Jumapili, 30 Novemba 2025

Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale!


Maombolezo 5:19-21. “Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi. Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”


Utangulizi:

Je? umewahi kufikiri kuwa siku kadhaa au miaka kadhaa huko nyuma ilikuwa bora katika maisha yako kuliko ilivyo sasa? Siku ambazo furaha yako ilikuwa timilifu, siku ambazo afya yako ilikuwa njema, siku ambazo uhusiano wako na Mungu ulikuwa mzuri sana, siku ambazo ulikuwa mwombaji sana, siku ambazo ulikuwa hukosi mikesha, huachi kufunga, siku ambazo hata upitie taabu gani hukuona shida, siku ambazo ni kama zilikuwa siku za ushindi wako, siku ambazo familia ziliishi kijamaa, tuliwatembelea Babu na Bibi zetu vijijini, tulikutana na ndugu wengi, ulikuwa na marafiki wengi, watu walikaa pamoja kwa umoja na upendo ulikuwa ni kama umefikia kilele cha hali ya juu cha furaha ya maisha, unazikumbuka siku zile na unatamani kama zingerudia tena upya! Hali kama hii ndiyo iliyomkuta nabii Yeremia alikumbuka siku za utukufu mkubwa wa Mungu katika Uyahudi, wakati Hekalu la Yerusalem lililojengwa na Suleimani bado halijatiwa moto na kubomolewa zilikuwa siku njema, lakini Mungu alikuwa ameziondoa na sasa anaona uharibifu na mambo hayako kama siku zile, anaona ni kama Mungu amewaacha na kuwasahau kwa muda mrefu na kwa siku nyingi sana.

Maombolezo 5:19-21. “Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi. Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Hali hii ni hali ya kuhuzunisha sana ni hali yenye mchanganyiko wa majonzi na kukata tamaa ni wakati ambapo maisha ya mwanadamu yanakuwa yamezidiwa na kumbukumbu ya mambo mabaya yaliyotokea na yanayoendelea katika wakati ulioko, huku ukikumbuka siku zile za utukufu ambazo sasa unatamani ungezirudisha siku nyuma, uweze kuzifurahia na kupata Amani, Kisaikolojia hili tukio linaitwa “Nostalgia”.  Nostalgia is a state of being sick emotional for the past period or homesick, university days etc. Hali ya kuumwa kihisia kwaajili ya kukumbuka mambo mazuri ya zamani au kukumbuka nyumbani au siku zako za chuoni na kadhalika, Yeremia sasa anaumwa ugonjwa huu na anamuomba Mungu kwamba asikawie anamuomba Mungu awageuze nao watageuka na azifanye mpya siku zao kama siku za zamani!, ilikuwa ni sauti ya kuomboleza iliyojaa uchungu hasa baada ya Hekalu la Yerusalem kutiwa moto na kubomolewa na mfalme wa Babeli mwaka 586 KK Yeye alikuwa ameshuhudia siku nzuri za utukufu wa Hekalu hilo na siku mbaya za uharibifu mkubwa Hekalu likiwa limebomolewa, watu wamechukuliwa kwenda uhamishoni, taifa limepoteza fahari yake, na Mungu anaonekana kuwa kimya kwa hiyo moyo wake umejaa ombi lenye huzuni, toba na matumaini. Wewe je unapitia hali ya namna gani hapo ulipo? Familia yako je? Umri wako je? Ndoa yako Je? Hali yako ya kiuchumi, hali yako ya kiroho? Uhusiano wako je? Kanisa lako je kuna uamsho? Watu wanampenda Mungu kama zamani? Uzuri wako? kazini kwako je zipi siku bora katika maisha yako? Leo tutachukua muda kujifunza kwa undani somo hili muhimu lenye kichwa Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale! Na tutajifunza somo hili litakalo kurejeshea matumaini kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vufuatavyo;-

·         Kilio cha kukumbuka siku za kale

·         Sababu za kukumbuka siku za kale  

·         Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale!

Kilio cha kukumbuka siku za kale

Maombolezo 5:19-21. “Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi. Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Kimsingi kifungu hiki yalikuwa ni maombolezo au kilio ya Nabii Yeremia ambaye alikuwa akiomboleza baada ya mashambulizi mazito na hali mbaya ambayo watu wake na yeye mwenyewe walikuwa wameishuhudia, uharibifu mkubwa uliofanywa na majeshi ya Wakaldayo chini ya utawala wa Nebukadreza mfalme wa Babeli, Yeremia alikuwa anaona uchungu na sasa anaomboleza juu ya mateso ya taifa huku akiona kana kwamba Mungu amewasahau na kuwaacha kwa hiyo Yeremia alikuwa akimlilia Mungu na kumtaka awarejeze katika hali yao waliyokuwa nayo mwanzo.

Kisaikolojia hisia hizi zinaitwa “Nostalgic feelings” yaani hii ni tabia ya mwanadamu kukumbuka siku nzuri za utukufu za zamani zilizokuwa za furaha kwaajili ya kufidia hali ngumu anayokutana nayo katika wakati ulioko, akili haitaki kuona mambo mabaya inataka mambo mazuri, akili haitaki nyakati ngumu inataka amani raha na utulivu tu kwa hiyo kwa mfano umri unapokuwa unaenda mtu anaanza kukumbuka enzi za ujana wake, anakumbuka siku za zamani shuleni, chuoni na kadhalika, katika mahusiano anaanza kukumbuka siku nzuri ambazo alikuwa na soko, anapendwa na kila mtu, unapokuwa mpweke unakumbuka zamani familia zilipokuwa zinakaa pamoja na kula na pamoja na sikukuu tulizokuwa tunaenda kwa Babu na Bibi na kujumuika pamoja, unapokuwa na afya mbaya unakumbuka siku zako ulizokuwa na uzima ukiwa na nguvu, ulipokuwa na uwezo wa kula nyama na mahindi ya kuchoma na sasa meno hayana uwezo huo tena, unakumbuka siku za kale mlivyokuwa mkihubiri injili, unakumbuka wahubiri wakubwa wa zamani, miujiza mikubwa iliyokuwa ikifanyika, unakumbuka nyakati ambazo ulikuwa maarufu, na wakati wa mafanikio, unakumbuka nyimbo za zamani, wachezaji wazuri wa timu yako uliyoipenda ilipokuwa ikitwaa ubingwa, unakumbuka vipindi maalumu ambavyo sasa ni kama vimepita na haviwezi kurudi tena, unakumbuka kipindi chako kiitwacho “the golden age” hii ni hali ya kawaida wakati mwanadamu anapopitia magumu, Israel walikumbuka chakula walichokuwa wanakula Misri japo walikuwa utumwani na waliteswa

Hesabu 11:4-6 “Kisha mkutano wa wafuasi waliokuwa kati yao, wakashikwa na tamaa; wana wa Israeli nao wakalia tena, wakasema, N'nani atakayetupa nyama tule? Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu.”

Hali kama hii inamkuta nabii Yeremia anakumbuka jinsi Wayahudi walivyokuwa na amani katika taifa lao, walivyokuwa wakipanda kwenda Hekaluni, anakumbuka Mungu alivyokuwa mtetezi wao na jinsi Mungu aliyokuwa akisema nao na kuwapa wafalme na mahitaji yao, sasa kila kitu kimebakia historia mambo yameharibika, watu wamechukuliwa uhamishoni Babeli, Taifa limepoteza matumaini hakuna uhai tena, watu wako utumwani Mungu yuko kimya amegeuza uso wake Yeremia anamlilia Mungu anamuomba kwa unyenyekevu, anamuuliza mbona umetuacha, umetuacha muda mwingi, yaani unakawia, utugeuze kwako nasi tutageuka, lakini zaidi ya yote zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.

Yeremia 5:20-21 “Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Sababu za kukumbuka siku za kale.

Maombolezo 5:19-21. “Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi. Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Kwa nini Yeremia anakumbuka siku za kale? Kwa nini wewe na mimi tunazikumbuka siku zile? Siku za kale ulikuwa ni wakati wa utukufu, ulikuwa ni wakati watu wamejitoa kwa uaminifu, ulikuwa wakati wa uhusiano mzuri na Mungu, ulikuwa ni wakati watu waliabudu na kutembea na uwepo wa Mungu na miujiza mingi ilifanyika, ulikuwa ni wakati wa uhusiano mzuri, urafiki mwema wakati wa kuoneana shauku, wakati ambapo kila unaloliomba linajibiwa ulikuwa ni wakati wa Baraka, akitokea adui watu walijaa Roho Mtakatifu na maadui walikimbizwa, taifa lilikuwa na heshima, watu walikuja kutafuta Hekima na kumuabudu Mungu wa Yakobo, watu walivyotoa sadaka kwa unyoofu wa moyo, katika mahusiano watu walipendana, sasa nyakati hizo haziko tena, majumba yamekuwa magofu, upako haupo, miujiza imepotea, watu hawana mikesha tena, hekalu limechomwa moto Yeremia analia anaomboleza anamwambia Mungu zifanye upya siku zetu kama siku za kale, msikilizaji wangu na msomaji wangu wewe u hali gani sasa? Uko wapi, familia yako iko wapi, ndoa yako iko wapi, malezi yako yako wapi, furaha yako iko wapi, utukufu wako uko wapi, u hali gani, kanisa lako li hali gani na wewe mwenyewe hali yako ya kiroho ikoje?  Je unaugua kama Yeremia? Asante Mungu kwaajili ya nabii Yeremia alimfahamu Mungu alijua ya kuwa Mungu anauwezo wa kuzifanya upya ziku zetu na kuzirejeza zikawa kama siku za kale, leo ni siku yako ambayo Bwana atazifanya upya siku zako Mungu wetu anauwezo wa kurejesha, neno la Mungu linatueleza hivyo ana uwezo wa kututia nguvu

Zaburi 103:1-5 “Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana. Naam, vyote vilivyo ndani yangu Vilihimidi jina lake takatifu. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana, Wala usizisahau fadhili zake zote. Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, Aukomboa uhai wako na kaburi, Akutia taji ya fadhili na rehema, Aushibisha mema uzee wako, Ujana wako ukarejezwa kama tai;”

Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale!

Mungu anawezaje kuzifanya upya siku zetu kama siku za kale? Yeremia alikuwa amegundua siri mojawapo muhimu katika dua yake ambayo inatufunulia maswala muhimu sana yanayoweza kutuasaidia na sisi katika Maisha yetu ili tusiweze kumezwa na huzuni kutokana na hali unayoipitia!

Maombolezo 5:21 “Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Katika lugha ya Kiebrania kifungu hiki muhimu kinasomeka hivi “Hashivenoo ADONAI elecha venashuvah, chadash yamenu ke’kedem” Kwa kiingereza maneno hayo yanasomeka hivi “turn us back Adonai and we will come back, renew our days, as they were in the past”

Hashivenoo (shuv)  - Uturudishe nyuma, utugeuze, uturejeshe, tugeuze, tubadilishe, ni neno linalotumika katika lugha ya Kiebrania mara nyingi likimaanisha kutubu, kubadilika moyo, kutoka dhambini, kumrudia Mungu, Yeremia hasemi tunageuka anasema utugeuze, akimaanisha Mungu ndiye chanzo cha toba ya kweli, hii inamaanisha toba ya kweli sio matokeo ya hisia zetu  na matakwa yetu wanadamu tu bali ni neema ya Mungu inayoufanya moyo wa mwanadamu ulainike na kumgeukia Mungu na kuamua kufuata njia za Mungu, kwa hiyo Yeremia anajua ya kuwa siku njema kama za zamani haziwezi kurejea hivi hivi bila ya msaada wa Mungu, ni lazima Mungu atuamshe tena na kuwasha upya moto ndani yetu utakaotusaidia kurudi kwake na sio maamuzi ya kibinadamu.

Warumi 9:15-16 “Maana amwambia Musa, Nitamrehemu yeye nimrehemuye, nitamhurumia yeye nimhurumiaye. Basi, kama ni hivyo, si katika uwezo wa yule atakaye, wala wa yule apigaye mbio; bali wa yule arehemuye, yaani, Mungu.”

Venashuvah – Tutageuka, tutaitikia, tutakubali, yaani tutakubali mabadiliko tutatii, Yeremia anatambua kuwa ili siku njema ziweze kurejeshwa ni lazima Mungu mwenyewe awashe moto wa mawasiliano na kugeuza mioyo yetu na kuturehemu na sisi nasi tuitikie kwa kutii kwa hiyo hapa tunajifunza kwamba uamsho ni ushirikiano kati ya Mungu na Mwanadamu, Mungu anapoanza kwa rehema zake sisi ni wajibu wetu kuitikia kwa toba na utii kwa uaminifu na moto ule utawaka.

Chadash (Chadesh) – Kufanywa upya kurejesha, kuhuhisha kujenga hari mpya, neno Chadash linatokana na neno Chodesh ambalo maana yake ni mwezi mpya mwenzi mchanga, mwezi unaochomoza kwa upya kutoka gizani, Yeremia anamsihi Mungu aanzishe jambo jipya katika mioyo yetu alete uhai katika mambo yote yalitopotea atupe mwanzo mpya arejeshe hali ya kiroho, kiuchumi na kimaisha aturejeshee furaha, atupe nuru hii pia ni kazi ya Mungu ndani yetu kutuhuisha

Zaburi 51:10-12 “Ee Mungu, uniumbie moyo safi, Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu Usinitenge na uso wako, Wala roho yako Mtakatifu usiniondolee. Unirudishie furaha ya wokovu wako; Unitegemeze kwa roho ya wepesi.”

Maombi ya Yeremia yalikuwa yamejaa ujuzi na hekima ya kuwa ni Mungu mwenyewe peke yake na mwitikio wetu kwa rehema zake unaoweza kusababisha mabadiliko na kurejeswa kwa siku zetu kama siku za kale, Kama watu wa Mungu wanataka kurejeshewa siku za furaha na amani basi ni lazima tumsihi Mungu kama Yeremia alivyoomba kwamba Mungu aturejeshe na sisi tukubali kurejea tukatae kupoa kiroho, tukatae ubaridi katika uhusiano wetu na Mungu ambaye ndiye chanzo cha Baraka, tumsihi Mungu afufue mambo yote yaliyokufa ndani yetu, aiponye mioyo iliyovunjika atupe uwezo wa kusamehe, atupe nguvu ya kuomba, atupe kuliheshimu neno lake, atupe ile hali ya kumuhofu, atupe kuihubiri injili ya kweli na Mungu ataturudishia siku zetu zilizopotea hii haimaanishi kuwa ataturudisha tulikotoka au kwenye miaka ile ya zamani, lakini maana yake zitakuja nyakati za kuburudishwa ambazo roho zetu zitafurahi tena na tutasahu maumivu yetu, Mungu yuko tayari kuzifanya upya siku zetu yuko tayari kuziburudisha siku zetu na kuyafutilia mbali machozi yetu yote badala ya kukumbuka mambo ya zamani yeye ameahidi kufanya mambo mapya katika maisha yetu.

Matendo 3:19-21 “Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu zamani; ambaye ilimpasa kupokewa mbinguni hata zije zamani za kufanywa upya vitu vyote, zilizonenwa na Mungu kwa kinywa cha manabii wake watakatifu tokea mwanzo wa ulimwengu.”

Isaya 43:18-19    “Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani. Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 



Hakuna maoni: