Mathayo 7:24-27 “Basi kila asikiaye hayo
maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga
nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma,
zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba.
Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu,
aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo
zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.”
Utangulizi:
Moja ya maneno ya msingi sana
yanayohitimisha hutuba maarufu ya Bwana Yesu, maarufu kama Hutuba ya Mlimani ni
pamoja na mfano wa mjenzi mwenye hekima na yule mjenzi mpumbavu, ambao ni mfano
alioutumia Yesu Kristo kukazia hutuba yake kuonyesha umuhimu wa kusikia na
kulitendea kazi neno lake, kimsingi kulitendea kazi neno kunajenga msingi imara
sana wa kiroho, msingi usiotikisika
katika maisha ya kila mwanafunzi wa Yesu, uwezo wa kustahimili majaribu na magumu, Lakini pia usalama wa
kukaa ndani ya Yesu, sawa na nyumba
iliyojengwa juu ya mwamba ambayo inakuwa na uwezo wa kustahimili dhuruba za
aina mbalimbali na kukaa kwa usalama na kudumu.
Luka 6:47-49 “Kila mtu ajaye kwangu, na
kuyasikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake. Mfano wake ni
mtu ajengaye nyumba, na kuchimba chini sana, na kuweka msingi juu ya mwamba; na
kulipokuja gharika, mto uliishukia nyumba ile kwa nguvu, usiweze kuitikisa; kwa
kuwa imejengwa vizuri. Lakini yule aliyesikia ila hakutenda, mfano wake ni mtu
aliyejenga nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ukaishukia kwa nguvu,
ikaanguka mara; na maangamizi yake nyumba ile yakawa makubwa.”
Kimsingi neno la Mungu linampa
umuhimu mkubwa mtu anayelitendea kazi neno la Mungu, na mfano huu Yesu aliutoa
sawa na tu na agizo linalotutaka tuwe watendaji wa neno na sio wasikiaji, moja
ya changamoto kubwa katika nyakati za leo, sio kukosekana kwa mafundisho au
watu kuisikia injili lakini changamoto kubwa iko kwamba ni nani analifanyia
kazi neno la Mungu, uwezo wetu wa kusikia hauko katika kusikia bali kutenda
Wayahudi wanaita agizo hilo SHEMA yaani
SIKIA Israel.
Marko 12:29-30 “Yesu akamjibu, Ya kwanza
ndiyo hii, SIKIA, Israeli, Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja; nawe mpende Bwana
Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote,
na kwa nguvu zako zote.”
Mathayo 21:28-32 “Lakini mwaonaje? Mtu
mmoja alikuwa na wana wawili; akamwendea yule wa kwanza, akasema, Mwanangu, leo
nenda kafanye kazi katika shamba la mizabibu. Akajibu akasema, Naenda, Bwana;
asiende. Akamwendea yule wa pili, akasema vile vile. Naye akajibu akasema,
Sitaki; baadaye akatubu, akaenda. Je! Katika hao wawili ni yupi aliyefanya
mapenzi ya babaye? Wakamwambia, Ni yule wa pili. Basi Yesu akawaambia, Amin
nawaambia, watoza ushuru na makahaba wanatangulia mbele yenu kuingia katika
ufalme wa Mungu. Kwa sababu Yohana alikuja kwenu kwa njia ya haki, ninyi
msimwamini; lakini watoza ushuru na makahaba walimwamini, nanyi hata mlipoona,
hamkutubu baadaye, ili kumwamini.”
Yakobo 1:22-25 “Lakini iweni watendaji wa
neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. Kwa sababu mtu akiwa
ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia
uso wake katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi
alivyo. Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo,
asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika
kutenda kwake.”
Kimsingi maandiko yote na mifano
yote hapo inatolewa kusisitiza ujumbe mmoja wa kulifanyia kazi neno la Mungu, yaani
kulitenda au kuliishi, Mtu anayelitendea kazi neno la Mungu huyu anafananishwa
na mtu aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba imara na kwa sababu hiyo dhoruba za
kimwili na kiroho na kiakili na kisaikolojia na mafundisho potofu, haziwezi
kumdhuru kwa sababu amejengwa juu ya Mwamba, Leo tutachukua muda kujifunza juu
ya somo hili Muhimu, Heri aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba na kuliangalia
somo hili katika vipengele vitatu vifuatavyo:-
·
Maana ya
neno Mwamba.
·
Heri
aliyejenga nyumba yake juu ya Mwamba.
·
Jinsi ya
kujijenga juu ya Mwamba.
Maana ya neno Mwamba.
Ni muhimu kufahamu kuwa moja ya
msamiati muhimu sana ambao umetumika mara nyingi katika neno la Mungu ni pamoja
na neno MWAMBA, Neno Mwamba
tunalolisoma katika maandiko kwa mujibu wa muktadha wake mara nyingi limetajwa
kwa Lugha ya Kiebrania kama neno Sela’,
Cῡr
na Kēphīm, sawa na maneno Kēphas
na Pétra
katika Lugha ya Kiyunani Katika Kiingereza
tunapata maneno Rock au neno Solid Foundation kwa Kiswahili Mwamba
au Msingi imara, Pamoja na neno hili kutumika kitaalamu katika maswala ya
miamba na ujenzi, katika uhalisia wake, katika Lugha ya kinabii mara nyingi
neno Mwamba lilitumika kumtaja Mungu
mwenyewe, Kristo au neno la Mungu:-
2Samuel 22:1-4 “Basi Daudi akamwambia Bwana
maneno ya wimbo huu, siku ile Bwana alipomwokoa mikononi mwa adui zake zote, na
mkononi mwa Sauli; akasema, Bwana ndiye jabali langu, na ngome yangu, na
mwokozi wangu, naam, wangu; Mungu wa MWAMBA wangu, nitamwamini yeye; Ngao
yangu, na pembe ya wokovu wangu, mnara wangu, na makimbilio yangu; Mwokozi
wangu, waniokoa na jeuri. Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa; Hivyo nitaokoka
na adui zangu.”
Zaburi 71:1-3 “Nimekukimbilia Wewe, Bwana,
Nisiaibike milele. Kwa haki yako uniponye, uniopoe, Unitegee sikio lako,
uniokoe. Uwe kwangu MWAMBA wa makazi yangu, Nitakakokwenda sikuzote. Umeamuru
niokolewe, Ndiwe genge langu na ngome yangu.”
Isaya 17:10 “Maana umemsahau Mungu wa
wokovu wako, wala hukuukumbuka MWAMBA wa ngome yako; kwa sababu hiyo ulipanda
mashamba yapendezayo, na kutia ndani yake mizabibu migeni.”
Zaburi 61:1-3 “Ee Mungu, ukisikie kilio
changu, Uyasikilize maombi yangu. Toka mwisho wa nchi nitakulilia nikizimia
moyo, Uniongoze juu ya MWAMBA nisioweza kuupanda. Kwa maana ulikuwa kimbilio
langu, Ngome yenye nguvu adui asinipate.”
Kumbukumbu 32:3-4 “Maana nitalitangaza Jina
la Bwana; Mpeni ukuu Mungu wetu. YEYE MWAMBA, kazi yake ni kamilifu; Maana,
njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, Yeye ndiye mwenye
haki na adili.”
1Wakorintho 10:4 “wote wakanywa kinywaji
kile kile cha roho; kwa maana waliunywea MWAMBA wa roho uliowafuata; na mwamba
ule ulikuwa ni Kristo.”
Unaona kwa msingi huo katika
lugha ya kinabii, Neno la Mungu halizungumzii Mwamba wa kawaida au jiwe la
kawaida au Msingi mgumu bali inamzungumzia Mungu mwenyewe na sifa zake
alizonazo za Uimara, Uthabiti, Usalama na Uwepo wake wa milele, Mungu
anapowaita watu wake yaani Kanisa anakuwa amewajenga juu ya Mwamba, na kwa sababu hiyo Shetani hana
uwezo, wala kuzimu hakuna uwezo wowote wa kulishinda Kanisa lake, kwa sababu
amelijenga juu yake yeye Mwenyewe
Mathayo 16:17-18 “Yesu akajibu, akamwambia,
Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali
Baba yangu aliye mbinguni. Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya MWAMBA
huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda.”
Waefeso 2:20-22 “Mmejengwa juu ya msingi wa
mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni. Katika
yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika
Bwana. Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika
Roho.”
Watu waliomwamini Bwana Yesu
wamejengwa juu ya Mwamba ambaye ni Yesu Kristo mwenyewe, na Neno lake, Mtu
akilitendea kazi neno la Mungu anafananishwa na mtu aliyejenga nyumba yake juu
ya MWAMBA yaani Kristo na neno lake,
huyu anakuwa amejijenga juu ya msingi imara usiotikisika, kwa ujumla neno la
Mungu linazungumzia maisha yaliyojengwa juu ya Mungu, Kristo wake na Neno lake
ambalo halibadiliki, pamoja na na jina lake lenye nguvu, maisha ya aina hii
humfanya mtu aishi kwa amani kwa sababu anamjua sana Mungu kwa hiyo hata apitie
dhuruba za aina yoyote duniani, dhuruba hizi haziwezi kumtikisa hata kidogo,
Kwa hiyo ili mtu awe imara katika maisha haya hana budi, kujijenga katika
kumjua sana Mungu, kumfahamu sana Yesu Kristo huu ni ndio utajiri unaoweza
kutuhakikishia usalama wa maisha ya kiroho na kimwili!
Yohana 17:2-3 “kama vile ulivyompa mamlaka
juu ya wote wenye mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele. Na
uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo
uliyemtuma.”
Ayubu 22:21 “Mjue sana Mungu, ili uwe na
amani; Ndivyo mema yatakavyokujia.”
Heri aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba.
Neno Heri maana yake ni Baraka
kubwa sana au amebarikiwa mtu yule aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba, Hapa
Mungu hamaanishi kujenga nyumba halisi, hapa anamaanisha mtu ambaye maisha yake
amewekeza juu ya Mungu, Juu ya Kristo na juu ya Neno la Mungu au jina lake, mtu wa aina hii Maandiko yanaonyesha kuwa mtu
aliyejijenga katika Kristo, kujikita katika kumfahamu Yesu Kristo, kulijua neno
lake na kuishi sawa na neno lake huyu ni
mtu asiyeweza kuyumbishwa na lolote hapa duniani na kuzimu pia, Kumbuka wala
malango ya kuzimu hayataliweza hii maana yake mtu aliyejijenga katika kumjua
Mungu maishani mwake hawezi kutikiswa hata kidogo!
Ni mtu asiyeweza kuyumbishwa – Kwa kawaida Mwamba huwa hauyumbishwi,
ni jiwe lenye msimamo, ni gumu ni la kudumu ni la milele, huwezi kulitikisa
unaweza kukimbilia juu ya MWAMBA au
chini yake na ukawa salama kwa hiyo ukijijenga juu ya Yesu na juu ya neno lake
na jina lake lililo takatifu sana unahakikishiwa usalama na uwepo wa kudumu na
kutokuonolewa au kutikiswa kwa sababu zozote zile, si kuwa hutapitia magumu
kabisa lakini hata ukipitia hayatakutikisa kabisa! Si kuwa hutapatwa na majaribu lakini yakikupata hatutatikiswa,
sababu uko juu ya mwamba
Mathayo 7:25 “mvua ikanyesha, mafuriko
yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake
imewekwa juu ya mwamba.”
Mtu aliyejikita katika kumjua
Mungu, aliyejikita katika kulijua neno lake mtu anayemtegemea Mungu katika kila
jambo sio kuwa hatakutwa na dhuruba, sio kuwa mafuriko hayatampiga, sio kuwa
pepo hazitavuma juu yake, hii ikimaanisha kuwa atapitia katika moto, atapita
katika dhiki, atapita katika maji, atapigwa na pepo zinazovuma lakini kwa kuwa
amejikita juu ya mwamba hakuna kitakachoweza kuufarakanisha uwepo wake na Yesu.
Zaburi 46:1-5 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio
na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa
ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma
na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake. Kuna mto, vijito vyake
vyaufurahisha mji wa Mungu, Patakatifu pa maskani zake Aliye juu. Mungu yu
katikati yake hautatetemeshwa; Mungu atausaidia asubuhi na mapema.”
Zaburi 27:1-4 “Bwana ni nuru yangu na
wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani?
Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu,
Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu
hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini. Neno Moja nimelitaka kwa
Bwana, Nalo ndilo nitakalolitafuta, Nikae nyumbani mwa Bwana Siku zote za
maisha yangu, Niutazame uzuri wa Bwana, Na kutafakari hekaluni mwake”
Zaburi 23:4 “Naam, nijapopita kati ya bonde
la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako
na fimbo yako vyanifariji.”
Isaya 43:1-2 “Lakini sasa, Bwana
aliyekuhuluku, Ee Yakobo, yeye aliyekuumba, Ee Israeli, asema hivi, Usiogope,
maana nimekukomboa; nimekuita kwa jina lako, wewe u wangu. Upitapo katika maji
mengi nitakuwa pamoja nawe; na katika mito, haitakugharikisha; uendapo katika
moto, hutateketea; wala mwali wa moto hautakuunguza.”
Ulinzi wa kudumu – Nyakati za agano la kale watu wengi sana walitafuta
usalama katika miamba, walifahamu kuwa kama kukitokea janga lolote lile mahali
salama ni kwenye JABALI au kwenye MWAMBA, ni MWAMBA ndio ulimpa mtu ulinzi na usalama wa kudumu kwa hiyo ujenzi
pia unaozingatia usalama unajengwa juu ya Mwamba na sio vinginevyo.
Zaburi 18:1-6 “Wewe, Bwana, nguvu zangu,
nakupenda sana; Bwana ni JABALI langu, na boma langu, na mwokozi wangu, Mungu
wangu, MWAMBA wangu ninayemkimbilia, Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, na
ngome yangu. Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa, Hivyo nitaokoka na adui zangu.
Kamba za mauti zilinizunguka, Mafuriko ya uovu yakanitia hofu. Kamba za kuzimu
zilinizunguka, Mitego ya mauti ikanikabili. Katika shida yangu nalimwita Bwana,
Na kumlalamikia Mungu wangu. Akaisikia sauti yangu hekaluni mwake, Kilio changu
kikaingia masikioni mwake.”
Mtu aliyejijenga juu ya mwamba
ana ulinzi wa kudumu, Maagano ya Mungu wetu sio ya siku moja ni agano la kudumu
ni agano la milele, kwa hiyo mtu akimtumainia Yesu Kristo ana ulinzi wa kudumu,
Yesu hafanyi jana tu yeye ni wa siku zote jana, leo na hata milele, ulinzi wake
ni wa milele, msamaha wake ni wa milele, fadhili zake ni za milele hakuna kitu kitakachoweza
kututenga na upendo wake, hatujamjia Yesu kwa majaribio bali tumemjia yeye kwa
sababu anastahili kujiliwa, yeye ni usalama wetu wa milele kwa jambo lolote
lile na kwa jaribu lolote lile!
Warumi 8:33-39 “Ni nani atakayewashitaki
wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia
adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika
wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. Ni nani
atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au
uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako
tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini
katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.
Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala
malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye
uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote
hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”
Usalama wa milele – Ni mwamba ndio humuhakikishia mtu usalama wa
milele, kwa hiyo mtu akijijenga juu ya mwamba anajihakikishia Msamaha, na uzima
kulindwa dhidi ya hatari zozote zile ziwe za kimwili na kiroho, mwamba unakupa
Amani hata kutokee mafuriko au pepo zinazovuma kama umejenga juu ya mwamba utalala usingizi mtamu
Waebrania 10:10-14 “Katika mapenzi hayo
mmepata utakaso, kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu. Na kila kuhani
husimama kila siku akifanya ibada, na kutoa dhabihu zile zile mara nyingi;
ambazo haziwezi kabisa kuondoa dhambi. Lakini huyu, alipokwisha kutoa kwa ajili
ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu;
tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake. Maana kwa
toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa.”
Yohana 10:27-29 “Kondoo wangu waisikia
sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala
hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba
yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika
mkono wa Baba yangu.”
Jinsi ya kujijenga juu ya mwamba.
Tumeona faida kubwa sana na
Baraka za mtu aliyejenga juu ya Mwamba, hata hivyo ni muhimu kwetu kujifunza
kwa kuhitimisha ili kuangalia kuwa tunawezaje kujijenga juu ya mwamba?
1.
Kumtegemea
Mungu – Kwa kuwa Mungu ndiye Mwamba maisha ya mtu anayemtegemea Mungu
hayategemei mabadiliko ya hali ya hewa au mambo, sisi tunaye Mungu
asiyebadilika, Sifa mojawapo ya mwamba ni kutokubadilika, miaka nenda miaka
rudi mwamba hubakia vile vile, siku zote, Mwamba ni mgumu una nguvu, mwamba ni
wa milele, mwamba ni wa kudumu, mwamba ni ngome, mwamba ni wa kuaminiwa, mwamba
ni wa kutumainiwa mwana unaweza kumlinda mtu dhidi ya adui, mwamba unakubeba.
Zaburi 62:1-8 “Nafsi
yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake. Yeye tu
ndiye MWAMBA wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. Hata lini
mtamshambulia mtu, Mpate kumwua ninyi nyote pamoja? Kama ukuta unaoinama, Kama
kitalu kilicho tayari kuanguka, Hufanya shauri kumwangusha tu katika cheo
chake; Huufurahia uongo. Kwa kinywa chao hubariki; Kwa moyo wao hulaani. Nafsi
yangu, umngoje Mungu peke yake kwa kimya. Tumaini langu hutoka kwake. Yeye tu
ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. Kwa Mungu
wokovu wangu, Na utukufu wangu; MWAMBA wa nguvu zangu, Na kimbilio langu ni kwa
Mungu. Enyi watu, mtumainini sikuzote, Ifunueni mioyo yenu mbele zake; Mungu
ndiye kimbilio letu.”
2.
Kudumu
Katika maombi na ibada – Maombi na ibada, kusoma neno la Mungu, kusikiliza
mahubiri mbalimbali, kujisomea neno la Mungu kulijadili na kujifunza
kunatutengenezea ukaribu wenye nguvu na Mungu na kwa sababu hiyo kwa kufanya
hivyo tunajiimarisha juu ya mwamba, tunakuwa na uhusiano wa karibu sana na
Mungu, kujitoa kwa Mungu “Devotions”
kunatushikamanisha na Mwamba na kwa sababu hiyo sio rahisi kwetu kuyumbishwa
kwa namna yoyote ile na mtu yeyote na fundisho lolote!
Yeremia 33:1-3 “Tena,
neno la Bwana likamjia Yeremia mara ya pili, hapo alipokuwa akali amefungwa
katika uwanda wa walinzi, kusema, Bwana alitendaye jambo hili, Bwana aliumbaye
ili alithibitishe; Bwana ndilo jina lake; asema hivi, Niite, nami nitakuitikia,
nami nitakuonyesha mambo makubwa, magumu usiyoyajua.”
3.
Kulitendea
kazi neno la Mungu – Kristo ameonyesha wazi kuwa kulitendea kazi neno lake
kunafananishwa na kujenga juu ya mwamba na kutokulitendea kazi neno lake
kunafanyanishwa na kujenga kwenye mchanga, kwa msingi huo hatuna budi
kulitendea kazi neno la Mungu kwa kadiri ya neema ili kuimarisha uhusiano wetu
na Mungu wetu na kumuelewa au kumjua yeye kwa kina na mapana na marefu.
Mathayo 7:24-27 “Basi
kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye
akili, aliyejenga nyumba yake juu ya MWAMBA; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja,
pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa
juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na
mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko
yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa
kubwa.”
4.
Kuishi
maisha ya toba – Ni maisha ya toba pekee yanayoweza kumsaidia mtu kudumisha
uhusiano wake na Mungu, watu wengi sana wanafikiri kuwa ujumbe kuhusu toba ni
ujumbe kwa wasiookoka lakini ukweli ni kuwa ujumbe wa toba unalihusu Kanisa na
unawahusu watu wa Mungu, Hakuna namna yoyote ile tunaweza kubaki katika Mwamba
yaani Yesu Kristo bila kuwa na toba neno toba katika kiyunani ni “Metanoia” maana yake kugeuka na kuacha
njia mbaya, toba inawahusu watu wa Mungu kugeuka na kuacha njia zao mbaya!
2Nyakati 7:14 “ikiwa
watu wangu, walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha, na kuomba, na
kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia toka mbinguni, na
kuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao. Sasa macho yangu yatafumbuka, na
masikio yangu yatasikiliza maombi ya watu waombao mahali hapa.”
Ufunuo 2:2-5 “Nayajua
matendo yako, na taabu yako, na subira yako, na ya kuwa huwezi kuchukuliana na
watu wabaya, tena umewajaribu wale wajiitao mitume, nao sio, ukawaona kuwa
waongo; tena ulikuwa na subira na kuvumilia kwa ajili ya jina langu, wala
hukuchoka. Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza.
Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza.
Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika
mahali pake, usipotubu.”
Ufunuo 2:13-15 “Napajua
ukaapo, ndipo penye kiti cha enzi cha Shetani; nawe walishika sana jina langu,
wala hukuikana imani yangu, hata katika siku za Antipa shahidi wangu, mwaminifu
wangu, aliyeuawa kati yenu, hapo akaapo Shetani. Lakini ninayo maneno machache
juu yako, kwa kuwa unao huko watu washikao mafundisho ya Balaamu, yeye
aliyemfundisha Balaki atie ukwazo mbele ya Waisraeli, kwamba wavile vitu
vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na kuzini. Vivyo hivyo wewe nawe unao watu
wayashikao mafundisho ya Wanikolai vile vile. Basi tubu; na usipotubu, naja
kwako upesi, nami nitafanya vita juu yao kwa huo upanga wa kinywa changu.”
5.
Kuishi
maisha Matakatifu – Mungu wetu ni Mtakatifu, hii sifa ya utakatifu ni sifa
yake yeye na hakuna awaye yote mwingine ambaye anasifa hii, Yeye kama Mwamba
moja ya sifa yake ni utakatifu, kwa hiyo ili mtu aweze kuwa salama juu ya
mwamba huu, maana yake maisha matakatifu yanamhusu, na hakuna njia ya mkato,
nyakati tulizo nazo imekuwa ngumu sana kusikia watu wakihubiri utakatifu lakini
wito wa Mungu kwa kanisa lake ni pamoja na kuishi maisha matakatifu ili
kujihakikishia usalama kwa Mungu wetu.
2Samuel 2:1-2 “Naye
Hana akaomba, akasema, Moyo wangu wamshangilia Bwana, Pembe yangu imetukuka
katika Bwana, Kinywa changu kimepanuka juu ya adui zangu; Kwa kuwa naufurahia
wokovu wako; Hakuna aliye MTAKATIFU kama Bwana; Kwa maana hakuna ye yote ila
wewe, Wala hakuna MWAMBA kama Mungu wetu.”
Isaya 6:1-3 “Katika
mwaka ule aliokufa mfalme Uzia nalimwona Bwana ameketi katika kiti cha enzi,
kilicho juu sana na kuinuliwa sana, na pindo za vazi lake zikalijaza hekalu.
Juu yake walisimama maserafi; kila mmoja alikuwa na mabawa sita; kwa mawili
alifunika uso wake, na kwa mawili alifunika miguu yake, na kwa mawili aliruka.
Wakaitana, kila mmoja na mwenzake, wakisema, MTAKATIFU, MTAKATIFU, MTAKATIFU,
ni Bwana wa majeshi; dunia yote imejaa utukufu wake.”
Walawi 20:26 “Nanyi
mtakuwa watakatifu kwangu mimi; kwa kuwa mimi BWANA ni MTAKATIFU nami
nimewatenga ninyi na mataifa, ili kwamba mwe wangu.”
1Petro 1:15-16. “bali
kama yeye aliyewaita alivyo MTAKATIFU, ninyi nanyi iweni watakatifu katika
mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni
mtakatifu.”
Heri yule aliyejenga Nyumba yake
juu ya Mwamba, maana yake heri mtu yule aliyewekeza maisha yake kwa Mungu wetu
na Kristo wake na Neno lake na jina lake, Mtu wa namna hii ana maisha thabiti
yasiyoyumbishwa na dhuruba, wala pepo wala mafuriko wala changamoto za aina
yoyote na ana uhakika wa uzima wa milele, Neno la Mungu linatoa wito kwetu
kuwekeza katika kristo kwa usalama wa uhakika wa maisha yetu!.
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni