara alizokuwa akizifanya, Kimsingi Isahara na maajabu sio kitu kibaya na ndio maana Yesu alifanya, lakini kimsingi wanadamu wanatakiwa kujifunza kumuamini Mungu na kujua ya kuwa Mungu anawajali na kuhusika na maisha yao hata bila ya Ishara na maajabu nahiki ndicho kiwango ambacho Yesu alitamani watu wakifikie:- tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Kusudi kuu la ishara na miujiza

·         Msipoona ishara na maajabu hamtaaamini kabisa

·         Jambo kubwa la msingi

Kusudi kuu la Ishara na miujiza.

Ishara na miujizaa ni mojawapo ya matukio makubwa ya kushangazwa yanayoyanywa na Mungu kupitia watumishi wake ambao amewapa karama mbalimbali kwa uwezo wa Roho Mtakatifu kuwawezesha watu hao kufanya mambo makubwa nay a kushangaza kwa idhini au kwa jina la Mungu, Tangu zamani katika Israel na hata baadaye nyakati za kanisa la kwanza na siku zoa leo katika jumuia nyingi za kikristo za uamsho kama Charismatic Movements na Pentecostal movements Ishara na miujiza imekuwa ni moja ya sehemu muhimu sana ya kiibada kwa kusudi la kuwaaminisha watu juu ya uwepo na utendani wa Mungu na kudhihirisha kuwa mungu hayuko mbali na watu wake na kuwa yeye ni msaada ulio karibu

 Zaburi 46:1 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.”

Kwa hiyo kumekuweko na msisistizo mkubwa sana wa injili na huduma nyingi za ukombozi na uponyaji, ambavyo kimsingi sio vibaya kwa sababu watu wanasaidiwa na kuponywa magiojwa yao na kusaidiwa kimwili, kiroho na hata kisaikolojia unapoona makundi makubwa ya watu wakitafuta uponyaji unaweza kuhisi huruma na hata kutamani kama ungekuwa na uwezo wa kuwasaidia watu wote ungeweza kuwasaidia lakini hata hivyo ni muhimu kufahamu kuwa kuna makusudi ya kuweko kwa ishara na miujiza , na ni muhimu kujiuliza kwanini Mungu anafanya hizi ishara na miujiza ?

1.       Kufunua ukuu wa Mungu -  Ishara zote zilizofanyika katika agano la kale na zinazofanyika hata sasa katika agano jipya makusudi yake makuu ni kufunua ukuu wa Mungu, ni ili watu wenye kiburi wanaojifikiri kuwa wao ni ka a miungu duniani wapate kutiishwa wajue ya kuwa Yuko Mungu anayetawala Dunia  na kila mmoja aweze kumjua yeye na jina lake na uweza wake na utendaji wake hatimaye waweze kumuabudu na kumuheshimu yeye ona

 

Warumi 9:17 “Kwa maana maandiko yasema juu ya Farao, ya kwamba, Nilikusimamisha kwa kusudi hili, ili nionyeshe nguvu zangu kwako, jina langu likatangazwe katika nchi yote.”

 

Maana yake ni nini kwamba miujiza yote ambayo Mungu aliitenda kuanzia wakati anawatoa wana wa Israel Huko Misri na mingine mingi muda usingeweza kutosha kutaja yote lakini kusudi mojawapo kubwa ni kuufunua ukuu wa Mungu ili dunia ipate kumuheshimu, kumtukuza, kumshukuru, na kutambua kuwa yeye ndiye kila kitu.

 

2.       Kuufunua utukufu wake – ishara zote alizozifanya Mungu katika agano la kale na jipya hata kuanzia kazi zake za uumbaji na maajabu yote na ishara ni kwaajili ya kuufunua utuklufu wake ni ili watu wote wajue na kumsifu Mungu kuwa ndiye Mungu,

 

Zaburi 19:1 “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, Na anga laitangaza kazi ya mikono yake.”

 

Unaona Mungu wetu anataka tumtukuze yeye, kumtukuza yeye ni sehemu ya ibada, ni sehemu ya kutambua ukuu wake, ni sehemu ya heshima , ni sehemu ya shukurani ni sehemu ya kuonyesha kuwa yuko mwenye serikali mbunguni na duniani na kuwa tunapaswa kumpa yeye utukufu, hii ni mojawapo ya sababu kwanini Mungu hufanya ishara na miujiza ona pia

 

Yohana 2:11 “Mwanzo huo wa ishara Yesu aliufanya huko Kana ya Galilaya, akaudhihirisha utukufu wake, nao wanafunzi wake wakamwamini.”

 

3.       Kwaajili ya huruma na upendo wake  Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai na Baba wa Mbinguni ni wamoja kwa uweza wa Roho Mtakatifu Yesu alitenda kazi ya uponyaji kwaajili ya kufunua huruma na upendo wa Mungu kwa wanadamu kama tulivyoona katika utangulzizi kuwa alifanya yote aliyoyafanya kwaajili ya huruma zake

 

Mathayo 9:35-36 “Naye Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme, na kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.”

 

Kazi hizi alizozifanya Kristo ni kwaajili ya maelekezo yote kutokwa kwa baba yake hivyo alifanya kile ambacho baba yake anakifanya

 

Yohana 5:19-20 “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile. Kwa kuwa Baba ampenda Mwana, naye humwonyesha yote ayatendayo mwenyewe; hata na kazi kubwa zaidi kuliko hizo atamwonyesha, ili ninyi mpate kustaajabu.”

 

Kwa hiyo kile alichokitenda Bwana Yesu kwa neno au kwa tendo kinadhihirisha na kufunua Moyo wa Mungu baba kwetu, Kristo Yesu ni chapa ya mng’ao wa utukufu wa Mungu kumuona Yesu ni Kumuona baba, kwa sababu hiyo ni Dhahiri kuwa Yesu/Mungu alifanya ishara na miujiza kwa kusudi la kufunua huruma na upenzo wake kwetu.      

 

4.       Kwaajili ya kulithibitisha neno Neno la Mungu linapotoka kwake au kwa kinywa cha nabii wake huwa haliendi bure naposema nabii hapa namiaanisha mtu anayesema kwa niaba ya Mungu yaani walimu, wachungaji, wainjilisti manabii na mitume, watmishi wote halali ambao wanazungumza kwa niaba ya Mungu wanapolisema neno lake halitekwenda bure litazaa matunda

 

Isaya 55:10-11 “Maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”

 

Kwa hiyo Mungu hulithibitisha neno lake kwa ishara  na miujiza, watu wanapotoka kwenda kulitangaza neno lake Mungu hufanya ishara na miujiza kwa kusudi la kulithibitisha neno lake ili watu wapate kusadiki ona 

 

Marko 16L17-20 “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya. Basi Bwana Yesu, baada ya kusema nao, akachukuliwa juu mbinguni, akaketi mkono wa kuume wa Mungu. Nao wale wakatoka, wakahubiri kotekote, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha lile neno kwa ishara zilizofuatana nalo.]

 

Matendo 14:3 “                Basi wakakaa huko wakati mwingi, wakinena kwa ushujaa katika Bwana, aliyelishuhudia neno la neema yake, akiwajalia ishara na maajabu yatendeke kwa mikono yao.”

 

Waebrania 2:3-4 “Kwa maana, ikiwa lile neno lililonenwa na malaika lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki, sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia; Mungu naye akishuhudu pamoja nao kwa ishara na ajabu na nguvu za namna nyingi, na kwa magawanyo ya Roho Mtakatifu, kama alivyopenda mwenyewe.”

 

Kwa hiyo tunaona wazi kuwa Mungu hufanya ishara na miujiza kwa kusudi la kulithibitisha neno lake lengo kuu likiwa watu wapate kusadiki kuamini, waokolewe wawekwe huru, waponye, wajengeke wakue katika Imani wakiamni kuwa yuko Mungu

 

5.       Ili watu wapate kumuamini – Kusudi kubwa na la juu Zaidi la Mungu kufanya ishara na miujiza ni ili watu wapate kumuamini wakubali kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, wamwamini yeye ili wapate wokovu wamjue Mungu na Yesu Kristo aliyemtuma

 

 Yohana 20: 30-31 “Basi kuna ishara nyingine nyingi alizozifanya Yesu mbele ya wanafunzi wake, zisizoandikwa katika kitabu hiki. Lakini hizi zimeandikwa ili mpate kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa kuamini mwe na uzima kwa jina lake.”       

Kusudi kubwa na la juu kabisa la ishara na miujiza ni ili watu wamamwini Mungu na wapate kuokolewa wamwamini Yesu Kuwa ni Bwana na mwokozi ili waokolewe, na wayahudi wapate kujua kuwa Yesu ndiye Masihi mwana wa Mungu aliye hai kwa hiyo kila muujiza alioufanya Yesu pamoja na maneno yake na matendo yake hitimisho lake ni ili watu wapate kumwamini kuwa yeye ni mwana wa mungu na ndiye njia na kweli na uzima

Yohana 2:11 “Mwanzo huo wa ishara Yesu aliufanya huko Kana ya Galilaya, akaudhihirisha utukufu wake, nao wanafunzi wake wakamwamini.”

               

Yohana 2:23Hata alipokuwapo Yerusalemu kwenye sikukuu wakati wa Pasaka, watu wengi waliamini jina lake, walipoziona ishara zake alizozifanya.”

Msipoona ishara na maajabu hamtaaamini kabisa.

Baada ya kuwa tumejifunza na kupata ufahamu kuhusu kusudi kuu la Isara na miujiza sasa swali kubwa la Msingi ni kwanini Bwana Yesu alitoa maonyo kwa watu waliokuwa tu wanataka kusaidiwa na kupata miujiza yao?

Yohana 4: 45-48 “Basi alipotoka Galilaya, Wagalilaya walimpokea; kwa kuwa wameyaona mambo yote aliyoyatenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu; maana hao nao waliiendea sikukuu.  Basi alifika tena Kana ya Galilaya, hapo alipoyafanya yale maji kuwa divai. Na palikuwa na diwani mmoja ambaye mwanawe hawezi huko Kapernaumu. Huyo aliposikia ya kwamba Yesu amekuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya, alimwendea, akamsihi ashuke na kumponya mwanawe; kwa maana alikuwa kufani. Basi Yesu akamwambia, Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa?”

Kimsingi sio kuwa Yesu alikuwa anazungumza na diwani pekee hapana Yesu alikuwa anazungumza na diwani na watu wote waliokuwa wamemkusanyikia mioyoni mwao wakiwa wanataka kuponywa na kuona ishara na miujiza aliyokuwa akiifanya hata kabla hawajamuamini, yaani kismingi watu walikuwa wana hamu na shauku ya kuona miujiza na ishara kuliko hata mwenye kufanya hizo sihara na miujiza, Yesu aliwakemea maalumu kwaajili yao, Hakumaanisha kuwa ishara na maajabu ni jambo baya kwao hapana lakini kuna kitu cha ziada Zaidi ya muujiza nah ii sio mara ya kwanza Yesu kutoa maonyo haya  ona

Yohana 6:25-29 “Hata walipomwona ng'ambo ya bahari, walimwambia, Rabi, wewe umekuja lini hapa? Yesu akawajibu, akasema, Amin, amin, nawaambieni, Ninyi mnanitafuta, si kwa sababu mliona ishara, bali kwa sababu mlikula ile mikate mkashiba. Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa, kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na Baba, yaani, Mungu. Basi wakamwambia, Tufanyeje ili tupate kuzitenda kazi za Mungu? Yesu akajibu, akawaambia, Hii ndiyo kazi ya Mungu, mmwamini yeye aliyetumwa na yeye.”

Nadhani sasa tunaweza kuona katika moja ya kemeo la Yesu kwamba watu walimfuata kwa sababu tu waliziona ishara na jambo hilo liko wazi Yohana 6:1-2 “Baada ya hayo Yesu alikwenda zake ng'ambo ya Bahari ya Galilaya, nayo ndiyo ya Tiberia. Na mkutano mkuu wakamfuata, kwa sababu waliziona ishara alizowafanyia wagonjwa.”

Kwa hiyo hoja ya Yesu Kristo ina umuhimu na msingi sana hususani katiika nyakati za leo, kuna watu leo ambao wameacha kumtafuta Mungu na mafundisho sahihi na badala yake wanatafuta ishara na miujiza , wanashindwa hata kuamini injili nyepesi tu ya wokovu  na kumjua Mungu wa kweli badala yake wanatafuta ishara na miujiza hii inadhoofisha sana nafasi ya kanisa kuwahudumia na kupata nafasi ya kuwajengea Imani sahihi, tumekuwa na wimbi kubwa la watu wanaotafuta maombezi kila wakati, wakristo wamedumaa na hawafikii ngazi ya kukomaa na kukua kiroho ili wao nao wawe na karama za Rohoni na kuwahudumia wengine badala yake wanahangaika huko na huko kutafuta maombizi kila likija wimbi moja na lingine, Yesu mwenyewe alikuwa anaonya hapa kwamba Imani hii ya kutaka kuhudumiwa tu kwa ishara na miujiza japo hiana ubaya lakini haitoshi kuwafanya watu wawe na imani ya kweli, Ishara na miujiza ni mwanzo tu wa swala zima la Imani ili tujenge Imani yetu kwa mtenda miujiza ambaye ni Bwana Yesu, onyo la Yesu ni kwa watu wote Msipoona na sio usipoona kwa hiyo kila mmoja wetu anakumbusha kuwa ishara huwa ainatuongoza katika jambo moja kubwa na la muhimu sana ambalo ni Yesu  

Jambo kubwa la msingi.

Ni muhimu kufahamu kuwa hakuna watu ambao wamewahi kushuhudia miujiza mikubwa na utendaji mkubwa wa Mungu kama wana wa Israel hivyo neno la Mungu linalalamika kuwa hawakuamini na hatimaye wengi waliangamizwa jangwani

 1Wakorintho 10:1-5 “Kwa maana, ndugu zangu, sipendi mkose kufahamu ya kuwa baba zetu walikuwa wote chini ya wingu; wote wakapita kati ya bahari; wote wakabatizwa wawe wa Musa katika wingu na katika bahari; wote wakala chakula kile kile cha roho; wote wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea mwamba wa roho uliowafuata; na mwamba ule ulikuwa ni Kristo.Lakini wengi sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani.”

Wana wa Israel Jangwani waliona muujiza mmoja baada ya muujiza mwingine Makusudi makubwa ya Mungu ni ili waoa wamuamini, wamtukuze, wamuheshimu na kumuabudu, watambue ya kuwa yeye ndiye anayemiliki, wamuamini yeye na neno lake na hatimaye waweze kuwa na badiliko la ndani linalotokana na kuamini, lakini badala yake hawakuamini, walinungunika roho zao hazikufanyika imara hawakumwamini na hivyo Mungu alichukizwa nao

Waebrania 3:14-19 “Kwa maana tumekuwa washirika wa Kristo, kama tukishikamana na mwanzo wa uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho; hapo inenwapo, Leo, kama mtaisikia sauti yake, Msifanye migumu mioyo yenu, Kama wakati wa kukasirisha. Maana ni akina nani waliokasirisha, waliposikia? Si wale wote waliotoka Misri wakiongozwa na Musa? Tena ni akina nani aliochukizwa nao miaka arobaini? Si wale waliokosa, ambao mizoga yao ilianguka katika jangwa? Tena ni akina nani aliowaapia ya kwamba hawataingia katika raha yake, ila wale walioasi? Basi twaona ya kuwa hawakuweza kuingia kwa sababu ya kutokuamini kwao.”

Kristo Yesu alikuwa anataka kuwaepusha wana wa Israel na jambo kama hili, fundisho lake ni kwa watu wote waaminio na hata wale ambao bado, muhimu tu kama kwetu sote Ishara na miujiza ikatuongoza katika kumtii Mungu na kumuheshimu, Yesu anataka tmuamini yeye hata tuspoona ishara na miujiza, Imani sahihi wakati wote hailazimishi Mungu atende kila tunataka inalazimisha mioyo yetu iamini katika Mungu katika namna ya iliyopitiliza na hiki ndicho Mungu anachokitaka

-          Ayubu 19:25-26 “Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi. Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivi, Lakini, pasipokuwa na mwili wangu nitamwona Mungu;”  

 

-          Daniel 3:14-18 “Nebukadreza akajibu, akawaambia, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, je! Ni kwa makusudi hata hammtumikii mungu wangu wala kuisujudia sanamu ya dhahabu niliyoisimamisha?      Basi sasa, kama mkiwa tayari wakati mtakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, kuanguka na kuisujudia sanamu niliyoisimamisha, ni vema; bali msipoisujudia, mtatupwa saa iyo hiyo katika tanuru iwakayo moto; naye ni nani Mungu yule atakayewaokoa ninyi na mikono yangu? Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakajibu, wakamwambia mfalme, Ee Nebukadreza, hamna haja kukujibu katika neno hili. Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme. Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.”        

Hitimisho:

Lazima ufikie wakati Imani yetu iwe kwamba Mungu ni Mungu tu na atabaki kuwa Mungu na kwamba lazima aonyeshe miujiza yake, na tunapaswa kumuamini iwe kuna muuiiza au hakuna muujiza, iwe tuna kazi au hatuna kazi, iwe tumeponywa au hatujaponywa, iwe amaejibu maombi aua amekataa, iwe amatuponya au hajatuponya iwe tumeolewa au hatujaolewa, iwe tumechumbiwa au hatujachumbiwa, iwe tumepata au tumekosa, iwe tumefaulu au tumefeli, iwe kuna raha au kuna shida, tuwe tunapata mema au mabaya tunamwamini Mungu hata pasipo ishara na maajabu tunamwamini Mungu kuwa yeye ndiye anayetawala kila jambo katika maisha yetu na tunaendelea kumuheshimu na kumpa utukufu

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!.



Hakuna maoni: