Jumanne, 1 Oktoba 2019

Bwana atawapigania nanyi mtanyamaza kimya!


Kutoka 14:10-14 “Hata Farao alipokaribia, wana wa Israeli wakainua macho yao, na tazama, Wamisri wanakuja nyuma yao; wakaogopa sana; wana wa Israeli wakamlilia BWANA. Wakamwambia Musa, Je! Kwa sababu hapakuwa na makaburi katika Misri umetutoa huko ili tufe jangwani? Mbona umetutendea haya, kututoa katika nchi ya Misri? Neno hili silo tulilokuambia huko Misri, tukisema, Tuache tuwatumikie Wamisri? Maana ni afadhali kuwatumikia Wamisri kuliko kufa jangwani. Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. BWANA atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya”.


Utangulizi:

Kutoka kwa wana wa Israel katika nchi ya utumwa huko Misri ilikuwa ni kama ishara kuu ya mwanzo mpya wa taifa la Israel, ilikuwa ndio siku yao ya kupata uhuru chini ya uongozi shupavu wa Musa, Hii ilikuwa ni siku ya kukumbukwa mno, Mungu mwenyewe aliwaamuru waikumbuke siku ile; Siku waliyokula Kondoo wa Pasaka!, Siku waliyoondoka katika nchi ya utumwa huko Misri.

Kushushwa kwa Bendera za kikoloni katika Nchi nyingi za Afrika na kupandishwa kwa bendera huru za mataifa ya Afrika ulikuwa ni mwanzo mpya wa matumaini makubwa ya kuishi kwa furaha na amani na utulivu tukiwa na Uhuru wetu, Kuoa au kuolewa, kwa wengi wetu ulikuwa ni mwanzo wa maisha mapya ya matumaini, hali kadhalika kumaliza shule na kupata vyeti vyetu vya aina mbalimbali, ulikuwa ni mwanzo mpya wa matumaini ya maisha mapya ya ndoto zetu, kuanza biashara, na mipango mingine mingi na hata kuokoka na kuanza imani yetu kwa nguvu tukiwa na uhusiano mgumu wenye nguvu na Mungu kote kunatujengea matumaini mapya na mwanzo mpya wa furaha na amani nyingi. Hii ni hali ya kawaida katika maisha ya binadamu, bila matumaini hatuwezi kuwa na mwanga mpya unaotuongezea nguvu ya kuishi na kusonga mbele. Lakini kama ilivyokuwa kwa wana wa Israel siku ile walipotoka Misri na utumwani kwa furaha; Uhuru wao ulionekana kama sio uhuru kamili kwa sababu Farao mfalme wa wamisri alighairi mpango wake wa kumuachia Musa na wana wa Israel kuwa huru, na hivyo yeye na majeshi yake yote walikusudia kuwarejeza utumwani, katika nchi ile ya taabu kule walikoteseka mpaka wakamlilia Mungu ili awaokoe! Hebu kumbuka walivyolia mpaka Mungu akawasikia na kumtuma Musa


Kutoka 3:7-10 “BWANA akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa. Haya, basi, nitakutuma sasa kwa Farao, ili upate kuwatoa watu wangu, hao wana wa Israeli, katika Misri.

Hali ya wana wa Israel kule utumwani Misri ilikuwa mbaya, Misri wakati huu lilikuwa ndio taifa kubwa duniani (Super Power Nation), walikuwa na Teknolojia ya hali ya juu kwa wakati huo nguvu ya kijeshi na kiuchumi ya hali ya juu ya ulimwengu wa waakati ule, utaratibu wa Kalenda za mwaka, sayansi ya tiba lakini nguvu za kiuchumi na kijeshi hali kadhalika uwezo wa nguvu za giza, wachawi na uabudu miungu uliokithiri; hakukua na taifa lingeweza kuthubutu kupigania uhuru wa Israel kutoka Misri isipokuwa Mungu mwenyewe, Na kwa hakika Mungu aliwasaidia, Mungu alimuadhibu Farao kwa mapigo makubwa mazito kumi ambayo yalimpelekea Farao na kiburi chake chote kusalimu amri, na kuwapa ruhusa Israel waende zao, maandiko yanasema Israel walindoka kwa jeuri/kwa kujiamini wakiamini kuwa chini ya Mkono wa Mungu na Musa mtumishi wake hakuna linaloshindikana lakini wakiwa katika kilele cha kufurahia mapinduzi yaliyofanywa na Mungu kwaajili yao na uhuru mzima walioupata Misri, Farao alihairisha mpango wa Mungu wa kuruhusu Israel iweze kuwa huru na kufurahia amani, kujitawala na kujitegemea! Akaamua awafuatilie na kuwarejesha Misri. Angalia.

Kutoka 14:5-8 “. Mfalme wa Misri aliambiwa ya kuwa wale watu wamekwisha kimbia; na moyo wa Farao, na mioyo ya watumishi wake, iligeuzwa iwe kinyume cha hao watu, nao wakasema, Ni nini jambo hili tulilotenda, kwa kuwaacha Waisraeli waende zao wasitutumikie tena? Akaandalia gari lake, akawachukua watu wake pamoja naye; tena akatwaa magari mia sita yaliyochaguliwa, na magari yote ya Wamisri, na maakida juu ya magari hayo yote. Na BWANA akaufanya moyo wake Farao mfalme wa Misri kuwa mgumu, naye akawafuata wana wa Israeli; kwa sababu wana wa Israeli walitoka kwa ujeuri.

Mpango wa wana wa Israel wa kufurahia uhuru wao na mpango mpya wa Mungu ulikuwa katika mashaka makubwa sana Baada ya Farao na majemadari wake kufikiri vinginevyo! Ni swala la kawaida sana kwa wanadamu kufikiri na kupanga mipango na mara tunapoiona mipangp hiyo imenyooka huwa tunajawa na furaha kubwa sana, tunakuwa na matumaini makubwa sana, na kuwaza maisha katika mwanga ulio bora!, je hujawahi kuona harusi kubwa na za kifahari zikifungwa? na nyingine kurushwa moja kwa moja katika vituo vya televisheni na watu mashuhuru wakihudhuria? Je huwa inachukua muda gani kuona ndoa hizo zikidumu na kukosa migogoro, ni mara ngapi tumeona na kushuhudia waliopendana wakitengana na kuanza kutumiana vijembe kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, mara ngapi watu wamekuwa na mipango mizuri ya kibiashara na wakaianza kwa ujeuri/kwa matumaini lakini inafikia kati kila kitu kinasambaratika? Mara ngapi tumewasaidia watu na kisha wakageuka kuwa mwiba katika maisha yetu, mara ngapi tumesalitiwa na tunaowapenda na kuwaamini? Mara ngapi ndoto zetu zimezimika na tukabaki tunalia na kutamani hata kufa? Mara ngapi tumejuta katika maisha yetu kuwa kama tungalijua yatupasayo kufanya tumgeweza kuyafanya hii ndio ilikuwa hali ya wana wa Israel walipotazama nyuma na kuona majeshi ya Farao yakiwakabili, ukweli ni kuwa walivunjika moyo na walikata tamaa sana, walimlilia Mungu lakini pia walimlaumu Musa, na waliona ilikuwa vema kama wangelikuwa watumwa wa wamisri kuliko kufia jangwani, walimlaumu Musa waliona kama mipango yake ilikuwa ikileta maumivu makubwa zaidi kuliko kule walikokuwa wakitoka walilia kwa kukata tamaa!

Kwa mujibu wa maelezo ya wataalamu wa Kijeografia eneo ambalo waisrael walikuweko lilikuwa ni eneo ambalo hawangeweza kwenda kushoto wala kulia wala kurudi nyuma, Nyuma ya Israel walikuwa wakikabiliwa na wamisri na mbele yao ilikuweko bahari ya shamu, kushoto na kulia kwao hakukuwa na upenyo ukweli walikuwa katika eneo dhahiri lisilo na upenyo, waliwekwa kwenye kona na ni wazi kabisa kilichokuwa kinawakabili kwa macho ya kawaida ilikuwa ni kifo tu, au kurudi utumwani, hawakuwa wamefunuliwa mpango kamili wa Mungu, hawakuwa wanajua kwamba kile alichokisema na kukifanya Mungu kulipaswa kuaminiwa kwa gharama yoyote ile  bali walikata tamaa! Tena walivunjika moyo na zaidi walilia machozi!

Hapa ninazungumza na watu ambao wamekata tamaa, matumaini yao ya kupona, kufanikiwa katika nyanja mbalimbali yanaonekana kama yamegonga ukuta, wale waliokuwa na ndoa zenye furaha na amani na mahusiano bora yaliyokuweko wakati wa uchumba wao sasa wanakutana na hali tofauti kabisa ndani ya ndoa zao, wale waliokuwa wakisomea fani za aina mbalimbali na kuwa na ndoto za kupata kazi na kuajiriwa sasa wametundika degree zao, hawana ujuzi wowote kila kazi wanayojaribu kuiomba wanaambiwa kuwa inahitajika mtu mwenye uzoefu, wengi wanajuta heri nisingechukua degree ya sheria, ualimu, uchumi, siasa, uongozi, miamba na kadhalika, Nchi nyingi za Afrika pia zimepitia katika hali kama hizi, watu walipopata uhuru walitegemea kuwa watakuwa na wakati mzuri wa kufurahia uhuru wao, walijua mambo yatakuwa mteremko baada ya kuwafukuza wakoloni, Japo wengi wamepiga hatua lakini wengi wanajuta na kusema heri tungeendelea kutawaliwa na wakoloni, hawajui mpango wa Mungu wa kutuacha tukawa huru, waliooa na kutana na changamoto wanajuta na kusema heri nisingeliolewa au heri nisingelioa, waliookoka wanaweza kusema heri nisingeliokoka, na hata walioitwa wanaweza kusema heri nisingelikubali wito wa kumtumikia Mungu, wengine wametumbuliwa, wengine wamepoteza umaarufu, wengine kila wakijaribu kutoka ni kama iko nguvu inawakandamiza chini ni kama hawaoni upenyo na wamekata tamaa wanalia kwa sababu hawazijui njia za Mungu,  waliojaribu biashara  wanasema ningejua nisingelijaribu biashara hii, waliotapeliwa na kulizwa wanajuta kwa kusema laiti ningelijua! Kuna majuto na kukata tamaa kila sehemu katika maisha yetu mambo hayapaswi kuwa hivyo!

Ni muhimu kuwa na ufahamu wa kutosha ya kwamba Mungu hataki tukate tamaa, Yeye anao mpango kamili juu ya maisha ya kila mmoja wetu, wakati mwingine Mungu anao mpango mzuri moyoni mwake na wakati mwingine anaweza kulifunua alifanyalo au atakalolifanya kwa kupitia watumishi wake au wale wanaotuongoza kisiasa lakini pia tunaweza kuyajua mapenzi yake kwa kuliangalia neno lake, Hakuna sababu ya kumlaumu Mungu, wala kuwalaumu viongozi wetu wala sera kadhaa za Taifa letu wala hatupaswi kujilinganisha na wengine tusikate tamaa Mungu hawezi kutuwazia mambo mabaya kama ilivyokuwa kwa wana wa Israel Mungu anatuwazia mema Neno la Mungu linasema katika
Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho
.

Mungu alikuwa na mpango mwema kwa wana wa Israel alikusudia kuwaweka huru kweli kweli alikusudia kuwasambaratisha wamisri ili wasirejee tena tabia yao ya kuwafuata fuata watu wa Mungu lakini mpango huu haukuwa wazi kwa Israel wote hawakuelewa, machoni pao waliona kifo na hali ya kukatisha tamaa lakini Musa alikuwa ameelezwa wazi na Mungu na kwamba angeshughulika na Farao angalia

Kutoka 14:1-4 Biblia inasema hivi “BWANA akasema na Musa, akamwambia, Waambie wana wa Israeli, kwamba warudi na kupiga kambi yao mbele ya Pi-hahirothi, kati ya Migdoli na bahari, kukabili Baal-sefoni; mtapanga mbele yake karibu na bahari. Naye Farao atasema katika habari za wana wa Israeli, Wametatanishwa katika nchi, ile jangwa imewazuia wasitoke. Nami nitaufanya uwe mgumu moyo wa Farao, naye atafuata nyuma yao; nami nitajipatia utukufu kwa Farao, na kwa jeshi lake lote; na Wamisri watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA. Basi wakafanya hivyo.  

Unaona Mungu hakuwa amemweleza Musa kuwa atafanya nini lakini Mungu alikuwa amemthibitishia Musa wazi kuwa hali watakayoipitia wana wa Israel italeta utukufu mkubwa kwa Mungu! Na ndio maana walipokuwa wakilalamika na kuonyesha kukata tamaa kutokana na hofu kuu Musa alikuwa anajua wazi kuwa Mungu atafanya jambo, Mungu atafanya kitu katika maisha yao alifahamu wazi kuwa Bwana atawapigania na kuwa nao watanyamaza kimyaa, Mungu alimwambia Musa kuwa awaambie wana wa Israel wasonge mbele waendelee na mpango wa kuelekea kanaani bila kujali kuwa nini kinawakabili nyuma yao.

Tatizo kubwa la wana wa Israel walikuwa hawayajui kabisa Mapenzi ya Mungu, wala hawakujua kuwa walikuwa wanapaswa kufanya sehemu yao wao walipaswa kusonge mbele, walipaswa kuendelea kujaribu tena na tena bila kukata tamaa walipaswa tu kusonga mbele, nisikilize kuwa mjane hakumaanishi kuwa Mungu amekusudia uaibike, kuwa yatima haimaanishi kuwa Mungu amekusudia kukwamisha mpango wake kwako, kufilisika au kushindwa kulipa mkopo wako haimaanishi kuwa kila kitu kimeishia hapo, kutumbuliwa au kuondolewa madarakani hakumaanishi kuwa Mungu amemaliza na wewe Mungu ana makusudi mema na mpango na maisha yako wewe songa mbele Liko jambo jema usilolijua limefichwa nyuma ya jaribu lako na ushindi wake ni wewe kutokukata tamaa.
Iko mifano kadhaa ya watu ambao walikutana na changamoto mbalimbali katika maisha yao na walisonga mbele na wakawa watu wakubwa sana duniani na maarufu sana lakini waliishinda siri ya kukata tamaa, walishinda vikwazo, walishinda sauti za nje zinazowambia umekwisha, huwezi tena na kadhalika ni marufuku kabisa  kukata tamaa, ni mwiko usikate tamaa ni sumu yaw ewe kuinuka tena angalia mifano hii
1.      Mwana sayansi Thomas Edison tumtafakari!

Je umewahi kufeli katika maisha yako labda mara moja au mbili? Je mwalimu wako amewahi kukuita mjinga? Kwa sababu umeshindwa kujibu maswali rahisi tu ya somo la hisabati? Je umewahi kutimuliwa kazini zaidi ya mara moja? Hauko peke yako Sir Thomas Edison mgunduzi wa balbu yaani Taa za umeme hakuwa na akili kama unavyodhani alikuwa nazo, Yeye aliambiwa na mwalimu wake kuwa hana analoliweza na alipoteza matumaini, alisimama masomo akiwa na miaka 12, Mzazi wake akielezwa kuwa mtoto wake ni mbumbumbu wa mwisho hakuna mwalimu anaweza kumsaidia, Hata katika ugunduzi wake wa taa za balbu alikosea na kushindwa mara 1000, aliwahi kufukuzwa kazini mara kadhaa, lakini haya hayakuwahi kumkatisha tamaa hata siku moja badala yake alipuuzia kabisa kila aina ya kukoseolewa alikokutana nako hakuwahi kukata tamaa, Huyu ndiye aliyegundua taa za Umeme Duniani, unaonaje kama angekata tamaa Bado tungekuwa tunatumia mishumaa na vibatali duniani hata leo, “kila jaribio moja utakalolikosea linakupa hatua moja zaidi mbele” wewe pia mwisho wako bado usikubali kumuacha adui yako aone machozi yako, wala usikubali kushindwa kwa haraka namna hiyo je umejaribu mara 1000? Usikate tamaa!


Pichani mwansayansi Thomas Edison Mgunduzi wa taa za Umeme Duniani

2.      J.K. Rowling
Je unamjua mtu awaye yote ambaye ni tajiri kuliko Malikia wa uingereza? Kama hujui ni mwanamama JK. Rowling, mwandishi maarufu wa mtiririko wa Mashairi yaitwayo “Harry Potter”, Yeye ana utajiri unaozidi Pound Billion 1.  Hakuzaliwa akiwa anatumia hata kijiko cha fedha  mdomoni mwake, hakuwa bora kwa lolote katika maisha yake ya awali na kuna wakati aliishi katika nyumba za kupanga huko Edinburgh nyumba ambazo zilikuwa za watu wa hali ya chini  na zenye usumbufu mkubwa wa panya, alikuwa ni mama asiye na mume aliyepambana mpaka jasho lake la mwisho kupata mahitaji yake ya siku tunaweza kusema alikuwa na maisha mabaya ya dhiki mno, hakuwa na ajira yoyote, na hakustahili hata kulea mtoto wa Mchapaji “Typewriter” wa kazi yake ya ushairi wakati alipoanza kuchapa kitabu chake, na hakuweza kuwa hata na nafasi ya kuchapa kwa amani akiwa nyumbani kwake isipokuwa kwenda katika ofisi ya uchapaji tu, Ukiacha kuwa leo kuna vitabu vyake vingi tunavyosoma kitabu chake cha kwanza kilikataliwa mara 12, Lakini msimamo wake na kutokukata tamaa umemfanya sasa kuwa mwanamke aliyefanikiwa sana na kuwa mfano wa kuigwa.

Ndugu msomaji wangu inawezekana unapitia katika hali fulani ngumu mno na badala ya kusonga mbele unakaata tamaa; wana wa Israel walikata tamaa walilia walimlaumu Musa na Musa alimlilia Mungu lakini majibu ya Mungu ilikuwa waambie wana wa Israel wasonge mbele

Kutoka 14:15 “BWANA akamwambia Musa, Mbona unanililia mimi? Waambie wana wa Israeli waendelee mbele.


Mungu atataka watu wasiokata tamaa watu watakao jaribu tena na tena kama Thomas Edison aliyegundua taa ya umeme alijaribu mara 1000 je wewe umejaribu mara ngapi, Mungu anakutaka usonge mbele, acha kuwalaumu viongozi wa kisiasa, acha kulaumu mfumo wa katiba na kudhani kuwa katiba mpya itakuwa suluhu ya matatizo yako,  acha kulaumu wazazi wako kuwa hawakukusomesha, acha kulaumu kuwa eti ulifukuzwa chuo , acha kulaumu kuwa ni kwa sababu hujaoa mke sahihi, au hujaolewa na mume sahihi, acha kulaumu kuwa ni kwa sababu ya talaka, acha kulaumu ni kwasabu etu ulidhulumiwa mirathi, acha visingizio, “Fumdi mbovu siku zote husingizia vifaa vyake “ hata kila kitu kikibadilishwa kama sisi hatutakuabali kufanya wajibu wetu hatuwezi kamwe kuona mambo mazuri ambayo Mungu ametuandalia katika dhiki na mateso tusiyoyajua, ni lazima tukubali kuzitumia changamoto tulizo nazo kama fursa, Hakuna ndege inaweza kupaa juu bila upinzani wa upepo, ili ndege ipae juu kwa urahisi inahitaji upinzani mkali sana wa upepo ndipo inapaa juu kabisa, Mungu anajua umuhimu wa changamoto katika maisha yetu na hivyo huziruhusu kwa utukufu wake

Mapito ya wana wa Israel haikuwa kitu kigeni kwa Mungu, Kwani yeye alikusudia moyo wa Farao uwe mgumu ili ajitwalie utukufu, sio hivyo tu aweze kukomesha kabisa Jeshi la Misri ili wasiwepo milele, ni wazi kuwa Misri na jeshi lote wangeendelea kuwepo wageweza kuwasumbua Israel hata kama wangefika kanaani kutokana na uwezo wao, hivyo Mungu alitaka ammalize adui kabisa ili Israel waende salama na waweze kuwa huru kwelikweli, Mungu alieleza mpango wake wazi kwa Musa katika


Kutoka 14:1-4 “BWANA akasema na Musa, akamwambia, Waambie wana wa Israeli, kwamba warudi na kupiga kambi yao mbele ya Pi-hahirothi, kati ya Migdoli na bahari, kukabili Baal-sefoni; mtapanga mbele yake karibu na bahari. Naye Farao atasema katika habari za wana wa Israeli, Wametatanishwa katika nchi, ile jangwa imewazuia wasitoke.  Nami nitaufanya uwe mgumu moyo wa Farao, naye atafuata nyuma yao; nami nitajipatia utukufu kwa Farao, na kwa jeshi lake lote; na Wamisri watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA. Basi wakafanya hivyo.”

Musa alikuwa anaufahamu mpango huu na kwa imani aliwatia moyo wana wa Israel kuwa wasiogope wasimame (Maana yake wasitikisike, maana yake wasonge mbele, maana yake wasiogope, maana yake wasione kuwa mwisho umefika, maana yake wasione kuwa Mungu hana mpango kamili dhidi yao) Mungu alikuwa amekusudia mema licha ya Israel kuwa na hofu Musa kama nabii alijua kuwa Mungu atafanya kitu alikuwa na imani kali sana alimuamini, yeye alishakuwa na uzoefu wa kutosha kuwa Mungu akisema lazima atatenda, aliamini kuwa Mungu hajawahi na hatawahi kuwmuangusha na alitabiri kuwa huo utakuwa mwisho wa majeshi ya Farao ingawa Musa hakuwa anajua kuwa Mungu atafanya kwa namna gani lakini imani yake ilikuwa juu sana kuwa kiko kitu Mungu atakifanya angalia maneno yake  katika


Kutoka 14:13-14 “Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. BWANA atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya
.

Msomaji wangu nataka kukuhakikishia ya Kwamba Mungu yuleyule aliyeabudiwa na Musa na manabii, Mungu wa Israel ndiye Mungu wa Dunia nzima ndiye Mungu tunayemuabudu acha kuamini kelele za wapita njia acha kuangalia ukubwa wa mawimbi ya kipinzani au ukubwa wa majaribu yanayokukuta Mungu yule nimwabuduye ni mkuu kuliko tatizo lako, Nasimama leo kama nabii Musa wa katika kizazi hiki  kukutia moyo ya kwamba songa mbele acha kulia, Mtazame Bwana Yesu, Uko upenyo mkuu juu ya shida zako, uko ufumbuzi, liko jibu la changamoto yako, Mungu anao mpango kamili katika maisha yako endelea kupambana mpaka dakika ya mwisho muombe Mungu na msihi akufungulie milango na fanya kazi kwa bidii panga pamoja na Mungu naye atakutokea, Songa mbele lawamba na vilio havina majibu songa mbele. Mungu atakusaidia katika jina la Yesu!

Bwana Yesu mtumwa wako ninaomba kwaajili ya msomaji wangu, tafadhali usimuache katika hali aliyo nayo, kama ulivyowasaidia wana wa Israel chini ya Musa Mtumishi wako naomba umsaidie yeye naye ili kwaajili ya utukufu wako hali anayoipitia iweze kuwa historia ya maisha yake na umpeleke katika kiwango kingine, Mungu mwenye uwezo wa kuinua wanyonge kutoka jalalani na kuwaketisha na wakuu ufanye hivyo kwa kila mmoja wetu na watanzania kwa ujumla Katika jina la Yesu Kristo Amen!

Asante kwa sababu utaondoa na kuitowesha kabisa hali ya kukata tamaa inayomkabili kila moja kwa jinsi yake, Naikemea hali ya kukata tamaa ndani ya kila mmoja wetu katika jina la Yesu Kristo Amen!
USIKATE TAMAA WAKATI WA DHIKI!
Rev. Innocent Kamote Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!..
0718990796

Jumapili, 22 Septemba 2019

Yeye aliye na Funguo za mauti na Kuzimu!

Ufunuo 1:17-18Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho,  na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.


Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu wazi kwamba tunaishi katika kizazi ambacho watu wanajaribu kujisahaulisha kuhusu kifo, watu wanajaribu kusahau kuwa kifo kipo, na kwa namna fulani wanadamu wanajaribu kila siku kubadili mtazamo wa kifo, kwa kuboresha Majeneza mazuri na kuyapamba kwa maua kiasi ambacho kifo kinaonekana kama ni monawapo ya sherehe ya kumuaga mtu, na sio hivyo tu hata makaburi yanapambwa kwa kujengewa vizuri kwa kiasi cha kugeuka kuwa bustani na maeneo ya kutembelea, hii yote ni kujaribu kukifanya kifo kionekane kuwa sio kibaya ! Laiki ukweli unabaki pale pale kuwa kifo ni adui mkubwa sana wa Mwanadamu  1Wakoritho 15:25-26 “Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti
Kifo ni tamko la Mungu ambalo limetamkwa kuwa kama mwandamu angemuasi Mungu basi kifo kigekuwa moja ya sababu ya uharibifu mkubwawa mwanadamu, kwa hiyo tangu mwanadamu anapozaliwa adui mkubwa anayefuata na kuanza kupambana naye ni mauti.
Yesu aliwajulisha wanafunzi wake mapema kuwa nao watakufa, tena watakufa kwaajili ya imani katika yeye Yohana 21:18-23 “Akasema, Amin, amin, nakuambia, Wakati ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga mwenyewe na kwenda utakako; lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka. Akasema neno hilo kwa kuonyesha ni kwa mauti gani atakayomtukuza Mungu. Naye akiisha kusema hayo akamwambia, Nifuate. Petro akageuka akamwona yule mwanafunzi aliyependwa na Yesu anafuata; (ndiye huyo aliyeegama kifuani pake wakati wa kula chakula cha jioni, akasema, Bwana, ni nani akusalitiye?) Basi Petro akamwona huyo, akamwambia Yesu, Bwana, na huyu je? Yesu akamwambia, Ikiwa nataka huyu akae hata nijapo, imekupasaje wewe? Wewe unifuate mimi. Basi neno hilo lilienea katikati ya ndugu ya kwamba mwanafunzi yule hafi. Walakini Yesu hakumwambia ya kwamba hafi; bali, Ikiwa nataka huyu akae hata nijapo, imekupasaje wewe?

Yesu alikuwa amewatabiria wanafunzi wake namna watakavyokufa kwaajili ya imani, na sasa anamwambia Petro namna atakavyokufa kwa utukufu wa Mungu, Petro alimuuliza Yesu je vipi kuhusu Yohana Yesu alimjibu ikiwa nataka huyu akae hata nijapo imekuopasaje wewe? Yaani vyovyote ni takavyo kwamba afe au akae mpaka mimi nijapo wewe inakuhusu nini wewe nifuate!      Petron aliuawa huko Roma kwa kusulubiwa kichwa chini miguu juu kama alivyotabiri masihi.

Hata hivyo historia ya Kanisa inatuambia kuwa Yohana pekee ndie mtume ambaye hakuuawa bali alikufa kifo cha kawaida, lakini vilevile kwa mujibu wa mwana historia maarufu wa kanisa katoliki aitwae Jerome Mtume Yohana alipitia shida dhiki na mateso makubwa sana kwani yeye aliishi karibu miaka 100, na hivyo alipitia vipindi vya mateso makali sana, wakati wa utawala wa Tatulian aliweza kusokotwa kwenye majani na akachomwa moto na alipoamka alijikungu’ta tu na nkuendelea na safari za injili, wakati wa utawala wa Domitian alidumbukizwa kwenye pipa la mafuta ya lami na kuchemshwa lakini alitoka akiwa hai, kutokana na kuwa na ugumu wa kifo alipelekwa uhamishoni kwenye kisiwa kiitwacho patmo iali ateseke na kufia huko, hata hivyo baada ya muda walikwenda kumchungulia na kukuta akiandika kitabu cha ufunuo na walimkata mkono, waliporejea mara ya pili walimkuta akiwa na mikono yake yote, Yohana aliishi maisha ya upweke lakini aliendelea kumuabudu Mungu, hata siku ya bwana  jumapili aliiadhimisha akiwa katika roho, akiwa amechoka kwa mateso haya Ndipo Yesu alimtokea na kumuagiza aandike kitabu hiki cha ufunuo, na jambo la kwanza Yesu alilolifanya ilikuwa ni kumtia moyo, Yesu alitaka kumtia moyo Yohana na kila mmoja wetu kuwa “Yeye anazo funguo za mauti na kuzimu

Yeye aliye na Funguo za mauti na kuzimu.
Kuwa na funguo za mauti na za kuzimu maana yake ni kuwa na mamlaka, au uwezo au mamlaka ya mwiho ya kuamua kuhusu kifo, Yesu ana uwezo juu ya kifo, anauwezo wa kuamua ufe au usife, kama uwezo huu angelipewa adui yetu angetufutilia mbali mara moja, Lakini ni Yesu ndiye anayeamua ni yesu ndiye anyeruhusu yeye ndio mwenye mamlaka mwenye udhibiti Hata maisha yake aliamua yeye mwenyewe kuyatoa na hakuna mtu aliyaondoa maisha yake ilikuwa ni kwa hiyari yake mwenyewe

Yohana 10:17-18 “Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena.  Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu.”

Yesu ana nguvu dhidi ya Mauti ana mamlaka nayo na ni yeye anayeamua kuwa wale wanaomuamini watakufa lini, yaani lini awachukue wakaungane naye na wakifa awapeleke wapi? Na ni yeye mwenye mamlaka ya kufufua  ni kama Yesu alikuwa anamwambia Yohana kuwa usiogope Mimi nalikufa na sasa ni hai yaani huoni mfano wangu? Mauti haina uwezo ndani yangu, kama jinsi ambavyo haikuwa na uwezo juu yako,

Nisikilize watu wanaweza kujaribu kukuua kwa maneno na matendo, wanaweza kusema ngoja tuone familia yake itakuwaje, ngoja tuone mwisho wake utakuaje? Wanaweza kusema hapa amepatikana hapa tumemuweza, huu ndio mwisho wake, hapa tumemkomesha, hapa hachomoki, hapa tumemaliza, safari hii tumemuweza, hapa ndio mwisho wa kila kitu, tutaona watasomaje, tutaona atakwepaje mtego huu, huduma yake itakufa, amekufa kiroho, ameishiwa hana jipya, duka lake linakufa, biashara yake haiwezi kusimama, hawezi kuzaa tena, jamaa kwishinei, zilikuwa kelele za bure tuna lolote wanaweza kusema lakini Neno la Mungu linatuambia ye kuwa yukomwenye funguo, hatupaswi kuogopa kelele za wasio na funguo, namuogopa mmoja tu mwenye funguo, mwenye mamlaka ambaye yeye akifunga hakuna afunguaye na akifungua hakuna afunguaye

Ufunuo 3:7 “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Filadelfia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye mtakatifu, aliye wa kweli, aliye na ufunguo wa Daudi, yeye mwenye kufungua wala hapana afungaye, naye afunga wala hapana afunguaye.



Nataka nikutie moyo leo kuwa usiogope yeye ndiye mwenye kufungua mlango na ndiye mwenye kufunga hakuna anyeweza kushindana naye kama ipo ipo tu, ana nguvu ya kuizuia mauti.
Alizuia mauti kwa shadrak, Meshak na Abednego wakatembea kati kati ya moto, aidha alizuia makanwa ya simba kwa Daniel aliyetupwa katika matundu ya simba Mungu akaifunga mauti, kumbuka wale simba walikuwa na njaa , huyu ndiye aliyemsaidia Yohana akaangwe kwenye pipa la lami na mauti isimuweze, yeye ndiye aliyakufa akafufuka changamka huna sababu ya kuogopa adui huyu ni mdogo tu.

Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumatatu, 16 Septemba 2019

Usimwache Mchawi kuishi!


Mstari wa Msingi: Kutoka 22:18 “Usimwache mwanamke mchawi kuishi.”

Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa moja ya amri kuu katika maandiko inasema “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa roho yako yote, kwa nguvu zako zote na kwa akili yako yoteLuka 10:27, Amri hii inaonyesha wazi kuwa Mungu anataka aabudiwe yeye peke yake na kwamba kuabudu miungu mingine ni moja ya machukizo makubwa sana kwa Mungu; Kutoka 20:3-6Usiwe na miungu mingine ila mimi. Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, BWANA, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao,  nami nawarehemu maelfu elfu wanipendao, na kuzishika amri zangu.”

Swala la watu kutafuta miungu mingine nje ya Mungu mwenyezi ni swala la siku nyingi na la zamani sana na shetani amefanikiwa sana kuwafanya watu waabudu miungu mingine kupitia waganga na wachawi badala ya Mungu, shetani anatumia Waganga, wachawi, wanajimu na kadhalika ili kuwafanya watu wasimuabudu Mungu na badala yake wamuabudu yeye au washirikiane na mashetani. Maandiko yanakataza kwa mkazo mkubwa mno swala la kushirikiana na Mashetani yaani ushirikina na uganga na uchawi. 1 Wakoritho 10:20-21Sivyo, lakini vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi kunywea kikombe cha Bwana na kikombe cha mashetani. Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani.”  Paulo mtume alikataza kabisa kwa herufi kuwa Kanisa kuwa na ushirika na Mashetani, Unaposikia mtu anaitwa mshirikina maana yake ni mtu mwenye ushirika na mashetani aidha kupitia wachawi au waganga wa kienyeji, swala hili ni katazo la kibiblia katika agano la kale Mungu aliwakataza kabisa wana wa Israel kujihusisha na maswala haya kabisa na mara kadhaa agizo la kuupinga uchawi na ushirikina liliambatana na kifo!

Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-
1.       Msimamo wa agano la kale kuhusu wachwi
2.       Msimamo wa Agano jipya kuhusu Wachwi
3.       Wito na ushauri wa kimungu kwa wachawi na washirikina

Msimamo wa agano la kale kuhusu wachawi.

·         Walawi 19:31Msiwaendee wenye pepo, wala wachawi; msiwatafute; ili kutiwa unajisi na wao; Mimi ndimi BWANA, Mungu wenu

·         Walawi 20:6Na mtu yule atakayewaendea wenye pepo, na wachawi, ili kuzini pamoja nao, nitakaza uso wangu juu ya mtu yule, nitamtenga na watu wake”.

·         Walawi 20:27  Tena mtu mume au mtu mke aliye na pepo, au aliye mchawi, hakika atauawa; watawapiga kwa mawe; damu yao itakuwa juu yao.”

·         Kumbukumbu 18:10-14Asionekane kwako mtu ampitishaye mwanawe au binti yake kati ya moto, wala asionekane mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa Bwana; kisha ni kwa sababu ya hayo Bwana, Mungu wako, anawafukuza mbele yako. Uwe mkamilifu kwa Bwana, Mungu wako. Maana mataifa haya utakaowamiliki huwasikiliza wanaoshika nyakati mbaya na kutazama bao; bali wewe, Bwana, Mungu wako, hakukupa ruhusa kutenda hayo.

·         1Nyakati 10:13 tunaelezwa wazi kuwa sababu za kifo cha mfalme wa kwanza wa Israel ilikuwa ni kwa sababu alikwenda kuuliza kwa wachwi “Basi Sauli alikufa kwa sababu ya kosa lake alilomkosa Bwana, kwa sababu ya neno la Bwana, asilolishika; na tena kwa kutaka shauri kwa mwenye pepo wa utambuzi, aulize kwake, asiulize kwa Bwana; kwa hiyo akamwua, na ufalme akamgeuzia Daudi, mwana wa Yese.”

·         Hasira ya Bwana Mungu huwaka kwa mtu anayejishughulisha na maswala ya ushirikina 2Nyakati 33:6 “Tena akawapitisha wanawe motoni katika bonde la mwana wa Hinomu; akatazama bao, akabashiri, akafanya uganga, akajishughulisha na hao wenye pepo wa utambuzi, na wachawi; akafanya mabaya mengi machoni pa Bwana, hata kumkasirisha.”

Msimamo wa agano jipya kuhusu wachawi.

·         Katika matendo ya mwili yanayotajwa katika agano jipya ya watu ambao hawataurithi ufalme wa Mungu na wachawi nao wamo Wagalatia 5:19-21 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”

·         Agano jipya pia linaeleza wazi kuwa wachawi sehemu yao itakuwa ni katika lile ziwa la Moto Ufunuo 21:8 “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili.

·         Hakuna lugha ya upole kwa wachawi Biblia inaonyesha wazi kuwa mitume hawajawi kuzungumza na wachawi kwa lugha ya kubembeleza wakati wote wachawi walikemewa na kuitwa katika toba ili waamini vinginevyoa adhabu kali ilikuwa ikiambatana nao ona kwa mfano Matendo 8:9-22 “Na mtu mmoja, jina lake Simoni, hapo kwanza alikuwa akifanya uchawi katika mji ule, akiwashangaza watu wa taifa la Wasamaria, akisema ya kuwa yeye ni mtu mkubwa. Wote wakamsikiliza tangu mdogo hata mkubwa, wakisema, Mtu huyu ni uweza wa Mungu, ule Mkuu. Wakamsikiliza, kwa maana amewashangaza muda mwingi kwa uchawi wake.Lakini walipomwamini Filipo, akizihubiri habari njema za ufalme wa Mungu, na jina lake Yesu Kristo, wakabatizwa, wanaume na wanawake.Na yeye Simoni mwenyewe aliamini akabatizwa, akashikamana na Filipo; akashangaa alipoziona ishara na miujiza mikubwa inayotendeka. Na mitume waliokuwako Yerusalemu, waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawapelekea Petro na Yohana; ambao waliposhuka, wakawaombea wampokee Roho Mtakatifu; kwa maana bado hajawashukia hata mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu. Ndipo wakaweka mikono yao juu yao, nao wakampokea Roho Mtakatifu. Hata Simoni alipoona ya kuwa watu wanapewa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ya mitume, akataka kuwapa fedha akisema,Nipeni na mimi uwezo huu, ili kila mtu nitakayemweka mikono yangu, apokee Roho Mtakatifu. Lakini Petro akamwambia, Fedha yako na ipotelee mbali pamoja nawe, kwa kuwa umedhania ya kuwa karama ya Mungu yapatikana kwa mali. Huna fungu wala huna sehemu katika jambo hili, kwa kuwa moyo wako si mnyofu mbele za Mungu. Basi, tubia uovu wako huu, ukamwombe Bwana, ili kama yamkini, usamehewe fikira hii ya moyo wakoMungu ni mwingi wa Rehema na upendo lakini nataka nikueleze wazi kuwa hana huruma na wachawi hata kidogo, kila mtumishi wa Mungu mwenye mamlaka ya kimungu ameruhusiwa kuwafanya lolote wachawi kusema nao kwa ukali na kuwaamuru kuavcha hila zao mbaya maan wao ni wana wa ibilisi Matendo ya Mitume 13:8-11 “.Lakini Elima, yule mchawi (maana ndiyo tafsiri ya jina lake), akashindana nao, akitaka kumtia yule liwali moyo wa kuiacha ile imani. Lakini Sauli, ambaye ndiye Paulo, akijaa Roho Mtakatifu, akamkazia macho, akasema, Ewe mwenye kujaa hila na uovu wote, mwana wa Ibilisi, adui wa haki yote, huachi kuzipotoa njia za Bwana zilizonyoka? Basi, angalia, mkono wa Bwana u juu yako, nawe utakuwa kipofu, usilione jua kwa muda. Mara kiwi kikamwangukia na giza, akazunguka-zunguka na kumtafuta mtu wa kumshika mkono na kumwongoza.” Wachawi huzipotosha njia za Bwana zilizonyooka Paulo anamuadhibu vikali Mchawi kwa sababu anajua kuwa Mungu yuko kiyuma nao na kuwa wachwi wakati wote hupinga na shauri la Mungu, wako kinyume na Mapenzi ya Mungu, Mungu alipokuwa anataka kuwaokoa wana wa Israel kutoka Misri wachawi waliweza kuigiza miujiza ya Mungu vilevile na walichangia kwa kiasi nkikubwa ugumu wa mowyo wa farao kwa sababu farao aliona hakuna jipa angalia Kutoka 7:22 “Lakini waganga wa Misri wakafanya mfano wa hayo kwa uganga wao; na moyo wake Farao ukawa mgumu, wala hakuwasikiza, kama BWANA alivyonena”. Unaona Biblia ya habari njema BHN inasomeka vizuri katika Kutoka 7:22 inasemaLakini wachwi wa Misri kwa kutumia uchawi waowakafanyoa vivyo hivyo,Kwa hiyo moyo wa farao ukabaki kuwa mgumu naye hakuwasikiliza Mose na Aroni kama mwenyezi Mungu alivyokua amesemaWachawi hawa ni wapinzani wa mipango ya Mungu, na wakati mwingine kwa mtu mwenye moyo kama wa Farao ni vigumu kupambanua na kujua katika ya mtu wa Mungu na Mchawi, farao alifikiri Musa yuko sawa na wachawi wake tu Mpaka pale Mungu alipodhihirisha uwezo wake ndipo wachawi wa farao wakamueleza wazi kuwa hiki ni chanda cha Mungu    Kutoka 8:19 “Ndipo wale waganga wakamwambia Farao, Jambo hili ni chanda cha Mungu; na moyo wake Farao ukawa mgumu asiwasikize; vile vile kama BWANA alivyonena.”  Hakuna popote katika Biblia mchawi au mganga ameonyeshwa kuwa ni mtumishi wa Mungu hakuna. Wote wanahukumiwa na Mungu kwa ukali na dhabu kuwa ni kifo au watubu na kumgeukia Mungu, Kazi kubwa ya wachawi ni kupinga na Mungu na makusudi yake, popote pale mtu wa Mungu unapofanya jambo na kuona kuwa kuna ushindani, kuna upinzani kuna ugumu usiokuwa wa kawaida, hakuna mtiririko unaokusudiwa funguka na kukemea nguvu za upinzani shetani ujue yupo au watumishi wake na wanafanya yao hivyo butua shughulika na Yane na Yambre ambao ndio hufanya hayo wanayoyafanya  yaani wanapingana na imani 2Timotheo 3:8Na kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani.

Wito na ushauri wa kimungu kwa  wachawi na washirikina
Biblia ina wito mmoja tu kwa wachawi, watubu ili yamkini Mungu awasamehe fikira yao mbaya, waache kuzipotoa njia za Bwana zilizonyooka na watubu na kugeuka na kuchomelea mbali vitabu vyao na mikoba yao na vifaa vyao vya uchawi Matendo ya Mitume 19:19 “Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu.” Biblia inaonyesha kuwa wachawi kule Efeso walitubu na kuziharibu kabisa kazi mabaya za gharama kubwa hawakuwa na aibu waliviharibu na kuviteketeza vyote bila kujalia gharama vifaa vyote vya uchawi walivichoma moto wito wa kibiblia ni kila mtu mbaya aache njia yake mbaya na amgeukie Mungu naye Mungu atamsamehe Isaya 55:6-7Mtafuteni Bwana, maadamu anapatikana, Mwiteni, maadamu yu karibu; Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie Bwana, Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa.”
Biblia inaonya kwa ukali sana kuhusu kujihusisha na ushirikina ukweli ni kuwa hakuna neno la Huruma kwa wachawi awe mwanaume au awe mwanamke adhabu ya wachawi ni kifo tu, Katika agano jipya trehema tunayoweza kuiona ni wao kuacha uchawi na kumuamini Yesu kama Bwana na mwokozi wa maisha yao, Neno la Mungu linaposema usimuache mwanamke mchawi kuishi, liko wazi kuwa hukumu ya wachawi ni kifo tu, kama unajihusiha na ushirikiana nakuonya kwa jina la Mwenyeji Mungu acha mara moja Mgeukie Yesu, mwambie akusamehe na kama unajihusisha na uganga acha acha mara moja na ili uweze kuwa salama Mgeukie Mungu acha kuwadanganya watu, acha kutumia pepo wa utambuzi, achana na mapepo ya uuguzi, acha kutumiwa na maimuna, subian, makata na vinyamkera na aina yoyote ya majini na mapepo yanayokutokea ua kukuotesha ndoto acha nakuonya, na kama unakwenda kwa waganga tubu na usirudie tena. Vinginevyo kifo cha kimwili na kiroho kinakuhusu.

Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Mungu na wakimbizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa kuwahudumia wakimbizi ni mpango wa Mungu!, Leo tutachukua Muda wa kutosha kwa kina na upana na urefu kuangalia huduma muhimu kwaajili ya wakimbizi Duniani, Mwaka 2004 pekee karibia watu milioni tatu na nusu walikuwa ni wakimbizi barani Afrika pekee, ambao walikimbia na kuishi nje ya nchi zao, na wengine zaidi ya milioni kumi walikuwa ni wakimbizi ndani ya nchi zao, wengi walikuwa hawakimbii tumatukio ya majanga ya kiasili nlakini walikuwa wanakimbia matatizo ya kisiasa, ugomvi wa kimadaraka, matatizo ya kidini, ukabila na maswala mengineyo je neno la Mungu linasema nini kuhusu wakimbizi, kanisa limewahi kutafakari nini kuhusu wakimbizi? Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Neno la Mungu na wakimbizi
·         Mungu anawajali wakimbizi
·         Wakimbizi na mafundisho ya agano jipya

Neno la Mungu na wakimbizi:

Biblia inatambua kuweko kwa watu ambao wamewahi kukimbia huko na huko mbali na Nchi zao, kaini alikuwa mtu wa kwanza kufahamu madhara ya ukimbizi Mwanzo 4:12,”Utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake, utakuwa mtoro na mtu asiye na kikao Duniani” Neno utakuwa mtoro ni sawa na utakuwa mkimbizi. Yakobo na Familia yake waliishimaisha ya ukimbizi kutokana na majanga ya njaa nchini kwao Mwanzo 47:3-4, “Farao akawauliza hao nduguze Kazi yenu ni nini? Wakamwambia Farao, Tumekuja kukaa ugenini katika nchi hii, kwa sababu wanyama wa watumwa wako hawana malisho, maana njaa ni nzito sana katika nchi ya kanaani, Basi twakusihi uturuhusu sisi watumwa wako tukae katika nchi ya gosheni” Yesu pia alikuwa mkimbizi huko Misri kwaajili ya kuokoa Maisha yake yaliyokuwa yakitafuta na mfalme Herode Mathayo 2:13-14. “Na hao walipokwisha kwenda zao tazama malaika wa Bwana alimtokea yusufu katika ndoto, akasema  Ondoka umchukue mtoto na mama yake , ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie kwa maana Herode anataka amwangamize, Akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku akaenda zake Misri” ziko sababu mbalimbali na mazingira ya aina mbalimbali yanayoweza kusababisha kila mmoja wetu kuwa mkimbizi kwa namna moja ama nyingine.

Mungu anawajali wakimbizi

Biblia iko wazi kuwa Mungu anawajali wakimbizi, alionyesha kujalia sana maisha ya Kaini hata pamoja na kuwa ukimbizi wake ulisababishwa na makosa yake mwenyewe Mwanzo 4:15. Mungu alimwambia Musa katika Torati kuandaa miji ya makimbilio kwaajili ya wakimbizi watakaokimbilia kutokana na sababu mbalimbali ama ambao watu wangelikuwa wanatafuta kuwaua, Kutoka  21:12-14, Hesabu 35:9-34, Mstari 10-13 inasema hivi  Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapovuka mto wa Yordani na kuingia nchi ya Kanaani,Ndipo mtajiwekea miji iwe miji ya makimbilio kwa ajili yenu; ili kwamba mwenye kumwua mtu, pasipo kukusudia kumwua, apate kukimbilia huko.Na hiyo miji itakuwa kwenu kuwa makimbilio, kumkimbia mwenye kutwaa kisasi, ili asiuawe mwenye kumwua mtu, hata atakaposimama mbele ya mkutano ahukumiwe. Na hiyo miji mtakayowapa itakuwa kwenu ni miji sita ya makimbilio”.  Kumbukumbu 4:41-43, 19:3-13, Nyakati 6:42-55. Mungu aliagiza pia kuwa wageni walioambatana na Israel pia wanahitaji kuheshimiwa kimsingi tunapaswa kuwajali aina zote za wakimbizi waliokimbia nchi zao kwa sababu zozote zile ziwe za kisiasa, vita uchumi njaa  na ugumu mwingine wote wanapaswa kuheshimiwa kuhifadhiwa kutunzwa vizuri, kupendwa na kuhifadhiwa,kwa heshima na usawa sawa na raia wengine tukiwahesabu kuwa ni ndugu na jamaa zetu Walawi 25, Isaya 16:1-4, Ezekiel 47:21-23 Lawi 19:33-34. Isaya 16: 3-4 inasema “Lete shauri; kata neno; fanya kivuli chako kuwa kama usiku kati ya mchana; wafiche waliofukuzwa; usiwachongee waliopotea. Watu wangu waliofukuzwa waache wakae pamoja nawe; katika habari za Moabu, uwe sitara kwake mbele ya uso wake anayeharibu; maana yeye atozaye kwa nguvu amekoma; afanyaye ukiwa ametoweka; waliokanyaga watu wametoka katika nchi.”  

         
Wakimbizi na mafundisho ya agano jipya

Agano jipya linasisitiza sana kuwahudumia wageni kuwapenda na kuwajali wenye mateso na masikini Mathayo 25:35-40,  kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia. Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? Ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi”. tofauti ya ndugu na wakimbizi iliondolewa kabisa katika agano jipya Yohana 13:34 kutokana na umoja wa waamini Yohana 17:20-23 na kutokana na udugu na wote kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo.

Hivyo ni muhimu kwa kanisa kujihusisha na kuwahudumia wakimbizi punde linapotokea swala la wakimbizi na kukutana na mahitaji yao ya muhimu haraka , kama usalama, upendo, chakula mavazi, malazi, maji safi,madawa, Kumbuka kuwa Yesu atakuja kubagua Kondoo na mbuzi kwa misingi ya namna tunavyowajudumia wengine au wenye uhitaji Mathayo 25:31-46, bila huduma hizi ni vigumu kwa wakimbizi kuikubali injili, wanyarwanda wana usemi usemao “Inda irimo ubusa ntigira amatwi” yaani tumbo tupu halina masikio, Ni muhimu kanisa likakumbuka hilo likakumbuka kuwahubiri injili lakini pia kusikiliza injili kutoka kwao ikiwa wanauwezo wa kuhudumu ili kuwalea na kukuza huduma zao punde warudipo au kuwa wamisionari katika taifa letu, hivi ndivyo nyakati za kanisa la kwanza walivyofanya pia Matendo 8;1-4, 18:1-2, Hali hii itainua heshima yao na kuwatia moyo, kanisa pia linapaswa kufanya kitu cha ziada sio tu kuwaletea maji katika birika bali kuwaelekeza namna wanavyoweza kuchimba visima wenyewe ili kujipatia maji, kanisa linapaswa pia kujihusisha katika swala zima la kuangalia chanzo cha ukimbizi na kukishughulikia hii ina maana kuwa kanisa linapaswa kujishughulisha na swala la kufanya upatanisho na kutafuta majibu ya matatizo ili kuyatatua na watu waweze kurejea katika nchi zao kwa amani badala ya kuiacha kazi hiiikafanywa na serikali zaidi, Kanisa ni lazima lisimamie demokrasia, Haki, upatanisho na mswala ya uongozi kwa ujumla, unaweza kufikiri kuwa kazi hii ni ya kiserikali zaidi nay a kijamii zaidi kuliko ya kiroho, lakini nataka nikuambie kuwa ni ya Kiroho zaidi na inapaswa kanisa kuwa sambamba na mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali yanayojihusisha na huduma kwa wakimbizi

Ni muhimu kuwahudumia vema wakimbizi wao pia ni binadamu, kuna historia za kutisha kuwa sehemu nyingine wakimbizi wanabakwa, wanakataliwa, wanawekewa uzio, au wanafanyiwa hila wafe,n.k. hivi karibuni katika nchi ya Syria kutokana na vita kumekuwa na wakimbizi wengi wanaokimbilia ulaya na wengine wanapitia Libiya lakini wengi wamefanyiwa hila wakikimbia kuokoa maisha yao wengine wameuawa na mataifa mengine yameingia hofu ya kuwapokea Mungu isaidie Dunia kuwa mahali panapofaa kukaa ni wajibu wetu kupiga vita kila kinachosababisha watu kukimbia nchi zao na kujaribu kutatua migogoro iliyoko Duniani ili kila Nchi ipate Ustawi unaokusudiwa na Mungu.
Yeye aliye na sikio na alisikie neno hili ambalo Roho aliambia kanisa.
Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima