Jumapili, 7 Septemba 2025

Chembe ya ngano isipoanguka!


Yoahana 12:23-25 “Naye Yesu akawajibu, akasema, Saa imefika atukuzwe Mwana wa Adamu. Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.”



Utangulizi:

Leo tunachukua muda kiasi kutafakari maneno ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyoyasema karibu na mwishoni kabisa mwa huduma yake Duniani, Yesu alikuwa ametembelewa na kundi kubwa la jamii ya watu wasiokuwa wayahudi, yaani Wayunani ambao kimsingi nao walikuwa na kiu na hamu na shauku ya kupata huduma ya Bwana wetu Yesu Kristo, Yesu anaiona shauku yao kama hitaji kubwa sana la kiroho kwa jamii ya watu wote duniani kama watu wanaomuhitaji Mungu na Mwokozi katika maisha yao, Hata hivyo kuhudumia jamii ya watu wote duniani kwa vyovyote vile kungemlazimu kutimiza mapenzi ya Mungu ya kufa msalabani ili aweze kuwa fidia ya wengi kama yanenavyo maandiko:-

Yohana 3:16 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”

Luka 2:34-35 “Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. Nawe mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi.”

Akifafanua juu ya mauti yake huku akiunganisha na mafundisho yahusuyo kujikana nafsi, Yesu anatumia mfano wa wakulima wa ngano ili kufafanua kanuni ya kiroho ya kuleta mafanikio na kuzaa matunda mengi inavyogharimu maisha ya waanzilishi ili kuleta uzima kwa wengi au kwa ulimwengu na ndipo anapotumia mfano wa Chembe ya ngano (Yaani mbegu ya ngano) kwamba ili iweze kutoa mazao mengi ni lazima ife na kuzikwa na inapoota yaani kufufuka inasababisha mazao mengi sana.

Tutajifunza ujumbe huu Chembe ya ngano isipoanguka kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-


·         Maana ya kuanguka kwa chembe ya ngano.

·         Chembe ya ngano isipoanguka!.

·         Faida za kuanguka kwa chembe ya ngano.


Maana ya kuanguka kwa chembe ya ngano.

Ni muhimu kufahamu kuwa Pamoja na ukulima wa zabibu, ufugaji wa wanyama wa aina mbalimbali,kama kondoo, mbuzi na ng’ombe, watu wa mashariki ya kati hususani Israel na baadhi ya waarabu ni watumiaji wazuri sana wa ngano kwaajili ya chakula na hasa mikate, sasa ili Yesu aweze kueleweka vizuri katika jamii yake alitumia mifano ya vitu vya karibu na vilivyozoeleka katika jamii yake ili aweze kuwasilisha ujumbe wa kiroho wenye maana inayoeleweka kwa watu wake, Yesu hapa anatumia mfano wa chembe ya ngano (yaani mbegu ya ngano) ambayo ili iweze kuzaa matunda mengi zaidi hutupwa au kuzikwa shambani na kisha inakufa katika udongo au ardhini na inapofufuka/kuota kama mmea na kuzaa inazalisha matunda au mbegu nyingine bora zaidi hii ndio kanuni ya kilimo.

Yohana 12:24 “Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi.”

·         Chembe ya ngano kwa kiyunani (Greek) inaitwa “ho kokkos tou sitou” kwa kiingereza “a grainof wheat”  ikimaanisha mbegu ya ngano

·         Kuanguka  kwa kiyunani (Greek) linatumika neno Piptō linalomaanisha kuanguka chini kwa hiyari, au kuangushwa kwa kusudi au kupanda

·         Kufa  kwa kiyunani (Greek) linatumika neno apothnēskō linalomaanisha kufa kimwili au kufa kwa hiyari yaani kwa kiingereza “Self- denial” “Self-sacrificial” kujitoa dhabihu, kujikana au kujikataa au kujitoa sadaka.

Waebrania katika mtazamo wao kuhusu mbegu siku zote waliamini ndani ya mbegu kua kuna UZIMA, URITHI, na KIZAZI, walikuwa wanatambua kuwa uhai hauwezi kuendelea bila ya kuwako kwa mbegu, lakini ili mbegu iweze kuendeleza uhai na uzima na urithi na kizazi ni lazima mbegu hiyo itolewe kutoka kwenye kuhifadhiwa na itupwe katika moyo wa ardhi, kisha ife na izikwe na kuchipuka ndipo iweze kuendeleza kizazi kwa hiyo mbegu katika mukthadha wa wayahudi inaitwa ZERA ikimaanisha UZAO 

Mwanzo 22:12-18 “Malaika wa BWANA akamwita Ibrahimu mara ya pili kutoka mbinguni akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”

Yesu alikuwa anatambua kwamba ni lazima ajidhabihu yeye mwenyewe kwaajili ya kuufikia ulimwengu, alifahamu wazi kuwa yeye hakuja kwaajili ya wayahudi pekee, bali alikuja kwaajili ya ulimwengu mzima, alifahamu kuwa anahitajika sio na wayunani pekee bali na ulimwengu mzima na kwa sababu hiyo, kujidhabihu kwaajili ya ulimwengu mzima kungerahisisha ukombozi utakaozaa matunda kwa Mungu wetu yaliyo mengi, Lakini wakati huo huo Yesu aliwataka wanafunzi wake wote ikiwa ni pamoja na wewe na mimi kuwa na ufahamu ya kuwa maisha ya uanzilishi wa kitu chchote yanahusisha kujitoa na kujidhabihu na matunda yake yangelikuja kuonekana mbeleni!, Yeye kama Uzao wa Ibrahimu ilikuwa ni lazima ajitoe sadaka yeye mwenyewe kwa hiyari ili mataifa yote waweze kubarikiwa

Tito 2:11-14 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa; tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu; ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi yote, na kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema.”

Waefeso 5:1-2 “Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; mkaenende katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato.”

Maandiko hayo yanadhihirisha wazi kuwa kusulubiwa kwa Yesu Kristo halikuwa tukio la kupangwa na wazee na wakuu wa makuhani, lakini lilikuwa ni tukio la Yesu Kristo mwenyewe kujidhabihu na kukubali kufa na kufufuka kutoka kwa wafu ili atukomboe wanadamu, Yeye alikuwa  ni chembe ya ngano ambayo ilikuwa lazima ianguke ili kusababisha mazao mengi sana duniani.                      

Chembe ya ngano isipoanguka!.

Yoahana 12:23-25 “Naye Yesu akawajibu, akasema, Saa imefika atukuzwe Mwana wa Adamu. Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.”

Yesu anatumia msemo huu  wa chembe yaani mbegu ya ngano kama mfano (Metaphor)  kuonyesha kuwa mbegu ili iweze kuleta mavuno mengi sana ni lazima ianguke, izikwe ardhini kisha inapochipuka yaani kuota na kustawi inaleta mavuno makubwa sana, kanuni hii ni kanuni ya kilimo lakini ni kanuni ya kiroho na kanuni ya kawaida katika maisha.

Yesu anaonyesha kuwa wakati mwingine ili mtu aweze kuzaa matunda, hakuna budi watu wajikane nafsi na kujidhabihu kama yeye, lakini sio hivyo tu kuishi maisha ya kumfuata Yesu na kumpendeza vile vile kunahitaji kujikana nafsi, Ni lazima ujikane ili uweze kuishi maisha matakatifu nay a mfano, bila kujikana ni ngumu kuona mazao

Luka 9:22-25 “akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka. Akawaambia wote, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha. Kwa kuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, au kujipoteza mwenyewe?

Chembe ya ngano isipoanguka hakuna lolote linaloweza kutokea, watu wasipojidhabihu na kujioa hakuwezi kutokea mabadiliko yoyote chanya katika jamii, mambo mengi tunayoyaona duniani na kuyafurahia wakati mwingine yamegharimu maisha ya watu wengine lakini wengi wanafaidika leo kutokana na kuumia kwa watu wengine, hususani waanzilishi wa mambo, Imani, mataifa, ustawi, uanzishwaji wa taasisi yoyote ile, upatikanaji wa Amani na kadhalika, huwa haviwezi kupata usitawi bila watu kujikana, kujiyoa na kujidhabihu, maisha ya kujitoa kwaajili ya jamii yanaweza kuumiza wachache lakini yakanufaisha wengi, Leo hii tunaushangilia wokovu na kujivunia lakini yaligharimu maisha ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo aligharimika pale msalabani na kwa kupigwa kwake tumepona

Marie Curie ambaye ni mgunduzi wa tiba ya kutumia mionzi (Radiation in Medicine) alifariki dunia tarehe 04 Julai 1934 huko ufaransa akiwa na miaka 66, Mwanamke huyu aliyekuwa mwanasayansi alihatarisha maisha yake hata kufa baada ya kuathiriwa na mionzi hiyo alipokuwa anafanya kazi za kitafiti na matumizi ya tiba ya mionzi ya (radium and Plonium) ambayo leo imekuwa msaada mkubwa sana katika tiba ya kiuchunguzi ya mionzi kama X-Rays

Katika maisha wakati mwingine mambo hayawezi kutokea mpaka watu wengine wamesimama kidete na kuhatarisha maisha yao au hata kufa kwaajili ya kusababisha mabadiliko yatokee, Mahatma Gandhi alijitoa maisha yake kusababisha nchi ya India kupata uhuru wake  kutoka kwa waingereza akianzisha harakati za kuandamana bila kufanya ghasia, akivumilia vifungo mbalimbali na hata wakati mwingine aliacha kula yaani akifunga na kujinyima ili haki za kibinadamu zipatikane  katika India inayofurahia matunda ya uhuru huo leo.

Wakristo, na watumishi wa Mungu katika mazingira mbalimbali, tunapaswa kuelewa Yesu alikuwa anamaanisha kwamba bila wengine kujitoa muhanga, maisha yao, fedha zao, starehe zao, mifungo yao, kesha zao, maisha ya familia zao, haki, na injili haiwezi kuwafikia watu wa Mungu, umasikini hauwezi kuondoka, unyonge hauwezi kuisha, ukandamizwaji hauwezi kukomeshwa, udhalimu hauwezi kutokomea, maovu yataendelea kuongezeka, amani haiwezi kupatikana, ubaguzi hauwezi kuisha, upendeleo hauwezi kuisha, haki haiwezi kupatikana, na uhuru wa kweli hauwezi kupatikana bila baadhi ya watu kujitoa dhabihu yaani  Chembe ya ngano isipoanguka! Inabakia ile ile!

Faida za kuanguka kwa chembe ya ngano.

Kuanguka kwa chembe ya ngano ni kujitoa au kujidhabihu kwaajili ya Mungu, Neno la Mungu linatueleza kuwa kujitoa ndio dhabihu iliyo hai, takatifu na ya kupendeza, kama mtu anataka kumpendeza Mungu basi ni lazima akubali kujitoa, au kujidhabihu, Kwa nini Mungu alipendezwa na Yesu Kristo hata kujivunia kuwa huyu ndiye mwanangu mpendwa ninayependezwa naye? Sababu kubwa ni kuwa Yesu alijitoa yeye mwenyewe

Warumi 12:1 “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana.”

Wafilipi 2:6-11 “ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

Mwanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo ni yule anayejitoa, unapodai kuwa unamfuata Yesu lakini hujitoi maana yake ni sawa na kuwa hauufuati mfano wake, Yeye mwenyewe anamkana kila mtu anayedai kuwa anamfuata yeye lakini hataki kuteseka kwaajili ya Kristo! Kimsingi huwezi kuwa mwanafunzi wa Yesu kama hutaki kugharimika na kumfuata

Luka 14:27 “Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.”

Kila anayejikana kwaajili ya Yesu Kristo na jamii nafsi yake haitapotea kwani atalipwa uzima wa milele, tunapojitoa na kujidhabihu hata kufa kwaajili ya wengine/kifo au mauti yako inayotokana na kujidhabihu haiwi mwisho badala yake unakuwa mwanzo wa uzima na maisha mapya yenye Baraka nyingi na yenye kukuzalia matunda

Isaya 53:5-11 “Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote. Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake. Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu. Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala hapakuwa na hila kinywani mwake. Lakini Bwana aliridhika kumchubua; Amemhuzunisha; Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi, Ataona uzao wake, ataishi siku nyingi, Na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake; Ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika. Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki Atawafanya wengi kuwa wenye haki; Naye atayachukua maovu yao.”     

Yoahana 12:25-26 “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele. Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu.”

Hitimisho.

Kuishi maisha matakatifu kunahitaji kujikana, kuishi kwaajili ya Kristo kunahitaji kujikana, kuwatumikia watu kunahitaji kujikana, kuanzisha kazi mpya kunahitaji kujikana, kufanya umisheni kunahitaji kujikana, kumtumikia Mungu kunahitaji kujikana, kufanya uinjilisti kunahitaji kujikana, kuimba kwaya kunahitaji kujikana, kuomba kunahitaji kujikana, kukesha kunahitaji kujikana, kila kitu duniani na mafanikio yoyote yale duniani hayawezi kuja kama hatuna kujikana, kuleta maendeleo kunahitaji kujikana, bila kujikana katika jambo lolote lile hakuwezi kuwako na matunda yanayokusudiwa, mwanafunzi ili afaulu mitihani yake anahitaji kujikana, kusoma kunahitaji kujikana, biashara inahitaji kujikana, kilimo kinahitaji kujikana maendeleo yoyote yake yanahitaji kujikana hali kadhalika maisha ya kiroho yanahitaji kujikana hii ndio kanuni ya mafanikio, ni lazima chembe ya ngano ianguke, isipoanguka inabakia ile ile, lakini ikifa ikizikwa inatoa mazao mengi sana hii ni kanuni ya wokovu, ni kanuni ya kiroho na ni kanuni ya maisha,  na ni kanuni ya kuleta mafanikio makubwa duniani chembe ya ngano isipoanguka ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi, Ni dua yangu na maombi yangu wasomaji wangu na wasilikizaji wangu tujitoe kwaajili ya kazi ya Mungu kabla ya kuangalia faida zetu binafsi.               

1Wakorintho 15:36-38 “Ewe mpumbavu! Uipandayo haihuiki, isipokufa; nayo uipandayo, huupandi mwili ule utakaokuwa, ila chembe tupu, ikiwa ni ya ngano au nyingineyo; lakini Mungu huipa mwili kama apendavyo, na kila mbegu mwili wake.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima.

+255718990796

Hakuna maoni: