Jumatatu, 29 Aprili 2019

Wamisri wakatuonea, wakatutesa, !


Kumbukumbu la torati 26:6-9 “Wamisri wakatuonea, wakatutesa, wakatutumikisha utumwa mzito.  Tukamlilia Bwana, Mungu wa baba zetu; Bwana akasikia sauti yetu, akaona na taabu yetu, na kazi yetu, na kuonewa kwetu.  Bwana akatutoa kutoka Misri kwa mkono wa nguvu, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa utisho mwingi, na kwa ishara, na kwa maajabu; naye ametuingiza mahali hapa, na kutupa nchi hii, nchi ijaayo maziwa na asali.”

 Sinagogi la Kiyahudi huko San Diego, lililoshambuliwa kwa Risasi 28/04/2019

Utangulizi:
Jana tarehe 28 April 2019  sawa na mwezi Nisan 23 5779 kwa kalenda ya kiyahudi, nilipata habari ya kuuawa kwa Myahudi mmoja kutokana na shambulio la risasi lililofanyika huko San Diego katika mojawapo ya sinagogi la kiyahudi, na wengine watatu kujeruhiwa vibaya, nilikuwa bado sijasahau tukio la kuuawa kwa wakristo wakati wa Pasaka Nchini Sri-lanka nikafikiri na kuwaza kwamba bado dunia ya leo iliyoendelea kuna watu bado wanafikiri wanaweza kuwepo duniani peke yao bila kuchanganyika na watu wanaotofautiana nao kimawazo kifikira kiitikadi na kiimani? Dunia inapaswa kutafakari kwa kina kuhusu ukomavu na uwezo wa kuchukuliana katika jamii na kupendana bila kujali tofauti zetu,
Biblia inasema katika 1Yohana 4:8Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo.” Hii ni wazi kuwa bado dunia haijamjua Mungu, na kuwa jamii inapaswa kukumbuka na kuhimiza na kufundisha kuhusu upendo, ni muhimu kufanya kilalinalowezekana kuing’oa chuki miongoni mwa wakazi wa dunia, na kukumbuka kuwa Yesu hakuwa mjinga alipokuwa akifundisha Upendo, alikuwa anajua wazi kuwa dunia itakuja kufikia na kuwa na matukio haya tunayoyashuhudia leo katika jamii iliyoendelea.
Katika kifungu cha maandiko ya msingi, Musa alikuwa anawakumbusha wana wa Israel sheria za Mungu na hususani kwa kizazi kipya ambao wengi waoa walizaliwa Jangwani au na wale waliotoka Misri wakiwa vijana na waliokuwa wadogo, Musa alikuwa akizungmzia kumtolea Mungu sadaka za shukurani watakazomtolea Mungu watakapokuwa katika nchi ya amani nchi iliyojaa maziwa na asali nchi ya Israel aliwalekeza kwamba watakapotoa wamkumbushe Mungu kuwa walionewa huko Misri, lakini walipomlilia Mungu akawaokoa na kuwaleta katika inchi hii iliyojaa maziwa na asali
Katika kifungu hiki Kumbukumbu la Torati 26:6 ““Wamisri wakatuonea, wakatutesa, wakatutumikisha utumwa mzito. .”
Biblia ya kiingereza  NIV inasomeka hivi Deuteronomy 26:6But the Egyptians mistreated us and made us suffer, subjecting us to harsh labor.”
Biblia ya Kiyahudi iitwayo (The Israel Bible) inasomeka hivi Deuteronomy 26:6The Egyptians DEALT HARSHLY WITH US and oppressed us; they imposed heavy labor upon us.”
Musa aliwakumbusha Jambo hili la msingi walikumbuke watakapokuwa wakiabudu, kwa sadaka ya shukurani, wamkumbushe Mungu kuwa walitendwa vibaya na wamisri neno kuonewa, kuteswa na kutendwa vibaya katika lugha ya Kiebrania linatumika neno “VAYAREIU”  likimaanisha kuwa lakini rafiki zetu walitugeuka,walitutenda mabaya, wakatuonea, wakatutesa, wakatudhulumu kisha wakatugeuza  kuwa watumwa kwa utumwa mbaya na mzito” Hii ilimaanisha kuwa Israel hawakushuka Misri wakiwa watumwa walikuwa rafiki wa wamisri, walikuwa wapendwa, walikuwa jamaa na ndugu wa waisrael, lakini hatimaye ukafika wakati wakawageuka, wakavunja urafiki, wakaanza kuwabagua na kutengeneza sheria za kuwabana, na kuwaonea na kuwatesa na kuwakandamiza na hatimaye kuwafanya watumwa wao, Ndipo ulipofika wakati wayahudi wakamlilia Mungu awatoe katika utumwa ule mzito na Mungu akawaokoa akawapeleka katika nchi ya ahadi, ambako huko npekee ndipo mahali ambapo Wayahudi watakuwa salama na wakamfurahia Mungu.
Leo hii sio Misri tu ambao wamewakaribisha Wayahudi kisha wakawaonea baadaye, ziko nchi nyingi tu ambazo zimewapokea wayahudi wakiwa kama marafiki, kama ilivyotokea Ujerumani na Uganda, lakini baadaye katika namna isiyoweza kueleweka watu hao waliwageuka nakuwaona wayahudi kama adui na watu wasiofaa, ili mtahudi aweze kuwa salama ni lazima popote pale walipo warudi katika nchi yao ya asili nchi yao ya ahadi ili wamuabudu Mungu pasipo hofu na watoe sadaka ya shukurani na mateso yao yote yatageuka kuwa historia
Wako watu wengi sana leo wanateseka lakini chanzo cha mateso yao hakikuwa chuki na majuto na dhuluma ambazo wanaziona sasa, inawezekana wewe ni House girl ulichukuliwa kama dada wa kazi kwa nia nzuri, ukaenda mjini kama rafiki na ndugu, na ukapokelewa vema huko ulikokwenda mama na baba wa nyuma uliyofikia walikataa kuitwa anko walisema utuite mama au baba, lakini baada ya siku kadhaa hali ilibadilika umeanza kuitwa hili, limbwa, paka , nyau. Fala na kadhalika.

Inawezekana ulioa au kuolewa kwa nia nzuri kabisa, wakati unachumbiwa ulikuwa ni rafiki, hukuwa mtumwa mliitana majina mazuri, sweetie, asali wangu, maua, dear, dally na kadhalika lakini hapa unaposoma ujumbe huu mambo yamegeuka wewe sasa ni jibwa, fala, lione, liangalie, sijui nililioa la nini, mlango wa nane, balaa nuksi, mwiba na kadhalika.
Inawezekana wakati uaajiliwa ulikaribishwa kwa furaha, bosi aliwataka wenyeji wakupe saada mkubwa utakaouhitaji, ulidekezwa, ulifanywa kama moja ya wamiliki wa kampuni, ulikuwa ni wakati wa furaha umepata kazi mpya, lakini baada ya sikukadhaa, Mambo yamebadilika, unaonekana kama mzigo, unateseka, unapelekeshwa unaonekana hifai tena.
Kila mahali walikokwenda Wayahudi walikaribishwa walipokelewa kwa ukarimu lakini leo watu wanawalipua, wanawapiga risasi, kama majambazi au watu wasiofaa, huko san diego wayahudi wameuawa katika sabato ya kwanza ya Pasaka walipokuwa katika ibada na mama mmoja mwenye miaka 60 alifariki na wengine watatu kujeruhiwa vibaya, mmoja akiwa kiongozi wa kidini Rabbi na mkuu wa sinagogi husika kinawafanya wengine wawe na chuki dhidi ya wengine, kwa nini wakristo wameuawa Srilanka na kwa nini waqyahudi wameshambuliwa nani atawasemea
Hujawahi kuona unakaribishwa mahali vizuri, unapeewa na ofisi, unasifiwa kila mahali unahesabika kama mtu mwema kisha baada ya muda wewe ndio unaonekana kama mwiba wa kila mmoja pale ulipo?
Hali hii ndio inayowatokea Israel Duniani kote, ndio inayoatokea Wakristo, watu wanaona kuwa ni haki kuvaa mabomu na kuwalipua
Iko siri moja kubwa na ya kipekee, ni kukaa katika ahadi za Mungu tu, Ili Israel iweze kuwa salama hawana budi kuungana na kukaa Israel pekee ili wajilinde wakae katika nchi ya ahadi waliyoahidiwa baba zao Ibrahimu Isaka na Yakobo ndio wanaweza kujithibitishia usalama wao.
Wako watu wengi leoa hawako salama kwa sababu walifanya urafiki na shetani, walipokelewa na shetani , ibilisi kwa furaha sana wakiwa kama marafiki, Lakini kumbuka kuwa shetani hana urafiki na mtu awaye yote lazima atakugeuka tu atakutesa atakugeuza kuwa mtumwa na atakudhulumu, shetani anataka ufanye mambo kwa faida yake na maslahi yake hakuna mafanikio ya kweli kwa shetani, ili uwe salama huna budi kurudi kwa Yesu kristo na kujificha kwake, yeye ndio nchi halisi ya ahadi na kwake kuna usalama, Kwa ibilisi haijalishi kuwa wewe ni mwenye haki au la kwake nifuraha kubwa ukiangamia yeye na watu wake hawatajali haki yako, wakati umefika wa wewe kukaa katika uwepo wa Mungu kwa usalama wako, ili amani ipatikane katika ndoa yako hakikisheni mnamkaribisha Mungu na kujifunza upendo kama yeye alivyoagiza.
Isaya 5:1 Mwenye haki hupotea, wala hakuna atiaye hayo moyoni; na watu watauwa huondolewa, wala hakuna afikiriye ya kuwa mwenye haki ameondolewa asipatikane na mabaya
Hakuna wanaojali kile kinachowapata wayahudi leo. Lakini Palestina ikiguswa tu dunia itapiga kelele hata kama wakati mwingine wao ndio wachokozi na ndio wanaoanzisha kurusha maroketi, Israel ikijibu kama sehemu na wajibu wa kujihami na kujilinda, Israel ikijilipizia kisasi kwa adui zake dunia inapiga kelele je wadhani Wayahudi sio watu, nani atawapigia kelele na kuielimsha jamii duniani kuwa nao wanastahili kutetewa na kuangaliwa kwa maslahi yao duniani, Mimi sisemi kwa sababu nina asili ya Kiebrania tu hapana bali nataka haki itetendeke duniani ifikie hatua tujifunze pendo lake Yesu na kuielimisha katika jamii yetu, kila mmoja anapaswa kujua kuwa kama tunampenda Mungu tutathamini uhai wa watu wake kuliko imani zetu, Dunia pia inapaswa kuelewa kuwa ili Israel iweze kuwa salama  nilazima waelekee katika nchi ya ahadi na kukaa katika taifa lao wenyewe, ili sisi nasi tuweze kuwa salama turudi katika uwepo wa Mungu. Tutafanikiwa. Israel walimlilia Mungu, akawasikia akaziona taabu zao na kuonewa kwao aakawaokoa kwa mkono wa nguvu ulionyooshwa na wakajiliwa na kipindi cha neema  I stand with Israel.”
Rev. Innocent Kamote.
Mkuu wa wajenzi mwenye hekima

Jumapili, 28 Aprili 2019

Sitakupungukia wala sitakuacha!

Mstari wa Msingi: Yoshua 1:5-8 “Hapatakuwa mtu ye yote atakayeweza kusimama mbele yako siku zote za maisha yako; kama nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo nitakavyokuwa pamoja na wewe; sitakupungukia wala sitakuacha. Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana ni wewe utakayewarithisha watu hawa nchi hii niliyowaapia baba zao ya kwamba nitawapa. Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako. Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana. Je! Si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako”.



Jumatatu ijayo kidato cha sita kote Nchini wanatarajia kuanza mitihani yao ya kumaliza Elimu ya juu ya sekondari, nafahamu sana katika wakati huu wengi watakuwa wana hofu kwamba mambo yatakuwaje japo kweli wengi wamejiandaa vizuri na hawana wasowasi kabisa kukabiliana na mtihani huo, lakini hata hivyo Mungu alinipa neno hili maalumu kwaajili yao kwamba “Naye Bwana, yeye ndiye atakayekutangulia, atakuwa pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha; usiogope wala usifadhaike.” Kumbukumbu la Torati 31:8

Ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha wakati mwingine tutakabiliana na changamoto za aina mbalimbali, ziko changamoto nyingi lakini mojawapo ya changamoto kubwa ni pale unapodhani kuwa uko peke yako au unakabiliana na muda ambao utabaki mwenyewe na wakati huo utapaswa kutatua changamoto zinazokukabili ukiwa peke yako, Bila mtu aliyekuwa anakupa msaada wa karibu, Mungu alifanya kazi na Musa kwa kiwango kikubwa na cha ajabu, Mungu pia alifanya kazi na Yesu Kristo kwa uweza mkubwa na waajabu, Musa alipokuwa ameondoka Yoshua alibaki mwenyewe na hivyo alikuwa na mashaka makubwa kuwa itakuwaje endapo atakabiliwa na changamoto nzito zilizoko mbele yake, sio hivyo tu hata wakati Yesu anaondoka wanafunzi wake walikuwa na wasiwasi mkubwa sana kwamba itakuwaje Jibu sahihi katika wakati huu lilikuwa ni kuwahakikishia kuwa nitakuwa pamoja nanyi, Mungu alimuhakikishia Yoshua kuwa atakuwa pamoja naye hatampungukia wala hatamuacha

Ni rahisi kwetu wanadamu tunapopita katika changamoto ngumu huku tukifikiri kuwa hakuna msaada ni rahisi kwetu kupiga kelele za kibinadamu kama zile alizopiga Yesu Kristo pale msalabani baada ya mateso mazito “Mungu wangu mungu wangu mbona umeniacha?” Mungu katika neno lake ameahidi mara kadhaa kwani anatujua vema umbo letu anajua udhaifu wetu na ameahidi kuwa hatatuacha kamwe, ushindi wetu katika maisha yetu unaanza na ujasiri huu kwamba Mungu yuko Pamoja nasi, Hatatuacha wala hatatupungukia.

Tunapokaribia kuingia katika vyumba vya mitihani wiki ijayo, ni kweli kuwa tutakaa wenyewe mbali na wenzetu mbali na walimu, tutakuwa tukikabiliana na maswali yaliyotungwa na watu tusiowajua sisi, wasio walimu wetu sisi na hivyo ni rahisi kuogopa mtihani kwa sababu tu umepewa jina la mtihani wa kitaifa, lakini hata ujapokuwa peke yako katika chumba chako cha mtihani kumbuka kuwa Bwana anatangulia mbele yako hatakuacha kabisa wala kukupungukia kabisa. Hakuna mtu alipewa wajibu wa kufanya na Mungu kisha Mungu asiwe pamoja nae, mmepewa wajibu wa kusoma kwa sasa na hilo ndio kusudi la Mungu kwaajili yenu katika kusudi hilo Bwana atakuwa pamoja nanyi, MSIOGOPE.

Mathayo 28:18-20 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; NA TAZAMA, MIMI NIPO PAMOJA NANYI SIKU ZOTE, HATA UKAMILIFU WA DAHARI

Hakuna maneno ya muhimu kama haya wakati tunakabiliana na changamoto yoyote mbeleni Mungu akikuambia kuwa yuko pamoja nawe tayari hii ni alama kubwa sana ya ushindi, lakini akikuambia kuwa hatakuacha wala nhatakupungukia ni zaidi ya ushindi, yeye atakuwa pamoja nawe ahadi hii imerejewa mara kadhaa katika maandiko kwa kusudi la kutuondolea woga na kutupa ujasiri na moyo wa kujiamini, kwamba atakuwa pamoja nasi, katikwa wakati wa msahaka na wasoiwasi kumbuka atakuwa pamoja nasi kwa uwepo mkubwa sana.

Mungu alimwambia Yakobo katika Mwanzo 28:11-17 “Akafika mahali fulani akakaa huko usiku kucha, maana jua lilikuwa limekuchwa; akatwaa jiwe moja la mahali pale akaliweka chini ya kichwa chake, akalala usingizi pale pale. Akaota ndoto; na tazama, ngazi imesimamishwa juu ya nchi, na ncha yake yafika mbinguni. Tena, tazama, malaika wa Mungu wanapanda, na kushuka juu yake. Na tazama, BWANA amesimama juu yake, akasema, Mimi ni BWANA, Mungu wa Ibrahimu baba yako, na Mungu wa Isaka; nchi hii uilalayo nitakupa wewe na uzao wako. Na uzao wako utakuwa kama mavumbi ya nchi, nawe utaenea upande wa magharibi, na mashariki, na kaskazini, na kusini; na katika wewe, na katika uzao wako, jamaa zote za dunia watabarikiwa. NA TAZAMA, MIMI NIPO PAMOJA NAWE, nitakulinda kila uendako, nami nitakuleta tena mpaka nchi hii, kwa maana sitakuacha, hata nitakapokufanyia hayo niliyokuambia. Yakobo akaamka katika usingizi wake, akasema, Kweli BWANA yupo mahali hapa, wala mimi sikujua. Naye akaogopa akasema, Mahali hapa panatisha kama nini! Bila shaka, hapa ni nyumba ya Mungu, napo ndipo lango la mbinguni.

Mungu anataka tuwe na ujuzi huu, kwamba yuko pamoja nasi, ujuzi wa aina hii ukiwa wazi mbele yetu hatutaogopa, tutakuwa na ujasiri, kwamba hata iweje yuko Mungu ambaye ni Mchungaji mwema na hivyo hatutapungukiwa na kitu, kwa vyovyote vile hatatupungukia wala hatakuacha hata tujapopita katika uvuli wa mauti

Daudi alipoifahamu siri hii hakuogopa alimtegemea Mungu na alijua wazi kuwa Mungu ni Mchungaji wake na kwamba hatapungukiwa, wala hataogopa mabaya au vitisho kwa maana yeye yupo pamoja naye, Hofu ni adui mkubwa wa mafanikio yetu, wanafunzi wengi wenye akili na uwezo wanaweza kufanya vema siku zote lakini wanaweza kuharibu wakati wa mitihani kwa sababu shetani huwatia hofu huwaogopesha lakini leo Bwana amenituma nikuamnbie kuwa usiogope Bwana yu pamoja nawe

Zaburi 23: 1-6 “Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu. Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza. Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake. Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana WEWE UPO PAMOJA NAMI, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika.   Hakika wema na fadhili zitanifuata Siku zote za maisha yangu; Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele.

Yoshua alichoambiwa na Mungu ni kuliamini neno lake tu, kwamba alisome, alitafakari na kulitii na kulifuata na kuwa akifanya hivyo haitakuja itokee amepungukiwa na kitu, Hutapungukiwa na kitu Yesu akikutuma, hii ni ahadi katika neno lake anapokuagiza Yesu hata kama huna kitu mfukoni hutapungukiwa 

Luka 22:35 “Akawauliza, Je! Hapo nilipowatuma hamna mfuko, wala mkoba, wala viatu, mlipungukiwa na kitu? Wakasema, La!

Waebrania 13:5-6 “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. Hata twathubutu kusema, Bwana ndiye anisaidiaye, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini?

Jambo kubwa na la msingi ni kuamini neno lake, na kulitendea kazi, na ndio maana, Mungu alimwambia Yoshua aliangalie neno la kulitafakari na kulishika atafanikiwa katika kila alifanyalo na kila aendako na kuwa hakuna kiti au mtu atakayeweza kusimamam mbele yake siku zote za maisha yake, Hitler Dikteta mkubwa sana alikuwa ni mtu asiye na hofu askari wake pia hawakuogopa walikuwa watii mno kwa neno la Hitler kwa kiwango cha kufa lakini Hitler anasema alikuwa anaogopa mitihani, sisis hatupaswi kuogopa kwa sababu Mungu ameahidi kwamaba atakuwa pamoja nasi, hii ni ahadi yake kwetu, na ni neno lake kwetu tuamini tu na utaona mafanikio makubwa katika mitihani itakayoanza jumatatu ijayo ya tarehe 6/05/2019 Bwana hatakupungukia wala hatakuacha amini tu neno lake.

Mathayo 7:24-27 “Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.

Sisi ni warithi wa Baraka zake Ibrahimu, Ibrahimu baba yetu wa imani alikuwa rafiki wa Mungu, Ibrahimu hakuishi maisha ya hofu Mungu alimtokea na kumwambia wazi kuwa yeye ni thawabu yake kubwa sana na Ngao yake

Mwanzo 15:1 “Baada ya mambo hayo neno la BWANA likamjia Abramu katika njozi, likinena, Usiogope, Abramu, Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana.

Baba katika jina la Yesu nawasogeza kidato cha sita nchi nzima nawaombea mtihani mwema, naamini neno lako litawafikia hata kama wengine wako shule za Bweni na hawajui Mungu amesema nao nini lakini mimi mtumwa wako kwa nenolako ulilonipa nawaombea wote uwe pamoja nao kama ulivyoahidi, katika neno lako, uwasaidie wote wanaokutegemea wewe Bwana nakuomba usiwaangushe ukawafanikishe na uwepo wako ukawe pamoja nao katika vyumba vyao vya mitihani kwaajili ya utukufu wako, asiwepo awaye yote wa kuwatisha wala kuwaingizia hofu, nawakinga kwa jina lako kutoka katika mashambulizi yote ya yule muovu nakusihi ukawe pamoja nao, Katika jina la Yesu Kristo wa Nazareth aliye hai, Amen!

Na. Rev Innocent Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima.

Ijumaa, 19 Aprili 2019

Mwondoshe huyu, utufungulie Baraba.!


Luka 23:18-25Wakapiga kelele wote pamoja, wakisema, Mwondoe huyu, utufungulie Baraba.  Naye ni mtu aliyetupwa gerezani kwa ajili ya fitina iliyotokea mjini, na kwa uuaji Basi Pilato alisema nao mara ya pili, kwa vile alivyotaka kumfungua Yesu.  Lakini wakapiga kelele, wakisema, Msulibishe. Msulibishe. Akawaambia mara ya tatu, Kwa sababu gani? Huyu ametenda uovu gani? Sikuona kwake hata neno lipasalo kufa. Basi nikiisha kumrudi nitamfungua. Lakini wakatoa sauti zao kwa nguvu sana, wakitaka asulibiwe. Sauti zao zikashinda. Pilato akahukumu kwamba haja yao ifanyike. Akamfungua yule aliyetupwa gerezani kwa ajili ya fitina na uuaji, yule waliyemtaka, akamtoa Yesu wamfanyie watakavyo”.


Utangulizi:
Moja ya mambo ya kuyatafakari na kujiuliza kwa kina hususani katika wakati huu wa Pasaka ni pamoja na tabia ya wanadamu ambayo ni tabia ya kushangaza sana, tabia hii ngumu kuelezeka kwamba inatokana na woga, kutokujiamini, saikolojia ya mkumbo, kushindwa kusimama katika kweli, unafiki, au namna gani, hii ni ile tabia yetu ya kung’angania vitu vibaya, viovu na vyenye kuleta shida katika maisha yetu na kupoteza vitu vyema vizuri na vyenye thamani au vyenye kuleta ukombozi kutoka katika changamoto tulizonazo, Mwondoshe huyu, utufungulie Baraba! Haya yalikuwa maneno ya watu wote siku Mwokozi wa ulimwengu huu alipohukumiwa kusulubiwa kwa kura za wanadamu ambao kwa nia moja walitaka asulubiwe na mtu mhalifu zaidi aweze kuachwa huru!

Nani maarufu kati ya Yesu na Baraba?

Wote tunaweza kukubaliana wazi kuwa kifo cha Yesu Msalabani kilikuwa kina kusudi la Mungu nyuma yake, ilikuwa ni lazima Yesu asulubiwe ili mimi na wewe tuokolewe kutoka katika adhabu ya dhambi zetu sio mimi na wewe tu bali na hata watu waovu labda huenda kuliko mimi na wewe kama ilivyokuwa kwa Baraba

Kinachonishangaza hapa na amabachoi nataka kukijadili kwa kina ni sababu gani inapelekea watu wampuuzie Yesu kwa kiwango hata cha kutokutaja jina lake, na wakati huo huo wamchague mtu mhaini na muuaji Baraba kwamba awe huru huku akitajwa kwa jina lakini Yesu akitajwa kama huyu? Je wadhani Yesu na baraba ni nani alikuwa maarufu zaidi?

Biblia au neno la Mungu linatueleza wazi kuwa Yesu Kristo ndiye alikuwa mtu maarufu zaidi katika karne yake kuliko mtu awaye yote, Yeye aliandamwa na maelfu ya watu kila alikokwenda ili waponywe magonjwa yao na kusikiliza hekima yake na mafundisho yake na wengine wakitaka tu kumuona, nataka nikuwekee wazi kabisa kuwa haikuwa jambo rahisi kuweza kumfikia Yesu hata kwa karibu, Bibliainaeleza kuwa watu walipanda hata juu ya miti ili angalau waweze kumuona

Luka 19:2-4Na tazama, palikuwa na mtu, jina lake Zakayo, mkubwa mmoja katika watoza ushuru, naye ni tajiri. Huyu alikuwa akitafuta kumwona Yesu ni mtu wa namna gani, asiweze kwa sababu ya umati wa watu, maana ni mfupi wa kimo.  Akatangulia mbio, akapanda juu ya mkuyu apate kumwona, kwa kuwa atakuja kuipitia njia ile” unaweza kuona Biblia inaeleza kuwa huyu alikuwa mtu mkubwa, tena alikuwa tajiri nyakati za leo tungeweza kumfananisha mtu huyu kama alikuwa waziri wa fedha hivi, alitamani kumuona Yesu lakini ilikuwa ni ngumu sana, maelfu ya watu walikuwa wakimzingira Yesu pande zote alikuwa maarufu Yesu kuliko mtu yeyote,


Luka 5:19Hata walipokosa nafasi ya kumpeleka ndani kwa ajili ya lile kundi la watu, walipanda juu ya dari wakampisha katika matofali ya juu, wakamshusha yeye na kitanda chake katikati mbele ya Yesu.” Wako watu walikosa nafasi ya kumuona Yesu kiasi ambacho walitoboa dari ya nyumba ili angalau waweze kufikisha mgonjwa wao kutokana na Yesu kuzungukwa na umati mkubwa wa watu, Yesu alikuwamaarufu kuliko mtu awaye yote, wewena mimi hata tukipanda daladala hakuna hata mtu mmoja anashituka au kugeuka kukuangalia, kondakta anaweza hata kukuamboa brother adjust tuikae watano watano hapo kati, Hii haikuwa hivyo kwa Yesu alijulikana mno, Biblia imejaa mifano mingi na habari nyingi kuhusu Yesu kuzingirwa na umati wa watu wakihitaji huduma kutoka kwake.

Watu walimzunguka Yesu kiasi ambacho yeye na wanafunzi wake walikosa hata nafasi ya kula Marko 3:20Mkutano wakakusanyika tena, hata wao wenyewe wasiweze hata kula mkate.”
Yesu alizungukwa na watu pande zote wakati mwingine alilazimika kukaa katika chombo cha majini ili kila mmoja aweze kumuona alipokuwa akifundisha Marko 4:1Akaanza kufundisha tena kando ya bahari. Wakamkusanyikia mkutano mkubwa mno, hata yeye akapanda chomboni, akakaa baharini, mkutano wote ulikuwako juu ya nchi kavu kando ya bahari.
Yesu hata aliposafiri aliandamwa sio tu na wanafunzi wake lakini biblia inasema umati mkubwa wa watu walifuatana pamoja naye Luka 7:11 “Baadaye kidogo alikwenda mpaka mji mmoja uitwao Naini, na wanafunzi wake walifuatana naye pamoja na mkutano mkubwa”.
Yesu ndiye mtu pekee ambaye hata Mama yake na ndugu zake walipotaka kumuona walipata taabu saba kufikia kutokana na kuzongwazongwa na watu Luka 8:19 “Wakamwendea mama yake na ndugu zake, wasiweze kumkaribia kwa sababu ya mkutano.”
Yesu ndiye kiongozi pekee ambaye maelfu ya watu walikusanyika pamoja ili kumuona, alikuwa na mvuto mkubwa kiasi ambacho watu waliweza kukanyagana Luka 12:1a. “Wakati huo, makutano walipokutanika elfu elfu, hata wakakanyagana,aidha maandiko yanaeleza wazi kuwa umati mkubwa wa watu ulimfuata kila mahali alikokwenda watu walitoka uyahudi, Yerusalem, Idumeya, Yordani, Tiro na hata Sidoni yaani sehemu za Lebanon ya leo, wengine wakimfuata kutoka Galilaya

Marko 3:7-10 “Naye Yesu akajitenga, yeye na wanafunzi wake, akaenda baharini. Mkutano mkuu ukamfuata, kutoka Galilaya, na Uyahudi, na Yerusalemu, na Idumaya, na ng'ambo ya Yordani, na pande za Tiro na Sidoni, mkutano mkuu, waliposikia habari za mambo yote aliyokuwa akiyatenda, wakamwendea. Akawaambia wanafunzi wake ya kwamba chombo kidogo kikae karibu naye, kwa sababu ya mkutano, wasije wakamsonga. Maana aliponya wengi, hata wote waliokuwa na misiba wakamrukia wapate kumgusa.”
Luka 9:12 “Na jua likaanza kushuka; wakamwendea wale Thenashara, wakamwambia, Uage mkutano, ili waende katika vijiji na mashamba ya kandokando wapate mahali pa kulala na vyakula, maana hapa tulipo ni nyika tupu”.  Yesu aliandamwa na umati mkubwa wa watu ambao walikuwa hawataki kumuachia kundi hili kubwa sana la watu walishuhudia miujiza ya ajabu ya kihistoria walishuhudia pia wakilishwa mikate na Yesu kiasi cha kushibisha biblia inataka kuwa wanaume 5000 walilishwa bila kuhesabu wanawake na watoto, vilema waliponywa, vipofu walifunguliwa, pepo walitolewa, wafu walifufuliwa na miujiza mingine mingi ya kuwahudumia watu      Biblia inaeleza kuwa Nafasi isingeliweza kutosha kuelezea kila alilolifanya Yesu Yohana 21:25 “Kuna na mambo mengi aliyoyafanya Yesu; ambayo yakiandikwa moja moja, nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa vile vitabu vitakavyoandikwa.”
Yesu aliwaponya wote walikuwa wanaumwa Mathayo 12:15, Alipowaona umati mkubwa wa watu waliokuwa kama kondoo wasio na Mchungaji aliwahurumia Mathayo 14:14 na umati mkubwa wa watu walimfuata kwa sababu waliona miujiza na ishara na jinsi alivyoponya wagonjwa Luka 19:37 lakini kama haiztoshi umati mkubwa sana ulikuwa pamoja naye alipomfufua lazaro Yohana 12:17  
Unaweza kupata picha na ushahidi wa kimaandiko namna na jinsi Yesu alivyokuwa mtu muhimu sana katika jamii, yeye hakuwa muhalifu, alizunguka huko na huko akiwahudumia watu na kuwahurumia na kuwaponya yeye alikuwa mwema sana katika maisha yao.

Kwa nini makutano walimchagua Baraba?

Swali linakuja sasa kwa nini Pilato alipowataka watu wayahudi hadharani kuchagua Mfungwa mmojawapo kati ya Yesu  mtenda miujiza na Baraba  muuaji watu walichagua tusichikidhani? Mbona ni kama jibu lilikuwa wazi sana lakini eti watu walijibu tena bila ya kumtaja jina Bwana Yesu kana kwamba hakuwa na faida yoyote kwao? Muondoshe huyu, tufungulie Baraba,
Uchaguzi huu wa watu unatuthibitishia wazi kuwa wakati huu Yesu hakuhesabika kuwa ni wa thamani kabisa, na alidharaulika na kutokuonekana kuwa kitu kwamkiwango ambacho baraba alionekana kuwa wa muhimu, umuhimu wa Yesu na Baraba kwa jamii ulikuwa na tofauti kubwa sana, wayahudi na jamii ya watu waliokuwepo sio tu kuwa walipiga kelele kuwa waachiwe Baraba lakini pia walionyesha wazi kuwa wanchukizwa na hawampendi kabisa Yesu Luka 23:23 inasema wazi kabisa kuwa walipiga kelele kwa nia moja wakisema Msulubishee msulubishee, hii inaonyesha wazi kuwa watu hawakuwa wamevutiwa na Yesu wala kazi zake
Hali halisi iliyokuwepo inaweza kukutoa Machozi kama tungekuwepo na sisi pale, tukiacha ujuzi kuwa Mungu alikuwa kazini kuwaokoa wanadamu na kuwafia wenye dhambi baraba akiwa mmoja wao, Lakini tujiulize je walikuwa wapi wale ambao kwa dhati kabisa walitemntewa mema na Yesu live? Liko wapi lile kundi lililokuwa likimfuata? Wako wapi wale waliokula mikate wakashiba na kutaka kumfanya kuwa mfalme?, je walishindwa kusema muachie Yesu kwa sababu mimi nilikuwa kipofu na sasa kwaajili yake ninaona? Wako wapi walemavu walioponywa? Wako wapi waliotolewa Pepo?, wako wapi walioponywa magonjwa yao? Wako wapi maakida ambao Yesu aliwaponya watumwa wao, yuko wapi mwanamke aliyekuwa akitokwa na damu na Yesu akamponya, yuko wapi Zakayo aliyetembelewa na Yesu Nyumbani kwake, yuko wapi Lazaro angeweza kusema mimi nilikuwa maiti siku nne huyu jamaa akanifufua, wako wapi wale waliomshangilia siku ya mitende na kutandaza nguo zao njiani na kuimba Hosana mwana wa Daudi?, yuko wapi yule aliyetolewa Jeshi kubwa la mapepo, wako wapi watu kutoka Galilaya, Yerusalemu, Dekapoli, Yudea, Tiro na Sidoni, Kama Yesu alikuwa akizxungukwa na watu mpaka anakosa nafasi ya kula ilikuwaje siku hii?
Hakuna mtu aliyemfikiri Yesu kuwa ni wa muhimu kwa wakati huu, Muimbaji mmoja wa kitanzania aliyeitwa Patric Balisidya aliimba akisema “ni mashaka ya hangaiko wema hawana maisha” akiwataja watu wema ambao walikuwa wema kwa watu wao lakini hata hivyo waliuawa dunia imejawa na chuki na wivu na ndiyo yaliyoipamba dunia, wema wamepakwa majivu wala hawaonekani, je itakuwaje kizazimkile wakifufuka na kuona leo Majengo makubwa yakiwa yamejengwa na watu wakimuabudu Yesu, au wakiona watu waliokuwa waovu kuliko baraba wakiwa wamebadilishwa kabisa kitabia wangesemaje? Wangesema wao walikuwepo na kuwa sisi leo tumechagua vibaya?

Mwondoshe huyu, utufungulie Baraba.!

Swali bado linabaki kwa nini umati huu haukumtetea Yesu, ukiachilia zile sababu za kiroho kuwa ni ili mapenzi ya Mungu ya kuwaokoa wenye dhambi yaweze kutimizwa? Kuna ukweli ulio wazi kibiblia kwamba chuki hii ilipandwa, chuki hii ilikuwa ni mbegu iliyopandwa kutoka kwa viongozi wa dini, chuki ni mbegu mbaya, mbegu mbaya kwa kawaida hustawi haraka na kwa nguvu zaidi kiasi cha kuweza kuharibu jamii, ilichukua muda mfupi sana wanyarwanda kuuana kwa mamia na maelfu kwa sababu tu mbegu ya chuki ilipandwa, mbeguu hii ya chuki ilipandwa na adui ilipandwa na shetani kupitia viongozi wa kidini  biblia inaweka wazi kuwa wao ndio waliowashawishi makutano  wamchague baraba Mathayo 27:20 biblia inasema “ Nao wakuu wa makuhani na wazee WAKAWASHAWISHI makutano ili wamtake Baraba, na kumwangamiza Yesu.”  Unaweza kuona pia katika Marko 15:11Lakini wakuu wa makuhani WAKAWATAHARAKISHA makutano, kwamba afadhali awafungulie Baraba.
Maandiko yanaonyesha kuwa chuki dhidi ya Yesu ilipandwa tu, ilikuwa ni mbegu kutoka kwa shetani, ilipandikizwa dhidi ya Yesu viongozi hawa wa dini walikuwa ni maadui wa Yesu, walipinga kila alichokuwa akikifanya, walipanga mipango ya kumuua, walitafuta makosa hata ya kutunga kwaajili yake, walitaharakisha na kuwachochea makutano wachague lililo ovu, wakati wote tunapoona watu wakitenda maovu ni lazima uelewe kuwa kuna mchochezi, alisema Sulemani kuwa moto hauwezi kuwaka pasipo kuchochewa kwa kuni, Mungu alikuwa amewapiga upofu kuchagua uovu na kukataa wema Yesu alikuwa amekwisha kuwaonya mbeleni kuwa ikiwa wameutendea vile mti mbichi itakuwaje kwa mti mbichi?
Inasikitisha kuwa watu waliacha kumuamini Yesu na waamini uongo, waliacha kumuamini mtenda miujiza wakaamini viogozi vipofu wa kidini, Mbegu ya chuki inapoingia katika eneo lolote lile hata kutaja jina lako inakuwa shida Yesu sasa anatajwa kama “huyu” mwondoshe huyu! Tufungulie Baraba
Ni wazi kabisa hata katika jamii leo watu wanaamua kuchagua njia mbovu na kuacha kuacha njia njema, leo ukisimama kupinga uovu na kuwashauri watu wema unaonakana kama adui,watu wenye akili leo na walioendelea wanapiga kura kuchagua uovu na kupitisha uovu huku wakiwa na majina yanayoashiria kuwa wao ni wa upande wa Mungu?  Katika wakati huu wa pasaka ni muhimu kila moja kujiuliza nani aondoshwe na nani afunguliwe! Nakushauri muondoshe Baraba katika maisha yako na mfungulie Yesu kristo mlango katika moyo wako
Yeye aliahidi kuwa anagonja na mtu akifungua ataingia kwake na kukaa naye Pasaka hii mkaribishe Yesu na mfukuze baraba katika maisha yako, usikubali kuangalia umati wa watu wanasemaje na wana maoni gani wewe simama umtetee Yesu hadharani.
Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.