Mathayo 6:31-34 “Msisumbuke, basi, mkisema,
Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa
huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo
yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote
mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe.
Yatosha kwa siku maovu yake.”
Utangulizi:
Mojawapo ya tatizo kubwa la
kiroho na kisaokolojia linalowakumba wanadamu ni pamoja na tatizo la kuogopa
kesho au wakati ujao, tatizo la kuhofia kuhusu kesho au wakati ujao kisakolojia
linaitwa “Chronophobia” au “time anxiety” hofu ya wakati hususani wakati ujao
ambayo kitaalamu inafafanuliwa kama “a
type of anxiety that involves worrying
about tomorrow or future” yaani ni aina ya msongo wa mawazo unaohusisha
kuogopa au hofu kuhusu kesho au wakati ujao, Neno
Chronophobia ni muunganiko wa maneno mawili ya kiyunani “Chronos” yaani muda na “phobos” yaani hofu kwa hiyo wanadamu wengi wanasumbuliwa na hofu kubwa sana
kuhusu itakuwaje kesho, katika Afrika wanawake wengi huongoza kwa hofu hii na
ndio maana wengi huogopa kufiwa na waume zao na utawasikia wakisema kuna leo na
kesho hali itakuwaje? Na wakati
mwingine watu huogopa kuwa huenda kuna jambo baya litawatokea na watu wengi
wanaogopa magumu, wengine huogopa muda kwa kufungwa gerezani, masikini huogopa
kwamba kesho itakuwaje, matajiri huogopa kufilisika, wenye vyeo huogopa
kuviachia, wafanya biashara huogopa hasara, Wengine huogopa muda kwa kufikiri
kuwa wamekawia katika maisha, Tatizo la hofu linaweza kuwako katika pembe
nyingi, Ingawa tatizo hili linaweza kuwa
la kawaida lakini kuna wanadamu wengine tatizo hili huwa kubwa zaidi kwao na linaweza
kufikia hatua likaathiri Imani yao na ni kwa sababu hii Neno la Mungu linamtaka
kila mmoja wetu kutokuogopa kuhusu kesho au wakati ujao na badala yake kumtegemea
Mungu.
Mathayo 6:34 “Basi msisumbukie ya kesho;
kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”
Kwa nini neno la Mungu linatuonya
kutokuogopa kesho? Hii ni kwa sababu Mungu ndiye anayeishika kesho, kesho yako
na wakati wako ujao uko mikononi mwa Mungu na ukilitambua hilo huwezi kuogopa lolote,
Kwa msingi huu basi leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu
juu ya somo hili “Namjua anayeishika
kesho” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-
·
Hofu ya
wanadamu kuhusu kesho.
·
Neno la
Mungu linasemaje kuhusu kesho.
·
Namjua
anayeishika kesho.
Hofu ya wanadamu kuhusu kesho.
Mathayo 6:25-34 “Kwa sababu hiyo
nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu,
mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi?
Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala
hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora
kupita hao? Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata
mkono mmoja? Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba, jinsi
yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti nami nawaambia, ya kwamba hata
Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. Basi,
ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo, na kesho hutupwa
kalibuni, je! Hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba? Msisumbuke,
basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote
Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji
hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote
mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe.
Yatosha kwa siku maovu yake.”
Katika hutuba yake ya mlimani
Mwalimu wetu mkuu na mwokozi wa maisha yetu Yesu Kristo hakuacha kuzungumzia
swala zima la hofu ya wanadamu kuhusu kesho, wanadamu wengi masikini kwa
matajiri wote wanakabiliwa na hofu kuwa itakuwaje kesho au maisha ya baadaye,
hofu hii inaweza ikawa sio tu kwa mahitaji ya kawaida nitakula nini na nitavaa
nini, lakini inaweza kuwa zaidi ya hapo, itakuwaje nikifiwa na mume, itakuwaje
nikifukuzwa kazi, itakuwaje nikifilisika, itakuwaje nikidaiwa kodi, itakuwaje
nikiachwa! Itakuwaje nikiugua? Itakuwaje nikishindwa uchaguzi, itakuwaje
nikifeli, nini kitatokea, itakuwaje uchumi ukiyumba? Na kadhalika hofu hii ni
tatizo kubwa la kiroho na kisaikolojia na Mungu analijua vema, anajua kuwa hofu
hizi zinaweza kumpelekea mtu akakosa Amani, akapoteza usingizi, na hatimaye
akapoteza Imani na matumaini na Ndio maana Yesu aliwafundisha wanafunzi wake
kwamba hawapaswi kuogopa kuhusu kesho kwa sababu Baba wa mbinguni anajua mahitaji
yetu na ndiye anayeishika kesho!.
Neno la Mungu linasemaje kuhusu kesho.
Neno la Mungu linatufundisha ya
kuwa ni Mungu ndiye mwenye uwezo wa kudhibiti kesho ya kila mmoja wetu, na
hakuna mwanadamu ambaye anaweza kujisumbua kuhusu kesho yake na akafanikiwa
bila neema na kibali cha Mungu, hofu yako wasiwasi wako na hata maandalizi yako
hayawezi kukuhakikishia kesho iliyo salama na kamili bila Mungu, kwa sababu
kesho haiko katika mikono ya mwanadamu bali iko katika mikono ya Mungu mwenyewe,
wako watu ambao walijisumbua sana kuhusu kesho na neno la Mungu likawatumia kama
mifano ya kutuonya kuwa huwezi kufanya kitu kuhusu kesho na ukajithibitishia
usalama bila ya Mungu! Kesho iko kwenye mapenzi ya Mungu! Mungu ndiye
anayeishika kesho ili mwanadamu asiwe na kiburi, Tancredo Neves alikuwa mgombea urais wa Brazili mwaka 1985 wakati
wa kampeni zake alisema nikipata kura 500,000 tu kutoka kwenye chama changu
hakutakuwa na wa kuzuia nisiwe Rais hata Mungu hataweza kunizuia, Kwa kweli
alipata kura hizo na akashinda uchaguzi, lakini aliugua ghafla na utumbo
ulijikunja akafariki siku moja kabla ya kuapishwa kuwa raisi Tarehe 21/4/1985.
Lazima kila mmoja kwa unyenyekevu akubali kuwa kesho iko mikononi mwa Mungu na
sio mikononi mwa mwanadamu.
Yakobo 4:13-15 “Haya basi, ninyi msemao,
Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya
biashara na kupata faida; walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni
nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya
kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.”
Luka 12:15-20 “Akawaambia, Angalieni,
jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo
navyo. Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa
sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka
akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge
nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha,
nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka
mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu
wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari
vitakuwa vya nani?”
Maandiko yanatuonya wazi kuwa
hakuna mwanadamu anayeweza kudai kwa sababu zozote zile kwamba anaweza kuwa na
uhakika wa kesho, na hata hivyo hatupaswi kuiogopa kesho pia, lakini kesho iko
katika mikono ya Mungu na kwa sababu hiyo neno la Mungu linatuonya kuiacha hofu
ya kesho katika mikono ya Mungu, badala yake tunatiwa moyo kumuamini Mungu na
kumtegemea yeye kwaajili ya mahitaji yetu ikiwepo kesho yetu, Neno la Mungu halitutii moyo kuogopa kuhusu
kesho kwaajili ya mahitaji yetu, wala halituhakikishii kuwa tunaweza
kutengeneza usalama wetu wa kesho kwa kujilimbikizia ua kujiwekea akiba au kwa
kutafuta sana kunakoambatana na hofu ya kesho na pia hakuna mwanadamu awaye
yote wa ngazi yoyote ile anayeweza kujithibitishia kuwa na kesho iliyo njema
nje ya uweza na mamlaka ya Mungu Mwenyewe. Kwa sababu hiyo hatupaswi kujivuna
au kujisifia lolote kuhusu kesho!
Mithali 27:1-2 “Usijisifu kwa ajili ya
kesho; Kwa maana hujui yatakayozaliwa na siku moja. Mwingine na akusifu wala si
kinywa chako mwenyewe; Mtu mgeni wala si midomo yako wewe.”
Neno la Mungu linaonyesha wazi
kuwa mwenye kesho ni Mungu tu, siku moja tu inaweza kuzaa jambo na
likabadilisha kila kitu katika maisha yetu, kwa sababu hiyo hatuna budi kuishi
kwa unyenyekevu na kwa kumtegemea Mungu pake yake, hatupaswi kuiogopa kesho
kama tunamwamini Mungu na wala hatupaswi kujihami kuhusu kesho kama iko
mikononi mwa Mungu hii maana yake ni nini? Maana yake ni kuwa Mungu ndiye
anayeishika kesho na ukimjua yeye hutaweza kuishi maisha ya hofu ya aina yoyote
ile, ukiwa na uhakika kuwa kesho yako iko kwake!
Namjua anayeishika kesho.
Ni muhimu kufahamu kuwa hakuna
hofu wala woga utakaokutawala endapo tu utagundua kuwa ni Mungu ndiye
anayeishikilia kesho yako, Mungu anaweza kubadilisha mambo kwa usiku mmoja tu,
ukitambua kuwa ni Mungu ndiye anayeishikilia kesho yako hakuna mwanadamu
atakayekutisha wala kukutetemesha kuhusu yajayo, kesho yako haiko katika mikono
ya wanadamu, iko katika mikono ya Mungu, ukimjua yeye anayeshika kesho
hautaogopa mabadiliko ya aina yoyote ile, utamtegemea yeye ambaye ni ngome
iliyo imara naye hatakuangusha,
Mwandishi wa Zaburi hakuwahi kuogopa mabadiliko yoyote yale kwa sababu alikuwa anamjua
Mungu na kutambua ya kuwa ndiye anayeshikilia kila kitu kwa hiyo lolote litokee
haliwezi kututisha kwa sababu yeye Mungu ndiye mwenye kesho yake!
Zaburi 46:1-7 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio
na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa
ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake
yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake. Kuna mto, vijito
vyake vyaufurahisha mji wa Mungu, Patakatifu pa maskani zake Aliye juu. Mungu
yu katikati yake hautatetemeshwa; Mungu atausaidia asubuhi na mapema. Mataifa
yalighadhibika, falme zikataharuki; Alitoa sauti yake, nchi ikayeyuka. Bwana wa
majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.”
Mungu wetu ni Mungu
asiyebadilika, Yeye ni Yeye yule jana leo na hata milele, Yu hai, na bado
anaendelea kubarikia watu wake, anaendelea kulinda watu wake, anakomboa watu
wake, bado ni mtawala wa mbingu na nchi majira na nyakati, ziko mkononi mwake,
hajawahi kupoteza nguvu zake wala uwezo wake Yeye bado ni Bwana Mungu
aliyeziumba mbingu na nchi na bahari na vyote vilivyomo, Ndiye aliyeigawa
bahari ya Shamu, akamzika Farao na majeshi yake, akawalisha watu wake kwa mana,
akawanywesha maji kutoka katika mwamba, akawapigania dhidi ya adui zao,
akatimiza ahadi zake kwa kuwapa nchi ya Mkanaani, nguvu zake hazijawahi
kupungua, alimfufua Lazaro, alimtoa Petro na Paulo na Sila gerezani, hakuna
nguvu inaweza kupingana naye, Yeye ndiye anayeishika kesho, kesho yako haiko
kwa waganga wa kienyeji, kesho yako haiko kwa bosi wako, kesho yako haiko kwa
wenye mamlaka au cheo, kesho yako haiko kwa wachawi, kesho yako haiko kwa
wapiga ramli kesho yako inashikwa na Mungu aliye hai, muumba wa mbingu na nchi,
uaminifu wake unazidi kizazi hata kizazi na yeye anatuwazia mema na yeye habadiliki
ni Yeye Yule jana leo na hata milele, Hakuna mtu anayeweza kuichafua kesho
yako, hakuna mtu anaweza kuizibia kesho yako, kesho yako iko katika mikono ya Mungu,
ukimjua anayeishika kesho yako hutaogopa, hakuna wa kukurudisha nyuma, tunaweza
tusijue lolote kuhusu kesho, lakini tunaweza kumjua anayeishika kesho! Naye ni
mwenye nguvu!
Kama Mungu ndiye anayeishika
kesho yako maana yake unaweza kumuamini yeye kuhusu kesho yako na kutokuogopa
wakati ujao ukijua ya kuwa anatuwazia mema na ana mpango mzuri kwaajili yako:-
Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo
ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa
ninyi tumaini siku zenu za mwisho.”
Kama Mungu ndiye anayeishika
kesho yako maana yake hupawi kuogopa endapo unazingirwa na maadui pande zote na
wanakukusudia mabaya hawawezi kutimiza mpango wao kwa sababu mpango wao sio
mkuu kama wa yule anayeishika kesho:-
Zaburi 31:13-15 “Maana nimesikia masingizio
ya wengi; Hofu ziko pande zote. Waliposhauriana juu yangu, Walifanya hila
wauondoe uhai wangu. Lakini mimi nakutumaini Wewe, Bwana, Nimesema, Wewe ndiwe
Mungu wangu. Nyakati zangu zimo mikononi mwako; Uniponye na adui zangu, nao
wanaonifuatia.”
Kama Mungu ndiye anayeishika
kesho yako maana yake ni yeye anayeweza kukulinda kwa nguvu zake na mkono wake
kiasi kwamba hutakuwa na lolote la kuogopa, hutaogopa wachawi, hutaogopa Shetani,
hutaogopa, laana, hutaogopa wanaoukutishia maisha Imani na tumaini litakuwa
kubwa kwa Bwana Mungu wako na hutaogopa vita wala majeshi makubwa ya adui
yajapojipanga kupigana nawe kwa sababu yuko anayeishika kesho yako!
Zaburi 27:1-5 “Bwana ni nuru yangu na
wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani?
Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu,
Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu
hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini. Neno Moja nimelitaka kwa
Bwana, Nalo ndilo nitakalolitafuta, Nikae nyumbani mwa Bwana Siku zote za
maisha yangu, Niutazame uzuri wa Bwana, Na kutafakari hekaluni mwake. Mradi
atanisitiri bandani mwake siku ya mabaya, Atanisitiri katika sitara ya hema
yake, Na kuniinua juu ya mwamba.”
Kama Mungu ndiye anayeishika
kesho yetu tunajengewa uhakika na matumaini ya kuwa anajishughulisha sana na
mambo yetu, atakutana na mahiaji yetu, na tutaishi kwa kujiamini bila kuogopa
tukijua ya kua kesho ni ya Baba mwenye upendo na rehema ataishughulikia, sina
ada italipwa, sina chakula nitakula, sina nguo nitavaa, sina raha nitapewa,
nina mizigo itapumzishwa, nina madeni yatalipwa, sioni njia ataniongoza, naona
giza atakuwa nuru!
Kumbukumbu 8:11-16 “Jihadhari, usije
ukamsahau Bwana, Mungu wako, kwa kutozishika amri zake, na hukumu zake, na
sheria zake, ninazokuamuru leo. Angalia, utakapokuwa umekula na kushiba, na
kujenga nyumba nzuri na kukaa ndani yake; na makundi yako ya ng'ombe na kondoo
yatakapoongezeka, na fedha yako na dhahabu yako itakapoongezeka, na kila kitu ulicho
nacho kitakapoongezeka; basi hapo moyo wako usiinuke, ukamsahau Bwana, Mungu
wako, aliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa; aliyekuongoza
katika jangwa lile kubwa lenye kitisho, lenye nyoka za moto na nge, nchi ya kiu
isiyokuwa na maji; aliyekutolea maji katika mwamba mgumu, aliyekulisha jangwani
kwa mana, wasiyoijua baba zako; apate kukutweza, apate kukujaribu, ili
kukutendea mema mwisho wako.”
Kama Mungu ndiye anayeishika
kesho yako, maana yake ni kuwa haitakuja utishike na kuweweseka kwa sababu yeye
yuko siku zote, alikuwako tangu mwanzo, habadiliki, hageuki wala hana kigeugeu,
wala kwake hakuna kubadilika badilika Yeye ni Yeye yule jana leo na hata milele Waebrania
13:8 “Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata
milele.”
Yakobo 1:17 “Kila kutoa kuliko kwema, na
kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake
hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeuka-geuka.”
Kama Mungu ndiye anayeishika
kesho yetu basi ni wazi kuwa hakuna jambo lolote lile linaloweza kututenga na
upendo wake, hakuna wa kutuhukumu, hakuna wa kututishia maisha, hakuna wa
kututishia kuhusu kesho, hakuna wa kutupunguzia kitu, hakuna wa kutupokonya ushindi,
hakuna wa kututisha kwa maana kesho iko mikononi mwake
Warumi 8:31-39 “Basi, tuseme nini juu ya
hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Yeye asiyemwachilia
Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje
kutukirimia na mambo yote pamoja naye? Ni nani atakayewashitaki wateule wa
Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu?
Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu,
naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. Ni nani
atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au
uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako
tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini
katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.
Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala
malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye
uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote
hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!
.jpg)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni