Jumapili, 16 Novemba 2025

Msigombane njiani!


Mwanzo 45:21-24 “Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli. Yusufu akawapa magari kama Farao alivyoamuru, akawapa na chakula cha njiani. Akawapa kila mtu nguo za kubadili; lakini Benyamini, alimpa fedha mia tatu na mavazi matano ya kubadili. Na babaye akampelekea kama hivi, punda kumi waliochukua mema ya Misri, na punda wake kumi waliochukua nafaka, na mikate, na chakula kwa babaye njiani. Akaagana na ndugu zake, wakaenda zao; naye akawaambia, Msigombane njiani.




Utangulizi:

Mojawapo ya agizo la msingi na la muhimu sana lililotolewa na Yusufu kwa ndugu zake ni pamoja na agizo hili, la “Msigombane njiani”, Agizo hili lilikuwa ni la muhimu na lenye kujenga umoja na amani ya kitaifa na kifamilia, hasa baada ya mafarakano, toba na msamaha na mapatano baada ya wana wa Israel kumuuza ndugu yao Yusufu utumwani ambako kwa neema ya Mungu alipata madaraka makubwa na akajitambulisha kwao, Yusufu anatoa maagizo haya ili kuilinda jamii yake wasiwe na mafarakano katika wakati wa mpito, kuelekea kwenye kuishi pamoja kwa furaha na amani kupitia mwaliko wake kwa familia nzima waje kuishi katika inchi ya Misri, wana wa Israel wangeliweza kuanza kushutumiana na kulaumiana kwaajili ya mambo yaliyopita wakati Yusufu amekwisha kutoa msamaha, maneno ya Yusufu kwao yanasimama kama onyo lenye kuweka msingi wa kuepusha migogoro njiani.

Neno la Mungu linaonya vikali kwamba katika vitu ambavyo ni chukizo kubwa kwa Mungu ni pamoja na kupanda mbegu ya fitina kati ya ndugu, yaani kugombanisha watu, Yusufu hakutaka kutoa ruhusa kwa ndugu zake ambao kimsingi aliwapima na kujua kuwa wamebadilika sana mioyoni mwao kwa hiyo asingelitoa nafasi ya wao kufarakana na kuumizana kwa sababu ya fitina na ugomvi kama wa mwanzo uliowafarakanisha wao na yeye kwa ndugu zake.

Mithali 6:16-19 “Kuna vitu sita anavyovichukia Bwana; Naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, Na mikono imwagayo damu isiyo na hatia;Moyo uwazao mawazo mabaya; Miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; Shahidi wa uongo asemaye uongo; Naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.”

Yusufu alikuwa amefahamu mpango wa Mungu, kwamba watu wanaweza kufarakana na kufitiniana lakini Mungu akawa amekusudia jambo jema katika fitina hizo na kutimiza mpango wake, kwa sababu hiyo sasa ulikuwa ni wakati wa kuhakikisha kuwa familia inakuwa na umoja, na inalinda mpango wa Mungu wa kuwa na amani, na kwa sababu hiyo agizo lake sio adhabu, bali ni somo la kiroho kwa jamii yake, taifa lake na ndugu zake kwamba wasigombane tena kwa sababu Mungu amekwisha kutimiza mpango wake kwao! Tutajifunza somo hili Msigombane njiani kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya kugombana njiani

·         Msigombane njiani

·         Athari za kugombana njiani


Maana ya kugombana njiani

Mwanzo 45:21-24 “Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli. Yusufu akawapa magari kama Farao alivyoamuru, akawapa na chakula cha njiani. Akawapa kila mtu nguo za kubadili; lakini Benyamini, alimpa fedha mia tatu na mavazi matano ya kubadili. Na babaye akampelekea kama hivi, punda kumi waliochukua mema ya Misri, na punda wake kumi waliochukua nafaka, na mikate, na chakula kwa babaye njiani. Akaagana na ndugu zake, wakaenda zao; naye akawaambia, Msigombane njiani.

Moja ya jambo ambalo linavuruga sana umoja wa kifamilia, kitaifa na kijamii ni pamoja na ugomvi, kugombana kuna athari kubwa sana yaani athari hasi katika maisha ya mtu mmoja mmoja, wanandoa, jamii na taifa, watu wanaogombana wanaharibiana na kuleteana athari kubwa sana kimaisha, kihisia na mahusiano na kuacha majeraha ya uchungu, hasira, kisasi, chuki na mgawanyiko, kwa ujumla ninaweza kusema hakuna sumu mbaya katika mahusiano kama ugomvi, watu wanapoanza kugombana, kuchukiana na kuchochea hasira na migawanyiko, mwelekeo wake unakuwa ni kutengeneza matatizo makubwa zaidi yanayoharibu maisha hususani ya wale wanaohusika katika ugomvi huo, akilijua hili Yusufu katika hekima yake na akili yake aliwaonya ndugu zake kuwa wasigombane njiani!, kama kuna jambo huwa linasikitisha sana katika jamii ni kuishi katika jamii inayogombana!

Kugombana njiani hasa maana yake ni nini? Katika lugha ya asili ya Kiebrania neno kugombana linasomeka kama neno “ragaz” au “tirgәzῡ” kwa Kiyunani “orgizethe”, au “orgē” maana zake kwa kiingereza ni  fall not out”, “quarrel”, “argue”, “become troubled”, “disagree in words”, kwa Kiswahili tunaweza kusema “Msikosoane”, au “msikoseane”, “Msigombane” au “msibishane”, Msisumbuane”, au msileteane taabu, msisumbuane kwa meneno, au msikose kufikia muafaka,  na neno njia kwa kiyunani ni “hodō” ambalo maana yake ni safari ya maisha, kwa hiyo sio tu njia ya kawaida lakini katika maisha, kwa msingi huo neno la Mungu linamtaka kila mmoja katika jamii, wanandoa, kanisa, ndugu, jamaa, marafiki na taifa lolote kwamba wasigombane njiani, yaani wasiwe na mafarakano katika safari ya maisha, watu waache kuwa na uchungu, waache hasira, wasiwe watu wasiofikia muafaka, kimsingi mafarakano yoyote humzimisha Roho Mtakatifu na kuondoa maarifa, hekima na busara katika mioyo ya watu.

Yusufu alikuwa na ufahamu kuwa mambo mabaya yanaweza kutokea pale watu, ndugu, wanandoa au jamii na taifa kwa ujumla wakiruhusu magomvi, wanafungua ufunguo wa shina la uchungu, kupoteza umoja, kuruhusu mafarakano, migawanyiko na hata mauaji lakini sio hivyo tu watu wanaogombana wanafanya upumbavu na kumuhuzunisha Roho Mtakatifu, na kuthibitisha kuwa wao bado hawana ukomavu wa kiroho, kiakili na kifikra na wanaharibu uhusiano wao na Mungu na kutengeneza kizuizi kwa maombi na baraka za Mungu zilizokusudiwa katika maisha yao. Ugomvi huwaweka watu katika vifungo vya kiroho na kuweka ukwazo wa wao kufunguliwa na kuwahuru

Mithali 20:3 “Mtu kujitenga na ugomvi ni heshima kwake; Bali kila mpumbavu ataka kugombana”.

Mathayo 5:22-26.“Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanum ya moto. Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.”

Msigombane njiani.

Mwanzo 45:24 “Akaagana na ndugu zake, wakaenda zao; naye akawaambia, Msigombane njiani.”  Kimsingi Yusufu alitoa agizo Msigombane njiani akiwa na uzoefu wa kutosha na mpana sana wa kutaka kuilinda jamii yake, kama kila Taifa, Kanisa, wanandoa  na jamii wanataka kujilinda ana aibu na kujilinda na kumpa shetani nafasi hawana budi kujilinda na mafarakakano, na ugomvi usio na tija, mtu mmoja Mwalimu wa zamani sana wa chuo cha Biblia Dodoma (AGBC) kwa sasa (CBC) Mwalimu Ndosi mwaka 2000 alisema hivi nanukuu “Watu wanapopendana huwa hatuulizi kwanini wamependana na wala hatuwaingilii, lakini watu wanapogombana tunaingilia na kuuliza ni kwanini wanagombana” mwisho wa kunukuu, Mwalimu Ndosi alikuwa anamaanisha kuwa watu wanapopendana huwa hakuna kelele kwa hiyo hakuna mtu anayesikia na kujua kuwa nini kinaendelea lakini watu wanapogombana kunakuwa na makelele na hivyo watu wengine huja kuingilia na kuuliza kwa nini mnagombana, ugomvi huleta aibu, na kumfanya kila mtu hata majirani kujiuliza kwanini hawa wanagombana, mnapopendana hakuna vikao, mnapogombana vikao vinaanza, mnapopendana mnafukuza maadui mnapogombana maadui wenu huanza kupata mwanya wa kuwaingilia na kuwavuruga zaidi hii ni kuanzia ngazi ya familia hadi ngazi ya kitaifa, hususani katika nyakati za leo ambako kuna uwazi mkubwa wa vyombo vya habari na mitandao ya kijamii hamuwezi kujificha, Kaini na Habili walipoanza kuwa na mzozo kwa sababu ya wivu wa Kaini kwa nduguye, Mungu aliingilia kati na kuanza kuuliza, lakini walipoishi kwa umoja, amani na upendo hata Mungu hakuuliza maswali, kwani hali ilikuwa shwari.

Mwanzo 4:3-11 “Ikawa hatimaye Kaini akaleta mazao ya ardhi, sadaka kwa BWANA. Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama. BWANA akamtakabali Habili na sadaka yake; bali Kaini hakumtakabali, wala sadaka yake. Kaini akaghadhibika sana, uso wake ukakunjamana. BWANA akamwambia Kaini, Kwa nini una ghadhabu? Na kwa nini uso wako umekunjamana? Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde. Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende uwandani]Ikawa walipokuwapo uwandani, Kaini akamwinukia Habili nduguye,akamwua. BWANA akamwambia Kaini, Yuko wapi Habili ndugu yako? Akasema, Sijui, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu? Akasema, Umefanya nini? Sauti ya damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika ardhi. Basi sasa, umelaaniwa wewe katika ardhi, iliyofumbua kinywa chake ipokee damu ya ndugu yako kwa mkono wako;”

Kaini hakutenda haki, hakufanya vizuri, lakini Habili alitenda haki na alifanya vizuri, waliishi kwa utulivu lakini walipoanza kugombana Mungu alisikia ugomvi wao, Mungu aliingilia kati na Mungu alielekeza njia ya kufanya, Mungu amekusudia kumpa kibali kila mmoja, na amekusudi kumbariki kila mmoja jambo la msingi ni kila mtu kusimama katika wajibu wake na kutenda haki,  UKITENDA VEMA HUTAPATA KIBALI? agizo la kutokugombana njiani lilikuwa linamtaka kila mmoja kutokuwa sababu ya ugomvi na sababu ya malumbano katika jamii, kama viko vyama vya siasa vyama hivyo vina wajibu wa kuwatumikia wananchi na kuwatendea haki na kuwaletea maendeleo, tuko katika safari ya kuelekea kwenye kilele cha maendeleo na hakuna sababu ya kugombana njiani, kama mtu anahisi kupoteza kibali, njia sahihi ni kufanya vizuri na kutokugombana, kila mmoja anapaswa kutimiza wajibu kwa maslahi mapana ya jamii na sio kwa manufaa ya watu wachache na ubinafsi, Yusufu aliwaasa ndugu zake kutokugombana sio kwa maslahi yao tu bali na masalahi ya familia nzima, alitaka kumlinda na Yakobo Baba yake, alifahamu kuwa ugomvi wa ndugu hawa njiani pia ungemuathiri Baba yao, ambaye alikuwa amedanganywa kuwa Yusufu amekufa na wakachukua kanzu yake na kuichana chana na kuitia damu na kumwambia Baba yao kuwa Yusufu amekufa!, Ugomvi wao ungemuhuzunisha mzee kule nyumbani na hasa kama sasa angejua ukweli kuwa sasa Yusufu yuko hai!.

Mwanzo 37:31-34 “Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi.”

Yusufu alikuwa anajua kuwa ugomvi wa kifamilia, kitaifa na kijamii unawahuzunisha sana wazee, alifahamu kuwa mgogoro wao unaweza kuwafikia wazazi na kuwafanya walie na kuhuzunika, wazee wetu ambao wametulea kwa shida na taabu mpaka tumekua wametuoza, wametusomesha na kuhakikisha ya kuwa tuna maisha haya tuliyo nayo wamestaafu na kutulia nyumbani, wamelitumikia taifa hili na kulipigania, wamepambana tangu kuipatia uhuru nchi yetu hatuwezi kuwalipa upumbavu, hatuwezi kuwapelekea maiti wala kanzu zilizojaa damu, mgogoro wa Kaini na Habili ulimuhuzunisha Adamu, migogoro yetu na ugomvi unahuzunisha watu wasio na hatia na kuwafanya wahuzunike na kujisikia vibaya, Mzozo na ugomvi ni aibu kubwa sana kwa familia, jamii na taifa msigombane njiani.

Wazee wetu wanahitaji habari njema, wanahitaji mavazi, chakula utulivu, Amani na kula mema ya nchi waliyoyataabikia na hawahitaji tena kusikia magomvi, wanahitaji kucheza na wajuu zao na sio kupelekewa kanzu zilizojaa damu, wala kupelekewa kazi ya kutatua migogoro ya ndoa zenu, wala kusikia habari mbaya wanahitaji habari njema iliyokamilika, mioyo yao ichangamke, Yakobo alipopokea habari njema roho yake ilifufuka ndani yake

Mwanzo 45:21-24 “Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli. Yusufu akawapa magari kama Farao alivyoamuru, akawapa na chakula cha njiani. Akawapa kila mtu nguo za kubadili; lakini Benyamini, alimpa fedha mia tatu na mavazi matano ya kubadili. Na babaye akampelekea kama hivi, punda kumi waliochukua mema ya Misri, na punda wake kumi waliochukua nafaka, na mikate, na chakula kwa babaye njiani. Akaagana na ndugu zake, wakaenda zao; naye akawaambia, Msigombane njiani.

Mwanzo 45:26-28 “Wakampasha habari, wakisema, Yusufu angali hai; naye ndiye mtawala katika nchi yote ya Misri. Moyo wake ukazimia, kwa sababu hakuwasadiki. Wakamwambia maneno yote ya Yusufu, aliyowaambia; na alipoona magari aliyoyapeleka Yusufu, ili kumchukua, roho ya Yakobo baba yao ikafufuka.Israeli akasema, Yatosha! Yusufu mwanangu angali hai; nitakwenda, nionane naye kabla sijafa.”

Israel/Yakobo alipopewa habari njema roho yake ikafufuka alisema neno moja tu YATOSHA hakutaka kusikia habari nyingine alijawa na furaha, aliona na magari aliyoletewa na mwanae; Je ugomvi wetu una manufaa gani kwa jamii, unamanufaa gani kwa watoto wetu, una manufaa gani kwa wanawake una manufaa gani hata kwetu wenyewe, ROHO YAKE IKAFUFUKA katika Kiebrania linatumika neno “Châyâh” kwa kiingereza “recovered” au “repaired” Yakobo alipokea uponyaji wa roho yake kwa sababu alipokea habari njema na akasema “Yatosha” ameridhishwa na habari njema na taarifa njema hiki ndio familia inataka kusikia, hiki ndicho jamii inataka kusikia, hiki ndio taifa na watu wa Mungu yaani kanisa tunataka kusikia, habari za ugomvi na mafarakano katika jamii huongeza migandamizo ya mawazo, hurudisha watu nyuma, huleta majeraha na vidonda vya moyo na kuufisha moyo tuache kugombana!

Yusufu aliweka katazo lenye kuleta Baraka na kujenga umoja wa kijamii,kifamilia na kitaifa ambao kimsingi unaruhusu uwepo wa Mungu na kusababisha baraka kubwa sana, safari ya kutoka Misri mpaka Kanaani kwa kutembea pamoja na punda na ngamia ingeweza kuchukua kati ya siku 10 -14 muda huu kama usingelikuwa na onyo kama hili la msigombane njiani wangefika wakiwa wamevurugana vya kutosha lakini pia ilikuwa aibu kwa wageni waliombatana nao kwa magari maalumu yaliyokuwa yanaenda kumpelekea Yakobo zawadi na kumchukua kuja Misri

Zaburi 133:1-3 “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, Ndugu wakae pamoja, kwa umoja. Ni kama mafuta mazuri kichwani, Yashukayo ndevuni, ndevu za Haruni, Yashukayo mpaka upindo wa mavazi yake. Kama umande wa Hermoni ushukao milimani pa Sayuni. Maana ndiko Bwana alikoamuru baraka, Naam, uzima hata milele.”          

Athari za kugombana njiani.

Neno la Mungu linatupa uwanja mpana wa kuelewa kuwa ugomvi una athari hasi, na zenye kuharibu, mahusiano ya kijamii na maisha ya kiroho, watu wanaoanzisha magomvi wanafananishwa na watu au mtu anayetoboa mtumbwi ukiwa kwenye maji, na mafuriko yanaweza kuuzamisha na safari ikakwama.

Mithali 17:12-14 “Afadhali mtu akutwe na dubu aliyenyang'anywa watoto wake, Kuliko na mpumbavu katika upumbavu wake. Yeye arudishaye mabaya badala ya mema, Mabaya hayataondoka nyumbani mwake. Mwanzo wa ugomvi ni kama kutoboa penye maji; Basi acheni ugomvi kabla haujafurika.”

Kwa hiyo tunajifunza kwamba kuna madhara au athari kubwa sana ya kimwili na kiroho na hata kisaikolojia inayosababishwa na ugomvi, na huenda Yusufu mwana wa Yakobo alikuwa na ufahamu huo na alitaka kuilinda na kuitunza familia yake kiroho na kimwili ili wawe na uhusiano mzuri na Mungu na pia wawe na uhusiano mzuri wao kwa wao hapa ziko athari kadhaa zitokanazo na kugombana njiani:-

Ø  Kutokugombana njiani kunatujengea uhusiano mwema na Mungu, wakati migogoro na ugomvi unaweza kuharibu mawasiliano yetu na Mungu na kuzuia maombi na ibada, kutokugombana kuna athari chanya kwani kunatujengea uhusiano mwema na Mungu.  Wanandoa wanaogombana sio tu kuwa wanaiweka ndoa yao rehani, lakini pia wajue ibada zao, maombi yao na dua zao haziwezi kukubalika kwa Mungu kama kuna mtu hujamalizana naye, hujapatana naye na kuweka mambo vizuri, ibada yako na sadaka yako hazikubaliwi

 

1Petro 3:7-9 “Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe. Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitikivu, wanyenyekevu; watu wasiolipa baya kwa baya, au laumu kwa laumu; bali wenye kubariki; kwa sababu hayo ndiyo mliyoitiwa ili mrithi baraka.”

 

Mathayo 523-24 “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.”

 

Ø  Ugomvi ni dalili ya kutokukomaa kiroho na kifikra – Paulo mtume anawaona watu wenye mafarakano kama watu waliokosa ukomavu, watu walio wachanga na wenye kuonyesha udunia kama ni Wakristo basi wanaitwa Wakristo wa mwilini. Lakini jamii yoyote ile isiyokuwa na ukomavu na subira hishia katika ugomvi

 

1Wakorintho 3:1-3 “Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo. Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi,kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?

 

Ø  Ugomvi humuuzunisha Roho Mtakatifu – watu wa Mungu wanapojihusisha na ugomvi, hasira, ghadhabu, uchungu, kelele na matukano ambayo kimsingi ni matunda au matokeo ya ugomvi humuuzunisha Roho Mtakatifu na kuanza kumfifisha katika kanisa la Mungu na jamii na taifa.

 

Waefeso 4:29-31 “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia. Wala msimhuzunishe yule Roho Mtakatifu wa Mungu; ambaye kwa yeye mlitiwa muhuri hata siku ya ukombozi.Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya;”

               

Ø  Ugomvi unaweza kuwakosesha watu ufalme wa Mungu – Ugomvi ni moja ya matunda ya mwili au kazi za mwili, na wote wanaohusika na ugomvi kamwe hawawezi kuurithi ufalme wa Mungu.

 

Wagalatia 5:19-21 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”

 

Ø  Ugomvi ni hekima ya Shetani – Ugomvi ni chanzo na sababu ya dhambi nyingine, Shetani katika hekima yake anajua namna na jinsi ya kuondoa Amani miongoni mwa wanajamii na taifa kwa sababu hiyo ugomvi ni hekima ya shetani anajua kabisa katika magomvi atazalisha kiburi, mafarakano na kusababisha uharibifu mkubwa utakaozaa dhambi nyingine ikiwezekana hata mauaji, sio hivyo tu ataondoa Amani  kwa mfano hata wanandoa hawawezi kufurahia ndoa kama ugomvi unakuwa ni moja ya mtindo wa maisha kwa hiyo upendo huathiriwa, Yakobo anaonyesha kuwa hii ni hekima ya kishetani kwani yeye ndiye sababu ya machafuko!

 

Yakobo 3:15-17 “Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani. Maana hapo palipo wivu na ugomvi ndipo palipo machafuko, na kila tendo baya. Lakini hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki.”

Hitimisho:

Neno la Mungu linatuagiza kwamba tutafute kwa bidii kuwa na amani na watu wote, nyakati za Biblia wazee wetu walihakikisha kuwa wanatafuta Amani kwa bidii, kwa kuwa tuko duniani hitilafu zinaweza kutokea lakini hitimisho lililobora kwa watu wa Mungu na watu wenye busara ni kuhakikisha kuwa wanazika tofauti zao na kuitafuta Amani kwa bidii na huo ndio moyo wa kiungu ambao wazee wetu wa imani walikuwa nao.

Warumi 12:18-20 “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana. Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake.”                

Waebrania 12:14-15 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”            

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Hakuna maoni: