Jumapili, 23 Novemba 2025

Je mama aweza kumsahau mtoto anayenyonya?

 

Isaya 49:14-16 “Bali Sayuni alisema, YEHOVA ameniacha, Bwana amenisahau.  Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe. Tazama, nimekuchora katika vitanga vya mikono yangu; kuta zako ziko mbele zangu daima.”




Utangulizi:

Upendo wa Mungu kwa watu wake ni mkubwa sana na wa kudumu, hata kuliko upendo wa mama anayenyonyesha, Mungu anajenga hoja kwa watu wake ambao walikuwa utumwani huko Babeli na walikuwa wanadhani ya kuwa kwa vile wanapita katika hali ngumu sana na wameonewa na adui zao kwa kiwango cha kusikitisha sana waliona kama Mungu amewaacha na pia kama vile amewasahau, akijibu hoja zao Mungu anaanza kwa kujibu manung’uniko yao kwa kuuliza swali Je mama aweza kumsahau mtoto anayenyonya? Asimuhurumie mwana watumbo lake? Kisha anasema hawa wanaweza, Lakini Mimi sitakusahau wewe! Mungu anatuonyesha kuwa yeye ana upendo na huruma ya kweli isiyotikisika kama ilivyo ya mama anyonyeshaye yeye ni zaidi! Yeye akionyesha jinsi wewe ulivyo wa muhimu kwake anasema amekuchora katika vitanga vya mikono yake.

Isaya 49:16-19 “Tazama, nimekuchora katika vitanga vya mikono yangu; kuta zako ziko mbele zangu daima.Watoto wako wafanya haraka, hao wakuharibuo, nao waliokufanya ukiwa, watatoka kwako.  Inua macho yako, ukatazame pande zote; hao wote wanajikusanya na kukujia. Kama niishivyo, asema Bwana, hakika utajivika na hao wote, kama kwa uzuri, nawe utajifungia hao, kama bibi arusi. Maana katika habari za mahali pako palipokuwa ukiwa, pasipokaliwa na watu, na nchi yako iliyoharibika hakika sasa utakuwa mwembamba usiwatoshe wenyeji wako, nao waliokumeza watakuwa mbali.”

Mungu anajizungumzia mwenyewe kuwa ni Mungu mwenye kujali, anajielezea kuwa huruma zake kwa watu wake sio za kawaida, upendo wake kwa watu wake hauwezi kufananishwa na lolote, yeye ana huruma na upendo na ni mwenye kujali kuliko mama anayenyonyesha, yaani kama mama anavyomuhurumia mwana wa tumbo lake, yeye ni zaidi, hakuna unachoweza kulinganisha naye namna anavyojali na kujihusisha na maisha ya watu wake, hakuna unachoweza kulinganisha nacho duniani, wote tunafahamu jinsi wakina mama wanavyowajali watoto wachanga lakini maelezo ya Mungu yanaonyesha kuwa kujali kwao huko hakuwezi kamwe kufananishwa na kujali kwa Mungu

Neno ameniacha katika lugha ya Kiebrania linasomeka kamaâzab” kwa kiingereza fosake ambalo limetumiwa mara 129 na katika Kiyunani limetumika neno “aniēmi” kwa kiingereza leave au abandoned  ambalo maana zake “turn away from entirely” sawa na neno kutelekeza katika Kiswahili au kuacha bila msaada au kukuacha kabisa katika ufafanuzi wa kutelekeza maana yake ni unyanyasaji wa kumuacha mtu anayehitaji msaada wako bila malezi au kumpa mahitaji yanayohitajika kwa kutokumjali, Mwanadamu anaweza kutelekeza na kuacha hata kitoto kichanga kinachonyonya lakini Mungu hawezi kukuacha wewe! Tutajifunza somo hili Je mama aweza kumsahau mtoto anayenyonya kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Yehova ameniacha, Bwana amenisahau.

·         Je mama aweza kumsahau mtoto anayenyonya.

·         Mimi sitakusahau wewe.


Yehova ameniacha, Bwana amenisahau

Isaya 49:14 “Bali Sayuni alisema, YEHOVA ameniacha, Bwana amenisahau.” Kulikuwa na manung’uniko miongoni mwa watu wa Mungu kutokana na hali ngumu walizokuwa wanazipitia wakaona ni kama Mungu amewaacha, na ni kama Mungu hawajali, Sayuni inawakilisha watu wa Mungu hapo, Sayuni ni mji wa Yerusalem na hapo unasimama kama uwakilishi wa watu wa Mungu, Mungu ameahidi mara nyingi katika neno lake ya kuwa atawasaidia watu wake na kuwaokoa, lakini wao walipokuwa wakiyatazama mazingira ya nje na hisia zao za ndani waliona kama wametelekezwa kama wameachwa, watu wa Mungu walichukuliwa utumwani na mfalme katili, mnyama sana, ambaye aliitiisha Dunia kwa hofu, akiiongoza dunia kwa mkono wa chuma yaani dikteta, alikuwa na nafsi ngumu sana katili mno, aliipiga Yerusalem yaani Sayuni, akaliharibu hekalu lao na kulitia moto, mji wote uliharibiwa, alikuwa tajiri sana kutokana na uwezo wake mkubwa wa kufanya biashara, alikuwa na nguvu kiasi cha kusahau kuwa kuna Mungu na kutaka hata kuabudiwa yeye, aliwaonea watu wa Mungu na kuwafanyia unyama, Wayahudi walipelekwa utumwani kilomita 1448 sawa na miles 900 kwa miguu moja kwa moja bila kupumzika wala kupewa nafasi ya kuomba au kusali njiani, waliishi maisha ya huzuni Babeli na walilia sana walipokumbuka Sayuni nyumbani kwao.

Zaburi 137:1-4 “Kando ya mito ya Babeli ndiko tulikoketi, Tukalia tulipoikumbuka Sayuni. Katika miti iliyo katikati yake Tulivitundika vinubi vyetu. Maana huko waliotuchukua mateka Walitaka tuwaimbie; Na waliotuonea walitaka furaha; Tuimbieni baadhi ya nyimbo za Sayuni. Tuuimbeje wimbo wa Bwana Katika nchi ya ugeni?

Kutokana na changamoto lukuki walizokuwa wamekutana nazo, waliona kuwa ni Dhahiri kuwa Mungu amewaacha na sio tu kuwa amewaacha lakini pia ni kama amewasahau, Mungu alikuwa amewaahidi kuwa atawaletea mwokozi, lakini hawakuona matumaini yoyote na badala yake hali yao ilizidi kuwa mbaya, Ndivyo wote tunavyofikiri kila wakati  na kujiona wakati hali inapokuwa mbaya, tunadhani ya kuwa maombi yetu hayasikiwi, hakuna mguso, hakuna uponyaji, hakuna nuru ni giza kila mahali, nasfi inasagika sagika tunanung’unika, tunalia tunadhani na kufikiri kuwa Mungu ametuacha, hivi ndivyo walivyokuwa wakifikiri Wayahudi wakati walipokuwa katika hali ngumu utumwani.

Je mama aweza kumsahau mtoto anayenyonya.

Kabla Mungu hajajibu hoja yao, aliwataka kwanza wafikiri kuhusu mfano wa mama anayenyonyesha, Mungu aliutumia mfano huu kwa sababu ulikuwa ni mfano uliokaribu na unaoleweka vema na wanadamu wote wenye akili timamu, mfano wa mama anayenyonyesha unajenga uzito mkubwa wa kisaokolojia, kihisia, na kiroho, kwa sababu

1.       Mama anayenyonyesha ana ukaribu wa hali ya juu sana na mwanaye – Ni vigumu sana Mama kuwa mbali na mtoto anayenyonya, na ndio maana utaweza kuona sio rahisi kumuacha hata kama mama ana safari mtoto anayenyonya yuko karibu sana na moyo wa mama yake na akili ya mama yake kwa hiyo kuna uhusiano wa karibu mno, mama anayenyonyesha akimtelekeza mtoto katika hali ya kawaida, kama hatafikiriwa kuwa ni katili basi huenda akafikiriwa kuwa hana akili, uhusiano wa mama na mtoto anyonyaye ni uhusiano wa asili uliokomaa na usioweza kutenganishwa katika mazingira yoyote kwa hiyo Mungu anatuthibitishia kuwa yeye anawahurumia watoto wake kuliko mama anayenyonyesha.

 

Zaburi 103:13-14 “Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, Ndivyo Bwana anavyowahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, Na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.”

 

2.        Mama anayenyonyesha anaijua hali ya mtoto kwa ukaribu zaidi – Mama anayenyonyesha anaijua hali ya mtoto kwa ukaribu zaidi kuliko watu wengine nyumbani, anaweza kujua kama ana joto, njaa na hali nyingine yoyote anayoipitia, Mungu anaonyesha kupitia mfano wa mama anyonyeshaye ya kuwa yeye anatujua vema zaidi kuliko mtu awaye yote anatujua kukaa kwetu, kuamka kwetu na mawazo yetu na maneno yetu hata kabla hatujayasema na zaidi ya yote hata nywele zetu za kichwani yeye Mungu peke yake anajua idadi yake

 

Zaburi 139:1-4 “Ee Bwana, umenichunguza na kunijua. Wewe wajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu; Umelifahamu wazo langu tokea mbali. Umepepeta kwenda kwangu na kulala kwangu, Umeelewa na njia zangu zote. Maana hamna neno ulimini mwangu Usilolijua kabisa, Bwana.”  

 

Luka 12:6-7 “Je! Mashomoro watano hawauzwi kwa senti mbili? Wala hasahauliwi hata mmojawapo mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi, bora ninyi kuliko mashomoro wengi.”

 

3.       Mama anayenyonyesha ni mwangalizi na mlinzi wa mtoto – Kitendo cha kunyonyesha humfanya mama awe mwangalizi wa karibu na wa muda wote wa mtoto na mlinzi, kwa hiyo mfano wa mama anayejali  unatufundisha ya kuwa Mungu ni mlinzi na mwangalizi wa karibu anayetuangalia usiku na mchana na hatuwezi kupotea katika macho yake, Mama mlezi hata wakati wa usiku halali wala hasinzii kwaajili ya kuhakikisha usalama wa mtoto

 

Zaburi 121:3-8 “Asiuache mguu wako usogezwe; Asisinzie akulindaye; Naam, hatasinzia wala hatalala usingizi, Yeye aliye mlinzi wa Israeli. Bwana ndiye mlinzi wako; Bwana ni uvuli mkono wako wa kuume. Jua halitakupiga mchana, Wala mwezi wakati wa usiku. Bwana atakulinda na mabaya yote, Atakulinda nafsi yako. Bwana atakulinda utokapo na uingiapo, Tangu sasa na hata milele.”

 

Isaya 46:3-4 “Nisikilizeni, enyi wa nyumba ya Yakobo, ninyi mlio mabaki ya nyumba ya Israeli, mliochukuliwa nami tangu tumboni, mlioinuliwa tangu mimbani; na hata uzee wenu mimi ndiye, na hata wakati wenu wa mvi nitawachukueni; nimefanya, nami nitachukua; naam, nitachukua na kuokoa.”

 

4.       Mama anayenyonyesha hawezi kusahau mtoto wake – haijawahi kutokea mama anayenyonyesha akasahau kuwa ana mtoto wake anayemtegemea yeye, Mungu anaonyesha kwa mfano huu kuwa hawezi kutusahau kamwe, na kulithibitisha hilo anasema wazi kuwa amatuchora katika vitanga vya mikono yake, wakati ambapo baba yako na mama yako wanaweza kukuacha yeye bwana anakupokea na kamwe hawezi kukuacha

 

Isaya 49:15-16    Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe. Tazama, nimekuchora katika vitanga vya mikono yangu; kuta zako ziko mbele zangu daima.”

 

Zaburi 27:9-10 “Usinifiche uso wako, Usijiepushe na mtumishi wako kwa hasira. Umekuwa msaada wangu, usinitupe, Wala usiniache, Ee Mungu wa wokovu wangu. Baba yangu na mama yangu wameniacha, Bali Bwana atanikaribisha kwake.”

Kwa hiyo neno la Mungu linatuthibitishia kuwa ziko nyakati ambapo hata mama wa kawaida wa kibinadamu anaweza kumsahau mtoto anayenyonya, Lakini sivyo kwa Mungu, ninakumbuka kuna wakati ambapo, kulitokea ajali ya jahazi kwenye bahari huko Pemba kuja Pangani, wakati wa ajali hiyo maji yalianza kuingia kwenye jahazi, na matokeo yake baadhi ya kina mama kwa hofu ya kifo waliwatupa watoto wao baharini, upendo huu wa asili wa akina mama kuna wakati unagoma lakini upendo na huruma ya Mungu wetu haina wakati wa kugoma, Je mama aweza kumsahau mtoto wake anayenyonya? Huyo anaweza lakini sio Mungu wetu tunayemtegemea na kumuabudu.


Mimi sitakusahau wewe.

Isaya 49:14-16 “Bali Sayuni alisema, YEHOVA ameniacha, Bwana amenisahau.  Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe. Tazama, nimekuchora katika vitanga vya mikono yangu; kuta zako ziko mbele zangu daima.”

Wakati jamii ilipokuwa inapitia changamoto za aina mbalimbali wao walidhani na kufikiri ya kuwa Mungu amewaacha na kuwasahau, Hata hivyo tunaona Mungu nanatumia mfano huo wenye mguso wa kupita kawaida kujijengea hoja madhubuti ili wanadamu waweze kufahamu jinsi Mungu wetu anavyojali, mama anapokuwa amemsahau mtoto kwa kawaida kibinadamu linakuwa ni jambo lenye kushangaza sana  wao wana upendo wa asili unaoumiza, Mungu anaonyesha kuwa yeye anaumia zaidi kuliko mwandamu wa kawaida na anaonyesha ya kuwa upendo wa mama unaweza kuharibika lakini sio wake, kwa hiyo hakuna makosa yanatokea katika maisha yako ukadhani Mungu amekosea au haoni, kila mwanadamu anapopita katika changamoto mbalimbli za maisha hufikiri kuwa Mungu amemuacha, Yesu pale Msalabani alilia Mungu wangu Mungu wangu mbona umeniacha lakini Mungu alikuwa na mpango wa kumfufua mwanae na kumpaisha juu Mbinguni na kuweka adui zake wote chini ya miguu yake, yeye anathibitisha ya kuwa hata kama upendo wa mama unaweza kufikia ukingoni wake hauwezi, Mungu anakujua, Mungu anakufikiria, Mungu anakujali, Mungu anakulinda, Mungu anakulisha, Mungu anakutunza,  Mungu anatupenda kupita upendo wa kibinadamu na upendo wake ni wa milele kwa hiyo haupaswi kuogopa unayoyapitia

Yeremia 31:3 “Bwana alinitokea zamani, akisema, Naam nimekupenda kwa upendo wa milele, ndiyo maana nimekuvuta kwa fadhili zangu.”

Ziko nyakati katika maisha yetu unaweza kufikri kuwa umeachwa na Mungu, leo nataka tujikumbushe kuwa mawazo hayo ni batili, na hasi na sivyo ilivyo kwa Mungu wetu kutokana na maneno yake ya uzima, Kila mtu anaweza kukuacha lakini sio Mungu wetu ahadi zake ni ndio na kweli na kamwe hawezi kukusahau wewe, Yeye ni mwaminifu kama alivyoahidi atatenda.

“Je mama aweza kumsahau mtoto anayenyonya? Huyo aweza, lakini Mungu hatakusahau wewe”

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni: