Alhamisi, 5 Oktoba 2023

Usinifanye laumu ya Mpumbavu!


Zaburi 39:7-9 “Na sasa ninangoja nini, Ee Bwana? Matumaini yangu ni kwako, Uniokoe na maasi yangu yote, Usinifanye laumu ya mpumbavu.  Nimenyamaza, sitafumbua kinywa changu, Maana Wewe ndiwe uliyeyafanya.



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu ya kwamba tuwapo duniani kama wanadamu tunakutana na changamoto nyingi, na changamoto hizi vyovyote iwavyo ni za kawaida tu wala usiogope, hakuna jambo jipya linalokupata kila jambo linalokupata ni la kawaida, na wala hauko peke yako wako wengi wanapitia au wamekwisha kupitia hivyo usiogope.

1Wakorintho 10:13 “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”

Daudi alikuwa mojawapo ya watu wa Mungu ambaye alipitia changamoto nyingi sana  na katika zaburi zake utaweza kugundua maswala kadhaa wa kadhaa ambayo sisi nasi tunayapitia katika maisha yetu, uko wakati ambapo Daudi alikuwa laumu yaani alifanywa LAUMU au alikuwa akilaumiwa kwa njia mbalimbali na kusemwa au kufanywa kuwa mfano wa matukio mabaya na yasiyofaa, au mfano wa watu ambao Mungu ni kama alikuwa akishughulika naye au kumuadhibu,  alilaumiwa sana Daudi kiasi cha kufikia kuvunjika moyo, aliumia au kuugua sana na hakukuwa na mtu wa kumuhurumia  wala kumsaidia hatimaye aliamua kumlilia Mungu  kama msaada wake ili asaidike naye ona:-

Zaburi 69:16-20 “Ee Bwana, unijibu, maana fadhili zako ni njema, Kwa kadiri ya rehema zako unielekee. Wala usinifiche uso wako, mimi mtumishi wako, Maana mimi nimo taabuni, unijibu upesi. Uikaribie nafsi yangu, uikomboe, Kwa sababu ya adui zangu unifidie. Wewe umejua kulaumiwa kwangu, Na kuaibika na kufedheheka kwangu, Mbele zako Wewe wako watesi wangu wote. Laumu imenivunja moyo, Nami ninaugua sana. Nikangoja aje wa kunihurumia, wala hakuna; Na wa kunifariji, wala sikumwona mtu.”           

Yawezekana nawe pia unapitia hali kama ya Daudi mwana wa Yese, unalaumiwa kila mahali, unaonekana kama sababu ya mabaya yaliyotokea katika jamii,  na hivyo unalaumiwa unaweza kulaumiwa kwa sababu ya  ndoa yako kuvunjika, unaonekana kama wewe ndio sababu ya kifo cha yule mgonjwa, unaonekana kama wewe ni sababu ya migogoro, unaonekana kuwa wewe ndio sababu ya ubadhirifu, unaonekana kama wewe ndio uliye changia ajali ile kutokea, au wewe ndio sababu ya mambo kwenda vibaya, unaweza kulaumiwa kwa sababu zozote zile, lawama wanafunzi wakifeli, lawama kwaya ikiharibu, lawama mboga ikiungua, chumvi ikizidi lawama, chumvi ikipungua, lawama, sukari ikizidi lawama, sukari ikipungua, lawama kwa sababu ya anguko la mtu Fulani, lawama ya kufukuzwa kazi kwa mtu Fulani, lawama timu yako imefungwa, lawama wewe ni kocha, lawama wewe ni kiongozi, lawama lawama lawama Daudi alipoona lawama zimeuvunja moyo wake alimuomba Mungu amsaidie lakini vilevile asiruhusu yeye kuwa laumu au mithali hata kwa watu wapumbavu!, tuwapo duniani hatuwezi kukwepa lawama, lakini si kila mtu ana haki ya kutulaumu,  tutajifunza somo hili zuri kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya Laumu

·         Mambo yanayoweza kusababisha lawama

·         Usinifanye Laumu ya mpumbavu

Maana ya Laumu

Zaburi 39:7-9 “Uniokoe na maasi yangu yote, Usinifanye laumu ya mpumbavu. Nimenyamaza, sitafumbua kinywa changu, Maana Wewe ndiwe uliyeyafanya.

Neno laumu au lawama linalotumika katika maandiko hususani katika biblia ya kiebrania ambayo ndiyo iliyoleta tafasiri ya biblia kwetu upande wa agano la kale linatumika neno “CHERPAH”  kimatamshi KHER- PAW unaweza kutamka KEPAH neno hili maana yake KUZUNGUMZWA VIBAYA, KUSEMWA VIBAYA KWA SABABU FULANI, KUSEMWA KWA KULAUMIWA, KUSUKUMIZIWA LAWAMA, KUSHUTUMIWA, KUFANYWA KUWA MFANO WA TABIA MBAYA KWA, KUSEMWA VIBAYA KWA SABABU WEWE NDIO UNAEONEKANA UMESABABISHA JAMBO BAYA KUTOKEA, KUSEMWA KWA SABABU YA MATUKIO YA AIBU, KUSEMWA KWA MAKUSUDI YA KUSHUSHA NA KUHARIBU HESHIMA YAKO, KUSEMWA NA KUSHUTUMIWA KWA KUSUDI LA KUKUHARIBIA SIFA Kiingereza Shame, au reproach, Neno Reproach linatafasiriwa kama Disapproval, Kushutumiwa kwa makusudi ya kukataliwa, na hii sio kwa sababu tu ulifanya jambo baya hapana wakati mwingine hata kwa sababu ya ubora au uzuri au mafanikio au muonekano wako, kutokana na mvuto mkubwa ulionao na jinsi jamii inavyokukubali au wanavyokubali huduma yako na kazi zako na nyimbo zako na lolote lile unalolifanya, wako watu kwa sababu zao moyoni wanaweza kutafuta namna ya kukulaumu tu, wanatafuta cha kusema kwa kusudi la kukuharibia sifa ambazo Mungu amekupa

Mfano Luka 23:35-39 “Watu wakasimama wakitazama. Wale wakuu nao walikuwa wakimfanyia mzaha, wakisema, Aliokoa wengine; na ajiokoe mwenyewe, kama ndiye Kristo wa Mungu, mteule wake. Wale askari nao wakamfanyia dhihaka, wakimwendea na kumletea siki, huku wakisema, Kama wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi, ujiokoe mwenyewe. Na juu yake palikuwa na anwani; HUYU NDIYE MFALME WA WAYAHUDI. Na mmoja wa wale wahalifu waliotungikwa alimtukana, akisema, Je! Wewe si Kristo? Jiokoe nafsi yako na sisi.”

Unaona lawama wakati mwingine inakuja tu kwa sababu ya wivu, Yesu hakuwa amefanya lolote baya lakini alilaumiwa, alishutumiwa alidhihakiwa na kukosolewa hata mtu aliyekuwa anasulubiwa pamoja naye alisema kama wewe ndiye Masihi basi jiokoe nafsi yako na sisi pia, hii ilikuwa ni lawama, siku ya mateso yake Yesu alilaumiwa, alilaumiwa kwa mambo mengi ya uongo, alilaumiwa kwa nukuu mbaya kutoka katika mahubiri yake, alilaumiwa kuwa alisema anaweza kulijenga katika siku tatu! na lawama nyingine nyingi zikiwa na makusudi ya kumvunjia heshima, kumdhihaki, kumuaibisha, kumfedhehi,  na kuharibu sifa zake aonekane mbaya, hafai na anatahili kuuawa

Je umewahi kukwepa maisha ya lawama? Mimi sijawahi kuyakwepa, lakini sio hivyo tu wakati mwingine hata sisi wenyewe huwalaumu watu wengine na kuwaona kama wao ndio sababu  ya kushindwa kwetu, mume anaweza kumlaumu mkewe kwa sababu ya tabia za watoto, watoto wanaweza kuwalaumu walimu kwa sababu ya kufeli kwao, na walimu pia wanaweza kuwalaumu wanafunzi kwa kusingizio kuwa ni wazito, lawama ziko kila mahali, Kanisani, katika ndoa, kazini, na hata ukiwa rais wa nchi watu watalaumu, maisha yakiwa magumu wanaweza kudhani kuwa wewe ndio sababu, hata ukiwa waziri wa Nishati umeme ukikatika watu wanaweza kukulaumu na hata kukutukana wakisema tayari waziri keshatuzimia umeme, katika maisha haya ni lawama lawama lawama, kukwepa maisha ya lawama kwa kiyunani ni ANEPILEPTONblameless, kutokushutumiwa au kulaumiwa!  Jambo hilo sio jepesi hata kidogo tuwapo duniani, tutalaumiwa sana jambo hili ni jambo la kawaida tu na hupaswi kuvunjika moyo!

Mambo yanayoweza kusababisha lawama.

Lawama ni tabia ya kibinadamu, lawama haitakuja iishie mpaka tunapoondoka Duniani, Hata mwanadamu anapofariki dunia watu wengi sana huuliza sababu ya kifo chake na kitu fulani kitabebeshwa lawama ya kifo hicho, maralia, presha, sukari, HIV, ajali uzembe, ujinga na kadhalika lazima kitakuwepo kitu cha kubebeshwa lawama ndipo mwanadamu aweze kupumua, mwanadamu hawezi kusikia Amani mpaka apate kitu cha kukisingizia, na kukipa lawama, mwanadamu analaumu ili kujisikia nafuu,  kutupia lawama wengine ni tatizo la kiroho na kisaikolojia ni njia ya kutafuta unafuu, Nini kinaweza kusababisha lawama?

Lawama ilijitokeza kwa mara ya kwanza kabisa baada ya anguko la Mwanadamu katika bustani ya Edeni Mara baada ya Mungu kuhoji sababu ya anguko la mwanadamu na kwanini Adamu na Eva walijificha walimpomsikia  ona

Mwanzo 3:9-13 “BWANA Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi? Akasema, Nalisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha. Akasema, Ni nani aliyekuambia ya kuwa u uchi? Je! Umekula wewe matunda ya mti niliyokuagiza usiyale? Adamu akasema, Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala. BWANA Mungu akamwambia mwanamke, Nini hili ulilolifanya? Mwanamke akasema, Nyoka alinidanganya, nikala.”

Kila mwanadamu mwenye upungufu, huwa anatafuta kujazilizia udhaifu wake kwa kutafuta visingizio, wanadamu wote katika uchanga wao na udhaifu wao hawako tayari kubeba lawama za wengine, marazote watu hutafuta wa kulaumu, ni wanadamu wachache sana ambao wanaweza kukubali kubeba adhabu au kuwajibika kwaajili ya watu wengine, ukomavu wa juu zaidi wa kiroho unatupeleka katika kiwango cha kufunika lawama za wengine na sisi kuwa mstari wa mbele katika kukubali kuzibela lawama. Bwana wetu Yesu ni kielelezo cha kubeba lawama sio za wanafunzi wake tu na lawama zetu zote wakati wote amekubali kuwajibika kwaajili yetu hata mbele za baba yake ona:-

Mathayo Luka 22:50-51 “Mmoja wao akampiga mtumwa wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio la kuume. Yesu akajibu akasema, Mwe radhi kwa hili. Akamgusa sikio, akamponya.”

Yesu hakutaka moja ya wanafunzi wake bila shaka (Petro) alaumiwe na kuwajibishwa kuwa alimkata mtu sikio na badala yake aliomba radhi kwa niaba yake na kumponya mtu aliyekatwa sikio, huku ni kuwajibika kwa kiwango kikubwa na cha juu zaidi katika hali ya ukomavu wa mtu wa rohoni, aidha alipokuwa Msalabani hakutaka kuwalaumu Askari kwa kitendo cha kumsulubisha na badala yake alijitishwa lawama na kuwaombea msamaha kwa baba yake!

Lawama nyingine tunaweza kusababisha sisi wenyewe kwa sababu ya makosa yetu na dhambi zetu Mfano Daudi alipofanya dhambi na Bathsheba Nabii nadhani alimweleza wazi kuwa kosa lake linaweza kuwapa adui zake na adui za Bwana sababu ya kulaumu/kukufuru ona

2 Samuel 12: 13-14Daudi akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa. Lakini, kwa kuwa kwa tendo hili umewapa adui za Bwana nafasi kubwa ya kukufuru, mtoto atakayezaliwa kwako hakika yake atakufa.”

Unaona  Neno kukufuru linalotumika hapo Kiebrabia ni NAATS  ambalo maana yake umewapa kudhihaki, umewapa kutukana umewapa kusema vibaya umewapa sababu za kulaumu,  unaona hapo ni kutokana na makosa aliyokuwa ameyafanya hapa, watu walipata nafasi ya kulaumu au kukufuru, watu hawakumlaumu Daudi tu bali walimlaumu na Mungu wake kwa sababu Mungu alijivunia Daudi kuliko mtu mwingine yeyote alisema nimemwona Daudi mwana wa Yese mtu anayeupendeza moyo wangu, wakati mwingine kwa sababu ya neema na rehema za Mungu zilizo juu yetu na wakati mwingine kwa sababu ya uhusiano wetu ulio karibu sana na Mungu adui wanaweza kupata sababu ya kulaumu, uko wakati wanaweza kutafuta hata namna ya kukuchafua ili mradi tu wapate sababu ya kukulaumu, hata hivyo Daudi alikuwa mtu wa toba alikwisha tubu na Mungu alikubali kumsamehe lakini kwa kuwa adui zake hawajui njia za Mungu ni wajinga ni wapumbavu hawajui njia za Mungu Yeye alimuomba Mungu asimfanye kuwa laumu ya mpumbavu.

Tuwapo duniani hatuwezi kukwepa lawama kwa sababu yako mambo mengi sana tunayoweza kuyafanya au kufanyiwa, kusababisha au kusababishiwa lawama, kuishi kwa kukwepa lawama sio jambo jepesi hata ukijifungia sana ndani watu wanalaumu kuwa unajitenga na watu,  na kwa bahati mbaya sasa wako watu wengine kama ilivyokuwa kwa Daudi wanaongoza kwa kulaumiwa, wakati mwingine unaweza kulaumiwa hata bila ya sababu na wakati mwingine kwa sababu, Daudi alikuwa anapitishwa na Mungu katika shule Fulani ili aweze kuwa bora zaidi, katika wakati huo wa mapito yake alikuwa akilaumiwa kila sehemu na kila mahali mpaka akazidiwa na lawama, naye aligundua kuwa anapaswa kumuomba Mungu kwaajili ya lawama anazokutana nazo, alihesabu kuwa ni Mungu ameruhusu yeye awe lawama na anamuomba Mungu asimfanye kuwa lawama  alimsihi Mungu mara kadhaa asimuache akawa lawama wala asiabike, Mungu hatakuacha ulaumiwe hata milele tangu zamani Mungu alikuwa amekusudia kumkomboa mwanadamu kutoka katika lawama, lawama zinazotokana na sisi, au jamaa zetu wanaotuzunguka  ama lawama za aina yoyote ile, lawama ni alama ya madhaifu kibinadamu.

Usinifanye Laumu ya mpumbavu

Kwa nini Daudi alimuomba Mungu asimfanye kuwa Laumu ya Mpumbavu? Daudi jambo la kwanza Kabisa alikuwa akimlilia Mungu ili kwamba mapito anayoyapitia yasifikiriwe kuwa anapita kwa sababu yeye ni mwenye dhambi, Daudi anamuomba Mungu kuwa ni wachache sana wanaomjua Mungu wanaoweza kuzielewa njia za Mungu na kujua sababu ya mapito yake, lakini wengi na hasa watu wajinga na wapumbavu wanaweza wasielewe njia za Mungu na hivyo wanaweza kufikiri kuwa Mungu anamfanya Daudi kuwa somo la mtu aliyeivunja torati  na hivyo Mungu anamnyoosha au anamfanyia kama mtu mwenye dhambi au kama mtu ambaye hajasamehewa! Au mtu ambaye Mungu ameondoa mkono wake kwake, au mtu ambaye Mungu anaona hasira juu yake, badala yake yeye ni mtu mwenye kibali kwa Mungu Zaburi 39:8 “Uniokoe na maasi yangu yote, Usinifanye laumu ya mpumbavu.”

Mpumbavu ni mtu ambaye kwa mujibu wa maandiko hana hekima au ufahamu kuhusu njia za Mungu, au mtu ambaye amekataa maarifa au mtu asiyemcha Mungu Mithali 1:7 “Kumcha Bwana ni chanzo cha maarifa, Bali wapumbavu hudharau hekima na adabu.”  Mpumbavu ni mtu asiyemjua Mungu au hata kuamini kuwa Mungu yupo, Zaburi 14:1-3 “Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu; Wameharibu matendo yao na kuyafanya chukizo, Hakuna atendaye mema. Toka mbinguni Bwana aliwachungulia wanadamu, Aone kama yuko mtu mwenye akili, Amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pamoja, Hakuna atendaye mema, La! Hata mmoja.” Mpumbavu pia anaweza kuwa mtu aliyeamini lakini hazijui njia za Mungu!

Wapumbavu ni watu wenye dhambi, wasiomcha Mungu watu wenye sifa mbaya, wenye kutenda machukizo, wasiotenda mema, wasio na akili, wasiomtafuta Mungu, au waliopotoka hawa hueneza lawama kwa kusudi la kumshutumu Mungu kupitia udhaifu wa kibinadamu, walio nao watumishi wake, Mungu ni baba kwetu uhusiano wetu na baba hakuna anayeweza kuuvunja, kwani we inakuuma nini Baba wa nyumba ya jirani akiwa anamuadhibu mwanaye?  Kuadhibiwa kwa Daudi na Mungu hakukuwa na maana kuwa Mungu hakuwa amesamehe dhambi zake bali Mungu alikuwa na kusudi la kutengeneza nidhamu kwa Daudi, Mungu alikuwa anashughulika na mtoto wake lilikuwa ni jambo jema sana kwani alitakiwa kufa lakini hata adhabu ya kifo ilifutwa, dhambi yake ilifutwa lakini Mungu alimuingiza katika shule ya Nidhamu tu, Mungu alikuwa anamkemea Daudi asirudie kufanya madudu, Mungu alikuwa anamkumbusha kuwa mnyenyekevu, anamkumbusha kutikutumia madaraka yake vibaya, anamkumbusha kuwa anaye baba wa kimbingu ambaye hataruhusu Israel iwe na wafalme wanaofanana na wafalme wa dunia hii

Waebrania 12:6-11 “Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi, Naye humpiga kila mwana amkubaliye. Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Basi kama mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu ninyi, wala si wana wa halali. Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi? Maana ni hakika, hao kwa siku chache waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye kwa faida yetu, ili tuushiriki utakatifu wake. Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.”        

Wakristo pamoja na watumishi wa Mungu wanaaswa katika maandiko, kutokuwa laumu, au wasiwe wenye kulaumiwa hata pamoja nakuishi katika ulimwengu huu wenye kizazi cha ukaidi na kilichopotoka ona

1Timotheo 3:2 “Basi imempasa askofu awe mtu asiyelaumika, mume wa mke mmoja, mwenye kiasi na busara, mtu wa utaratibu, mkaribishaji, ajuaye kufundisha;” 

Wafilipi 2:14-15 “Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”           

Katika nyakati zetu ni muhimu zaidi kuwa na maombi kama ya Daudi ya kumsihi Mungu asituifanye kuwa laumu kwa wapumbavu  na pia kwa wenye hekima, ni muhimu kuomba maombi kama haya kama hayajawahi kukuta Mshukuru Mungu lakini wenzako mara kadhaa watu wasio na nia njema wametutafuta sana ili watuchafue wapate cha kulaumu, Lakini ashukuriwe Mungu kwa neema yake ametutunza, Lakini nasema kama ilivyo kwa Daudi maombi yake yalikuwa ni muhimu sana  na yanatufunza kitu cha ziada katika nyakati zetu, Hii ni dua yangu na ninakuombea na wewe Mungu akutunze usiwe na lawama katika maisha yako na huduma ambayo bwana ameiweka ndani yako, waimbaji, wahubiri, viongozi, na wasanii pamoja na watumishi wote wa Mungu na wakristo kwa ujumla mtu asitulaumu!, Mungu amtunze kila mmoja wetu ili kwamba asipatikane mtu wa kutulaumu kwa habari ya utumishi wetu kwa Mungu, na kwa habari ya karama hii tunayoitumikia, kama tutakuwa na nidhamu na Munu ametufunza nidhamu kamwe Bwana hatatuacha tuangukie katika lawama za wapumbavu,

2Wakorintho 8:20-21 “Tukijiepusha na neno hili, mtu asije akatulaumu kwa habari ya karama hii tunayoitumikia; tukitangulia kufikiri yaliyo mema, si mbele za Bwana tu, ila na mbele ya wanadamu.”

Wapumbavu, tukitoa pepo watasema tunatoa kwa mkuu wa pepo, wapumbavu tukifanikiwa watasema sisi ni freemason, wapumbavu ukipitia changamoto mbalimbali wanasema tuna dhambi, hawajui njia za Mungu!, Daudi alikuwa na uhusiano na Mungu kama mtu na baba yake na Mungu alikuwa ameahidi kuwa akikosea atashughulika naye mtu mpumbavu hawezi kuelewa Daudi aliomba kwamba asifanyike laumu ya mpumbavu, mtu asiyeelewa njia na uhusiano alionao Daudi na Mungu

2Samuel 7:14-15 “Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu; akitenda maovu nitamwadhibu kwa fimbo ya binadamu na kwa mapigo ya wanadamu; lakini fadhili zangu hazitamwondoka, kama vile nilivyomwondolea Sauli, niliyemwondoa mbele yako.”

Daudi au mwana wa Daudi awaye yote anaposhughulikiwa na Mungu mpumbavu na anyamaze, kwani haimaanishi kuwa Mungu ameondoa fadhili zake, kwa mtumishi wake lakini baba yuko kwenye chuo cha Nidhamu na mtumishi wake

 1Wakorintho 11:32 “Ila tuhukumiwapo, twarudiwa na Bwana, isije ikatupasa adhabu pamoja na dunia.” Katika kiingereza mstari huu unasomeka hivi 1Corinthians 11:32 “But when we are judged by the Lord we are being disciplined so that we will not be condemned with the worldkwa msingi huo Mtu wa Mungu anapopita katika majaribu ni Mungu mwenyewe ndiye anayejua kwanini anapitia hayo, labda Mungu anampa mtu shule ya nidhamu ili asihukumiwe na watu wa dunia au kama watu wa dunia hii, Hivyo Daudi alikuwa na uelewa kuwa anapitia njia ngumu lakini bado ana uhusiano mzuri na Mungu, na hivyo wasio haki wanyamaze kimya hawana hadhi ya kumlaumu Daudi, Ndugu yangu Hakuna mtu mwenye hadhi ya aina yoyote ile mwenye haki ya kuinua mdomo wake kuhusu maisha yako, mtu akikushutumu ajue wazi kuwa hana haki, wala hadhi ya kuinua kinywa chake kuhusu maisha yako, Mungu sio wa mtu Fulani tu Mungu ni Mungu wa wote wenye mwili, ninapochapwa na baba yangu wewe inakuhusu nini, kila mmoja na familia yake na kila famuilia na sharia zake, mwache kuwashutumu wengine kama hamuwaombei, wala kuwashauri, wala kuwatakia Amani, kwani hakuna mtu awaye yote ajuaye uhusiano wako na Mungu, siri ya mapito yako iko kati yako wewe na baba yako wa mbinguni, USINIFANYE LAUMU YA MPUMBAVU!

 

Na Rev. Innocent  Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima


Hakuna maoni: