Jumapili, 27 Aprili 2025

Kwa maana wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya mtoto!


Mathayo 2:19-21 “Hata alipofariki Herode, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto huko Misri, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mamaye, ushike njia kwenda nchi ya Israeli; kwa maana wamekufa walioitafuta roho ya mtoto. Akaondoka akamchukua mtoto na mamaye, akafika nchi ya Israeli.”



Utangulizi:

Malaika wa Bwana alimwambia Yusufu maneno haya alipokuwa akali akiishi Misri, mahali alikokuwa ameelekezwa kwaajili ya kwenda kumficha mtoto Yesu baada ya kutafutwa kuuawa na Mfalme Herode mkuu, kwa hofu ya kutokutaka kuwepo kwa mfalme mpya wa Wayahudi, tabia ya Herode ilikuwa ni matokeo ya wivu wake na mpango wa kishetani wa kutaka kuharibu mpango na mapenzi ya Mungu kwaajili ya ukombozi wa mwanadamu kwa kutaka kumuua Yesu. Somo hili ni maonyo kwa watu wote wasio na mapenzi mema kwa kazi na mpango wowote wa Mungu, Mungu yuko tayari kuulinda mpango wake na makusudi yake kwa gharama yoyote ile, na hakuna mtu awaye yote anayeweza kuwa bora kuliko mpango na makusudi ya Mungu!

Mathayo 2:13 – 14 “Na hao walipokwisha kwenda zao, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize. Akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku, akaenda zake Misri;”

Herode ambaye alitafuta kumuangamiza Yesu alikuwa amekwishakufa, Yesu alipaswa kukulia Nazareth katika inchi ya Israel inchi ya utumishi wake na aliyekuwa kipingamizi cha mpango huo alikuwa ameondolewa na Bwana mwenyewe hivyo Kristo angetekeleza mapenzi ya Mungu bila kizuizi, katika inchi ya Israel kwa sababu hiyo sasa malaika wa Bwana anatoa wito wa wao kurejea huku akiweka bayana sababu za kurejea ni kuwa wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya mtoto!

Mathayo 2:22-23 “Lakini aliposikia ya kwamba Arkelao anamiliki huko Uyahudi mahali pa Herode babaye, aliogopa kwenda huko; naye akiisha kuonywa katika ndoto, akasafiri pande za Galilaya, akaenda, akakaa katika mji ulioitwa Nazareti; ili litimie neno lililonenwa na manabii, Ataitwa Mnazorayo.”

Tutajifunza somo hili “Kwa maana wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya mtoto” kwa kuzingatia vipengele viwili vifuatavyo:-

 

·         Hatari ya kuzuia mpango wa Mungu.

·         Kwa maana wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya Mtoto.

 

Hatari ya kuzuia mpango wa Mungu

Ni muhimu kufahamu kuwa hakuna jambo baya na la hatari sana duniani kama kujaribu kuzuia mapenzi ya Mungu au Mpango wa Mungu, mtu awaye yote wa mamlaka ya aina yoyote ile ambaye atasimama kuzuia kusudi la Mungu au kujaribu kusimamisha mpango wa Mungu juu ya kile alichokikusudia Mungu anajiweka katika hatari isiyoweza kusimulika, kuzuia makusudi ya Mungu wakati wowote na kwa sababu zozote zile ni kuingia katika mfumo wa Mungu. Mfalme Herode mkuu kwa ujumla hakufurahia taarifa za kuzaliwa kwa Masihi ambaye kimsingi ni mfalme wa wayahudi, na badala yake alianza mipango mikakati ya kutaka kumuua Yesu na kuharibu mpango wa Mungu wa ukombozi kwa mwanadamu, Kiburi cha kibinadamu na ulevi wa madaraka ulimfanya mfalme huyu mjinga kujifikiri ya kuwa yeye ni Muhimu kuliko mpango wa Mungu, na kwa akili zake ndogo alifanikiwa kusababisha misiba kwa wamama wa Bethelehemu waliokuwa na watoto wadogo chini ya miaka miwili.

Mathayo 2:3-8 “Basi mfalme Herode aliposikia hayo, alifadhaika, na Yerusalemu pia pamoja naye. Akakusanya wakuu wa makuhani wote na waandishi wa watu, akatafuta habari kwao, Kristo azaliwa wapi? Nao wakamwambia, Katika Bethlehemu ya Uyahudi; kwa maana ndivyo ilivyoandikwa na nabii, Nawe Bethlehemu, katika nchi ya Yuda, Hu mdogo kamwe katika majumbe wa Yuda; Kwa kuwa kwako atatoka mtawala Atakayewachunga watu wangu Israeli. Kisha Herode akawaita wale mamajusi faraghani, akapata kwao hakika ya muda tangu ilipoonekana ile nyota. Akawapeleka Bethlehemu, akasema, Shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha kumwona, nileteeni habari, ili mimi nami niende nimsujudie.”

Mathayo 2:16-18 “Ndipo Herode, alipoona ya kuwa amedhihakiwa na wale mamajusi, alighadhabika sana, akatuma watu akawaua watoto wote wanaume waliokuwako huko Bethlehemu na viungani mwake mwote, tangu wenye miaka miwili na waliopungua, kwa muda ule aliouhakikisha kwa wale mamajusi. Ndipo lilipotimia neno lililonenwa na nabii Yeremia, akisema, Sauti ilisikiwa Rama, Kilio, na maombolezo mengi, Raheli akiwalilia watoto wake, Asikubali kufarijiwa, kwa kuwa hawako.”

Mipango ya Herode na mikakati yake na kughadhibika kwake kunaonyesha Dhahiri nia ya moyo wake ilikuwa ni kuuufutilia mbali kabisa mpango wa Mungu, ni ujinga ulio wazi kuwa Herode aliweza hata kuita wakuu wa makuhani na kuuliza kuwa masihi anazaliwa wapi na akaelezwa kwa mujibu wa maandiko, lakini alikuwa amefanya upumbavu mkubwa sana kwani nadhani alipaswa pia kuwauliza makuhani hao hao kuwa kuna madhara gani anaweza kuyapata mtu anayejaribu kuzuia mapenzi ya Mungu?  Na neno la Mungu lingemjibu hivi:-

Isaya 14:26-27 “Hilo ndilo kusudi lililokusudiwa duniani mwote, na huo ndio mkono ulionyoshwa juu ya mataifa yote. Maana Bwana wa majeshi amekusudia, naye ni nani atakayelibatili? Na mkono wake ulionyoshwa, ni nani atakayeugeuza nyuma?

Ayubu 9:4 “Yeye ni mwenye hekima moyoni, na mwenye uwezo katika nguvu; Ni nani aliyejifanya kuwa mgumu juu yake, naye akafanikiwa?

Wakati wote, mahali popote na saa yoyote kila mtu wa Mungu ni lazima ahahakikishe kuwa linapokuja swala ambalo ni mapenzi ya Mungu, sisi kamwe tusiwe sababu ya kuharibu au kuzuia mpango huo kwani kwa kufanya hivyo tunaweza kujikuta tunapingana na mapenzi ya Mungu jambo ambalo ni hatari na linaweza kuleta madhara makubwa sana, tuache kiburi na kujifikiri ya kuwa sisi ni maalumu sana, umaalumu wetu unaweza kuwa na maana kama tuko kwaajili ya kutimiza mpango wake, lakini umaalumu wetu unaweza kupotea ikiwa tu tunasimama kama kizuizi cha ule mpango halisi wa Mungu neno linaonyeshqa huwezi kuwa mgumu kwa mapenzi ya Mungu kisha ukatoboa! 

Matendo 5:38-39 “Basi sasa nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu.”

Maandiko yanaonya vikali swala zima la kujaribu kushindana na mapenzi ya Mungu, onyo linatolewa kuwa kama kazi imetokana na binadamu inaweza kuvunjwa lakkini ikiwa imetokana na Mungu huwezi kuvunja  na kinyume chake mtu utakuwa unajiingiza kwenye mfumo wa Mungu, nakumbushia kuwa Mungu habadiliki, Mungu yule yule wa agano la kale ndiye huyu huyu wa Agano jipya, Rehema zake zinadumu hata kizazi na kizazi kwa wamchao, lakini jicho lake li juu ya watenda mabaya aliondoe kabisa kumbukumbu lao duniani.

Zaburi 34:15-16 “Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake hukielekea kilio chao. Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya, Aliondoe kumbukumbu lao duniani.”

 

Kwa maana wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya Mtoto

Herode alikuwa moja ya wafalme ambaye alishindana na kusudi la Mungu kuhusu Maisha ya Yesu, alikuwa anataka kumwangamiza, alisahahu kujifunza kutoka kwa Farao ambaye mara kadhaa alikuwa akikataa mpango wa Mungu wa kuwaachilia wana wa Israel waende katika nchi iliyokusudiwa na Mungu na matokeo yake Taifa la Misri lilipatwa na mapigo mazito yaliyosababisha hasara kubwa kwa Farao na raia wake na mwishoe msiba wa wazaliwa wote wa kwanza  wa binadamu na wanyama uliwapata Misri nzima na kama haitoshi Farao na majeshi yake wote walifutwa na Mungu katika bahari ya shamu, na hakukuweko mtu aliyesalia hata kupeleka habari ya kile kilichowakuta!

Yeye ni mwenye akili moyoni, na mwenye nguvu nyingi, ni nani aliyemwasi naye akasalimika? Herode aliyaasi mapenzi ya Mungu na hivyo uwezo wake wa kuwa salama uliondolewa, kumbukumbu lake duniani lilifutwa, huwezi kuufunga mpango wa Mungu kwa vizuizi vya kibinadamu, Herode aliyatafuta sana maisha ya Yesu Kristo Mwana wa Mungu ili kuyaangamiza na kwa dhamiri mbaya kabisa aliangamiza watoto wengi kule Bethelehemu ili yamkini ikiwezekana miongoni mwao awe ni Bwana wetu Yesu Kristo, Nini kilimtokea Herode maandiko yanaeleza tu kuwa alikufa ona:-

Mathayo 2:19-21 “Hata alipofariki Herode, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto huko Misri, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mamaye, ushike njia kwenda nchi ya Israeli; kwa maana wamekufa walioitafuta roho ya mtoto. Akaondoka akamchukua mtoto na mamaye, akafika nchi ya Israeli.”

Hata hivyo Maandiko hayajaelezea kwa kina yaliyomkuta Herode, lakini kwa taarifa za Mwandishi maarufu wa kihistoria  wa karne ya kwanza Myahudi Flavius Josephus  anaelezea kuwa mara baada ya kuagiza askari kuwaua watoto wadogo wasio na hatia kwa kusudi la kummaliza na Yesu, kule Bethelehemu Mfalme huyo aliandamwa  na maumivu makali sana yasiyokoma, kujinyonga kwa utumbo mwembamba na kupata maumivu makali sana, kubanwa na pumzi mfano wa mtu mwenye pumu, maumivu makali katika kila sehemu ya mwili wake, mashambulizi makali ya figo, kumomonyoka kwa seli za mwili wake (gangrene) na maambukizi mabaya katika via vyake vya uzazi, kwa maelezo ya Mwanahitoria huyu nguli wa kiyahudi anaeleza kuwa pia siku zake za mwisho akiwa na mashaka makubwa sana aliuwa baadhi ya watoto wake wa kiume kwa hofu kuwa wangeweza kumpindua, na  mwisho aliagiza kuwa wakamatwe viongozi muhimu wa kiyahudi na serikali yake na kuamuru kuwa wauawe siku atakayokufa akiwa na mashaka kuwa hakuna mtu atakayeomboleza msiba wake kwa vile alivyokuwa katili, kwa nini haya yalimkuta Herode? Kutokana na kupingana na mapenzi ya Mungu na Mungu alimfutilia mbali ili mpango wa ukombozi kupitia Yesu Kristo uweze kukaa katika njia yake na mapenzi ya Mungu yaweze kusimama!

Hitimisho:

-          Hakuna mwanadamu anaweza kuzuia mpango wa Mungu hata siku moja iwe ndani ya mtu au katika agenda za Mungu  nay ale ambayo watumishi wake manabii wamesema

-          Mungu ataendelea kuweka ulinzi dhidi ya wale anaowatumia kwa mapenzi yake, na kujaribu kuwaharibu au kuharibu kitu cha Mungu kilichomo ndani yao ni kujiweka katika wakati mbaya wa kuharibiwa wewe na Mungu mwenyewe, Mungu huangalia maslahi yake mapana zaidi kuliko tamaa zako finyu, na kutaka kwako kujijengea umaarufu acha kabisa kushindana na makusudi ya Mungu na mpango wake.

-          Mungu akikugundua kuwa wewe ni kikwazo kwaajili ya kazi yake atakuondoa kwa wakati wake ili mpango wake uweze kutimia, Maneno haya wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya mtoto  yanadhihirisha wazi kuwa Mungu alisimamamia kifo cha Herode ili mpango wake na agenda yake ndani ya Yesu Kristo iweze kuendelea, Siku zote Mungu ataondoa kila kikwazo kinachosimama mbele ya watoto wake  ili makusudi yake yaweze kutimia, do not mess-up with the G.O.D of Israel, usimkosee Mungu wa Wayahudi hata siku moja 

 

-          Kutoka 14:13-14 “Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. BWANA atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya.”

 

-          Tunajifunza kuwa Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa neema wanyenyekevu

 

Yakobo 4:6 Lakini hutujalia sisi neema iliyozidi; kwa hiyo husema, Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.”

Mtu yeyote anayezuia mapenzi ya Mungu na kazi ya Mungu na makusudi ya Mungu hatadumu Mungu ana mwisho wa kila Herode anayeitafuta roho ya mtoto aiangamize, ikiwa uko katika mpango wa Mungu usiogope, kwani wanaoyatafuta maisha yako ili kuyaharibu wanaharibu ya kwao na kwa ghafla kama ilivyokuwa kwa Herode kiburi chao kitafikia mwisho.               

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Ijumaa, 25 Aprili 2025

Uwezo wa kuwakubali wengine!


Filemoni 1:9-15 “lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia. Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye zamani alikuwa hakufai, bali sasa akufaa sana, wewe na mimi pia; niliyemtuma kwako, yeye mwenyewe, maana ni moyo wangu hasa; ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili. Lakini sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari. Maana, labda ndiyo sababu alitengwa nawe kwa muda, ili uwe naye tena milele;”




Utangulizi:

Moja ya kitabu ambacho kinazungumzia vizuri huduma nzima ya wokovu pamoja na upatanishi ni pamoja na kitabu cha Filemoni, Katika kitabu hiki ambacho kinaunganisha watu wakuu watatu, Onesmo ambaye ni mkosaji, Filemoni aliyekosewa na Paulo mtume kama mpatanishi,Paulo mtume ambaye anasimama kama mpatanishi hapa anamtaka Filemoni amkubali Onesmo ambaye alimkosea hapo awali na sasa amejirekebisha baada ya kukutana na Yesu Kristo akiwa gerezani, somo kubwa tunalojifunza hapa ni kuwa je mtu aliyekukosea, au aliyekosea anapokuwa amejirudi, je unaendelea kumuhesabu kama mhalifu? Au utamkubali? wako baadhi ya wapendwa ambao kama mtu alikosea wakati Fulani basi wataendelea kumuhesabu kama mhalifu miaka yake yote na hawako tayari kuachana na stori za zamani kuhusu maisha ya mtu na badala yake wanatumiwa na Shetani kuendelea kugandamiza watu wa Mungu ambao maisha yao yamebadilika. Msimamo wa aina hiyo unapingana kabisa na uwezo na utendaji wa Mungu ambaye hubadilisha maisha ya watu siku hadi siku kwa kadiri watu hao wanavyokubali kujiachia katika neema ya Mungu iwezayo kubadilisha na maisha yetu sote. 

 

1Timotheo 1:12-16 “Nami namshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenitia nguvu kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu, akaniweka katika utumishi wake; ingawa hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri, lakini nalipata rehema kwa kuwa nalitenda hivyo kwa ujinga, na kwa kutokuwa na imani. Na neema ya Bwana wetu ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi. Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.”


Maisha ya kiroho ni Mchakato, ambao unahitaji uvumilivu, ikiwa ni pamoja na kuwavumilia watu ili wabadilike na tena waokolewe na tena wakue kiroho na tena na kuwasamehe na kuamini katika nguvu ya Damu ya Yesu yenye uwezo wa kubadilisha watu, Paulo ni mdau na mfano wa mchakato wa mabadiliko hayo,  katika kitabu cha Filemoni leo yako mambo ya kujifunza kuhusiana na swala hilo hasa kwa mabadiliko aliyoyapata mtumwa wa Filemoni aliyeitwa Onesmo ambaye, Mungu alimuokoa na kuyabadili maisha yake kabisa, tutajifunza somo hili Uwezo wa kuwakubali wengine kwa kuzingatia vipengele vinne vifuatavyo:-

 


·         Wajibu wa Mkristo anapokosewa

·         Kuendeleza uwezo wa kusamehe

·         Kuendeleza uwezo wa kuwakubali wengine

·         Kuendeleza uwezo wa kupenda kama Yesu

 


Wajibu wa Mkristo anapokosewa

Filemoni 1:10-18 “Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye zamani alikuwa hakufai, bali sasa akufaa sana, wewe na mimi pia; niliyemtuma kwako, yeye mwenyewe, maana ni moyo wangu hasa; ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili.Lakini sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari. Maana, labda ndiyo sababu alitengwa nawe kwa muda, ili uwe naye tena milele; tokea sasa, si kama mtumwa, bali zaidi ya mtumwa, ndugu mpendwa; kwangu mimi sana, na kwako wewe zaidi sana, katika mwili na katika Bwana. Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe. Na kama amekudhulumu, au unamwia kitu, ukiandike hicho juu yangu.”

Onesmo alikuwa ni mtumwa wa Filemoni, Nyakati za Biblia karne ya kwanza kumiliki watumwa kwa watu waliokuwa na uchumi mkubwa lilikuwa ni swala la kawaida, na Onesmo alikuwa ni Mtumwa wa Filemoni, Mtumwa huyu hakuwa mwaminifu na pia alikuwa hajaokoka, hivyo alimtoroka Filemoni na kukimbia mbali huku akimwibia Filemoni na kumsababishia hasara ya fedha nyingi katika wakati ule mtumwa alikuwa ananunuliwa kwa dinari 500, dinari moja kwa kawaida ni sawa na Shilingi za Tanzania  8,575.29/- kwa hiyo Dinari mia 500 ni sawa na shilingi 4,287,645/- kwa hiyo licha ya fedha alizoiba Onesmo yeye mwenyewe alikuwa ni ghali kwa kiwango cha milioni nne na laki mbili na mia sita arobaini na tano za mwaka 1952, hukumu ya mtumwa aliyekimbia katika utawala wa Kirumi ilikuwa ni kifo, Lakini hata hivyo mtumwa huyu aliwekwa gerezani,  na kwa neema ya Mungu lilikuwa ni gereza lile lile alilokuwa amefungwa Paulo mtume, kwa hiyo Paulo alimuhubiri Kristo kwa mfungwa huyu na kumlea kiroho gerezani na akapokea badiliko kubwa sana, Sasa mfungwa huyu alikuwa amepata nafasi ya kutoka na kukubali kurejea kwa Filemoni, na ndipo Paulo anamwandikia Filemoni ili aweze kumsamehe! Je ungelikuwa ni wewe ungeweza kumsamehe? Kukoseana ni jambo la kawaida katika maisha haya, ni ukweli ulioko kama tu sisi nasi tunavyomkosea Mungu mara kadhaa, Lakini hata hivyo kwa upande wa Binadamu uwezo wetu na degree (Viwango) zetu na mitazamo yetu inatofautiana sana  je Neno la Mungu linatuelekeza nini mtu anapokukosea?

Mathayo 18:7 “Ole ni wa ulimwengu kwa sababu ya mambo ya kukosesha! Maana hayana budi kuja mambo ya kukosesha; lakini ole wake mtu yule aliletaye jambo la kukosesha!

Luka 17:1-3 “Akawaambia wanafunzi wake, Makwazo hayana budi kuja, lakini ole wake mtu yule ambaye yaja kwa sababu yake! Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa wadogo hawa. Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe.”

Biblia haiungi mkono watu kukoseana lakini inaonya pia wale wenye kukosesha hata hivyo kwa watu wa Mungu tunapaswa kusamehe, hatupaswi kuwa kama watu wa ulimwengu huu au wale wa jicho kwa jicho na jino kwa jino, sisi tunapaswa kuhakikisha kuwa Mungu anatukuzwa kwa namna yoyote ile pale watu wanapotukosea, kwa hiyo Onesmo alikuwa amebadilika, injili ilikuwa imembadilisha na Paulo namuomba Filemoni sasa ampokee Onesmo kwa sababu sasa amebadilika, tunajifunza kuwa tunapaswa kuwa na Rehema na kuwakubali tena watu waliowahi kufanya makosa kana kwamba hawajawahi kukosea kwani hivyo ndivyo Mungu anavyotufanyia na sisi pale tulipokuwa tumewahi kumkosea

Isaya 43:25 “Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe, wala sitazikumbuka dhambi zako.”

Mathayo 5:38-41 “Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino; Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili. Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili.”

Jifunze kuachilia, jifunze kuwa kama Mungu, jifunze kuwakubali kwa upya watu waliokosea na wakajirekebisha, wahesabie kuwa ni wenye kufaa sana kuliko mwanzo, Paulo anaonyesha kuwa Onesmo sasa anamfaa sio tu Filemoni hata na yeye na kama isingelikuwa ni mtumwa wake huenda yeye angemchukua ili amtumikie katika vifungo vyake.  

     

Kuendeleza uwezo wa kusamehe

Filemoni 1:10-12 “Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye zamani alikuwa hakufai, bali sasa akufaa sana, wewe na mimi pia; niliyemtuma kwako, yeye mwenyewe, maana ni moyo wangu hasa;”

Kusamehe ni moja ya tabia ya Kikristo, Paulo mtume hapa anaonyesha umuhimu mkubwa na uwezo wake wa kusamehe, na kuonyesha kuwa ana moyo sio wa kusamehe tu bali wa kukubali  na kuwahurumia wengine, anamuombea Msamaha Onesmo, lakini yeye anamkubali kama mwanae aliyemzaa huko gerezani na anasema huyu ni moyo wake hasa, kumbuka ni vigumu sana kwa wachungaji wa leo na wakristo wa leo kumkubali mtu aliyewahi kukosea kwa kiwango kama hiki, Je unaweza kumuita mkosaji aliyetubu na kubadilika na kusema huyu ni moyo wangu hasa? Wakati mwingine tunakosa huruma na kuwakandamiza wengine kupitia makosa waliyowahi kuyafanya, na kuyahubiri kwa kukandamiza ili yamkini wasikubalike tena, wengi wetu ni kama hatuamini katika mchakato wa Mungu kubadilisha mtu aliyekosea, ni muhimu kukumbuka kuwa damu ya Yesu Kristo iliyomwagika kwa wokovu iko rahisi sana kumsafisha aliyeokolewa na akakosea, Mkristo aliyekomaa kiroho ana uwezo wa kuendeleza moyo wa kusamehe na kumuhesabu mwingine kuwa yuko sawa kama hajawahi kukosea, Onesmo hakuwa tatizo tena kwa Paulo mtume Lakini kazi ilikuwa kwa Filemoni, je ataweza kumkubali tena mtumwa yule aliyemuingizia hasara?  Paulo kwa waraka huu anauandaa moyo wa Filemoni kuendeleza uwezo wa kusamehe, tusiwe na uchungu tena, tuwe na huruma na tusamehe.

Waefeso 4:31-32 “Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya; tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.”

Kama tumeamua kumfuata Kristo, basi ni lazima kuuiga moyo wake, yeye hakuwa mnafiki kama tulivyo leo, leo hii unaweza hata usikaribishwe katika makanisa Fulani kwa sababu tu wana historia yako ya nyuma kwamba uliwahi kukosea na pengine wala hawajawahi kuthibitisha kama yalikuwa makosa hasa, pengine hata ulichafuliwa tu, lakini watu wakakushikia bango kana kwamba wana funguo za mbinguni, dini leo zimejaa watu wanafiki wakubwa sana ambao wamejaa ufarisayo wakimuhubiri Kristo huku wakiwafungia watu mlango huo huo wa Yesu Kristo kwa mioyo yao mizito isiyotaka kuachilia, Paulo Mtume alikuwa tofauti na anamshihi Filemoni ambaye pia alimzaa kiroho na kanisa lilikuwa katika nyumba yake kwamba yeye asiwe mfano wa hao bali ampokee Onesmo, Paulo anasema hata kama unamdai Yeye yuko tayari kulipa, Petro alimkana Yesu mara tatu, lakini jambo la kushangaza ni kuwa Yesu alipofufuka mtu wa kwanza kumtaja miongoni mwa wanafunzi wake ilikuwa ni Petro tena kwa agizo la malaika

Luka 22:54-62 “Wakamkamata, wakamchukua, wakaenda naye nyumbani kwa Kuhani Mkuu. Na Petro alimfuata kwa mbali. Na walipokwisha washa moto katikati ya kiwanja, waliketi pamoja, naye Petro akaketi kati yao. Ndipo mjakazi mmoja akamwona ameketi mwangani, akamkazia macho akasema, Na huyu alikuwa pamoja naye. Akakana, akisema, Ee mwanamke, simjui. Baadaye kitambo mtu mwingine alimwona akasema, Wewe nawe u mmoja wao. Petro akasema, Ee mtu, si mimi. Halafu, yapata saa moja, mtu mwingine alikaza kusema, Hakika na huyu alikuwa pamoja naye, kwa kuwa yeye pia ni Mgalilaya. Petro akasema, Ee mtu, sijui usemalo. Na papo hapo alipokuwa katika kusema, jogoo aliwika. Bwana akageuka akamtazama Petro. Petro akalikumbuka lile neno la Bwana jinsi alivyomwambia, Leo kabla hajawika jogoo utanikana mara tatu. Akatoka nje akalia kwa majonzi.”

Marko 16:6-7 “Naye akawaambia, Msistaajabu; mnamtafuta Yesu Mnazareti, aliyesulibiwa; amefufuka; hayupo hapa; patazameni mahali walipomweka. Lakini enendeni zenu, mkawaambie wanafunzi wake, na Petro, ya kwamba awatangulia kwenda Galilaya; huko mtamwona, kama alivyowaambia.”

Kwa nini unadhani Yesu aliwaagizia malaika kuwaambia wale wanawake kuwa wakawaambie wanafunzi wake na Petro pia ingawa Petro alikuwa amemkana Yesu mara tatu? Hii inatufundisha kuwa Yesu alimwamini Petro, alimpenda na hakuyahesabu yaliyotokea nyuma kuwa ni kitu cha kushikilia na sasa anaenda mbali zaidi anampa majukumu ya kulisha kondoo zake, jambo kama hili linaweza kufanywa na watu au watumishi wenye moyo mkubwa kama wa Yesu au Paulo mtume watu waliozoezwa kusamehe wengine na kuwaamini kwa upya!

Yohana 21:15-17 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu. Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.”

Maandiko yameamuru kusamehe pale mtu anapokosea na kutubu, na ni muhimu kwetu kuwaamini tena kama Mungu amewaamini tena wewe ni nani usiyewaamini, wakati mwingine tunaweza kukaza shingo zetu kuwakataa kwa sababu ya wivu na uchanga wa kiroho, wako watu kwa uchanga wao hufikiri kuwa wengine hawana mchango tena kwa mwili wa Kristo, wanadhani kama mioyo yao ilivyo ya kifarisayo  basi na Yesu yuko hivyo hivyo, hii ni roho ya kujihesabia haki.

Wakolosai 3:12-13 “Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi.  Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”


Kuendeleza uwezo wa kuwakubali wengine

Filemoni 1:15-17. “Maana, labda ndiyo sababu alitengwa nawe kwa muda, ili uwe naye tena milele; tokea sasa, si kama mtumwa, bali zaidi ya mtumwa, ndugu mpendwa; kwangu mimi sana, na kwako wewe zaidi sana, katika mwili na katika Bwana. Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe.”

Wakati Onesmo alipokuwa anatoroka alikuwa mwenye dhambi, mhalifu na mtumwa, Lakini alipokuwa anarejea sasa ni Mtakatifu na ndugu katika Bwana ni zaidi ya mtumwa anamfaa Filemoni na anamfaa Paulo Mtume, Paulo anamuomba Filemoni amkubali, Paulo anataka Filemoni aendeleze uwezo wa kuwakubali wengine, Je wewe unaweza kumkubali? Mtu aliyekosea na sasa amerudi kwako upya?  Kama wakristo tunapaswa kuwa na moyo wa kuwakubali wengine bila kujali yaliyotokea nyuma katika historia yao, Hakuna kiwango cha kusema unamkubali huyu na huyu unamshusha chini kidogo kwa sababu eti alikuwa hivi au vile kumbuka mfano wa mwana mpotevu

Wagalatia 3:28-29. “Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu. Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.”

Luka 15:25-32 “Basi, yule mwanawe mkubwa alikuwako shamba na alipokuwa akija na kuikaribia nyumba, alisikia sauti ya nyimbo na machezo. Akaita mtumishi mmoja, akamwuliza, Mambo haya, maana yake nini? Akamwambia, Ndugu yako amekuja, na baba yako amemchinja ndama aliyenona, kwa sababu amempata tena, yu mzima. Akakasirika, akakataa kuingia ndani. Basi babaye alitoka nje, akamsihi. Akamjibu baba yake, akasema, Tazama, mimi nimekutumikia miaka mingapi hii, wala sijakosa amri yako wakati wo wote, lakini hujanipa mimi mwana-mbuzi, nifanye furaha na rafiki zangu; lakini, alipokuja huyu mwana wako aliyekula vitu vyako pamoja na makahaba, umemchinjia yeye ndama aliyenona. Akamwambia, Mwanangu, wewe u pamoja nami sikuzote, na vyote nilivyo navyo ni vyako. Tena, kufanya furaha na shangwe ilipasa, kwa kuwa huyu ndugu yako alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana.”                

Ni Imani yangu kuwa utakuwa ka ma Paulo mtume na utakuwa kama Filemon wao bila shaka walimkubali Onesmo, lakini kama wewe hukubali huna tofauti na yule mwana mkubwa ambaye alikasirika wakati baba yake alipompokea mwana wake aliyekuwa amepotea, endeleza uwezo wa kuwakubali wengine. Paulo mtume alitaka Onesmo apokelewe na Philemoni kana kwamba Filemoni anampokea Paulo Mtume hii ni kiwango cha juu sana cha kukubaliwa kwa Onesmo!


Kuendeleza uwezo wa kupenda kama Yesu

Filemoni 1:4-7 “Namshukuru Mungu wangu sikuzote, nikikukumbuka katika maombi yangu; nikisikia habari za upendo wako na imani uliyo nayo kwa Bwana Yesu na kwa watakatifu wote; ili kwamba ushirika wa imani yako ufanye kazi yake, katika ujuzi wa kila kitu chema kilicho kwetu, katika Kristo. Maana nalikuwa na furaha nyingi na faraja kwa sababu ya upendo wako, kwa kuwa mioyo ya watakatifu imeburudishwa nawe, ndugu yangu.”

Filemoni 1:21 “Kwa kuwa nakuamini kutii kwako ndiyo maana nimekuandikia, nikijua ya kuwa utafanya zaidi ya hayo nisemayo.”

Paulo alikuwa anamfahamu Filemoni kama lilivyo jina lake maana ya jina PHILEMON  maana yake Mpendwa/Mpenzi Filemoni alikuwa mwanafunzi wa Paulo Mtume alikuwa vizuri kiuchumi kulikuwa na Kanisa nyumbani mwake alikuwa ni mtumishi wa Mungu alikuwa na upendo sana lakini pia alikuwa mtii kwa Paulo mtume, kwa hiyo Paulo hakuwa na shaka juu ya agizo lake kupokelewa na kukubalika kwa Onesmus, Filemoni alikuwa na uwezo huo, wako watumishi hawana uwezo wa kupokea mtu aliyekosea lakini wako watumishi wenye uwezo mkubwa wa kutokuhukumu na kuwapokea kwa mikono miwili wale waliokosea na kuwahesabu kuwa wanastahili, tendo la aina hii linaendeleza na kukuza uwezo wa kupenda kama Yesu Kristo, Yesu alitupenda pasipo sababu, tunapokuwa na upendo kwa wengine bila kujali walifanya nini na historia yao ya nyuma ikoje tunaendeleza kile ambacho Kristo alifanya kwetu, maisha ya aina hiyo ni zaidi ya injili.

1Yohana 2:9-11Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa. Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru, wala ndani yake hamna kikwazo. Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza, tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha macho.”

Ikiwa katika moyo wako kuna mtu unamchukia basi unajiumiza mwenywe, haujiweki katika nafasi ya kufurahia msamaha na upendo wa Mungu unabaki gizani, kwa hiyo jipime sana na jichunguze kama uko katika upendo wa kweli na kama hauna siku nzuri na saa nzuri ya kuanza ni sasa, anza kujenga mazoezi ya kupenda nje ya mipaka ya kawaida kama Yesu Kristo aliagiza kuwapenda maadui zetu, iweje tushindwe kuendeleza kuwapenda wale tu waliokosea zamani na sasa hawako kama zamani tena? Paulo alimkubali sana Onesmo, na alikuwa anamuamini Filemoni kwamba angeliweza kabisa kubeba agizo la waraka wake kwa kumkubali Onesmo na kumuhesabu kama ndugu

Filemoni 1:8-20 “Kwa hiyo, nijapokuwa nina ujasiri katika Kristo kukuagiza likupasalo; lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia.    Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye zamani alikuwa hakufai, bali sasa akufaa sana, wewe na mimi pia; niliyemtuma kwako, yeye mwenyewe, maana ni moyo wangu hasa; ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili. Lakini sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari. Maana, labda ndiyo sababu alitengwa nawe kwa muda, ili uwe naye tena milele; tokea sasa, si kama mtumwa, bali zaidi ya mtumwa, ndugu mpendwa; kwangu mimi sana, na kwako wewe zaidi sana, katika mwili na katika Bwana. Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe. Na kama amekudhulumu, au unamwia kitu, ukiandike hicho juu yangu. Mimi Paulo nimeandika kwa mkono wangu mwenyewe, mimi nitalipa. Sikuambii kwamba nakuwia hata nafsi yako. Naam, ndugu yangu, nipate faida kwako katika Bwana; uniburudishe moyo wangu katika Kristo.”

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Ijumaa, 18 Aprili 2025

Ufahamu kuhusu njia ya Msalaba! (Via Dolorosa)


1Wakorintho 1:18-24 “Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, Na akili zao wenye akili nitazikataa.Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu? Kwa maana katika hekima ya Mungu, dunia isipopata kumjua Mungu kwa hekima yake, Mungu alipenda kuwaokoa waaminio kwa upuzi wa lile neno linalohubiriwa. Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani wanatafuta hekima; bali sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulibiwa; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa Wayunani ni upuzi; bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu.”




Utangulizi:

Leo ni siku ya ijumaa kuu, wakristo wote nchini wanaungana na wakristo wenzao duniani kuadhimisha na kukumbuka Mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo na kuuawa kwake msalabani kwaajili ya ukombozi wa wanadamu kulikotokea huko Yerusalem zaidi ya miaka 2000 iliyopita, Katika siku hii ya leo nataka kuzungumzia Ufahamu kuhusu njia ya Msalaba.

Huenda wewe umewahi kusikia au kuhusika kwa namna moja ama nyingine katika ibada iitwayo ibada ya njia ya Msalaba! Na huenda umewahi kujiuliza ibada hii ni ibada ya namna gani, asili yake ni nini na je ni mapokeo au ni mafundisho ya kibiblia, ina kweli gani na ina dosari gani ni mambo gani mazuri tunaweza kujifunza kutoka katika ibada hii, yepi ya kibiblia na yepi sio ya kibiblia, kwa wakristo wa makanisa ya kikatoliki na Anglican ya High Church njia ya msalaba inaweza kuwa sio kitu kigeni, Hususani katika wakati ule wa Kwaresma na katika siku ya leo ya ijumaa kuu – Kwaresma maana yeke ni (40), lakini kwa makanisa ya kipentekoste inaweza kuwa kitu kigeni, vyovyote iwavyo vile kuna mambo ya kujifunza kwa kila mmoja wetu uwe ni mpentekoste au mkatoliki na muanglikan na wengineo, yako mambo ambayo Roho Mtakatifu anataka tujifunze kwa msingi huo basi Leo basi Mwalimu Mkuu Mungu Roho Mtakatifu ametupa neema ya kujifunza maswala muhimu katika ibada hii ya njia ya msalaba na tutajifunza kwa kina na mapana na marefu kwa kusudi tu la kuelewa yale yaliyoko katika njia ya msalaba na kufaidika. Kwa ufahamu na maarifa. Tutajifunza somo hili Ufahamu kuhusu njia ya msalaba kwa kuzingatia vipengele vinne vifuatavyo:-

 

·         Historia ya njia ya Msalaba.

·         Mafundisho Muhimu katika njia ya msalaba.

·         Mambo yasiyo ya kibiblia katika njia ya Msalaba.

·         Faida ya mafundisho ya njia ya Msalaba.

 

Historia ya njia ya Msalaba

Ni muhimu kufahamu kuwa ibada ya njia ya msalaba asili yake ilitokana na ibada ya kutafakari kwa kina na kujifunza maswala mbali mbali kuhusu mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo tangu alipohukumiwa na Pilato hadi wakati alipokufa Msalabani na alipozikwa, ibada hii huadhimishwa kwa kirefu aidha wakati wa Kwaresma (40) ama wakati wa sikukuu ya ijumaa kuu, Katika wakati huo watu waliomwamini Yesu hujumuika kwa pamoja katika kujifunza na kutafakari Mateso ya Yesu na hivyo kujiimarisha kiroho, kiimani,toba na kiufahamu, wakati wa kutafakari mateso hayo lakini lengo kuu likiwa ni kupandikiza fundisho hilo Muhimu kuhusu kuteswa kusulubiwa na kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo fundisho ambalo ni msingi mkuu wa ukombozi wa Mwanadamu, na Imani yetu, kwani kama Kristo asingelisulubiwa na kufa na kufufuka katika wafu Imani yetu ingelikuwa ni bure.

1Wakorintho 15:13-20 “Lakini kama hakuna kiyama ya wafu, Kristo naye hakufufuka; tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwetu ni bure na imani yenu ni bure. Naam, na sisi tumeonekana kuwa mashahidi wa uongo wa Mungu; kwa maana tulimshuhudia Mungu ya kuwa alimfufua Kristo, ambaye hakumfufua, ikiwa wafu hawafufuliwi. Maana kama wafu hawafufuliwi, Kristo naye hakufufuka. Na kama Kristo hakufufuka, imani yenu ni bure; mngalimo katika dhambi zenu. Na hapo wao nao waliolala katika Kristo wamepotea. Kama katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi tu maskini kuliko watu wote. Lakini sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala.”

Ibada hii ilianza mnamo karne ya 4 baada ya Yesu Kristo, kama matokeo ya wakristo waliokuwa na tabia ya kutembelea Yerusalem na kupita katika njia ile halisi aliyopitia Yesu Kristo kutoka jumba la hukumu la Anthonio akielekea Golgotha au Kalvari mahali ambako alisulubiwa, wakristo hao wa kale walikuwa na tabia ya kutembelea Yerusalem (Kufanya hija) na kupita hatua kwa hatua na kusimama katika kila eneo la kihistoria kwa kutafakari kujifunza na kufanya maombi kwa kukumbuka mateso ya Yesu Kristo.

Moja ya watu mashuhuri waliokuwa wakifanya ibada hii na baadaye kuyatambua maeneo hayo muhimu ya mateso ya Yesu ni pamoja na mama wa Mfalme Constantine aliyejulikana kama Malkia Hellena ambaye alikuwa ni Mkristo kabla ya mwanae kumuamini Bwana Yesu Baadaye.

Mnamo karne ya 13-14 watawa wa Kifransisko (Franciscans) walipewa jukumu la kuyahifadhi maeneo hayo ya njia ya Msalaba huko Yerusalem chini ya utawala wa Sultan wa Ottoman 1342 na wao walifanya kazi hii ikiwa ni pamoja na kuieneza ibada hii katika maeneo mbali mbali ya ulaya, mpaka karne ya 18 Papa Clement XIV alikubali kupitisha vituo 14 rasmi katika ibada hii ya njia ya msalaba vinavyotambulika mpaka leo, hata hivyo baadhi ya wakristo waliongeza kituo cha 15 kuzungumzia kuhusu kufufuka kwa Yesu na wengine huona kuwa wakati ibada ya njia ya msalaba hufanyika ijumaa kuu, basi kituo cha 15 kinaweza kuadhimishwa sikukuu ya pasaka. Vituo tisa tu kati ya vituo vile 14 ni matukio ya kweli ya kibiblia wakati vituo vitano 5 matukio yake si ya kibiblia bali yanatokana na masimulizi ya kale yaliyoaminiwa na watu kwa miaka na kwa taarifa za kimapokeo.

Ibada hii ya njia ya Msalaba ilipewa umuhimu mkubwa katika nyakati za pasaka kwa sababu ilikuwa ikiwasaidia wakristo kupata nafasi ya kutafakari kwa undani mateso ya Yesu Kristo kama njia ya kujiimarisha kiimani katika maisha ya kiroho. Katika lugha ya kilatini njia hii ya Msalaba inajulikana kama “Via Dolorosa” kwa kiingereza “Sorrowful Way” au “Way of Suffering” au “The Painful Path” yaani njia ya huzuni au njia ya mateso, au njia ya maumivu, hapa tunaiita njia ya msalaba, njia hii iko katika mji wa zamani wa Yerusalem na inaaminika njia hiyo ndiyo ile aliyoipitia Yesu kuelekea mahali alikosulubiwa.

Isaya 53:3 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; MTU WA HUZUNI NYINGI, AJUAYE SIKITIKO; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu.”  


Mafundisho Muhimu katika njia ya msalaba

Kutokana na mwamko mkubwa wa kiinjili tulio nao leo, Njia ya msalaba inaweza kuonekana kuwa ni ibada ya kimapokeo, lakini ukiichunguza kwa undani utaweza kugundua kuwa kulikuwa na nia njema ya kutaka kuwafundisha watu kwa kina sana kuhusu mateso ya Yesu Kristo, japo kutokana na ufinyu wa kiufahamu uliokuwako nyakati hizo, na upungufu mkubwa wa Elimu na maarifa ya wakati ule, uwezo wa kufikisha mafundisho hayo ulikuwa duni, na wa kitoto hata pamoja na kuhusisha picha, lengo kuu lilikuwa halijafikiwa na sasa Roho Mtakatifu aliniamuru kuwa wakati wa kuweka sawa fundisho hili kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho umewadia nami kwa neema ya Mungu niliyopewa kama mkuu wa wajenzi ninafanya kazi hii leo ya kuliweka wazi fundisho hilo kwa maarifa yake katika msingi wa kimaandiko.

Ni ukweli ulio wazi na usiopingika kuwa katika kufuatilia yale yaliyomo katika ibada ya njia ya msalaba utaweza kugundua kuwa yako mafundisho muhimu sana na mazuri na ya kweli ya kujifunza katika maswala kadhaa lakini vile vile yako maswala machache ambayo tunaweza tusiyape kipaumbele kwa sababu hayana ushahidi wa kimaandiko na sio ya msingi kwa sababu hiyo ingawa Papa Clement XIV alikubali kupitisha vituo 14 vya kimafundisho, Mimi nitajadili vifungu tisa tu na kuweka pembeni vile visivyo na ushahidi wa kimaandiko na vilivyo na asili ya kimapokeo lakini vinakubalika katika masimulizi ya wakristo wa kale. Baada ya maelezo hayo sasa tunangalie yale tunayoweza kujifunza kutoka katika njia ya Msalaba:-


1.       Yesu Kristo Mbele ya Pilato: # 1

 

Katika eneo la kwanza tunapotafakari kuhusu mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo, utagundua hukumu iliyo mbaya zaidi kuwahi kutokea duniani, ni hukumu ya kifo kwa mtu ambaye kimsingi hakuwa na hatia, Watu, wakuu wa makuhani pamoja na Pilato waliyaacha maisha ya mtu mwenye haki kuingia hukumuni na kuuawa pasipo hatia kwa ujumla ilikuwa ni hukumu ya uonevu mkubwa usioweza kusimuliwa, hii inathuthibitishia kuwa uovu wa mwanadamu ulikuwa umefikia ngazi ya juu kabisa ambapo mtu mwema alionekana kuwa mbaya na mtu mbaya alionekana kuwa mwema, jamii ilikuwa ikishabikia uovu kuliko wema.

 

Mathayo 27:22-25 “Pilato akawaambia, Basi, nimtendeje Yesu aitwaye Kristo? Wakasema wote, Asulibiwe. Akasema, Kwani? Ni ubaya gani alioutenda? Wakazidi sana kupiga kelele, wakisema, Na asulibiwe. Basi Pilato alipoona ya kuwa hafai lo lote, bali ghasia inazidi tu, akatwaa maji, akanawa mikono yake mbele ya mkutano, akasema, Mimi sina hatia katika damu ya mtu huyu mwenye haki; yaangalieni haya ninyi wenyewe. Watu wote wakajibu wakasema, Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu.”

 

Yohana 19:6-8 “Basi wale wakuu wa makuhani na watumishi wao walipomwona, walipiga kelele wakisema, Msulibishe! Msulibishe! Pilato akawaambia, Mtwaeni ninyi basi, mkamsulibishe; kwa maana mimi sioni hatia kwake.Wayahudi wakamjibu, Sisi tunayo sheria, na kwa sheria hiyo amestahili kufa, kwa sababu alijifanya kuwa Mwana wa Mungu. Basi Pilato aliposikia neno hilo, akazidi kuogopa.”

 

Hukumu hii ya Yesu Kristo ina maswala kadhaa ya kujifunza

 

a.       Inatufundisha jinsi ambavyo Yesu asiye na hatia alivyokubali adhabu mbaya zaidi ya kwenda kufa msalabani kwaajili ya makosa yetu na dhambi zetu,- Hukumu hii ya Yesu inadhihirisha jinsi wanadamu walivyo waovu na walivyooza na kupotoka katika kutenda dhuluma, tunajifunza jinsi dhambi ilivyo mbaya na jinsi ilivyoweza kusababisha majeraha makubwa katika moyo wa mwana wa Mungu, Hata hivyo kwa sababu ya upendo wake kwa wanadamu Yesu kristo anaonekana kukubali kuiachia dhuluma ishinde.

 

Isaya 53:3-8 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote. Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake. Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu.”

 

b.      Inatufundisha jinsi Yesu alivyohukumiwa kwa makosa ya uongo.- Kimsingi hukumu hii ilikuwa ya dhuluma, isiyo ya haki na ambayo haikuzingatia sheria ya kiyahudi wala za kirumi, Mashitaka ya Yesu Kristo kwa kweli yalitolewa na watu waliokuwa wamepikwa na wakuu wa makuhani ili kutoa ushahidi wa uwongo, wala hakimu mwenyewe hakupata ushahidi wa wazi ambao ungeweza kumtia Yesu hatiani na kupelekea kupata adhabu ya kifo kibaya kuliko maelezo aidha hakukuwa na nafasi ya upelelezi wa kina kuhusu makosa anayosingiziwa Yesu Kristo badala yake kwa kupitia ushahidi wa kuunga unga tu yakafanyika maamuzi mabaya na ya kusikitisha sana !

 

Luka 23:1-4 “Wakasimama mkutano wote, wakampeleka kwa Pilato.Wakaanza kumshitaki, wakisema, Tumemwona huyu akipotosha taifa letu, na kuwazuia watu wasimpe Kaisari kodi, akisema kwamba yeye mwenyewe ni Kristo, mfalme. Pilato akamwuliza, akisema, Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi? Akajibu akamwambia, Wewe wasema. Pilato akawaambia wakuu wa makuhani na makutano, Sioni neno lililo ovu katika mtu huyu.”

 

Mathayo 26:59-61 “Basi wakuu wa makuhani na baraza yote wakatafuta ushuhuda wa uongo juu ya Yesu, wapate kumwua; wasiuone wangawa walitokea mashahidi wa uongo wengi. Hata baadaye wawili wakatokea, wakasema, Huyu alisema, Naweza kulivunja hekalu la Mungu, na kulijenga kwa siku tatu.”

 

Yohana 18:38 “Pilato akamwambia, Kweli ni nini? Naye akiisha kusema neno hilo akawatokea Wayahudi tena, akawaambia, Mimi sioni hatia yo yote kwake.”

 

c.       Tunajifunza kwamba hukumu yake ni matokeo ya wivu na uhasama na sio haki – Wakuu wa makuhani na viongozi wa dini walimuonea Yesu wivu, kwa sababu alikuwa anafanya wanafunzi wengi kuliko wao, alikuwa maarufu kuliko wao, alikuwa na huduma yenye nguvu na upako kuliko wao, alikuwa akifanya miujiza mingi na mikubwa wakati wao hawakuwa na kitu, mafundisho yake yalijaa amri na mamlaka, Yesu alikemea sana dhambi ya unafiki ambayo kimsingi ilikuwa ikiwatafuna mafarisayo na viongozi wa dini na kwa sababu hizo walifanya njama za wazi za kutaka kumuua, na ni ukweli ulio wazi kwamba  hukumu hii ya kifo likuwa ni mauaji ya makusudi na haikuwa haki.

 

Yohana 11:47-50 “Basi wakuu wa makuhani na Mafarisayo wakakusanya baraza, wakasema, Tunafanya nini? Maana mtu huyu afanya ishara nyingi.Tukimwacha hivi, watu wote watamwamini; na Warumi watakuja, watatuondolea mahali petu na taifa letu. Mtu mmoja miongoni mwao, Kayafa, aliyekuwa Kuhani Mkuu mwaka ule, akawaambia, Ninyi hamjui neno lo lote; wala hamfikiri ya kwamba yafaa mtu mmoja afe kwa ajili ya watu, wala lisiangamie taifa zima.”

 

Mathayo 23:13-16 “Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi waingie. [Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnakula nyumba za wajane, na kwa unafiki mnasali sala ndefu; kwa hiyo mtapata hukumu iliyo kubwa zaidi.] Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na akiisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa jehanum mara mbili zaidi kuliko ninyi wenyewe. Ole wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu atakayeapa kwa hekalu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga.”

 

d.      Tunajifunza ya kuwa hukumu hii ilikuwa ya kinafiki na ya uovu – kimsingi haikuwa hukumu iliyozingatia sheria wala utaratibu, Kesi iliendeshwa usiku, hii ilikuwa kinyume cha utaratibu na kudhihirisha kuwa lilikuwa swala la njama  na uovu, hakukuwa na muda wa kujitetea, kesi ilihukumiwa kwa kura, ambapo jambazi na mashuhuri Baraba aliachiwa huru na Yesu Mwalimu na mtenda miujiza alichaguliwa kufa, hakimu aligundua kuwa Yesu hakuwa na hatia lakini hakuzingatia haki kwa sababu ya hofu ya fitina za kiyahudi na kwa unafiki alitoa hati ya hukumu ya kifo.

 

Mathayo 27:16-22 “Basi palikuwa na mfungwa mashuhuri siku zile, aitwaye Baraba. Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda. Na alipokuwa ameketi juu ya kiti cha hukumu, mkewe alimpelekea mjumbe, kumwambia, Usiwe na neno na yule mwenye haki; kwa sababu nimeteswa mengi leo katika ndoto kwa ajili yake. Nao wakuu wa makuhani na wazee wakawashawishi makutano ili wamtake Baraba, na kumwangamiza Yesu. Basi liwali akajibu, akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi katika hawa wawili? Wakasema, Baraba. Pilato akawaambia, Basi, nimtendeje Yesu aitwaye Kristo? Wakasema wote, Asulibiwe.”

 

Pamoja na kuwa kuhukumiwa kwa Yesu Kristo kwa njia ya uonevu ilikuwa ni njia ya Mungu ya kuleta ukombozi wa mwanadamu, Hukumu hii inatukumbusha wajibu wa watu kuhukumu kwa haki, kuhukumu kwa kuangalia mambo juu juu kunaweza kutuletea gharama kubwa sana na kutukosesha mbele za Mungu, kitendo hiki cha kuhukumiwa vibaya kwa Yesu kinatukumbusha kuwa wakati wa kukumbuka mateso ya Bwana Yesu tunakumbushwa kuhukumu kwa haki na kuacha dhuluma na kufanya upepelezi wa kesi mbalimbali ili kupata ushahidi wa kujiridhisha na sio kukimbilia kutoa uamuzi wa haraka haraka, umewahi kujiuliza ni kwanini Baraba alikuwa amefungwa na haikuwa tatizo lakini kulikuwa na haja gani ya kutokuchelewesha hukumu ya Bwana Yesu hata kwa kifungo tu? Neno la Mungu linatutaka kama tunahukumu basi tuhukumu kwa haki.

 

Yohana 7:24-26 “Basi msihukumu hukumu ya macho tu, bali ifanyeni hukumu iliyo ya haki. Basi baadhi ya watu wa Yerusalemu wakasema, Je! Huyu siye wanayemtafuta ili wamwue? Na kumbe! Anena waziwazi, wala hawamwambii neno! Yamkini hao wakuu wanajua hakika ya kuwa huyu ndiye Kristo?

 

Tunajifunza ya kuwa Yesu Kristo ambaye alikuwa na uwezo wa kuagiza malaika waje kumuokoa na hali iliyokuwa ikimkabili alikubali kupoteza haki zake, wakati mwingine katika maisha haya ya uchaji wa Mungu tutadhulumiwa na kupoteza haki zetu, haya yanaweza kutupata na wakati mwingine wenye kukudhulumu wakawa ni wapendwa kabisa, lakini Neno la Mungu linasema ni afhadli kudhulumiwa na ni afhadhali kupoteza wakati mwingine na kule kuachilia kutatujengea heshima mbele za Mungu

 

1Wakorintho 6:6-7 “Bali mwashitakiana, ndugu kwa ndugu, tena mbele yao wasioamini.  Basi imekuwa upungufu kwenu kabisa kwamba mnashitakiana ninyi kwa ninyi. Maana si afadhali kudhulumiwa? Maana si afadhali kunyang'anywa mali zenu?

 

e.      Njia ya msalaba inatukumbusha wakristo kumuomba Mungu ili watu wema na watenda haki watawale ikiwezekana sisi wenyewe tuwepo madarakani ili kutawala kwa haki, inapendeza sana watu wenye haki wakitawala na inachukiza sana na kuleta kuugua waovu wakitawala.

 

Mithali 29:2 “Wenye haki wakiwa na amri, watu hufurahi; Bali mwovu atawalapo, watu huugua.”

 

Kanisa lina wajibu wa kuombea mihimili ya maamuzi katika inchi ili haki iweze kutendeka kila mahali, na wale walioko kwenye maamuzi wanapaswa kujifunza kuwa na ujasiri na kusimama katika haki kwa gharama yoyote ile na kutokuiga mfano wa Pilato katika hukumu hii ya ajabu aliyoifanya. Hata hivyo wote tunakumbuka kuwa ingawa Yesu alionewa katika kesi hii alionewa kwa sbabu yetu na kwaajili ya ukombozi wetu.

       

 

2.       Yesu Kristo anaubeba Msalaba: # 2

 

Kuubeba msalaba ni ishara ya kujitoa dhabihu, kujikana kujitoa sadaka, kuwa tayari kwa majaribu na taabu na masumbufu ya Imani, Msalaba ni ishara ya kuvumilia magumu na sio kubeba mizigo, ni nafasi ya kumfuata Yesu Kristo, njia zake tabia zake na utii, baada ya hukumu ya kifo iliyokuwanya uongo kutolewa Yesu alikabidhiwa Msalaba wake na kukubali kuubeba alifanya hivyo kwa hiyari na kwaajili yetu!

 

Yohana 19:15-17 “Basi wale wakapiga kelele, Mwondoshe! Mwondoshe! Msulibishe! Pilato akawaambia, Je! Nimsulibishe mfalme wenu! Wakuu wa makuhani wakamjibu, Sisi hatuna mfalme ila Kaisari. Basi ndipo alipomtia mikononi mwao ili asulibiwe; nao wakampokea Yesu. Akatoka, hali akijichukulia msalaba wake, mpaka mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, au kwa Kiebrania, Golgotha.

 

Kitendo cha Yesu Kristo kukubali kuubeba msalaba kinatufundisha jinsi ambavyo Yesu Kristo alikuwa tayari sasa kuyatii mapenzi ya baba yake, kumbuka kufa kwake msalabani ulikuwa ni mpango wa Mungu na ni mapenzi yake, kukubali kuubeba msalaba kulikuwa ni ishara ya kwanza kwamba Yesu Kristo sasa anakubaliana na mateso ambayo kimsingi haikuwa rahisi kukubaliana na njia ile aliyoipitia

 

Luka 22:41-42 “Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, akapiga magoti akaomba, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.”

 

Wafilipi 2:6-9 “ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina;”

 

Yesu kukubali kuubeba msalaba ilikuwa ni ishara ya upendo mkubwa kwa wanadamu self- sacrificial love, Yeye alikuwa tayari kuyapoteza maisha yake kwaajili yetu, alikubali kuabishwa na kuibeba fedhea ya dhambi na kuteketeza maisha yeke kwaajili ya upendo wake kwetu

 

Yohana 15:13 “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.”

 

Ni watu wachache sana duniani ambao wanaweza kukubali kutatoa maisha yao kwaajili ya wengine, kuubeba msalaba ilikuwa ni alama kubwa sana ya kuwa Yesu Kristo hakuwa na ubinafsi, wakati huu wa maadhimisho ya pasaka tunapokumbuka mateso yasiyo na kifani ya Bwana Yesu ni muhimu kukumbuka kuwa Mungu alituumba pia kwaajili ya wengine na ya kuwa mtu aliyekomaa kiroho katika ngazi ya juu zaidi ni yule ambaye yuko tayari kuyatoa maisha yake kwaajili ya wengine! Kama sio wengine kujitoa kwaajili yetu huenda tusingelikuwa hapa leo, Lakini wokovu wetu, maisha yetu na kuwepo kwetu kumetokana na watu wengine kutuvumilia na kuyatekekeza aisha yao ili sisi tuwepo!

 

Isidor Straus alikuwa moja ya wafanya biashara wakubwa sana mwenye asili ya kijerumani na alikuwa mbunge pia katika baraza la wawakilishi huko Marekani mtu huyu alikuwa tajiri mkubwa na mwenye mali nyingi sana wakati wa ajali ya meli maarufu ya Titanic ilipokuwa inazama waokoaji walitoa kipaumbele kwa watu wenye uwezo mkubwa na matajiri ili kuokoa maisha yao kwanza watu ambao walijulikana kama VIP. Katika namna ya kushangaza mfanya biashara huyu Isdor Straus aliyekuwa na uwezo mkubwa hata wa kununua Meli kama Titanic mara sita, Yeye alikataa kuokolewa na boti za uokoaji na kuomba waokolewe kwanza wanawake na watoto, Mkewe aliyeitwa Ida pia alikubali kubaki na mumewe na kukataa nafasi ya kuokolewa na boti maalumu na hivyo walikubali kufa kwa kuzama majini anaingia kwenye kumbukumbu ya watu waliokubali kufa kwaajili ya usalama wa wengine huku ni kujitoa kwa hiyari ya hali ya juu sana na kusikokuwa na ubinafsi.

 

Kuubeba msalaba kwa Bwana wetu Yesu Kristo kunatufunza hapa kwamba kila mwanafunzi wa Yesu anapaswa kuelewa kuwa tumeitwa sio kumwamini tu bali pia na kushiriki mateso kwaajili ya kusudi la Mungu, maisha yetu katika Bwana yanapaswa kuwa ni maisha ya kujitoa kwaajili ya wengina na kuwa mbali na ubinafsi.

 

Wafilipi 1:29 “Maana mmepewa kwa ajili ya Kristo, si kumwamini tu, ila na kuteswa kwa ajili yake;”

 

Kila mwanafunzi wa Yesu anapaswa kujua kuwa kuna nyakati utaubeba msalaba wake kwaajili ya wengine na kwaajili ya utii kwa Mungu wetu, kuifuta njia ya Yesu Kristo njia ya msalaba ni pamoja na kujikana na kukataa ubinafsi kwa faida yetu na ya mwili wa Kristo, mambo mengi duniani leo yangefanyika kwa weledi mkubwa kama tu watu wataacha ubinafsi na kujiangalia wenyewe na kwa kufanya hivyo neno la Mungu linatufundisha kuwa tunapoteza badala ya kuingiza.

 

Luka 9:23-25 “Akawaambia wote, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha. Kwa kuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, au kujipoteza mwenyewe?

 

Kukubali kuubeba msalaba kunatufundisha vilevile uwezo mkubwa wa kuvumilia magumu, Mungu ana makusudi na mpango wake mkubwa katika maisha ya kila mwanadamu aliyemuamini na wakati wingine Baraka hizo zimefichwa katika njia ngumu tunazozipitia, kukubali msalaba ilikuwa ni njia ya unyenyekevu ya hali ya juu sana na njia nzito ya kujifunza kuvumilia, wakati wote kuvumilia kunaleta thawabu kubwa sana thawabu zilizojificha, Yesu alistahimili mapingamizi makubwa sana  na kwa uvumilivu huo aliinuliwa juu sana

 

Waebrania 12:2-3 “tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.”

 

Tendo la Yesu kuukubali Msalaba sio tu la kihistoria lakini linatufundisha wakristo mtindo wa maisha, tunajifunza kutii mapenzi ya Mungu na kuwa waaminifu hata kufa,  Tunajifunza unyenyekevu,  tunajifunza kuvumilia (uvumilivu), na tunajifunza msamaha  na kukubali njia na mpango wa Mungu wa ukombozi wa Mwanadamu.

 

3.       Simon yule Mkirene asaidia kubeba msalaba. # 5

 

Simon Mkirene anajitokeza kama mtu aliyeshurutishwa na Askari katika kusaidia kuubeba msalaba wa Yesu; hata hivyo katika namna ya kushangaza sana Mtu huyu kwa hiyari yake alikubali kuubeba msalaba wa Yesu pamoja naye, angeliweza kukataa kwani halikuwa swala lililomuhusu, lakini alimuhurumia Yesu Kristo, na kwa jambo hili aliweza kuingia katika rekodi ya injili zinazofanana yaani “synoptic Gospel” zote kwa hiyo kuna kitu cha muhimu sana cha kutufunza katika swala zima la njia ya msalaba. Kwanza anatajwa kwa tukio lake hili katika injili zote tatu ona:-

 

a.       Mathayo 27:32 “Hata walipokuwa wakitoka, wakamwona mtu Mkirene, jina lake Simoni; huyu wakamshurutisha auchukue msalaba wake.”

 

b.      Marko 15:21 “Wakamshurutisha mtu aliyekuwa akipita, akitoka mashamba, Simoni Mkirene, baba yao Iskanda na Rufo, ili auchukue msalaba wake.”

 

c.       Luka 23:26 “Na walipokuwa wakimwondoa walimkamata mtu mmoja, Simoni Mkirene, aliyekuwa ametoka shamba, wakamtwika msalaba, auchukue nyuma yake Yesu.”

Simon huyu alikuwa ni mgeni kutoka Kirene (Cyrene) ambako kunajulikana kama Libya leo hizi zilikuwa ni pande za Afrika ya kaskazini, mtu huyu kama alikuwa myahudi basi alikuwa akiishi Afrika na huenda alipanda Yerusalem kwaajili ya maadhimisho ya pasaka, Yeye alilazimishwa kuubeba msalaba wa Yesu, Na kwa hiyari yake alikubali kwani angeweza kukataa lakini alishiriki kuubeba msalaba wa Yesu pamoja naye, kimsingi tunajifunza jinsi mtu huyu alivyokuwa tayari kushiriki taabu pamoja na wengine alimsaidia Yesu kubeba msalaba na kushiriki mateso ya wengine, kwa sababu hiyo yeye alikuwa na moyo wa kuchukuliana na mizigo ya wengine lakini pia alikuwa na uwezo wa kufurahi na wanaofurahi na kulia pamoja na wanaolia, hapa alihuzunika na kulia pamoja na Yesu Katika taabu yake.

Wagalatia 6:2 “Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo.”

Warumi 12:15 “Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao.”

Simon Mkirene licha ya kuwa mtu aliyekuwa tayari kuchukuliana mzigo na wengine, na kuwa mtu anayelia na wale waliao pia anatukumbusha wajibu wetu wa kuyashiriki mateso ya Kristo, kila mtu aliyeokolewa anapaswa kukumbuka ya kuwa tumeitwa au tumepewa sio kumwamini tu bali na kuteswa kwaajili ya Kristo, kwaajili ya njia hii ya wokovu wakati mwingine tutapata mateso na changamoto za aina mbalimbali lakini hatuna budi kukubali kupita katika njia hizo:-

Wafilipi 1:29 “.Maana mmepewa kwa ajili ya Kristo, si kumwamini tu, ila na kuteswa kwa ajili yake;”

2Timotheo 2:3-8 “Ushiriki taabu pamoja nami, kama askari mwema wa Kristo Yesu. Hakuna apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye aliyemwandika awe askari. Hata mtu akishindana katika machezo hapewi taji, asiposhindana kwa halali. Yampasa mkulima mwenye taabu ya kazi kuwa wa kwanza wa kupata fungu la matunda. Yafahamu sana hayo nisemayo, kwa maana Bwana atakupa akili katika mambo yote. Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao wa Daudi kama inenavyo injili yangu.”

Historia ya kanisa inaonyesha kuwa Mzee huyu ambaye alikubali kuyashiriki mateso ya Bwana Yesu hatimaye watoto wake yeye na familia yake waliokolewa na watoto wake wakamuamini Bwana Yesu na kuwa watu maarufu sana nyakati za Kanisa la Kwanza, watoto wa mzee Simeoni Mkirene walikuwa ni (Alexander na Rufus) Iskanda na Rufo na walikuwa wanafunzi waaminifu sana wa Bwana Yesu, tukio la mtu huyu mwenye huruma kutoka Afrika kumsaidia Yesu, kulisababisha muujiza wa yeye kuokolewa pamoja na familia yake na wakawa maarufu sana katika kanisa lakini pia walikuwa waaminifu na mama yao Rufo akawa kama mama wa wakristo wengi na mitume wengi sana baadaye akiwepo Paulo mtume ona

Warumi 16:18 “Nisalimieni Trifaina na Trifosa, wenye bidii katika Bwana. Nisalimieni Persisi, mpenzi aliyejitahidi sana katika Bwana. Nisalimieni Rufo, mteule katika Bwana, na mamaye, aliye mama yangu pia.”

Mafundisho ya njia ya msalaba hapa yanatufundisha kuwa kupitia Simeoni kwamba kila mwanadamu anapaswa kuwa na matendo ya huruma kwa wahitaji, tunaposaidia watu kwa namna na jinsi mbalimbali maana yake tunamsaidia Yesu bila sisi kujua, Ingawa Yesu peke yake ndiye mwokozi wa ulimwengu Lakini kitendo cha Simeoni kusaidia msalaba hakumfanyi yeye kuwa mwokozi bali kunamuweka yeye kuwa miongoni mwa watu wanaosaidia wengine, kuokolewa, kumpokea Yesu, kukutana na mahitaji yao na kwa sababu hiyo kushiriki kwa namna moja ama nyingine katika kuifikisha injili duniani. tunapowatendea mema wengine kwa sababu ya Imani yetu katika Kristo tunamtendea Yesu bila kujua:-

Mathayo 25:34-40 “Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu; kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia. Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? Ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.”

Aidha Simeoni Mkirene katika picha ya kinabii anatufundisha ya kuwa Mungu ataitumia Afrika katika kuitangaza injili wakati wa uchungu na mateso au wakati mgumu dunia yote itakapokuwa imeharibika kwa uovu na ukatili Mungu ataitumia Afrika kusaidia kuenea kwa injili katika siku za mwisho wakati dunia ikiwa imeharibika kwa sababu hiyo Afrika inakumbushwa kuwa tayari kuihubiri injili wakati wa uharibifu wa dunia.

4.       Huruma kwa wanawake wa Yerusalem! #  8

Akiwa katika njia ya msalaba katikati ya mateso Yesu anakutana na wanawake wa Yerusalem ambao kimsingi walikuwa wakimuhurumia kwa sababu ya mateso yake na hata kumlilia, wao walikuwa wanakumbuka mambo yote mazuri ambayo Yesu aliwatendea watu wasio na shukurani na kuwa sasa kwa wivu wanamuweka matatani wamama hawa wanalia na kuomboleza lakini inaonekana Yesu anawahurumia wao zaidi  na kuwaonya

Luka 23:27-31 “Mkutano mkubwa wa watu wakamfuata, na wanawake waliokuwa wakijipiga vifua na kumwombolezea. Yesu akawageukia, akasema, Enyi binti za Yerusalemu, msinililie mimi, bali jililieni nafsi zenu na watoto wenu. Kwa maana tazama, siku zitakuja watakaposema, Heri walio tasa, na matumbo yasiyozaa, na maziwa yasiyonyonyesha. Ndipo watakapoanza kuiambia milima, Tuangukieni, na vilima, Tufunikeni. Kwa kuwa kama wakitenda mambo haya katika mti mbichi, itakuwaje katika mkavu?

Wakati wanawake hawa wa Yerusalem wakiwa wanamsikitikia Yesu Kristo na kumuhurumia na kumuombolezea na kumlilia, Yesu ambaye wakati huu alikuwa kwenye mateso na akiwa amebeba msalaba na maumivu, Yesu anaonyesha kuyajali maisha yao hasa na maisha yao ya baadaye, ingawa alikuwa katika maumivu makali lakini alikuwa na huruma kwa kuwa alikuwa anajua yanayokuja mbeleni kama nabii, Yesu aliwaonya wanawake hao kulia na kuomboleza sio kwaajili yake bali kwaajili yao na watoto wao, Kimsingi Yesu alikuwa anaona hukumu kubwa inayokuja dhidi ya Yerusalem miaka michache baadaye na hii ilikuwa inajumuisha kubomolewa na kuvunjiliwa mbali kwa mji wa Yerusalm na Israel nzima tukio hilo lililotokea mwaka wa 70 baada ya Kristo wakati huu ikiwa ni mwaka wa 33 baada ya Kristo ukweli ni kuwa ilipita miaka 37 tu na Yerusalem ulibomolewa vibaya na watu wengi kuuawa na wayahudi kukimbilia uhamishoni wengi sana na Askari wa kirumi walipita kila mji na kila kijiji wakiua watu na kuchinja kila myahudi, ulikuwa ni wakati wa historia mbaya zaidi kuwahi kutokea, watoto wa wanawakw wale walioonywa na Yesu ndio waliokutana na hukumu ile mbaya!

Jililieni nafsi zenu na watoto wenu yalikuwa ni maonyo ya Yesu aliyekuwa katika mateso akionya juu ya watoto wa Yerusalem ya kuwa watapitia mateso makali na makubwa sana kutokana na kizazi kile kumsulubisha mwokozi, Yesu anaonya kuwa itakuwa dhiki ya hatari ambayo watu watasema heri matumbo yaliyo tasa, kuashiria huzuni kubwa itakayowapata wayahudi kwa kuona watoto wao wakiuawa, Yesu anawaonya wao kuwa tayari kwa hukumu hiyo na kuwataka kuwa afadhali watubu na kujihurumia wenyewe.

Aidha katika somo hili la njia ya msalaba tunaonywa kuwa hatupaswi tu kuhuzunika kwaajili ya kuteswa na kufa kwa Yesu Kristo badala yake tunapaswa kuwa na ufahamu kwanini alikufa na faida ya kifo chake inatuletea wokovu, huzuni kubwa na mbaya zaidi sio kwa sababu Yesu anateswa na kufa bali kama sisi tutakosa nafasi ya kuzifurahia faida za msalaba.

Yesu aliendelea kuonya kuwa ikiwa wanaufanyia hivi mti mbichi itakuwaje kwa mti mkavu,  lilikuwa ni onyo pia kuwa kama mtu mwema kama Yesu anatendewa ukatili kama ule hebu jaribu kufikiri wale wasio na toba, kama Mungu anaruhusu mateso kama haya kwa mtu mwenye haki, kutatokea nini kwa wale wasio haki.

Yesu alionya kuwa ni lazima watu watambue kuwa Mungu ni Mungu mwenye haki na atahukumu kwa dhati, na kamwe watu wasichukulie uvumilivu wake kama nafasi ya kujifanyia wanayoyataka, ni lazima tuwafundishe watoto wetu kuishi maisha ya haki na kuikulia njia ya Bwana, aidha kile alichokisema Yesu kwa wanawake wa Yerusalem alikwisha kukisema kwa kina kwa wanafunzi wake katika Mathayo 24 akiwaonya kuhusu siku za mwisho na pia kuhusu Anguko la mji wa Yerusalem.

Mathayo 24:2-12 “Naye akajibu akawaambia, Hamyaoni haya yote? Amin, nawaambieni, Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa. Hata alipokuwa ameketi katika mlima wa Mizeituni, wanafunzi wake wakamwendea kwa faragha, wakisema, Tuambie, mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini dalili ya kuja kwako, na ya mwisho wa dunia? Yesu akajibu, akawaambia, Angalieni, mtu asiwadanganye. Kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ni Kristo; nao watadanganya wengi. Nanyi mtasikia habari za vita na matetesi ya vita; angalieni, msitishwe; maana hayo hayana budi kutukia; lakini ule mwisho bado. Kwa maana taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na njaa, na matetemeko ya nchi mahali mahali. Hayo yote ndiyo mwanzo wa utungu. Wakati huo watawasaliti ninyi mpate dhiki, nao watawaua; nanyi mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu. Ndipo wengi watakapojikwaa, nao watasalitiana, na kuchukiana. Na manabii wengi wa uongo watatokea, na kudanganya wengi. Na kwa sababu ya kuongezeka maasi, upendo wa wengi utapoa.”

Kitendo cha Yesu kukutana na wanawake wa Yerusalem na kuwaonya wajililie nafsi zao na watoto wao kinatukumbusha wajibu wetu kama kanisa kuzingatia na kukumbuka maonyo yote kuhusu unabii wa siku za mwisho, tunakumbushwa kuwa tunaishi katika nyakati za hatari na kwa sababu hiyo kila mtu anapaswa  kuchukua tahadhari na kujikumbusha kuwa kanisa hatuko salama na badala yake ni jukumu la kila mkristo kujitazama na kujihami na kuzipima roho/mafundisho ya watumishi wa Mungu katika nyakati hizi za hatari.

1Timotheo 4:1-2 “Basi Roho anena waziwazi ya kwamba nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani; kwa unafiki wa watu wasemao uongo, wakichomwa moto dhamiri zao wenyewe;

2Timotheo 3:1-5 “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi,wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema,wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu;wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.”

Kristo pia anatukumbusha wajibu wetu wa kuhakikisha kuwa tunajiangalia sisi wenyewe kuwa tukoje na Mungu badala ya kunyoosha vidole kwa wengine, tunafundishwa kuacha kufikiria wengine wanapopitia shida na changamoto kuwa labda huenda wana makosa makubwa kuliko yetu na badala yake tunakumbushwa kujiangalia wenyewe na kutubu kwa sababu kama wenye haki wanateseka ni zaidi sana kwa mtu asiye haki hataweza kustahimili

Luka 6:41-42 “Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii? Au, utawezaje kumwambia ndugu yako, Ndugu yangu, niache nikitoe kibanzi kilicho ndani ya jicho lako, nawe huiangalii boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe? Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe, ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi kilichomo katika jicho la ndugu yako.”

Luka 13:1-5 “Na wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichanganya damu yao na dhabihu zao. Akawajibu akawaambia, Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo.”    

Tangu zamani imekuwepo dhana Fulani ya kufikiri kuwa wale wanaopatwa na mabaya labda walikuwa waovu kuliko sisi, au wanaopatwa na ajali, Lakini Yesu anatukumbusha kuwa wao wanaweza kuwa sio waovu kuliko waliobaki na hivyo iko haja ya kuitumia nafasi tuliyo nayo ya Amani na uhai kwaajili ya toba na kujiweka tayari kwaajili ya Mungu wetu

5.       Yesu anavuliwa nguo # 10

Tunajifunza Nini Kupitia Kitendo cha Yesu Kuvuliwa Nguo Kabla ya Kusulubiwa? Kitendo cha Yesu kuvuliwa nguo kabla ya kusulubiwa ni sehemu muhimu ya mateso yake, na kina maana kubwa kiroho na kimaandiko. Tukio hili linatajwa katika Injili zote nne:

·         Mathayo 27:28, 35 – “Wakamvua nguo, wakamvika vazi jekundu.35 Walipokwisha kumsulibisha, waligawa mavazi yake, wakipiga kura; [ili litimie neno lililonenwa na nabii, Waligawa nguo zangu kati yao, na juu ya vazi langu walipiga kura.]

 

·         Marko 15:20, 24 – “Baada ya kumdhihaki, wakamvua lile joho la rangi ya zambarau, wakamvika mavazi yake mwenyewe... Wakagawana nguo zake, wakizipigia kura waone nani atakaye pata kitu gani.”

 

·         Luka 23:34 – “Yesu akasema, Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo. Wale wakagawana mavazi yake kwa kura.”

 

·         Yohana 19:23-24 – “Askari walipomsulubisha Yesu, walitwaa mavazi yake, wakayagawa mafungu manne, kila askari Fungu Lake; na lile joho lake pia. Na hilo joho halikuwa na mshono, limetengenezwa kwa kipande kimoja tangu juu hata chini. Wakaambiana, ‘Tusilikate, ila tuzipige kura tupate kujua litakuwa la nani.’ Hii ilikuwa ili andiko litimie, lililosema: Wamegawana mavazi yangu kati yao, na nguo yangu wameipigia kura.”

Maana na Mafundisho Tunayopata Kutoka kwa Kitendo hiki

a.       Utimilifu wa Unabii wa Agano la Kale- Kitendo hiki kilikuwa ni utimilifu wa Zaburi 22:18 – “Wamegawana mavazi yangu, na nguo yangu wameipigia kura.”

Hii inaonyesha kuwa mateso ya Yesu hayakuwa ya bahati mbaya bali ni sehemu ya mpango wa Mungu uliotabiriwa tangu zamani. Yesu alikuwa akiyatimiza mapenzi ya Mungu, na kila andiko alilokuwa ameandikiwa, kwa hiyo hakuna kilichotokea Msalabani ambacho kilitokea kwa bahati mbaya hii inadhihirisha wazi kuwa haya yalikuwa ni mapenzi ya Mungu.

 

b.      Yesu alihisi aibu na fedheha kwa ajili Yetu - Kuvuliwa nguo hadharani ni tendo la aibu na fedheha. Kwa Wayahudi, kuona mtu akiwa uchi hadharani lilikuwa jambo la kudhalilisha sana, kitendo cha kuwekwa uchi ni kitendo cha kuaibishwa ni tukio la kudharaulika sana, hili ndio tukio lililomtokea Adamu na Eva katika Bustani ya Edeni walipokula lile tunda walilokatazwa, wakati wote tunapotenda dhambi tukumbuke kuwa tunajiweka katika aibu na tunajivua nguo, Yesu anapovuliwa nguo anatukumbusha wajibu wetu ya kuwa ni yeye pekee anayeweza kutuvalisha vazi lililo bora, kwani pale msalabani alivuliwa nguo kwaajili ya matendo yetu, alifanywa vile kwa sababu dhambi zetu zilizowekwa juu yake na dhambi kwa kweli ni aibu mbele za Mungu.

 

Isaya 47:3 “Uchi wako utafunuliwa, Naam, aibu yako itaonekana. Nitalipa kisasi; simkubali mtu ye yote.”

 

Nahumu 3:5-6 “Tazama, mimi ni juu yako, asema Bwana wa majeshi; nami nitafunua marinda yako mbele ya uso wako; nami nitawaonyesha mataifa uchi wako, na falme aibu yako. Nami nitatupa uchafu uchukizao juu yako, kukufanya uwe mchafu, nami nitakufanya kuwa kitu cha kutazamwa kwa dharau.”

 

Isaya 53:3-5 – “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa.Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

 

Waebrania 12:2 – “tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu

 

Hii inatufundisha kuwa Yesu alikubali fedheha yetu ili sisi tupate heshima mbele za Mungu. Yesu Aliacha Kila Kitu kwa Ajili Yetu-Yesu alipovuliwa nguo, alikuwa hana kitu chochote cha kidunia. Hii inatuonyesha kuwa alijitoa kikamilifu kwa ajili ya wokovu wetu: Hili linatufundisha kuwa hakuna kitu cha kidunia kinachopaswa kutuzuia kumfuata Kristo, lakini pia tubakumbushwa ile kweli ya kuwa hatukuja duniani na kitu na tutaondoka duniani bila kitu.

 

2 Wakorintho 8:9 – “Kwa kuwa mnajua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, ya kwamba alipokuwa tajiri, alikubali kuwa maskini kwa ajili yenu, ili ninyi mpate kuwa matajiri kupitia umaskini wake.”

 

Yesu analishauri kanisa kujificha kwake kwa toba katika ulimwengu wa roho tunapotubu na kucha maovu yetu Yesu hutuvika mavazi meupe na kutuficha dhidi ya aibu yetu na kutuondoa katika mashaka

 

Ufunuo 3:17-19 “Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi. Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, na mavazi meupe upate kuvaa, aibu ya uchi wako isionekane, na dawa ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona. Wote niwapendao mimi nawakemea, na kuwarudi; basi uwe na bidii, ukatubu.”

 

Kama Mungu alivyomfunika Adamu kwa mavazi yaliyo bora katika bustani ya Edeni atatuhifadhi sisi kwa haki yake kwani yeye alifanyika dhambi ili sisi tuwe haki

 

2 Wakorintho 5:21 – “Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu ndani yake.”

Dunia ilimnyima Yesu Heshima yake yote, Lakini yeye alituheshimisha, na kutokana na kukubali kudharauliwa kwa kiwango hicho Yesu ameinuliwa juu kuliko mtu awaye yote na amekekirimiwa jina lipitalo majina yote na ameketi mkono wa kuume wa nguvu wa Mungu baba mwenyezi mbinguni.


6.       Yesu anawambwa Msalabani na kusulubiwa # 11

 

Yohana 19:16-18 “Basi ndipo alipomtia mikononi mwao ili asulibiwe; nao wakampokea Yesu. Akatoka, hali akijichukulia msalaba wake, mpaka mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, au kwa Kiebrania, Golgotha.Wakamsulibisha huko, na wengine wawili pamoja naye, mmoja huku na mmoja huku, na Yesu katikati.”

 

Yesu alifanya kazi nyingi sana za kuponya na kufundisha watu neno la Mungu lakini moja ya kazi muhimu kabisa aliyoifanya na kuikamilisha ni kufa msalabani kwaajili ya dhambi za ulimwengu kupitia njia ya kusulubiwa msalabani

 

Mathayo 1:21 “Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao.”

               

Yohana 1:29 “Siku ya pili yake amwona Yesu anakuja kwake, akasema, Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu!”

 

Pamoja na tukio hili Mateso yake, kufa kwake na kufufuka kwake msalabani, Yesu ilikuwa sio tu anapaswa kufa lakini pia analipaswa kufufuka kwaajili yetu, kitendo cha yeye kufufuka kinampa nafasi ya kuwa kuhani mkuu na mwombezi na mpatanishi kwaajili yetu huko mbinguni

 

Warumi 8:33-34 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.”

 

Warumi 4:24-25 “bali na kwa ajili yetu sisi mtakaohesabiwa vivyo hivyo, sisi tunaomwamini yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu katika wafu; ambaye alitolewa kwa ajili ya makosa yetu, na kufufuliwa ili mpate kuhesabiwa haki.”

 

Warumi 5:9-11 “Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye. Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake; zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake. Wala si hivyo tu, ila pia twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho.”

 

Kusulubiwa kwake msalabani kunatukumbusha upendo mkubwa sana wa Mungu kwa wanadamu ambapo Mungu kwa hiyari yake mwenyewe anaamua kuwakomboa wanadamu kwa adhabu aliyojipa yeye mwenyewe kwa ajili ya upendo wake kwetu

 

Yohana 3:16 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”

 

7.       Yesu Kristo anafia msalabani # 12

 

Mathayo 27:45-50. “Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa. Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha? Na baadhi yao waliohudhuria, waliposikia, walisema, Huyu anamwita Eliya. Mara mmoja wao akaenda mbio, akatwaa sifongo, akaijaza siki, akaitia juu ya mwanzi, akamnywesha. Wale wengine wakasema, Acha; na tuone kama Eliya anakuja kumwokoa. Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake.”

 

Kitendo cha Yesu Kristo kufa msalabani kinathibitisha wazi kuwa Yesu aliikamilisha kazi yote na unabii, hata alipopaza Sauti na kusema imekwisha Yesu alikuwa na maana ya kuikamilisha kazi yote aliyokuwa ameandikiwa aikamilishe, Yesu alihakikisha kuwa kila neno lililonena na Mungu limetimia na hivyo hakukuwa na unabii wowote kuhusu mateso yake ambao ulikuwa haujatimia

 

-          Kazi ya upatanisho kati ya Mungu na wanadamu ilikuwa imekamilishwa Warumi 5:10 “Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake; zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake.”

 

-          Kristo alikuwa amefanyika sadaka kamili ya dhambi kwaajili yetu Waebrania 10:10-14 “Katika mapenzi hayo mmepata utakaso, kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu. Na kila kuhani husimama kila siku akifanya ibada, na kutoa dhabihu zile zile mara nyingi; ambazo haziwezi kabisa kuondoa dhambi. Lakini huyu, alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu; tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake. Maana kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa.”

 

-      Kazi ya kuwashinda maadui wakubwa wa mwanadamu, Shetani, dhambi na mauti ilikamilishwa, kwa kifo chake msalabani alilipa deni la dhambi, na kumvua shetani enzi na mamlaka

 

Wakolosai 2:14-15 “akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo.”

 

Waebrania 2:14-15 “Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi, awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa.”

 

8.       Yesu anashushwa Msalabani # 13

 

Yohana 19:38-40 “Hata baada ya hayo Yusufu wa Arimathaya, naye ni mwanafunzi wa Yesu, (lakini kwa siri, kwa hofu ya Wayahudi), alimwomba Pilato ruhusa ili auondoe mwili wake Yesu. Na Pilato akampa ruhusa. Basi akaenda, akauondoa mwili wake. Akaenda Nikodemo naye, (yule aliyemwendea usiku hapo kwanza), akaleta machanganyiko ya manemane na uudi, yapata ratli mia. Basi wakautwaa mwili wake Yesu, wakaufunga sanda ya kitani pamoja na yale manukato, kama ilivyo desturi ya Wayahudi katika kuzika.”          

 

Kitendo cha mwili wa Bwana Yesu kushushwa kutoka msalabani na kufanyiwa maandalizi ya kuzikwa kilikuwa ni kitendo kinachotufundisha unyenyekevu mkubwa, Kumbuka yeye alikuwa ni mwana wa Mungu lakini hapa alikuwa amekufa, mtu aliyefariki dunia huwa hajimudu kabisa, anafanyiwa kila kitu anasaidiwa na wanadamu wenzake, huu ndio wakati ambapo tunawahitaji wanadamu wenzetu washughulike na sisi, wawe masikini au matajiri, tunajifunza kuwaheshimu watu na kutembea duniani kwa unyenekevu.

 

Wale waliokuja kumzika Yesu Kristo kama rafiki yao na mwalimu wao, walionyesha upendo wa kweli hata katika wakati mgumu lakini maziko makubwa ya heshima walioyafanya yanatukumbusha kuwa kila mwanadamu duniani hata kama alizarauliwa kiasi gani anapaswa kuzikwa kwa heshima zote, Yesu anatimiza unabii wa Samsoni ambaye alikataliwa na kukosa heshima alipokuwa akali hai, lakini alipofariki nduguze walikuja kuutwaa mwili wake na kumhifadhi, alidharauliwa alipokuwa hai na aliheshimiwa sana baada ya kifo chake.

 

Waamuzi 16:31. “Ndipo ndugu zake, na watu wote wa nyumba ya baba yake wakatelemka, wakamtwaa wakamchukua, wakamzika kati ya Sora na Eshtaoli, katika kiwanja cha kuzikia cha Manoa baba yake. Naye alikuwa mwamuzi wa Israeli muda wa miaka ishirini.”

 

Ingawa Yesu alishushwa kama maiti isiyokuwa na uwezo wowote yeye bado alijua kuwa atafufuka, Yesu anatufundisha kuwa kifo sio mwisho wa kila kitu, kwani liko tumaini la maisha mapya, mtu akimuamini Yesu hafi bali anapita kutoka mautini na kuingia uzimani

 

Yohana 11:25-16. “Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?

 

9.       Kristo Yesu anazikwa  Kaburini # 14

 

Tendo la kuzikwa kwa Yesu Kristo linathibitisha kuwa Yesu alikufa kweli kimwili kwaajili ya dhambi zetu, Yesu alizikwa pia kama sehemu ya kutimiza unabii kuhusu kuzikwa pamoja na waovu

 

Yohana 19:41-42 “Na pale pale aliposulibiwa palikuwa na bustani; na ndani ya bustani mna kaburi jipya, ambalo hajatiwa bado mtu ye yote ndani yake. Humo basi, kwa sababu ya Maandalio ya Wayahudi, wakamweka Yesu; maana lile kaburi lilikuwa karibu.”

 

Isaya 53:8-9 “Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu.Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala hapakuwa na hila kinywani mwake.”

 

1Wakorintho 15:3-4 “Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzo yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; na ya kuwa alizikwa; na ya kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko;”   

 

Mathayo 12:39-40 “Akajibu, akawaambia, Kizazi kibaya na cha zinaa chatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya nabii Yona.Kwani kama vile Yona alivyokuwa siku tatu mchana na usiku katika tumbo la nyangumi, hivyo ndivyo Mwana wa Adamu atakavyokuwa siku tatu mchana na usiku katika moyo wa nchi.”        

 

Tendo la kukubali kuzikwa linatufundisha unyenyekevu mkubwa aliokuwa nao Bwana wetu Yesu Kristo, unyeyekevu huu hatimaye ulimuinua sana Bwana Yesu, kimsingi tunajifunza hata kuwa njia mojawapo ya juu kabisa ya ukristo ni pamoja na unyenyekevu, unyenyekevu hutupelekea kuinuliwa juu sana na Bwana.

 

Wafilipi 2:5-8 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba.”

 

Mambo yasiyo ya kibiblia katika njia ya Msalaba.

Njia ya msalaba ni fundisho muhimu sana linalohusiana na tafakari ya kile kilichomkuta Bwana wetu Yesu Kristo wakati wa mateso yake, kutafakari kuhusu mateso ya Bwana Yesu hakutufanyi sisi kuwa na huzuni bali kunatufanya kuwa na furaka kwa sababu ndio njia iliyochaguliwa na Mungu kwa ukombozi wetu, kwa hiyo njia ya msalaba ina mambo mengi muhimu ya kutufunza kibiblia, hata hivyo kuna mambo yasiyo ya kibiblia ambayo tunaweza kuyachukulia tahadhari

-          Maandiko hayajaeleza kokote pale kwamba Yesu aliwahi kuanguka na msalaba, tunaweza kuona kuwa ni kweli Yesu alikuwa dhaifu kiasi cha kusaidiwa Msalaba wake na Simeoni Mkirene lakini swala la Yesu kuanguka na msalaba mra ya kwanza na ya pili na ya tatu halina rekodi yoyote katika maandiko na ingawa inaweza kuwa hivyo katika historia na masimulizi ya kale lakini hatuwezi kuwa na msimamo thabiti kwa sababu Biblia iko kimya kuhusu matukio hayo  kwa sababu hiyo kituo cha tatu Yesu kuanguka na msalaba mara ya kwanza  na kituo cha saba Yesu kuanguka na msalaba mara ya pili na kituo cha tisa cha Yesu kuanguka na msalaba mara ya tatu hakiwezi kujumuishwa katika fundisho la kibiblia kwa sababu hakuna mwanafunzi wa Yesu aliyeandika hilo wala waandishi wengine wala mitume hawajawahi kugusia hilo kokote, Penginepo pia hakuwezi kuwepo na fundisho zuri linalohusiana na kuanguka.

 

-          Kuhusu swala la Yesu kukutana na mama yake njiani wakati wa mateso pia linaweza kuwa na utata kwa sababu Biblia iko kimya, lakini tunao uhakika kuwa Mariamu na ndugu za Yesu zake Yesu Kristo walikuwepo wakati Yesu anasulubiwa lakini hatujaelezwa kuwa walikutana mahali fulani njiani isipokuwa kwa masimulizi ya wakristo wa nyakati za kanisa la Kwanza kwa sababu hiyo tukio hili linalotengeneza kituo cha nne  miongoni mwa wakatoliki na Anglican hatukiingizi katika fundisho la njia ya msalaba, maandiko yanaonyesha ni kama Yesu alimuona mama yake na wanafunzi wake akiwa tayari ametundikwa juu ya msalaba hata kama inawezekana mama yake aliongozana na watu waliofuatilia mateso

 

Yohana 19:26-27 “Basi Yesu alipomwona mama yake, na yule mwanafunzi aliyempenda amesimama karibu, alimwambia mama yake, Mama, tazama, mwanao. Kisha akamwambia yule mwanafunzi, Tazama, mama yako. Na tangu saa ile mwanafunzi yule akamchukua nyumbani kwake.”

 

-          Kuhusu swala la Yesu kukutana na Mwanamke aliyeitwa Veronica na kuwa mwanamke huyu alimfuta jasho lake na picha ya Yesu ikasalia katika kitambaa cha mama huyu, pia ni swala la kimapokeo na masimulizi tu na hakuna taarifa za kibiblia, aidha jina Veronica kimsingi sio jina la asili la Kiyahudi jina hilo ni la kilatini, na katika kigiriki labda jina Berenice la Ugiriki au Makedonia lingeweza kutumika, jina Veronika lina asili ya maneno mawili ya kilatini “Vera Icon” ambalo tafasiri yake ni true image kwa hiyo masimulizi kuhusu mwanamke huyu na tukio la picha ya Yesu kubaki katika kitambaa chake halina uthibitisho wa kimaandiko kwa sababu hiyo kituo cha sita kinachohusiana na uwepo wa Veronika hakina uhalali wa kimaandiko kwa hivyo kuanguka wa Yesu mara tatu, kukutana na Mariamu na kukutana na Veronica kunaingia katika kundi la mambo yasiyo ya kibiblia.

 

-          Jambo lingine ni kuwa hakuna sababu ya kutumia picha au sanamu katika kuadhimisha au kujikumbusha kuhusu njia ya msalaba kwani njia hiyo ipo kule Yerusalem na picha za kila kituo zipo kwa hiyo picha za vituo zinaweza kutumika katika kufundisha mafundisho yote ya njia ya malaba kwani siku hizi watu wanaelewa tofauti na miaka ya zamani ambapo watu wengi walikuwa hawajui kusoma na kuandika, mfano picha niliyoitumia mimi katika kielelezo hapo juu ni picha ya njia halisi hiyo aliyoitumia Yesu iitwavyo via dolorosa na njia hiyo ipo hata leo kule Yerusalem nchini Israel

 

-          Fundisho kuhusu njia ya msalaba sio la kikatoliki na Anglican pekee linauhusu mwili wa Kristo na hivyo kila Mwalimu wa neno la Mungu anaweza kulitumia kwa mafundisho sahihi na semina za pasaka katika kuwatafakarisha watu mateso na kifo cha Bwana Yesu na wakato wowote tunapotaka kutafakari au kujikumbusha kuhusu aina ya mauti na mateso aliyokutana nayo Yesu.  Kupitia fundisho hili ni Imani yangu kuwa walimu wa neno la Mungu watapata ufahamu mkubwa zaidi wa kuyaweka sawa mafundizho haya kwa njia iliyo bora zaidi katika siku za usoni.

 

Yohana 8:31-32 “Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”


Na Rev. Innocent Samuel Kamote.


Mkuu wa wajenzi mwenye hekima.