Jumapili, 21 Juni 2026

Kumbe ni Lea badala ya Raheli!


Mwanzo 29:20-26 “Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda. Yakobo akamwambia Labani, Nipe mke wangu, maana siku zangu zimetimia; niingie kwake. Labani akakusanya watu wote wa mahali pale, akafanya karamu. Ikawa wakati wa jioni akamtwaa Lea, binti yake, akamletea Yakobo, naye akaingia kwake. Labani akampa Lea mjakazi wake Zilpa, awe mjakazi wake. Ikawa, kulipokuwa asubuhi, kumbe! Ni Lea. Akamwambia Labani, Nini hii uliyonitenda? Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya? Labani akasema, Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa;”



Utangulizi:

Hakuna linalotokea kwa bahati mbaya Duniani, wakati mwingine Mungu anaweza kuruhusu, ufanye kazi, au biashara, au huduma au usomee fani ambayo kimsingi inaweza ikawa sio chaguo lako, na hali kadhalika unaweza kuwa katika mahusiano na mtu ambaye moyo wako unaweza usiwe umemridhia moja kwa moja isipokuwa ni kwa sababu ya mazingira fulani, katika maisha yangu nimekuwa karibu na wanafunzi na walimu na watu wa kada mbalimbali za kitaaluma, na nimesikia kwa masikio yangu wengine wakisema nilitaka kuchukua masomo ya Sayansi, lakini walimu walinishauri nichukue masomo ya Sanaa, nilitaka kuchukua masomo ya Sanaa lakini wazazi wangu walinishauri nichukue Sayansi, nilitaka kuwa daktari lakini serikali ilinipangia ualimu, nilitaka kuwa mwanasheria lakini nililazimika kuwa mwanahabari, nilikuwa na mipango yangu kadhaa lakini nimejikuta nimekuwa Mwalimu, Mungu katika hekima yake wakati mwingine anaweza kuruhusu ubebe mzigo ambao moyo wako hungependelea kuubeba kwa kusudi la kutimiza mpango wake usioweza kuuona kwa wakati huo au kwa macho yako na sio hivyo tu wakati mwingine Mungu anaruhusu hivyo kwaajili ya ukuaji wa kiroho, kukufundisha kuacha mapenzi yako na kusikiliza ya kwake, kukufundisha uvumilivu, kupenda kisichoweza kupendeka na kukunyima kutimiza mapenzi yako uli uweze kujisalimisha kwenye mapenzi yake, hali kama hiyo ndiyo iliyomtokea Yakobo wakati anataka kuoa, alijiandaa na kufanya kazi kwa bidii kwaajili ya Raheli lakini akaozwa Lea bila kutaka!, Kumbe ni Lea badala ya Raheli.

Mwanzo 29:16-20 “Labani alikuwa na binti wawili, jina la mkubwa ni Lea, na jina la mdogo ni Raheli. Naye Lea macho yake yalikuwa dhaifu, lakini Raheli alikuwa mzuri wa umbo, na mzuri uso. Yakobo akampenda Raheli akasema, Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo. Labani akasema, Afadhali nikupe wewe kuliko mtu mwingine; kaa kwangu. Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda.”

Kuna maumivu kiasi fulani ambayo wengine wanaweza wasiyaseme kwa maneno lakini yakaishia moyoni, maumivu ya kupata ua kufanya jambo ambalo kimsingi hujalipenda toka moyoni, hujalitamani, hujalitaka wala hujaliomba, au hujalisomea, unaweza kabisa katika maisha ukasomea ujuzi fulani kisha ukapangiwa mwingine, unaweza kuomba kazi fulani na ukapewa nyingine unaweza kutarajia kuwa ungeoa mke wa aina fulani au ukaolewa na mume wa aina fulani, lakini ukaishia kuolewa na mwingine, ungetaka idadi fulani ya watoto au watoto wa jinsia fulan unashangaa umepewa wa aina fulanii, au ulikuwa na ndoto ya maisha fulani na ukajikuta unaishi maisha tofauti, haya ndiyo yaliyo mtokea Yakobo, alipoenda kwa mjomba wake kuoa alikuwa na nia ya kumpata Raheli na kimsingi alimpenda Raheli aliwekeza nguvu zake na akili zake na hisia zake kwa Raheli, na akatumika miaka saba ili ampate kipenzi wake Raheli lakini siku ya harusi yake anaamka asubuhi kumbe ni Lea! Hali hii inawakuta watu wengi,  katika maisha kujikuta kuwa wana kile walichokua hawajakitaka, ujumbe huu ni kwa watu wanaopitia hali kama hiyo na Mungu ana makusudi na wewe na anataka kusema nawe, tutajifunza ujumbe huu KUMBE NI LEA BADALA YA RAHELI kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu  vifuatavyo:-

·         Inapokuwa Lea badala ya Raheli

·         Kumbe ni Lea badala ya Raheli

·         Kusudi la Mungu kupitia Lea

Inapokuwa Lea badala ya Raheli

Wote tutakuwa tunakumbuka kuwa baada ya Yakobo kuchukua mbaraka wa Esau na mgogoro kujitokeza katika familia Rebeka alimshauri Isaka kuwa kijana wao na aende kwa kaka yake Rebeka yaani Labani ili ajipatie mke huko badala ya kujitwalia mke katikati ya Wakanaani ambao roho yake Rebeka haikuwaridhia, Yakobo alisafiri kuelekea Haran kwa mjomba wake Labani ili ajipatie mke huko na alipofika huko kimsingi Yakobo alimpenda sana Raheli kwa sababu ndiye aliyekuwa anamvutia kimwili na kiumbo na kwa uzuri, walipatana na mjomba wake kuwa mahari itakuwa ni kumtumikia kwa miaka 7 kwaajili ya Raheli, kwa hiyo Yakobo alifanya kazi kwa bidii sana kwaajili ya kile alichokuwa amekiona, amekitamani na kukipenda, mke wa ndoto yake, stori nzima iko hapa:-

Mwanzo 29:16-30 “Labani alikuwa na binti wawili, jina la mkubwa ni Lea, na jina la mdogo ni Raheli. Naye Lea macho yake yalikuwa dhaifu, lakini Raheli alikuwa mzuri wa umbo, na mzuri uso. Yakobo akampenda Raheli akasema, Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo. Labani akasema, Afadhali nikupe wewe kuliko mtu mwingine; kaa kwangu.Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda. Yakobo akamwambia Labani, Nipe mke wangu, maana siku zangu zimetimia; niingie kwake. Labani akakusanya watu wote wa mahali pale, akafanya karamu.Ikawa wakati wa jioni akamtwaa Lea, binti yake, akamletea Yakobo, naye akaingia kwake. Labani akampa Lea mjakazi wake Zilpa, awe mjakazi wake. Ikawa, kulipokuwa asubuhi, kumbe! Ni Lea. Akamwambia Labani, Nini hii uliyonitenda? Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya? Labani akasema, Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa; timiza siku zake saba, nasi tutakupa huyu naye kwa utumishi utakaonitumikia, miaka saba mingine. Yakobo akafanya hivi, akatimiza siku zake saba. Naye akampa Raheli binti yake kuwa mkewe. Labani akampa binti yake Raheli mjakazi wake Bilha, awe mjakazi wake. Akaingia kwa Raheli naye, akampenda Raheli kuliko Lea, akatumika kwa ajili yake miaka saba mingine.”

Unaweza kuona mtu anafanya kazi kwa bidii na kwa kujituma kweli kweli akiwa na ndoto ya kumpata Raheli lakini hatimaye anakuja kupewa Lea, hili linaweza kuwa jambo lenye kuumiza sana kwamba unafanya kazi, unasoma au unajituma kwaajili ya malengo fulani alafu unakuja kujikuta ni kama ulimwengu unataka ufanye jambo lingine, jambo hili linaumiza, unatoa juhudi zako zote, unatoa muda wako wote, unawekeza moyo wako wote lakini matokeo yanakuwa sio yale uliyoyatarajia, hali hii iko hivyo duniani, kuna watu wamewapenda sana wachumba zao, wakawafulia, wakawapikia, wakawa wakiwajulia hali lakini na kuwapa kila kitu, lakini yule bwana akaja akaoa mwanamke mwingine, kuna watu wamejitoa kwaajili ya wachumba wao wakawasomesha wakawahudumia na kuwafadhili, hata wakafunga na kuomba kwaajili yao kwa kulia, lakini wakaja kuolewa na mwanaume mwingine, kuna watu walikuwa na ndoto ya kuendesha ndege lakini leo ni Askari polisi, kuna watu walitaka kuwa madaktari lakini leo ni walimu, Moyo wako unaweza kuchoka na kuumia na kuumizwa na matarajio yaliyovunjika na unaweza kujiuliza Mungu kwa nini hali hii inakuwa hivi? Unasomea fani Fulani kisha unakuja kupata kazi flani tofauti na ile uliyoisomea na iliyoko moyoni mwako! Wala sicho ulichokitarajia, unahisi kuchanganyikiwa, unahisi kuumia na unaanza kumuhoji Mungu! Imekuwaje? Ndoto yangu ilikuwa hii mbona nafanya jambo hili?

Mithali 13:12 “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.”

Tunao watu wengi sana leo hii katika jamii ambao mioyo yao imejeruhiwa kwa kuwa na matokeo wasiyoyatarajia, mtu amesoma kwa bidii na kufanya mtihani wake kwa umakini anakuja kupata Division three ambayo hakuitegemea, unaweza kuolewa na mume ambaye  hata hukuwa na hata hisia naye, unaweza kuwa na mke ambaye huna hata hisia naye lakini mnajikuta ndio mnaishi, yako maisha ambayo unaweza kuwa ndani yake lakini moyo wako ukawa haupo humo, haki hii ndiyo ilityomtokea Yakobo anampenda Raheli na ameganya kqzi miaka saba kwaajili yake, lakini amepewa Lea, kwa hiyo katika maisha yetu inapokuwa Lea badala ya Raheli watu hukosa amani na furaha na kuona kama maisha yameshakataa na wakati mwingine unaweza kuwaza na kufikiri umekosea wapi katika kaninu za maisha, unaweza kujikuta hufurahii maisha, hufurahii kazi, unakosa furaha kwa kile ulichonacho na ukijilinganisha na wengine ndio unachoka unaweza kudhani wewe una balaa, lakini nataka nikugusie kuwa Mungu ana mpango!, Hakuna jambo lolote linalotokeaau kukupata nje ya mpango wa Mungu, hapa duniani hatujaja kutimiza mpango wetu, tumekuja duniani kutimiza mpango na mapenzi ya Mungu, hivyo sio jambo la ajabu yakakupata yaliyo mageni

Kumbe ni Lea badala ya Raheli

Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa njia za Mungu ziko juu sana kuliko njia za mwanadamu na wala mawazo yetu si kama mawazo yake, njia za Mungu ziko juu sana, mpango wa Mungu ni mkuu kuliko matakwa ya mwanadamu, Mungu hafanyi kazi kwa kusikiliza hisia zeu, ana mpango mkubwa sana kuliko hisia zako, Hapa duniani ulizaliwa kwa kusudi la Mungu na kwa sababu hiyo mwenye mji wake ni Mungu na mwenye mpango wake ni yeye kwa hiyo wewe unaweza kumtaka Raheli lakini Mungu akakupa Lea, unaweza kudhani kuwa dunia imekulazimisha Lea na we ulitaka Raheli lakini, Lea ndio mpango kamili wa Mungu. Raheli unaweza kuwa sio mpango wa kudumu wala wa milele lakini Lea unaweza kuwa mpango wa Mungu wa kudumu na wa milele, na wenye faida unajua nini  watoto wote maalumu ambao Mungu alikuwa na kusudi lake la kudumu walipita kwa Lea na sio Raheli

Mwanzo 29:31-35 “BWANA akaona ya kwamba Lea hakupendwa, naye akafungua tumbo lake; bali Raheli alikuwa hazai. Lea akapata mimba akazaa mwana, akampa jina lake, Reubeni, maana alisema, Kwa kuwa BWANA ameona teso langu; sasa mume wangu atanipenda. Akapata mimba tena akazaa mwana, akasema, Kwa kuwa BWANA amesikia ya kwamba mimi sikupendwa, amenipa na huyu; akamwita jina lake Simeoni. Akapata mimba tena, akazaa mwana, akasema, Basi wakati huu mume wangu ataungana nami, kwa sababu nimemzalia wana watatu. Kwa hiyo akamwita jina lake Lawi. Akapata mimba tena, akazaa mwana. Akasema, Mara hii nitamsifu BWANA; kwa hiyo akamwita jina lake Yuda; akaacha kuzaa.”

Mungu aliwatumia Walawi, kutoka kwa Lea kuwa makuhani kwaajili ya utumishi wa Mungu katika nyumba yake na Mungu na Mungu alimtumia Yuda kutoka kwa Lea kuleta viongozi mashuhuri na wacha Mungu kama Daudi na kupitia Lea na Yuda alimleta Yesu Kristo

Mathayo 1:1-2.“Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa Isaka; Isaka akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yuda na ndugu zake;”

Mungu aliruhusu Lea kuwepo katika maisha ya Yakobo kwa sababu Lea ndio ulikuwa mpango wa Mungu, Lea alikuwa ni darasa la unyenyekevu, Lea alikuwa ni chuo cha uvumilivu, Lea alikuwa ni shule ya haki ya Mungu, Lea ilikuwa ni shule ya kujifunza kupenda kile ambacho Mungu amekupangia, Mungu anatufundisha kumfuata yeye na sio hisia zetu, Lazima ufike wakati katika maisha yetu tuamue kufuata hisia zetu au kutimiza mpango wa Mungu, Lea alilazimika kutaka kumpendeza Yakobo lakini hata pamoja na kumzalia watoto wengi wa kume mfuluzizo bado Yakobo hakuona nguvu za Mungu, Lea aliamua kumuita mtoto wake Yuda akisema NITAMSIFU BWANA Furaha ya kweli haipatikani kwa wanadamu bali inapatikana kwa Mungu, Mungu aliona kitu ndani ya Lea ambacho kimsingi hakikuweko ndani ya Raheli Mungu anaona kile ambacho wanadamu hawakioni, Lea hakuwa mzuri wa uso lakini alikuwa mzuri moyoni, Yule aliyeyependwa na aliyekuwa mzuri wa uso moyoni hakuwa ameshikamana na Mungu na aliibeba  kwa kuiiba miungu ya baba yake na alikufa baaadae kwa neno la Yakobo ona:-

Mwanzo 31:19-35 “Basi Labani alikuwa amekwenda kuwakata manyoya kondoo zake, na Raheli akaviiba vinyago vya babaye. Yakobo akamhadaa Labani, Mshami, kwa kuwa hakumwambia ya kwamba anakimbia. Basi akakimbia yeye na yote aliyokuwa nayo; akaondoka akauvuka mto, akaelekeza uso wake kwenda mlima wa Gileadi. Hata siku ya tatu Labani akaambiwa ya kwamba Yakobo amekimbia, akatwaa ndugu zake pamoja naye, akamfuata mwendo wa siku saba. Akampata katika mlima wa Gileadi. Mungu akamjia Labani, Mshami, katika ndoto ya usiku, akamwambia, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Labani akamfikia Yakobo, na Yakobo alikuwa amepiga hema zake katika mlima, na Labani na ndugu zake wakapiga hema zao katika mlima wa Gileadi. Labani akamwambia Yakobo, Umefanya nini? Umenihadaa, ukawachukua binti zangu kama mateka waliotwaliwa kwa upanga. Mbona umekimbia kwa siri ukanihadaa, wala hukuniambia, nipate kuagana nawe uende zako kwa furaha, na nyimbo, na ngoma, na kinubi? Wala hukuniacha niwabusu wanangu, na binti zangu; basi umetenda upumbavu. Ninao uwezo mkononi mwangu wa kukufanyia madhara; lakini Mungu wa baba yako usiku huu ameniambia, akisema, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Basi sasa, umetoka kwa sababu umetamani sana nyumba ya baba yako. Mbona basi umeiiba miungu yangu? Yakobo akajibu, akamwambia Labani, Kwa sababu naliogopa, nikasema, Usije ukaninyang'anya binti zako kwa nguvu. Awaye yote utakayemwona kuwa nayo miungu yako, yeye asiishi. Mbele ya ndugu zetu ukitambue kilicho chako kwangu, ukakichukue. Maana Yakobo hakujua ya kwamba Raheli ameiiba. Labani akaingia katika hema ya Yakobo, na hema ya Lea, na hema ya vijakazi wawili, wala hakuiona. Akatoka katika hema ya Lea, akaingia katika hema ya Raheli. Basi Raheli alikuwa amevitwaa vile vinyago ameviweka katika matandiko ya ngamia, na kuvikalia. Labani akapapasa hema yote wala hakuviona. Naye Raheli akamwambia babaye, Bwana wangu asikasirike kwa sababu siwezi kuinuka mbele yako, maana nimeshikwa na mambo ya kike. Akatafuta, wala hakuviona vile vinyago.”

Raheli alikuwa muabudu miungu, aliiba miungu ya baba yake Neno vinyago linalotajwa hapo katika Kiebrania linatajwa kama “Teraphim” ambao ni miungu midogo midogo yenye sura kama ya mwanadamu ambayo ilichongwa na kuabudiwa zamani hasa huko mashariki ya mbali na ambayo ilitumika kwa uganga na uchawi na kupigia ramli, miungu hii ilichongwa kwa mfano wa wanadamu na iliyorithiwa toka mababu na mababu na ilirithishwa kwa viongozi wa familia kwa hiyo kuwa na miungu hiyo kulimaanisha kutaka kuwa kiongozi wa familia  na Labani alipokuja kuulizia miungu hiyo Raheli aliificha, Yakobo bila kuelewa alimwambia  Labani yeye atakayekutwa na miungu yako na asiishi, tukio hili lilipelekea kifo cha mapema cha Raheli, Kumbe Lea alimuabudu Mungu wa kweli lakini Raheli miungu!

Mwanzo 35:16-18 “Wakasafiri kutoka Betheli, hata ukabaki mwendo wa kitambo tu kufika Efrathi, Raheli akashikwa na utungu wa kuzaa, na utungu wake ulikuwa mzito. Ikawa alipokuwa anashikwa sana na utungu, mzalisha akamwambia, Usiogope, maana sasa utamzaa mwanamume mwingine. Ikawa hapo katika kutoa roho yake, maana alikufa, akamwita jina lake Benoni, lakini babaye alimwita Benyamini.”

Je bado una huzuni ya kumkosa Raheli? Mungu alikuwa na mpango, sio kila Raheli ni Baraka na sio kila Lea ni Laana wakati mwingine Raheli ni tamaa yako na Lea ni mapenzi ya Mungu kwako, Mpango wa Mungu haujafichwa ndani ya kile unachikipenda bali uko ndani ya kile alichokupa, acha kutokukubaliana na Lea katika maisha yako, Lea sasa anahitaji upendo wako, ni muhimu sasa ukakubaliana na kile ambacho Mungu amekiruhusu katika maisha yako, ni lazima ukubali mapenzi ya Mungu na kutafuta kusudi la ndani la hali uliyo nayo, badala ya kujutia kile ulichonyimwa furahia kile ulichopewa na Mungu na kipokee kwa shukurani maana katika hilo uko mpango wa Mungu, Yesu anatoka kwa Lea na sio kwa Raheli, kile usichokipenda kinaweza kubeba hatima yako! Na kusudi la Mungu katika mpango wake, yako mambo tunaweza kuchagua na yako mambo Mungu mwenyewe anakuchagulia, furahia kile Mungu amekuchagulia, hakuna bahati mbaya katika kile Mungu amekupangia, oooo kumbe ni Lea badala ya Raheli.

Kusudi la Mungu kupitia Lea

Mungu anataka kutufunza hapa kuwa wakati mwingine katika hekima yake atafanya mambo kinyume na yale tunayoyatarajia ambayo kimsingi ni shauku na tamaa zetu au hisia zetu, Mungu anataka kuivunja ile hali ya kujitegemea katika maamuzi yetu anataka ukomavu anataka kurekebisha tabia zetu anataka kutuumbia moyo wa kuwa na uhusiano wa karibu sana na yeye ili tumtegemee yeye, hali hizo zote zinaruhusiwa kwaajili ya ukamilifu wetu kwa hiyo wale wote ambao wako katika hali kama ile aliyoipitia Yakobo wanapaswa kuelewa kuwa ni mchakao wa Mungu utimize mapenzi yake na sio ya kwako kwa hiyo fanya kwa upendo na uaminifu kile ambacho Mungu amekuchagulia.

Warumi 8:28-29 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi.”

Mungu anataka tuache kujitegemea na kujitumainia na badala yake tuishi kwa kumtegemea yeye, Mungu ataupiga chini mpango wetu wa ubinafsi na atabadilisha mambo ili tumtegemee yeye

2Wakorintho 12:7-9. “Na makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi. Kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba kinitoke.Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu.”

Mungu anataka utii hata katika mazingira magumu, kwa msingi huo badala ya kujiuliza kwanini mimi ninayapitia haya wewe jiulize Mungu atatukuzwaje kwenye jambo hili, Je kwa kuwa tumepewa uhuru wa kuchagua wadhani ya kuwa Mungu hana nafasi ya kuonyesha ubwana wake katika maisha yetu? Ubinafsi wetu na starehe zetu lazima zife linapokuja swala la kutimiza mpango wa Mungu, Kumbe ni Lea badala ya Raheli.

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni: