Jumapili, 26 Aprili 2026

Walinisukuma sana ili nianguke!

 


Zaburi 118:10-14. “Mataifa yote walinizunguka; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. Walinizunguka, naam, walinizunguka; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. Walinizunguka kama nyuki, Walizimika kama moto wa miibani; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. Ulinisukuma sana ili nianguke; Lakini Bwana akanisaidia. Bwana ni nguvu zangu na wimbo wangu, Naye amekuwa wokovu wangu.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha yetu wakati mwingine tunaweza kujikuta tumezungukwa na shinikizo la vitisho kutoka kila upande wa maisha yetu, unaweza kuzingirwa na mazingira hatarishi ya vita kutoka kila pembe ya maisha yako, unaweza kuzingirwa na shinikizo la upweke, shinikizo la kukosa afya, shinikizo la afya ya akili, shinikizo la kifedha na kiuchumi, shinikizo la hofu ya changamoto za kazini, shinikizo la matukio ya kutisha na kuumiza moyo, shinikizo la mabadiliko katika maisha, malezi, ndoa, na kadhalika hizi zote zinaweza kuwa hali zinazokusukuma ili ukate tamaa na kuvunjika moyo, na kuzungukwa na hofu za kifo, lakini Neno la Mungu leo linatukumbusha kuwa Bwana atakusaidia, yeye ni nguvu na wokovu, atakuwa msaada mkubwa kwetu tutakapoliitia jina lake atatusikia na atatuitikia kwa wingi wa neema na rehema zake.

Zaburi 116:1-5 “Haleluya. Nampenda Bwana kwa kuwa anaisikiliza Sauti yangu na dua zangu. Kwa maana amenitegea sikio lake, Kwa hiyo nitamwita siku zangu zote. Kamba za mauti zilinizunguka, Shida za kuzimu zilinipata. Naliona taabu na huzuni; Nikaliitia jina la Bwana. Ee Bwana, nakuomba sana, Uniokoe nafsi yangu. Bwana ni mwenye neema na haki, Naam, Mungu wetu ni mwenye rehema.”

Mungu atakuwa msaada wako wewe na mimi tunapokuwa katika mashinikizo ya maisha haya, iwe shinikizo la kimwili au la kiroho Mungu atakusaidia nawe utaufurahia uweza wa Bwana katika kututetea na kutupigania katika hali yoyote ile unayoipitia usilie wala usikate tamaa utasaidiwa naye

·         Maana ya kusukumwa sana.

·         Walinisukuma sana ili nianguke.

·         Nguvu za Mungu wakati wa kusukumwa.


Maana ya kusukumwa sana.

Zaburi 118:12-13 “Walinizunguka kama nyuki, Walizimika kama moto wa miibani; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. Ulinisukuma sana ili nianguke; Lakini Bwana akanisaidia.”

Kimsingi kifungu hiki cha maandiko kinaonyesha kuwa Mwandishi alikuwa amezingirwa na majeshi ya mataifa mbalimbali na kumuwekea shinikizo kubwa kutoka kila upande ili waweze kumshinda lakini aliwakatilia mbali kwa jina la Bwana na kuwashinda, Kimsingi maadui walimsonga sana ili ikiwezekana ashindwe na kumalizwa lakini Bwana alimsaidia.

Kwa asili maneno Ulinisukuma sana ili nianguke; lakini Bwana akanisaidia yanapaswa kusomeka hivi Walinisukuma sana ili nianguke Lakini Bwana akanisaidia, hii ni kwa sababu maadui waliokuwa wakimsonga walikuwa ni wengi na sio mmoja na ukweli huo unaweza kuthibitishwa na matoleo mengine ya Biblia kwa mfano Biblia za kiingereza zifuatazo zinaonyesha kuwa neno hili lilipaswa kuwa katika wingi “Walinisukuma” na sio katika umoja “Ulinisukuma” angalia kwa makini English

Christian Standard Bible inasema hiviThey pushed me hard to make me fail but the Lord helped me

Contemporary English Version inasema hiviTheir attacks were so fierce that I nearly fell, but the Lord helped me

New International Version inasema hiviI was pushed back and about to fall, but the Lord helped me

God’s word translation inasema hivi They pushed hard to make me fall, but the Lord helped me

Unapoangalia asili ya kifungu kizima utaweza kugundua kuwa mwandishi alikuwa akizungumzia kwa wingi, wingi wa maadui, wingi wa mataifa, wingi wa mashinikizo ya changamoto  na majaribu ya kufutiliwa mbali na maadui na kwa msaada wa Mungu aliwakatilia mbali maadui zake kumbuka walikuwa wengi kama nyuki lakini aliwateketeza kama moto wa miiba, sasa hebu tuangalie maana ya kusukumwa, Neno kusukumwa katika lugha ya Kiebrania linasomeka kama “dâchâh dâchach” linalosomeka kwa sauti “daw-khaw” ambalo kwa kiingereza linasomeka kama “outcast”  ambapo maelezo yake ni someone who is rejected or cast out, as from home or society or some way excluded, looked down upon or ignored kwa tafasiri ya Kiswahili ni mtu aliyekataliwa na jamii, aliyefukuzwa nje ya nyumbani au katika jamii, mtu aliyeonekana kuwa hana maana wa kudharaulika, asiyefaa kwa lolote asiye na mchango wowote, kwa hiyo mwandishi alikuwa ni mtu aliyekataliwa, aliyefukuzwa na anayewindwa na maadui kila upande auawe huku akiwa katika mashinikizo mbalimbali yanayomkabili kila upande kiroho na kimwili kiakili na kisaikolojia kwa ujumla alikuwa kama anazidiwa kiasi cha kukaribia kuzimia au kushindwa, maadui hawakutaka awe na utulivu kila wakati walimchokoza na kumsumbua na walitaka kuhakikisha anatokomea huko huko shimoni, hata hivyo mwandishi aliwashinda adui zake wote na hatimaye alirudi katika jamii na kuwa mtu mkubwa sana, Jambo ambalo liliwashangaza watu wote, Mateso haya yalimpata Daudi kimsingi

Zaburi 118:22-23 “Jiwe walilolikataa waashi Limekuwa jiwe kuu la pembeni. Neno hili limetoka kwa Bwana, Nalo ni ajabu machoni petu.” 

Walinisukuma sana ili nianguke.

Kimsingi zaburi hii iliandikwa na Daudi kutokana na maisha aliyoyapitia, lakini kwa vile mtu huyu alikuwa nabii alikuwa pia anazungumza kwa niaba ya Israel, Yesu Kristo pamoja na wewe na mimi, Israel ni Taifa ambalo linaonelewa na kuchukiwa na jamii ya kimataifa sana, ni taifa ambalo adui zake wanatamani walifute lisiwepo, linazingirwa na watu wanaolichukia kutoka kila upande, hata sasa tunapozungumza Israel iko katika vita na baadhi ya nchi za kiarabu na vikundi vya kigaidi wote wakipeleka shinikizo ili ikiwezekana waweze kuwafuta, Israel inachukiwa na Hamas (Harakat al-Muqawama al-Islamiya au Islamic Resistance Movement) hiki ni chama cha siasa nan a Jeshi la waislamu wa Sunni walioko Palestina Eneo la Ukanda wa Gaza, Lengo lao likiwa ni kufutilia mbali wayahudi kokote duniani, Inachukiwa na Hezbollah (Hezb Jeshi au chama Allah- Mungu) Chama cha Mungu au Jeshi la Mungu hawa walioko Lebanon wakisaidiwa na Iran neno Hezbollah maana yake chama cha Allah lengo lao kuu ni kuiangamiza Israel hili ni kundi la kigaidi la Washiha, Israel inachukiwa na Iran ambao wanaiona Israel kama kansa ambayo inatakiwa kufutwa, wanapambana na mamlaka ya Palestina huko ukanda wa Magharibi, inashambuliwa na kundi la wa Houthis hawa wanaitwa Ansar Allah ni tawi la Madhehebu ya Shiha (Shiite) ambao wako Yemen wanaoungwa mkono na Iran, kila mahali kuna shinikizo na yote yanalenga kuwamaliza watu wa Mungu, Daudi kama nabii anaiona Israel kuwa watasaidiwa na Mungu na pamoja na mashinikizo yanayowakabili kama yeye alivyozingirwa na maadui Mungu ataandaa meza machoni pa watesi wetu.

Zaburi 23:4-5. “Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji.Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika.”

Aidha unabii huu pia unamhusu Yesu Kristo, ambaye naye alikataliwa na jamii na kukatiliwa mbali na watu wake na kuteswa vibaya walimsukumia mbali hata katika shimo la mauti lakini Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, Yesu huyu atakuja tena na kuwa mtawala wa ulimwengu wakati wa utukufu pale Israel litakapokuwa taifa kubwa litakaloitawala Dunia mfalme wake atakuwa ni Yesu

Isaya 53:3-5 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

Unabii huu pia unakuhusu wewe na mimi, Shetani anatuchukia bure anafanya mashambulizi kupitia watu na mapepo anatushinikiza kila sehemu na kila mahali kwaajili ya kumpenda Mungu tumekuwa na maadui kila mahali, kwaajili ya kumtumikia Mungu tunachukiwa lakini tunakumbushwa na zaburi hii ya kuwa Mungu hatatuacha hivi hivi hatimaye atakuja kutusaidia nasi tutatawala pamoja na Bwana wetu Yesu Kristo katika ufalme wake!

Mwandishi anatumia lugha picha kuonyesha bidii na juhudi za maadui dhidi yetu wanasukuma sana wanajitahidi wana hasira, lakini hata hivyo kwa msaada wa Mungu maadui walishughulikiwa mmoja baada ya mwingine kwa kukatiliwa mbali kwa jina la Bwana tunaweza kuwa na maadui wa kimwili, maadui wa kiroho na maadui wa maisha yaani masumbufu ya maisha haya na yanaweza kutuletea shinikizo za namna mbalimbali lakini kwa mujibu wa mwandishi ni kuwa Bwana atatusaidia.

Tunaweza kusukumwa na watu kupitia chuki zao, wivu, kejeli au vitendo vya kutukatisha tamaa, mambo haya yanaweza kufanywa na wenzetu, majirani na hata wanafamilia wanaweza kutusukuma kwa maneno au kwa vitendo, Yusufu alitupwa shimoni alitendwa vibaya lakini Mungu alimsaidia.

Mwanzo 49:22-25 “Yusufu ni mti mchanga wenye kuzaa, Mti mchanga wenye kuzaa karibu na chemchemi, Matawi yake yametanda ukutani. Wapiga mishale walimtenda machungu, Wakamtupia, wakamwudhi, Lakini upinde wake ukakaa imara, Mikono yake ikapata nguvu, Kwa mikono ya Mwenye Enzi wa Yakobo; Kwa jina la mchungaji, yeye jiwe la Israeli, Naam, kwa Mungu wa baba yako atakayekusaidia; Kwa mibaraka ya mbinguni juu. Mibaraka ya vilindi vilivyo chini, Mibaraka ya maziwa, na ya mimba.”

Tunaweza kusukumwa wakati mwingine na hali mbaya ya maisha, ugumu wa maisha kutokumudu hali ngumu ya maisha umasikini, magonjwa makali, kushindwa au hasara za kifedha, zote zionaweza kutumika kama misukumo inayokugandamiza ili uanguke, unaweza kusukumwa na upinzani wa nguvu za giza, nguvu za mashetani kusukumwa na hofu, woga na mashaka au majaribio ya kuachana na imani, mifumo ya dunia  ya uchumi na siasa yote yanaweza kukufanya ukawa katika shinikizo ambalo linalenga kukuangusha vyote hivi vinalenga kukusukuma ili uanguke lakini Mungu ndiye msaada wetu, Mungu wetu yuko pamoja nasi, Mungu wetu atatusaidia hatakuacha uaibike!

Zaburi 124:1-8 “Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Israeli na aseme sasa, Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Wanadamu walipotushambulia. Papo hapo wangalitumeza hai, Hasira yao ilipowaka juu yetu. Papo hapo maji yangalitugharikisha, Mto ungalipita juu ya roho zetu; Papo hapo yangalipita juu ya nafsi zetu Maji yafurikayo. Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”

Nguvu za Mungu wakati wa kusukumwa.

Neno la Mungu linaonyesha wazi kuwa wakati watu, maisha na shatani anapoifanya kazi ya kutusukuma ili tushindwe kumbe Mungu ananyoosha mkono wake kutusaidia hiki ndicho anachokishuhudia mwandishi wa zaburi, na kutukumbusha kuwa msaada wetu uko kwa Mungu yeye ndiye anayetusaidia hataacha tuanguke, wala hataacha tuzimie hasinzii wala halali atafanya kitu tu

Zaburi 118:10-14. “Mataifa yote walinizunguka; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. Walinizunguka, naam, walinizunguka; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. Walinizunguka kama nyuki, Walizimika kama moto wa miibani; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. Ulinisukuma sana ili nianguke; Lakini Bwana akanisaidia. Bwana ni nguvu zangu na wimbo wangu, Naye amekuwa wokovu wangu.”

Isaya 41:10-13 “usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu. Tazama, wote walioona hasira juu yako watatahayarika na kufadhaika; watu washindanao nawe watakuwa si kitu, na kuangamia. Utawatafuta wala hutawaona wale wapiganao nawe; watakuwa si kitu; watakuwa kama kitu kisichokuwa, wale waliofanya vita juu yako. Kwa maana mimi, Bwana, Mungu wako, nitakushika mkono wako wa kuume, nikikuambia, Usiogope; mimi nitakusaidia.”

Yeremia 1:18-19 “Maana, tazama, nimekufanya leo kuwa mji wenye boma, na nguzo ya chuma, na kuta za shaba, juu ya nchi yote; juu ya wafalme wa Yuda, na juu ya wakuu wake, na juu ya makuhani wake, na juu ya watu wa nchi hii. Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema Bwana, ili nikuokoe.”

Haijalishi kuwa maisha yako yanazingirwa na mashinikizo ya namna gani lakini kila mahali Mungu yuko na atakusaidia, watu wanaweza kuinuka kinyume nawe, hali inaweza kuinuka kinyume nawe, mazingira yanaweza kuwa kinyume nawe, wakuu wa dini wanaweza kuwa kinyume nawe, lakini Mungu atakuwa msaada mkubwa kwako yeye atakufanya wewe kuwa mji wenye boma, na nguzo ya chuma na ukuta wa shaba maana yake Mungu anakuhakikishia kuwa huwezi kuvamiwa pamoja na mashinikizo ya upinzani na vitisho vya kila aina wewe katika yeye ni Mshindi na zaidi ya kushinda, haijalishi nani wanakusukuma ili uangamie, nani anakuusukuma ili uanguke kwa jina la Bwana watakatiliwa mbali katika jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima.

Hakuna maoni: