Jumapili, 9 Novemba 2025

Dawa isiyoshindwa!


Yeremia 8:21-22 “Kwa sababu ya maumivu ya binti ya watu wangu nimeumia mimi; nimevaa kaniki; ushangao umenishika. Je! Hapana zeri katika Gileadi? Huko hakuna tabibu? Mbona, basi, haijarejea afya ya binti ya watu wangu?




Utangulizi:

Tuwapo duniani kama wanadamu wakati mwingine yako majeraha na maumivu ya mambo tunayokutana nayo katika maisha ambayo ni magumu kupona hususani majeraha ya moyoni, wako watu ambao wanaishi kwa mashaka, wamevunjika moyo, wamekosa amani, wamekata tamaa, wana misiba ya aina mbalimbali katika maisha na wengine wameumizwa na mioyo yao imejaa uchungu hakuna utulivu katika maisha yao, wamelia machozi mpaka wamechoka, hawawezi kutibiwa katika hali ya kawaida, hawawezi kusaidiwa na wanasaikolojia wala washauri nasaha, wanateseka, wana maumivu endelevu wana makovu, mashaka na mgandamizo wa mawazo wameshindwa kupata tiba ya kibinadamu inayoweza kuwasaidia, hakuna dawa, leo nawajulisha kuwa iko Dawa isiyoshindwa!

Nyakati za Biblia ilikuwepo dawa inayojulikana kama “Dawa isiyoshindwa” ambayo ilikuwa na uwezo wa kutuliza maumivu na kurejesha afya ya mtu aliyeumizwa dawa hii ilijulikana kama Zeri ya Gileadi, dawa hii Zeri ilikuwa inapatikana katika sehemu ya kaskazini Mashariki ya Israel katika bonde la mto Jordan, dawa hii ilikuwa inatumika kutibu na kufariji watu waliopatwa na maumivu na majeraha ya aina mbalimbali sugu, Dawa hii ilijipatia umaarufu mkubwa na ilikuwa ni moja ya bidhaa adimu sana.

Kwa hiyo ilikuwa kama mtu amejeruhiwa na kuumizwa, na kisha ikaonekana kana kwamba Jeraha lake haliponi na akahangaika kutumia dawa nyingi sana na zikigonga ukuta basi dawa ya mwisho ilipendekezwa kuwa Zeri kwa sababu, Zeri ilikuwa ni dawa isiyoshindwa kwa jitihada za kibinadamu.

Yeremia 46:11-12 “Panda uende Gileadi, ukatwae zeri, Ee binti, bikira wa Misri; unatumia dawa nyingi bure tu; hupati kupona kamwe. Mataifa wamesikia habari za aibu yako, nayo dunia imejaa kilio chako; maana shujaa amejikwaa juu ya shujaa mwenzake, wameanguka wote wawili pamoja.”

Leo basi tutachukua muda kuzungumzia kwa ufupi kuhusiana ana dawa hii isiyoshindwa iliyotumika kutibu majeraha sugu unhealed wounds or chronic wound iliyoitwa Zeri ya Gileadi kwa kuzingatia vipengele vya msingi vitatu vifuatavyo:-



·         Ufahamu kuhusu Zeri ya Gilead

·         Matumizi ya Zeri nyakati za Biblia

·         Dawa isiyoshindwa



Ufahamu kuhusu Zeri ya Gilead

Ni muhimu kufahamu kuwa Zeri nyakati za Biblia ulikuwa ni mmea ambao ulitumika kutengenezea viungo na mafuta yenye harufu nzuri ambayo yalitumika kutibu majeraha na vidonda sugu pamoja na maradhi mbalimbali yaliyoshindikana, Dawa hii ilipatikana katika eneo maarufu huko Jordani kaskazini mashariki mwa Israel katika bonde la mto Jordani ambako kulikuwa na misitu mizito yenye mimea ya dawa zenye thamani kubwa ukiwepo mmea huu uitwao Zeri ambao kwa Kiebrania unaitwa “Tsoriy”  na kwa kiingereza “Balm of Gilead”  Sifa mojawapo ya Zeri ilikuwa ni kutibu kwa haraka, kuleta faraja na urejesho wa uponyaji wa jeraha lililoshindikana, Kama mtu alikuwa anakuheshimu sana mojawapo ya zawadi ambayo angeweza kukuletea pamoja na viungo mbalimbali basi angeweza kukupatia na zeri katika zawadi zake, lakini moja ya biashara kubwa sana nyakati za agano la kale pamoja na mambo mengine ilikuwa ni  Zeri ambayo kimsingi inapatikana Gilead tu!

Mwanzo 37:23-25 “Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji. Nao wakakaa kitako kula chakula; wakainua macho yao, wakaona, msafara wa Waishmaeli wanakuja wakitoka Gileadi na ngamia zao, wakichukua ubani na zeri na manemane, wakisafiri kuvichukua mpaka Misri.”

Mwanzo 43:11-13 “Israeli, baba yao, akawaambia, Kama ndivyo, fanyeni hivi; twaeni tunu za nchi katika vyombo vyenu, mkamchukulie mtu huyo zawadi, zeri kidogo, na asali kidogo, ubani, na manemane, na jozi, na lozi. Mkatwae fedha maradufu mikononi mwenu, na fedha zile zilizorudishwa kinywani mwa magunia yenu zirudisheni mikononi mwenu; labda zilisahauliwa. Mtwaeni na ndugu yenu, mwondoke na kurudi kwa mtu yule.”

Matumizi ya Zeri nyakati za Biblia

Nyakati za Biblia ilikuwa kama mtu amepata majeraha na kuumia na kutibiwa kwa tiba za aina nyingine na tiba hizo zikashindikana kisha jeraha likachukua wiki zaidi ya nne mpaka sita bila kupona kwa matabibu wa kila aina basi shauri la mwisho kwa mgonjwa angeshauriwa apande kwenda Gilead kwani huko angeweza kupata tiba  ya zeri dawa isiyoshindwa ambayo ilijulikana kama zeri ya Gilead

Yeremia 8:21-22 “Kwa sababu ya maumivu ya binti ya watu wangu nimeumia mimi; nimevaa kaniki; ushangao umenishika. Je! Hapana zeri katika Gileadi? Huko hakuna tabibu? Mbona, basi, haijarejea afya ya binti ya watu wangu?

Yeremia 46:11-12 “Panda uende Gileadi, ukatwae zeri, Ee binti, bikira wa Misri; unatumia dawa nyingi bure tu; hupati kupona kamwe. Mataifa wamesikia habari za aibu yako, nayo dunia imejaa kilio chako; maana shujaa amejikwaa juu ya shujaa mwenzake, wameanguka wote wawili pamoja.”

Yeremia 51:6-8 “Kimbieni kutoka kati ya Babeli, kila mtu na ajiokoe nafsi yake; msikatiliwe mbali katika uovu wake; maana ni wakati wa kisasi cha Bwana, atamlipa malipo. Babeli umekuwa kikombe cha dhahabu mkononi mwa Bwana; kilicholevya dunia yote; mataifa wamekunywa mvinyo wake; kwa sababu hiyo mataifa wameingiwa na wazimu. Babeli umeanguka na kuangamia ghafula; mpigieni yowe; twaeni zeri kwa maumivu yake; ili labda apate kuponywa.”

Unaona nyakati za Biblia mtu alipokuwa anaugua na mauti ikaonekana inanyemelea maisha ya mgonjwa na kuiondolea familia faraja suluhu kubwa ilikuwa ni kwenda Gilead au kutafuita tabibu mwenye ujuzi wa kutibu kwa kutumia Zeri ili yamkini kuweza kurejesha afya ya muathirika, hii ilikuwa ni dawa isiyoshindwa ilikuwa ni suluhu na mwisho wa changamoto ya mtu, wagonjwa waliposikia Zeri imepatikana walirudisha matumaini wakijua ya kuwa uponyaji wao umepatikana kwani Zeri iliponya maumivu yao kwa haraka na kuwarejeshea matumaini, na kuwaondolea msongo wa mawazo  na mashaka ya wauguzaji na kilio cha waliokata tamaa kingefikia ukingoni, zeri ilirudisha mzunguko wa uhai wa damu, ingedhoofisha maambukizi, na kurejesha mfumo wa kinga kwa haraka! Na kuziponya seli zilizoanza kufa na kusababisha uponyaji ulikuwa ni mmea wa ajabu na wa faida.


Dawa isiyoshindwa

Kimsingi maandiko ya agano la kale yalikuwa yanatoa picha ya kinabii (metaphor) iliyokuwa ikimuonyesha Yesu Kristo kama dawa ya kweli isiyoshindwa, Yesu Kristo ndiye zeri ya Gilead, yeye ndiye mwenye uwezo wa kutibu, majeraha ya moyo na kuleta faraja kwa watu waliokosa tiba katika mazingira mengine ya kawaida, Zeri ya Gilead ilikuwa ikitoa unabii kivuli wa dawa halisi isiyoshindwa na ni dawa ya milele yenyewe inauwezo wa kuponya kila kilichoshindikana katika mazingira ya kawaida ya kibinadamu, Uponyaji uliotolewa na zeri ulikuwa ni uponyaji wa muda tu lakini uponyaji unaotolewa na Yesu Kristo ni uponyaji wa milele, Yesu sio tu anauwezo wa kuponya majeraha lakini pia ana uwezo wa kuponya mioyo iliyojerushiwa kwa dhambi na changamoto mbalimbali za maisha

Yesu Kristo ni tabibu wa roho zote zilizojeruhiwa, kama zeri iliponya mwili na maumivu yake Yeye Yesu Kristo ana uwezo wa kuponya mwili nafsi na roho na kufutilia mbali majeraha yote ya moyoni na uchungu wa aina mbalimbali, sio hivyo tu kila ugonjwa na changamoto zilizowakumba watu ambazo zilishindikana kwa matabibu wote zilipoletwa kwa Yesu Kristo ilikuwa ni kama mtu amepanda kwenda Gileaed  kwani angepokea uponyaji wake wa uzina huu bna ule ujao wa milele!

Luka 4:17-19 “Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.”

Marko 5:25-29 “Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya aliposikia habari za Yesu, alipita katika mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona. Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, naye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule.”

1Petro 2:23-25 “Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa. Kwa maana mlikuwa mnapotea kama kondoo; lakini sasa mmemrudia Mchungaji na Mwangalizi wa roho zenu.”

Je hapana zeri katika Gilead? Je hakuna tabibu huko? Mbona watu wanaumia mbona watu hawaponi? Ni kwa sababu watu hawataki wenyewe kuja kwa Yesu, kama watu wa Mungu watajinyenyekesha na kutubu  na kuacha njia zao mbaya uponyaji upo na unawasubiria watu wa Mungu, tunatoa wito kwa watu wote waliojeruhiwa na wenye maumivu waje kwa Yesu kwa uponyaji yeye ni dawa ya kweli yeye ni dawa isiyoshindwa!

2Nyakati 7:13-15 “Nikizifunga mbingu isiwe mvua, tena nikiamuru nzige kula nchi, au nikiwapelekea watu wangu tauni; ikiwa watu wangu, walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha, na kuomba, na kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao. Sasa macho yangu yatafumbuka, na masikio yangu yatasikiliza maombi ya watu waombao mahali hapa.”

Ni tabibu wa karibu, tabibu wa ajabu! Tenzi Na:7


Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni: