Ijumaa, 3 Aprili 2026

Hana umbo wala uzuri hata tumtamani!

 


Isaya 53:2-5 “Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”




Utangulizi:

Leo ni siku ya Ijumaa kuu! Wakristo wote Nchini wanaungana na wakristo wote duniani kukumbuka na kuadhimisha kuteswa, kusulubiwa na kufa msalabani kwa Yesu Kristo wa Nazareth kulikotokea huko nje ya Yerusalem Israel miaka zaidi ya 2000 iliyopita, Katika kujikumbusha tukio hilo kama lilivyotabiriwa na Nabii Isaya zaidi ya miaka 700 kabla ya kuzaliwa kwake, Mateso yake haya yalifanyika dhidi yake huku akiwa hakufanya kosa lolote, lakini maandiko yanaeleza kuwa yalimkuta hayo kwaajili ya uponyaji wa wanadamu kwa sababu imeandika kwa kupigwa kwake sisi tumepona

1Petro 2:22-24 “Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa.”

Kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kutafakari na kujifunza kwa kina somo hili “HANA UMBO WALA UZURI HATA TUMTAMANI” kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu muhimu vifuatavyo:-


·         Maana ya neno hana umbo wala uzuri hata tumtamani

·         Yeye hana umbo wala uzuri hata tumtamani

·         Faida ya Mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo 


Maana ya neno hana umbo wala uzuri hata tumtamani.

Ni muhimu kufahamu kuwa nabii Isaya alitabiri kuhusu mateso ya Yesu Kristo miaka 700 kabla ya Kristo kuzaliwa na hatimaye unabii wake ulikuja kutimizwa, akimuona katika kioo cha kinabii Isaya anasema kuhusu Masihi katika mateso yake “Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani.” Maneno haya yana maana gani sasa hebu tuyarejee tena.

Isaya 53:2 “Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani.”  

Maneno haya hayamaanishi kamwe kuwa Yesu hakuwa mzuri au hakuwa na mvuto wa kimwili hapana Yesu alikuwa mzuri sana na kijana mwenye mvuto wa kupita kawaida, lakini Isaya anamuona katika kipindi cha mateso yake Yesu akiwa ameharibiwa vibaya na kuchakazwa katika sehemu zote muhimu za mwili wa kibinanadamu, Neno la Kiebrania linalotumika kuelezea umbo ni “tô’ar” na uzuri ni “Hâdâr” ambayo kwa kiingereza ni “appearance” na “majesty” maana yake ni kuwa mwili wake uliharibiwa vibaya sana “disfigured” na heshima yake au utukufu wake ulidhalilishwa na kushushwa kupita maelezo “dishonoured”  kwa hiyo Isaya ni kama anaelezea kuwa wakati wa mateso yake Yesu Kristo hakuna mtu angeweza kutamani kumuona, mateso yale yaliharibu kabisa muonekano wake  na yalidhalilisha kabisa utu wake, hakuwa na utukufu wa kifalme, wala huwezi kutamani kumuona  na kwa sababu hiyo alidharauliwa sana, Mateso yake yalikuwa kama njia ya kumvunjia heshima na kumdhalilisha kabisa na kuharibu heshima yake waliomsulubisha sio tu walikuwa na uwepo wa kishetani lakini pia walimuonea wivu kutokana na uzuri aliokuwa nao na wakakusudia kuuharibu kwa hiyo chuki za waliomsulubisha pia na wivu ulihusika katika kuhakikisha kuwa wanamuharibu kabisa sura yake na kumvunjia kabisa Heshima yake anaelezea mwandishi wa historia wa kiyahudi wa Karne ya kwanza Flavours Josephus walitaka kuhakikisha kuwa anakuwa na huzuni na nafasi ya kujisikitikia

Isaya 53:3-4 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa.”

Yeye hana umbo wala uzuri hata tumtamani!

Kama tulivyoona maana ya kauli ya hana umbo wala uzuri hata tumtamani ambayo ina maanisha ule uzuri aliokuwa nao Yesu Kristo na utukufu wake uliweza kuharibiwa vibaya kiasi ambacho mtu hangeweza kufikiri kuwa huyu ni mtu au ni mwanadamu yaani aliharibiwa katika namna ambayo ni ngumu kujua kuwa huyu ni mtu yaani watesi walihakikisha wanambomoa uso wake na mwili wake na nafsi yake na roho yake maandiko yanaeleza kuwa aliharibiwa katika kiwango ambacho hakuna mwanadamu aliwahi kuharibiwa hivyo

Isaya 52:14 “Kama vile wengi walivyokustaajabia, (uso wake ulikuwa umeharibiwa sana zaidi ya mtu ye yote, na umbo lake zaidi ya wanadamu),

Isaya 53:5 “Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”    

Watesi wa Yesu Kristo walihakikisha kuwa Yesu anateseka kwa namna zote, anateseka kihisia, kimwili, kijamii, kiroho na kisaikolojia, walimuharibu na kuuchakaza mwili wake kwa mateso ambayo Biblia inaeleza hakuna mtu alichakazwa kwa mtindo na mfumo kama aliofanyiwa Yesu, inawezekana filamu ya “Passion of Christ” ikawa imeonyesha kwa kiwango Fulani uhalisia wa mateso yake, maandiko yakisema aliharibiwa ujue aliharibiwa kweli!  

Kihisia – Yesu alikataliwa na watu wake, alisalitiwa na Yuda Iskariote, kisha wanafunzi wake walimkimbia na wakati wa mateso alibaki peke yake, Petro alimkana mara tatu, mateso haya yakiongozwa na uwepo wa kishetani yalikuwa ni kwaajili ya kusababisha manung’uniko katika moyo wa Yesu apate maumivu ya kihisia na kudhalilika

Yohana 1:10-11 “Alikuwako ulimwenguni, hata kwa yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua. Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea

Mathayo 26:14-16 “Wakati huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa makuhani, akasema, Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha. Tokea wakati huo akawa akitafuta nafasi apate kumsaliti.            

Mathayo 26:56 “Lakini haya yote yamekuwa, ili maandiko ya manabii yatimizwe. Ndipo wanafunzi wote wakamwacha, wakakimbia.”

Luka 22:59-61 “Halafu, yapata saa moja, mtu mwingine alikaza kusema, Hakika na huyu alikuwa pamoja naye, kwa kuwa yeye pia ni Mgalilaya. Petro akasema, Ee mtu, sijui usemalo. Na papo hapo alipokuwa katika kusema, jogoo aliwika. Bwana akageuka akamtazama Petro. Petro akalikumbuka lile neno la Bwana jinsi alivyomwambia, Leo kabla hajawika jogoo utanikana mara tatu.”

Kimwili – Maandiko yanaonyesha kuwa mtumishi wa Mungu (Yesu Kristo) angeteswa katika kiwango ambacho asingeliweza kutambulika, askari wa kirumi walikuwa kama wenye mzuka au walipagawa lilipokuja swala la mateso ya Kristo, walimpiga mijeledi mingi katika namna isiyoweza kuhesabika, walimvika taji ya miiba, huku wakimpiga makofi na kumtemea mate, aliwambwa msalabani akisulubiwa mikono na miguu, kimsingi hakuna mateso makali kama kusulubiwa msalabani, lakini kabla ya hilo wanajeshi wa kirumi walishika mijeledi na kumfunga Yesu kwenye kizimba ambapo unavuliwa nguo na kutandikwa mijeledi, Mijeledi ilikuwa ni fimbo yenye nyuzi kumi na mbili na zile nyuzi zilikuwa na vipande vya vyuma na mifupa ya wanyama wagumu, askari wawili wanaume wenye nguvu walitandika kwa kushindana na wengi waliopitia adhabu hii walichanika tumbo na utumbo ulimwagika nje, unabii wa Isaya na ule wa Daudi katika Zaburi unathibitisha hali mbaya ya mateso ya Kristo namna alivyokuwa

Zaburi 22:14-18 “Nimemwagika kama maji, Mifupa yangu yote imeteguka, Moyo wangu umekuwa kama nta, Na kuyeyuka ndani ya mtima wangu. Nguvu zangu zimekauka kama gae, Ulimi wangu waambatana na taya zangu; Unaniweka katika mavumbi ya mauti, Kwa maana mbwa wamenizunguka; Kusanyiko la waovu wamenisonga; Wamenizua mikono na miguu. Naweza kuihesabu mifupa yangu yote; Wao wananitazama na kunikodolea macho. Wanagawanya nguo zangu, Na vazi langu wanalipigia kura.”             

Yohana 19:1-3 “Basi ndipo Pilato alipomtwaa Yesu, akampiga mijeledi. Nao askari wakasokota taji ya miiba, wakamtia kichwani, wakamvika vazi la zambarau. Wakawa wakimwendea, wakisema, Salamu! Mfalme wa Wayahudi! Wakampiga makofi.”

Mathayo 26:67-68 “Ndipo wakamtemea mate ya uso, wakampiga makonde; wengine wakampiga makofi, wakisema, Ewe Kristo, tufumbulie; ni nani aliyekupiga?

Mathayo 27:29-31 “Wakasokota taji ya miiba, wakaiweka juu ya kichwa chake, na mwanzi katika mkono wake wa kuume; wakapiga magoti mbele yake, wakamdhihaki, wakisema, Salamu, Mfalme wa Wayahudi! Kisha wakamtemea mate, wakautwaa ule mwanzi, wakampiga-piga kichwani. Walipokwisha kumdhihaki, wakalivua lile vazi, wakamvika mavazi yake, wakamchukua kumsulibisha.”

Kijamii - Yesu aliteswa kijamii. Alidhihakiwa hadharani dhidi ya watu wale waliokuwa wakimuheshimu, alihesabiwa pamoja na wahalifu yeye akiwekwa kati kati yao, lakini alivuliwa nguo hadharani tukio hili lilikuwa la udhalilishaji na uaibishaji , jamii hiyo hiyo wakati wa hukumu yake walipiga kelele wakisema asulubiwe asulubiwe!

Isaya 53:12 “Kwa hiyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu, Naye atagawanya nyara pamoja nao walio hodari; Kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa, Akahesabiwa pamoja na hao wakosao. Walakini alichukua dhambi za watu wengi, Na kuwaombea wakosaji.”        

Yohana 19:23 “Nao askari walipomsulibisha Yesu, waliyatwaa mavazi yake, wakafanya mafungu manne, kwa kila askari fungu lake; na kanzu nayo. Basi kanzu ile haikushonwa, ilikuwa imefumwa yote pia tangu juu.”

Kiroho – kwa kuwa alikuwa amezibeba dhambi za ulimwengu mzima, kwa wakati ule Mungu alikuwa amemuacha, kwa hiyo kwa wakati ule ilikuwa ni kama Mungu amemuacha na kumtenga, Mungu hakumwangalia kama mwanae!

Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.            

Mathayo 27:45-46 “Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa. Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?                         

Faida ya Mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo.

Tunapoadhimisha mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyeyatoa maisha yake kufa msalabani ni muhimu kwetu kufahamu kuwa Yesu alikubali kufa Msalabani na kuharibiwa vibaya katika namna tuliyojifunza kwa sababu ya makosa yetu na maovu yetu na kwaajili ya tukio hili ziko faida nyingi zinazopatikana kwa kufa kwake Msalabani.

Isaya 53:4-5 “Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

Kwa tendo la Yesu Kristo kufa Msalabani, alizibeba dhambi zetu, na kuwapatanisha wanadamu kwa Mungu kwa kuondoa kiambaza kilichokuwepo kati yetu na Mungu na sio hivyo tu bali aliziharibu nguvu za shetani za kupata mashiko ya kutushitaki akituletea uponyaji wa mwili nafsi na roho lakini kuu kuliko yote ni uzima wa milele

-          Tunapata msamaha wa dhambi kwa sababu aliimwaga damu yake pale msalabani na pasipo kumwagika damu hakuna ondoleo la dhambi

 

Waebrania 9:22 “Na katika Torati karibu vitu vyote husafishwa kwa damu, na pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo.”

 

-          Tunapata uponyaji wa mwili nasfi na roho kwa sababu mateso yake yalibeba na kusulubisha magonjwa yetu, maumivu yetu na udhaifu wetu

 

1Petro 2:24 “Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa.”

 

-          Tunapata Amani ya ndani kabisa iliyopotea, Kila mtu aliyempokea Yesu hata pamoja na kupitia changamoto za aina mbalimbali duniani utaweza kugundua kuwa anapewa Amani ya ndani sana ambayo kimsingi gharama zake zililipwa pale msalabani adhabu aliyopewa ilituletea sisi Amani ya kweli ya maisha ya ndani sana na mwanadamu

 

Amani Isaya 53:4-5 “Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

 

-          Tunaupata ushindi dhidi ya shetani na nguvu zake zote za giza, tendo la kufa kwa Yesu Kristio msalabani baada ya kusulubiwa kwake maaana yake alizivua  enzi  na mamlaka yaani nguvu zake na utendaji wake shetani

 

Wakolosai 2:14-15 “akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo.”

 

-          Msalaba ni njia ya uzima huu na uzima wa milele, Kifo cha Yesu kimetuletea uzima wa mwili na uzima wa kiroho  kwa hiyo katika yeye tunao uzima wa milele

 

Yohana 10:10-11 “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele. Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.“

 

1Yohana 5:12-13 “Yeye aliye naye Mwana, anao huo uzima; asiye naye Mwana wa Mungu hana huo uzima. Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu.

Hitimisho

Wokovu una gharama kubwa sana umegharimu maisha ya mwana wa Mungu, hatuna budi kuujali na kutokuupuuzia ili tuweze kupona, aliharibiwa namna ile ili sisi tutengenezwe na kufaa mbele za Mungu, basi tuukubali wokovu.

Waebrania 2:2-4 “Kwa maana, ikiwa lile neno lililonenwa na malaika lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki, sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia; Mungu naye akishuhudu pamoja nao kwa ishara na ajabu na nguvu za namna nyingi, na kwa magawanyo ya Roho Mtakatifu, kama alivyopenda mwenyewe.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima       

Hakuna maoni: