Jumapili, 19 Aprili 2026

Kuzungukwa na mabaya yasiyohesabika!


Zaburi 40:11-13 “Nawe, Bwana, usinizuilie rehema zako, Fadhili zako na kweli yako na zinihifadhi daima. Kwa maana mabaya yasiyohesabika Yamenizunguka mimi. Maovu yangu yamenipata, Wala siwezi kuona. Yamezidi kuliko nywele za kichwa changu, Na moyo wangu umeniacha. Ee Bwana, uwe radhi kuniokoa, Ee Bwana, unisaidie hima.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kwamba kuna nyakati katika maisha yetu ambapo mtu unaweza kujikuta katikati ya matatizo mengi kwa wakati mmoja, Kibiblia hali hiyo sio ngeni na kama unakutana na hali kama hiyo wewe sio wa kwanza, Mwandishi wa zaburi hii anaelezea naye hali halisi ya mambo yaliyomkuta, akiwa katika mashinikizo ya changamoto zaidi ya moja anazungukwa na mabaya yasiyohesabika na kutusaidia sisi kuelewa njia ya kufuata na kufanya wakati tunapozungukwa na mabaya yasiyohesabika, usifikiri wakati wowote kuwa labda una laana au una nuksi au Mungu anapatiliza makosa na dhambi zako hapana, ziko nyakati tu katika maisha ya mwanadamu inaweza kutokea ukapita katika hali kama hiyo na hayo ni mambo ya kawaida na wala hupaswi kukata tamaa

2Wakorintho 4:8-10 “Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi; siku zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu.”

Unaona mtume Paulo anaeleza pamoja na kuwa mtu wa Mungu lakini walikuwa wakizungukwa na mabaya yasiyohesabika yeye anaeleza kwa lugha nyingine kuwa twadhikika pande zote, twaona shaka, twaudhiwa, twatupwa lakini hawakati tamaa, hawasongwi, hawazidiwi, hawaangamizwi wala Mungu hawaachi, kuwa mtu wa Mungu au kuwa katika agano na Mungu haimaanishi kuwa na maisha mepesi, iangalie Israel katika ulimwengu wa kimwili ina picha halisi katika ulimwengu wa kiroho sawa na yale unayoyapitia, wanashambuliwa na Hezibollah, (Washiha wenye siasa kali) wanashambuliwa na Hamas (Wasuni wenye siasa kali), wanashambuliwa na Houthis (Wa Ansar wenye siasa kali) wanashambuliwa na Palestinian Islamic Jihad hawa wote wanafanya mauaji, wanateka watu, wanalipua mabomu, wanarusha maroketi na makundi haya yote ya kigaidi yanafadhiliwa na taifa Fulani lenye uchumi mzuri,  jambo linalowafanya wasiishi kwa amani ni ukweli ulio wazi bila mkono wa Mungu Israel isingeliweza kusimama, halikadhalika watu wa Mungu kila upande unashambuliwa na adui yetu shetani na hili ni swala la kawaida katika maisha ya watu wa Mungu hupaswi kuogopa, kwa sababu halitadumu, Leo basi tutachukua muda  kujifunza somo hili  Kuzungukwa na mabaya yasiyohesabika! Kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-

·         Kuzungukwa na mabaya yasiyohesabika.

·         Mambo ya kufanya unapozungukwa na mabaya yasiyohesabika.

·         Msaada wa Mungu wakati unazungukwa na mabaya yasiyohesabika.

Kuzungukwa na mabaya yasiyohesabika

Neno  mabaya yasiyohesabika katika lugha ya asili ya Kiebrania yanasomeka “Ra’ot ein mispar” katika muunganiko huo wa maneno au misamiati miwili ya Kiebrania tunapata neno “Ra’ot” ambalo maana yake kwa kiingereza “trouble” au “evils” kwa Kiswahili ni mabaya, maovu, shinikizo, changamoto au matatizo na neno “Ein Mispar”  ambalo maana yake “countless”, au “without number” yasiyohesabika, yasiyo na idadi, kwa hiyo neno “Ra’ot ein mispar” linapounganishwa pamoja kwa kiingereza unapata neno “countless troubles” au “evil without numbers  maana yake ya kina ni kuwa mtu anayepitia matatizo mengi mfululizo au matatizo mengi kwa wakati mmoja, au changamoto zisizoweza kuhesabika au kujulikana zinaisha lini, mtu anayepitia mashinikizo kutoka pande zote hali hii inapompata mwanadamu kimsingi unaweza kukata tamaa na unazidiwa nguvu  unajiuliza kimsingi unawezaje kutoka katika hali hiyo kama ni magonjwa unajihisi mauti inakuzunguka kila upande mtu unaweza kupitia changamoto nyingi mpaka ukajiuliza kichwani nimekanyaga wapi, wakati Ayubu, Yeremia na Yona  wanapitia hali kama hii ya kuzungukwa na mabaya yasiyohesabika  wao kwa nyakati tofauti tofauti walisema:-

Ayubu 19:8-10 “Yeye ameiziba njia yangu nisipate kupita, Na kutia giza katika mapito yangu. Amenivua utukufu wangu, Na kuiondoa taji kichwani mwangu. Amenibomoa pande zote, nami nimetoweka; Na tumaini langu ameling'oa kama mti.”

Maombolezo 3:1-7 “Mimi ni mtu aliyeona mateso Kwa fimbo ya ghadhabu yake. Ameniongoza na kuniendesha katika giza Wala si katika nuru. Hakika juu yangu augeuza mkono wake Mara kwa mara mchana wote. Amechakaza nyama yangu na ngozi yangu; Ameivunja mifupa yangu. Amejenga boma juu yangu, Na kunizungusha uchungu na uchovu. Amenikalisha penye giza, Kama watu waliokufa zamani. Amenizinga pande zote hata siwezi kutoka; Ameufanya mnyororo wangu mzito.”

Yona 2:3-5 “Maana ulinitupa vilindini, Ndani ya moyo wa bahari; Gharika ya maji ikanizunguka pande zote; Mawimbi yako yote na gharika zako zote zimepita juu yangu. Nami nikasema, Nimetupwa mbali na macho yako; Lakini nitatazama tena kukabili hekalu lako takatifu. Maji yalinizunguka, hata nafsini mwangu; Vilindi vilinizunguka; Mwani ulikizinga kichwa changu;”

Wenzetu hawa kwa nyakati tofauti tofauti kama ilivyokuwa kwa Daudi mwandishi wa zaburi tunayoitafakari walipitia katika nyakati za kuzungukwa na mabaya yasiyohesabika, kwa hiyo kuzungukwa na mabaya sio jambo geni kwa watakatifu na watu wa Mungu ni hali ya kimaandiko na tunajifunza hivyo kutoka katika maandiko kila mtu wa Mungu anaweza kupitia. Mpendwa je wewe unazungukwa na mabaya yasiyohesabika pande zote?  Watu wa Mungu katika maandiko walipitia, je unapopita katika hali kama hiyo unafanyaje? Wenzetu walifanyaje? Yako mambo ya kufanya  

Mambo ya kufanya unapozungukwa na mabaya yasiyohesabika

Zaburi 40:11-13 “Nawe, Bwana, usinizuilie rehema zako, Fadhili zako na kweli yako na zinihifadhi daima. Kwa maana mabaya yasiyohesabika Yamenizunguka mimi. Maovu yangu yamenipata, Wala siwezi kuona. Yamezidi kuliko nywele za kichwa changu, Na moyo wangu umeniacha. Ee Bwana, uwe radhi kuniokoa, Ee Bwana, unisaidie hima.”

Tunajifunza kutoka katika andiko la Msingi wakati wenzetu walipozungukwa na mabaya yasiyohesabika hawakulaumu mtu wala hawakutafuta mchawi wala sababu au kufikiri kuwa wamerogwa na badala yake WALIOMBA usinizuilie rehema maana yake waliomba rehema, fadhili zako zinihifadhi daima walitafuta fadhili za Bwana, walimueleza Mungu wazi wazi kuwa changamoto hizi zimewazidi, walieleza moyo umekufa ganzi, na waliomba msaada wa Mungu, kilio cha mtu anayezungukwa na mabaya humfanya Mungu aingilie kati sawasawa na ahadi zake katika neno lake

Zaburi 50:15 “Ukaniite siku ya mateso; Nitakuokoa, na wewe utanitukuza.” Kwa hiyo neno la Mungu linaonyesha kuwa kila aliyezungukwa  na mabaya yasiyohesabika aliliitia jina la Bwana katika taabu yake na Bwana akasikia na kuwaokoa, sisi nasi tukiliitia jina la Bwana Mungu atasikia na kujibu

Pamoja na maombi na kulia na kumimina mioyo yao mbele za Mungu watakatifu waliotutangulia WALIMTUMAINI Bwana, hapo tunajifunza kuwa walitambua kuwa hakuna mwingine anayeweza kuwasaidia isipokuwa Mungu, hii ni kwa sababu ni kawaida kibinadamu kufikiria mtu wa kukusaidia unapopita katika changamoto fulani fulani lakini lakini wanadamu wanaweza kutumiwa kukuletea shinikizo kubwa zaidi wakati wa changamoto zako hivyo omba kisha weka tumaini lako kwa Bwana

Mithali 3:3-6 “Rehema na kweli zisifarakane nawe; Zifunge shingoni mwako; Ziandike juu ya kibao cha moyo wako. Ndivyo utakavyopata kibali na akili nzuri, Mbele za Mungu na mbele ya mwanadamu. Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako.”

Zaburi 56:1-4 “Mungu, unirehemu, maana yuko atakaye kunimeza, Mchana kutwa ananionea akileta vita. Adui zangu wanataka kunimeza mchana kutwa, Maana waletao vita juu yangu kwa kiburi ni wengi. Siku ya hofu yangu nitakutumaini Wewe; Kwa msaada wa MUNGU nitalisifu neno lake. Nimemtumaini Mungu, sitaogopa; Mwenye mwili atanitenda nini?

Msaada wa Mungu wakati unazungukwa na mabaya yasiyohesabika

Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu huwa pamoja na wale wanaopitia au kuzungukwa na mabaya yasiyohesabika, na hatakuacha uangamie Paulo anaeleza kuwa twazikika pande zote lakini hatuangamii kwa nini Paulo anasema kuwa hatutaangamia hata tupitapo katika changamoto nzito?

2Wakorintho 4:8-10 “Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi; siku zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu.”

1.       Bwana huwa Karibu ili kuokoa na kuponya - Zaburi 34:19 “Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, Na waliopondeka roho huwaokoa. Mateso ya mwenye haki ni mengi, Lakini Bwana humponya nayo yote.”

2.       Bwana atakuwa pamoja nawe na atakupa watu - Isaya 43:2-4 “Upitapo katika maji mengi nitakuwa pamoja nawe; na katika mito, haitakugharikisha; uendapo katika moto, hutateketea; wala mwali wa moto hautakuunguza. Maana mimi ni Bwana, Mungu wako; Mtakatifu wa Israeli, mwokozi wako, nimetoa Misri kuwa ukombozi wako; nimetoa Kushi na Seba kwa ajili yako. Kwa kuwa ulikuwa wa thamani machoni pangu, na mwenye kuheshimiwa, nami nimekupenda; kwa sababu hiyo nitatoa watu kwa ajili yako; na kabila za watu kwa ajili ya maisha yako.”

3.        Bwana atafanya mlango wa kutokea - 1Wakorintho 10:13 “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”

4.       Bwana atakusaidia Isaya 41:10-13 “usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu. Tazama, wote walioona hasira juu yako watatahayarika na kufadhaika; watu washindanao nawe watakuwa si kitu, na kuangamia. Utawatafuta wala hutawaona wale wapiganao nawe; watakuwa si kitu; watakuwa kama kitu kisichokuwa, wale waliofanya vita juu yako. Kwa maana mimi, Bwana, Mungu wako, nitakushika mkono wako wa kuume, nikikuambia, Usiogope; mimi nitakusaidia.”

5.       Bwana atakupa hatima iliyo njema – Yakobo 5:10-11 “Ndugu, watwaeni manabii walionena kwa jina la Bwana, wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu. Angalieni, twawaita heri wao waliosubiri. Mmesikia habari ya subira yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”

Hitimisho

Ndugu zangu kaka zangu na dada zangu kuzungukwa na mabaya yasiyohesabika sio mwisho wako ni hatua ya Mungu kukupeleka katika kiwango kingine ni daraja tu ni mlango wa miujiza mikubwa Bwana hatakuacha uzidiwe ataleta msaada wake haraka, hauna sababu ya kulia au kulalamika au kukata tamaa najua wakati unapozungukwa na mabaya yasiyohesabika ni wakati ambapo kila kitu kinakatisha tamaa ni wakati ambapo unaweza kupoteza tumaini lakini neno la Mungu limetutia moyo ya kuwa Mungu hatatuacha atatuokoa na kutuponya, atakuwa pamoja nawe na atatoa watu wakusaidie, atafanya mlango wa kutokea, atakuwa pamoja nawe hakuna kitu kitakachoweza kusimama mbele yako, yeye atakusaidia na kukupa mwisho ulio mwema jambo kubwa la msingi ni kusimama na kuuona wokovu wa Bwana, Kama Mungu anavyowasaidia Israel na kuwalinda na kuwatetea pamoja na kuzingirwa na wabaya wasiohesabika kila upande lakini Mungu haogopi atakuandalia meza katikati ya watesi wako

Kutoka 14:13-14 “Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. BWANA atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya.”

Wimbo: “Roho wa Bwana twakualika utawale, Karibu Roho, fanya mapenzi ya Bwana”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni: