Jumapili, 17 Agosti 2025

Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote!


Yohana 3:30-31 “Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua. Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote. Yeye aliye wa dunia, asili yake ni ya dunia, naye anena mambo ya duniani. Yeye ajaye kutoka mbinguni yu juu ya yote.”




Utangulizi:

Moja ya watu waliokuwa na uwezo mkubwa sana wa kumuelezea vizuri Yesu Kristo na kumtambulisha kwa watu ni pamoja na Yohana Mbatizaji, huyu ni moja ya manabii waliopata neema ya ajabu sana ya sio tu kutabiri kuhusu ujio wa Maisihi, lakini kuonyesha moja kwa moja mubashara kuhusu Yesu Kristo, Mjadala kuhusu Yesu ulikuja baada  ya watu kumuhoji kuhusu habari za Yesu ambaye watu wengi walikuwa wameanza kumuendea, huku wengine wakiendelea kuonyesha heshima kubwa kwa Yohana Mbatizaji wakifikiri kwa kuwa alitokea nyikani na alikuwa kama Eliya kimtazamo na kimuonekano kwamba huenda ndiye angefaa kuwa masihi, Hata hivyo yeye aliendelea kuwasisitizia kuwa huyo anayefanya wanafunzi wengi ndiye masihi na yeye hana budi kupungua ili huyo aweze kuzidi

Yohana 3:26-31 “Wakamwendea Yohana, wakamwambia, Rabi, yeye aliyekuwa pamoja nawe ng'ambo ya Yordani, yeye uliyemshuhudia, tazama, huyo anabatiza na watu wote wanamwendea. Yohana akajibu, akasema, Hawezi mtu kupokea neno lo lote isipokuwa amepewa kutoka mbinguni. Ninyi wenyewe mwanishuhudia ya kwamba nalisema, Mimi siye Kristo, bali nimetumwa mbele yake. Aliye naye bibi arusi ndiye bwana arusi; lakini rafiki yake bwana arusi, yeye anayesimama na kumsikia, aifurahia sana sauti yake bwana arusi. Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua. Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote. Yeye aliye wa dunia, asili yake ni ya dunia, naye anena mambo ya duniani. Yeye ajaye kutoka mbinguni yu juu ya yote.”

Yohana anamuelezea Yesu kwa ufunuo mkubwa ambao sio rahisi mwanadamu wa kawaida kuwa nao, Yeye anamuelezea Yesu kama Yeye ajaye kutoka juu, ana anamfunua hivyo kwa umati mkubwa wa watu akimaanisha kuwa Yesu sio nabii wa kawaida wala Mwalimu wa kawaida wa duniani bali huyu ashuka kutoka mbinguni, Yohana alikuwa akiuthibitishia ulimwengu kuwa Yesu ana mamlaka kubwa sana kuliko hata yeye mwenyewe, Yesu ana asili ya uungu na sio ya kibinadamu tu, Kila Mwalimu wa kweli wa neno la Mungu ni lazima awe na uhakika wa Yesu ni nani na awe anajua kumuelezea vizuri, na kutokujaribu kuchukua nafasi yake na kumleta Yesu mzima mzima kwa jamii ili jamii imkubali na kupata masaada kutoka kwake, leo tutachukua muda kuijadili kauli hii ya Yohana Mbatizaji Yeye ajaye kutoka juu! kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Asili ya Yesu Kristo.

·         Yeye ajaye kutoka juu.

·         Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote!


Asiili ya Yesu Kristo!

Yohana ni moja ya manabii wa ajabu sana na wa tofauti mno, Kabla ya wanafunzi wa Yesu kutuelezea kwa kina kuwa Yesu Kristo ni nani Yohana mbatizaji ni mtu wa kwanza kutuelezea ukuu wa Yesu Kristo Yeye anamuelezea Yesu kama ambaye asili yake si ya dunia kama alivyo Yohana na manabii wengine na sisi, Yesu anaelezewa na Yohana Mbatizaji kama ambaye asili yake ni ya mbinguni yaani Yeye ajaye kutoka juu!

Yohana 3:31 “Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote. Yeye aliye wa dunia, asili yake ni ya dunia, naye anena mambo ya duniani. Yeye ajaye kutoka mbinguni yu juu ya yote.”

Yohana anatufunulia hapa kwamba Yesu amekuja kutoka mbinguni na hivyo asili yake sio ya dunia, ukweli huu unakubalina na mafundisho ya kibiblia na maneno ya Bwana mwenyewe kwamba Yeye amekuwepo kabla hata ya Ibrahimu baba wa Imani ya kiyahudi hajakuwepo, Yeye Ibrahimu asijakuwako mimi niko (“Before Abraham was born I am!”) yaani kabla Ibrahimu hajazaliwa mimi niko alisema Yesu Kristo mwenyewe.

Yohana 8:56-58 “Ibrahimu, baba yenu, alishangilia kwa vile atakavyoiona siku yangu; naye akaiona, akafurahi. Basi Wayahudi wakamwambia, Wewe hujapata bado miaka hamsini, nawe umemwona Ibrahimu? Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Yeye Ibrahimu asijakuwako, mimi niko.”

Neno la Mungu vilevile linathibitisha ya kuwa Yesu Kristo kabla ya kuvaa mwili wa kibinadamu alikuweko tangu milele kama neno la Mungu na alihusika katika kuumba ulimwengu na hapa Duniani alijifunua kwetu kwa utukufu kama wa mwana pekee wa Mungu.

Yohana 1:1-3,1 4 “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu.Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika. 14 Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli.”

Kwa msingi huo neno la Mungu linabainisha wazi kuwa Yesu Kristo hakuwa mwanadamu wa kawaida, mamlaka yake na uwezo wake ulikuwa uko juu ya kawaida ya kibinadamu kama anavyoeleza Nabii Yohana mbatizaji, ufahamu huu kwa kweli sio ufahamu wa kawaida ni lazima uwe umefunuliwa na Roho Mtakatifu kumfahamu na kumtambua Yesu kuwa ni mtu wa namna gani, mapema kabla ya kuzaliwa kwake nabii Mika aliyeishi karibu wakati sawa na nabii Isaya alieleza mpaka mahali atakapozaliwa Masihi na kuutaja mji atakaozaliwa kuwa ni Bethelehemu, lakini kama haitoshi alieleza kuwa mtu huyu asiyekuwa wa kawaida asili yake imekuwepo tokea enzi na enzi.

Mika 5:2 “Bali wewe, Bethlehemu Efrata, uliye mdogo kuwa miongoni mwa elfu za Yuda; kutoka kwako wewe atanitokea mmoja atakayekuwa mtawala katika Israeli; ambaye matokeo yake yamekuwa tangu zamani za kale, tangu milele.”

Nabii Isaya akitabiri kuhusu kuja kwa masihi Yaani Bwana Yesu yeye naye alitabiri na kuonyesha kuwa Yesu atakuwa mfalme wa ajabu na baba wa milele, na Mungu mwenye nguvu, kwa ujumla maandiko yanamuelezea Yesu kwa namna pana zaidi kuliko watu wengine wanavyoweza kufikiri au kukosoa kwa kukosa maarifa Isaya anasema:-

Isaya 9:6-7 “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa Jina Lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani Hayatakuwa na mwisho kamwe, Katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; Kuuthibitisha na kuutegemeza Kwa hukumu na kwa haki, Tangu sasa na hata milele. Wivu wa Bwana wa majeshi ndio utakaotenda hayo.”

Kwa msingi huo sio kuwa wakristo wanamkuza tu Yesu Kristo na wengine wanadhani kuwa tunakufuru, lakini ni ukweli ulio wazi manabii walimfunua Yesu Kristo kwetu pamoja na mitume wake ambao kwaasili ni wayahudi wanatuwekea wazi kuwa Yesu Kristo asili yake ni Mbinguni na kuwa alikuwako huko toka milele na sio hivyo tu tunaelezwa kuwa alikuwa Mungu na kwa kuja kwake duniani ililikuwa swala la unyenyekevu mkubwa na kujidhili au kujishusha kwa namna isiyoweza kufananishwa au labda kuwa sawa na mtumwa ingawa yeye alijijua kuwa hakuwa mtu wa kawaida, Paulo mtume analiweka hilo sawa katika waraka wake kwa Wafilipi ona:-

Wafilipi 2:5-8 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba.”

Kwa sababu hiyo Yohana alimtambua Yesu kuwa alikuwa mwanadamu wa viwango vingine, mwanadamu asiyekuwa wa kawaida alisema huyu ni mkuu mno akionyesha ukuu wa Yesu Kriso katika kiwango ambacho yeye mwenyewe alisema hastahili hata kulegeza gidamu za viatu vyake:-

Luka 3:16-17 “Yohana alijibu akawaambia wote, Kweli mimi nawabatiza kwa maji; lakini yuaja mtu mwenye nguvu kuliko mimi, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto; ambaye pepeo lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake, na kuikusanya ngano ghalani mwake, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika.”  

Yohana anatusaidia wanazuoni kutokumchukulia Yesu Kristo kama mtu wa kawaida au kama manabii wengine, Yesu Kristo hafananishwi wala kulinganishwa na kitu chochote, kujishusha kwake na unyenyekevu wake wa kukubali kudhalilishwa msalabani kusiwanye wanadamu wawe na nafasi ya kumdhalilisha na kumkufuru badala yake wanapaswa kuogopa na kumchukulia kwa heshima kubwa kwani ni zawadi ya kipekee ambayo Mungu amewapa wanadamu ili tuweze kuokolewa Yesu yeye asili yake ni juu, yaani yeye ametokea Mbinguni ambako alikuweko tangu mwanzo, Yeye yuko juu y asana kuliko ufalme wowote, mamlaka yoyote, usultani wowote, enzi yoyote, na jina lolote litajwalo ulimwenguni humu na vitu vyote viliumbwa kwa njia yake na kwaajili yake

Waefeso 1:17-21 “Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeye; macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo; na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake; aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia;”             

Wakolosai 1:16-19 “Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni vitu vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake. Naye amekuwako kabla ya vitu vyote, na vitu vyote hushikana katika yeye. Naye ndiye kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa; naye ni mwanzo, ni mzaliwa wa kwanza katika wafu, ili kwamba awe mtangulizi katika yote. Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae;”

Kwa msingi huu kwa uchunguzi wa kimaandiko utakubaliana nami kwamba Yesu, Yu Juu ya yote kama yanenavyo maandiko!

Yeye ajaye kutoka juu

Wako watu katika nyakati za leo hususani watu wanaoendesha mijadala ya kidini ambao humchukulia Yesu kwa mchezo mchezo na wala hawataki kumuelezea Yesu Katika namna ambayo maandiko humuelezea, mijadala ya aina hii, Nabii Yohana mbatizaji aliizima kabisa kwani wanazuoni wa wakati huo walitaka kumlinganisha Yeye (Yohana mbatizaji) au nabii (Yahaya bin Zekaria) na Masihi Bwana Yesu, wao walimtazama kwa mtazamo wa nje tu na kuona kama Nabii Yohana alionekana wa maana sana labda huenda hata kuliko Yesu, kwa sababu yeye alitokea Porini/Nyikani/jangwani na alivaa nguo za ngozi na singa za ngamia akila nzige na asali, akijiepusha na maisha ya kawaida ya mitaani akiishi nyikani, kujidhabihu kwake kulionekana kimtazamo kuwa alikuwa nabii kweli kweli na  maarufu sana labda huenda kuliko hata Masihi, Yesu alivyokuja na mtindo wake wa maisha pengine pia na kuonekana kwake kama kijana mdogo wa miaka 30 hivi, Yohana alitahadharisha kuwa Yesu sio wa kulinganishwa naye kumlinganisha yeye Yesu ni sawa tu na msimamizi wa harusi na Bwana harusi mwenyewe, aliwathibitishia kuwa maagizo yote anayoyatoa Yesu ni muhimu akasikilizwa kwa kuwa Yeye ni wa mbinguni na Yohana ni wa duniani, Yesu ni wa mbinguni anatoka juu na yuko juu ya manabii wengine wote ambao asili yao ni ya dunia na wananena mambo ya duniani Lakini sivyo ilivyo kwa Yesu Kristo ambaye asili yake ni juu na ananena maswala kutoka mbinguni!.

Yohana 3:25-31 “Basi palitokea mashindano ya wanafunzi wa Yohana na Myahudi mmoja juu ya utakaso.Wakamwendea Yohana, wakamwambia, Rabi, yeye aliyekuwa pamoja nawe ng'ambo ya Yordani, yeye uliyemshuhudia, tazama, huyo anabatiza na watu wote wanamwendea. Yohana akajibu, akasema, Hawezi mtu kupokea neno lo lote isipokuwa amepewa kutoka mbinguni. Ninyi wenyewe mwanishuhudia ya kwamba nalisema, Mimi siye Kristo, bali nimetumwa mbele yake. Aliye naye bibi arusi ndiye bwana arusi; lakini rafiki yake bwana arusi, yeye anayesimama na kumsikia, aifurahia sana sauti yake bwana arusi. Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua. Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote. Yeye aliye wa dunia, asili yake ni ya dunia, naye anena mambo ya duniani. Yeye ajaye kutoka mbinguni yu juu ya yote.”                 

Yohana alikuwa akiwahakikishia watu kuwa mamlaka ya Yesu sio ya kawaida  na kuwa iko juu kwa namna ambayo haiwezi kulinganishwa na mamlaka nyingine yoyote, alisema tena sifa za Yesu zinapaswa kuzidi na za kwake yaani Yohana mbatizaji zinapaswa kupungua, Yesu ni mwenye mamlaka na nguvu na hekina na akili na ujuzi na maarifa na ufahamu kuliko mtu mwingine yeyote, hakuna mamlaka, wala serikali,  wala usultani wala uongozi, wala bosi wala mwenye mamlaka wala mwenye serikali inayoweza kuzidi mamlaka aliyonayo Yesu Kristo, Yesu mwenyewe anathibitisha kuwa ameshuka kutoka mbinguni na anatakeleleza mapenzi ya baba yake wa mbinguni:-

Yohana 6:32-38 “Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha mbinguni, bali Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni. Kwa maana chakula cha Mungu ni kile kishukacho kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima. Basi wakamwambia, Bwana, sikuzote utupe chakula hiki. Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe. Lakini naliwaambia ya kwamba mmeniona wala hamwamini. Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe. Kwa kuwa mimi sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka.”

Yesu anadhihirisha wazi katika neno lake ya kuwa kama ile mana ilivyoshuka kutoka mbinguni na kuwapa uzima wa muda baba za wayahudi huko jangwani ambao kimsingi walikufa, yeye alikuwa anamaanisha kuwa ile mana ilikuwa ni ishara ya kuwa baba anawapa chakula kishukacho kutoka mbinguni na kuwa kama wakimuamini hawataona njaa tena na ya kuwa hawatakufa bali watakuwa na uzima wa milele wakati watu waliona kuwa yeye ni mwana wa seremala tu na wakidhani kuwa masihi atashuka moja kwa moja kwa jinsi ya kuonekana kimwili kama atakavyokuja mara ya pili duniani, Lakini masihi alikuja bila wao kuelewa. Ujio wa Yesu Kristo kutoka juu mbinguni una faida kubwa sana katika maisha ya wanadamu wote kama tutatambua kuwa Yesu yuko juu ya yote na kumuamini kuna faida lukuki ambazo tutafaidika kwa imani hii, Neno ajaye kutoka juu katika kiyunani linasomeka “Erchomai anōthen esti epanō ambapo maneno mawili “Anōthen na epanaō” yana maana “From the beginning he is over on” yaani mwenye mamlaka au mwenye cheo cha juu cha kijeshi tangu mwanzo, hii inazungumzia kuwa katika mamlaka za kijeshi Yesu ni jemadari tangu mwanzo na ni jemadari aliyeko juu ya mambo yote ya mbinguni na duniani, anaweza kukupigania vita ya aina yoyote ile, na anaweza kuagiza au kuamuru majeshi ya malaika kama amiri jeshi mkuu.         

Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote!

Yohana sio tu katika majibu yake anataka kuonyesha kuwa Yesu asili yake sio ya dunia na kuwa Yesu asili yake ni kutoka juu, lakini pia anakazia kuwa yuko juu ya yote, Yohana anapotuelezea kuwa Yesu yuko juu ya yote anafunua faida kubwa zenye maana pana sana kwa kila mwamini ulimwenguni, hii inaonyesha kuwa Yesu ana mamlaka yote mbinguni na duniani, ana heshima ya kipekee na nafasi ya kwanza katika kila jambo, Yesu kuwa juu ya yote ina maana gani na faida gani hasa

-          Ana mamlaka yote mbinguni na Duniani – Mathayo 28:18 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” maana yake Serikali yake iko juu ya serikali zote, dola yake iko juu ya dola zote, mamlaka ya  kimwili na kiroho iko na yeye, kama ni kukata rufaa unakata kwake, kama ni hospitali ya rufaa yeye ndio hospitali ya mwisho, kama umeonewa yeye ndiye yuko juu ya wale waliokuonea ana mamlaka yote kama kuna watu wanajitukuza na kujiiinua juu yako basi kumbuka ya kuwa Yeye ana mamlaka kubwa kuliko hiyo yu juu ya yote, chochote kinachojiinua dhidi yako kikumbushwe kuwa Yuko aliye juu zaidi yake

 

-          Jina lake lina nguvu kuliko majina yote – Wafilipi 2:9-11 “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

 

-          Hukumu yote ya wanadamu imewekwa chini yake – Matendo 17:31 “Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.”

 

Yohana 5:22-23 “Tena Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote; ili watu wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba. Asiyemheshimu Mwana hamheshimu Baba aliyempeleka.”   

 

-          Sisi tu warithi pamoja naye – Warumi 8:16-17 “Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu; na kama tu watoto, basi, tu warithi; warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo; naam, tukiteswa pamoja naye ili tupate na kutukuzwa pamoja naye.”

 

-          Yeye ndiye anayehusika na ufufuo – Yoahan 11:25 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi;”

 

-          Akifunga hakuna afunguaye, akifungua hakuna afungaye – Ufunuo 3:7-8 “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Filadelfia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye mtakatifu, aliye wa kweli, aliye na ufunguo wa Daudi, yeye mwenye kufungua wala hapana afungaye, naye afunga wala hapana afunguaye. Nayajua matendo yako. Tazama, nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga, kwa kuwa unazo nguvu kidogo, nawe umelitunza neno langu, wala hukulikana jina langu.”

 

-          Yeye ndiye mwanzo na mwisho Alfa na Omega – Ufunuo 1:8 “Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, asema Bwana Mungu, aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja, Mwenyezi.”

 

-          Ana mamlaka ya kusamehe dhambi – Marko 2:5-10 “Naye Yesu, alipoiona imani yao, akamwambia yule mwenye kupooza, Mwanangu, umesamehewa dhambi zako. Na baadhi ya waandishi walikuwako huko, wameketi, wakifikiri mioyoni mwao, Mbona huyu anasema hivi? Anakufuru. Ni nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa mmoja, ndiye Mungu? Mara Yesu akafahamu rohoni mwake kwamba wanafikiri hivyo nafsini mwao, akawaambia, Mbona mnafikiri hivi mioyoni mwenu? Vyepesi ni vipi, kumwambia mwenye kupooza, Umesamehewa dhambi zako, au kusema, Ondoka, ujitwike godoro lako, uende? Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (hapo amwambia yule mwenye kupooza)        

 

-          Ana mamlaka dhidi ya shetani - Wakolosai 2:14-15 “akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo.”

 

Yesu Kristo kuwa juu ya yote maana yake ana mamlaka ya kila kitu mbinguni na duniani na kuwa kila kitu kiko chini yake, yeye ni chanzo cha wokovu wetu wa mwili nafsi na roho, ni kiboko ya mahitaji yetu yote na ni mwenye nguvu dhidi ya adui zetu wote chochote kinachojiinua juu yako kikumbushe tu kuwa Yeye ajaye kutoka juu yu juu ya yote, mashetani, mapepo, wenye mamlaka wenye uwezo, wanajimu na wachawi, wasihiri, wapiga ramli, waganga wa kienyeji, waonevu,  magonjwa na mateso ya aina mbalimbali yakumbushwe tu kuwa Yeye ajaye kutoka juu  huyo yu juu ya yote, dhuruba yoyote ikikusumbua, mateso yoyote yakikusumbua, magonjwa yoyote yakikusumbua, majungu yoyote yakikusumbua, mtu yeyote akikusumbua, mwenye mamlaka yeyote akizingua, changamoto zozote zikikusumbua unapaswa kuzikumbusha tu kuwa AJAYE KUTOKA JUU HUYO YU JUU YA YOTE, Kristo Yesu sio wa kulinganishwa na nabii yeyote, wala mtume yeyote wa dini yeyote wala mwanafalsafa yeyoye, wala mwasiasa yeyote, wala msanii yeyote, wala kiongozi yeyote, watambulishe na kuwajulisha kuwa ajaye kutoka juu huyu yu juu ya yote, kama liko jambo linajitukuza juu yako, linaonekana kuwa gumu kwa sababu yoyote,  lina jina la kutisha, linakuogopesha, linakunyima usingizi, linakudhoofisha, iwe ni ndoa, watoto, kazini, biasharani, mdeni na kadhalika wote washitakie kwa Huyu mwamba aliye juu ya yote, aliye juu ya majeshi yote anayeweza kukushindia vita yoyote ambaye asili yake sio ya dunia huyu amekuja kutoka juu ana mamlaka yote kwa faida ya mahitaji yetu yu juu ya yote! Yesu kuwa juu ya yote maana yeke tunaweza kuliitia jina lake kwa changamoto zozote zile maana yeye yuko juu ya hizo, haupaswi kuogopa, haupaswi kulia, haupaswi kuhuzunika, haupaswi kusikitika tunaye aliye juu ya yote!

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

0718990796

Hakuna maoni: