Matendo 13:1-3 “Na huko
Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni
Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa
ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia
Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa
kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao
juu yao, wakawaacha waende zao.”
Utangulizi.
Leo nataka
kuzungumzia mojawapo ya ibada ya muhimu na ya msingi na ya zamani sana, katika
utamaduni wa kanisa na kimaandiko na hii ni ibada ya kuwekea mikono au kuwekewa
mikono, Ibada hii ni ya muhimu kwa sababu ni ya kimaandiko na inaendelea
kutenda kazi hata katika siku zetu, ingawa kuna umuhimu wa kujikumbusha ili
tuweze kuwa na uelewa wa kina na mapana na marefu kuhusu kuwekea au kuwekewa
mikono, kuwekea au kuwekewa mikono kuna uwezo wa kuruhusu neema ya Mungu juu ya
maisha ya huduma na utumishi wa mtu, aidha pia mikono inahusika katika
kupitisha Baraka, neema na uponyaji wa mwili nafsi na roho kwa hiyo uko umuhimu
wa Kanisa kuwa na uelewa.
Kumbukumbu 34:9 “Na
Yoshua, mwana wa Nuni, alikuwa amejaa roho ya hekima; maana Musa alikuwa
amemwekea mikono yake juu yake; wana wa Israeli wakamsikiliza, wakafanya kama
Bwana alivyomwamuru Musa.”
2Timotheo 1:6-7 “Kwa
sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa
kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya
upendo na ya moyo wa kiasi.”
Kwa msingi huu
leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu kuhusu swala zima la
kuwekea au kuwekewa mikono, ambalo kimsingi ni lazima liambatane na maombi kama
ilivyo kwenye swala la kufunga, au kupaka mafuta vilevile kuweka mikono
huendana na kuomba au kusema maneno yanayoambatana na kusudi la kuwekea mikono
huko, ili kulitungua kusudi hilo kutoka katika ulimwengu wa roho na mkao wa
Moyo kwa kusudi la kutimiza mapenzi ya Mungu, tutajifunza somo hili Kanuni za
kuwekea au kuweka Mikono kwa kuzingatia vipengele vifuatavyo:-
·
Asili ya kuwekea au kuwekewa
mikono.
·
Makusudi ya ibada ya kuwekea au
kuwekewa mikono
·
Kanuni za kuwekea au kuwekewa
mikono
Asili ya kuwekea au kuwekewa mikono.
Kuwekea mikono
au kuwekewa mikono “laying on of hands”
ni tendo la ibada la kimwili ambapo mtu au watu au kikundi cha watu huweka
mikono inayoambatana na maombi juu ya wengine kama ishara ya kiroho yenye lengo
la kubariki, kuhamisha mamlaka, kuweka wakfu viongozi, kuwatenga watu kwaajili
ya huduma, kufanya maombezi ya uponyaji, kuchochea karama, kurithisha Baraka na
kutambulisha na ubatizo wa Roho Mtakatifu, Tendo hili ingawa linafanyika katika
mwili kiibada linaunganisha mamlaka ya Mungu ndani ya Mwanadamu anayepokea
kusudi hilo. Ni ishara inayoonekana ya neema ya Mungu isiyoonekana na uweza wa
Roho Mtakatifu.
Tendo la kuwekea
mikono kwa asili linaonekana katika maandiko ya Kiebrania likitajwa kwa
kiebrania kwa neno “Semikhah” kwa
kiingereza “succession” kwa kiwahili
ni kurithisha kwa mfululizo, mfano kutoka katika uongozi wa mtu mmoja kwenda
katika uongozi wa mtu mwingine kwa kurithishana kwa Amani au kwa lengo la
kuendeleza au kusaidia au kupitisha mfano Musa alipozidiwa na majukumu ya
kichungaji katika kanisa lililokuwako Jangwani alichagua wazee sabini “70” kwa maelekezo ya Mungu na kuwawekea
mikono na kwa tendo hilo sehemu ya utendaji wa Musa iliwapata wazee wale sabini ili waweze
kumsaidia majukumu yake.
Hesabu 11:24-29 “Musa
akatoka, akawaambia watu maneno ya Bwana; akawakutanisha watu sabini miongoni
mwa wazee wa watu, akawaweka kuizunguka Hema. Ndipo Bwana akashuka ndani ya
wingu, akanena naye, akatwaa sehemu ya roho iliyokuwa juu ya Musa, akaitia juu
ya wale wazee sabini; ikawa, roho hiyo ilipowashukia, wakatabiri, lakini
hawakufanya hivyo tena. Lakini watu wawili walisalia kambini, jina la mmoja
aliitwa Eldadi, na jina la wa pili aliitwa Medadi; na roho ile ikawashukia; nao
walikuwa miongoni mwao walioandikwa, lakini walikuwa hawakutoka kwenda hemani;
nao wakatabiri kambini. Mtu mmoja kijana akapiga mbio, akaenda akamwambia Musa,
akasema, Eldadi na Medadi wanatoa unabii kambini. Yoshua mwana wa Nuni,
mtumishi wa Musa tangu ujana wake, akajibu akasema, Ee bwana wangu Musa,
uwakataze. Musa akamwambia, Je! Umekuwa na wivu kwa ajili yangu; ingekuwa heri
kama watu wote wa Bwana wangekuwa manabii na kama Bwana angewatia roho yake.”
Hesabu 27:16-20 “Bwana,
Mungu wa roho za wenye mwili wote, na aweke mtu juu ya mkutano, atakayetoka
mbele yao, na kuingia mbele yao; atakayewaongoza watokapo, na kuwaleta ndani;
ili mkutano wa Bwana wasiwe kama kondoo wasio na mchungaji. Bwana akamwambia
Musa, Mtwae Yoshua, mwana wa Nuni, mtu mwenye roho ndani yake, ukamwekee mkono
wako; kisha ukamweke mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya mkutano wote; ukampe
mausia mbele ya macho yao. Nawe utaweka juu yake sehemu ya heshima yako, ili
mkutano wote wa wana wa Israeli wapate kutii.”
Asili nyingine
ya kuwekea mikono ilifanywa na makuhani kwa kuweka mikono yao juu ya mnyama
kwaajili ya sadaka ya kuteteketezwa ya dhambi, Kuhani angeweka mikono yake juu
ya mnyama kama ishara ya kusafirisha dhambi ya hatia kutoka kwa mwanadamu
anayeombewa au kufanyiwa upatanishi kuelekea kwa mnyama huyo kisha angechinjwa
na kuteketezwa kama ishara ya msamaha wa dhambi kutoka kwa muathirika, aidha
tukio kama hili lilifanywa na kuhani mkuu kwaajili ya dhambi za taifa kwa
mwanambuzi wa hazazeli mbuzi wa kafara ambaye angechukua uovu wa watu na
kupotelea nao jangwani.
Walawi 1:2-5 “Nena na wana
wa Israeli, uwaambie, Mtu wa kwenu atakapomtolea BWANA matoleo, mtatoa matoleo
yenu katika wanyama wa mifugo, katika ng'ombe na katika kondoo. Matoleo yake
kwamba ni sadaka ya kuteketezwa ya ng'ombe, atatoa ng'ombe mume mkamilifu;
ataleta mlangoni pa hema ya kukutania, ili akubaliwe mbele ya BWANA. Kisha
ataweka mkono wake juu ya kichwa cha hiyo sadaka ya kuteketezwa; nayo itakubaliwa
kwa ajili yake, ili kufanya upatanisho kwa ajili yake. Naye atamchinja huyo
ng'ombe mbele ya BWANA; kisha wana wa Haruni, hao makuhani, wataileta karibu
hiyo damu, na kuinyunyiza damu yake kando-kando katika madhabahu iliyo hapo
mlangoni pa hema ya kukutania.”
Walawi 16:21-22 “Na Haruni
ataweka mikono yake miwili juu ya kichwa cha yule mbuzi aliye hai, na kuungama
juu yake uovu wote wa wana wa Israeli, na makosa yao, naam, dhambi zao zote;
naye ataziweka juu ya kichwa chake yule mbuzi, kisha atampeleka aende jangwani
kwa mkono wa mtu aliye tayari.Na yule mbuzi atachukua juu yake uovu wao wote,
mpaka nchi isiyo watu; naye atamwacha mbuzi jangwani.”
Asili nyingine
ya tendo la kuwekea mikono ni kwaajili ya urithi au kuhamisha Baraka, ambapo
tunaona Yakobo akiwarithi watoto wa Yusufu na kuwa wa kwake, huku akiweka mkono
wa kuume juu ya mdogo na mkono wa kushoto juu ya mkubwa ili kumuinua Efraimu na
kumshusha Manase katika mbaraka wake.
Mwanzo 48:13-16 “Yusufu
akawaweka wote wawili, Efraimu katika mkono wake wa kuume, kuelekea mkono wa
kushoto wa Israeli; na Manase katika mkono wake wa kushoto, kuelekea mkono wa
kuume wa Israeli, akawasogeza karibu naye. Israeli akanyosha mkono wake wa
kuume akauweka juu ya kichwa cha Efraimu, aliyekuwa mdogo, na mkono wake wa
kushoto akauweka juu ya kichwa cha Manase, huku akijua atiavyo mikono; maana
Manase ndiye aliyezaliwa kwanza. Akambariki Yusufu, akasema, Mungu ambaye baba
zangu, Ibrahimu na Isaka, walienenda mbele zake, yeye Mungu aliyenilisha,
maisha yangu yote, hata siku hii ya leo, naye Malaika aliyeniokoa na maovu
yote, na awabariki vijana hawa; jina langu na litajwe juu yao, na jina la baba
zangu, Ibrahimu na Isaka; na wawe wingi wa watu kati ya nchi.”
Ibada ya kuwekea
mikono imekuwa na matumizi makubwa sana katika nyakati za agano jipya katika
mazingira mbalimbali, Mwandishi wa kitabu cha Waebrania anayataja mafundisho ya
msingi katika Kristo na mojawapo ya mafundisho haya ni pamoja na ibada za
kuwekea mikono
Waebrania 6:1-3 “Kwa
sababu hiyo, tukiacha kuyanena mafundisho ya kwanza ya Kristo, tukaze mwendo
ili tuufikilie utimilifu; tusiweke msingi tena wa kuzitubia kazi zisizo na
uhai, na wa kuwa na imani kwa Mungu, na wa mafundisho ya mabatizo, na kuwekea
mikono, na kufufuliwa wafu, na hukumu ya milele. Na hayo tutafanya Mungu
akitujalia.”
Makusudi ya ibada ya kuwekea au kuwekewa mikono.
Kwa ujumla
unapolichunguza neno la Mungu kuhusu swala zima la kuwekea mikono utaweza
kugundua kuwa ibada ya kuweka mikono au kuwekea mikono inafanyika kwa makusudi
ya aina mbalimbali kama ifuatavyo:-
1.
Kwa kusudi la kubariki – Kimsingi moja
ya sababu ya kuwekea mikono au kuwekewa mikono ni kwaajili ya Baraka za Mungu
kwa yule anayewekewa mikono, Baraka za Mungu humfanya mtu awe na kibali na awe
na mafanikio katika jambo analolifanya au analowekwa kulifanya kwaajili ya
ufalme wa Mungu au kwa makusudi mengine, Mfano tunaona Yakobo akiweka mikono
juu ya wajukuu zake ili kuwatakia Baraka za kinabii katika maisha yao, Lakini
sio hivyo tu tunamuona bwana Yesu akiweka mikono juu ya watoto kwa kusudi la
kuwabariki, aidha katika tamaduni za kikanisa pia watu wamekuwa wakiwawekea
mikono wana ndoa wakati wa kuwatakia maisha mema katika ibada ya ndoa hili
linaingia katika kundi hili la kuwekea mikono ili kuwabariki.
Mwanzo 48:20 “Akawabariki siku ile akasema, Katika ninyi Waisraeli
watabariki, wakisema, Mungu na akufanye kama Efraimu na Manase. Akamweka
Efraimu mbele ya Manase.”
Mathayo 19:13-15 “Ndipo akaletewa watoto wadogo ili aweke mikono yake juu
yao na kuwaombea; wanafunzi wake wakawakemea. Lakini Yesu akasema, Waacheni
watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme
wa mbinguni ni wao. Akaweka mikono yake juu yao, akatoka huko.”
Na kwa mujibu wa maelekezo ya kibiblia kama mtu atafanya ibada ya
kubariki anayebariki anapaswa kuwa mkubwa kwa sababu Baraka hutoka kwa mkubwa
kwenda kwa mdogo, kwa maana mtu huyo awe kuhani kwa maana ya mtumishi wa Mungu
ambaye ni mkubwa kwa mamlaka aliyopewa na Mungu ya kubariki, lakini pia awe
mkubwa kiumri, kwa hiyo ile mila ya kuwekewa mkono na mtoto mdogo kwa kuamini
kuwa atakubariki ni kinyume na maelekezo ya kibiblia
Waebrania 7:1-7 “Kwa maana Melkizedeki huyo, mfalme wa Salemu, kuhani wa
Mungu aliye juu, aliyekutana na Ibrahimu alipokuwa akirudi katika kuwapiga hao
wafalme, akambariki; ambaye Ibrahimu alimgawia sehemu ya kumi ya vitu vyote;
(tafsiri ya jina lake kwanza ni mfalme wa haki, tena, mfalme wa Salemu, maana
yake, mfalme wa amani; hana baba, hana mama, hana wazazi, hana mwanzo wa siku
zake, wala mwisho wa uhai wake, bali amefananishwa na Mwana wa Mungu); huyo
adumu kuhani milele. Basi, angalieni jinsi mtu huyo alivyokuwa mkuu, ambaye
Ibrahimu, baba yetu mkuu, alimpa sehemu ya kumi ya nyara. Na katika wana wa
Lawi nao, wale waupatao ukuhani, wana amri kutwaa sehemu ya kumi kwa watu wao,
yaani, ndugu zao, kwa agizo la sheria, ijapokuwa wametoka katika viuno vya
Ibrahimu. Bali yeye, ambaye uzazi wake haukuhesabiwa kuwa umetoka kwa hao, alitwaa
sehemu ya kumi kwa Ibrahimu, akambariki yeye aliye na ile ahadi. Wala
haikanushiki kabisa kwamba mdogo hubarikiwa na mkubwa.”
2.
Kwa kusudi la kurithisha Uongozi – sababu
nyingine ya ibada ya kuwekea mikono ni kwaajili ya kurithisha uongozi, “Semikhah” kwa kiingereza “succession” hii hufanyika kwa kusudi la kumrithisha kiongozi kutoka kwa
uongozi wa zamani kuja kwa uongozi mpya, wakati huu sehemu kama ile ya heshima
au Roho yule yule aliyetenda kazi na kiongozi aliyepita hufanya kazi na
kiongozi ajaye hata kama ni katika mtindo na mfumo wa aina nyingine na tabia
nyingine lakini Roho ni yeye yule, Jambo hili linapofanyika sehemu ya heshima
au mamlaka iliyokuweko juu ya kiongozi wa awali huamia kwa uongozi mpya na
kumpa neema ya kutumika sawa na kiongozi wa awali au zaidi katika namna
nyingine apendavyo Roho yeye yule.
Hesabu 27:16-20 “Bwana, Mungu wa roho za wenye mwili wote, na aweke mtu
juu ya mkutano, atakayetoka mbele yao, na kuingia mbele yao; atakayewaongoza
watokapo, na kuwaleta ndani; ili mkutano wa Bwana wasiwe kama kondoo wasio na
mchungaji. Bwana akamwambia Musa, Mtwae Yoshua, mwana wa Nuni, mtu mwenye roho
ndani yake, ukamwekee mkono wako; kisha ukamweke mbele ya Eleazari kuhani, na
mbele ya mkutano wote; ukampe mausia mbele ya macho yao. Nawe utaweka juu yake
sehemu ya heshima yako, ili mkutano wote wa wana wa Israeli wapate kutii.”
3.
Kwa kusudi la kuombea uponyaji na kufanya miujiza – Neno la Mungu linaonyesha kuwa ibada ya kuweka mikono pia inaweza
kufanywa kwa nia ya kufanya maombezi na kuwaponya watu au kutumiwa na Mungu kwa
njia ya miujiza, kwa hiyo utaweza kuona Yesu, na mitume kadhaa akiwemo Petro na
Paulo na kadhalika ambao waliweza kuwaombea watu kwa kuwawekea mikono na
wakapokea uponyaji, hata Yesu Kristo mwenyewe aliahidi ya kuwa wale wamuaminio
watatumiwa kwa ishara mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuweka mikono juu ya
wagonjwa nao kupokea afya
Marko 6:4-5 “Yesu akawaambia, Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika
nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake. Wala hakuweza kufanya
mwujiza wo wote huko, isipokuwa aliweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache,
akawaponya.”
Matendo 9:11-12 “Bwana akamwambia, Simama, enenda zako katika njia iitwayo
Nyofu, ukaulize katika nyumba ya Yuda mtu aitwaye Sauli, wa Tarso; maana,
angalia, anaomba; naye amemwona mtu, jina lake Anania, akiingia, na kumwekea
mikono juu yake, apate kuona tena.”
Matendo 28:7-8 “Karibu na mahali pale palikuwa na mashamba ya mkuu wa
kisiwa, jina lake Publio; mtu huyu akatukaribisha kwa moyo wa urafiki,
akatufanya wageni wake kwa muda wa siku tatu. Ikawa babaake Publio alikuwa
hawezi homa na kuhara damu. Paulo akaingia kwake, akaomba, akaweka mikono yake
juu yake, na kumpoza.”
Marko 16:17-18 “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina
langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa
kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa,
nao watapata afya.”
4.
Kwa kusudi la kumpokea Roho Mtakatifu – Uko
ushahidi wa kimaandiko unaoshiria kuwa pamoja na kuweko kwa njia nyingi sana za
watu kubatizwa kwa Roho Mtakatifu, inaonekana pia kuwa watu huweza kupokea
Ubatizo wa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono
mfano
Matendo 8:14-19 “Na mitume waliokuwako Yerusalemu, waliposikia ya kwamba
Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawapelekea Petro na Yohana; ambao
waliposhuka, wakawaombea wampokee Roho Mtakatifu; kwa maana bado hajawashukia
hata mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu. Ndipo wakaweka
mikono yao juu yao, nao wakampokea Roho Mtakatifu. Hata Simoni alipoona ya kuwa
watu wanapewa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ya mitume, akataka kuwapa
fedha akisema, Nipeni na mimi uwezo huu, ili kila mtu nitakayemweka mikono
yangu, apokee Roho Mtakatifu.”
Matendo 19:1-6 “Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita
kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko;
akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia
kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo
gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana. Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa
ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani,
Yesu. Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Na Paulo,
alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza
kunena kwa lugha, na kutabiri.”
5.
Kwa kusudi la kuchochewa kwa karama – Wakati
mwingine watu wa Mungu huwa na karama za Roho Mtakatifu ndani yao na vipawa
mbalimbali lakini wakati mwingine karama zina tabia ya kujificha na hivyo mtu
anaweza kuwekewa mikono na karama zikachochewa, tunapoendelea kumtumikia Mungu
kama ilivyokuwa kwa Timotheo kwa muda Fulani wakati mwingine kuna uwezekano wa
moto kupungua kutokana na changamoto mbalimbali Paulo alimtaka Timotheo ili
kumuwekea mikono yake ili karama ziendelee kuwaka na kufanyakazi kwa kiwango
cha juu Zaidi, karama pia huweza kuambukizwa ndani ya Mtu kwa kuwekewa mikono.
2Timotheo 1:6-7 “Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu,
iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga,
bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”
1Timotheo 4:13-14 “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya
na kufundisha. Usiache kuitumia karama ile iliyomo ndani yako, uliyopewa kwa
unabii na kwa kuwekewa mikono ya wazee.”
6.
Kwa kusudi la kusimika au kuweka wakfu viongozi wa kanisa na wale
walioitwa katika wito maalumu – Viongozi wote
makanisani wanapokuwa wameteuliwa au kuchaguliwa kwaajili ya kutimiza majukumu
yao kadhaa waliyoitiwa na Roho Mtakatifu katika kanisa wanapaswa kuwekewa
mikono ili wapokee neema ya kuwawezesha kubeba majukumu yao ya kikanisa au ya
kitumishi kwa hiyo nyakati za kanisa la Kwanza kila walipoweka viongozi
waliwawekea mikono.
Matendo 6:5-6 “Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote;
wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, na Filipo, na
Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na Nikolao mwongofu wa Antiokia; ambao
wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao.”
Matendo 13:1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na
manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio
Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli.
Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu
akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia.Ndipo wakiisha
kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”
7.
Huwezi kupokea roho chafu kwa kuwekewa mikono – Kumekuwepo na hofu kubwa sana kutoka kwa washirika na hata baadhi ya watumishi wa Mungu mbali mbali
wakionya kuwa uko uwezekano wa kupokea roho chafu kutokana na kuwekewa mikono,
ni muhimu kufahamu kuwa Mkrito aliyeokoka vizuri na aliye muaminifu hawezi
kamwe kupokea roho chafu kwa kuwekewa mikono
na mhudumu asiye mwaminifu, Mkristo aliyeokoka vema na kujazwa Roho
Mtakatifu yeye ni Hekalu la Roho Mtakatifu na Roho wa Mungu anakaa ndani yake
1Wakorintho 6:19 “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu
aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe;”
Roho wa Mungu aliye ndani ya waamini au watu waliookoka ni mkuu
kuliko yeye aliyeko katika ulimwengu huu kwa hiyo utabarikiwa na kufanikiwa kwa
sababu ya tendo la kiungu na ibada inayofanyika ndani yako na sio kwa sababu ya
hali ya mtumishi anayekuwekea mikono
1Yohana 4:4 “Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi
mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika
dunia.”
Yesu anaonyesha katika maandiko na mafundisho yake kuwa Mwamini
hupewa kile anachokiomba na Mungu sio dhalimu kwamba akupe nyoka wakati umeomba
samaki, au nge wakati umeomba yai na jiwe wakati umeomba Mkate Mungu huangalia
moyo na atakupa sawasawa na uhitaji wa moyo wako na sio kwa sababu ya hali ya
muhubiri au kiongozi anayekuwekea mikono
Luka 11:9-13 “Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi
mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa. Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye
atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Maana ni yupi kwenu aliye baba,
ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki atampa
nyoka? Au akimwomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa
watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho
Mtakatifu hao wamwombao?”
Hana alipata mtoto katika wakati ambao watoto wa Eli yule kuhani
walikuwa wameharibika na neno la Bwana lilikuwa adimu lakini kupitia maneno ya
Eli na uhitaji wa mwanamke yule moyoni Mungu alijibu maombi nyake sawasawa na
uhitaji wake kiyume kabisa na hali ya kuhani nyumbani mwa Bwana kwa hiyo hali
ya kuhani sio changamoto ya kumfanya mtu asipokee kitu halisi anachikitamani na
kukihitaji kutoka kwa Mungu.
Kanuni za kuwekea au kuwekewa mikono
Kama utakuwa
umefuatilia vema somo hili utagundua kuwa kuweka mikono ni swala la kiroho na
la Muhimu na kwa sababu hiyo lina kanuni zake, haliwezi kufanyika hovyo hovyo
ama bila kufuata utaratibu na maelekezo ya kibiblia, kuwekea watu mikono ni
njia ya kuruhusu neema ya Mungu kutoka kwa Roho Mtakatifu kupitia mikono yetu
na kutimiza kusudi lake kwa mtu anayewekewa Mikono kwa hiyo tukio hili kama
ilivyo kwa tukio la kupaka mafuta ni lazima lifanyike pamoja na maombi. Lakini
pia kwa kuzingatia kanuni, kila anayeweka mikono ni lazima awe anajua anachokifanya
na kujiuliza kwa nini anafanya na kusudi la kufanya hivyo, hivyo jambo hili
lisifanyike ilimradi tu kwani ni ibada kamili.
Anayeweka mikono ni lazima awe anajua anachokifanya – Mtu anayeweka mikono anatakiwa awe anajua ni kwa nini anafanya
hivyo, hili ni swala la kiroho na ni swala la maisha ni swala la kuinua mtu na
kushusha mtu kwa hiyo anayeweka mikono anatakiwa kuwa na ujuzi na kile
anachikifanya kwanza akiwa na ufahamu wa kawaida lakini pia kama ameongozwa na
Mungu au roho ya kinabii kufanya hivyo ni lazima aelewe kusudi linalomuongoza katika kuwekea mikono, Kwa mfano
wakati Yakobo anamuwekea mkono wa kuume Efraimu na mkono wa kushoto Manase
wakati Manase ndiye mkubwa na Efraimu ndiye mdogo, Yusufu alikuwa akielewa na
kufikiri kuwa babaye anakosea lakini Yakobo alisisitiza kuwa anajua
anachokifanya ona kumbe muwekewa mikono anapaswa kujua anachokifanya
Mwanzo 48:13-19 “Yusufu
akawaweka wote wawili, Efraimu katika mkono wake wa kuume, kuelekea mkono wa
kushoto wa Israeli; na Manase katika mkono wake wa kushoto, kuelekea mkono wa
kuume wa Israeli, akawasogeza karibu naye. Israeli akanyosha mkono wake wa
kuume akauweka juu ya kichwa cha Efraimu, aliyekuwa mdogo, na mkono wake wa
kushoto akauweka juu ya kichwa cha Manase, HUKU AKIJUA ATIAVYO MIKONO; maana
Manase ndiye aliyezaliwa kwanza. Akambariki Yusufu, akasema, Mungu ambaye baba
zangu, Ibrahimu na Isaka, walienenda mbele zake, yeye Mungu aliyenilisha,
maisha yangu yote, hata siku hii ya leo, naye Malaika aliyeniokoa na maovu
yote, na awabariki vijana hawa; jina langu na litajwe juu yao, na jina la baba
zangu, Ibrahimu na Isaka; na wawe wingi wa watu kati ya nchi. Yusufu alipoona
kwamba babaye anaweka mkono wake wa kuume juu ya kichwa cha Efraimu, ikawa
vibaya machoni pake. Akauinua mkono wa babaye auondoe katika kichwa cha
Efraimu, ili auweke juu ya kichwa cha Manase. Yusufu akamwambia babaye, Sivyo,
babangu, maana huyu ni mzaliwa wa kwanza; weka mkono wako wa kuume kichwani
pake. Babaye akakataa, akasema, NAJUA, MWANANGU NAJUA, yeye naye atakuwa taifa,
yeye naye atakuwa mkuu; lakini ndugu yake mdogo atakuwa mkubwa kuliko yeye, na
uzao wake watakuwa wingi wa mataifa.”
Unaona utagundua
katika kifungu hiki kuwa Yusufu na Yakobo walikuwa wanajua kuwa anayewekewa
mikono wakati wa Baraka ikiwa atawezewa mkono wa kuume huyu ndiye atakuwa
mkubwa na anayewekewa mkono wa kushoto atakuwa mdogo, hii ni kanuni ya kibiblia
ambayo watumishi wengi wa Mungu huikosea hasa wakati wa kubariki maharusi kwa
mfano unakuta wanaweka mikono hovyo na wakati mwingine mke anawekewa mkono wa
kuume na mume anawekewa mkono wa kushoto hili ni kosa kubwa la kiufundi na kosa
katika kanuni ya kuwekea mikono muweka mikono ni lazima awe anajua
anachikifanya NAJUA MWANANGU NAJUA, HUKU
AKIJUA ATIAVYO MIKONO je unajua jinsi ya kuweka mikono au unaweka tu? Sio hivyo tu jua kuwa sasa naweka
mikono kwaajili ya uponyaji, au naweka mikono kwaajili ya kuchochea karama, au
naweka mikono kwaajili ya kuweka kiongozi na kadhalika na wakati wote lile
kusudi la kuweka mikono litatamkwa kwa maombi (kunuizia), unapoweka mikono
kusimika kiongozi muwekee mkono wa kuume sio wa kushoto, shikiwa maiki na mtu
kisha tumia mikono yako yute miwili muwekee mikono kiongozi mkuu, unakuta mtu
ameshima maiki kwa mkono wa kulia anaweka wakfu kiongozi akitumia mkono wa
kushoto na watu wote wanakodoa macho na kuona tukio hilo kama tukio la kawaida
inaumiza sana watu kukosea kanuni za kuwekewa watu mikono!, Yusufu aliumia
alipoona Manase anawekewa mkono wa kushoto kwa nini kwa sababu alitambua
kimsingi kanuni hii
Kuweka au kuwekea mikono ni urithi wa kiroho – Katika ulimwengu wa roho tendo la kumuwekea mtu mikono ni tendo
la kurithi, au kurithisha tunajifunza kuwa wakati Yakobo anaweka mikono juu ya
Manase na Efraimu hawa walikuwa wajukuu wake lakini kitendo cha kuwawekea
mikono kilibadilisha mfumo wa maisha ya Manase na Efraimu kutoka kuwa wajukuu
zake na kuwa watoto wake sawa kabisa na Simeoni na Reuben ona
Mwanzo 48:3-6 “Yakobo
akamwambia Yusufu, Mungu Mwenyezi alinitokea huko Luzu, katika nchi ya Kanaani,
akanibariki, akaniambia, Mimi hapa, nitakuongezea uzao wako, na kukuzidisha,
nami nitakufanya uwe kundi la mataifa; kisha nitawapa wazao wako nchi hii baada
yako, iwe milki ya milele. Basi sasa wanao wawili uliozaliwa katika nchi ya
Misri kabla sijaja kwako Misri ni watoto wangu, yaani, Efraimu na Manase
watakuwa wangu, kama Reubeni na Simeoni. Na wazao wako utakaozaa baada ya hawa
watakuwa wako; kwa jina la ndugu zao wataitwa katika urithi wao.”
Hii maana yake
ni nini anayeweka mikono anawarithi anaowawekea mikono kuwa wanaye na
wanaowekewa mikono wanamrithi anayewawekea mikono kuwa baba yao nadhani ni
katika dhana kama hii kumekuwa na hofu kwa watu wengi kuogopa kuwekewa mikono
na kila mtu kwa kuhofia kuwa baba wa mtu ambaye humjui vema au kuwarithi watoto
usiowafahamu vema kwa kuwa katika ulimwengu wa roho mnabadilishana DNA za
kimamlaka na uongozi
Kuwekea mtu mikono ni kumuidhinisha au kumtambulisha – Tendo la kuwekea mtu mikono ni tendo la kumuidhinisha au
kumtambulisha mtu kihuduma au kumuweka katika mamlaka ya uongozi, unamuweka mtu
wakfu kwaajili ua huduma aliyoteuliwa au kuchaguliwa kuifanya kama ushemasi,
umisheni na kadhalika kwa hiyo kitendo cha kumuwekea mikono ni utambuzi wa
hadharani kuhusu aina ya wito aliyoitiwa anayewekea mikono au kuchochea karama
au kuhamishia karama na mamlaka kumuwezesha mtu huyo kutumikia vema kusudi
alilowekewa na ndio maana bado Biblia
inatoa tahadhari kuwa na umakini na unayemuwekea mikono ili kama ni mwovu
kumuwekea mikono maana yake ni kushiriki kazi zake mbovu au kushiriki uovu kwa
hiyo lazima unayemuwekea mikono uwe umemthibitisha kuwa hatakuaibisha
1Timotheo 5:21-22 “Nakuagiza
mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, na mbele za malaika wateule, uyatende
hayo pasipo kuhukumu kwa haraka; usifanye neno lo lote kwa upendeleo. Usimwekee
mtu mikono kwa haraka, wala usizishiriki dhambi za watu wengine. Ujilinde nafsi
yako uwe safi.”
Unapomuwekea mtu
mikono kwaajili ya huduma maana yake unagonga muhuri wako na kumuidhinisha mtu
huyo katika huduma ile aliyoitiwa sasa endapo mtu huyu hayuko sawa maana yake
kushindwa kwake kunawakilisha kushindwa kwako, wekea mikono mtu
anayekuwakilisha vema, ambaye umemfunza vema
Kuwekea mikono ni njia ya kupitisha neema ya Mungu.- tendo la kuwekea mikono kama ilivyo tendo la kupaka mafuta yote
ni matendo ya kuipitisha neema ya Mungu kupitia mikono yetu kwenda kwa wengine
kwa hiyo ni lazima tendo hili litumike pamoja na Maombi, kama ni kwaajili ya
mgonjwa kutakuwa na dua maalumu kwajili ya mgonjwa kama ni kwaajili ya kuweka
wakfu kiongozi dua itatamkwa ya kuweka wakfu kwa viongozi wanaohisika na
waliokidhi vigezo
Yakobo 5:14-15 “Mtu wa
kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka
mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na
Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”
Matendo 15:40-41 “Lakini
Paulo akamchagua Sila, akaondoka, akiombewa na wale ndugu apewe neema ya Bwana.
Akapita katika Shamu na Kilikia akiyathibitisha makanisa.”
Kwa hiyo ibada
zote za kuwekea mikono iwe ni kwaajili ya uponyaji, kubariki ndoa kuweka
viongozi zote maana yake ni kuruhusu neema ya Mungu ipite juu ya wahusika na kuwawezesha
katika wajibu unaohusika kwa hiyo ni lazima maombi yahusike kwa sababu hiyo
kuwekea mikono sio uchawi ni njia ya kupitisha neema ya Mungu kwa hiyo kuwekea
mikono ni njia inayoonekana ya kupitisha mambo yasiyoonekana ya kiungu kwenda
kwa watu husika, kwa umaalumu wake kwa kanisa na ulimwengu lakini mwenye kutoa
Baraka hizo ni Mungu mwenyewe, wakati wa kubariki watoto tunaweza kuwawekea
mikono, wakati wa kubatiza tunaweza kumuwekea mtu mikono na kumuombea neema ya
maisha ya uchaji wa Mungu na utumishi, wakati wa kuombea wagonjwa tunaweza
kuwaombea wagonjwa neema ya kupokea uponyaji, wakati wa kubariki maharusi
tunaweza kuwaombea maharusi neema na wakati wa kuweka wakfu viongozi mashemasi,
makasisi, maaskofu na kadhalika na hata wakati wa kusimika askofu na viongozi
mbalimbali ni vema wakawekewa mikono kuwaombea neema ya Mungu kisha Mungu
mwenyewe atafanya kazi yake pamoja na watu wake kwa makusudi yaliyokusudiwa,
kumbuka wakati wa kuwekea maharusi mikono ya Baraka weka mkono wa kuume kwa
mume na mkono wa kushoto kwa mke kufanya kinyume na hayo ni kutengeneza
migogoro ya kiroho na kimaongozi kwani Mungu hadhihakiwi waweka mikono lazima
wajue nini wanachokifanya wakati wanaweka mikono. Ikiwa kanisa linaweka mikono
kwa askofu mkuu, na askofu mkuu aliyekuwepo madarakani hayuko, askofu mkuu
mteule atawekewa mikono na mtu mwenye mamlaka ya askofu mkuu aliyetsaafu au wa
kanisa lingine, ama kutoka kwa wamishionari waanzilishi wa kanisa husika au mtu
mwenye mamlaka ya huduma ya kitume.
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni