Jumapili, 12 Aprili 2026

Kuyachuchumilia yaliyo mbele!

 


Wafilipi 3:12-14 “Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.”



Utangulizi:

Mojawapo ya changamoto kubwa sana katika ufanisi wa maendeleo ya mwanadamu kiroho na kimwili na kisaikolojia ni pamoja na kutokusahau yaliyo nyuma, “Living in the Past” kutokuyasahau yaliyo nyuma kumewafunga watu wengi sana na kuwawekea mipaka ya kiimani, kuchelewesha ukuaji wao wa kiroho, kuzuia maendeleo yao ya safari ya kiuchumi, kuwadumaza katika hali zote kuwanyima maisha ya ushindi, kuathiri uwezo wa kufanya maamuzi, kupunguza nguvu zao kwa mambo yajayo na kushindwa kuamini ahadi ya Mungu kuhusu mambo yajayo, hali hii iliwasumbua sana wana wa Israel ambao hata walipookolewa kutoka Misri, hawakuliona baadaye tendo lile kuwa ni kubwa sana na badala yake walinung’unika mara kwa mara wakikumbuka kule Mungu alikowaokoa katika inchi ya utumwa, tena wakikumbuka vitu vidogovidogo kama matango na mboga.

Hesabu 11:4-6 “Kisha mkutano wa wafuasi waliokuwa kati yao, wakashikwa na tamaa; wana wa Israeli nao wakalia tena, wakasema, N'nani atakayetupa nyama tule? Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu.”

Kutokuyasahau yaliyo nyuma na kuamua kuyachuchumilia yaliyo mbele kunaweza kukufanya usizione sababu za wito wa Mungu na baraka alizokusudia kwako, kumbuka kila kitu duniani kina mchakato na maisha yana mchakato wake na mwandishi wa mchakato huo ni Mungu, sasa basi anapokuwa amekupitisha mahali na ukawa unalalamika unaweza kusababisha kupoteza Baraka zilizokusudiwa kwako, kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kujifunza somo hili muhimu “Kuyachuchumilia yaliyo mbele” kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya kuyachuchumilia yaliyo mbele

·         Umuhimu wa Kuyachuchumilia yaliyo mbele!

·         Athari za kutoyasahau yaliyo nyuma


Maana ya kuyachuchumilia yaliyo mbele

Wafilipi 3:13 “Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele;”

Kabla hatujaingia ndani kuangalia kile ambacho Mungu amekusudia kusema nasi leo ni muhimu kwetu kuyafanyia uchunguzi maandiko au maneno yanayotumiwa na Paulo Mtume katika fungu hili la maandiko yana maana gani, Waraka huu wa wafilipi uliandikwa kwa lugha ya kiyunani (Koine Greek) ambayo ndiyo ilikuwa lugha ya kisomi na kitaaluma ya nyakati za karne ya kwanza kwa hiyo kitabu hiki kiliandikwa mnamo mwaka wa 62BK  na maneno haya kuyachuchumilia yaliyo mbele yanasomeka hivi katika kiyunani (Epekteinomenos tois emprosthen)  neno Epekteinomenos au epekteinomai kwa kiingereza linasomeka “stretching oneself forward“ ambalo maana yake ni kujinyoosha kuelekea mbele kwa nguvu  neno hili hasa lina asili ya mkao anaotakiwa kujiweka mwanariadha anapokimbia mbio za Olympic  ili aweze kushinda, kulingana na sheria za Olympic umaliziaji wa mkimbiaji wa riadha huamuliwa wakati kiwiliwili chake kinapovuka mstari wa kumalizia, kwa hiyo katika mbio za riadha kutanguliza miguu au mikono hakuhesabiwi kama umaliziaji wa mbio ulio halali, aidha mwanariadha anayetafuta ushindi huwaga hana muda wa kuangalia nyuma wala pembeni nguvu zake zote  fahamu zake zote huelekezwa katika kufikia lengo na kwa sababu hiyo kila msuli na kila mfumo wa fahamu na neva hufanya kazi kwa bidii kuelekea katika malengo yake, Kwa hiyo Paulo mtume anatumia mfano wa wanariadha kwa sababu ilikuwa maarufu sana nyakati za kanisa la kwanza, wakati wote Mungu anapotaka ushindi utokee katika maisha ya watu wake huwaambia wasonge mbele

Isaya 43:18-19 “Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani.Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani.”

Kutoka 14:14-15. “BWANA atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya. BWANA akamwambia Musa, Mbona unanililia mimi? Waambie wana wa Israeli waendelee mbele.”  

Unaona! Katika fundisho lake Paulo Mtume hataki Wafilipi wajidhanie kuwa wamekwisha kufika au wamekuwa wakamilifu akitumia mfano wake anamtaka kila Mkristo kusonga mbele kwa nguvu kwa imani na utii, kwa bidii, kwa nguvu kwa tumaini na kutokuangalia nyuma mpaka kuhakikisha ya kuwa tunapata tuzo mbinguni na kuyafikia malengo yetu yaliyo mbele, kwa hiyo kama mwanariadha uliye katika mbio za ushindani wa kiroho angalia mbele tu!

Umuhimu wa Kuyachuchumilia yaliyo mbele!

Ni muhimu kujiuliza kwa nini Paulo Mtume siku zote alikuwa akiyachuchumilia yaliyo mbele na akisahau yaliyo nyuma, Kuangalia nyuma kungempa historia ya matukio yaliyopita ambayo kimsingi yangemshika na kumpunguzia mwendo wake wa kusonga mbele katika imani aku kumpa kuridhika sawa na mwanariadha anavyoweza kupoteza mwelekeo kama ataangalia nyuma, Yeye alikuwa mtu mwenye bidii katika Torati kuliko mtu yeyote, aliishika sheria kiasi ambacho kwa habari ya sheria hakuwa na dhambi, lakini alipompata Yesu na kubaini ubora wa Yesu Kristo hata pamoja na mateso makali yaliyokuwa yakimpata alidhamiria kuwa ataendelea kuwa na Yesu, hatamuacha Yesu atashikamana na Yesu atashikamana na injili na hatarudi nyuma kwa sababu yoyote, aliwaonya Wafilipi hivi na kujionyesha yeye mwenyewe kuwa mfano kwa sababu ya watu waliofundisha mafundisho ya Sheria ya Musa na tohara ambao yeye aliwaitwa umbwa au watu wajikatao akitaka kuwaonyesha Wafilipi faida ya kumfuata Yesu na kuachana na mafundisho ya kale yasiyo na msingi, Paulo alikuwa na mafanikio makubwa katika dini ya kiyahudi na heshima kubwa lakini alipuuzia kwaajili ya Kristo. Alipompata Kirsto hakuangalia pembeni tena alikaza kwenda mbele

Yeye aliliudhi Kanisa 1Wakorintho 15:9 “Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu.”

Wagalatia 1:13-15 “Maana mmesikia habari za mwenendo wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu. Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu. Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake,”

Wafilipi 3:2-7 “Jihadharini na mbwa, jihadharini na watendao mabaya, jihadharini na wajikatao. Maana sisi tu tohara, tumwabuduo Mungu kwa Roho, na kuona fahari juu ya Kristo Yesu, wala hatuutumainii mwili.Walakini mimi ningeweza kuutumainia mwili. Mtu ye yote akijiona kuwa anayo sababu ya kuutumainia mwili, mimi zaidi. Nalitahiriwa siku ya nane, ni mtu wa taifa la Israeli, wa kabila ya Benyamini, Mwebrania wa Waebrania, kwa habari ya kuishika torati, ni Farisayo, kwa habari ya juhudi, mwenye kuliudhi Kanisa, kwa habari ya haki ipatikanayo kwa sheria sikuwa na hatia. Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo.”

Kila mtu aliyemuamini Bwana wetu Yesu Kristo kama Bwana na mwokozi wa maisha yake anapaswa kusahau yote yaliyopita na kuweka akili zake zote na nguvu zake zote na moyo wake wote na fahamu zake zote kuyachuchumilia yaliyo mbele, hii haimaanishi kuyafuta kabisa lakini maana yake maisha yaliyopita kama yalikuwa ya raha au ya taabu yalikuwa ya heshima ama kuvunjiwa heshima, yasiwe na machango wowote katika hali yako ya sasa kwa kukufanya kuangalia nyuma na kumpuuzia Kristo na badala yake kujitoa kwa nguvu zetu zote katika kumcha Mungu na kumtumikia bila hata kujali hali unayopitia sasa, Neno la Mungu linaonyesha wazi kuwa Mungu havuitiwi kamwe na watu wasio na maamuzi thabiti na badala yake anawataka watu wenye msimamo watakaosonga mbele wazima wazima na sio nusu nusu, ushindi wetu utapatikana sio kwa kuitanguliza mguu au mkono bali kiwiliwili chote

-Mke wa Lutu alitazama nyuma wakati Mungu alipowaokoa Lutu na familia yake kutoka Sodoma, na matokeo yake hukumu ilimpitia ya kuwa nguzo ya chumvi, yeye alikamatwa na maisha ya zamani, badala ya kuyasahau yaliyipita alishikamana nayo na yakaharibu hatima yake, hatima yako inaweza kuathiriwa na mambo ya nyuma

Mwanzo 19:16-26 “Akakawia-kawia; nao wale watu wakamshika mkono, na mkono wa mkewe, na mkono wa binti zake wawili, kwa jinsi BWANA alivyomhurumia, wakamtoa wakamweka nje ya mji. Ikawa walipomtoa nje, mmoja alisema, Jiponye nafsi yako usitazame nyuma, wala usisimame katika hilo bonde po pote; ujiponye mlimani, usije ukapotea. Lutu akawaambia, Sivyo, bwana wangu! Tazama, mtumwa wako ameona kibali machoni pako, nawe umezidisha rehema zako ulizonifanyia kwa kuponya nafsi yangu, nami siwezi kukimbilia mlimani nisipatwe na yale mabaya, nikafa. Basi mji huu u karibu, niukimbilie, nao ni mdogo, nijiponye sasa huko, sio mdogo huu? Na nafsi yangu itaishi. Akamwambia, Tazama, nimekukubali hata kwa neno hili, kwamba sitauangamiza mji huo uliounena. Hima, ujiponye huko, maana siwezi kufanya neno lo lote, hata uingiapo humo. Kwa hiyo jina la mji ule likaitwa Soari. Jua lilikuwa limechomoza juu ya nchi Lutu alipoingia Soari. Ndipo BWANA akanyesha juu ya Sodoma na juu ya Gomora kiberiti na moto toka mbinguni kwa BWANA. Akaangusha miji hiyo na Bonde lote, na wote waliokaa katika miji hiyo, na yote yaliyomea katika nchi ile. Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi.”

Luka 9:62 “Yesu akamwambia, Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu.”

Siri ya maisha ya ushindi iko katika kuyachuchumilia yaliyo mbele na kusahau yaliyo nyuma kama mtu anataka kusonaga mbele ni lazima asahau kushindwa kwake, asahau maumivu yote ya nyuma, asamehe endapo wako watu waliomuumiza, asahau majuto na aibu, asahau mafanikio yanayokufanya ujivune na kupata kiburi,  sahau hata watu ambao walikuwa karibu nawe na makusudi ya kuwa karibu nao yameisha, na umwangalie Yesu Kristo zaidi kwaajili ya mafanikio yako ya baadae , unapoyachuchumilia yaliyo mbele unafungua mlango mpya  na mlango huo unakufanya ukimbie mbio zako na kuufikia mwisho wenye ushindi na Mungu atakupa nguvu ya kukimbia hadi mwisho.

Athari za kutoyasahau yaliyo nyuma.

Wakati wowote watu wanapoangalia nyuma wanakuwa watumwa wa yaliyopita, Kristo alitukomboa ili tuishi maisha mapya yenye tumaini na uhuru yasiyo na hofu kwa hiyo kutokuyasahau yaliyo nyuma kunaathiri maisha yako

1.       Kunakufanya usiendelee kiroho, kimwili na kisaikolojia kwa sababu unaweza kukwama na hatia aibu au majuto,  na ukajiona hustahili Baraka mpya za Mungu, au ukabweteka na kile ulicho nacho!

2.       Kunakufanya uharibu furaha ya sasa – badala ya kumshukuru Mungu kwa yaliyopo na kukusaidia kusonga mbele unabaki unalilia yaliyopita  au unaridhika  na kile unachiokiona!

3.       Kutosahau yaliyo nyuma kunakufanya usiweze kuyafikia malengo mfano Paulo alikuwa analenga la kufika mbinguni na kupata thawabu na kukaa na bwana milele

4.       Kutokuyasahu yaliyo nyuma kunakufanya uwe mwoga wa hatua mpya – unashikwa na hofu ya kushindwa au unajutia mafanikio yaliyopita

5.       Kutoyasahau yaliyo nyuma kunakufanya uishi wakati uliopita badala ya wakati wa sasa wa kusudi la Mungu

Paulo alichagua neno moja tu kuyasahau yaliyopita na kuyachuchumilia yaliyo mbele hii ndio siri ya ushindi inayotoa ujasiri na kukufanya usiogope lolote, Neno la Mungu linatoa wito leo kuwa ni lazima usahahu kushindwa kwako, usahahu mafanikio yako ya nyuma, sahahu aibu, au kujilinganisha na wengine sahahu maumivu yako, usiishi katika majuto angalia mbele na Mungu atakutokea, kama unahitaji mafanikio makubwa zaidi chuchumilia yaliyo mbele!

Kumbukumbu 31:8 “Naye Bwana, yeye ndiye atakayekutangulia, atakuwa pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha; usiogope wala usifadhaike.”     

Mithali 4:25-27 “Macho yako yatazame mbele, Na kope zako zitazame mbele yako sawasawa. Ulisawazishe pito la mguu wako, Na njia zako zote zithibitike; Usigeuke kwa kuume wala kwa kushoto; Ondoa mguu wako maovuni.

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima

Hakuna maoni: