Jumapili, 4 Januari 2026

Kuzingirwa kwa ukigo usioonekana!

 

Ayubu 1:7-9 “Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. Kisha Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu. Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha Bwana bure? Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.”



Utangulizi:

Leo tunalenga kujifunza au kujikumbusha juu ya ulinzi wa Mungu usioonekana kwa watu wanaomwamini Mungu, katika kifungu cha maandiko ya msingi tunafunuliwa moja ya jambo la msingi lililoko katika ulimwengu wa roho ambalo macho yetu hayawezi kuona na huu ni ulinzi wa Mungu kupitia Malaika, Ukuta wa moto, Ukuta wa shaba, na wigo au ukigo usioonekana ambao kimsingi unawekwa na Mungu mwenyewe kwa watu wake, siri hii ya ukigo wa ulinzi uliowekwa na Mungu inafunuliwa na Shetani mwenyewe ambaye anakiri kuwa alikuwa hawezi kumshambulia Ayubu kwa sababu Mungu alikuwa amemuwekea ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo, ulinzi huu wa Mungu ni ulinzi usioonekana, ni ulinzi wa kiroho unaotokana na uhusiano wetu na Mungu na ni ulinzi unaowekwa na Mungu mwenyewe katika ulimwenguwa roho.

Zekaria 2:5 “Kwa maana mimi, asema Bwana, nitakuwa ukuta wa moto kuuzunguka pande zote, nami nitakuwa huo utukufu ndani yake.”

Yeremia 15:20-21 “Nami nitakufanya kuwa kama ukuta wa boma la shaba juu ya watu hawa; nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, ili nikuokoe, na kukuponya, asema Bwana. Nami nitakuokoa na mkono wa watu wabaya, nami nitakukomboa katika mkono wao wenye kutisha.”

Kwa msingi huo leo, tutachukua muda kujifunza somo hili Kuzingirwa kwa ukigo usioonekana kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya ukigo usioonekana.

·         Kuzingirwa kwa ukigo usioonekana.

·         Jinsi ya kuzingirwa na ukigo usioonekana.


Maana ya ukigo usioonekana.

Siri ya kwamba watu wanaomcha Mungu wanazingirwa na ukigo pande zote inawekwa wazi kwa mara ya kwanza na Shetani mwenyewe wakati wa mazungumzo yake na Mungu katika ulimwengu wa roho kuhusu Mtumishi wa Mungu Ayubu aliyekuwako huku Duniani, Shetani katika mazungumzo yake na Mungu anaonekana kumjua vema Ayubu, kwa sababu hakuuliza ni Ayubu yupi? Na tena inaonekana wazi alikuwa anafahamu Ayubu anaishi wapi? Alikuwa anamfahamu Ayubu vizuri nje ndani na bila shaka alikuwa anafahamu kuwa Ayubu ni Mtumishi wa Mungu ambaye alikuwa mwaminifu kama maandiko yasemavyo, habari hii inatufunulia kwa kina kuwa kuna uwezekano wasaidizi wa shetani yaani mapepo na wenye mamlaka na wakuu wa giza kwa namna Fulani wamewahi kuwa na mpango mkakati wa kumshambulia Ayubu na huenda walishindwa, na walitoa taarifa kwa bwana wao kuwa Yule Bwana hawezekani analindwa na nguvu za Mungu, na inawezekana hatimaye hata Shetani mwenyewe alijaribu kumtembelea Ayubu na kujaribu kutaka kusababisha uharibifu lakini mbinu zilishindikana, ilibainika wazi kuwa Ayubu anazingirwa na ulinzi maalumu wa Mungu, na kila anachikifanya Mungu amekibariki.       

Ayubu 1:7-9 “Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. Kisha Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu. Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha Bwana bure? Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.”

Tunafunuliwa hapo kuwa ulinzi huu wa Mungu ambao hapo unatajwa kama UKIGO sio ulinzi unaoweza kuonekana kwa macho ya nyama, ni ulinzi maalumu unaotokana na uhusiano bora kati ya Ayubu na Mungu, inawezekana Ayubu hakuwa anaujua, wala hakuna mtu aliyeweza kuuona kwa macho lakini Shetani katika ulimwengu wa roho alifahamu kuwa Ayubu anazingirwa na ukigo pande zote, ulinzi huu wa Mungu hautokani na juhudi zetu wala haki yetu kwa hiyo sio sisi tunaoweza kuuweka ulinzi huo bali Bwana mwenyewe anawalinda watu wake, hii ni zawadi ya kila aaminiye.

1Petro 1:3-5 “Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa rehema zake nyingi alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; tupate na urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu. Nanyi mnalindwa na nguvu za Mungu kwa njia ya imani hata mpate wokovu ulio tayari kufunuliwa wakati wa mwisho.”

Sasa ulinzi huo maalumu wa Mungu au nguvu za Mungu zinatotulinda kwa mujibu wa Shetani ameziita ukigo, UKIGO hasa ni nini? Neno ukigo linalotumika katika maandiko hapo katika Lugha ya Kiebrania linasomeka neno “sûk” au neno ώuk” ambalo linatamkwa sook kwa Kiingereza “Hedge” ambalo maana yake ni Ukuta au Ukingo maalumu unaomzingira mtu kwa kusudi la kuweka mipaka ili asizuriwe, it’s a way of protecting oneself against quality loss of financial, circumstances, health garden, properties, flocks etc. ni njia ya kulinda ubora wa mtu, uchumi, mazingira, afya, bustani, mali, na mifugo ili isipatwe madhara  hii ni maana ya kawaida ya UKIGO lakini Ukigo aliouona Shetani katika maisha ya Ayubu ulikuwa ni ukigo wa kiroho, yaani ukigo usioonekana “An unseen hedge” huu sasa ukigo usiionekana ni ukigo wa kiroho unaowekwa na Mungu kwa mtu aliyeokoka kumuwezesha mtu huyo kuwa na ulinzi wa Mungu kwa habari ya maisha yake na mali zake, uchumi wake, afya yake, watoto wake, mifugo yake mashamba yake na kadhalika, An unseen hedge is a spiritual barrier of divine protection placed by God around belivers and their possessions. Kwa hiyo mtu anayemcha Mungu analindwa na Mungu katika ulimwengu wa roho kiasi ambacho shetani analalamika kuwa hawezi kusababisha uharibifu katika jambo lolote kwa sababu Mungu anakulinda.

Kuzingirwa kwa ukigo usioonekana.

Kwa hiyo sasa tunapata ufahamu ya kuwa kila mtu aliyeokoka, kila amwaminiye Mungu, kila aliyeamini, analindwa na Mungu katika ulimwengu wa roho bila yeye mwenyewe kutambua na unaweza kulitambua hilo endapo utaruhusiwa kuona kwa macho ya rohoni, Neno la Mungu linatufunulia hivyo kwamba kila mtu aliyeokoka anazingirwa na UKIGO usioonekana, ulinzi huu hauonekani kwa macho lakini ni halisi, ni ulinzi wa kiroho na hauwezi kuonekana kwa macho ya nyama, ni ulinzi unaowekwa na Mungu mwenyewe na sio kwa jitihada za kibinadamu, ulinzi huu unazunguka Maisha yako, uhai wako, afya yako, familia yako, mali zako, watu wako, mazingira yako, Tunaweza kujifunza kutokana na Nabii Elisha nyakati za agano la kale namna na jinsi alivyokuwa na utambuzi ya kuwa uko ulinzi katika ulimwengu usioonekana kwa macho ambao unawazingira watu wa Mungu pande zote ona

2Wafalme 6:15-17 “Hata asubuhi na mapema mtumishi wake yule mtu wa Mungu alipoondoka, na kwenda nje, kumbe! Pana jeshi la watu, na farasi na magari, wameuzingira mji ule. Mtumishi wake akamwambia, Ole wetu! Bwana wangu, tufanyeje? Akamjibu, Usiogope; maana walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao. Elisha akaomba, akasema, Ee Bwana, nakusihi, mfumbue macho yake, apate kuona. Bwana akamfumbua macho yule mtumishi; naye akaona; na tazama, kile kilima kilikuwa kimejaa farasi na magari ya moto yaliyomzunguka Elisha pande zote.”

Unaona hapo tunaona kuwa Elisha alikuwa na ufahamu kuwa analindwa na jeshi kubwa sana la malaika wasioonekana kwa macho ya nyama lakini alipomuombea mtumishi wake naye alipewa uwezo wa kuona na kugundua kuwa kulikuwa na magari ya farasi ya moto yaliyowazunguka pande zote, huu ulikuwa ukigo wa kiroho unaowazingira watumishi wa Mungu pande zote, mtu mmoja alisema ikiwa Elisha wa agano la kale alilindwa kiasi hiki ni wazi kuwa waamini katika Kristo nyakati hizi za agano jipya wanalindwa zaidi na nguvu za Mungu na ukigo usioonekana  katika ulimwengu wa roho, kuliko Elisha ambaye Yesu alikuwa hajamfia Msalabani, ikieleza namna watu wa Mungu wanavyolindwa Biblia iko wazi kwamba kila aliyemwamini Yesu analindwa iwe anajua au hajui

Marko 16:15-18 “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa. Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.”

Awaye yote ambaye anamtegemea Mungu na kumcha yeye na kuendelea kukaa katika uwepo wa Mungu kimsingi anajiweka katika ulinzi wa Mungu, kwa sababu hiyo kimsingi kila mtu anayemtumainia Mungu anajiweka katika kuzingirwa kwa ukigo usioonekana, inaweza kuwa malaika, ama ukuta wa moto au ukuta wa shaba na kadhalika na ni Mungu ndiye anayetulinda kupiria serikali yake ya mbinguni, ile mamlaka ya kiungu inahusika na ulinzi wetu

Zaburi 91:1-11 “Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu Atakaa katika uvuli wake Mwenyezi. Nitasema, Bwana ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini. Maana Yeye atakuokoa na mtego wa mwindaji, Na katika tauni iharibuyo. Kwa manyoya yake atakufunika, Chini ya mbawa zake utapata kimbilio; Uaminifu wake ni ngao na kigao. Hutaogopa hofu ya usiku, Wala mshale urukao mchana, Wala tauni ipitayo gizani, Wala uele uharibuo adhuhuri, Ijapo watu elfu waanguka ubavuni pako. Naam, kumi elfu mkono wako wa kuume! Hata hivyo hautakukaribia wewe. Ila kwa macho yako utatazama, Na kuyaona malipo ya wasio haki. Kwa kuwa Wewe Bwana ndiwe kimbilio langu; Umemfanya Aliye juu kuwa makao yako. Mabaya hayatakupata wewe, Wala tauni haitaikaribia hema yako. Kwa kuwa atakuagizia malaika zake Wakulinde katika njia zako zote.”

Daniel 6:18-22 “Kisha mfalme akaenda nyumbani kwake, akakesha usiku kucha, akafunga; na vinanda havikuletwa mbele yake; na usingizi wake ukampaa. Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba. Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno.”

Kwa msingi huo kupitia maandiko haya na ufunuo wa neno la Mungu tunajifunza hapa kuwa mtu anayemtegemea na kumtumainia Mungu anazingirwa kwa ukigo usioonekana katika ulimwengu wa roho ni pale tu unapokuwa na macho ya rohoni na unapolielewa neno la Mungu ndipo unapoweza kuelewa ya kuwa katika ulimwengu wa roho tunao ukigo usioonekana yaani tunao ulinzi usioonekana kwa macho.                             

Jinsi ya kuzingirwa na ukigo usioonekana.

Tunahakikishiwa kuwa ukigo usioonekana ni Dhahiri kwa watu wa Mungu, na ni wa muhimu, lakini swali kubwa ni kuwa tunawezaje kuzingirwa na ukigo huu usiioonekana je tunaweza kuomba ulinzi wa Mungu? Maandiko yanaonyesha wazi kuwa sio dhambi kuomba ulinzi wa Mungu, japokuwa Mungu mwenyewe huwa anawalinda watu wake kwa hiyari yake na mapenzi yake, Shetani alipolaumu kuhusu ulinzi wa Ayubu alisema wewe umemzingira kwa ukigo pande zote maana yake ilikuwa ni Mungu kwa hiyari yake na kwa mapenzi yake alimlinda Ayubu

Ayubu 1:7-10 “Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. Kisha Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu. Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha Bwana bure? Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.”

Hata hivyo ingawa ulinzi wa Mungu ni tukio la hiyari linalofanywa na Mungu mwenyewe maandiko hayakatazi kuomba ulinzi wa Mungu, viko viashiria kadhaa wa kadha vya kimaandiko vinavyotuthibitishia kuwa tunaweza kuomba ulinzi wa Mungu na huu ni ukweli usioweza kupingika, mfano katika sala ya Bwana iliyofundishwa na Bwana Yesu kuna sehemu ya kujiombea ulinzi, lakini sio hivyo tu Yesu katika maombi yake yeye mwenyewe alituombea ulinzi

Mathayo 6:13 “Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. [Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.]”   

Yohana 17:14-16 “Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.”

Ezra 8:21-23 “Ndipo nikaamuru kufunga, hapo penye mto Ahava, ili tupate kujinyenyekeza mbele za Mungu, na kutafuta kwake njia iliyonyoka, kwa ajili yetu sisi wenyewe, na kwa ajili ya watoto wetu, na kwa mali yetu yote. Maana naliona haya kumwomba mfalme kikosi cha askari na wapanda farasi, ili kutusaidia juu ya adui njiani; kwa maana tulikuwa tumesema na mfalme, tukinena, Mkono wa Mungu u juu ya watu wote wamtafutao, kuwatendea mema; bali uweza wake na ghadhabu yake ni kinyume cha wote wamwachao. Basi tukafunga, tukamsihi Mungu wetu kwa ajili ya hayo; naye akatutakabali.”

Kwa hiyo tunajifunza ya kwamba mojawapo ya njia ya kuzingirwa na ukigo usioonekana ni pamoja na kuomba ulinzi wa Mungu kwaajili yetu japo kuwa swala la kulindwa na Mungu liko katika mikono yake, na sisi tu mali yake  

Njia nyingine ya kukaribisha ulinzi wa Mungu au kuzingirwa na ukigo usioonekana katika maisha yetu ni kuwa na Maisha ya kumcha Mungu, Neno la Mungu linathuthibitishia ya kuwa Mungu huwazingira kwa ngao wale wanaotembea katika haki yaani wale wanaomcha Mungu.

Zaburi 5:11-12 “Nao wote wanaokukimbilia watafurahi; Watapiga daima kelele za furaha. Kwa kuwa Wewe unawahifadhi, Walipendao jina lako watakufurahia. Kwa maana Wewe utambariki mwenye haki; Bwana, utamzungushia radhi kama ngao.”

Zaburi 34:7-9 “Malaika wa Bwana hufanya kituo, Akiwazungukia wamchao na kuwaokoa. Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini. Mcheni Bwana, enyi watakatifu wake, Yaani, wamchao hawahitaji kitu.”

Ulinzi wa Mungu unathibitika wazi kwa wale wanaomcha Mungu, ni muhimu kufahamu kuwa ahadi za Mungu zinategemea (Conditional) pande zote mbili, Mungu anatoa ahadi ya kutupigania na kutulinda lakini ni wajibu wetu kumtii, kama utaharibu ukigo wako wewe mwenyewe utauharibu kwa kutokuwa mwaminifu kwa Mungu na hapo ni lazima utakula mkong’oto, hapa nisikupake mafuta kwa mgongo wa chupa niweke wazi kuwa kama ukimkosea Mungu huna budi kutubu na kurekebisha kwa haraka usitegemee ulinzi wa Mungu wakati wa kuasi kinyume na mapenzi yake ndio maana siku hizi hata walokole wanarogwa! Wanarogwaje kwa sababu wanaishi maisha ya kawaida na kuendelea katika dhambi huku wakidhani Mungu anatendelea kuwa mlinzi kwao tuambiane ukweli usimpe ibilisi nafasi, Mungu alimuhakikishia Joshua ushindi yaani maana yake pamoja na ulinzi lakini sharti ilikuwa lazima atende sawasawa  na yote yaliyoandika katika kitabu cha torati ya Musa vinginevyo unapigwa ona:-

Yoshua 1:5-7 “Hapatakuwa mtu ye yote atakayeweza kusimama mbele yako siku zote za maisha yako; kama nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo nitakavyokuwa pamoja na wewe; sitakupungukia wala sitakuacha.Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana ni wewe utakayewarithisha watu hawa nchi hii niliyowaapia baba zao ya kwamba nitawapa. Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako.”

Yoshua 7:1-12 “Lakini wana wa Israeli walifanya dhambi katika kitu kilichowekwa wakfu; maana Akani, mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila ya Yuda, alitwaa baadhi ya vitu vilivyowekwa wakfu; hasira ya Bwana ikawaka juu ya wana wa Israeli. Kisha Yoshua akatuma watu kutoka Yeriko mpaka mji wa Ai, ulio karibu na Bethaveni, upande wa mashariki wa Betheli, akawaambia, akisema, Pandeni juu mkaipeleleze nchi, basi wakapanda juu wakaupeleleza Ai. Wakarejea kwa Yoshua wakamwambia, Wasiende watu wote, ila waende watu kama elfu mbili, tatu, wakaupige Ai; usiwataabishe watu wote kwa kuwaendesha huko; maana watu hao ni wachache tu. Basi watu wakaenda huko wapata elfu tatu tu; nao wakakimbia mbele ya watu wa Ai. Watu wa Ai wakawapiga watu kama thelathini na sita; wakawafuatia kutoka mbele ya mlango mpaka Shebarimu, wakawapiga huko kwenye matelemko; mioyo ya watu ikayeyuka, ikawa kama maji. Yoshua akararua mavazi yake, akaanguka kifudifudi mbele ya sanduku la Bwana hata jioni, yeye na wazee wa Israeli; wakatia mavumbi vichwani mwao. Yoshua akasema, Ee Bwana MUNGU, kwa nini umewavusha watu hawa mto wa Yordani, ili kututia katika mikono ya Waamori, na kutuangamiza? Laiti tungelikuwa radhi kukaa ng'ambo ya Yordani Ee Bwana, niseme nini baada ya Israeli kuwapa visogo adui zao? Maana Wakanaani na wenyeji wote wa nchi hii watasikia habari hii, nao watatuzingira, na kulifuta jina letu katika nchi. Nawe utafanya nini kwa ajili ya jina lako kuu? Bwana akamwambia Yoshua, Haya! Inuka, mbona umeanguka kifudifudi hivi? Israeli wamefanya dhambi, naam, wamelivunja agano langu nililowaagiza; naam, wametwaa baadhi ya vitu vilivyowekwa wakfu; tena wameiba, tena wameficha na kuvitia pamoja na vitu vyao wenyewe. Ndiposa wana wa Israeli hawawezi kusimama mbele ya adui zao; wakawapa visogo adui zao, kwa sababu wamelaaniwa; mimi sitakuwa pamoja nanyi tena, msipokiharibu kitu kile mlicho nacho kilichowekwa wakfu.”

Kumbukumbu 1:41-45 “Ndipo mkanijibu, mkaniambia, Sisi tumefanya dhambi juu ya Bwana, tutakwea kupigana kwa mfano wa yote tuliyoamriwa na Bwana. Mkajifunga kila mtu silaha zake za vita, mkafanya wepesi kukwea mlimani. Bwana akaniambia, Uwaambie, Msiende, wala msipigane; kwani mimi si kati yenu; msije mkapigwa mbele ya adui zenu. Basi niliwaambia, msinisikize, bali mliasi amri ya Bwana, mkajikinai, na kukwea mlimani. Na Waamori waliokuwa wakikaa katika mlima huo, waliwatokea juu yenu, wakawafukuza, kama wafukuzwao na nyuki, wakawapomoshea Seiri mpaka Horma. Mkarudi mkalia mbele za Bwana; Bwana asiisikize sauti yenu, wala hakuelekeza masikio yake kwenu.”             

Neno la Mungu linatufundisha wazi hapo kuwa ulinzi wa Mungu ni Dhahiri kwa wale wamchao, lakini kama tukimuasi tunakuwa tumeharibu ukigo unaotuzingira na kwa sababu hiyo ni rahisi kushindwa na kushambuliwa na inaweza kuwa aibu kwetu, kama watu wanamtaka Mungu basi wamtake jumla jumla na sio nusu nusu, Neno la Mungu linasema yeye abomoaye boma nyoka watamuuma

Muhubiri 10:8-9 “Mwenye kuchimba shimo atatumbukia ndani yake; Na yeye abomoaye boma, nyoka atamwuma. Mwenye kuchonga mawe ataumizwa kwayo; Naye apasuaye miti huona hatari katika hiyo.”    

Kama hujaokoka na unahitaji ulinzi wa Mungu basi ni vema ukampokea Yesu,awe bwana na mwokozi wa maisha yako, Damu ya Yesu ni ulinzi na usalama wa maisha yako na Yule muharibifu anapoona alama ya damu yeye atapita juu yako na hataleta madhara katika nyumba yako kwa sababu umeiamini ile kazi iliyofanywa naye pale Msalabani.

Kutoka 12:12-13 “Maana nitapita kati ya nchi ya Misri usiku huo, nami nitawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri, wa mwanadamu na wa mnyama; nami nitafanya hukumu juu ya miungu yote ya Misri; Mimi ndimi BWANA. Na ile damu itakuwa ishara kwenu katika zile nyumba mtakazokuwamo; nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu, lisiwapate pigo lo lote likawaharibu, nitakapoipiga nchi ya Misri.”

Kuzingirwa na ukigo usioonekana ni swala la uhakika kwa wana wa Mungu, Nanyi mnalindwa na nguvu za Mungu, ukweli tunaweza tusione kwa macho kile kinachoendelea katika ulimwengu wa roho lakini neno la Mungu linatuhibitishia kuwa tunalindwa, malaika wapo, ukuta wa moto uko unatuzunguka na mbingu zinatambua uwepo wetu na mahitaji yetu na wema wake utatuzunguka

Zakarika 2:5 “Kwa maana mimi, asema Bwana, nitakuwa ukuta wa moto kuuzunguka pande zote, nami nitakuwa huo utukufu ndani yake.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima        

Hakuna maoni: