Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi
Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui
zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu
nisivyovichukua.”
Yohana 15:24-25 “Kama nisingalitenda kwao
kazi asizozitenda mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wametuona
mimi na Baba yangu, na kutuchukia. Lakini litimie lile neno lililoandikwa
katika torati yao, Walinichukia bure.”
Utangulizi:
Je umewahi kupitia hali katika
maisha ambapo umekumbana na watu katika mazingira fulani kisha wakakuchukia tu
bila ya sababu? Au wakakupinga tu au
wakakukataa, au ukakaliwa vikao, au kuitwa kwenye mabaraza ya watu waliojaa
chuki na wivu wewe ukawa ndio agenda na kisha yakatolewa maamuzi ya kukuhukumu
wewe hata bila ya sababu yenye mashiko?
“Walinichukia bure bila ya sababu” ni moja ya usemi wenye nguvu sana wa
kibiblia ambao kivuli chake ni Zaburi 69:4 na Asili yake ni Yohana 15:24-25 ambapo Daudi pamoja na
Yesu Kristo wanaelezea namna na jinsi walivyochukiwa na watu au maadui zao bila
ya sababu, wakiwashambulia na kuwachukia
na kuwahukumu, na kuwapinga, na kuwafukuza bila sababu za haki, au kwa
sababu ya chuki, wivu na kutokueleweka!, hata ingawa kuchukiwa, kukataliwa,
kutokueleweka, na kuhukumiwa isivyo haki kunaweza kuwa na maumivu fulani kisaikolojia
au kimwili, lakini kimaandiko jambo hili sio jipya kwani Biblia inatufundisha
namna ya kuonyesha jinsi kupokea na kuonyesha mwitikio kwa mambo madogo kama
haya kiroho na sababu kwa nini
unachukiwa bure bila sababu za maana, tutajifunza somo hili zuri Walinichukia bure! kwa kuzingatia
vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo;-
·
Maana ya
kuchukiwa bure!
·
Sababu za
kuchukiwa bure
·
Jinsi ya
kupokea na kuitikia chuki zao za bure
Maana ya kuchukiwa bure!
Yohana 15:24-25 “Kama nisingalitenda kwao
kazi asizozitenda mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wametuona
mimi na Baba yangu, na kutuchukia. Lakini litimie lile neno lililoandikwa
katika torati yao, Walinichukia bure.”
Ni muhimu kufahamu kuwa neno
kuchukiwa katika lugha ya Kiebrania linatumika neno śānē ambalo maana yake kwa kiingereza ni to detest, oppose or treat as an enemy kwa Kiyunani (Greek) ni miseō ambalo kwa kiingereza ni to detest, reject, persecute or love less
intentionally katika msamiati wa kisaikolojia linatumika
neno “antipathy” ambalo kiingereza
ni a strong feeling of dislike kwa
hiyo kuchukiwa katika lugha ya Kiswahili kwa maana hizo hapo juu tunaweza
kutafasiri kama Hisia kali za kutokukubali, hisia za kukukataa, hisia za
kukupinga, hisia za kukuona kama adui, hisia za kutokukupenda, hisia za
kutamani wakutese au upatwe na mabaya au usiwepo, au kuhisi kukuchukia tu bila
sababu za maana za makusudi au za kutokukusudia chuki hii inasukumwa na wivu wa
kiroho moyoni mwa watu kwa sababu ya kibali cha kiungu ndani yako, kwa hiyo
chuki hii wakati mwingine inaweza kutoka kwa watu waliokuzidi kila kitu, wana cheo, wana mali, wana elimu, wakati
mwingine hata umri mkubwa kuliko wako lakini wakikuona tu wanakuchukia bila
sababu na unaweza kujiuliza mbona mimi sina lolote kama wao lakini wanakuchukia
tu, Daudi anasema walionichukia ni hodari
wanaotamani kumkatilia mbali wana nguvu lakini hata hivyo walimchukia
bure tu, hii ni chuki ambayo asili yake ni mambo ya rohoni na wivu wenye
uchungu!
Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko
nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu
kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.”
Hapo tumeona maana ya neno chuki
lakini vile vile neno “bure” katika
biblia ya kiebrania linasomeka kama “hinnām” ambalo kwa kiingereza ni “unjustly” na katika biblia ya
kiyunani linasomeka kama “dōrean” ambalo maana yake “undeservedly” katika Kiswahili cha kimahakama kuchukiwa
huku kulikuwa kusikokuwa na sababu za haki, kwa dhuluma, bila makosa ya
kimahakama, bila kukutwa na hatia, isivyohalali, kwa hiyo watu wanaweza
kukuchukia wewe kwa sababu isiyoweza kuthibitishwa kimahakama, kwamba mtuhumiwa
ana makosa gani, kwa mfano Daudi alilipishwa kwa nguvu vitu ambavyo hakuvichukua,
au Yesu alihukumiwa mahakamani huku hakimu akigundua kuwa ilikuwa ni wivu tu,
walimtoa kwa husuda, hakuwa amewakosea wao, wala mtu yeyote.
Mathayo 27:17-18 “Basi walipokutanika,
Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye
Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda.”
Unaona ndugu yangu unaweza
kuchukiwa bure katika maisha haya ya kutembea na Yesu unaweza kupigwa vita,
unaweza kuchukiwa bila ya sababu, unaweza kuchukiwa kwa sababu zisizo za kweli
wala za haki, unaweza kuchukiwa hata na watu uliowahi kuwaomba msamaha hata
pamoja na kuwa wamekukosea wao, chuki hii ni chuki ya husuda na haina mashiko,
yanapokutokea haya katika maisha ya wokovu na wakati mwingine kutoka kwa watu
waliookoka tena wenye nguvu kuliko wewe fahamu umebeba kusudi kubwa na maalumu,
fahamu wewe ni mwanafunzi wa Yesu kweli kweli wala usifadhaike, Neno la Mungu
linatufunulia siri hizo muhimu zinazopelekea wewe uchukiwe
Sababu za kuchukiwa bure.
Ni muhimu kufahamu kuwa chuki za
bure kwako zinafunua maana pana sana za kiwango cha kiroho ulichokifikia,
wakristo wengi leo wanaishi maisha ya kinafiki na sio wakweli kwa Mungu wala
kwa wanadamu, wengi wanaishi maisha ya kuigiza, wanaonekana kama watu maarufu
kwa nje, wakiwa na elimu kubwa, na vyeo vikubwa na wenye pesa na nguvu lakini
hawana nguvu za kiroho walishakufa zamani na wamepoteza kabisa kujiamini, na
kiroho wamefilisika, unapokuwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu na mfuasi wa kweli
wa Bwana Yesu katika karne hizi, watakupendea nini? Wakupende kwa lipi? Kama
wewe ni mwana wa Mungu tu hawakupendi, kama hujawahi kuwafanya lolote tu
wanakuchukia bure je wataweza kuwapenda adui wa kweli ambao Yesu amesema
wapendeni adui zenu? Waombeeni wanaowaudhi?, huoni kuwa agizo hilo ni la juu
zaidi? Wewe maisha yako yanawapa tabu, kama Yesu alivyowapa taabu mafarisayo na
masadukayo, kwa hiyo unapoona wanakuchukia bure ziko sababu nyingi na hapa na
ainanisha chache:-
1. Kwa sababu wewe ni nuru – Mtu wa Mungu
ni hivi unapoishi maisha ya nuruni, hapa maana yake wewe ni mkweli kwa Mungu,
unapokosea unatubu, na unasonga mbele na huna kinyongo na mtu na Mungu yuko
upande wako na anakutetea na kukupigania basi elewa hivi maisha yako ya nuruni
yanalifanya giza lidhalilike, hata kama husemi lolote lakini kuishi kwako kwa
haki hata bila ya maneno kunawafunua wenye dhambi, kwa hiyo watu wanaweza
kukuchukia sio kwa sababu ya kitu umefanya bali kwa sababu kuna kitu
unakiwakilisha
Yohana 3:19-21
“Na hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja
ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa
maovu. Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru,
matendo yake yasije yakakemewa. Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili
matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu.”
1Yohana 2:9-11
“Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia
ndugu yake, yumo gizani hata sasa. Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru,
wala ndani yake hamna kikwazo. Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza,
tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha
macho.”
2. Kwa sababu wewe si wa ulimwengu huu – Mtu
wa Mungu kama wewe ni wa Yesu Kristo hivi unadhani ulimwengu utakupenda? Ukupende
wewe nani? Ukupende wewe umeutendea nini? Ukupende wakati unafunua siri za
Mungu? Ukupende wakati hata Yesu Mwenyewe walimchukia bure wewe kama u
mwanafunzi wa Yesu utachukiwa tu, Yesu alisema kama mimi mwenyewe walinickukia
mwanafunzi hampiti Mwalimu wake yaani kila mwanafunzi wa kweli wa Yesu
atachukiwa tu, mpendwa chuki hiyo ni ushahidi wa wazi kwamba unamlingania Yesu
Kristo, kuchukiwa kwako sio ushahidi wa kushindwa kwako bali ni ushahidi ya
kuwa unamuishia Yesu Kristo na sio hivyo tu hata mafundisho yetu
yatakataliwa kama yalivyokataliwa ya Yesu
Yohana 15:18-20
“Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa
umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu,
ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali
mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia.
Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa
waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na
lenu.”
3. Kwa sababu wewe ni wa rohoni na wao ni wa
mwilini – Mtu wa Mungu ninataka nikuambie ya kwamba ulimwengu tulio nao una
makundi makuu mawili tu, haijalishi kundi hilo liko kanisani au nje lakini
kokote kwenye watu kuna aina mbili za watu watu wa rohoni na watu wa mwilini,
wale wa mwilini huwaudhi wale wa rohoni hii ni kanuni ya kibiblia iliyokuwako
zamani na inatenda kazi hata sasa, kama wewe ni mzaliwa wa kiroho utaudhiwa na
yule wa mwilini tu ona
Wagalatia 4:29 “Lakini kama vile siku zile yule aliyezaliwa kwa mwili
alivyomwudhi yule aliyezaliwa kwa Roho, ndivyo ilivyo na sasa.”
4. Kwa sababu ya kibali cha Mungu juu yako – Ndugu
yangu mpendwa kama Mungu amekupa kibali, Mungu amekupaka mafuta, Mungu ana
matumizi na wewe Mungu ana kusudi na wewe kibali cha Mungu juu yako kinawanyanyasa
kisaikolojia wale wasio na kibali hicho sasa wakuchekee? Wakutie moyo,
wakukubali wakati wanatamani kusikia umeharibikiwa, wanatamani hata ufe leo,
Daudi anasema wanaomchukia ni wengi kuliko nywele za kichwa chake, kaangalie
mashariki ya kati Israel inapendwa? Wanatamani waifutilie mbali wanatamani
waikatilie mbali ndivyo ulivyo na wewe mtu wa Mungu, kibali chako kinawasumbua
haijalishi hali ya nje kuwa wao wana nguvu lakini upako wako unawanyanyasa ndio
maana wanakuchukia bure
1Samuel 29:6-8
“Hata ikawa, walipokuwa wakienda, hapo Daudi
aliporudi baada ya kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka katika miji yote ya
Israeli, kwa kuimba na kucheza, ili kumlaki mfalme Sauli; wakatoka na matari,
na shangwe, na vinanda. Nao wale wanawake wakaitikiana wakicheza, wakasema,
Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake. Basi Sauli akaghadhibika
sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi
wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme? ”
Mwanzo 37:3-11
“Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote,
maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa
baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema
naye kwa amani. Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi
kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi
tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama,
na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake
wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi
kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto
nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na
tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake
na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je!
Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake
wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”
5. Kwa sababu ya wivu wenye uchungu – Mpendwa
wakati mwingine wewe unachukiwa bure kwa sababu ya wivu, ni wivu tu, kuna kitu
wakijilinganisha na wewe au na ninyi
wanakuona kabisa unakwenda mbele, wanakuona kabisa uko tofauti hata kama
kwa sasa huna kitu wanakuona na wanajua uweza wa Mungu juu yako na kile ambacho
Mungu amewekeza ndani yako wakupende kwa lipi wakati wamejaa wivu, wamejaa wivu
huu ni wivu wenye uchungu wivu wa kujilinganisha na wao na wakijilinganisha na
wewe wanaona kuna kitu cha ziada kwako wivu huu wa kujilinganisha unaitwa “phthonos” kwa kiingereza “is hatred rooted in comparison” Yesu alichukiwa kwa sababu alikuwa na
kitu cha ziada kuliko mafarisayo na masadukayo, kwa hiyo walikuwa na wivu
uliojaa chuki aina hii ya wivu wakati mwingine huwazungumzia watu vibaya na mambo mabaya ili wao waonekane wema yule
mwema aonekane mbaya.
Mathayo
27:17-18 “Basi walipokutanika, Pilato akawaambia,
Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana
alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda.”
Matendo 5:16-20
“Nayo makutano ya watu wa miji iliyoko kandokando
ya Yerusalemu wakakutanika, wakileta wagonjwa, nao walioudhiwa na pepo wachafu;
nao wote wakaponywa. Akaondoka Kuhani Mkuu na wote waliokuwa pamoja naye, (hao
ndio walio wa madhehebu ya Masadukayo), wamejaa wivu, wakawakamata mitume
wakawaweka ndani ya gereza; lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza
usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno
yote ya Uzima huu.”
Waebrania
12:14-15. “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu
wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia
sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na
kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”
6. Kwa sababu ya vita vya kiroho – Wakati
mwingine ile chuki inatokana na mapepo, kwa kadiri shetani alivyo adui yetu na
anavyotuchukia sisi ndivyo anavyowatumia mapepo na maajenti wake au wakristo
dhaifu kutumiwa na mapepo kutushambulia kwa hio wakati mwingine hii chuki kubwa
unayoiona dhidi yako mtu wa Mungu ni ya shetani akiwatumia watu wake au vyombo
vyake ili kupingana na kile ambacho Mungu amewekeza ndani yako
Waefeso 6:12 “Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama;
bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya
pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”
7. Kwa sababu ya kuishi maisha ya utauwa
- kila unapokusudia na kuthubutu
kuishi maisha ya tofauti na wengine maisha ya utakatifu na kuimarisha uhusiano
wako wa siri na Mungu watu wabaya na
wadanganyaji wanaendelea kuteseka na
watakucukia, wewe jaribu kuishi na kuigiza kila alichikifanya bwana Yesu, jitoe
kama yeye fuata mfano wake uone kama dunia itakupongeza hata kidogo! Utachukiwa, utateswa, utadhihakiwa, utakataliwa,
utaonekana huna faida, kwa sababu maisha ya kujitoa kwa Mungu yanapingana nay a
dunia hii, viwango vya kuishi kama Kristo vinawaudhi wahuni, vinawapa changamoto na kuwafanya wote walio
vufuvugu na wasiookoka wakose Amani, kwa
hiyo kuchukiwa ni sehemu ya gharama za uaminifu wako kwa Mungu au kumfuata Yesu
kwa uaminifu
2Timotheo
3:12-15 “Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya
utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa. lakini watu wabaya na wadanganyaji
wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika. Bali wewe ukae
katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina
nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko
matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo
katika Kristo Yesu.”
Jinsi ya kupokea na kuitikia chuki zao za bure
Ni jambo la kumshukuru Mungu
kwamba Mungu ametupa akili na ufahamu katika neno lake namna na jinsi ya
kushughulika na watu wanaotuchukia na njia hizo ni njia za kiroho, ambazo
kimsingi zitakufanya wewe kuzidi bali adui zako kupungua, njia hizi ukizitumia
zitakamilisha uwezo wako wa kiroho na kukunoa na kukufanya wewe uendelee kukua
kiroho zaidi na kumfanania baba wa mbinguni
1. Kunyamaza kimya – Moja ya njia ya
kiroho ambayo Yesu Kristo aliitumia pale waliokuwa wakimchukia walipokuwa
wakimsingizia mambo ya uongo ambayo hayana ukweli wowote bali kwa lengo la
kumchafua na kuharibu tu wito wake yeye alikaa kimya, alipoonewa aikaa kimya
alipoteswa na kutukanwa alikaa kimya, Neno kukaa kimya katika kiyunani ni “loidoreō”
kwa kiingereza ni “revile” ambalo maana yake ni “to insult verbally” hakutumia lugha
chafu kujibu alinyamaza kimya badala ya kujibu “silence over revenge” na
alijikabidhi kwa Mungu ahukumuye kwa haki, Mpendwa mwachie Mungu atajibu kwa
haki, Mungu huwapigania watu wakimya
1Petro 2:21-23
“Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye
aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.Yeye hakutenda
dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha
matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa
haki.”
Isaya 53:7 “Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa
chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo
Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake.”
Hesabu 12:1-9 “Kisha Miriamu na Haruni wakamnenea Musa kwa sababu ya
mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa; maana, alikuwa amemwoa mwanamke Mkushi.
Wakasema, Je! Ni kweli Bwana amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia? Bwana
akasikia maneno yao. Basi huyo mtu, huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya
wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi. Bwana akanena ghafula na Musa, na
Haruni na Miriamu, na kuwaambia, Tokeni nje ninyi watatu, mwende hemani mwa
kukutania. Basi hao watatu wakatoka nje. Bwana akashuka katika nguzo ya wingu
akasimama pale mlangoni pa Hema, akawaita Haruni na Miriamu, nao wakatoka nje
wote wawili. Kisha akawaambia,
Sikizeni basi maneno yangu; Akiwapo nabii kati yenu, Mimi, Bwana, nitajifunua
kwake katika maono, Nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi
wangu, Musa; Yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote; Kwake nitanena mdomo
kwa mdomo, Maana, waziwazi wala si kwa mafumbo; Na umbo la Bwana yeye ataliona.
Mbona basi ninyi hamkuogopa Kumnenea mtumishi wangu, huyo Musa? Hasira za Bwana
zikawaka juu yao; naye akaenda zake.”
2. Waombee wanao kuudhi – Maandiko
yanatufundisha kutoka mafundisho na maendo ya Bwana wetu Yesu na watakatifu
walioyutangulia kuwa kuna haja ya kuwaombea wale wanaotuchukia, tuwaonee huruma
na tuwapende kwa sababu wao ni dhaifu
Mathayo 5:43-45
“Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na,
Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni
wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye
huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.”
Luka 23:33-34 “Na walipofika mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, ndipo
walipomsulibisha yeye, na wale wahalifu, mmoja upande wa kuume, na mmoja upande
wa kushoto. Yesu akasema, Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo. Wakagawa
mavazi yake, wakipiga kura.”
3. Endelea kutenda mema - Lengo kubwa la shetani wakati mwingine
kukushambulia kupitia watu ni ili wewe uwe mtu mbaya, uone kuwa kila unapotenda
mema unalipwa mabaya kwa hiyo unaamua kufunga milango yako ya wema na kuwa
mbinafsi lakini neno la Mungu linatutaka tuendelee kuwa washindi kwa kutenda
mema, kadiri unavyoendelea kuwa mwema na kutenda haki wema wako utawanyamazisha
maadui zako na kila ubaya wanaokuzushia
Warumi 12:19 “Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya
Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena
Bwana.Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana
ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake. Usishindwe na ubaya,
bali uushinde ubaya kwa wema.”
4. Endelea kupiga kazi, endelea kumtumikia
Mungu – Wakati maadui zako wanapokushambulia wewe ongezea viwango vya
kumtumikia Mungu na kufanya kazi kwa bidii, kadiri unavyoendelea kumtumikia
Mungu kwa bidii Mungu ataendelea kukubariki na kazi unazozifanya zitatangaza
kile kitu Mungu ameweka ndani yako, na
kuudhihirishia ulimwengu kuwa yeye yuko na wewe, unapoendelea kumtumikia Mungu
kwa nguvu Baraka zako zinaendelea kuongezeka na adui zako wanaendelea kuwekwa
uchi neno la Mungu linasema adui zako watakuonyesha maungo yao, yaani uchi zao
zitafunuliwa, aibu zao zitawekwa wazi, utupu wao utahukumiwa na kazi
unazozifanya wataaibika na kazi yako itasema si biblia imesema kwa matunda yao
mtawatambua, je mti mbaya unaweza kuzaa matunda mema?
Kutoka 23:25-27 “Nanyi
mtamtumikia BWANA, Mungu wenu, naye atakibarikia chakula chako, na maji yako;
nami nitakuondolea ugonjwa kati yako. Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba, wala
aliye tasa, katika nchi yako; na hesabu ya siku zako nitaitimiza.Nitatuma
utisho wangu utangulie mbele yako, nami nitawafadhaisha watu wote
utakaowafikilia, nami nitawafanya hao adui zako wote wakuonyeshe maungo yao.”
Yohana 10:37-38 “Kama
sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa
hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu
ndani yangu, nami ni ndani ya Baba.”
Chuki kutoka kwa wapendwa na
watumishi wenzako haimaanishi kuwa Mungu amekuacha bali inakufundisha kuelewa
maswala ya kiroho, sio kuwa wakati wote watu watakuchukia kwa sababu wewe ni
muovu hapana bali kwa sababu wao ni dhaifu kiroho, Mungu anakufundisha uwezo wa
kuvumilia kabla ya kukuinua kukubariki na kukutumia, Mungu anakufundisha kuwa
kama Yeye, wewe hujasahaulika, wewe hujashindwa wewe uko sawa na Daudi, uko
sawa na Yusufu unafafanana na Yesu na ndio maana unachukiwa bila ya sababu za
halali, wewe utakuwa kiroho vizuri zaidi, ukiyamudu hayo machungu yote ujue
wazi kuwa thawabu yako ni kubwa sana mbinguni
Mathayo 5:11-12 “Heri ninyi
watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili
yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa
maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu.”
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni