Jumatatu, 10 Februari 2020

Chochea Karama ya Mungu iliyo ndani yako!

2Timotheo 1:3-6Namshukuru Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile nikukumbukavyo wewe daima, katika kuomba kwangu usiku na mchana.  Nami natamani sana kukuona, nikiyakumbuka machozi yako, ili nijae furaha; nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo. Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu.”


Utangulizi:


Ni muhimu kufahamu kuwa kila mwanadamu amezaliwa kwa kukiwa na kusudi fulani au wajibu fulani wa kuutimiza ulioko ndani yake, na katika wajibu huo ili aweze kuutimiza ipaswavyo, Mungu huweka karama au kipawa kwaajili ya kumuwezesha mtu huyo kutimiza kusudi la Mungu lililowekwa ndani yake 


Hata hivyo karama au kipawa kinapokuwa ndani ya mtu kuna maswala kadhaa yanayopaswa kufanyika ili kiweze kukua au kukomaa au kujitokeza katika ubora wake swala hilo sio lingine ni kuchochea kipawa hicho kilichomo ndani ya mtu aliyekusudiwa na Mungu kutumiwa katika shughuli husika. Tutajifunza somo hili muhimu kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-



·         Maana ya kuchochea Karama
·         Jinsi karama zinavyochochewa!
·         Namna karama zinavyochochewa!


Maana ya kuchochea Karama 

Paulo mtume anamwandikia Muhubiri na kiongozi kijana na mchanga katika Imani na maongozi ili kumtia moyo wakati yeye akiwa anaelekea ukingoni wakati huu Paulo mtume alikuwa gerezani kwa sababu ya injili, akisubiri kuuawa kwake muda si mrefu kwa hiyo anaandikwa waraka huu akiwa na hisia kali sana akijua ya kuwa anatengwa na wapendwa wake lakini vilevile akijua kuwa Timothy atakabiliwa namaswala mengi ya kuhubiri injili, uongozi, nausimamizi wa kanisa na shughuli nyingunezo katika jamii, na sasa anataka kumtia moyo ili asimame kiume awe imara ahakikisha anafanya kazi kwa bidii na uaminifu na ndipoi anaposema manenoi haya “Kwa sababu hiyo nakukumbusha uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani kwa kuwekewa mikono yangu”Neno hili katika biblia ya kiingereza NKJV (New King James Version) linasomeka hivi “Therefore I remind you to stir up the gift of God which is in you trough the laying of my hands” Biblia  nyingine zimetumia neno “Keep a blaze the gift” na neno “rekindle the gift” Maneno ya kiyunani yanayotumika katika lugha hii ni “xesikono” yaani kuchochea mfano wa kusogeza vijinga vya moto ili moto wa kutumia kuni uweze kuendelea kuwaka, kwa kawaida moto wa kuni kama umewashwa na ukaachwa bila kuchochewa unaanza kuzimika na ili uendelee kuwaka vema unahitaji kuchochewa, Moto unapochochewa huwa na tabia ya kuendelea kuwaka na kubaki katika hali ileile na nguvu ileile au kuwaka zaidi.  Paulo anamtaka Timotheo aendelee kuwaka na kubaki katika hali ile ile na nguvu ileile au kuwaka zaidi, akiwa na imani ileile kama iliyokuwa kwa bibi yake loisi na mama yake Eunike nay eye mwenyewe aliwa kamawao na kuzidi. Kwa hiyo wale wanaotumia tafasiri ya kuchochea kwa maana ya kukoroga mfano wa sukari kwenye chai maana hjii ni ya kipuuzi kwa mujibu wa asili ya maandiko haya hayazungumzii kukoroga yanazungumzia kuongeza moto kuchochea kuhakikisha moto unabaki pale plale au unaendelea.


Hii ina maana gani? Matokeo makubwa katika jambo lolote tunalolifanya yatawezekana kama moto wetu hautazimika, Chakula kitaiva vizuri na Matunda yataonekana kama hakuna mtu anazimia moyo, Mungu amempa kila moja wetu karama na vipawa kwaajili ya shughuli mbali mbali, ili kufanikisha huduma na utumishi aliouweka ndani yetu na ndani ya kila mmoja wetu, Kama wewe ni mwana michezo mfano Bondia na umefanikiwa kuchukua mikanda mbalimbali ya kimataifa haupaswi kuishia hapo, Kama ni shule ya msingi au sekondari na imefanikiwa kiwilaya au kimkoa au kitafifa kushika nafasi nzuri ya juu kwa kufaulisha zaidi katika mitihani ya kitaifa haipaswi kuridhika na kubweteka na kukaa hapohapo tu, Kama ni kanisa limefanikiwa kuwahubiri injili watu maelefu kwa maelfu na kuwaleta kwaq Yesu hawapaswi kuridhika na kuishia hapohapo, kama Mungu amekupa nafasi ya kuwa Kiongozi mkubwa wanchi yaani Rais, au makamu wa Rais au waziri waziri mkuu, au  jaji mkuu au mkuu wa jeshi la pilisi, au Magereza, au uhamiaji, au zimamoto au kujenga taifa au mkuu wa majezi ya ulinzi na usalama,  spika wa bunge au mkuu wa mkoa au mbunge au mkuu wa wilaya na kadhalika na viongozi wengine wote na katika kanisa vilevile Hatupaswi kuishia hapo lazima tuichochee moto wa maendeleo na kuhakikisha kuwa kila tulifanyalo haliwi nguvu ya soda lazima tuchochee moto wa maendeleo na kuhakikisha kuwa tunasonga mbele na kupiga hatua kubwa sana hiki ndicho Mungu anachokitaka,  Mungu anataka moto uwe mkali zaidi, Nimeona pia katika nchji yetu Makocha wengi wa mpira wa miguu wanatoka katika nji nyingine kana kwamba hatuna makocha hodari hapa nyumbani Makocha wa nyumbani wanapaswa kuchochea uwezo wao na kujiapiza kuifunga kila timu yenye kocha mgeni mpaka wakubali kuwa nyumbani tunaweza hiki ndio kitu Mungu anataka, mpaka ulimwengu ugundue kuwa wako watu wanaweza, ikiwa wewe ni muhubiri hubiri injili kwa viwango na ufanisi mkubwa, ikiwa wewe ni mwanamuziki wa injili imba kwa mafundisho yaliyo sahihi huku wewe mwenyewe ukiwa ni kielelezo cha kila unachokihubiri, mwimbaji wa nyimbo za kawaida wekeza hisia zako zote kwa bidii, mchezaji wa mpira, bondia, mwanariadha, mwalimu, mwanafunzi, nakila mtu hata katika ndoa zetu hatuna budi kuhakikisha kuwa tunachochea upendo, uzalendo na mshikamano na kuhakikisha kuwa unawake na kuwa moto mkali sana na tutaona maendeleo makubwa katika taifa letu, Kila mmoja akichochea kipawa na karama aliyopewa na Mungu matunda yetu hayawezi kuzimika na kila sekta katika taifa letu itaonekana ikistawi kwa namna ya kipekee na ya tofauti, Na ndio maana Paulo mtume alikuwa anamtaka Timotheo aichochee karama ya Mungu iliyomo ndani yake, Leo mimi nawataka wananchi wote kwa pamoja tuchochee kila karama na kipawa kilichomo ndani yetu kila ambacho Mungu ametupa na kuwa tusizimie moyo wala tusiogope.

Paulo mtume alikuwa akimuomba Mungu na kutamani kuona Maisha ya Timotheo yanakwenda juu zaidi ya pale alipokuweko na kuwa imani yake inapaa na kuongezeka, Paulo alikuwa anajua kuwa Timotheo ana vipawa vingi na anajua kuwa zikichochewa atafanya na kuwa bora zaidi, Kila mtu na kila mmoja wetu ana kipawa fulani ndani yake na karama ambazo mungu ameweka ndani yetu kwa makusudi mbalimbali lakini hatuwezi kujigundua mpaka mtu mwingine aone, atuchochee na kututia moyo, Kila mwanadamu anahitaji kutiwa moyo, Hakuna mwanadamu anayefurahia kutukanwa kila siku na kukashifiwa na kuambiwa kuwa hana lolote, Ni lazima tuwe na tabia chanya yenye kuwajenga na kuwatia moyo wengine badala ya kuwa watu wenye kuonyesha kuwa wengine hawawezi ilihali kumbe ni sisi ndio hatuwezi, swala la kutia moyo mtu na kumuona mtu akifanya vema halihitaji kusomea saikolojia ni falsafa ya asili tu “Natural Philosophy” Mara kadhaa mtoto anapoanza kusimama katika mila na desturi zetu huwa tunawaimbia kamimama peke yake kwamakusudi la kuwatia moyo wasimame, kweli kweli  na hatimaye husimama, Wanamichezo wa soka na wa aina mbalimbali wanawahitaji sana washabiki wao kufika kwa wingi uwanjani ili kuwatia moyo na kuwashangilia jambo hili huwapa moyo na kuwafanya wafanye bidii na kufanikiwa, Mungu anapokuwa ameweka vipawa ndani yetu na karama za aina mbalimbali zinahitaji watu wenye ujuzi wa kututia moyo na kuhakikisha kuwa kwa namna chanya wanatujenga na kututia moyo ili kipawa na karama zisipotee na kufifia.


Jinsi Karama zinavyochochewa!


Ndani ya Timotheo kulikuwa na Huduma au karama ya Uongozi, yeye aliitwa na Mungu na kufanya kazi na Paulo mtume akisimamia makanisa alikuwa anapaswa kuyaongoza makanisa alikuwa nafanya kazi za kichungaji, alikuwa ni mwangalizi wa makanisa ya Mungu ni askofu kijana, alikuwa Muhubiri wa injili lakini kama binadamu alikuwa muoga kidogo, na alikuwa mwenye haiba ya aibu hivi na Paulo alifahamu jambo hili  na hivyo alitaka kumtia moyo asiogope kwani Mungu hakutupa roho ya woga ona 2Timotheo1:7Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.” Hii maana yake ni kuwa Mungu anaweza kutupa vipawa vikubwa sana ndani yetu lakini kuna madhaifu ya kibinadamu inaweza kuwa woga, inaweza kuwa tunaona aibu au tunakosa nidhamu na kadhalika au tunaweza kuwa waoga na kwa kujua hili ndipo Mungu huwapa watu wake Roho Mtakatifu ili kuwawezesha kuwa wajasiri na kukabiliana na kila aina ya upinzani na kuweza kujihami dhidi ya upinzani wowote tutakaokutana nao Luka 12:11-12 “Na watakapowapeleka ninyi mbele ya masinagogi na maliwali na wenye mamlaka, msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu jinsi mtakavyojibu au kusema; kwa kuwa Roho Mtakatifu atawafundisha saa ile ile yawapasayo kuyasema”. Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.” na Warumi 8;26 “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.” Mungu yupo kututia nguvu na kutuwezesha na kutupa nidhamu na kiasi kuweza kushinda changamoto mbalimbali tunazokabiliana nazo katika maisha, Roho Mtakatifu hutuombea na kutusaidia kwa sababu anajua udhaifu wetu na hivyo hatupaswi kuogopa, kwa hiyo kuchochea kwetu hapa ni pamoja na kumtanguliza Mungu mbele katika kila tunalolifanya na Roho Mtakatifu atakuwepo kutusaidia kwa dhamiri njema!


Namna karama zinavyochochewa


Kwa kuwa Karama na vipawa hutoka kwa Mungu, ni lazima Mungu atangulizwe mbele, katika karama za maongozi ya kanisa na vipawa vya roho mtakatifu kamwe hatuwezi kutumia akili zetu wenyewe wala hatupaswi kutumia ngubvu zetu Roho Mtakatifu hufanya kazi na sisi kama tutakubalia atutumia kwa hiyo lazima kwetu kuwekewa Mikono na watumishi wa Mungu ili watuombee neema ya Mungu katikalile tunalokwenda kulifanya 

1.       2Timotheo 1;6 “Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu.” 

     Viongozi wa kanisa wanapotuombea neema na kuweka mikono yao juu yetu kazi zile zilizowekwa mbele yetu zinapata kibali cha kiungu na karama zilizokuwa zimejificha huibuka, hekima na maarifa hutukalia na ndio maana mtu akiwekewa mikono na kubarikiwa mwenendo wa maisha yake huwa tofauti Matendo ya mitume 13: 1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.” Mtu wa Mungu anapowekewa mikono na kuombewa neema kwaajili ya majukumu aliyopewa roho ya maarifa na hekima ya kutekeleza wajibu wake kwa uzuri hukaa juu yake Kumbukumbu la torati 34:9 “Na Yoshua, mwana wa Nuni, alikuwa amejaa roho ya hekima; maana Musa alikuwa amemwekea mikono yake juu yake; wana wa Israeli wakamsikiliza, wakafanya kama Bwana alivyomwamuru Musa.” Yoshua aliweza kuwa kiongozi shujaa na mwenye imani na akasikilizwa na wana wa Israel kwa kuwa aliwekewa mikono na Musa hivyo kwa kuwekewa mikono na kuombewa neema kamama zilizoko ndani yako zinaweza kuchochewa kwa msaada wa Roho Mtakatifu.


2.       Kubali kufundishwa 


1Timotheo 4:13 “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha.Paulo Mtume pia alimwambia Timotheo afanye bidii sana katika kusoma, Tayari Timotheo alikuwa ni Muhubiri wa Injili na alikuwa ni mwangalizi wa makanisa lakini anatakiwa afanye bidii sana katika kusoma, uko ujuzi mwingi umejificha katika vitabu, lakini kutokana na watu wengi kuwa na uvivu wa kusoma na kuelimika wamezima moto au wameshindwa kuuchochea moto na kuchochea vipawa vyao, kila kitu duniani kinahitaji kujiongeza, wako watu wengi sana hawafurahii ndoa zao kwa sababu wanandoa wameridhika na hali ile ile na ujuzi uleule na hawataki kujaribu kujifunza na kutafuta mambo mengine kutoka vitabuni, wako wafanya biashara ambao biashara zao zimedumaa kwa sababu wana mbinu zilezile na mitindo ileile, wafanyakazi katika taasisi, walimu na kadhalika wanapaswa kujiongeza, serikali mara kadhaa katika sekta ya elimu wamebadili silabasi, mifumo ya mitihani, mbinu za ufundishaji bila kutoa semina  ya kutosha na kueleweka kwa kwa walimu, ili waendane na mfumo mpya na kuwapeleka katika ngazi ya juu, wapo wachungaji wamesoma zamani na mambo yamebadilika wanapaswa kupata semina elekezi katika Nyanja zao ili kujiongeza na kuchochea uelewa walio nao mpaka kuwapeleka ngazi nyingine kila ki[pawa karama na nafasi Mungu anayotupa inahitaji maarifa ya kutosha  na bidii katika kujifunza ili ifanyike kwa usahihi zaidi


Kuna baadhi ya karama na vipawa ambavyo Mungu ameweka ndani yetu ambavyo ili vifanye kazi na kunolewa na kutumika katika viwango vya juu lazima kusoma na kujisomea na kujiongeza kuhusike au mazoezi makali na miiko yake au nidhamu zake zihusike, siku hizi kumeibuka wimbi kubwa sala la watu wanaomtumikia Mungu huku wakiwa hawana mafunzo ya utumishi huo, huu ni msiba mkubwa sana nakubali kuwa utumishi ni huduma na ni karama na ni kipawa lakini kinaweza kufanya kazi vizuri kwa kupitia mafunzo aidha mafunzo rasmi au mafunzo yasiyo rasmi lakini ni muhimu kupitia mafunzo hayo kwa muda wa kutosha ili utumishi wetu uwe na ufanisi na hii ndio njia mojawapo ya kuichochea Karama, Mungu humtumia mtu vuziri zaidi baada ya kumuandaa kwa muda wa kutosha na mrefu zaidi Matendo ya Mitume 7:22Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri, akawa hodari wa maneno na matendo” Mungu alimtumia sana nabii Musa lakini Musa alikuwa msomi alifundishwa hekima yote ya wamisri na akawa Hodari wa maneno na matendo, ni kwa kusoma tunaweza kuchochea Karama zilizoko ndeani yetu na tukawa watu Hodari, lazima ufikie wakati tukubali kujifunza tuwasikilize walimu na kuwatii, tuwasikilize wazazi na kuwatii, tuwasikilize makocha na kuwatii, tujifunze kwa waliostaafu, tujifunze kwa waliotutangulia, tujifunze hata kwa walioshindwa kwa kuwauliza walishindwaje ili sisi tusipite katika njia ileile.  

Matendo 18:24-26 “Basi Myahudi mmoja, jina lake Apolo, mzalia wa Iskanderia, mtu wa elimu, akafika Efeso; naye alikuwa hodari katika maandiko. Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; na kwa kuwa roho yake ilikuwa ikimwaka, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi habari za Yesu; naye alijua ubatizo wa Yohana tu. Akaanza kunena kwa ujasiri katika sinagogi; hata Prisila na Akila walipomsikia wakamchukua kwao, wakamweleza njia ya Bwana kwa usahihi zaidi.                 

Maandiko yanaonyesha jinsi Apollo alivyokuwa mtu mwenye Elimu na alikuwa hodari katika maandiko na alikuwa Muhubiri hata hivyo alihitaji kujua maswala kadhaa kwa usahihi zaidi na mwalimu wa neno la Mungu Prisilla na Akila ambao walikuwa ni watumishi wa Mungu Pamoja na Paulo mtume wao walimfundisha njia ya bwana kwa usahihi zaidi ili kuichochea huduma yake, Tunapokubali kujifunza tunajiweka katika kutumiwa na Mungu katika viwango bora zaidi na kusaidia kupunguza makosa ya kibinadamu, hivyo unapobaini kuwa una kipawa fulani tafuta watu sahihi watakaosaidia kukinoa ili kukiweka kitaalamu zaidi, ili utumiwe vema na kwa ubora zaidi.

3.       Hakikisha unaonana na watu sahihi.

Mungu anapokuwa ameweka Karama au kipawa au aina fulani ya maono, mwanzoni ni rahisi sana watu kukataa kutambua kipawa au karama uliyo nayo na unaweza kujikuta uko katika mazingira ya watu ambao wanaweza kuua kile ulicho nacho kwa nia njema au mbaya lakini pia kwa kutokujua kuwa umebeba nini, Nilipotembelea taifa la Korea ya kusini mwaka 2016 niliwahi kukutana na wat kadhaa wanaotumia mkono wa kushoto kwa ubora sana kama mimi na watanzania wenzangu tunaotumia mkono wa kulia, Mkorea mmoja akaniambia kuwa watu wanaotumia mkono wa kushoto ni wenye akili sana na hapa Korea wako wengi mno, kwa haraka nilisikia uchungu moyoni kabla ya kujibu lolote niliwaza kuwa ina maana sisi tunaotumia mkono wa kulia hatuna akili? Lakini haraka sana jibu llikuja na nikamwamboa mkorea yule kuwa kama ni hiyo Afrika watu wengi wana akili sana kwa sababu kila mtoto anayezaliwa na niliowaona mimi wanatumia mkono wa kushoto lakini wazazi wetu hutuchapa na kutukemea kisha hutufundisha kutumia mkono wa kulia kwa sababu kwetu Afrika kutumia mkono wa kushoto kwa mila na desturi zetu sio jambo la busara na halna heshima, na mkorea yule aliacha majivuno yake,  kwa nini nimetumia mfano huu hapa unaweza kuwa na kipawa cha aina fulani na unaweza kuwa umezaliwa nacho unaweza kuwa unapenda kuchora na wazazi wanaweza kudhani unajisomea kumbe unachora na wakakukataza kuchora ili kwamba usome lakini kumbe wanaua kitu cha thamani ulichojaliwa na Mungu, Unaweza kuwa unapenda sana kucheza mpira lakini wazazi wakakukataza ili kwamba usije ukaumia au uweze kuweka mkazo katika kusoma lakini kumbe wakawa wanafifisha kipawa kilichoko ndani yako!  Mtu mwenye karama au kipawa ili aweze kukichochea hana budi kuhakikisha kuwa anaelekea mahali sahihi ili kupata mafunzo na kutiwa moyo zaidi kuhusu kipawa chake ona katika  

Luka 1:39-40 “Basi, Mariamu akaondoka siku hizo, akaenda hata nchi ya milimani kwa haraka mpaka mji mmoja wa Yuda, akaingia nyumbani kwa Zakaria akamwamkia Elisabeti.”

 Unaweza kujiuliza kuwa ni kwa nini Mariamu alipotaarifiwa  na Malaika Gabriel kuwa atakuwa na Mimba na atamzaa Masihi ambaye ni mrithi wa kiti cha enzi cha Daudi milele? Na tunaona Mariamu anafanya haraka kwenda kumtembelea Elizabeth na kukaa kwake miezxi mitatu wakati malaika anamwambia jambo hili Mariamu pia alimueleza jambo jingine kwa kusudi la kumtia moyo Mariamu maana alijiuliza inawezekanaje jambo hili kutokea naye hajui mume? Malaika alitaka kumuonyesha Mariamu kuwa Mungu hashindwi jambo na hata Elizabeth aliyeitwa tasa sasa ana ujauzito wa miezi sita ona:-

Luka 1:34-37 “Mariamu akamwambia malaika, Litakuwaje neno hili, maana sijui mume? Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu atakujilia juu yako, na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu. Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.” 


Unaona Jambo hili lilimfanya Mariamu kwenda haraka sana kwa Elizabeth kwa sababu alikuwa amechanganyikiwa kwa maono makubwa ambayo malaika alisema naye ni kama malaika alikuwa amemuonyesha wazi kuwa mtu sahihi anayeweza kukusaidia kwa wakati huu ni Elizabeth ambaye naye Mungu amemfanyia mambo makubwa na magumu yaliyoshindikana kibinadamu Mariamu hangeweza kumwambia mama yake. Wala mwalimu wake au mtu yeyote aliyemjua alijua kuwa mtu aqnayeweza kumuelewa ni Elizabeth tu mtu mwenye maono na ndoto na muujiza na kipawa na karama kama zake 


Luka 1:36-37” Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.Mariamu alikuwa ametiwa moyo kupitia maneno haya alihitaji kujifunza kwa mtu sahihi aliyemtangulia alihitaji muongozo, alihitaji kupokea uzoefu, Elizabeth ndiye aliyekuwa mtu sahihi wakati huu wa kumtia moyo Mariamu, kumfundisha, kumuelekeza, kumuonyesha upendo na urafiki, kumpandisha imani na kumtetea ona maneno ya Elizabeth 

Luka 1:41-45 “Ikawa Elisabeti aliposikia kule kuamkia kwake Mariamu, kitoto kichanga kikaruka ndani ya tumbo lake; Elisabeti akajazwa Roho Mtakatifu; akapaza sauti kwa nguvu akasema, Umebarikiwa wewe katika wanawake, naye mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Limenitokeaje neno hili, hata mama wa Bwana wangu anijilie mimi?  Maana sauti ya kuamkia kwako ilipoingia masikioni mwangu, kitoto kichanga kikaruka kwa shangwe ndani ya tumbo langu. Naye heri aliyesadiki; kwa maana yatatimizwa aliyoambiwa na Bwana.”   


Unadhani Mariamu angeenda kwa mtu asiye sahihi ingekuwaje angeambiwa Mungu wangu ni nani atakayekuelewa umekwisha unaanzaje kumwambia mtu una mimba unawezaje kutimiza ndoto hii unawezaje kuifanya biashara hii, unawezaje kuandkia andiko maoni haya ndugu yangu hii ni kazi ngumu sana haiwezekani, vifaa vimepanda sana haiwezekani, ujenzi ni gharama mno hutaweza unapokuwa na karama au ndoto au maono enenda  kwa mtu sahihi Elizabeth anamwambia Mariamu tena akiwa amejaa Roho Mtakatifu Naye heri aliyesadiki; kwa maana yatatimizwa aliyoambiwa na Bwana.”   Elizabeth anamwambia mariamu ulichoambiwa na Mungu kitatimia tu na ni baraka kubwa kama utaamini, mwamini Mungu yeye anaweza ndipo Mariamu akamuadhimisha Mungu na kutulia kwa Elizabeth kwa miezi mitatu, Unapokuwa na njozi au hata mapito na majaribu enenda kwa watu wanaopitia majaribu kama yako mtazungumza lugha moja, unapokuwa na karama waone waliokutangulia  walio sahihi wenye kipawa kama chako jifunze kutoka kwao ambao lugha zao zitakuwa chanya watakuambia UTATOBOA TU, Mwanangu utatoka hii kitu nakuhakikishia utatoka kirahisi tu, hivyo ndivyo unavyoweza kuichochea karama iliyo ndani yako.


4.       Kuwa mkomavu.

Acha ulimbukeni, watu wengi sana wameua vipawa vyao kwa sababu ya ulimbukeni, vipawa vinapowapa mafanikio wanakuwa na mbwembwe nyingi, kiburi kinapanda na kujidai, wakijifikiri kuwa wao ni watu maarufu sana wanapoteza adabu na kujali utu, wanaongeza mbwembwe nyingi sana, wanakosa umakini,  na wanaacha kujilinda Kipawa ni zawadi ni uwakili ni amana ambayo Mungu amewekeza ndani yako lazima uilinde 2Timotheo 1:14 “Ilinde ile amana nzuri kwa Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu.”  Unawezaje kujilinda kuhakikisha kuwa uko vilevile au unazidi mno lazima ujilinde na kiburi, watu wenye mafanikio sana duniani wala hawajidai,  Hawana maringo, hawajifanyi wanajua, wanapokea ushauri, wanajali wengine. Ni vema tukajivika unyenyekevu kwa sababu njia ya Mungu ya kutupeleka juu ni kujishusha 1Petro 5:6 

Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake;”  Kumbe kanuni ya Mungu ya kukukweza ni kujishusha na kuishi maisha ya unyenyekevu. Unyenyekevu ndio unaoonyesha ukomavu lakini tukiwa na kiburi ni muhimu kufahamu kuwa hatuko mbali na aibu Mitahli 11:2 “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; Bali hekima hukaa na wanyenyekevu. Watu wengi wenye vipawa na karama   wameharibu sifa zao kwa sababu ya kiburi na hivyo wamefupisha muda wao wa kumtumikia Mungu au kutimiza kusudi walilokusudiwa na Mungu duniani ni kutokana na kujinyenyekeza sana Yesu aliinuliwa sana hii ndio kanuni ya mafanikio ya kutunza kipawa chako mbele za Mungu na wanadamu nia nyenyekevu itakuweka juu kama ilivyomuweka yesu juu mno Wafilipi 2:5-11” Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.” 


5.       Usikubali kupoa
 

Tunaweza kuchochea karama vilevile kwa kuhakikisha kuwa hatuuzimi moto wa Mungu ulioko ndani yetu, usikubali kupoa au kuwa vuguvugu, Maandiko yanaonyesha kuwa Mungu akikupa amekupa na haondoi kipawa wala karama alizoweka ndani yetu lakini ni kwa nini watu hufulia na kuisha kabisa sababu kubwa ni kupoa au kuwa vuguvugu Mungu anachukizwa sana na watu vuguvugu maandiko yanaonyesha uwezo wa kupoa uko katika mikono yetu na uwezo wa kuwa Moto pia, Mungu ameweka karama ndani yako wewe ni wajibu wako kuhakikisha unabaki moto Ufunuo 3:15-16 “Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto. Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.” Unaona Mungu hapendezwi na watu vuguvugu hii maana yake anatujua vema anataka tuwe moto, au ukishindwa uwe baridi ijulikana umekwisha umepoa lakini kamwe Mungu hataki tuwe vuguvugu atakutapika ndio maana utaweza kuona watu wanaibuka kisha wanatokweka na karama na vipawa vinakwisha. 


6.       Usimzimishe Roho Mtakatifu.

Biblia inaeleza katika 1Wathesalonike 5:19 “Msimzimishe Roho;” Roho Mtakatifu ni Mungu na ndiye chanzo cha Karama na vipawa vyote anavyowapa wanadamu, Kumzimisha Roho Mtakatifu maana yake nini  Roho Mtakatifu kama Mungu Hakuna mtu anaweza kumzimisha  haiwezekani lakini sisi wenyewe tena tunaweza kuanza kumuhuzunisha Roho wa Mungu kutokana na mtindo wa maisha unaomuhuzunisha Roho Mtakatifu kama Mungu na kumfanya aondoe neema yake Waefeso 4:30 “Wala msimhuzunishe yule Roho Mtakatifu wa Mungu; ambaye kwa yeye mlitiwa muhuri hata siku ya ukombozi.”  Tunapofanya dhambi na uasi endelevu dhidi ya Mungu Roho wa Mungu anaweza kutuacha na ushujaa wetu utakuwa umefikia kikomo na ndio maana Daudi aliomba asiondolewe Roho Mtakatifu Zaburi 51:11 “Usinitenge na uso wako, Wala roho yako mtakatifu usiniondolee.” Kwa Msingi huo tukiishi mtindo wa maisha unaomnyima Mungu Roho Mtakatifu kutuongoza na kutusaidia huku yeye akiwa chanzo cha vipawa vyetu tutapoteza uwepo wake Napenda sana tafasiri ya Kiibrania ya neno Msimzimishe Roho wenyewe wanatumia neno “KABAH” sawa na kusema Msimkabe Roho Mtakatifu, Msimbanie, kiingereza Do note Expelled, au do not neglected  au Quench not,  Kwa maana hiyo sisi wenyewe ndio tunawajibu wa kujiachia katika neema ya Mungu, kwa kufunga, kuomba, kusoma neno, kuabudu, kujiweka karibu na Mungu kuutafuta uso wake kwa bidii, kutubu kwa haraka endapo tumekosea na tutaona Roho wa Mungu alkiendelea kukifungua kipawa kilichopo ndani yetu kidogo kidogo. Na kututumia kwa viwango vikunbwa na vya hali ya juu.

7.       Uwe hodari

Watu wenye vipawa wanapigwa vita sana wanapambana watu wenye wivu, Ibilisi pia hapendi kwa sababu karama ni silaha za maangamizi zinampa Mungu utukufu na kuharakisha kazi ya Mungu na kwa sababu hizo upinzani ni lazima, Karama na vipawa pia Mungu huzitumia kuinua maisha binaksi ya Muhusika kwaajili ya hayo ni lazima uwe hodari na uwe shujaa Yoshua 1:9 “Je! Si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako.” Mungu anataka tuwe hodari na tuwe na moyo wa ushujaa kwa sababu anajua kuna changamoto mbele yetu, Kila mtu anayetaka kuzichochea karama akumbuke kuwa mbali na hofu na awe na ujasiri, kwa sababu kila utakapoitumia Karama uliyonayo kutainuka wasiopendezwa na watajaribu kwa kila jinsi na kila namna kupingana nawe kama nduguze Yusufu walivyochukizwa naye hata kutaka kumuua kwaajili ya ndoto  alizokuwa nazo  

Mwanzo 37:5-11 “Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia;  akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi?  Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.Unaweza kuona Mungu anampa ndoto Yusufu kuwa mtawala, ana maono mazito kwaajili ya kuja kuisaidia familia yake ana karama ya maongozi, ana karana ya unabii na kipawa cha kutafasiri ndoto kipawa hiki kingembeba na kumpeleka kwenye kiwango kingine kingeisaidia jamii na ndugu nzake pia lakini wao ndio walikuwa wa kwanza kuona wivu na hata kutaka kumuua kabisa ona 

Mwanzo 37:18-20 “Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake.” 


 Unaweza kuona ndugu zake Yusufu walikusudia kumuua kwa sababun ya ndoto zake yaani ileile karama aliyopewa iliwavutia maadui, ningeweza kukupa mifano Mingi kama Daudi alivyotaka kuuawa na Sauli kwa sababu ya karama, ningeweza kukupa mfano wa Samsoni alivyowindwa na Wafilisti kutokana na ngvu zake na uwezo wake wa ajabu aliokuwa nao, ningekueleza jinsi Yesu alivyokuwa tishio kwa viongozi wa dini sio kwa sababu alikuwa mwovu bali kwa wema uliovutia watu kwa maelfu yao na miujiza mikubwa aliyoifanya, ningekuopa habari za Petro na Yohana walivyokutana na uopinzani kwa sababu ya muujiza mashuhuri walioufanya, sikwambii habari za Paulo aliyetumiwa kufanya miujiza na kuwavuta wengi kwa Yesu alivyotaka kuuawa,  sikwambii habari za Daniel ambaye alifanyiwa njama za kila namna kutokana na vipawa alivyokuwa navyo, sikwambii Michael Jakcson alivyochukiwa na wazungu na kufanyiwa kila aina ya hila kutokana na vipawa,  haya na mengineyo ni mifano ni mifano tu inayokutaka uwe makinina uhakikishe unakuwa na ushujaa na moyo mkuu ili kutokuizima ile karama iliyoko ndani yako! Kipawa na karana zina tabia ya kuvutia watu wema na wabaya  


Luka 11: 53-54 “Alipotoka humo, waandishi na Mafarisayo walianza kumsonga vibaya, na kumchokoza kwa maswali mengi, wakimvizia, ili wapate neno litokalo kinywani mwake.” Unaweza kuona namna na jinsi waandishi yaani walimu nwa sheria na Mafarisayo walivyokuwa wakimzongazonga Yesu na kumchokoza ili waweze kumsonga kwa maswali mengi kusudi lao kuu ni kupata neno la Kumshitaki, ili kumuharibia Mungu akupe hekima na Busara  kama alivyompa Yesu ili kujilinda na kujihami na maadui.

Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu

Na Rev. Innocent Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

0718990796

Jumapili, 2 Februari 2020

Mtu wa kumtendea Mema!



2Samuel 9:1-8 “Kisha Daudi akasema, Je! Amesalia mtu mmoja katika nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema kwa ajili ya Yonathani? Palikuwa na mtumishi mmoja wa nyumba ya Sauli, jina lake Siba, basi wakamwita aende kwa Daudi; na mfalme akamwuliza, Wewe ndiwe Siba? Naye akasema Mimi, mtumwa wako ndiye. Mfalme akasema, Je! Hakuna hata sasa mtu ye yote wa nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema ya Mungu? Siba akamwambia mfalme, Yonathani anaye mwana hata sasa, aliye na kilema cha mguu. Mfalme akamwambia, Yuko wapi? Siba akamwambia mfalme, Tazama, yumo katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari. Basi mfalme Daudi akatuma watu, akamwondoa katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari. Basi Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli akaenda kwa Daudi, akaanguka kifudifudi, akasujudu. Daudi akasema, Mefiboshethi! Naye akaitika, Mimi hapa, mtumwa wako! Daudi akamwambia, Usiogope, maana bila shaka nitakutendea mema; kwa ajili ya Yonathani, baba yako, nami nitakurudishia mashamba yote ya Sauli, baba yako; nawe utakula chakula mezani pangu daima. Akasujudu, akasema, Mimi mtumwa wako ni nini, hata ukamwangalia mbwa mfu kama mimi?


Utangulizi:

Moja ya watu muhimu sana katika Biblia ambao tunaweza kujifunza mambo mengi sana kutoka kwao ni Pamoja na Mfalme Daudi mwana wa Yese, Huyu ni mtu mwenye moyo wa ajabu na roho nzuri sana alimpenda Mungu na aliwapenda wanadamu wengine, Maandiko yanaonyesha wazi kuwa Mungu alipendezwa naye angalia katika Matendo 13:22 “Na alipokwisha kumwondoa huyo, akamwinua Daudi awe mfalme wao ambaye alimshuhudia, akisema, Nimemwona Daudi, mwana wa Yese, mtu anayeupendeza moyo wangu, atakayefanya mapenzi yangu yote.Mungu alipendezwa naye kwa sababu aliyatenda mapenzi ya Mungu yote.

Licha ya kuwa na madhaifu kama Mwanadamu Daudi alikuwa mtu mwema sana uwezo wake wa kutenda mema uliweza kuwashangaza wengi. Alikuwa ni mtu asiyelipiza kisasi hata kwa wale waliomfanyia mabaya, lakini vilevile alikuwa ni mtu aliyekumbuka na kushika ahadi/agano kama alivyopatana na Yonathan mwana wa Sauli, leo tutachukua Muda kutafakari kwa kina na mapana na marefu moja ya matukio ya kushangaza sana yaliyofanywa na mfalme huyu wa ajabu.

Mtu wa Kumtendea mema.!

Katika fungu la maandiko ya msingi utaweza kuona moyo wa Daudi, akiulizia swala la muhimu sana lenye kuonyesha kuwa alikuwa na moyo wa ajabu sana, Yeye baada ya kuziona fadhili za Mungu katika maisha yake naye alitaka kuonyesha fadhili zake kwa mtu anayeweza kumuhurumia 2Samuel 9:1 Kisha Daudi akasema, Je! Amesalia mtu mmoja katika nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema kwa ajili ya Yonathani?


a.       Je amesalia mtu mmoja katika nyumba ya Sauli? Daudi aliwahi kuuliza swali kama hili katika 1Samuel 7 wakati anawaza kufanya Jambo kwaajili ya Mungu, na anawaza kumjengea Mungu Hekalu, Sasa Daudi anauliza swali lingine Muhimu mtu wa kumtendea mema?

Swali la Daudi linaonyesha upendo mkubwa sana na wa ajabu mno, Ni wazi kuwa Sauli alitengeneza uadui mkubwa sana, na vita ya siku nyingi na Daudi,  2Samuel 3:1Basi kulikuwa na vita siku nyingi kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi; Daudi akaendelea akasitawi lakini Nyumba ya Sauli ikaendelea kudhoofika”Na ni wazi kuwa kwa mujibu wa tamaduni ya sheria za kifalme utawala mpya wa kifalme unapotawala unatakiwa kuwauwa na kuwateketeza kabisa ukoo wa mtawala aliyepita au awaye yote mwenye uhusiano na utawala uliopita ili utawala mpya uweze kuwa salama, Lakini katika habari hii tunamuona Daudi akifanya jambo la tofauti kabisa kinyume na kanuni za kawaida za kujilipizia kisasi dhidi ya uadui wa Sauli, lakini vile vile kanuni ya kujihami na kujihakikishia anatawala vema na kwa amani ilikuwa ni lazima kuimaliza kabisa Familia ya adui yake, lakini katika namna ya kushangaza mno Daudi yeye anatafuta mtu wa familia ya adui zake na kutafuta mtu wa kuwatendea mema!.

b.      Nipate kumtendea mema kwaajili ya Jonathan: Aidha Daudi pia alifanya hivi kwasababu alikumbuka agano alilolifanya na Jonathan pamoja na uhusiano mwema aliokuwa nao 1Samuel 20:14-15 “Nawe utanionyesha fadhili za Bwana, ili nisife, si wakati huu tu maadamu mimi ni hai; lakini pamoja na hayo, hata jamaa yangu pia hutawaondolea kabisa fadhili zako; la, hata wakati ule Bwana atakapokuwa amewaondoa kabisa adui za Daudi wote pia katika uso wa nchi.” Kwa hiyo wema wa Daudi haukuwa katika hisia zake pekee lakini pia ulikuwa kwaajili ya kukumbuka agano lake alilolifanya na Jonathan, Daudi alitaka kuwa mwaminifu kulitimiza agano lile kwa rafiki yake aliyempenda na kumuokoa na kifo kutoka kwa baba yake yaani Jonathan.


Kutenda wema katika mazingira magumu:

2Samuel 9: 2-4 “Palikuwa na mtumishi mmoja wa nyumba ya Sauli, jina lake Siba, basi wakamwita aende kwa Daudi; na mfalme akamwuliza, Wewe ndiwe Siba? Naye akasema Mimi, mtumwa wako ndiye. Mfalme akasema, Je! Hakuna hata sasa mtu ye yote wa nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema ya Mungu? Siba akamwambia mfalme, Yonathani anaye mwana hata sasa, aliye na kilema cha mguu. Mfalme akamwambia, Yuko wapi? Siba akamwambia mfalme, Tazama, yumo katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari.

a.       Siba aliyekuwa mtumwa wa Sauli alikuwa ndiye mtu pekee aliyekuwa anajua habari za uzao wa Sauli uliosalia na ndiye aliyekuwa anajua wapi walipo, Hii inamaanisha kuwa kijana pekee wa Uzao wa sauli aliyekuwa amebakia alikuwa amejificha kijana huyu alijulikana kama Mefibosheth


b.      Daudi alikua anamuhitaji mtu huyu ili kutunza agano alilofanya na Yonathan, ulikuwa sasa ni wakati wa kuonyesha wema wa Mungu, kwa Jonathan kutokana na agano lile kuwa Mungu atakapokuwa amemfadhili Daudi asiache kumkumbuka Yonathan na kumwacha hai juu ya uso wa nchi kwamba ni yeye au uzao wake huu ndio ulikuwa msingi mkubwa wa Daudi katika maamuzi yake alitaka mtu wa ukoo wa Sauli amuonyeshe wema wa Mungu kama jinsi Mungu alivyomfadhili yeye.


c.       Daudli alitaarifiwa na Siba kuwa yuko mwana wa Yonathan ambaye pia ni mlemavu wa miguu, Mwana huyu wa Yonathan alipata ulemavu wakati wa utoto, siku ya kifo cha baba yake na babu yake walipouawa vitani alipokuwa akikimbizwa mafichoni alipokuwa mdogo aliangushwa kwa bahati mbaya na kuwa mlemavu 2Samuel 4:4 “Naye Yonathani, mwana wa Sauli alikuwa na mwana aliyekuwa na kilema cha miguu. Alikuwa amepata miaka mitano, habari za Sauli na Yonathani zilipofika Yezreeli, na yaya wake akamchukua akakimbia ikawa, alipokimbia kwa haraka, huyo mtoto akaanguka, akawa kilema. Na jina lake aliitwa Mefiboshethi. Ni wazi kuwa Yaya wake alimchukua kijana ili kuokoa maisha yake kwa kukimbia baada ya kusikia kuwa Sauli na Yonathan wameuawa vitani, aliogopa na alikuwa anafahamu kuwa utawala mpya kwa vyovyote vile  wangewaua warithi wote wa ufalme wa Sauli kama zilivyo mila na Desturi.


d.      Mwana wa Yonathan kwa vyovyote vile Methibosheth ndiye aliyekuwa anatakiwa kuwa Mrithi wa kiti cha ufalme, Kijana wa Kwanza wa Sauli alikuwa ni Yonathan na  sasa Sauli na Yonathan walikuwa wameuawa vitani hivyo Methibosheth kama mzaliwa wa kwanza wa Yonathan ufalme ulikuwa una muhusu, Na Daudi alipaswa kuhakikisha kuwa anamuua kwanza Mefibosheth ili utawala wake uweze kuwa imara kwa mujibu wa mila na desturi za kifalme kwa sababu tishio kubwa la ufalme wa Daudi angekuwa ni Methibosheth

Katika kitabu cha 2Samuel 16:5-8 “Basi mfalme Daudi alipofika Bahurimu, tazama, kulitoka huko mtu wa jamaa ya nyumba ya Sauli, jina lake akiitwa Shimei, mwana wa Gera; alitoka, akalaani alipokuwa akienda. Tena akamtupia Daudi mawe, na watumishi wote wa mfalme Daudi; na watu wote na mashujaa wote walikuwako mkono wake wa kuume na mkono wake wa kushoto. Na Shimei alipolaani, alisema hivi, Nenda zako! Nenda zako! Ewe mtu wa damu! Ewe mtu usiyefaa! Bwana amerudisha juu yako damu yote ya nyumba ya Sauli ambaye umetawala badala yake; naye Bwana ametia ufalme katika mkono wa Absalomu mwanao; kisha, angalia, wewe umetwaliwa katika uovu wako mwenyewe, kwa sababu umekuwa mtu wa damu.Maandiko yanaonyesha kuwa jamaa wa Sauli bado walikuwa wanapingana na Daudi na kuna uwezekano mkubwa watu wa aina hii walikuwa wengi katika Israel ambao hawakukubaliana na jambo hili la Daudi kutawala kwa sababu waliona kama ilikuwa ni halali na haki wana wa Sauli kutawala badala yake, mmojawapo ni huyu aliyeitwa Shimei. Aidha Ishbosheth ambaye alikuwa ni Mjomba wa Mefibosheth alianzaisha vita kali sana na Daudi kwaajili ya Ufalme katika Israel, kwa hiyo ilikuwa wazi kuwa Mefibosheth angeweza kufanya hivyo kwaajili ya ufalme.

Hali ya Methibosheth

Daudia liambiwa kuwa yuko katika Nyumba ya Makiri mwana wa Amiel, Hii inaonyesha wazi kuwa Mathibosheth alikuwa katika hali duni na mbaya na ya chini sana kimaisha, hakuwa hata na nyumba yake mwenyewe, alihifadhiwa katika nyumba ya mtu mwingine, Makiri mwana wa Amiel hata hivyo baadaye inaonekana alikuwa anampenda mfalme Daudi, na alikuwa muwazi na mkweli, Hata mwana wa Daudi Absalomu alipomuasi baba yake Makiri alikuwa upande wa kumsaidia Daudi hata hatari kubwa zilipomkabili ona 2Samuel 17:27-29 “Ikawa, Daudi alipofika Mahanaimu, Shobi, mwana wa Nahashi wa Raba, wa wana wa Amoni, na Makiri, mwana wa Amieli wa Lo-debari, na Barzilai, Mgileadi wa Rogelimu, wakaleta magodoro, na mabakuli, na vyungu, na ngano, na shayiri, na unga, na bisi, na kunde, na dengu, na asali, na siagi, na kondoo, na samli ya ng'ombe, wapate kula Daudi na watu waliokuwa pamoja naye; kwani walisema, Watu hao waona njaa, tena wamechoka, nao wana kiu huku nyikani.”

Maandiko yanaonyesha kuwa kijana huyu alikuwa mnyenyekevu mno aliweza kuonyesha unyenyekevu mkubwa sana kwa Mfalme Daudi ona mstari 5-6 “Basi mfalme Daudi akatuma watu, akamwondoa katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari. Basi Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli akaenda kwa Daudi, akaanguka kifudifudi, akasujudu. Daudi akasema, Mefiboshethi! Naye akaitika, Mimi hapa, mtumwa wako!

a.       Mfalme Daudi alituma watu wakapate kumleta Mephibosheth nyumbani kwake kwa hakika tukio hili lilikuwa ni lenye kuogopesha sana kwake wakati watumishi wa Daudi wanagonga Hodi nyumbani kwa Makiri na kudai kuwa anaitwa kwa mfalme katika akili zake ilikuwa inaeleweka kabisa kuwa anakwenda kukutana na kifo kwa sababu ndivyo ilivyokuwa desturi ya kifalme kwaajili ya kujihami katika mamlaka zao,  Kitendo cha watumishi wa Daudi kwenda kwa Makiri na kumuhitaji Mephibosheth ilikuwa ni ishara wazi kuwa hawezi kujificha tena, na labda kama angejisikikia salama ni labda kwa kufikiri tu kuwa labda mfalme mpya hajui habari zake.

b.      Alijiinamisha na kumsujudia Mfalme: kwa mujibu wa tamaduni ni wazi kuwa mpaka wakati huu lazima kijana huyu alikuwa amejaa hofu ya hali ya juu na kwa hakika alikuwa na hofu kubwa isiyo na kifani yeye alikuwa amejificha tangu utoto wake na hajawahi kuwa na uhusiano wowote na Mfalme Daudi hivyo hakuwa na uhakika wa uzima wake ila alikiona kifo tu cha kihiyari bila ubishi.


c.       Mstari 7-8 Daudi alihakikisha anamuondolea Hofu Mephibosheth “Daudi akamwambia, Usiogope, maana bila shaka nitakutendea mema; kwa ajili ya Yonathani, baba yako, nami nitakurudishia mashamba yote ya Sauli, baba yako; nawe utakula chakula mezani pangu daima. Akasujudu, akasema, Mimi mtumwa wako ni nini, hata ukamwangalia mbwa mfu kama mimi? 
          

i.                     Usiogope: Daudi alimwambia Mephibosheth japo neno hili lingekuwa halina maana kama Daudi asingelisema kwa nini anafanya haya au anamwambia usiogope alimuhakikishia kumrejeshea mali za babu yake na kukaa pamoja naye katika kiti cha enzi cha utawala wake.

ii.                   Bila shaka nitakutendea mema kwaajili ya Yonathan baba yako, Daudi alimuhakikishia Mephibosheth kuwa alikuwa na agano na Yonathan baba yake 1Samuel 20 kwamba atamuonyesha fadhili za Mungu hata kwa uzao wake na hivyo Daudi pia alikuwa akitimiza agano hata kama Yonathan alikuwa amekufa.

iii.                  Nitakurudishia Mashamba yote ya Sauli: Daudi pia alimwambia Mephibosheth kwamba atapokea kila kilichokuwa mali yake, Inawezekana Mephoibosheth aliyajua haya  kuwa ni mali yake lakini alikuwa amejificha, alikuwa anaogopa, alikuwa anaishi maisha ya umasikini mkubwa uliokithiri, alijua ya kuwa amekwisha kupoteza kila kitu na kuwa hawezi kufanya lolote kwa uwazi, hangeweza kufanya kitu kuhusu Mashamba yake  kwa sababu kujitokeza kwake kungekuwa ni kuhatarisha maisha yake na kujiweka wazi kwa Daudi, Lakini Daudi kama mfalme mwema anakwenda kinyume na fikra za kitamaduni za wafalme wengine yeye anamtambua na kumfanyia wema mtu ambaye angekuwa hatari katika ufalme wake.

iv.                 Pia utakula mezani Pangu daima: hii nayo ilikuwa ni zaidia ya kawaida Mephibosheth anapewa heshima ya kuwa karibu sana na Mfalme anakaa mezani kwa mfalme hii ni heshima kubwa sana nikama anatawala pamoja naye ahadi kama hii Yesu aliwaahidi wale wamuaminio, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kuwa watakula na kunywa Mezani pake huko mbinguni Luka 22:30mpate kula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu; na kuketi katika viti vya enzi, huku mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli.”

Muitikio wa Mephibosheth

Mtumwa wako ni nani hata ukamwangalia mbwa mfu kama mimi?:

Ni ukweli ulio wazi kuwa kijana huyu mjukuu wa Sauli hakujifikiri hata kidogo kuwa anastahili kitu, ni wazi kuwa hakustahili ukarimu mkubwa namna ile, Yeye alijifananisha na mbwa mfu tu!, yaani mbwa mfu ni kiumbe asiye na umuhimu wala thamani yoyote, kama vile mwanadamu anapoona njiani mbwa aliyekufa, huwa hakuna anayeonyesha kujali zaidi ya kupita kando na kutema mate, Yeye alikuwa amejificha siku zote za maisha yake, akiogopa na huku akiwa amezungukwa na umasikini mkubwa sana akijua wazi kuwa anastahili kuuawa iweje leo afikiriwe kwa kiwango kikubwa namna ile?

Maelekezo ya Mfalme Daudi kwa Siba 9-12

Ndipo mfalme akamwita Siba, mtumwa wa Sauli, akamwambia, Mali yote yaliyokuwa ya Sauli na ya nyumba yake nimempa mwana wa bwana wako. Nawe utamlimia nchi hiyo, wewe, na wanao, na watumwa wako; nawe utamletea mwana wa bwana wako matunda yake, apate chakula ale; lakini Mefiboshethi, mwana wa bwana wako, atakula chakula mezani pangu sikuzote. Basi huyo Siba alikuwa na wana kumi na watano na watumwa ishirini. Ndipo Siba akamwambia mfalme, Mimi, mtumwa wako, nitatenda hayo yote kama bwana wangu, mfalme, alivyoniamuru. Na kwa habari za Mefiboshethi, mfalme alisema, Atakula mezani pangu, kama mmojawapo wa wana wa mfalme. Huyo Mefiboshethi alikuwa na mwana mdogo, jina lake akiitwa Mika. Na watu wote waliokaa nyumbani mwa Siba walikuwa watumwa wa Mefiboshethi.

a.       Wewe na wanao na watumwa wako mtafanya kazi kwaajili yake, Ardhi ambayo Daudi alimpa Mephbosheth aliamuriwa siba na familia yake wamlimie na kuitunza kwaajili ya chakula cha Familia ya Mephibosheth kwa sababu yeye sasa anakula katika meza ya mfalme

b.      Yeye atakula mezani kwangu kama moja ya wana wa Mfalme, Mephibosheth alikuwa na furaha kujua kwamba Daudi hakuwa na mpango wa kumuua na alishangaa kupewa zawadi na kufanyiwa mambo makubwa ya kushangaza.


c.       Daudi aliitimiza ahadi yake kwa Mephibosheth na alikaa Yerusalem japo alikuwa mlemavu wa miguu, Hakuweza kujificha tena wala kumuogopa mfalme, familia ya Sauli sasa waliishi wazi miongoni mwa watu wa Mungu, alikula siku zote katika meza ya mfalme, hakuwa masikini tena maisha yake yalikuwa mazuri, alitawala pamoja na Daudi lakini alikuwa mlemavu wa miguu

Neema ya Daudi na wema wake kwa Methibosheth ni unabii wa Neema ya Mungu kwetu, sisi ndio Methibosheth wa leo

·         Sisi ni masikini, tumejificha, tuna hofu, ni vilema na tunamuogopa Mungu tumejificha mbali na uso wake kabla Yesu hajatutafuta, tumejificha kwa sababu ni wenye dhambi tunastahili kifo, hatuko katika ufalme wa Mungu
·         Tumetengwa na Mungu wetu kwa sababu ya makosa na dhambi za wazazi wetu, tangu kuzaliwa
·         Tumejificha mbele za Mungu kwa sababu hatuujui wema wake wala hatuujui upendo wake kwetu
·         Mungu anatufikiri sisi kabla ya sisi kumfikiri yeye
·         Wema wa Mungu umetufikia kwa sababu ya wema wa mtu mwingine Ni kwaajili ya Yesu Mungu ametupa neema Kama ilivyokuwa kwaajili ya Yonathan Mefibisheth alipata neema
·         Wema wa Mungu umekuja kwetu kwa sababu ya agano alilolifanya ba baba zetu
·         Tunapaswa kuupokea wema wa Mungu kwa unyenyekevu mkubwa!
·         Mungu ameturudishia kila kilichopotea, na kutupa zaidi ya kile tulichopoteza
·         Mungu amerudisha zaidi ya tulivyotegemea
·         Mungu ametukaribisha mezani pake sasa tuko karibu naye na tutakuwa na ushirika wa kudumu na yeye
·         Tunapewa watumwa wa kututumikia

·         Heshima aliyotupa Mfalme yaani Mungu wetu haiondoi ukweli kuwa sisis ni walemavu lakini ni neema na tunapaswa kusimama katika neema na kubadilisha mtazamo wa namna tunavyojiona

Somo kutoka kwa Daudi

·         Tuwatafute maadui zetu na kuwatendea mema.
·         Tuwatatute masikini, dhaifu na wenye ulemavu waliojificha na kuwabariki
·       Tuwabariki hata wale wasiostahili, tuwabariki wengine pia kwa sababu ya wengine tuwaonyeshe wema wa Mungu wetu wengine Dini ya kweli ni kuwaangalia wale wasiojiwezana kukutana na mahitaji yao, Yakobo 1:27 “ Dini iliyo safi, Isiyo na taka, mbele za Mungu Baba ni hii, kwemda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao na kujilinda na dunia pasipo mawaa.” Ni jambo la kusikitisha sana kuwa watu wengi siku hizi hasa waliomwamini Yesu wameacha kutenda mema, aidha watu wengi wanapopata madaraka makubwa huyatumia madaraka hayo kuhakikisha kuwa wengine hawainuki tena, watahakikisha wanamshughulikia kila wanayefikiri ni adui yao, watahakikisha kuwa wale walio tishio kwao wanawakandamiza mpaka wapotee, watahakikisha kuwa maisha ya wengine yanaharibika, Daudi hakuwa mtu wa namna hiyo, Mungu alipomuonyesha fadhili, aliwafadhili wengine hususani wale waliokuwa na hofu, waliokuwa wamejificha, waliokuwa wamepoteza kila kitu, waliokuwa hawana furaha Kama vile Yesu alivyosema sikuja kuwaita watu wema wapate kutubu bali wenye dhambi maana walio na afya hawahitaji Daktari, bali wale wasio na afya, Ni muhimu kujiuliza leo kuwaunaitumiaje nafasi iliyo nayo kwa manufaa ya wengine? Je wewe unaye mtu wa kumtendea mema?
Na. Rev. Innocent Kamote.
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!