Jumapili, 5 Aprili 2026

Kupandishwa toka shimo la uharibifu!


Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kwamba tuwapo duniani ziko nyakati ambazo tunaweza kupita katika mazingira ya hatari sana, mazingira ya kutisha ambayo kimsingi yanaweza kukuweka katika hali ya kukosa msaada wala hata kusikilizwa kwa sauti yako na ukakosa msaada ni nyakati ambazo unaweza kuchagua kifo kuliko uhai, wakati ambao unaweza kuchagua kukata tamaa kuliko kujipa moyo, nyakati ambazo umezama katika giza na huoni hata dalili ya nuru unachokiona mbele yako ni dalili za uharibifu yaani mauti, hali hiyo inaweza kuwa misiba, inaweza kuwa upotevu wa mali, inaweza kuwa kutapeliwa fedha nyingi, inaweza kuwa changamoto za kiafya inaweza kuwa mashambulizi kutoka kwa maadui, watu wanaokuchukia, inaweza kuwa magonjwa makubwa yasiyo na tiba na kadhalika hayo yanapokushambulia katika lugha ya kibiblia linaitwa shimo la uharibifu, katika nyakati hizo hata Mungu huonekana kuwa kimya unaweza ukamuita na ukasubiri na bado akakunyamazia, kipindi hicho huwa ni kipindi kigumu sana kwa mwanadamu na waandishi wa mashairi ya kibiblia wamekiita shimo la uharibifu! Je umewahi kupita au je unapita katika shimo la uharibifu? wako watu walipita

Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana

Katika maandiko yetu ya msingi, tunajifunza ushudua wa Daudi mwandishi wa zaburi hii akimshukuru Mungu baada ya kumuokoa na kumtoa katika shimo la uharibifu, lenye matope na uterezi, kuimarisha hatua zake na kutia wimbo mpya kinywani mwake, Pamoja na kuwa zaburi hii ilimuhusu Daudi, inamuhusu vile vile Yesu Kristo ambaye aliteswa akafa na kuzikwa na kufufuka siku ya tatu akitolewa katika shimo la uharibifu (kaburi), sio hivyo tu zaburi hii inamuhakikishia kila mmoja wetu kuwa Mungu atakutoa katika shimo la uharibifu unalolipitia, tutajifunza somo hili Akanipandisha toka shimo la uharibifu!  kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo;-


·         Maana ya shimo la uharibifu

·         Kupandishwa toka shimo la uharibifu

·         Mamlaka ya kupandishwa toka shimoni  


Maana ya shimo la uharibifu.

Shimo la uharibifu katika lugha ya Kiebrania linaitwa “Shâ’ôn bôr” kwa kiingereza ni “Horrible pit” au  “Destruction bore”, au “tumult Pit” au “Sheol” kuzimu au kaburi au hatari ya kifo, ambalo maana yake ni shimo lenye kutisha, au shimo la uharibifu, au shimo la mateso, lenye kelele, lenye kuchanganya, Mwandishi anajaribu kusimulia hali ngumu ambayo Mungu anaweza kuiacha mtu wake akaipitia ambayo kimsingi, ni hali ya shinikizo kubwa sana la mateso ambayo kibinadamu ni vigumu kuyaepuka ni shimo ambalo unanasa na huwezi kujiokoa shimo la utelezi, shimo hili ni kama kuingizwa kaburini ukiwa umekufa ambako sio rahisi kutoka kwa nguvu zako na akili zako za kibinadamu mpaka kwa msaada wa Mungu, Ni Mungu peke yake ndiye anayeweza kukutoa huko!

Zaburi 28:1-2 “Ee Bwana, nitakuita Wewe, mwamba wangu, Usiwe kwangu kama kiziwi. Nisije nikafanana nao washukao SHIMONI, Ikiwa umeninyamalia. Uisikie sauti ya dua yangu nikuombapo, Nikipainulia patakatifu pako mikono yangu.”

Zaburi 88:3-6 “Maana nafsi yangu imeshiba taabu, Na uhai wangu umekaribia kuzimu. Nimehesabiwa pamoja nao washukao SHIMONI; Nimekuwa kama mtu asiye na msaada. Miongoni mwao waliokufa nimetupwa, Kama waliouawa walalao makaburini. Hao ambao Wewe huwakumbuki tena, Wametengwa mbali na mkono wako. Mimi umenilaza katika shimo la chini, Katika mahali penye giza vilindini.”

Zaburi 30:1-3 “Ee Bwana, nitakutukuza kwa maana umeniinua, Wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu. Ee Bwana, Mungu wangu, Nalikulilia ukaniponya. Umeniinua nafsi yangu, Ee Bwana, kutoka KUZIMU. Umenihuisha na kunitoa Miongoni mwao washukao SHIMONI.”

Isaya 38:17-18 “Tazama; nalikuwa na uchungu mwingi kwa ajili ya amani yangu; Lakini kwa kunipenda umeniokoa na SHIMO LA UHARIBIFU; Kwa maana umezitupa dhambi zangu zote nyuma yako. Kwa kuwa KUZIMU hakuwezi kukusifu; mauti haiwezi kukuadhimisha; Wale washukao SHIMONI hawawezi kuitarajia kweli yako.”

Unaona neno shimo katika maandiko au shimo la uharibifu linazungumzia hali ya hatari, hali ya mateso makali, kukata tamaa, hali ya kushindwa na kukandamizwa ni shida na taabu ambazo zinaelekea kelele za mauti na wakati huohuo huwezi kujiokoa au kujitoa katika shimo hilo kwa kuwa ni shimo la matope, hali hii inaweza kufanana kabisa na hali ya mateso aliyoyapitia Bwana wetu Yesu Kristo na kufa kwake msalabani ambapo hakupata msaada wowote wakati wa mateso, kwa hiyo wakati mwingine tunapitia hali kama hiyo ambayo kimsingi tunaweza kufikia kukata tamaa, shimo hili linaweza kuwa shimo la madeni, linaweza kuwa shimo la umasikini, linaweza kuwa shimo la magonjwa, linaweza kuwa shimo la msongo wa mawazo, linaweza kuwa shimo la dhambi, linaweza kuwa shimo la mauti, linaweza kuwa shimo la kushindwa kiroho, linaweza kuwa la matatizo

Kupandishwa toka shimo la uharibifu.

Tunapoadhimisha msimu huu wa pasaka na kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo kutoka kwa wafu, tunajikumbusha vile vile kazi ya Mungu ya kuwatoa wanadamu kutoka katika mashimo ya uharibifu mashimo ambayo huwezi kujitoa bila nguvu ya ufufuo, kukutoa katika shimo lako, Yesu alipokufa aliwekwa shimoni na adui zake walililinda na kaburi ili kuhakikisha ya kuwa hatoki humo, Yesu aliingia katika shimo la mateso, alikataliwa na watu jamii nzima ilizomewa jamii ikisema asulubiwe asulubiwe, alipigwa mijeledi, na kuwambwa msalabani akiwa uchi na kufa msalabani na kuzikwa mahali pa giza nene, kaburi lake na mateso yake yalikuwa ni alama ya aibu, kifo, na kushindwa katika macho ya wanadamu, wanadamu wakikuchukia ni kawaida yao kukuweka shimoni

-          Walimuweka Yusufu katika shimo la matope Mwanzo 37:18-24 “Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake. Reubeni akasikia akamwokoa katika mikono yao, akasema, Tusimwue. Reubeni akawaambia, Msimwage damu; mtupeni katika birika hii iliyopo nyikani, wala msimguse; ili apate kumwokoa katika mikono yao, akamrudishe kwa baba yake. Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji.”

 

-          Walimuweka Yeremia katika shimo la matope Yeremia 38:6-9 “Basi wakamtwaa Yeremia, wakamtupa katika shimo la Malkiya, mwana wa mfalme, lililo katika uwanda wa walinzi; wakamshusha kwa kamba. Na mle shimoni hamkuwa na maji, ila matope tu; naye Yeremia akazama katika matope hayo. Basi, Ebedmeleki, Mkushi, towashi, aliyekuwa katika nyumba ya mfalme, aliposikia kama wamemtia Yeremia shimoni; na wakati huo mfalme alikuwa amekaa katika lango la Benyamini; Ebedmeleki akatoka nyumbani mwa mfalme, akamwambia mfalme, akisema,Ee bwana wangu, mfalme, watu hawa wametenda mabaya katika mambo yote waliyomtenda Yeremia, nabii, ambaye wamemtupa shimoni; naye hakosi atakufa pale alipo, kwa sababu ya njaa; kwa kuwa hapana mkate kabisa katika mji.”         

 

-          Walimtupa Daniel katika shimo lenye simba wakali Daniel 6:16-17 “Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danieli.”

 

Wote waliowekwa shimoni hapo juu walichukiwa, walikataliwa walifanyiwa hila na njama ili ikiwezekana waweze kumalizwa na wasitoke lakini Mungu alikuwa pamoja nao, Daudi pia aliishi mashimoni yaani katika mapango  akitafutwa kuuawa, Yesu Kristo aliwekwa kwenye shimo yaani kaburi, na liliwekwa Muhuri kama la Daniel wote walikuwa wanakabiliwa na mauti, walikandamizwa, walionewa, waliteswa Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa ni Mungu mwenyewe ndiye aliyewatoa kutoka katika shimo la uharibifu kama mwandishi wa Zaburi anavyosema

Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana

Wakati wa shida yako unapopita katika shimo la uharibifu unaweza kuliitia jina la Bwana naye atakuokoa kutoka shimoni uwezo huo na mamlaka hiyo ya kumtoa mtu kutoka shimoni iko mikononi mwa Mungu, Mwandishi wa zaburi alikuwa katika wakati mgumu aliliitia jina la Bwana na Mungu akikuwa kimya kwa Muda lakini baadae alimchungulia na kisha akamtoa akaimarisha hatua zake, akamuweka juu ya mwamba na kisha akatia wimbo mpya, ni maombi yangu pasaka hii iwe ushuhuda  

Ayubu 33:23-24 “Kwamba akiwapo malaika pamoja naye, Mkalimani, mmoja katika elfu, Ili kumwonyesha binadamu hayo yampasayo; Ndipo amwoneapo rehema, na kusema, Mwokoe asishuke SHIMONI; Mimi nimeuona ukombozi.”

Ayubu 33:28-30 “Yeye ameikomboa nafsi yangu isiende SHIMONI, Na uhai wangu utautazama mwanga. Tazama, hayo yote ni Mungu anayeyafanya, Mara mbili, naam, hata mara tatu, kwa mtu, Ili kurudisha roho yake itoke SHIMONI, Ili atiwe mwanga kwa mwanga wa walio hai.

Yona 2:5-6 “Maji yalinizunguka, hata nafsini mwangu; Vilindi vilinizunguka; Mwani ulikizinga kichwa changu; Nalishuka hata pande za chini za milima; Hiyo nchi na mapingo yake yalinifunga hata milele; Lakini umeipandisha nafsi yangu kutoka SHIMONI, Ee Bwana, Mungu wangu,”

Zaburi 103:3-4 “Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, Aukomboa uhai wako na KABURI, Akutia taji ya fadhili na rehema,”          

Mamlaka ya kupandishwa toka shimoni 

Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana

Mwandishi wa Zaburi hii yaani Daudi anaonyesha ya kuwa hakuna mwingine anayeweza kumtoa mtu katika shimo la uharibifu isipokuwa Bwana mwenyewe kwa hiyo anasema alimgoja Bwana kwa uvumilivu yaani kwa Saburi, ukombozi wetu unaanza pale tunapoliitia jina la Bwana na kuvumilia yeye ndiye mwenye mamlaka ya kukuchomoa kutoka katika shimo lenye matope, lenye utelezi, yeye anayo mamlaka ya kukutoa katika minyororo, na mazingira yoyote magumu na kubadilisha yale yasiyowezekana na yakawezekana, Hakuna shimo lolote ambalo linaweza kuwa refu kuliko mkono wa Mungu, Mungu anapokutoa hukuweka juu ya mwamba na kuimarisha hatua zako na kukupa ushuhuda mpya wimbo mpya na kila mtu atajifunza kutoka kwako na watu watamtumaini na kumtegemea Mungu, shimo lolote la kushindwa, shimo la dhambi, shimo la mauti, shimo la kukata tamaa, shimo mateso, shimo la madeni, shimo la uharibifu, shimo la aibu, na changamoto.

Katika jina la Yesu Kristo, mwenye mamlaka ya mauti na uzima, mwenye ufunguo wa Daudi naamuru kila mmoja aliyewekwa katika shimo la uharibifu shimo hilo likuachie haraka, shimo la mapepo, shimo la uchawi, shimo la madeni, shimo la kukataliwa, shimo la kusalitiwa, shimo la kuonewa, shimo  la mafarakano, shimo la talaka, shimo na uharibifu katika ndoa, shimo la uharibifu katika familia,  shimo la utumwa wadhambi, shimo la magonjwa sugu, shimo la uonevu naamuru katika jina la Yesu Kristo aliyefufuka kutoka kwa wafu, kila shimo lililokumeza likutapike likuachie katika jina la Yesu Kristo wa Nazareth aliye hai, Bwana akuchomoe katika shimo la matope kama Mchungaji anavyomchomoa Kondoo wake katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai Amen!

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Hakuna maoni: