Jumatano, 28 Januari 2026

Hatimaye ndugu tuombeeni!


Warumi 15:30-32 “Ndugu zangu, nawasihi kwa Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa upendo wa Roho, jitahidini pamoja nami katika maombi yenu kwa ajili yangu mbele za Mungu; kwamba niokolewe na wale wasioamini katika Uyahudi, na tena huduma yangu niliyo nayo huko Yerusalemu ikubalike kwa watakatifu; nipate kufika kwenu kwa furaha, kama apendavyo Mungu, nikapate kupumzika pamoja nanyi.”




Utangulizi:

Ni muhimu kwetu kama kanisa kuwa na ufahamu, kuwa kuna changamoto kubwa katika kanisa la Mungu na changamoto mojawapo  kubwa ni hii ya kutokuwaombea watumishi wa Mungu, changamoto hii inaweza kuwa inachangiwa na ufahamu finyu wa neno la Mungu, au kutokutiliwa mkazo kwa fundisho hili muhimu na la msingi la kuwaombea watumishi wa Mungu, Mtume, Nabii, Mwinjilisti, Mchungaji na Mwalimu asiyekuwa na waombaji kwaajili yake hana tofauti na Askari aliyeingia vitani pake yake, akishambuliwa yeye hakuna tena msaada mwingine, Ni muhimu kuwa na maarifa na ufahamu ya kuwa kila huduma katika ufalme wa Mungu ina vita na mashambulizi mengi  ya upinzani wa ibilisi huelekezwa kwa watumishi wa Mungu, tunapowaombea tunawasaidia katika ulimwengu wa roho kuepushwa na mashambulizi makali na kuwawekea ulinzi dhidi ya utawala wa giza.

Mathayo 26:30-31 “Nao walipokwisha kuimba, wakatoka nje kwenda mlima wa Mizeituni. Ndipo Yesu akawaambia, Ninyi nyote mtachukizwa kwa ajili yangu usiku huu kwa kuwa imeandikwa, Nitampiga mchungaji, na kondoo wa kundi watatawanyika.”

Wakati Mungu amewatenga watumishi wake wawe kama chombo cha kuwakilisha kazi yake duniani, shetani naye anawalenga wawe silaha maalumu ya kuharibu kazi ya Mungu, au anaweza kutumia hila na mbinu mbalimbali kwa kusudi la kuwakwamisha ili kazi ya Mungu asiendelee mbele na ndio maana kwa kujua hali ilivyo katika ulimwengu wa Roho Paulo Mtume mara kwa mara aliwaomba watu wa makanisa mbalimbali wamuombee, tusipokuwa  na watu wa kutuombea katika huduma zetu tunajiweka katika hatari ya vita kali na kukabiliana na mashambulizi ya huduma peke yako, Jambo ambalo linaweza kusababisha ukadhoofika mapema na kuchoka.

2Wathesalonike 3:1-4 “Hatimaye, ndugu, tuombeeni, neno la Bwana liendelee, na kutukuzwa vile vile kama ilivyo kwenu; tukaokolewe na watu wasio haki, wabaya; maana si wote walio na imani. Lakini Bwana ni mwaminifu, atakayewafanya imara na kuwalinda na yule mwovu. Nasi tumemtumaini Bwana kwa mambo yenu, kwamba mnayafanya tulivyowaagiza, tena kwamba mtayafanya.”

Tutajifunza somo hili muhimu Ndugu tuombeeni kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-

 

·         Umuhimu wa kuwaombea watumishi wa Mungu.

·         Hatimaye ndugu tuombeeni.

·         Mifano ya watumishi wa Mungu waliokuwa na timu za waombaji.

 

Umuhimu wa kuwaombea watumishi wa Mungu.

Ni muhimu kuwa na ufahamu na maarifa kuwa watumishi wa Mungu wa aina zote wanahitaji maombi, na sio tu kuombewa  na washirika pekee lakini ikiwa uko uwezekano pia wawe na timu yaani kikundi au watu maalumu ambao wanaifanya kazi hiyo kwa uaminifu, Swala la kuombewa kwa watumishi wa Mungu ni swala la kiroho kabisa, na ni la kibiblia, kuomba maombi kwa washirika wetu ni swala la kibiblia na ni swala la unyenyekevu unaoonyesha kuwa tunahitaji neema ya Mungu baadhi ya watumishi wa Mungu wanafikiri kuomba maombi kwa washirika na kuwa na timu maalumu ya kuwaombea ni kuonyesha udhaifu, Jambo hili sio sahihi Kwani neno la Mungu linaonyesha kuwa watumishi wa Mungu wanahitaji kuombewa, Nyakati za Kanisa la kwanza walipoteza viongozi Muhimu sana wenye uwezo mkubwa sana katika jamii ya Kikristo mpaka walipopata ufunuo wa kuhakikisha kuwa wanaomba kwa nguvu na juhudi kubwa kwaajili ya wachungaji wao.

Matendo 6:8-13 “Na Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano; lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye. Hata wakashawishi watu waliosema, Tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu. Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi, wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati;”

Matendo 7:57-60 “Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli. Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu. Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.”

Matendo 12:1-5 “Panapo majira yale yale Herode mfalme akanyosha mikono yake kuwatenda mabaya baadhi ya watu wa kanisa. Akamwua Yakobo, ndugu yake Yohana, kwa upanga. Na akiona ya kuwa imewapendeza Wayahudi akaendelea akamshika na Petro. Siku hizo zilikuwa siku za mikate isiyochachwa. Alipokwisha kumkamata, akamweka gerezani akamtia mikononi mwa vikosi vinne vya askari wanne wanne, wamlinde, akitaka baada ya Pasaka kumtoa na kumweka mbele ya watu.Basi Petro akalindwa gerezani, nalo kanisa likamwomba Mungu kwa juhudi kwa ajili yake.”

Tunaona jinsi nyakati za kanisa la kwanza shetani alivyowatumia watu waovu kupinga kazi ya Mungu hasa kwa kuwaua viongozi wa kanisa wale waliokuwa mstari wa mbele katika kuieneza kazi ya injili, aliuawa Stefano na pia Yakobo Mtume ndugu yake Yohana, na Petro akakamatwa, ni wazi kabisa huu ulikuwa ni mpango mkakati wa kishetani wa kutaka kulidhoofisha kanisa, kwa hiyo hata kama kanisa lilikuwa linaomba sasa waliongeza kasi ya kumuomba Mungu kwa juhudi kwaajili ya viongozi wengine, tunasoma kuwa hata Petro alikamatwa lakini kanisa lilipoomba kwa juhudi Mungu alimtuma malaika wake na Petro akawekwa huru, tangu wakati huu, viongozi na washirika walielewa kuwa wanapaswa kuwalinda watumishi wa Mungu kwa maombi na kuwaombea ili kazi ya kueneza neema hii iweze kusonga mbele, kazi ya Mungu ina upinzani mkubwa na viongozi ndio wanaowindwa zaidi kwa sababu hiyo ni muhimu sana kwa kanisa kuomba, kuwa na programu endelevu za maombi ya kimkakati kuwaombea watumishi wa Mungu, kazi ya Mungu iweze kuendelea, ishara na miujiza viweze kufanyika, Na neno la Mungu liendelee kuhubiriwa kwa ujasiri.

Matendo 4:21-31“Nao walipokwisha kuwatisha tena wakawafungua, wasione njia ya kuwaadhibu, kwa sababu ya watu; kwa kuwa watu wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa hayo yaliyotendeka; maana umri wake yule mtu aliyefanyiwa ishara hii ya kuponya ulipita miaka arobaini. Hata walipofunguliwa, wakaenda kwa watu wao, wakawapasha habari ya mambo yote waliyoambiwa na wakuu wa makuhani na wazee. Nao waliposikia, wakampazia Mungu sauti zao kwa moyo mmoja, wakisema, Mola, wewe ndiwe Mungu, ndiwe uliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; nawe ulinena kwa Roho Mtakatifu kwa kinywa cha babaetu Daudi, mtumishi wako, Mbona mataifa wamefanya ghasia, Na makabila wametafakari ubatili? Wafalme wa dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya Kristo wake. Maana ni kweli, Herode na Pontio Pilato pamoja na Mataifa na watu wa Israeli, walikusanyika katika mji huu juu ya Mtumishi wako mtakatifu Yesu, uliyemtia mafuta, ili wafanye yote ambayo mkono wako na mashauri yako yamekusudia tangu zamani yatokee. Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu. Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote wakajaa Roho Mtakatifu, wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.”

Kwa hiyo kwa kuwaombea watumishi wa Mungu kanisa linashiriki kuwatia moyo kiroho kwaajili ya huduma zao, kutunza hisia zao, kuwaombea waweze kuwa na afya njema  na waweze kustahimili hasa wanapokutana na upinzani, waweze kubeba vema majukumu ya kikanisa na wawe na nguvu wakati wa kupambana na vita vya kiroho, kufanya hivyo pia ni njia ya kushiriki Baraka ya kazi wanayoifanya ya kuihubiri injili kwa usahihi na kuwalinda dhidi ya yule muovu, Mungu awape hekima ya maongozi, lakini zaidi ya yote ni njia ya kuonyesha upendo na ushirika pamoja nao.

Maandiko yanaonyesha pia shetani anaweza kuwazuia watumishi wa Mungu wasilifikie eneo Fulani kwa injili, Anga la Thesalonike lilikuwa gumu kwa Paulo mtume alipohubiri Thesalonike alikutana na upinzani mkali sana lakini sio hivyo tu hata alipotaka kurejea tena kwa kusudi la kuwaimarisha Shetani alimzuia na watumishi wengine, kwa hiyo shetani ni adui wa injili na ni adui wa wale wanaoipeleka injili anaweza kuwazuia wasifike eneo Fulani

1Wathesalonike 2:17-18 “Lakini sisi, ndugu, tukiwa tumefarakana nanyi kwa kitambo, kwa uso si kwa moyo, tulizidi kutamani kwa shauku nyingi kuwaona nyuso zenu.Kwa hiyo tulitaka kuja kwenu, naam, mimi Paulo, mara ya kwanza, na mara ya pili, na Shetani akatuzuia.”

Kama shetani anaweza kumzuia Paulo Mtume na timu yake wasifike Thesalonike kuwaimarisha wakristo waliozaliwa katika hali ya dhiki nyingi tena sio mara moja jiulize anashindwaje kutuzuia wewe na mimi ambao hatuna mwombezi zaidi ya wake zetu, tena wakati mwingine anatugonganisha nao ili maombi yetu yazuiliwe, tunahitaji maombi ya watu waaminifu atakaotambua kile ambacho tumekibeba na kulia na kuomboleza na kufunga kwaajili yetu. 

Hatimaye ndugu tuombeeni

2Wathesalonike 3:1-4 “Hatimaye, ndugu, tuombeeni, neno la Bwana liendelee, na kutukuzwa vile vile kama ilivyo kwenu; tukaokolewe na watu wasio haki, wabaya; maana si wote walio na imani. Lakini Bwana ni mwaminifu, atakayewafanya imara na kuwalinda na yule mwovu. Nasi tumemtumaini Bwana kwa mambo yenu, kwamba mnayafanya tulivyowaagiza, tena kwamba mtayafanya.”

Wote tunafahamu kuwa Paulo Mtume alikuwa ni moja ya viongozi hodari sana katika kuifanya kazi ya Mungu, Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa Paulo mtume alitumiwa na Mungu kwa viwango vikubwa na vya juu sana katika kulijenga kanisa la Mungu, naweza kusema kuwa hakuna mtu anaweza kudai kuwa yeye ni wa kiroho kumzidi Paulo Mtume neno la Mungu linaonyesha ya kuwa alifanya kazi kuliko mitume wote, alipewa mafunuo makubwa kuliko mtu yeyote, lakini pia alitumiwa na Mungu kufanya miujiza ya kupita kawaida kwa mikono yake

1Wakorintho 15:9-10 “Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami.”

2Wakorintho 12:2-4 “Namjua mtu mmoja katika Kristo, yapata sasa miaka kumi na minne, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua). Mtu huyo alinyakuliwa juu mpaka mbingu ya tatu. Nami namjua mtu huyo, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua); ya kuwa alinyakuliwa mpaka Peponi, akasikia maneno yasiyotamkika, ambayo haijuzu mwanadamu ayanene.”

Matendo 19:11-12 “Mungu akafanya kwa mikono ya Paulo miujiza ya kupita kawaida; hata wagonjwa wakaletewa leso na nguo zilizotoka mwilini mwake, magonjwa yao yakawaondokea, pepo wachafu wakawatoka.”

Hata pamoja na kutumiwa hivyo sana na Mungu, na kupewa mafunuo makubwa sana na kufanya kazi ya Mungu kwa neema kubwa kuliko mitume wote bado Paulo mtume kwa unyenyekevu mkubwa alionekana katika nyaraka nyingi akiomba kuombewa, mara kwa mara utaona akiomba maombi, ndugu tuombeeni, hatimaye ndugu tuombeeni, jitahidini pamoja nami katika maombi, hakuwa na kiburi wala hakufikiri kuwa anaweza peke yake na kumbuka kuwa yeye mwenyewe alikuwa mwombaji, watu wengi sana wa Mungu hawaijui siri hii wanadhani kuomba kuombewa na washirika ni kuonyesha  udhaifu, wanadhani ni sisi tu ndio wenye wajibu wa kuwaombea washirika  na ni kama washirika hawapaswi kutuombea  jambo hilo sio sahihi, au kuwa na timu ya watu wanaoomba kwaajili yako au hata wanaoomba pamoja nawe, huo sio udhaifu ni unyenyekevu na ni ukweli usiopingika kibiblia kuwa tunahitaji kuombewa, tunahitaji watu waaminifu, waliojitoa wanaojua nini wanakifanya kutuombea, tunahitaji maombi!

Warumi 15:30-32 “Ndugu zangu, nawasihi kwa Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa upendo wa Roho, jitahidini pamoja nami katika maombi yenu kwa ajili yangu mbele za Mungu; kwamba niokolewe na wale wasioamini katika Uyahudi, na tena huduma yangu niliyo nayo huko Yerusalemu ikubalike kwa watakatifu; nipate kufika kwenu kwa furaha, kama apendavyo Mungu, nikapate kupumzika pamoja nanyi.”

Waefeso 6:18-20 “kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote; pia na kwa ajili yangu mimi, nipewe usemi kwa kufumbua kinywa changu, ili niihubiri kwa ujasiri ile siri ya Injili; ambayo kwa ajili yake mimi ni mjumbe katika minyororo; hata nipate ujasiri katika huyo kunena jinsi inipasavyo kunena.”

Wakolosai 4:2-3 “Dumuni sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani; mkituombea na sisi pia, kwamba Mungu atufungulie mlango kwa lile neno lake, tuinene siri ya Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa,”

2Wakorintho 1:9-11. “Naam, sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti katika nafsi zetu ili tusijitumainie nafsi zetu, bali tumtumaini Mungu, awafufuaye wafu, aliyetuokoa sisi katika mauti kuu namna ile; tena atatuokoa; ambaye tumemtumaini kwamba atazidi kutuokoa; ninyi nanyi mkisaidiana nasi kwa ajili yetu katika kuomba, ili, kwa sababu ya ile karama tupewayo sisi kwa msaada wa watu wengi, watu wengi watoe shukrani kwa ajili yetu.”

Tunapowaombea watumishi wa Mungu wanapewa ujasiri, wanatumiwa na Mungu kwa miujiza, neno la Mungu linaenea kwa nguvu huku likishinda nguvu za upinzani, milango ya injili inafunguka, wananusuriwa na hatari za namna mbalimbali, huduma inaenea katika mataifa mengi kama wana kesi au wamefungwa minyororo inaachilia, lakini zaidi ya yote wanalindwa ili kwamba wasipepetwe katika imani wala imani zao zisitindike, Yesu alimuombea Petro awe imara,  Imani yake isitindike, ni maombi  yet utu ndio yatakayowadumisha watumishi wa Mungu na kuwafanya imara katika imani, mtumishi asiyeombewa hawezi kusimama, washirika wasio na akili husengenya na kuwashutumu watumishi wa Mungu wanapoingia majaribuni wakisahau kuwa hawajawahi hata siku moja kufanya wajibu wao wa kumlilia Mungu kwaajili yao ili wasimame imara na kushinda vikwazo vyote vinavyowakabili.

Luka 22:31-32. “Akasema, Simoni, Simoni, tazama, Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano; lakini nimekuombea wewe ili imani yako isitindike; nawe utakapoongoka waimarishe ndugu zako.”

Mifano ya watumishi wa Mungu waliokuwa na timu za waombaji

Kwa kufahamu siri hii ya kuwa kila mtumishi wa Mungu anahitaji maombi, baadhi ya watumishi wa Mungu waligundua kuwa kama Paulo Mtume aliyekuwa wa kiroho sana bado kuna nyakati alihitaji maombi ni zaidi sana mimi na wewe tunahitaji maombi, ndugu unahitaji kuombewa ninahitaji sana maombi yako pia, Katika historia ya kanisa, wahubiri wengi waliotumiwa na Mungu na kuleta uamsho mkubwa hawakuwa wanategemea kipawa na upako wao peke yao,  wala maombi yao peke yao lakini vile vile walikuwa na timu maalumu za waombaji waliobeba huduma zao kwa maombi endelevu na ya kudumu!

John Wesley – alizaliwa june 28 1703 na kufariki 2March 1791 moja ya mwinjilisti mkubwa sana duniani na mwanatheolojia maarufu ambaye likuwa sababu ya uamsho mkubwa wa kanisa la Uingereza, alikuwa na vikundi vidogo vidogo vingi kama madarasa ya maombi, hakuruhusu kufanya huduma bila nidhamu ya kiroho, alisababisha uamsho mkubwa huko uingereza na kusababisha mabadiliko makubwa ya kijamii, maadili  katika kazi na familia  na kusababisha kanisa lililodumu hadi leo, tunajifunza kwake kuwa maombi ya pamoja huzalisha mabadiliko ya kitaifa

Charles Finney – Ni moja ya wahubiri waliotumiwa sana na Mungu kuleta uamsho mkubwa alizaliwa 29 August 1792 na kufariki mwaka 16 August 1875, alikuwa ni muhudumu wa kanisa la American Presbyterian alijulikana  sana kama kiongozi wa uamsho mkubwa wa Pili katika Marekani, alikuwa akisimama kabla hata ya kuhubiri watu walililia toba kabla ya mahubiri kuanza na kulikuwa na uamsho mkubwa sana nyakati zake lakini yeye alisema wazi “Mahubiri yangu yalibebwa na Maombi ya Nash” Daniel Nash maarufu kama (Father Nash) alikuwa mtu mmoja maalumu ambaye kazi yake ilikuwa ni kuomba bila kukoma kabla ya Finney kuhubiri, Daniel Nash alikuwa anaenda katika mji husika ambao Finney angehubiri kwa muda kuanzia wiki au miezi kabla, akifunga na kuomba, Mahubiri yenye matokeo makubwa sana hutanguliwa na maombi makubwa sana.

D. L Moody – Moja ya wainjilisti maarufu sana Duniani  alizaliwa February 5 1837 na kufariki December 1899 jina lake kwa urefu ni Dwight Lyman Moody maarufu kama D.L Moody mwinjilisti maarufu wa kimarekani alihubiri injili na kusababisha maelefu ya watu kuokoka huko ulaya na Marekani, aliendelea na huduma bila kuwa na Skendo injili ilienea kupitia yeye kizazi kwa kizazi  lakini yeye alikuwa na timu ya waombaji waliokuwa wakikaa nyuma ya pazia wakati yeye alipokuwa anahubiri alisema “Ni Afadhali nopate watu 10 wanaoomba kuliko 10,000 wanaonisikiliza” mafanikio yoyote ya jukwaani ni matokeo ya kazi katika chumba cha maombi

Reinhard Bonnke – Muhubiri mkubwa sana Duniani chini ya huduma ya Christ for All nations (CfaN) amehubriri watu zaidi ya milioni 79 waliookoka katika huduma yake, Mungu alimtumia kwa miujiza mikubwa wakati akihubiri Afrika, huduma yake ilimuwezesha kutembelea bara zima, Muhubiri huyu mwenye asili ya Ujerumani alikuwa na mtandao mkubwa sana wa kimataifa wa waombaji, ambao walifunga wiki kadhaa na saa kadhaa kila alipokuwa akifanya mkutano wa injili Bonke alikuwa na timu mahususi ya kuombea huduma yake kwa hiyo tunajifunza hapo kuwa Huduma kubwa huitaji Jeshi kubwa la siri la waombaji.

Billy Graham – Moja ya wahubiri wakubwa walioheshimika sana Marekani alizaliwa 7 November 1918 na kufariki 21 February 2018 alikuwa na timu ya maombi iliyoitwa “The prayer Partners” yeye hakuwahi kukubali mkutano wowote ufanyike bila maandalizi ya maombi ya muda mrefu, Mungu alimpa neema ya kuhubiria maraisi wa aina mbalimbali, mataifa mengi na mamilioni ya watu alikaa katika huduma kwa karibu miaka 60 bila kuharibiwa na maswala ya fedha, umaarufu kiburi au wanawake, tunajifunza kutoka kwake ya kuwa maombi hutunza sio huduma tu hata sifa nzuri za muhubiri anayeombewa.

David Yonggi Cho – Mwanzilishi wa Kanisa la Yoido Full Gosple Church alizaliwa 14 February 1936 na kufariki 14 september 2021 ni moja ya waanzilishi wa maswala ya mlima wa maombi (Prayer Mountain) alitenga wachungaji na waombaji kila wakati kwaajili ya kufunga na kuomba na kukemea au kupigana vita vya kiroho, matokeo yake akawa ndiye mchungaji mwenye kanisa kubwa zaidi kuliko watu wote duniani kwa nyakati zake, alichangia kwa kiasi kikubwa uamsho ulioko Korea ya kusini, na alifanikiwa kwa kuanzisha mfumo wa cell groups au makanisa ya nyumbani ambao nao ulibebwa na maombi, tunajifunza kutoka kwake kuwa kanisa linalotaka kukua kwa haraka lazima lijikite katika mzizi wa kuomba.

Zachary Kakobe – Ni mwanzilishi wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship nchini Tanzania, moja ya makanisa ya kipentekoste yenye asili yake nchini Tanzania na si kutoka nje, Muhubiri maarufu sana mwenye kanisa kubwa huko Mwenge jijini Dar es Salaam, Mchungaji Kakobe ana mfumo wa cell ziitwazo “Power House” ambapo washirika katika maeneo mbalimbali kila mtaa waliko washirika hukutana kila alhamisi kwa maombi mbalimbali  ya kikanisa ikiwa ni pamoja na kumuombea Mchungaji, aidha ana kikundi maalumu ya maombi kijulikanacho kwa jina la  Ana binti Fanuel ambao pamoja na mambo mengine humuombea Mchungaji sawasawa na maelekezo yake kikundi hiki kinaundwa na wajane maalumu ambao hutunzwa na kanisa, Matokeo yake Kanisa lake limeweza kuenea nchi nzima kwa muda mfupi, kuna uamsho mkubwa sana unaofukuta chini kwa chini, washirikia wake wamejengwa katika misingi ya kuomba kwa kuyataja maandiko, wanapenda mafundisho na wanaishi kwa nidhamu. Alizaliwa 6 June 1955 huko, Kakonko, Kigoma, uamsho katika kanisa lake unakua kwa kasi kupitia maombezi, semina na mikutano ya ndani kwa ndani, pamoja na yeye mwenyewe kuwa mwombaji, Kakobe mara kwa mara amesisitiza kuombewa, kama ilivyokuwa kwa Paulo mtume, Kumbe maombi yana nguvu ya kuwaleta maelefu kwa Yesu, kuwafanya wanafunzi hata bila kuathiri, shughuli na utendaji wa maisha ya kawaida ya watu na kujenga kanisa imara

 

Hitimisho!

Unapochunguza kwa makini mifano hii michache ya wahubiri ambao Mungu aliwatumia kwa uamsho mkubwa sehemu mbalimbali duniani utabaini kuwa maombi yanahusika kwa kiasi kikubwa, sitaki kusema kuwa kila uamsho unaletwa na maombi lakini nataka kusema kuwa, mahuburi na uamsho wa kina na endelevu unajengwa kwa maombi, watumishi wa Mungu tutake maombi kwa washirika wetu, hata pamoja na sisi wenyewe kuwa waombaji, lakini pia tuwe na timu za maombi watu wanaotuombea kwa kina, na sio vibaya kuwa na timu ya watu wanaoomba pamoja nawe au wanaokuombea, Yesu alimtaka Petro, Yakobo na Yohana, wakeshe au waombe pamoja naye, Licha ya kuwa alikuwa wa kiroho sana na ni mwana wa Mungu, nadhani ni afadhali mara elfu kuwa na waombaji  wanaokuombea kwa huduma yako kuliko kuwa na walinzi wanaokulinda “Body guards

Mathayo 26:36-38 “Kisha Yesu akaenda pamoja nao mpaka bustani iitwayo Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa, hata niende kule nikaombe. Akamchukua Petro na wale wana wawili wa Zebedayo, akaanza kuhuzunika na kusononeka.Ndipo akawaambia, Roho yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa; kaeni hapa, mkeshe pamoja nami.”

Mtumishi wa Mungu mwombe Mungu akupe watu sahihi watakaokubebea mzigo katika maombi, omba Mungu akupe hekima kuchagua watu wasiri waliojaa maisha ya maombi wanyenyekevu, waaminifu, wenye upendo na mzigo au wajane wenye umri mkubwa wanaofanya kazi ya kuomboleza kwaajili yako, waelezee maono yako au mzigo unaotaka wakubebee, wafundishe masomo mbalimbali kuhusu kuomba, tengeneza mfumo au muda maalumu wa kuomba na siku maalumu za kuomba,  hata pamoja na kuwa na idara za maombi, amini sana katika watu wachache ambao maalumu au kipekee watakuwa wanakuombea, anza na watu wachache sana kikundi cha maombi kinatakiwa kuwa na watu 3-12 tengenezeni mawasiliano ya siri, wafundishwe kuishi maisha ya kujitoa na utakatifu, wenye matumizi mazuri ya kinywa wasio na mafarakano waandae kwa mafundisho maalumu ya waombaji kwaajili ya mtumishi wa Mungu kisha anzeni kuomba!

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 18 Januari 2026

Walinichukia bure!


Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.”

Yohana 15:24-25 “Kama nisingalitenda kwao kazi asizozitenda mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wametuona mimi na Baba yangu, na kutuchukia. Lakini litimie lile neno lililoandikwa katika torati yao, Walinichukia bure.”



Utangulizi:

Je umewahi kupitia hali katika maisha ambapo umekumbana na watu katika mazingira fulani kisha wakakuchukia tu bila ya sababu?  Au wakakupinga tu au wakakukataa, au ukakaliwa vikao, au kuitwa kwenye mabaraza ya watu waliojaa chuki na wivu wewe ukawa ndio agenda na kisha yakatolewa maamuzi ya kukuhukumu wewe hata bila ya sababu yenye mashiko? “Walinichukia bure bila ya sababu” ni moja ya usemi wenye nguvu sana wa kibiblia  ambao kivuli chake ni Zaburi 69:4 na Asili yake ni Yohana 15:24-25 ambapo Daudi pamoja na Yesu Kristo wanaelezea namna na jinsi walivyochukiwa na watu au maadui zao bila ya sababu, wakiwashambulia na kuwachukia  na kuwahukumu, na kuwapinga, na kuwafukuza bila sababu za haki, au kwa sababu ya chuki, wivu na kutokueleweka!, hata ingawa kuchukiwa, kukataliwa, kutokueleweka, na kuhukumiwa isivyo haki kunaweza kuwa na maumivu fulani kisaikolojia au kimwili, lakini kimaandiko jambo hili sio jipya kwani Biblia inatufundisha namna ya kuonyesha jinsi kupokea na kuonyesha mwitikio kwa mambo madogo kama haya kiroho  na sababu kwa nini unachukiwa bure bila sababu za maana, tutajifunza somo hili zuri Walinichukia bure! kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo;-

·         Maana ya kuchukiwa bure!

·         Sababu za kuchukiwa bure

·         Jinsi ya kupokea na kuitikia chuki zao za bure


Maana ya kuchukiwa bure!

Yohana 15:24-25 “Kama nisingalitenda kwao kazi asizozitenda mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wametuona mimi na Baba yangu, na kutuchukia. Lakini litimie lile neno lililoandikwa katika torati yao, Walinichukia bure.”

Ni muhimu kufahamu kuwa neno kuchukiwa katika lugha ya Kiebrania linatumika neno śānē  ambalo maana yake kwa kiingereza ni to detest, oppose or treat as an enemy  kwa Kiyunani (Greek) ni miseō ambalo kwa kiingereza ni to detest, reject, persecute or love less intentionally  katika msamiati wa kisaikolojia linatumika neno “antipathy” ambalo kiingereza ni a strong feeling of dislike kwa hiyo kuchukiwa katika lugha ya Kiswahili kwa maana hizo hapo juu tunaweza kutafasiri kama Hisia kali za kutokukubali, hisia za kukukataa, hisia za kukupinga, hisia za kukuona kama adui, hisia za kutokukupenda, hisia za kutamani wakutese au upatwe na mabaya au usiwepo, au kuhisi kukuchukia tu bila sababu za maana za makusudi au za kutokukusudia chuki hii inasukumwa na wivu wa kiroho moyoni mwa watu kwa sababu ya kibali cha kiungu ndani yako, kwa hiyo chuki hii wakati mwingine inaweza kutoka kwa watu waliokuzidi kila kitu,  wana cheo, wana mali, wana elimu, wakati mwingine hata umri mkubwa kuliko wako lakini wakikuona tu wanakuchukia bila sababu na unaweza kujiuliza mbona mimi sina lolote kama wao lakini wanakuchukia tu, Daudi anasema walionichukia ni hodari  wanaotamani kumkatilia mbali wana nguvu lakini hata hivyo walimchukia bure tu, hii ni chuki ambayo asili yake ni mambo ya rohoni na wivu wenye uchungu!

Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.”

Hapo tumeona maana ya neno chuki lakini vile vile neno “bure” katika biblia ya kiebrania linasomeka kama “hinnām” ambalo kwa kiingereza ni “unjustly” na katika biblia ya kiyunani linasomeka kama “dōrean” ambalo maana yake “undeservedly”  katika Kiswahili cha kimahakama kuchukiwa huku kulikuwa kusikokuwa na sababu za haki, kwa dhuluma, bila makosa ya kimahakama, bila kukutwa na hatia, isivyohalali, kwa hiyo watu wanaweza kukuchukia wewe kwa sababu isiyoweza kuthibitishwa kimahakama, kwamba mtuhumiwa ana makosa gani, kwa mfano Daudi alilipishwa kwa nguvu vitu ambavyo hakuvichukua, au Yesu alihukumiwa mahakamani huku hakimu akigundua kuwa ilikuwa ni wivu tu, walimtoa kwa husuda, hakuwa amewakosea wao, wala mtu yeyote.

Mathayo 27:17-18 “Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda.”

Unaona ndugu yangu unaweza kuchukiwa bure katika maisha haya ya kutembea na Yesu unaweza kupigwa vita, unaweza kuchukiwa bila ya sababu, unaweza kuchukiwa kwa sababu zisizo za kweli wala za haki, unaweza kuchukiwa hata na watu uliowahi kuwaomba msamaha hata pamoja na kuwa wamekukosea wao, chuki hii ni chuki ya husuda na haina mashiko, yanapokutokea haya katika maisha ya wokovu na wakati mwingine kutoka kwa watu waliookoka tena wenye nguvu kuliko wewe fahamu umebeba kusudi kubwa na maalumu, fahamu wewe ni mwanafunzi wa Yesu kweli kweli wala usifadhaike, Neno la Mungu linatufunulia siri hizo muhimu zinazopelekea wewe uchukiwe

Sababu za kuchukiwa bure.

Ni muhimu kufahamu kuwa chuki za bure kwako zinafunua maana pana sana za kiwango cha kiroho ulichokifikia, wakristo wengi leo wanaishi maisha ya kinafiki na sio wakweli kwa Mungu wala kwa wanadamu, wengi wanaishi maisha ya kuigiza, wanaonekana kama watu maarufu kwa nje, wakiwa na elimu kubwa, na vyeo vikubwa na wenye pesa na nguvu lakini hawana nguvu za kiroho walishakufa zamani na wamepoteza kabisa kujiamini, na kiroho wamefilisika, unapokuwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu na mfuasi wa kweli wa Bwana Yesu katika karne hizi, watakupendea nini? Wakupende kwa lipi? Kama wewe ni mwana wa Mungu tu hawakupendi, kama hujawahi kuwafanya lolote tu wanakuchukia bure je wataweza kuwapenda adui wa kweli ambao Yesu amesema wapendeni adui zenu? Waombeeni wanaowaudhi?, huoni kuwa agizo hilo ni la juu zaidi? Wewe maisha yako yanawapa tabu, kama Yesu alivyowapa taabu mafarisayo na masadukayo, kwa hiyo unapoona wanakuchukia bure ziko sababu nyingi na hapa na ainanisha chache:-

1.       Kwa sababu wewe ni nuru – Mtu wa Mungu ni hivi unapoishi maisha ya nuruni, hapa maana yake wewe ni mkweli kwa Mungu, unapokosea unatubu, na unasonga mbele na huna kinyongo na mtu na Mungu yuko upande wako na anakutetea na kukupigania basi elewa hivi maisha yako ya nuruni yanalifanya giza lidhalilike, hata kama husemi lolote lakini kuishi kwako kwa haki hata bila ya maneno kunawafunua wenye dhambi, kwa hiyo watu wanaweza kukuchukia sio kwa sababu ya kitu umefanya bali kwa sababu kuna kitu unakiwakilisha

 

Yohana 3:19-21 “Na hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu. Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru, matendo yake yasije yakakemewa. Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu.”

 

1Yohana 2:9-11 “Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa. Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru, wala ndani yake hamna kikwazo. Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza, tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha macho.”          

 

2.       Kwa sababu wewe si wa ulimwengu huu – Mtu wa Mungu kama wewe ni wa Yesu Kristo hivi unadhani ulimwengu utakupenda? Ukupende wewe nani? Ukupende wewe umeutendea nini? Ukupende wakati unafunua siri za Mungu? Ukupende wakati hata Yesu Mwenyewe walimchukia bure wewe kama u mwanafunzi wa Yesu utachukiwa tu, Yesu alisema kama mimi mwenyewe walinickukia mwanafunzi hampiti Mwalimu wake yaani kila mwanafunzi wa kweli wa Yesu atachukiwa tu, mpendwa chuki hiyo ni ushahidi wa wazi kwamba unamlingania Yesu Kristo, kuchukiwa kwako sio ushahidi wa kushindwa kwako bali ni ushahidi ya kuwa unamuishia Yesu Kristo  na sio hivyo tu hata mafundisho yetu yatakataliwa kama yalivyokataliwa ya Yesu

 

Yohana 15:18-20 “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na lenu.”

 

3.       Kwa sababu wewe ni wa rohoni na wao ni wa mwilini – Mtu wa Mungu ninataka nikuambie ya kwamba ulimwengu tulio nao una makundi makuu mawili tu, haijalishi kundi hilo liko kanisani au nje lakini kokote kwenye watu kuna aina mbili za watu watu wa rohoni na watu wa mwilini, wale wa mwilini huwaudhi wale wa rohoni hii ni kanuni ya kibiblia iliyokuwako zamani na inatenda kazi hata sasa, kama wewe ni mzaliwa wa kiroho utaudhiwa na yule wa mwilini tu ona  

 

Wagalatia 4:29 “Lakini kama vile siku zile yule aliyezaliwa kwa mwili alivyomwudhi yule aliyezaliwa kwa Roho, ndivyo ilivyo na sasa.”

 

4.       Kwa sababu ya kibali cha Mungu juu yako – Ndugu yangu mpendwa kama Mungu amekupa kibali, Mungu amekupaka mafuta, Mungu ana matumizi na wewe Mungu ana kusudi na wewe kibali cha Mungu juu yako kinawanyanyasa kisaikolojia wale wasio na kibali hicho sasa wakuchekee? Wakutie moyo, wakukubali wakati wanatamani kusikia umeharibikiwa, wanatamani hata ufe leo, Daudi anasema wanaomchukia ni wengi kuliko nywele za kichwa chake, kaangalie mashariki ya kati Israel inapendwa? Wanatamani waifutilie mbali wanatamani waikatilie mbali ndivyo ulivyo na wewe mtu wa Mungu, kibali chako kinawasumbua haijalishi hali ya nje kuwa wao wana nguvu lakini upako wako unawanyanyasa ndio maana wanakuchukia bure

 

1Samuel 29:6-8 “Hata ikawa, walipokuwa wakienda, hapo Daudi aliporudi baada ya kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka katika miji yote ya Israeli, kwa kuimba na kucheza, ili kumlaki mfalme Sauli; wakatoka na matari, na shangwe, na vinanda. Nao wale wanawake wakaitikiana wakicheza, wakasema, Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake. Basi Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme?

 

Mwanzo 37:3-11 “Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani. Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”

 

5.       Kwa sababu ya wivu wenye uchungu – Mpendwa wakati mwingine wewe unachukiwa bure kwa sababu ya wivu, ni wivu tu, kuna kitu wakijilinganisha na wewe au na ninyi  wanakuona kabisa unakwenda mbele, wanakuona kabisa uko tofauti hata kama kwa sasa huna kitu wanakuona na wanajua uweza wa Mungu juu yako na kile ambacho Mungu amewekeza ndani yako wakupende kwa lipi wakati wamejaa wivu, wamejaa wivu huu ni wivu wenye uchungu wivu wa kujilinganisha na wao na wakijilinganisha na wewe wanaona kuna kitu cha ziada kwako wivu huu wa kujilinganisha unaitwa “phthonos” kwa kiingereza “is hatred rooted in comparison”  Yesu alichukiwa kwa sababu alikuwa na kitu cha ziada kuliko mafarisayo na masadukayo, kwa hiyo walikuwa na wivu uliojaa chuki aina hii ya wivu wakati mwingine huwazungumzia watu vibaya  na mambo mabaya ili wao waonekane wema yule mwema aonekane mbaya.

 

Mathayo 27:17-18 “Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda.”

 

Matendo 5:16-20 “Nayo makutano ya watu wa miji iliyoko kandokando ya Yerusalemu wakakutanika, wakileta wagonjwa, nao walioudhiwa na pepo wachafu; nao wote wakaponywa. Akaondoka Kuhani Mkuu na wote waliokuwa pamoja naye, (hao ndio walio wa madhehebu ya Masadukayo), wamejaa wivu, wakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza; lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu.”

 

Waebrania 12:14-15. “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”    

 

6.       Kwa sababu ya vita vya kiroho – Wakati mwingine ile chuki inatokana na mapepo, kwa kadiri shetani alivyo adui yetu na anavyotuchukia sisi ndivyo anavyowatumia mapepo na maajenti wake au wakristo dhaifu kutumiwa na mapepo kutushambulia kwa hio wakati mwingine hii chuki kubwa unayoiona dhidi yako mtu wa Mungu ni ya shetani akiwatumia watu wake au vyombo vyake ili kupingana na kile ambacho Mungu amewekeza ndani yako

 

Waefeso 6:12 “Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”

 

7.       Kwa sababu ya kuishi maisha ya utauwa -  kila unapokusudia na kuthubutu kuishi maisha ya tofauti na wengine maisha ya utakatifu na kuimarisha uhusiano wako wa siri na Mungu watu wabaya  na wadanganyaji wanaendelea kuteseka  na watakucukia, wewe jaribu kuishi na kuigiza kila alichikifanya bwana Yesu, jitoe kama yeye fuata mfano wake uone kama dunia itakupongeza hata kidogo!  Utachukiwa, utateswa, utadhihakiwa, utakataliwa, utaonekana huna faida, kwa sababu maisha ya kujitoa kwa Mungu yanapingana nay a dunia hii, viwango vya kuishi kama Kristo vinawaudhi wahuni,  vinawapa changamoto na kuwafanya wote walio vufuvugu na wasiookoka  wakose Amani, kwa hiyo kuchukiwa ni sehemu ya gharama za uaminifu wako kwa Mungu au kumfuata Yesu kwa uaminifu

 

2Timotheo 3:12-15 “Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa. lakini watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika. Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.”   

 

Jinsi ya kupokea na kuitikia chuki zao za bure

Ni jambo la kumshukuru Mungu kwamba Mungu ametupa akili na ufahamu katika neno lake namna na jinsi ya kushughulika na watu wanaotuchukia na njia hizo ni njia za kiroho, ambazo kimsingi zitakufanya wewe kuzidi bali adui zako kupungua, njia hizi ukizitumia zitakamilisha uwezo wako wa kiroho na kukunoa na kukufanya wewe uendelee kukua kiroho zaidi na kumfanania baba wa mbinguni

1.       Kunyamaza kimya – Moja ya njia ya kiroho ambayo Yesu Kristo aliitumia pale waliokuwa wakimchukia walipokuwa wakimsingizia mambo ya uongo ambayo hayana ukweli wowote bali kwa lengo la kumchafua na kuharibu tu wito wake yeye alikaa kimya, alipoonewa aikaa kimya alipoteswa na kutukanwa alikaa kimya, Neno kukaa kimya katika kiyunani ni “loidoreō kwa kiingereza ni “revile” ambalo maana yake ni “to insult verbally” hakutumia lugha chafu kujibu alinyamaza kimya badala ya kujibu “silence over revenge”  na alijikabidhi kwa Mungu ahukumuye kwa haki, Mpendwa mwachie Mungu atajibu kwa haki, Mungu huwapigania watu wakimya

 

1Petro 2:21-23 “Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki.”

 

Isaya 53:7 “Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake.”

 

Hesabu 12:1-9 “Kisha Miriamu na Haruni wakamnenea Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa; maana, alikuwa amemwoa mwanamke Mkushi. Wakasema, Je! Ni kweli Bwana amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia? Bwana akasikia maneno yao. Basi huyo mtu, huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi. Bwana akanena ghafula na Musa, na Haruni na Miriamu, na kuwaambia, Tokeni nje ninyi watatu, mwende hemani mwa kukutania. Basi hao watatu wakatoka nje. Bwana akashuka katika nguzo ya wingu akasimama pale mlangoni pa Hema, akawaita Haruni na Miriamu, nao wakatoka nje wote wawili. Kisha akawaambia, Sikizeni basi maneno yangu; Akiwapo nabii kati yenu, Mimi, Bwana, nitajifunua kwake katika maono, Nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; Yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote; Kwake nitanena mdomo kwa mdomo, Maana, waziwazi wala si kwa mafumbo; Na umbo la Bwana yeye ataliona. Mbona basi ninyi hamkuogopa Kumnenea mtumishi wangu, huyo Musa? Hasira za Bwana zikawaka juu yao; naye akaenda zake.”

 

2.       Waombee wanao kuudhi – Maandiko yanatufundisha kutoka mafundisho na maendo ya Bwana wetu Yesu na watakatifu walioyutangulia kuwa kuna haja ya kuwaombea wale wanaotuchukia, tuwaonee huruma na tuwapende kwa sababu wao ni dhaifu

 

Mathayo 5:43-45 “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.”

 

Luka 23:33-34 “Na walipofika mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, ndipo walipomsulibisha yeye, na wale wahalifu, mmoja upande wa kuume, na mmoja upande wa kushoto. Yesu akasema, Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo. Wakagawa mavazi yake, wakipiga kura.”

 

3.       Endelea kutenda mema -  Lengo kubwa la shetani wakati mwingine kukushambulia kupitia watu ni ili wewe uwe mtu mbaya, uone kuwa kila unapotenda mema unalipwa mabaya kwa hiyo unaamua kufunga milango yako ya wema na kuwa mbinafsi lakini neno la Mungu linatutaka tuendelee kuwa washindi kwa kutenda mema, kadiri unavyoendelea kuwa mwema na kutenda haki wema wako utawanyamazisha maadui zako na kila ubaya wanaokuzushia

 

Warumi 12:19 “Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana.Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake. Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.”

 

4.       Endelea kupiga kazi, endelea kumtumikia Mungu – Wakati maadui zako wanapokushambulia wewe ongezea viwango vya kumtumikia Mungu na kufanya kazi kwa bidii, kadiri unavyoendelea kumtumikia Mungu kwa bidii Mungu ataendelea kukubariki na kazi unazozifanya zitatangaza kile kitu Mungu ameweka ndani yako,  na kuudhihirishia ulimwengu kuwa yeye yuko na wewe, unapoendelea kumtumikia Mungu kwa nguvu Baraka zako zinaendelea kuongezeka na adui zako wanaendelea kuwekwa uchi neno la Mungu linasema adui zako watakuonyesha maungo yao, yaani uchi zao zitafunuliwa, aibu zao zitawekwa wazi, utupu wao utahukumiwa na kazi unazozifanya wataaibika na kazi yako itasema si biblia imesema kwa matunda yao mtawatambua, je mti mbaya unaweza kuzaa matunda mema?

 

Kutoka 23:25-27 “Nanyi mtamtumikia BWANA, Mungu wenu, naye atakibarikia chakula chako, na maji yako; nami nitakuondolea ugonjwa kati yako. Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba, wala aliye tasa, katika nchi yako; na hesabu ya siku zako nitaitimiza.Nitatuma utisho wangu utangulie mbele yako, nami nitawafadhaisha watu wote utakaowafikilia, nami nitawafanya hao adui zako wote wakuonyeshe maungo yao.”   

 

Yohana 10:37-38 “Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba.”

 

Chuki kutoka kwa wapendwa na watumishi wenzako haimaanishi kuwa Mungu amekuacha bali inakufundisha kuelewa maswala ya kiroho, sio kuwa wakati wote watu watakuchukia kwa sababu wewe ni muovu hapana bali kwa sababu wao ni dhaifu kiroho, Mungu anakufundisha uwezo wa kuvumilia kabla ya kukuinua kukubariki na kukutumia, Mungu anakufundisha kuwa kama Yeye, wewe hujasahaulika, wewe hujashindwa wewe uko sawa na Daudi, uko sawa na Yusufu unafafanana na Yesu  na  ndio maana unachukiwa bila ya sababu za halali, wewe utakuwa kiroho vizuri zaidi, ukiyamudu hayo machungu yote ujue wazi kuwa thawabu yako ni kubwa sana mbinguni


Mathayo 5:11-12 “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu.”              

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote


Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 11 Januari 2026

Mwanzi uliopondeka hatauvunja!


Isaya 42:1-4 “Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu. Hatalia, wala hatapaza sauti yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli. Hatazimia, wala hatakata tamaa, hata atakapoweka hukumu duniani; na visiwa vitaingojea sheria yake.”



Utangulizi:

Kaka zangu na dada zangu katika Bwana, Leo tutachukua muda kujifunza mojawapo ya unabii wa muhimu sana katika huduma ya Masihi ambao kimsingi ulikuja kutimizwa katika agano jipya, Wakati wa huduma ya Masihi hapa duniani, Unabii huu ambao kimsingi unatufundisha kusudi kubwa la huduma na moyo wa Masihi Yesu Kristo hapa ulimwenguni, jinsi alivyojawa na huduma iliyojaa rehema na upendo unaopitiliza mipaka ya kawaida ya huduma za kibinadamu na kidini.

Mathayo 12:15-21 “Naye Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote, akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.”

Kwa ujumla unabii wa Isaya na kutimia kwake kunatukumbusha jambo muhimu sana na lenye kutia moyo ya kuwa Ufalme wa Mungu unatenda kazi katika msingi wa rehema, urejesho na huruma zisizotikisika! “Mwanzi uliopondeka hatauvunja na utambi utokao moshi hatauzima” vinawakilisha nini hasa katika ujumbe huu? Bila shaka Mungu Roho Mtakatifu atatupa kuelewa; Tutajifunza somo hili Mwanzi uliopondeka hatauvunja kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-

·         Ufahamu kuhusu mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi

·         Huduma ya kimasihi mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi

·         Mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi


Ufahamu kuhusu mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi.

Ni muhimu kufahamu kuwa usemi wa “mwanzi uliopondeka na utambi utoka moshi” ni usemi wenye maana gani kinabii kabla ya kuunganisha na kuangalia huduma ya kimasihi itakavyokuwa, Neno mwanzi linalotumika katika maandiko ya kiingereza linatumika neno “REEDS” ambalo kwa Kiswahili maana yake ni nyasi, Hata hivyo nyasi ziko za aina mbalimbali, kwa hiyo nyasi hizi katika

lugha ya Kiebrania zinaitwa kwa kutumia neno Kāneh kwa lugha ya Kilatini na Kiyunani linatumika neno Canna kwa kiingereza Cane  mmea huu kwa kawaida ulistawi sana pembeni mwa mto Jordan katika taifa la Israel kwa Kiswahili unaitwa MWANZI, majani ya Mwanzi au Cane kwa Kiyunani yanajulikana kama kálamos au Calamus, kwa Kiswahili Kalamu. Nyakati za agano la kale kabla ya kuwepo kwa teknolojia ya uandishi tuliyo nayo sasa Manabii na waandishi walitumia majani ya muanzi kama kalamu ya kuandikia, waliyatumia majani haya na kuchovya kwenye wino na kuyatumia kuandikia katika karatasi maalumu za nyakati hizo (Papyrus) au Magombo ya chuo ya ngozi, walichovya katika bakuli la wino kwa kutumia majani hayo yaliyoitwa kalamu na kisha kuyatumia kuandikia endapo kalamu ingechoka au kupondeka waliitupa na kuchomoa jani lingine la muanzi yaani kalamu na kutoka kwenye kitita cha majani hayo na kulitumia kuandika, waandishi wangeifanya kazi hiyo ngumu kutwa nzima na usiku, huku usiku wakitumia taa ya kibatali iliyotumia mafuta na utambi, manabii na waandishi walifanya kazi ya kuandika mpaka mafuta yangewaishia na taa ikazimika na utambi ungebaki unafuka moshi hapo wangezima kabisa na kulala wakiwa wamechoka sana kitendo cha kuvunjika kwa Kalamu au kuisha kwa utambi kulikwamisha kwa kiwango kikubwa kazi nzima ya uandishi, wakati huu nabii Isaya alipokea ujumbe wa kinabii kwamba kazi hiyo ya kuchosha itakuwa nyepesi, wakati wa Masihi, na wakati wa Masihi kalamu haitavunjika wala utambi hautaisha na kufuka moshi, uwepo wake utasababisha uzima katika mazingira yote.

Isaya 42:1-3 “Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu. Hatalia, wala hatapaza sauti yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli.”

Huduma ya kimasihi mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi

Kimsingi Mwanzi uliopondeka na utambi unaofuka moshi ulikuwa ni usemi uliotumika kuelezea pia kitu ambacho kimepoteza maana, hakifai tena kwa matumizi, kitu kinachokwamisha kazi ya uandishi kusonga mbele, lakini sio hivyo tu usemi huu ulitumika pia kuwaita mataifa mengine wasio wayahudi yaani mataifa, hao waliitwa pia mwanzi uliopondeka, na utambi utokao moshi ulimaanisha watu wa Mungu ambao wamepoteza thamani yao, yaani walikuwa Nuru na sasa wamezimika hawafai tena kwa matumizi, Mwanzi mataifa wasiofaa, Utambi wayahudi waliopoa.

Mwanzi uliopondeka – Uliwakilisha mataifa au watu wenye dhambi lakini pia, walemavu au wagonjwa, watu wasio na matumaini, waliokandamizwa ambao kila kitu kwao kimepoteza maana wamepoteza maana katika jamii, hawafai, wamevunjika, hawana matumizi tena, ni wa kutupwa, wanyonge, waliochoka nafsi zao, sababu ya changamoto, wenye laana, wenye mikosi wasioofaa kitu, wasio na uhakika wa wokovu, wanaohesabika kuwa sio kitu wanaosubiria kuchomwa moto.

Utambi utokao moshi – Uliwakilisha watu wa Mungu Israel wenyewe waliokuwa nuru lakini wamepoteza thamani wamepoa wamerudi nyuma, hawana thamani tena ni watenda dhambi wamepoa, wote wanaosubiria hukumu yao tu hawana kitu cha ziada zaidi ya kukwamisha kazi.

Isaya anaona kuwa wanasubiri maamuzi ya hakimu ambaye ni Masihi, yeye anajua atawahukumuje hiki ndicho Isaya alichokuwa anakiona katika unabii wake lakini anaona kama Masihi atakapokuja huenda mambo yatakuwa tofauti, kwani hukumu zake ni tofauti na uweza wake ni tofauti yeye Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima kwa kuwa yeye ana Roho wa Mungu, anapendezwa na Mungu anajua atayatimiza vipi mapenzi ya Mungu, Kwa Masihi hakutakuwa na mtu asiye na faida, hakutakuwa na mtu wa kutupwa, au kuzimwa ni wakati wa uamsho mkubwa sana Masihi atatenda kwa namna ya tofauti sana na mitazamo ya dini ya Kiyahudi

Huyu mataifa wanamtumainia, Kimsingi Isaya aliyatabiri maswala hayo katika unabii wake na Kristo Yesu alipokuja Duniani aliyatimiza haya na ndio Mathayo alipoyaona alikumbuka kile alichokuwa amekitabiri nabii Isaya akaandika sawa na unabii wa Isaya

Mathayo 12:15-21 “Naye Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote, akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.”

Masihi alipokuja alihukumu kwa haki kwani kwanza aliwaona wote kuwa ni wenye dhambi, Mataifa na Wayahudi pia na hakukuwa na aliye bora kuliko mwingine wote wanahitaji msaada wake, Wayahudi na Mataifa mengine wote ni wenye dhambi wote wanamuhitaji Masihi hakuna mwenye haki hata mmoja wala hakuna anayemtafuta Mungu wala hakuna anayetenda mema hata mmoja wala hakuna anayemcha Mungu, hakuna aliye bora kuliko mwingine hakuna mwenye nafuu wote wanahitaji rehema za Mungu na Masihi amekuja kwaajili hiyo hakuja kuhukumu amaekuja kutangaza rehema za Mungu, amekuja kutangaza msamaha wa dhambi, fadhili za Mungu na kuponya mwili na roho

Warumi 3:9-18 “Ni nini basi? Tu bora kuliko wengine? La! Hata kidogo. Kwa maana tumekwisha kuwashitaki Wayahudi na Wayunani ya kwamba pia wamekuwa chini ya dhambi; kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja. Koo lao ni kaburi wazi, Kwa ndimi zao wametumia hila. Sumu ya fira i chini ya midomo yao. Vinywa vyao vimejaa laana na uchungu. Miguu yao ina mbio kumwaga damu. Uharibifu na mashaka yamo njiani mwao. Wala njia ya amani hawakuijua. Kumcha Mungu hakupo machoni pao.”

Huduma ya Masihi inatoa rehema kwa wote waliovunjika na waliopoa wanaofuka moshi tu lakini moto umezimika wote wanamuhitaji Yesu, achochee utambi uwake na aponye waliovunjika,  uvumilivu na upole na upendo wa Bwana wetu Yesu Kristo ndio unaowavumilia watu leo na kuwapa nafasi ili waponywe na moto uwake tena, lakini sio hivyo tu Yesu yuko tayari kushughulika na wote walioumizwa, wanaohitaji rehema na upendo wake yeye yuko tayari kuwahudumia na kuwaponya watu wote wanapaswa kumuendea na watu wote wanapaswa kulitegemea jina lake, Yeye hazimii wala hakati tamaa na mtu, watu wote watamtumainia na kuliitia jina lake yeye yuko tayari kusaidia.

Matendo 4:10-12 “jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”                 

Mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi.

Mathayo 12:15-21 “Naye Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote, akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.”

Mathayo alipokuwa anawaona watu mbalimbali matajiri kwa masikini, wenye nguvu na wasio na nguvu wakimiminika kwa kutafuta msaada kwa Yesu alikumbuka kutimia kwa unabii wa Isaya na anaunukuu.

Huduma ya Masihi ilikazia ukweli kuwa Yesu hakuja kwaajili ya wenye nguvu, wala wenye kujitosheleza, wanaojifikiria kuwa wao ni wakamilifu amekuja kwaajlii ya waliovunjika wasio na faida waliozimika, Yesu alitakasa wenye ukoma, aliwagusa wakoma waliokuwa wamekataliwa, alisamehe wenye dhambi, aliwarejesha hata wale waliomkana mara tatu kama Petro, alishughulika na wale ambao wangestahili kubadilishwa na kutupwa, Mwanzi uliovunjika haukufaa tenza kwa waandishi zaidi ya kuchomwa moto na kutumia mwingine na utambi uliofuka moshi ulisubiri kubadilishwa, Lakini Masihi yeye angehuisha vile vinavyoonekana kutokufaa viweze kufaa kwa utukufu wa Mungu

Luka 5:30-32 “Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.”

Marko 16:6-7 “Naye akawaambia, Msistaajabu; mnamtafuta Yesu Mnazareti, aliyesulibiwa; amefufuka; hayupo hapa; patazameni mahali walipomweka. Lakini enendeni zenu, mkawaambie wanafunzi wake, na Petro, ya kwamba awatangulia kwenda Galilaya; huko mtamwona, kama alivyowaambia.”             

Yohana 21:15-17 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam ,Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu. Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.”

Huduma ya kimasihi ni huduma ya uponyaji wa mwili nafsi na roho, ni huduma ya uvumilivu ni huduma ya huruma na upendo ni huduma ya kuchukuliana  na ni huduma ambayo haioni mkamilifu inaona kuwa kila mtu anahitaji huduma yake isipokuwa wale wenye kiburi tu na wale wanaojihesabia haki, kila mtu na kila mmoja anamuhitaji Bwana Yesu na ukarabati wa watu wa Mungu wa aina zote unatakiwa kupatikana kanisani, kanisani sio mahali pa watakatifu tu ni mahali pa watu wote wenye nguvu na dhaifu atakayekuja kuchuja ni Yesu mwenyewe, wajibu wetu sisi ni kuhubiri injili, na kuwafundisha watu na Neno la Mungu lenyewe litawabadilisha, Yesu mwenyewe atawaokoa na kuwasamehe watu wake yeye ndiye anayeweza kuwafinyanga watu wake wakawa kama yeye alivyo, hukumu halali itatolewa siku ya mwisho na mwenyewe sio sisi

Mathayo 13:47-50 “Tena ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lililotupwa baharini, likakusanya samaki wa kila namna; hata lilipojaa, walilivuta pwani; wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali walio wabaya wakawatupa. Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika watatokea, watawatenga waovu mbali na wenye haki, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.”

Uko uwezekano kuwa unaona ujumbe huu huku ukiwa umevunjika moyo, una ndoa iliyovunjika, una uchumba uliovunjika una mahusiano yaliyopondeka, una nuru iliyozimika una hasara katika biashara na hujui utainukaje, una madeni, au utambi wako wa rohoni umezimika, matumaini ya maisha yako na ndoto zako zimekwama mahali.  Giza limetanda na kila kitu kinaonekana kukwama katika maisha yako, uwezo wako wa kusimama tena umepotea, muda wako umepotea, unajiuliza itakuwaje tena katika maisha yangu? Itakuwaje katika roho yangu? Je naweza kusimama tena hata baada ya kuharibu namna hii? Lakini kwa uwezo wa Bwana wetu Yesu Kristo, yeye anakuganga na kukuponya na kukuinua tena nakuhakikishia moto uliozimika utawaka na moyo uliovunjika utainuka hii ndio kazi ya Masihi amka leo acha kulia katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai, Yesu alikuja kwaajili ya watu kama wewe watu ambao wanatarajiwa kutupwa, na wanaoonekana kutokufaa katika jamii wenye matumaini yaliyofifia yeye haogopi hayo na anatoa mwaliko kuwa watu wote wenye changamoto zozote zile waje kwake

Mathayo 11:28-29 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;”

“Maombi yangu yafike kwako Moyo, uliopondeka hutadharau, Kiu yangu na haja yangu, nifanane nawe nifanane nawe, nifanane nawe, Nifanye kama wewe, unifinyange, nifinyange, wakinitazama wakuone wewe unifinyange, nifinyange”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!