Jumapili, 24 Agosti 2025

Basi sasa unipe mlima huu!


Yoshua 14:12-13Basi sasa unipe mlima huu, ambao Bwana alinena habari zake siku hiyo; kwani wewe ulisikia siku hiyo jinsi Waanaki walivyokuwa huko, na miji ilivyokuwa mikubwa yenye boma; yumkini yeye Bwana atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza watoke nje, kama Bwana alivyonena. Yoshua akambarikia, akampa Kalebu, huyo mwana wa Yefune, Hebroni kuwa urithi wake.”



Utangulizi:

Leo tutakuwa na muda wa kutafakari sehemu mojawapo muhimu ya kitabu cha Yoshua katika kifungu cha Yoshua 14:6-13, ambapo kimsingi tunaweza kupata mafundisho ya kushangaza sana tunayoyapata kutoka kwa Kalebu mmoja wa wapelelezi 12 waliotumwa na Musa kuichunguza nchi ya Kanaani. Ni jambo la kushangaza kwamba Mungu hakuwa amemsahahu mtu huyu sawasawa na ahadi yake aliyompatia kwa kinywa cha Musa mtumishi wake, kimsingi wakati mwingi sana ulikuwa umepita na sasa Kalebu ana miaka 85 lakini bado anaonyesha imani thabiti kwa Mungu, uvumilivu na ukakamavu na kama mtu mwenye subira kubwa na tumaini la maisha asiyekata tamaa, ambapo licha ya muda mrefu kuwa umepita anaikumbushia ile ahadi, huku akiwa tayari kuipambania haki yake aliyoahidiwa na Mungu, baada ya watu wengine wote kuogopa kuingia katika nchi ya Mkanaani na kupambana na majitu yaliyokuwa yanaimiliki nchi hiyo na Mungu akamuahidi Kalebu na Yoshua.

Hesabu 14:28-31 “Waambieni, Kama niishivyo, asema Bwana, hakika yangu kama ninyi mlivyonena masikioni mwangu, ndivyo nitakavyowafanyia ninyi; mizoga yenu itaanguka katika jangwa hili, na wote waliohesabiwa miongoni mwenu, kama jumla ya hesabu yenu, tangu waliopata umri wa miaka ishirini na zaidi, hao walioninung'unikia, hakika yangu hamtaingia ninyi katika nchi, ambayo niliinua mkono wangu ya kwamba nitawaketisha humo, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni. Lakini Watoto wenu, ambao mlisema watakuwa mateka, ndio nitakaowaleta na kuwatia ndani, nao wataijua nchi ninyi mliyoikataa.”

Tutajifunza ujumbe huu muhimu “Basi sasa unipe mlima huu” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Sababu za ahadi ya Mungu kwa Kalebu na Yoshua.

·         Basi sasa unipe mlima huu.

·         Mambo ya kujifunza kutoka kwa Kalebu.


Sababu za ahadi ya Mungu kwa Kalebu na Yoshua.

Ni muhimu kufahamu kwanza ni kwanini Mungu aliwapenda na kuwaahidi Kalebu na Yoshua kwamba watairithi nchi ya Kanaani tofauti na wenzao miongoni mwa wapelelezi 12 waliotumwa na Musa kuipeleleza nchi ya Kanaani, ili tuweze kujifunza kutoka kwake na kuwa na moyo kama wa Kalebu na Yoshua hatimaye nasi tuweze kuzifurahia Baraka za Mungu. Kalebu na Yoshua walikuwa ni askari waaminifu na watiifu kwa Mungu, wote walikuwa wametokea Misri katika nchi ya utumwa wakiwa vijana wadogo, na walipata bahati ya kuchaguliwa miongoni mwa wapelelezi 12 waliotumwa kuipeleleza nchi ya Kanaani zoezi la upelelezi lilichukua siku 40, waliporejea walitoa taarifa kwa Musa nao walikiri kuwa inchi ile kweli ilikuwa ni nchi njema na ni kweli ilikuwa ni nchi ya maziwa na asali, na miji yake ilikuwa ni mikubwa na yenye ngome na watu wake walikuwa hodari lakini pia waliwaona wana wa Anaki, aidha pia walifanikiwa kuja na vishada vikubwa vya zabibu kutoka nchi ya Mkanaani.

Hesabu 13:27-28 “Wakaenda wakafika kwa Musa, na kwa Haruni, na kwa mkutano wote wa wana wa Israeli, katika jangwa la Parani, huko Kadeshi; wakawaletea habari, wao na mkutano wote, wakawaonyesha matunda ya nchi. Wakamwambia wakasema, Tulifika nchi ile uliyotutuma, na hakika yake, ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali, na haya ndiyo matunda yake. Lakini watu wanaokaa katika nchi ile ni hodari, na miji yao ina maboma, nayo ni makubwa sana; na pamoja na hayo tuliwaona wana wa Anaki huko. Amaleki anakaa katika nchi ya Negebu; na Mhiti, na Myebusi, na Mwamori wanakaa katika milima, na Mkanaani anakaa karibu na bahari; na kando ya ukingo wa Yordani.”                

Hata hivyo katika namna ya kushangaza sana taarifa hii iliwatisha baadhi ya wana wa Israel wasiokuwa thabiti katika imani, kwani wao badala ya kuona fursa waliogopa na kufadhaika sana  na kwa mawazo yao walikimbilia kunung’unika na kulalamika badala ya kumuamini Mungu kwamba anaweza kuwarithisha nchi ile kama alivyowaahidi, wapelelezi wengine 10, walikazia kuwa haiwezekani kuirithi inchi ile kwa sababu zao za mitazamo ya kibinadamu, Lakini Kalebu na Yoshua wao walikuwa na mtazamo tofauti kwani walirarua nguo zao na kuwatia moyo watu Kuwa hawapaswi kuogopa kwani Mungu ni mwaminifu na angewapa nchi ile na watu wale walikuwa ni kama chakula kwao.

Hesabu 13:31-33 “Kalebu akawatuliza watu mbele ya Musa, akasema, Na tupande mara, tukaitamalaki; maana twaweza kushinda bila shaka. Bali wale watu waliopanda pamoja naye wakasema, Hatuwezi kupanda tupigane na watu hawa; kwa maana wana nguvu kuliko sisi. Wakawaletea wana wa Israeli habari mbaya ya ile nchi waliyoipeleleza, wakasema, Ile nchi tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi inayowala watu wanaoikaa; na watu wote tuliowaona ndani yake ni watu warefu mno. Kisha, huko tuliwaona Wanefili, wana wa Anaki, waliotoka kwa hao Wanefili; tukajiona nafsi zetu kuwa kama mapanzi; nao ndivyo walivyotuona sisi.”                

Hesabu 14:6-9 “Na Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, waliokuwa miongoni mwao walioipeleleza nchi, wakararua nguo zao; wakanena na mkutano wote wa wana wa Israeli wakasema, Nchi ile tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi njema mno ya ajabu. Ikiwa Bwana anatufurahia, atatuingiza katika nchi hii atupe iwe yetu, nayo ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali. Lakini msimwasi Bwana, wala msiwaogope wale wenyeji wa nchi, maana wao ni chakula kwetu; uvuli uliokuwa juu yao umeondolewa, naye Bwana yu pamoja nasi; msiwaogope.”

Kutokana na ujasiri wa Kalebu mwana wa Yefune na Yoshua mwana wa Nuni ambao walionyesha ujasiri mkubwa uliochangiwa na uaminifu wao na imani yao kwa Mungu, Mungu aliapa kuwaangamiza wengine waliolalamika na kunung’unika lakini aliahidi kuwa sivyo itakavyokuwa kwa Kalebu na Yoshua kwa kuwa wao walikuwa na kitu cha ziada na cha tofauti na hivi ndo walivyokua:-

-          Alimfuata Bwana kwa moyo wake wote – Hesabu 14:23-24 “hakika yangu hawataiona hiyo nchi niliyowaapia baba zao, wala katika hao wote walionidharau hapana atakayeiona; lakini mtumishi wangu Kalebu, kwa kuwa alikuwa na roho nyingine ndani yake, naye AMENIANDAMA KWA MOYO WOTE, nitamleta yeye mpaka nchi hiyo aliyoingia; na uzao wake wataimiliki.”

 

Neno ameniandama kwa moyo wote katika maandiko ya kiebrania linasomeka kama ‘achr Rûach ambalo kwa kiingereza ni wind by resemblance yaani amekuwa na roho ya kufanana nami au punzi inayonifanania, maana yake Kalebu alikuwa anaona mambo sawasawa na jinsi Mungu anavyoona, wakati watu wengine wote wanaona mambo hayawezekani Kalebu na Yoshua wao walikuwa wanaona mbona inawezekana, Mungu alimuahidi Kalebu inchi ile kuwa atairithi yeye na watoto wake kwa sababu aliona kama Mungu anavyoona, aliona yasiyowezekana kibinadamu yanawezekana kwa Mungu, alikuwa na mtazamo wa yanayowezekana  wakati wanadamu wakiona yasiyowezekana.

               

-          Walimfuata Bwana kwa kila neno – Kumbukumbu 1:34-36 “Bwana akaisikia sauti ya maneno yenu, akaghadhibika, akaapa, akasema, Hakika yangu hapana mmoja miongoni mwa watu hawa wa kizazi hiki kibaya atakayeiona nchi hiyo nzuri, niliyowaapia baba zenu kuwapa,isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, huyo ataiona; nami nitampa yeye na watoto wake nchi hiyo aliyoikanyaga; KWA KUWA AMEMFUATA BWANA KWA KILA NENO.”

 

Neno amemfuata Bwana kwa kila neno kwenye lugha ya kiebrania linatumika neno Mâlmâlâ ‘Achar ambalo katika kiingereza ni neno Wholly Conjugation au Wholly Conjugate ambalo kwa Kiswahili ni kuenda Sambamba, kufuata barabara, au kufanya au kuungana kwa hiyo sifa nyingine aliyokuwa nayo Kalebu ni kuwa aliungana na Mungu katika neno lake lote, kile kilichozungumzwa na Mungu yeye aliungana nacho kama kilivyosemwa, hakuwa kinyume na neno, alilifuata, alilitenda aliungana nalo na kwa sababu hiyo Mungu anaapa kuwa atairithi nchi. 

 

-          Alimwandama bwana kwa utimilifu – Yoshua 14:13-14 “Yoshua akambarikia, akampa Kalebu, huyo mwana wa Yefune, Hebroni kuwa urithi wake. Kwa hiyo Hebroni ukawa urithi wa Kalebu, mwana wa Yefune, Mkenizi, hata leo; kwa sababu ALIMWANDAMA BWANA, MUNGU WA ISRAELI, KWA UTIMILIFU.”

 

Neno alimuandama kwa utumilifu katika maandiko ya kuiebrania linasomeaka kama Mâlmâlâ kusomeka linasomeka maw-lay kwa kiingereza ni neno concecrate ambalo maana yake kwa utakatifu, kwa unyoofu, kwa kujiweka wakfu, kwa njia tofauti na wengine yaani wakati wengine wanaasi wanazungumza kinyume na ahadi ya Mungu Kalebu yeye alifanya kwa unyoofu kwa utakatifu, kwaajili ya hili Mungu alimpa ahadi, Kalebu hafuati mkumbo             

 

-          Walikuwa na roho nyingine – Hesabu 14:22-24 “kwa sababu watu hawa wote, ambao wameuona utukufu wangu na ishara zangu, nilizozitenda huko Misri, na huko jangwani, pamoja na haya wamenijaribu mara hizi kumi, wala hawakuisikiza sauti yangu; hakika yangu hawataiona hiyo nchi niliyowaapia baba zao, wala katika hao wote walionidharau hapana atakayeiona; lakini mtumishi wangu Kalebu, KWA KUWA ALIKUWA NA ROHO NYINGINE ndani yake, naye ameniandama kwa moyo wote, nitamleta yeye mpaka nchi hiyo aliyoingia; na uzao wake wataimiliki.”

 

Neno alikuwa na roho nyingine katika maandiko ya kiebrania linasomeka kama Achr rûach ambayo kwa kiingereza “Strange Spirit”, roho nyingine, yaani tofauti na wengine ambao walikuwa na roho ya hofu, roho ya woga, yeye alikuwa na Roho Nyingine roho ambayo sio ya kibinadamu, Roho kama ya Mungu, ukiwa na roho nyingine tofauti na wanadamu wa kawaida wewe unakuwa na mtazamo mwingine, mtazamo wa tofauti, unaona kwa jinsi nyingine na kutazama mambo kwa jicho lingine, jicho la kigeni.

Basi sasa unipe mlima huu

Kalebu huyu ambaye hakuwa mtu wa kawaida na alikuwa na kitu cha ziada, akiwa na roho ya kufanana na Mungu, akiwa na moyo wa unyoofu, akiwa anaungana na neno la Mungu, akiwa na roho nyingine tofauti na wayahudi wengine yeye sasa anaidai nchi ya Kanaani aliyoahidiwa na Mungu na anamkumbusha Yoshua kwamba sasa ni wakati wa kupewa urithi wake, na kwa vile Yoshua alikuwepo anamkumbusha yale yote Mungu aliyokuwa ameahidi kwa kinywa cha mtumishi wake Musa, mbele ya Yoshua walipokuwa pamoja naye ni miaka 45 imepita sasa ahadi ilitolewa alipokuwa na miaka 40 sasa anakumbushia kile alichoahidiwa na Mungu, na hataki bure anasema yuko tayari kupigana kwaajili ya ardhi ile tena pale pale wanapoishi majitu yaani wana wa Anaki hili ni jambo la kushangaza sana

Yoshua 14:6-13 Wakati huo wana wa Yuda walimkaribia Yoshua hapo Gilgali; na Kalebu, mwana wa Yefune, huyo Mkenizi, akamwambia, Wewe wajua hilo neno Bwana alilomwambia Musa, huyo mtu wa Mungu, katika habari zangu, na katika habari zako wewe, tulipokuwa katika Kadesh-barnea. Mimi nilikuwa mtu wa miaka arobaini umri wangu, hapo Musa mtumishi wa Bwana aliponituma niende kutoka Kadesh-barnea ili kuipeleleza hiyo nchi; nami nilimletea habari tena, kama ilivyokuwa ndani ya moyo wangu. Lakini wale ndugu zangu waliokwea kwenda pamoja nami waliiyeyusha mioyo ya watu; ila mimi nilimfuata Bwana, Mungu wangu, kwa utimilifu. Kisha Musa akaniapia siku hiyo, akasema, Hakika hiyo nchi ambayo miguu yako imekanyaga itakuwa ni urithi kwako wewe, na kwa watoto wako milele, kwa sababu wewe umemfuata Bwana, Mungu wako, kwa utimilifu. Sasa basi, angalia, yeye Bwana ameniweka hai, kama alivyosema, miaka hii arobaini na mitano, tangu wakati huo Bwana alipomwambia Musa neno hilo, wakati Israeli waliokuwa wakienenda barani; na sasa tazama, hivi leo nimepata miaka themanini na mitano umri wangu. Hata sasa mimi nina nguvu zangu hivi leo kama nilivyokuwa siku hiyo Musa aliyonituma; kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, na nguvu zangu ndivyo zilivyo sasa, kwa vita na kwa kutoka nje na kuingia ndani. Basi sasa unipe mlima huu, ambao Bwana alinena habari zake siku hiyo; kwani wewe ulisikia siku hiyo jinsi Waanaki walivyokuwa huko, na miji ilivyokuwa mikubwa yenye boma; yumkini yeye Bwana atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza watoke nje, kama Bwana alivyonena. Yoshua akambarikia, akampa Kalebu, huyo mwana wa Yefune, Hebroni kuwa urithi wake.Kwa hiyo Hebroni ukawa urithi wa Kalebu, mwana wa Yefune, Mkenizi, hata leo; kwa sababu alimwandama Bwana, Mungu wa Israeli, kwa utimilifu. Basi jina la Hebroni hapo kwanza uliitwa Kiriath-arba; huyo Arba alikuwa ni mtu mkubwa kupita wenziwe wote katika hao Waanaki. Hiyo nchi nayo ikatulia, vita vikakoma.”

Miaka mingi imepita lakini Kalebu bado yuko vile vile hakuna kuchuja, nguvu zake ziko vile vile na anataka ardhi na kama ilivyo kawaida ya wanadamu wengi sio rahisi sana kuona faida za kukaa mlimani, tunapenda nchi tambarare iliyonyooka, watu wengi hawapendi milima, na zaidi ya yote mlima huu ulikuwa unamilikiwa na majitu makubwa wana wa Anaki, katika namna ya kushangaza sana Kalebu yeye anautaka mlima huo na yuko tayari kuupigania imani yake haijapoa miaka 45 imepita yeye yuko vile vile, moyo wake uko vile vile anamuamini Mungu vile vile akiwa na nguvu zile zile, akiwa na ujasiri ule ule hajachoka katika mapambano hii inatufundisha kitu kikubwa sana.

Hebroni ilikuwa ni safu ya milima katika milima ya uyahudi kusini mwa Yudea,  ambako ni ukanda wa Magharibi leo, mji wa Hebroni ni moja ya mji unaoheshimika sana na wayahudi kama moja ya miji mitakatifu walikozikwa wazee wetu Ibrahim, Isaka na Yakobo katika pango la Makpela  kwa hiyo ni eneo zuri kihistoria, wakati wa Yoshua sasa eneo hilo lilikaliwa na majitu, lakini Kalebu alikuwa anaiona fursa katika mlima aliouomba kuliko nchi tambarare, kiusalama na kiulinzi yeye angeishi juu na kama askari angeweza kuwaona adui kwa mbali na kuwa salama, chini ya milima kulikua na bonde zuri ambalo lingeweza kufaa kwa kilimo na mifugo na juu ya mlima makazi salama, sasa Kalebu anataka hilo, Kalebu mtazamo wake ni wa tofauti, ni kama ana moyo wa kufanya mambo kwa njia tofauti, ni kama mtu anayesema wakati watu wanaogopa kuendesha ndege mimi nitaendesha, ni kama mtu anayesema wakati watu wanaogopa hisabati mimi ninapenda hisabati, ni kama mtu anayesema wakati watu wanaogopa masomo ya sayansi mimi nitachukua sayansi, Moyo wa Kalebu ni moyo usioogopa mambo magumu, unaona fursa katika mambo yasiyowezekana hauchagui mambo mepesi, unachagua mambo magumu, unaona fursa katika mambo magumu, unawaza na kuyataja yanayoonekana hayawezekani kuwa yanawezekana “BASI SASA UNIPE MLIMA HUU” haijalishi umri umekwenda kiasi gani anataka MLIMA HUU ni mzee lakini bado anawaza na kufikiri akiona maono kama kijana tu, hasemi umri wangu umeenda, hasemi nguvu zangu zimeisha, ametunza Imani yake na uwepo wake vilevile, Kalebu hapoi wala haboi, mtazamo wake kuhusu Mungu uko vilevile wakati makanisa mengi yanapoa yanapofikia umri wa miaka 40, wakati wakristo wengi wanapoa wanapokaa sana katika wokovu, Kalebu hapoi, Kalebu bado anaona maono, Kalebu bado ana ndoto Kalebu bado anamuamini Mungu, haoni kuwa Mungu amechelewa, wala hana muda wa kumlaumu Mungu, anakumbushia haki zake, yuko tayari kwa mapambano, Kalebu hachoki mikesha, Kalebu hachoki kufunga, Kalebu hachoki kuomba, Kalebu hachoki mikutano ya injili, Kalebu hachoki kuhubiri vijijini, Kalebu  hachoki kufungua makanisa, Kalebu hachoki kusoma, Kalebu hachoki kujitoa, Kalebu hachoki kuishi maisha matakatifu, Kalebu hachoki kulifuata neno, Kalebu hachoki kuwa na roho ile ile ya Mungu, Kalebu hachoki kunena kwa lugha, Kalebu ana ujasiri ule ule wa kuhubiri sokoni, Kalebu, ana moto uleule aliokuwa nao jangwani, Kalebu hachoki kuvumilia, Kalebu hachoki kusubiria, Kalebu hachoki majaribu Kalebu hataki kuweka silaha chini Kalebu Kalebu Kalebu una miaka 85 sasa umezeeka, nguvu zako zimeisha, umestaafu sasa Kalebu si utulie, Kalebu si nikutafutie eneo tambarare, Kalebu si ukae karibu na mimi? Kalebu anasema BASI SASA UNIPE MLIMA HUU Mungu wangu ni moyo wa namna gani huu Kalebu? Umepigana vita vingi Kalebu, ukae chini utulie ule mema ya nchi inatosha sasa Kalebu, Kalebu “BASI SASA UNIPE MLIMA HUU” kuna waanaki huko Kalebu, Kalebu nitawafukuza huko, Bwana atakuwa pamoja nami, nguvu zangu hazijapungua niko vilevile kama hapo Musa aliponiapia “BASI SASA UNIPE MLIMA HUU” “shakarabashata skarabatulabosolitasaka Kalebu sotoribakarashika sata rakata risatika yekresatabsoliboso rokosotoka sebetaolasiotifaBASI SASA UNIPE MLIMA HUU neno la Mungu linasema “KWA HIYO HEBRONI UKAWA URITHI WA KALEBU, MWANA WA YEFUNE, MKENIZI, HATA LEO

Mambo ya kujifunza kutoka kwa Kalebu.

-          Ni lazima tuwe na Imani thabiti kwa ahadi za Mungu  -  Kalebu alikuwa ni mtu wa imani na hakuwahi kuchoka katika kumuamini Mungu ni miaka 45 imepita tangu alipokuja kuichunguza na kuipeleleza nchi na hata ingawaje wapelelezi wengine walileta habari chochezi kinyume na imani Kalebu tangu wakati ule aliamini kuwa Mungu hawezi kuwaangusha anakumbuka ahadi za Mungu na hakua na lawama kuwa Mungu amechelewa  au amekawia anaendelea kuipigania haki yake sawa na jinsi na namna ile ile aliyokuwa nayo awali.

 

Yoshua 14:9-12 “Kisha Musa akaniapia siku hiyo, akasema, Hakika hiyo nchi ambayo miguu yako imekanyaga itakuwa ni urithi kwako wewe, na kwa watoto wako milele, kwa sababu wewe umemfuata Bwana, Mungu wako, kwa utimilifu. Sasa basi, angalia, yeye Bwana ameniweka hai, kama alivyosema, miaka hii arobaini na mitano, tangu wakati huo Bwana alipomwambia Musa neno hilo, wakati Israeli waliokuwa wakienenda barani; na sasa tazama, hivi leo nimepata miaka themanini na mitano umri wangu. Hata sasa mimi nina nguvu zangu hivi leo kama nilivyokuwa siku hiyo Musa aliyonituma; kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, na nguvu zangu ndivyo zilivyo sasa, kwa vita na kwa kutoka nje na kuingia ndani. Basi sasa unipe mlima huu, ambao Bwana alinena habari zake siku hiyo; kwani wewe ulisikia siku hiyo jinsi Waanaki walivyokuwa huko, na miji ilivyokuwa mikubwa yenye boma; yumkini yeye Bwana atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza watoke nje, kama Bwana alivyonena.”                

 

Kalebu ni moja ya mashujaa wa Imani aliyeweza kusubiria ahadi ya Mungu kwa muda mrefu bila kukata tamaa, wakati Ibrahimu alimsubiri Isaka kwa miaka kama 25 hivi, na Daudi alisubiria ufalme kwa miaka kama 20, Yakobo alivumilia kwa mjomba wake kwa miaka 20 lakini Kalebu alivumilia kwa zaidi ya miaka 45 je wewe ni mvumilivu kwa kiasi gani?

 

-          Kuwa tayari kukabiliana na changamoto – Kalebu alikuwa na ujasiri wa hali ya juu, hakuiomba Hebroni hivi hivi tu, Hebroni ulikuwa ni mlima na sio tambarare na zaidi ya yote ulikuwa unamilikiwa na wana wa Anaki ambao kimsingi walikuwa ni majitu, wale wale walioogopewa na wengine Yeye Kalebu hakuogopa alikuwa tayari kukabiliana na hali hiyo huku akimtegemea Mungu kwamba angekuwa pamoja naye akiamini kuwa atawafukuza.

 

Yoshua 14:12 “Basi sasa unipe mlima huu, ambao Bwana alinena habari zake siku hiyo; kwani wewe ulisikia siku hiyo jinsi Waanaki walivyokuwa huko, na miji ilivyokuwa mikubwa yenye boma; yumkini yeye Bwana atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza watoke nje, kama Bwana alivyonena.”

 

-          Hakuogopa umri wake – Kalebu alikuwa mvumilivu sana na alikuwa na nguvu amefikisha miaka 85 lakini anajisikia ndani yuko vile vile na uwezo ule ule wa kukabiliana na changamoto zile zile alikuwa ni mbobezi katika maswala ya vita na jeshi, jangwa lilikuwa limemuimarisha na kumfanya kuwa mtu mgumu, umri kwake haukuwa kikwazo cha kuzirithi ahadi za Mungu na kuzipambania aliendelea kuwa na maono na imani na matumaini.

 

Yoshua 14:11 “Hata sasa mimi nina nguvu zangu hivi leo kama nilivyokuwa siku hiyo Musa aliyonituma; kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, na nguvu zangu ndivyo zilivyo sasa, kwa vita na kwa kutoka nje na kuingia ndani.”

 

-          Aliendelea kuwa mwainifu siku zote – Kwa kweli maneno ya Kalebu yanaonyesha kuwa alikuwa mwaminifu na aliendelea kuwa vile vile mpaka mwisho, uaminifu wake kwa Mungu tangu ujana wake  mpaka wakati huu anaonekana kuwa alikuwa mtu asiyekata tamaa, shujaa na mtu aliyeendelea kumtegemea Mungu huku akikumbuka ahadi zake na haki yake aliudai mlima huo kwa sababu alikuwa na uhakika na Mungu wake kuwa hatomwangusha

 

Yoshua 14:7-8 “Mimi nilikuwa mtu wa miaka arobaini umri wangu, hapo Musa mtumishi wa Bwana aliponituma niende kutoka Kadesh-barnea ili kuipeleleza hiyo nchi; nami nilimletea habari tena, kama ilivyokuwa ndani ya moyo wangu. Lakini wale ndugu zangu waliokwea kwenda pamoja nami waliiyeyusha mioyo ya watu; ila mimi nilimfuata Bwana, Mungu wangu, kwa utimilifu.”   

       

Hitimisho:

Kalebu anampa somo kila mmoja wetu kuhusu imani, uvumilivu, subira, ujasiri, na uaminifu kwa Mungu, alikuwa ni mtu asiyeogopa changamoto wala mtu wa kukata tamaa, hakukuwa na hata tone la hofu maishani mwake kauli yake BASI SASA UNIPE MLIMA HUU iwe changamoto kwetu kwamba tuteendelea kumuamini Mungu sio kwa mambo mepesi tu bali hata kwa mambo magumu, na tutaendelea kuwa wavumilivu bila kujali muda, na tutaendelea katika imani bila kupoa, na tutaendelea kuwa na ujasiri wa kukabiliana na magumu bila kujali umri na kuwa tayari kumtumikia Mungu mpaka siku zetu za mwisho!

 

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Hakuna maoni: