Ijumaa, 21 Machi 2025

Malipizo ya ndoa!


Mwanzo 20:3-7 “Lakini Mungu akamjia Abimeleki katika ndoto ya usiku, akamwambia, Umekuwa mfu wewe kwa sababu ya mwanamke huyu uliyemtwaa, maana ni mkewe mtu. Basi Abimeleki alikuwa hakumkaribia, akasema, Ee BWANA, Je! Utaua hata taifa lenye haki? Je! Hakuniambia mwenyewe, Huyu ni ndugu yangu? Na mwanamke mwenyewe naye alisema, Huyu ni ndugu yangu. Kwa ukamilifu wa moyo wangu, na kwa kuwa safi mikono yangu, nimefanya hivi. Mungu akamwambia katika ndoto, Nami nimejua ya kwamba kwa ukamilifu wa moyo wako umefanya hivi, ndipo nami nikakuzuia usinitendee dhambi, kwa hiyo sikukuacha umguse. Basi sasa umrudishe mwanamke kwa mtu huyo, maana yeye ni nabii, naye atakuombea, upate kuishi. Bali usipomrudisha, fahamu ya kwamba kwa hakika utakufa wewe na watu wote ulio nao.”



Utangulizi:

Leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu swala zima linalohusiana na Malipizo ya ndoa, Somo kuhusu malipizo ya ndoa ni mojawapo ya somo gumu ambalo, liko katika fungu la masomo yaitwayo chakula kigumu, na kwa sababu hiyo sio rahisi sana kupokelewa vema na hata kutendewa kazi linapokuwa limefundishwa au kuhubiriwa makanisani, hata hivyo hatuwezi kuacha kuisema kweli yote ya Mungu vilevile kama Neno la Mungu linavyoagiza, sisi tunahubiri agizo lote la Mungu (All Gospel)

Waebrania 5:11-14 “Ambaye tuna maneno mengi ya kunena katika habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa kusikia. Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi mmekuwa mnahitaji maziwa wala si CHAKULA KIGUMU. Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.”

Somo kuhusu malipizo ya ndoa linazungumzia katika ujumla wake swala zima la kumrejesha mume au mke ambaye kwa asili sio wa kwako, yaani kama unaishi na mke au mume ambaye sio wa kwako wewe ni dhalimu na unasababisha laana au madhara makubwa sana katika familia yako na mbele za Mungu na ni wazi kuwa ni vigumu sana kwako kuurithi ufalme wa Mungu na pia unaweza kufa! Au kupata majanga.

Yohana 4:16-18 “Yesu akamwambia, Nenda kamwite mumeo, uje naye hapa. Yule mwanamke akajibu, akasema, Sina mume. Yesu akamwambia, Umesema vema, Sina mume; kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako; hapo umesema kweli.”

Kwa msingi huo basi tutajifunza somo hili MALIPIZO YA NDOA kwa kuzingatia vipengele vitatu viuatavyo:-


·         Maana ya Malipizo

·         Kwa nini Malipizo ya Ndoa?

·         Faida za kufanya Malipizo ya Ndoa.


Maana ya Malipizo

Neno malipizo  Katika lugha ya kiyunani linatajwa kama neno “Epistrofi” au “apodidōmoi” ambalo kwa kiingereza tunapata neno Restitution au restoration au compensation au reparation ambalo kwa kiswahili ni kurejesha, kurudisha au kulipa au kufidia, Katika Lugha ya Kiebrania linatumika neno “shuv” ambalo maana yake ni kurudisha “to return” Neno hili katika mafundisho kuhusu wokovu linaenda sambamba na kazi ya toba au matokeo ya kutubu  na kusudi kubwa la jambo hili ni kutafuta amani au suluhu na ustawi wa kweli miongoni mwa jamii, malipizi au malipizo yanaweza kufanywa kwa sababu ya kurekebisha makosa ya zamani ikiwemo kama ulidhulumu, au ulikosea au ulimtakili mwenzi wako na mambo mengine, Malipizo ni sehemu ya mafundisho ya wokovu ambao msingi wake unaanzia katika torati na unakaziwa katika injili pia, tunaokolewa kwa imani na kwa neema baada ya kuamini na kutubu, hata hivyo malipizi ni sehemu muhimu ya kuonyesha toba yetu kivitendo kuelekea wengine!,

Luka 19:8-10 “Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne. Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Kwa msingi huo tunapata picha na kujifunza kuwa Malipizo ni matunda yatokanayo na toba, yaani kabla ya kukutana na Yesu, au kabla ya kuokoka au hata ndani ya wokovu kama ulimdhulumu mtu na baadaye ukatubu, toba yako itaambatana na kurejesha vile vitu ulivyodhulumu, kivitendo, kurejesha vitu vya watu ni tunda la kuonyesha jamii na Mungu badiliko kubwa ulilonalo la uamuzi wako wa kurejea kwa Mungu sawa tu na waganga na wachawi wanavyochoma vifaa vya kichawi na uganga! Baada ya kuokolewa kwao.

1Samuel 12:3-5 “Nami nipo hapa; basi, mnishuhudie mbele za Bwana, na mbele ya masihi wake,nalitwaa ng`ombe wa nani? au nalitwaa punda wa nani? au ni nani niliye mdhulumu? Ni nani niliyemwonea? Au kwa mkono wa nani nimepokea rushwa inipofushe macho? NAMI NITAWARUDISHIA NINYI. Nao wakasema, hukutudhulumu, wala hukutuonea, wala hukupokea kitu kwa mkono wa mtu awaye yote.  Akawaambia, Bwana ni shahidi juu yenu, na masihi

Walawi 6:2-5 “Mtu awaye yote akifanya dhambi, na kuasi juu ya BWANA, akamdanganya mwenziwe katika jambo la amana, au la mapatano, au la kunyang'anya, au kumwonea mwenziwe; au kuzumbua kitu kilichopotea na kutenda la uongo juu yake, na kuapa kwa uongo; katika mambo hayo yote mojawapo atakalolitenda mtu, na kufanya dhambi kwalo; ndipo itakapokuwa, akiwa amefanya dhambi, na kupata hatia, atarudisha hicho alichokipata kwa kunyang'anya, au kitu kile alichokipata kwa kuonea, au ile amana aliyowekewa, au kitu kile kilichopotea alichokizumbua yeye, au kitu cho chote ambacho amekiapia uongo; ATAKIRUDISHA HATA KWA UTIMILIFU WAKE, kisha ataongeza na sehemu ya tano zaidi juu yake; naye atampa huyo mwenyewe, siku hiyo ambayo atakapohukumiwa kuwa mwenye hatia.”

Kutoka 22:10-13 “Mtu akimpa mwenziwe punda, au ng'ombe, au kondoo, au mnyama ye yote, ili amtunzie; yule mnyama akafa, au akaumia, au akachukuliwa mtu asione; patakuwa na kiapo cha BWANA katikati ya watu hao wawili, kwamba alipeleka mkono wake kutwaa mali ya mwenziwe, na mwenyewe atakubali hayo, wala hatalipa. Lakini kwamba aliibiwa mnyama huyo, SHARTI AMLIPE YULE MWENYEWE. Kwamba aliraruliwa na mnyama mkali, na amlete uwe ushahidi; hatalipa kwa ajili ya mnyama aliyeraruliwa.”

2Samuel 12:1-6 “Ndipo Bwana akamtuma Nathani aende kwa Daudi. Naye akamwendea, akamwambia, Palikuwa na watu wawili katika mji mmoja; mmoja wao alikuwa tajiri, wa pili maskini. Yule tajiri alikuwa na kondoo na ng'ombe wengi sana; bali yule maskini hakuwa na kitu, ila mwana kondoo mmoja, mdogo, ambaye amemnunua na kumlea; naye akakua pamoja naye, na pamoja na wanawe; hula sehemu ya posho lake, na kukinywea kikombe chake, na kulala kifuani mwake, akawa kwake kama binti. Hata msafiri mmoja akamfikilia yule tajiri, naye akaacha kutwaa mmoja wa kondoo zake mwenyewe au mmoja wa ng'ombe zake mwenyewe, ili kumwandalia yule msafiri aliyemfikilia, bali alimnyang'anya yule maskini mwana-kondoo wake, akamwandalia yule mtu aliyemfikilia. Ndipo hasira ya Daudi ikawaka sana juu ya mtu yule; akamwambia Nathani, Aishivyo Bwana, mtu huyo aliyetenda jambo hili, HAKIKA YAKE ASTAHILI KUFA; NAYE ATAMRUDISHIA YULE MWANA-KONDOO MARA NNE, kwa sababu ametenda neno hili, na kwa sababu hakuwa na huruma.”

Filemoni 1:10-19 “Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye zamani alikuwa hakufai, bali sasa akufaa sana, wewe na mimi pia; niliyemtuma kwako, yeye mwenyewe, maana ni moyo wangu hasa; ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili. Lakini sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari. Maana, labda ndiyo sababu alitengwa nawe kwa muda, ili uwe naye tena milele; tokea sasa, si kama mtumwa, bali zaidi ya mtumwa, ndugu mpendwa; kwangu mimi sana, na kwako wewe zaidi sana, katika mwili na katika Bwana. Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe. NA KAMA AMEKUDHULUMU, AU UNAMWIA KITU, UKIANDIKE HICHO JUU YANGU. MIMI PAULO NIMEANDIKA KWA MKONO WANGU MWENYEWE, MIMI NITALIPA. Sikuambii kwamba nakuwia hata nafsi yako.

Kwa hiyo tunajifunza hapa kwamba watu waliompokea Yesu kama Bwana na mwokozi wa maisha yao aidha kabla au hata baada kama umedhulumu kitu chochote cha mtu basi baada ya toba unapaswa kukirudisha kitu hicho, au kukilipa au vitu hivyo kwa kufanya hivyo unaonyesha kuzaa matunda ya toba, rejesha vitu vyovote ambavyo ulidhulumu, kabidhi bunduki ulizokuwa ukizitumia kwa ujambazi polisi,vitabu ulivyoiba shuleni au Maktaba au ukiharibu kitu cha mtu, au kupoteza mali ya mtu ilipie kwa kufanya hivyo unaonyesha matunda ya toba na huko ndio kunaitwa kufanya malipizo au malipizi.

Mathayo 3:7-8 “Hata alipoona wengi miongoni mwa Mafarisayo na Masadukayo wakiujia ubatizo wake, aliwaambia, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja? Basi zaeni matunda yapasayo toba;

Ni katika hali kama hiyo kama umechukua na kukaa na mke wa mtu au unaishi na mume wa mtu ambaye aliolewa kihalali katika ndoa yake au kuoa kwa halali katika ndoa yake na kisha akaachana na mumewe au mkewe na ukawa unaishi naye wewe na mume huyo au mke huyo bado yu hai basi mwanamke huyo au mwanaume huyo umemchukua kwa dhuluma na kwa sababu hiyo unapaswa kufanya malipizo au marejesho ya ndoa, rudisha mwanamke huyo kwa mumewe, au rudisha mwanaume huyo kwa mkewe mwachie aende, toba ya kweli inahusisha kuacha dhuluma, na Mungu hafurahii udhalimu achia mke au mume wa mtu haraka! Hali kadhalika kwa fedha, mali, ardhi na vitu ulivyodhulumu virejeshwe haraka

Mwanzo 20:3-7 “Lakini Mungu akamjia Abimeleki katika ndoto ya usiku, akamwambia, Umekuwa mfu wewe kwa sababu ya mwanamke huyu uliyemtwaa, MAANA NI MKEWE MTU. Basi Abimeleki alikuwa hakumkaribia, akasema, Ee BWANA, Je! Utaua hata taifa lenye haki? Je! Hakuniambia mwenyewe, Huyu ni ndugu yangu? Na mwanamke mwenyewe naye alisema, Huyu ni ndugu yangu. Kwa ukamilifu wa moyo wangu, na kwa kuwa safi mikono yangu, nimefanya hivi. Mungu akamwambia katika ndoto, Nami nimejua ya kwamba kwa ukamilifu wa moyo wako umefanya hivi, ndipo nami nikakuzuia usinitendee dhambi, kwa hiyo sikukuacha umguse. BASI SASA UMRUDISHE MWANAMKE KWA MTU HUYO, maana yeye ni nabii, naye atakuombea, upate kuishi. BALI USIPOMRUDISHA, FAHAMU YA KWAMBA KWA HAKIKA UTAKUFA WEWE NA WATU WOTE ULIO NAO.”

Kwa hiyo neno la Mungu katika kanuni zake linatuelekeza kufanya malipizo ya kitu chochote ambacho tunakaa nacho pasipo haki, Lengo kuu la kufanya malipizo ni kutafuta kwa bidi kuwa na amani na watu wote, kutenda haki, na kuonyesha badiliko la kweli lililofanywa na Mungu ndani ya mioyo yetu, kwa hiyo ni vema kurudisha chochote ulichoiba, ulichodhulumu, lipa madeni ya kila unachodaiwa, fanya marekebisho makubwa ya kitabia, malipizo ni sehemu ya toba na sehemu muhimu ya wokovu wetu, tunafanya hayo ili tusilaumiwe katika mioyo yetu na rehema za Mungu ziwe juu yetu na tuweze kusamehewa,  na kusamehe, lakini kubwa zaidi tusiwe kwazo la namna yoyote wala  watu wa kulaumiwa!

“2Wakorintho 6:3-4 “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe; bali katika kila neno tujipatie sifa njema, kama watumishi wa Mungu; katika saburi nyingi, katika dhiki, katika misiba, katika shida;”           

Kwa nini Malipizo ya Ndoa?

Unaweza kujiuliza ni kwa nini Malipizo ya ndoa?, Ni muhimu kufahamu kwa kina na mapana na marefu ni kwanini Maandiko yazungumzia swala zima la Malipizo na pia kwa nini tuzungumzie malipizo ya ndoa? Kwaajili ya kujibu swala hilo ni lazima kwanza kupata ufafanuzi wa jinsi na namna Mungu ambaye ndiye mwanzilishi wa ndoa anavyoichukulia ndoa.

Ndoa ni taasisi iliyoasisiwa na Mungu katika bustani ya Edeni ambapo Mungu alimuumba mtu mke na mtu mume na kuwabariki kuwa wakazae na wakaongezeke, Kwa sababu hiyo ndoa ni utaratibu uliowekwa na Mungu kwaajili ya upatikanaji wa familia, taifa na jamii, ndoa imekusudiwa kuwa taasisi ya kudumu mpaka kifo na ndoa ni ya jinsia mbili tofauti ya kike na ya kiume na imethibitishwa na Yesu Kristo. Miaka ya zamani hakukuwa na vyeti vya ndoa au ndoa zilikuwa hazisajiliwi, lakini kijamii zilikuweko ndoa za kimila na zote Mungu aliziheshimu, kwa sababu hiyo Mungu katika mtazamo wake huziona ndoa zote kuwa ni halali endapo zimefuata utaratibu wowote uwe wa kimila, kikabila, kidini, kiislamu, kikristo, kibudha, kihindu, kienyeji, kiserikali na kadhalika, jambo kubwa la msingi la kujiuliza ni kama unataka kuoa au kuolewa je yule unayemuoa au anayekuoa hajawahi kuwa na ndoa nyingine? Jiulize alioa kwanza? Aliolewa kwanza? Je mumewe au mkewe yu hai? Kwa sababu wale wanaooana wanaingia kwenye kifungo cha maisha na kuwako kwa cheti hakuifanyi ndoa hiyo kuwa halali kama mambo ya msingi ya kujua kama mwanaume huyo au mwanamke huyo hana kifungo kingine cha ndoa, au kama alikuwa na mtu mwanzoni.

Mathayo 19:4-10 Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe. Wakamwambia, Jinsi gani basi Musa aliamuru kumpa hati ya talaka, na kumwacha? Akawaambia, Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi. Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini. Wanafunzi wake wakamwambia, Mambo ya mtu na mkewe yakiwa hivyo, haifai kuoa.” 

1Wakorintho 7:10-11 “Lakini wale waliokwisha kuoana nawaagiza; wala hapo si mimi, ila Bwana; mke asiachane na mumewe; lakini, ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe.”

Ndoa ilikusudiwa na Mungu iwe taasisi ya kudumu na uwezekano wa kuwa huru unaweza kutokea ikiwa tu kifo kimejitokeza na sio vinginevyo, kwa hiyo mwanaume au mwanamke atakuwa huru kuoa au kuolewa na mwingine endapo mwenzi wake atafariki dunia, kwa hiyo ndoa iwapo duniani ni ya kudumu na Mungu hatambui kuvunjika kwa ndoa duniani

1Wakorintho 7:39 “Mwanamke hufungwa maadamu mumewe yu hai, lakini ikiwa mumewe amefariki, yu huru kuolewa na mtu ye yote amtakaye; katika Bwana tu.”

Warumi 7:2-3 “Kwa maana mwanamke aliye na mume amefungwa na sheria kwa yule mume wakati anapokuwa yu hai; bali akifa yule mume, amefunguliwa ile sheria ya mume. Basi wakati awapo hai mumewe, kama akiwa na mume mwingine huitwa mzinzi. Ila mumewe akifa, amekuwa huru, hafungwi na sheria hiyo, hata yeye si mzinzi, ajapoolewa na mume mwingine.”    

Unaweza kuona kama mwanamke aliolewa na mumewe akiwa hai, na mwanamke huyo akaolewa na mwanaume mwingine mwanamke huyo huitwa mzinzi, kwa hiyo Mungu katika mpango wake anatambua kuwa kifo peke yake ndicho kinachoweza kumuweka huru mtu mbali na ndoa yake kwa hiyo uhakikisho wa kuwa mtu huyo yuko huru ni lazima ufanyike kabla watu hawajaingia katika agano la ndoa, na ili mtu asiishi na mke wa mtu au mume wa mtu iko haja ya kupata kibali cha wazazi hasa wa mwanamke hata kama ni ndoa ya kimila wazazi wa mwanamke wakithibitisha kuwa mwanamke huyu yuko huru kuolewa anaweza kuolewa.

Mwanzo 24:54-57 “Wakala wakanywa, yeye na watu waliokuwa pamoja naye, nao wakakaa usiku. Wakaondoka asubuhi, naye akasema, Nipeni ruhusa niende kwa bwana wangu. Ndugu yake na mama yake wakasema, Msichana na akae kwetu kama siku kumi, zisipungue, baadaye aende. Naye akawaambia, Msinikawilishe, mradi BWANA amefanikisha njia yangu; nipeni ruhusa niende kwa bwana wangu. Wakasema, Na tumwite huyo msichana, tumwulize mwenyewe. Wakamwita Rebeka wakamwuliza, Je! Utakwenda na mtu huyu? Akasema, Nitakwenda. Ndipo wakampeleka Rebeka ndugu yao, na yaya wake, na mtumishi wa Ibrahimu, na watu wake.”

Katika mtazamo wa Mungu ndoa ilikusudiwa na Mungu iwe ya milele, kwa hiyo Mungu hakubaliani na swala la talaka, swala la talaka linaweza kufanywa kimahakama na hakimu au na kadhi, lakini swala la kuachana halina uhusiano na viongozi wa kidini na kiimani, kwa sababu maandiko yanakataza kuachana, Mungu anachukia kuachana, Kimsingi Mungu hamtegemei mtu aliyemuamini yeye kuwa na ndoa itakayovunjika, wala ndoa ya kikristo haijawahi kukusudiwa kuwa ya watu wengi, kuachana na kutalikiana kunaonyesha uchanga wa kiroho, upofu wa kiimani, ukosefu wa ukomavu, hitaji la kimsaada, kushindwa kumtii Mungu na kuchukuliana na wanadamu wengine wenye udhaifu, au kushindwa kuvumilia, au kukosekana kwa upendo, kuachana ni hiyana, kuachana ni kushindwa kusamehe, kuachana ni kushindwa kupatana ni kushindwa kuwa na amani na watu wote, ni uwezo mdogo wa kutatua migogoro, ni changamoto ya kiadilifu.

Mwanzo 2:22-24 “na ule ubavu alioutwaa katika Adamu BWANA Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa Adamu. Adamu akasema, Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume. Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.”

Mathayo 19:4-10 Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe. Wakamwambia, Jinsi gani basi Musa aliamuru kumpa hati ya talaka, na kumwacha? Akawaambia, Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi. Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini. Wanafunzi wake wakamwambia, Mambo ya mtu na mkewe yakiwa hivyo, haifai kuoa.”

Malaki 2:13-16 “Tena mnatenda haya nayo; mnaifunikiza madhabahu ya Bwana kwa machozi, kwa kulia na kwa kuugua, hata asiiangalie tena hiyo dhabihu, wala kuitakabali mikononi mwenu na kuiridhia. Lakini ninyi mwasema, Ni kwa sababu gani? Ni kwa sababu Bwana amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana, angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako. Hakuna mtu mmoja aliyetenda hivi, ambaye alikuwa na ufahamu kidogo. Au je! Kuna mtu mmoja atafutaye mzao mwenye kumcha Mungu? Kwa hiyo jihadharini roho zenu; mtu awaye yote asimtende mke wa ujana wake mambo ya hiana. Maana mimi nakuchukia kuachana, asema Bwana, Mungu wa Israeli; naye aifunikizaye nguo yake kwa udhalimu namchukia, asema Bwana wa majeshi; basi jihadharini roho zenu, msije mkatenda kwa hiana.”

Neno la Mungu linatufundisha ya kuwa kinachoweza kuvunjwa ni uchumba tu, uchumba unaweza kuvunjwa na kumuacha kila mmoja huru kwa sababu tu ya uasherati, yaani mfano kama umeposa mtu mke au umemchumbia na kabla ya ndoa ikabainika kuwa mke huyo sio muaminifu kwa maswala ya ngono mke huyo (Mchumba) unaweza kumuacha, Biblia ya Kiebrania inatumia neno mke kuanzia katika hatua ya awali ya uchumba, kwa mfano Yusufu na Mariamu waliokuwa wamechumbiana, Yusufu alipoona mkewe au mchumba wake ana mimba yeye aliamua kumuacha kwa siri kwa hiyvo maandiko hayatumii neno mchumba kwa sababu neno mchumba katika kiebrania haliko bali yanatumia neno mke kwa hiyo kama mke au mchumba au mwanamwali “arusa” akionekana amefanya uasherati basi uchumba au uhusiano huo ungevunjika, lakini swala la kuachana haliwezi kufanyika baada ya kuoana ambako kimsingi ni agano.

Mathayo 1:18-20 “Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri. Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu.”          

Kumbukumbu 22:22-25 “Akifumaniwa mtu mume amelala na mwanamke aliyeolewa na mume, na wafe wote wawili, mtu mume aliyelala na mwanamke, na yule mwanamke naye; ndivyo utakavyoondoa uovu katika Israeli. Pakiwa na kijana aliye mwanamwali ameposwa na mume, na mwanamume akimkuta mjini, akalala naye; watoeni nje katika lango la mji ule, mkawapige kwa mawe hata wafe; yule kijana, kwa kuwa hakupiga ukelele, naye yu ndani ya mji; na yule mume, kwa kuwa amemtweza mke wa mwenzake; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako. Lakini yule mtu mume kama akimkuta kondeni kijana aliyeposwa, naye mume akamtenza nguvu, akalala naye; yule mtu mume aliyelala naye na afe pekee;”           

Kwa kuwa ni mpango wa Mungu ndoa kutokuvunjika ni muhimu kufahamu kuwa hata mtu anapookoka mmoja na mwingine ikawa bado hiyo sio sababu ya muhimu kuachana Mungu ametuita katika Amani, wengi wa wale wanaoachwa kwa sababu ya wokovu wanaachwa kwa sababu ya kukosa hekima, unakaa sana kanisani na kupuuzia usimamizi wa nyumba yako, unakosa kiasi, unaonyesha heshima kubwa kwa mchungaji wako kuliko mume wako na ujinga ujinga mwingine, lakini hata nyumbani unaangalia sana program za tv za wahubiri fulani bila kuweka uwiano wa kuwaachia na wengine waangalie mambo yao, aina hizi za wokovu wa kipumbavu wa kutokutumia akili au kukosa hekima kumesababisha migogoro mikubwa baada ya watu kuokoka, viongozi wa kiroho weka ratiba, tunza muda waachie watu waende majumbani kwao kwa waume zao na watoto wao, ukichagua viongozi basi zingatia sana mahusiano yake nyumbani kama mumewe hataki mwachie huru mtu wa watu! Ili wewe usiwe sababu ya migogoro hiyo!

Maandiko yamekataza talaka katika agano jipya, Mungu anachukia kuachana na kwa sababu hizo endapo watu wataachana neno la Mungu linawataka wakae hivyo hivyo au wapatane warudiane lakini wasiachane, hii maana yake kwa kuwepo kwetu duniani, inaweza kutokea watu wakahitilafiana kiasi cha kutengana na kujitafuta kwa muda na kujitafakari na baada ya mioyo kupoa basi watu hao na wapatane na warudiane.

1Wakorintho 7:10-11 “Lakini wale waliokwisha kuoana nawaagiza; wala hapo si mimi, ila Bwana; mke asiachane na mumewe; lakini, ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe.”

1Wakorintho 7:12-16 “Lakini watu wengine nawaambia mimi, wala si Bwana, ya kwamba iwapo ndugu mmoja ana mke asiyeamini, na mke huyo anakubali kukaa naye asimwache. Na mwanamke, ambaye ana mume asiyeamini, na mume huyo anakubali kukaa naye, asimwache mumewe. Kwa maana yule mume asiyeamini hutakaswa katika mkewe; na yule mke asiyeamini hutakaswa katika mumewe; kama isingekuwa hivyo, watoto wenu wangekuwa si safi; bali sasa ni watakatifu. Lakini yule asiyeamini akiondoka, na aondoke. Hapo huyo ndugu mume au ndugu mke hafungiki. LAKINI MUNGU AMETUITA KATIKA AMANI. Kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? Au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo?

Kwa msingi huo sasa Malipizo ya ndoa yanatupa nafasi ya kujitafakari Kama tunaishi na mume wa mtu au mke wa mtu? Wokovu wetu unaweza kulaumiwa na uadilifu wetu kutiliwa mashaka endapo umeokoka lakini mke au mume unayeishi naye sio wa kwako na zaidi ya yote unaishi katika zinaa na hauwezi kamwe kuurithi ufalme wa Mungu kutokana na kuishi kwako katika zinaa na mume au mke asiyekuwa halali kwako

1Wakorintho 6:8-10 “Bali kinyume cha hayo ninyi wenyewe mwadhulumu watu na kunyang'anya mali zao; naam, hata za ndugu zenu. Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang'anyi.”

Mungu ametuita katika Amani, maana yake sio mpango wake aokoe mmoja alafu itokee Muachane kwa sababu ya wokovu, kwa msingi huo bado Mpango wa Mungu uko vile vile katika swala la kutikuachana kwa sababu Paulo alitioa maoni yake na sio agizo la Bwana

Faida za kufanya Malipizo ya Ndoa.

Malipizo ya ndoa yana faida gani?  Yanasaidia nini? Malipizo ya ndoa ni sehemu muhimu ya theolojia ya uadilifu (Moral theology) tunapoifanyia kazi inaonyesha kujutia kwetu kwa dhati na maamuzi yetu ya kubadilika kiimani na kimaadili, malipizo ni kama tiba inayofanyika au tunayoifanya kwa watu ambao tumewajeruhi,  hatuwezi tu kupuuzia na kudai kuwa tunampenda Mungu huku kuna watu wanaumia na kukumbuka kuwa umemchukulia mumewe au umemchukulia mkewe na uko naye na unaendelea naye huku unadai umeokoka, kwa hiyo ni kama unaamua kumuabudu tu Mungu huku kuna mtu una shida naye au ana shida na wewe!, unawezaje kabisa kujikausha katika wokovu huku unamiliki mume au mke asiyekuwa wako? Hapo unaendeleza zinaa bila kujali ni baraza gani limepitisha swala lako.

Malipizo ni sehemu muhimu sana ya mafundisho ya wokovu ambayo makanisa mengi wanaikaushia na kuwaacha watu waende motoni kwa kutokuwakumbusha watu hao kutenda haki, kutenda kwetu haki ni pamoja na kuwaomba radhi wale tuliowakosea, kurejesha vitu vyao tulivyodhulumu na kuwarejeshea wake zao au waume zao ambao tumewachukua kibabe au kwa tamaa zetu au hata kwa kuhalalisha talaka kimahakama. Unamuona baba yule au mama yule anajifanya kaokoka lakini anaishi na mke wa mtu au mume wa mtu! Ushuhuda wa aina hii unaifanya injili kukutana na wakati Mgumu, kila anayeoa ni lazima ajue wazi na mapema kuwa ndoa sio swala la kuchukulia mzaha!

Unapoendelea kukaa na mume wa mtu au mke wa mtu unakiuka agizo la Mungu na katazo lake kwani ndoa huunganishwa na Yeye mwenyewe na wewe unafanya ukaidi na kusimama mahali ambapo utahukumiwa, andiko limesema alichokiunganisha Mungu mwanadamu asikitenganishe wewe ndiye huyo mwanadamu sasa uliyetenganisha ndoa ya watu, tarajia hukumu ya kutisha kutoka kwa Mungu aliye hai asiyedhihakiwa! Endapo unaishi na mke wa mtu au unaishi na mume umetenganisha kile Mungu alichokiunganisha.

Marko 10:6-9. “Lakini tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke. Kwa sababu hiyo mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja; hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi ALICHOKIUNGANISHA MUNGU, MWANADAMU ASIKITENGANISHE.”

Malipizo ni tunda la toba ya kweli, Zakayo alipopokea wokovu moja kwa moja aliyajua mapenzi ya Mungu na kuamua kurejesha vile alivyodhulumu na Yesu alithibitisha kuwa huu ndio wokovu wa kweli, unaokokaje huku umeacha mkeo? Umeacha mumeo? Unakaa na mali ya watu au unaona sawa sawa hapo ni mene mene tekeli na peresi

Luka 19:8-10. “Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne. Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu.Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Malipizo ni maonyo kwa watu wasiokaa kwa utaratibu, Mungu wetu ni Mungu wa utaratibu, kama kanisa litatoa mpenyo na njia rahisi ya watu kuachana na kuoa tena kama watakavyo, au kuachwa na kuolewa tena kama watakavyo tutatoa mpenyo kwa watu kuishi bila utaratibu, na kujifanyia kama watakavyo na hata kufikia hatua ya kushika ngazi za juu za kimaongozi katika kanisa huku wakiwa na historia mbaya ya ndoa zao, ni lazima kanisa lichukue hatua barabara na kusimama kama Yesu mwenyewe alivyoweka msimamo mkali katika swala zima la ndoa. Ni lazima watu waishi kwa utaratibu.

1Wathesalonike 5:14-15 “Ndugu, twawasihi, waonyeni wale wasiokaa kwa utaratibu; watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge; vumilieni na watu wote. Angalieni mtu awaye yote asimlipe mwenziwe mabaya kwa mabaya; bali siku zote lifuateni lililo jema, ninyi kwa ninyi na kwa watu wote.

Malipizo ni ishara ya kuwa sasa unataka Amani na unaitafuta Amani kwa bidii, neno la Mungu limetuagiza kutafuta Amani kwa bidii, kutafuta Amani sio swala jepesi na wala haliji kwa maombi linakuja kwa sisi kuachukua hatua madhubuti na wakati mwingine kuingia gharama kubwa sana kuitafuta Amani.

Waebrania 12:14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao;”   

Warumi 12:17-18. “Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.”

Malipizo ni utii wa amri ya pili iliyokuu kivitendo isemayo Mpende jirani yako kama nafsi yako, na ile sheria ya dhahabu inayosema watendeeni wengine yale mnayotaka nanyi mtendewe, ama siwatendee wengine mambo ambayo hungependa nawe utendewe!

Mathayo 22:37-39 “Akamwambia, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako.”

Luka 6:31 “Na kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”

Malipizo yanatukumbusha gharama ya dhambi na kutuhakikishia kuwa hatuna mpango tena wa kuishi katika dhambi na hatia na hatuko tayari tena kuyarudia matapishi, kwamba ulifanya upumbavu na hutaki kufanya upumbavu tena, Malipizo ni kujitia nidhamu ni kujiadhibu na kujiwekea msingi kuwa haitakuja urudie tema makosa kama yale  

Mithali 26:11 “Kama vile mbwa arudiavyo matapiko yake; Kadhalika mpumbavu afanya upumbavu tena.

Malipizo ni kufanya masahihisho ya makosa tuliyoyafanya kwa Mungu na kwa wahusika tuliowakosea zamani ili tuweze kuwa na dhamiri njema isiyo na hatia mbele za Mungu na wanadamu na watu wote wanaotuzunguka ili tusilaumiwe kwa habari ya karama hii tunayoitumikia yaani wokovu, kama sisi ni watumishi wa Mungu au watu tuliookolewa na tunaishi na mke au mume asiyekuwa wakwako, jamii inapata kigugumizi na inashindwa kukuelewa kuwa wewe ni mtu wa namna gani na uhusiano wako na Mungu ukoje ikiwa utakuwa na madai ya kumcha Mungu huku una mume au mke wa mtu!

Matendo 24:16 “Nami ninajizoeza katika neno hili niwe na dhamiri isiyo na hatia mbele za Mungu na mbele ya watu siku zote.”

Matendo 26:20bali kwanza niliwahubiri wale wa Dameski na Yerusalemu, na katika nchi yote ya Uyahudi, na watu wa Mataifa, kwamba watubu na kumwelekea Mungu, WAKIYATENDA MATENDO YANAYOPATANA NA KUTUBU KWAO.”      

2Wakorintho 8:20-21 “Tukijiepusha na neno hili, mtu asije akatulaumu kwa habari ya karama hii tunayoitumikia; tukitangulia kufikiri yaliyo mema, si mbele za Bwana tu, ila na mbele ya wanadamu.        

Malipizo hutusaidia kusonga mbele, yanasababisha ujisamehe mwenyewe na kukupa fursa ya kuwa huru kwa Mungu na kuyafanya maombi yako yasizuiliwe, Malipizo hudhihirisha upendo wa kweli, na kinyume chake ni kudhihirisha kuwa hatuna upendo kufanya huduma, kuhubiri, kuomba sana kuwa na vyeo vikubwa katika madhehebu yetu kote kunaweza kuhesabika kuwa hakuna maana Mbele za Mungu na wanadamu kama kuna watu tumewajeruhi na kuwaumiza na kujikausha huku tukijifanya tunaendelea mbele na Mungu wetu, Mungu hadhiakiwi iko siku utavuna kile ulichokipanda, dua zako na maombi yako na kila ulifanyalo ni bure kama huna upendo, kama hujali kuwa kuna watu wanaugua na kupata shida kwaajili yako, manabii wengi, na mitume wengi na waimbaji wengi wa injili wengi wameacha wake zao wa awali na wameoa wengine, huku wakiendelea kutumiwa na Mungu na kusifiwa huku na kule lakini wake zao wanalia na watoto wao wanalia, wengine wana watoto hawawajali wala hawawatunzi na ili hali wao wana mafanikio makubwa sana somo hili linakuja kwako kukutaka uwe mkristo wa kweli na usimame katika kweli vinginevyo njia ya jehamnamu ni nyeupe sana haijalishi unafanya nini.

1Wakorintho 13:1-8 “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu. Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote. Upendo haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika.”

Hitimisho:

Baada ya kuwa tumefahamu hayo hatuna budi kutambua kua mtu anayekua kwenye uzinzi hawezi kurithi ufalme wa Mungu. Kwa msingi huo kama unajitambua kuwa una malipizi ya ndoa basi ni muhimu kwako kuyafanyia kazi maneno haya, hata hivyo hekima ya kiungu inahitajika sana katika kuchukua maamuzi haya, lakini usipochukua unahesabika miongoni mwa wadhalimu na hautaurithi ufalme wa mbinguni.

1Wakoritho 6:9-10 “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang'anyi.”

kwa msingi huo itatupasa kuhesabu gharama kabla na kujenga mnara na kujipima na kujiangalia ili tuchague kuingia mbinguni au la, Zaidi ya yote omba sana Amani ya Mungu itamalaki na kukuwezesha kutii maagizo haya magumu ambayo ni mifupa katika mafundisho ya wokovu, ni mafundi9sho magumu kwa sababu yanagusa hisia na mwingiliano wa kisaokolojia lakini hatuna budi kumtii Mungu kuliko nafsi zetu. 

Yohana 14:27 “Amani nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga.”

Watumishi wa Mungu tuisimamie kweli, Mungu hapokeii uso wa mwanadamu, tuache kujifanya kuwa sisi ni miungu na kuwa tunaweza kutangua neno la Mungu au kulibadilisha kwa kuwaachia watu waishi watakavyo, tunaweza kupoteza watu wengi na kuwacha waende jehanamu au kufa wakiwa wameacha utata duniani ikiwa haijulikani kama wako mbinguni au motoni, lililotukuka kwa wanadamu ni chukizo kwa Mungu hebu tuisimamie kweli na kuwaonya watu vinginevyo damu zao na roho zao zitadaiwa mikononi mwetu, tujifunze kujua taarifa za watu kwa usahihi iwe ni washirika au wachungaji ili tusifanye makosa ya kupoteza roho za watu kwa kuwapaka mafuta ili hali tungewaeleza ukweli wangeweza kupona na kwenda Mbinguni, awezae kulipokea neno hili na alipokee lakini Mungu atatudai damu ya watu ambao amewaleta karibu yetu na tukashindwa kuwaambia ukweli kwa kuogopa kuwakwaza. Mimi nimenawa!

Ezekiel 33:7-9. “Basi wewe, mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli; basi ulisikie neno hili kinywani mwangu, ukawape maonyo yangu. Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa, nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa roho yako.”

 

Na. Rev Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!           

Alhamisi, 13 Machi 2025

Umuhimu wa kuwa na Amani na watu wote!


Waebrania 12:14-15 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”




Utangulizi:

Moja ya kanuni za muhimu sana katika ufalme wa Mungu ni pamoja na swala zima la kuhakikisha kuwa unakuwa na amani na watu wote, Maandiko yanatoa wito wa kufanya bidii kutafuta Amani na watu wote, Hili ni jambo la Msingi, Kwa kuwa tuko duniani kuzuka na kutokea kwa migogoro ni swala la kawaida sana katika jamii hususani watu wanapoishi pamoja, lakini hata hivyo kama watu wa Mungu au watu wenye ukomavu hatupaswi kuiacha migogoro hiyo ikadumu kwa Muda mrefu na kuwatia unajisi watu wengine, Migogoro katika maandiko inafananishwa na shina la uchungu, shina ni chanzo, na kwa sababu hiyo mti wowote ambao shina lake litakuwa chungu, ni rahisi mti huo kueneza uchungu katika matawi yake na au hata katika matunda yake na kwa sababu hiyo katika ukuaji wa kiroho migogoro huathiri utiririkaji wa neema ya Mungu na kuleta upungufu wa neema ya Mungu katika maisha ya waamini, Lakini tunapofanya bidii ya kutafuta Amani tunazuia uchungu huo na kujiimarisha kuwa wana wa Mungu

Mathayo 5:9 “Heri wapatanishi; Maana hao wataitwa wana wa Mungu.” Neno wapatanishi hapo katika lugha ya asili ya kiyunani linasomeka kama “eirēnopoios” kwa kiingereza “peacemakers” wanaosababisha amani itokee au iwepo hao ni watu wenye baraka kubwa, wamebarikiwa sana kama maandiko yanenavyo na kiyume chake wanaosababisha makwazo wanaitwa ole yaani waliolaaniwa na ambao adhabu kubwa sana inaweza kuwakabili.

Luka 17:1-4 “Akawaambia wanafunzi wake, Makwazo hayana budi kuja, lakini ole wake mtu yule ambaye yaja kwa sababu yake! Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa wadogo hawa. Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe.”

Wakiyajua haya wazee wetu wa imani zamani sio kuwa hawakuwahi kukutana na migogoro ya ina mbalimbali walikutana nayo lakini walikuwa na bidii kuhakikisha kuwa wanarejesha amani au kuepusha kabisa migogoro miongoni mwao wakitumia busara kubwa sana, kwa sababu hiyo maandiko yanamtaka kila mmoja wetu kuhakikisha kuwa anatunza amani kila wakati kunapotokea migogoro ya aina mbalimbali au kuzima kwa haraka migogoro na vyanzo vinavyoashiria kutoweka kwa Amani kabla mambo hayajaharibika kabisa, Katika maandiko iko mifano ya watu kama kina Abrahamu, Isaka, na Yakobo na wengineo ambao kwa namna moja ama nyingine walifanya kila jitihada ya kuhakikisha kuwa wanadhibiti migogoro na kutafuta Amani ya kudumu katika maisha yao ya uchaji Mungu na uhusiano na watu wengine, tutajifunza somo hili umuhimu wa kuwa na amani na watu wote kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Mifano ya wazee waliotafuta kuwa na amani na watu wote

·         Baraka ya kuwa na amani na watu wote

·         Umuhimu wa kuwa na amani na watu wote  


Mifano ya wazee waliotafuta kuwa na amani na watu wote.

Neno Amani linalotumika katika maandiko kwa agano la kale linatumika neno la kiibrania “Shālōm” na katika maandiko ya agano jipya linatumika neno “eirēne” kimatamshi “Irene” maneno haya katika tafasiri ya kiingereza maana yake ni “it is a condition of being freedom from any kind of disturbance wether outwardly or inwardly” yaani ni hali ya kuwa mbali na usumbufu wa aina yoyote wa nje au wa ndani, usumbufu huu unaweza kuwa wa nafsi au familia, au taifa na kadhalika, neno hilo Shālōm pia lilitumiwa na Wayahudi kumtakia mtu mafanikio ya kimwili na kiroho na lilitumika katika matumizi ya kila siku ya kumtakia mtu mema wakati wa salamu, kwa hiyo hii hasa ndio Amani na utulivu au hali ya kutokuwa na vita au uhasama au ugomvi na mtu na hii ndio Amani ambayo maandiko yanaagiza tuwe nayo na watu wote, Amani hii ni msingi mkubwa wa mafanikio na ustawi mkubwa wa mwanadamu popote alipo duniani.

Maandiko yana mifano mingi inayoonyesha kuwa wazee wetu katika kusafiri kwao duniani walikutana na changamoto za namna mbalimbali ambazo zingeweza kuharibu amani na maisha yao pia, lakini katika namna ya kushangaza sana maandiko yanatuonyesha namna na jinsi wazee wetu walivyokuwa na busara na hekima iliyopelekea wao kuepusha changamoto za aina mbalimbali ambazo zingeweza kuwa sababu ya ukosefu wa amani katika maisha yao duniani na kwa sababu hiyo walifanya kila linalowezekana kuhakikisha kuwa wanapata Amani hata pale ilipotokea wamehitilafiana na mtu, hapa iko mifano kadhaa ya watu walioitafuta Amani kwa bidi ona:-

Mfano wa Ibrahimu na Lutu.

Mwanzo 13:5-12 “Na Lutu aliyesafiri pamoja na Abramu, yeye naye alikuwa na makundi ya ng'ombe na kondoo, na hema. Na ile nchi haikuwatosha, ili wakae pamoja; maana mali zao zilikuwa nyingi, hata wasiweze kukaa pamoja. Kukawako ugomvi kati ya wachunga wanyama wa Abramu, na wachunga wanyama wa Lutu; na siku zile Wakanaani na Waperizi walikuwa wakikaa katika nchi. Abramu akamwambia Lutu, Basi, usiwepo ugomvi, nakusihi, kati ya mimi na wewe, wala kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako; maana sisi tu ndugu. Je! Nchi hii yote haiko mbele yako? Basi ujitenge nami, nakusihi; ukienda upande wa kushoto, nitakwenda upande wa kuume; ukienda upande wa kuume, nitakwenda upande wa kushoto. Lutu akainua macho yake, akaliona Bonde lote la Yordani, ya kwamba lote pia lina maji, kabla BWANA hajaharibu Sodoma na Gomora, lilikuwa kama bustani ya BWANA, kama nchi ya Misri hapo unapokwenda Soari. Basi Lutu akajichagulia Bonde lote la Yordani; Lutu akasafiri kwenda upande wa mashariki; wakatengana wao kwa wao. Abramu akakaa katika nchi ya Kanaani, na Lutu akakaa katika miji ya lile Bonde; akajongeza hema yake mpaka Sodoma.”

Wachungaji wa Abrahamu na Lutu walianza kugombana kwa sababu mifugo yao ilikuwa imeongezeka sana kiasi ambacho nchi ilikuwa haiwatoshi kwa sababu walikaa pamoja, Abrahamu aliona wazi kuwa jambo hili lisingelileta matokeo mema na kwa sababu hiyo alimwita Lutu na kutoa mapendekezo kwa kumsihi ajitenge naye, Abrahamu hakuwa na choyo wala ubinafsi alimpa Lutu chaguo la kwanza kuchagua na kumueleza wazi kuwa endapo atachagua kwenda kushoto yeye atakwenda kulia na akichagua kwenda kulia yeye atachagua kwenda kushoto, hakukuwa na ubinafsi moyoni lakini msingi mkuu ulikuwa ni USIWEPO UGOMVI KATI YA MIMI NA WEWE  MAANA SISI NI NDUGU, Abrahamu aliipa Amani kipaumbele cha kwanza kuliko maslahi binafsi. Aliamini kuwa Mungu atambariki vyovyote iwavyo bila kujali chaguo lake litamuathiri kwa kiwango gani:-

Amani ya kweli haipatikani kwa kushinda siku zote inapatikana kwa unyenyekevu na kuwa tayari kupoteza haki zako na wakati mwingine hata mazuri tuliyokuwa tukiyatarajia kwa faida ya Amani yenyewe kuliko mafarakano, Amani wakati mwingine inatutaka kumuachia Mungu na sisi kujitoa ili Amani iwe faida ya pande zote mbili, kumpata ndugu yako ni kwa muhimu sana kuliko faida za ubinafsi na tamaa ya moyo! Nyakati tulizo nazo leo wako watu ambao wako tayari kupoteza ndugu na marafiki kuliko kuitafuta Amani, Maandiko yanatufunza kuwa Amani ni ya muhimu kuliko kupoteza ndugu au rafiki na hiki ndio Abrahamu anatufundisha katika maisha yake.

1Wakorintho 8:13 “Kwa hiyo, chakula kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele, nisije nikamkwaza ndugu yangu.”

Mfano wa Isaka na Wafilisti (wenyeji).

Mwanzo 26:12-22 “Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi. Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko. Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”

Isaka alikuwa na mafanikio makubwa sana alistawi mno, jambo hili liliamsha wivu kwa wenyeji yaani wafilisti walijaribu kutafuta na kufukia siri ya mafanikio ya Isaka, Isaka alikuwa akichimba visima yeye na Abrahamu baba yake walikuwa na ujuzi wa kuchimba visima, Isaka alipata visima vilivyobubujisha maji na hivyo alivitumia kwa umwagiliaji na unyweshaji wa mifugo na kwa sababu hiyo alifanikiwa na kustawi sana, wenyeji waliona wivu, waliogopa mafanikio yake walimuogopa na yeye pia lakini pia walimsumbua walianza kufukia visima hivyo kwa uchafu wakimlazimisha kuchimba vingine, hata hivyo kila alipochimba kisima kingine Wafilisti walikigombania na kudai kuwa kisima ni chao!

Isaka hakupambana nao wala hakutaka kulipa kisasi wala kutafuta ushahidi kuwa visima vilikuwa mali ya baba yake na badala yake alihama na kuchimba kisima kingine alifanya hivyo kila mara walipofukia kisima chake au kukigombania kwa kudai kuwa ni mali yao, hatimaye alichimba kingine tena na kingine tena na kingine tena na hatimaye mwisho wakaona aibu wala hawakukigombania tena akakiita kisima hicho “Rehoboth” maana yake Bwana ametufanyia nafasi, na wafilisti hawakukigombania tena.

Isaka aliipata Amani yake kwa kukubali kuachilia na kupoteza, alijitahidi kila wakati kuepuka migogoro isiyo na sababu za kimsingi ambayo yeye aliona itavuruga Amani na hivyo aliamua kutumia nafasi ya kuachilia (withdraw) au kujiepusha, wakati mwingine ili kuipata Amani itatugharimu kuachilia, itatugharimu kwenda mbali ili kuepusha migogoro badala ya kusisitiza haki zetu, hatimaye Mungu ataongeza neema kwa wale wanaotafuta amani kwa bidii na kwa mioyo yao

1Petro 3:10-12 “Kwa maana, Atakaye kupenda maisha, Na kuona siku njema, Auzuie ulimi wake usinene mabaya, Na midomo yake isiseme hila. Na aache mabaya, atende mema; ATAFUTE AMANI, AIFUATE SANA. Kwa kuwa macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake husikiliza maombi yao; Bali uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya.”

Mfano wa Yakobo na Labani

Mwanzo 31:22-55 “Hata siku ya tatu Labani akaambiwa ya kwamba Yakobo amekimbia, akatwaa ndugu zake pamoja naye, akamfuata mwendo wa siku saba. Akampata katika mlima wa Gileadi. Mungu akamjia Labani, Mshami, katika ndoto ya usiku, akamwambia, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Labani akamfikia Yakobo, na Yakobo alikuwa amepiga hema zake katika mlima, na Labani na ndugu zake wakapiga hema zao katika mlima wa Gileadi. Labani akamwambia Yakobo, Umefanya nini? Umenihadaa, ukawachukua binti zangu kama mateka waliotwaliwa kwa upanga. Mbona umekimbia kwa siri ukanihadaa, wala hukuniambia, nipate kuagana nawe uende zako kwa furaha, na nyimbo, na ngoma, na kinubi? Wala hukuniacha niwabusu wanangu, na binti zangu; basi umetenda upumbavu. Ninao uwezo mkononi mwangu wa kukufanyia madhara; lakini Mungu wa baba yako usiku huu ameniambia, akisema, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Basi sasa, umetoka kwa sababu umetamani sana nyumba ya baba yako. Mbona basi umeiiba miungu yangu? Yakobo akajibu, akamwambia Labani, Kwa sababu naliogopa, nikasema, Usije ukaninyang'anya binti zako kwa nguvu. Awaye yote utakayemwona kuwa nayo miungu yako, yeye asiishi. Mbele ya ndugu zetu ukitambue kilicho chako kwangu, ukakichukue. Maana Yakobo hakujua ya kwamba Raheli ameiiba. Labani akaingia katika hema ya Yakobo, na hema ya Lea, na hema ya vijakazi wawili, wala hakuiona. Akatoka katika hema ya Lea, akaingia katika hema ya Raheli. Basi Raheli alikuwa amevitwaa vile vinyago ameviweka katika matandiko ya ngamia, na kuvikalia. Labani akapapasa hema yote wala hakuviona. Naye Raheli akamwambia babaye, Bwana wangu asikasirike kwa sababu siwezi kuinuka mbele yako, maana nimeshikwa na mambo ya kike. Akatafuta, wala hakuviona vile vinyago. Yakobo akakasirika, akagombana na Labani. Yakobo akajibu, akamwambia Labani, N'nini hatia yangu? Nayo ni nini dhambi yangu, hata ukanifuatia namna hii? Umepapasa-papasa vyombo vyangu vyote; ni kitu gani ulichokiona cha nyumbani mwako? Kiweke hapa mbele ya ndugu zangu, na ndugu zako, wakaamue kati yetu. Miaka hii ishirini nimekaa kwako; kondoo zako wala mbuzi zako wake hawakuharibu mimba wala waume katika wanyama wako sikuwala. Kilichoraruliwa na hayawani sikukuletea, mimi mwenyewe nimetwaa hasara yake, wewe umekidai katika mkono wangu, ikiwa kilichukuliwa mchana, au ikiwa kilichukuliwa usiku. Hii ilikuwa hali yangu; mchana jua likanipata, na baridi usiku, usingizi ukanitoka machoni mwangu. Miaka hii ishirini nimekaa nyumbani mwako; nilikutumikia miaka kumi na minne kwa binti zako wawili, na miaka sita kwa wanyama wako, nawe umebadili mshahara wangu mara kumi. Kama Mungu wa baba yangu, Mungu wa Ibrahimu na Hofu ya Isaka, hangalikuwa pamoja nami, hakika sasa ungalinifukuza mikono mitupu. Mateso yangu na kazi za mikono yangu Mungu ameziona, akakukemea usiku huu. Labani akajibu, akamwambia Yakobo, Hao binti ni binti zangu, na wana ni wanangu, na wanyama ni wanyama wangu, na yote uyaonayo ni yangu; nami naweza kuwatendea nini leo binti zangu na wana wao waliowalea? Haya! Na tufanye agano, mimi na wewe, liwe kwa ushahidi kati ya mimi na wewe. Yakobo akatwaa jiwe akalisimamisha kama nguzo. Yakobo akawaambia ndugu zake, Kusanyeni mawe. Wakatwaa mawe, wakafanya chungu, nao wakala huko karibu na ile chungu. Labani aliiita Yegarsahadutha, lakini Yakobo aliiita Galedi. Labani akasema, Chungu hii ni shahidi kati ya mimi na wewe hivi leo. Kwa hiyo likaitwa jina lake Galedi, na Mispa, maana alisema, Mungu avizie kati ya mimi na wewe, wakati tusipoonana. Ukiwatesa binti zangu, na ukitwaa wake zaidi ya binti zangu, wala hapana mtu pamoja nasi, tazama, Mungu ni shahidi kati ya mimi na wewe. Labani akamwambia Yakobo, Tazama chungu hii utazame na nguzo niliyoitia kati ya mimi na wewe.  Chungu hii na iwe shahidi, na nguzo hii na iwe shahidi, ya kuwa mimi sitapita chungu hii kuja kwako, wala wewe hutapita chungu hii na nguzo hii uje kwangu, kwa madhara. Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Nahori, Mungu wa baba yao, ahukumu kati yetu. Yakobo akachinja sadaka katika mlima, akawaita ndugu zake waje wale chakula, nao wakala chakula, wakakaa usiku kucha mlimani. Labani akaondoka asubuhi na mapema, akawabusu wanawe na binti zake, akawabariki; kisha Labani akaenda zake, akarudi kwao.”

Mgogoro wa Yakobo na Labani ulikuwa mgogoro mkubwa sana Mtu ameishi kwa mjomba wake mwenye hila nyingi ambaye amemfanyia uonevu wa kila aina, Maandiko yanaweka wazi kuwa Labani alijaribu kumrubuni Yakobo mara nyingi sana huku akibadilisha mshahara wake zaidi ya mara kumi, Hali ya maisha katika nyumba ya Labani ilikuwa ngumu mno kiasi ambacho Yakobo aliamua kutoroka unaweza kuona na kuwaza mtu anamtoroka mjomba wake kwa siri, huku hakukuwa kuachana kuzuri kwa watu ambao ni ndugu hata hivyo Labani alibaini na kumfuatia Yakobo akiwa amejawa na hasira nyingi, bila kujali kuwa amemrubuni Yakobo na kuyatumia maisha ya ujana wake wote kwa faida zake.

Baada ya kukabiliana kwa maneno makali hatimaye Yakobo na Labani waliamua kufanya agano ili kwamba asiwepo mtu atakayempandia mwenzake kwa madhara, Waliamua kusimamisha jiwe kubwa kama Ushahidi na kulitia mafuta kwamba hakuna mtu aatakayelivuka jiwe hilo kumuendea mwenzake kwa madhara, Jiwe hilo liliwahakikishia Amani na usalama licha ya kuwa walikuwa wamejeruhiana moyo kwa siku nyingi na kwa maumivu makubwa, lakini waliamua kuiacha Amani ishinde na kila mmoja kuendelea na maisha yake.

Wakati mwingine ili Amani ipatikane hatuna budi kukabiliana na mtu uso kwa uso, na kuyazungumza na kupata suluhu na makubaliano, Amani inahitaji watu wasameheane, na kujiwekea mipaka ili Amani iweze kuwepo, Haikuwa rahisi kuipata Amani ukiwa na mjomba kama Labani, Lakini Labani licha ya kuonywa na Mungu alikumbuka kuwa Yakobo pia ni mkwewe na mali alizonazo pia ni za wanae na wajukuu zake, waliamua kumaliza tofauti zao.

Mfano wa Yakobo na Esau.

Mwanzo 32:6-11 “Wale wajumbe wakarudi kwa Yakobo wakisema, Tulifika kwa ndugu yako, Esau, naye anakuja kukulaki, na watu mia nne pamoja naye. Ndipo Yakobo akaogopa sana, na kufadhaika sana, akawagawanya watu waliopo pamoja naye, na kondoo, na ng'ombe, na ngamia, wawe matuo mawili. Akasema, Akija Esau kwa kundi la kwanza, akalipiga, kundi litakalosalia litaokoka. Yakobo akasema, Ee Mungu wa baba yangu Ibrahimu, na Mungu wa baba yangu Isaka, BWANA, uliyeniambia, Rudi uende mpaka nchi yako, na kwa jamaa zako, nami nitakutendea mema; mimi sistahili hata kidogo hizo rehema zote na kweli yote uliyomfanyia mtumwa wako; maana nalivuka mto huo wa Yordani na fimbo yangu tu, na sasa nimekuwa matuo mawili. Uniokoe sasa na mkono wa ndugu yangu, mkono wa Esau, maana mimi namwogopa, asije akanipiga, na mama pamoja na wana. Walikuwa ni watu ndugu mapacha waliokuja kuumizana sana, Yakobo alinunua kwa hila haki ya mzaliwa kwa kwanza ya Esau, kama haikutosha Yakobo aliiba mbaraka wa mzaliwa wa kwanza waliachana kwa uchungu mkubwa sana Esau akiapa kuwa atamuua Yakobo, baada ya miaka mingi sana Yakobo alipokuwa akirejea alihofia kwamba Esau atalipa kisasi

Yakobo na Esau waliachana vibaya sana, ni mapacha ni ndugu wote wameokoka lakini Yakobo kwa hila alinunua haki ya mzaliwa wa kwanza na baadaye kuchukua mbaraka wa mzaliwa wa kwanza, jambo ambalo lilimuudhi sana Esau ambaye aliapa kuwa angemuua Yakobo, wakati Yakobo anarejea nyumbani alipatwa na hofu kuwa huenda ndugu yake anakuja kumuua, matukio mabaya na kuachana vibaya kuliweka jeraha kubwa sana katika maisha yao Yakobo alimuomba Mungu kwaajili ya hofu hiyo.

Yakobo alitumia zawadi, alitumia maombi kwa Mungu, na aliamua kujinyenyekeza sana na kuinama mbele ya Esau mara saba  kwa hiyo badala ya Esau kumshambulia alimkimbilia na kumkumbatia na kisha wote wakapaza sauti na kulia, bila kujali yaliyojiri, walihitimisha mkasa wao kwa kupatana, walichagua Amani badala ya visasi na viapo vya kumalizana

Amani ya kweli ili ipatikane inahitaji kujinyenyekeza, toba na kumuomba Mungu, sio hivyo tu na kuwa na bidii ya kuitafuta, kumuomba Mungu ni kwa Muhimu kwa sababu Mungu anaweza kuponya majeraha ya ndani kabisa na kujenga tena uhusiano mpya na kuponya majeraha yote ya ndani tunapochukua hatua ya kuitafuta Amani. Fikiria namna Yakobo alivyotanguliza zawadi nyingi na jinsi alivyojinyenyekesha sana na Fikiria Esau alivyoahirisha mpango wake wa kumuua Yakobo, wakati mwingine ni lazima kujishusha, kununua moyo na nduguyo kwa zawadi na kuonyesha heshima kubwa sana gharama hizo ndio bidii inayotajwa katika maandiko ya kwamba sio kila wakati kuitafuta Amani linaweza kuwa jambo rahisi. Lakini inatulazimu kuitafuta Amani kama agizo la Mungu lilivyo.
 

Baraka ya kuwa na amani na watu wote 

Kuwa na Amani na watu wote ni jambo lenye Baraka kubwa sana, linaleta ustawi wa kimwili na kiroho kwa wale wanaotafuta Amani, lakini kisaikolojia na kimwili kuwa na Amani kunapunguza migandamizo ya mawazo, kunakupa Amani ya moyo inayokufanya kuendelea kukua kiroho na kiakili, kujenga uhusiano mwema na watu, kuleta ukomavu na ukuaji wa kiroho, kujenga furaha, kuondoa mashaka, kuleta utulivu na furaha, mawasilano mazuri msamaha, na kujenga mazingira ya Amani na utulivu, ziko faida kadhaa za kibiblia pia ambazo zinatokana na kuweko kwa Amani, kama ifuatavyo:-

1.       Uhusiano wako na Mungu kuimarika - 1Yohana 2:9-11 “Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa. Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru, wala ndani yake hamna kikwazo. Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza, tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha macho.”

 

2.       Kukubaliwa kwa sadaka zako – Mathayo 5:23-26 “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.”

 

3.       Kusikilizwa kwa maombi yako – 1Petro 3:7 “Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.”

 

4.       Kusamahehewe dhambi zako – Marko 11:25-26 “Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.] ”            

 

5.       Shina la uchungu lisije likasumbua wengi – Shina la uchungu kwa kiyunani ni “Pikria” kwa kiingereza ni “bitterness” au uchungu, kwa kawaida shina au mzizi ndio unaosambaza maji na virutubisho katika mmea na majani sisi kama mwili wa Kristo ni kama mti, shina linapokuwa la uchungu, uchungu huo unasambaa na kuwanajisi wengine, Neno la Mungu linatutaka tuwe na Amani na watu wote ili kuepusha kuwanajisi wengine kwa sababu ya uchungu na ugomvi na ushindani walio nao watu wengine, na kupungukiwa na neema ya Mungu katika maisha yetu.

 

Waebrania 12:14-15 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”

 

6.       Kuonyesha ujuzi wako wa kumjua Mungu - 1Yohana 4:8-12 “Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo. Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu. Wapenzi ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana. Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wo wote. Tukipendana, Mungu hukaa ndani yetu, na pendo lake limekamilika ndani yetu.”   

                 

Umuhimu wa kuwa na amani na watu wote. 

Ni jambo la kusikitisha kuona na kusikia kila mahali siku hizi watu wa Mungu wakiwa mstari wa mbele kwa migogoro, kila mahali siku hizi inaumiza kusikia kuwa mtumishi huyu hapatani na huyu, au askofu huyu ana bifu na huyu, Mchungaji huyu haviivi chungu kimoja na yule, tungetarajia migogoro  na mafarakano kuwa kwa washirika wachanga au kwa watu wasiomjua Mungu, lakini jambo la kusikitisha ni kuwa migogoro mingi leo inaongozwa na watu wa Mungu tena wale ambao ni viongozi, au wako katika nafasi ya wao kuwa wapatanishi, au waamuzi, Inasikitisha kuona leo Mshirika na Mchungaji wake wana ugomvi, inasikitisha kuona mtu ana ugomvi wa miaka na miaka na mtu mwingine na hawamalizi alafu ni watu wa Mungu inaumiza sana sana kuona watu wa Mungu wakiwa hawataki suluhu leo,  Najua kuwa maandiko yanaeleza wazi kuwa siku za mwisho kutakuwa nyakati za hatari na tabia nyingi mbaya zitajitokeza lakini hata hivyo hayo hayapaswi kuwatokea watu wa Mungu kwa sababu maandiko yametujulisha kila kitu kwa uwazi lakini kama watu wa Mungu watakuwa hivyo ni wazi kuwa hakuwezi kuwa na mbingu ya watu wenye mafarakano na nadhani wote wanaweza kuachwa aliyekwazwa na aliyekwaza pia.

2Timotheo 3:1-5 “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.”

Haiwezekani watu wa Mungu wanaolijua neno la Mungu na tena wanaolihubiri na kulifundisha kisha wakawa hawataki Amani inasikitisha sana na tujifunze kutoka kwa wazee wetu wa Imani ambao wao walikutana na changamoto mbali mbali lakini walihakikisha kuwa wanakuwa na amani na watu wote, tukumbuke kuwa bila unyenyekevu sio rahisi kuwa na amani, bila kujishusha na kukubali kupoteza haki zako na kuachilia hatuwezi kuwa na Amani, kuipata Amani ni gharama, lakini kama tukiweka ubinasfi na maslahi yetu sio rahisi kuipata Amani, tukikosa uvumilivu na subira ni ngumu kuwa na amani, tukiwa hatuna msamaha na kuikiishi bila mipaka ni vigumu kwetu kuwa na amani, bila kuachilia hatuwezi kuwa na Amani, bila kupoteza hatuwezi kuwa na Amani, haijalishi nani mkubwa nani mdogo bila kuchukua hatua za kipatanishi na maridhiano na urejesho ni vigumu kuwa na amani neno la Mungu limetuagiza kuwa na amani na watu wote hivyo hatuna budi kulitii na kulifanyia kazi tafuta Amani:-

Warumi 12:17-21 “Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana. Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake.Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.”

Amani haiwezi kuja yenyewe ni Lazima itafutwe, na ndio maana Mungu katika hekima yake anatuagiza katika neno lake anawaagiza wenye haki waitafute Amani

Zakaria 8:16-23 “Haya ndiyo mtakayoyatenda; kila mtu na aseme kweli na jirani yake; hukumuni kweli na hukumu ya amani malangoni mwenu; wala mtu wa kwenu asiwaze mabaya moyoni mwake juu ya jirani yake; wala msipende kiapo cha uongo; maana hayo yote ndiyo niyachukiayo, asema Bwana. Tena neno la Bwana wa majeshi likanijia, kusema, Bwana wa majeshi asema hivi, Saumu ya mwezi wa nne, na saumu ya mwezi wa tano, na saumu ya mwezi wa saba, na saumu ya mwezi wa kumi, zitakuwa furaha na shangwe, na sikukuu za kuchangamkia, kwa nyumba ya Yuda; basi zipendeni kweli na amani. Bwana wa majeshi asema hivi, Itatokea halafu ya kwamba watakuja mataifa na wenyeji wa miji mingi; wenyeji wa mji huu watauendea mji huu, wakisema, Haya! Twendeni zetu kwa haraka tuombe fadhili za Bwana, na kumtafuta Bwana wa majeshi; Mimi nami nitakwenda. Naam, watu wa kabila nyingi na mataifa hodari watakuja Yerusalemu kumtafuta Bwana wa majeshi, na kuomba fadhili za Bwana. Bwana wa majeshi asema hivi, Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”

Amani ni ufunguo wa mafanikio na ustawi wa mwanadamu kimwili na kiroho, unapokuwa na amani inakusaidia kuwaza na kufikiri maswala ya maendeleo, na kuelekea kwenye ubunifu mkubwa na uzalishaji katika maisha na kazi zetu na ndoa zetu na familia zetu, kila mtu anapaswa kuwa na amani ya ndani na nje na mwanadamu anapokuwa na amani na kuitafuta sana Amani inaleta mchango mkubwa wa ufanisi katika jamii na kutufanya tuishi kwa furaa na amani, watu Fulani wanapoishi katika migogoro yao ni lazima wajue kuwa migogori yao inatuumiza hata sisi tulio nje ya migogoro hiyo kwa sababu hatufurahii kusikia migogoro hiyo upendo haufurahii udhalimu, kila mwenye mgogoro na mtu malizana nao haraka, wako watu wamekufa wakiwa hawajatengeneza maasi na maovu na uharibifu walioufanya kwa wenzao na kuwaumiza, wakafanya shingo zao kuwa ngumu, wakafa wakiwa hawajatafuta Amani!

1Wakorintho 13:4-6 “Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni;haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli;”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!       

0719990897