Jumatatu, 30 Machi 2015

UJUMBE: KUTIWA MAFUTA KWA MTI WA MIIBA



WAAMUZI 9:1-6, 7-15
Biblia Inasema katika Mistari hii ya msingi “1. Abimeleki, mwana wa Yerubaali, akaenda Shekemu kwa ndugu za mama yake, akanena nao, na wote waliokuwa wa nyumba ya baba ya mama yake, akasema,               2. Haya, neneni tafadhali masikioni mwa waume wote wa Shekemu, mkaulize, Je! Ni lipi lililo jema kwenu, kwamba hao wana wa Yerubaali wote, ambao ni watu sabini, watawale juu yenu, au kwamba mtu mmoja atawale juu yenu? Tena kumbukeni ya kwamba mimi ni mfupa na nyama yenu.      3. Hao ndugu za mama yake wakanena habari zake masikioni mwa hao watu wote wa Shekemu maneno hayo yote; na mioyo yao ikaelekea kumwandama Abimeleki; kwa kuwa walisema, Huyu ni ndugu yetu. 4. Wakampa vipande vya fedha sabini vilivyotoka katika nyumba ya Baal-berithi, na kwa fedha hizo Abimeleki akaajiri watu wapuuzi mabaradhuli, wafuatane naye. 5. Kisha akaenda nyumbani kwa babaye huko Ofra, akawaua nduguze, hao wana wa Yerubaali, watu sabini, akawaua juu ya jiwe moja; lakini Yothamu, mwana mdogo wa Yerubaali, alisalia; kwa maana alijificha. 6. Kisha hao watu wote wa Shekemu wakakusanyika pamoja, na jamaa yote ya Milo, wakaenda na kumtawaza Abimeleki awe mfalme, karibu na huo mgandi ulio karibu na ngome iliyo katika Shekemu. “
7. Kisha walipomwambia huyo Yothamu, yeye akaenda, akasimama juu ya kilele cha kilima cha Gerizimu, akapaza sauti yake, akapiga kelele, na kuwaambia, Nisikieni mimi, enyi watu wa Shekemu, ili kwamba Mungu naye apate kuwasikia ninyi. 8. Siku moja miti ilitoka ili kuutia mmoja mafuta uwe mfalme juu yao; ikauambia mti mzeituni, Tawala wewe juu yetu. 9. Lakini huo mzeituni ukaiambia, Je! Niache mafuta yangu, ambayo kwangu mimi watu wamheshimu Mungu na wanadamu, ili niende nikayonge-yonge juu ya miti? 10. Kisha miti ikauambia mtini, Njoo wewe, utawale juu yetu.     11. Lakini huo mtini ukaiambia, Je! Niuache utamu wangu, na matunda yangu mazuri, niende nikayonge-yonge juu ya miti?  12. Kisha miti ikauambia mzabibu, Njoo wewe, utawale juu yetu. 13. Huo mzabibu nao ukaiambia, Je! Niiache divai yangu, ambayo humfurahisha Mungu na wanadamu, ili niende nikayonge-yonge juu ya miti? 14. Ndipo hiyo miti yote ikauambia mti wa miiba, Njoo wewe, utawale juu yetu.     15. Huo mti wa miiba ukaiambia miti, Kwamba ninyi mwanitia mafuta niwe mfalme juu yenu kwelikweli, basi njoni mtumaini kivuli changu; na kwamba sivyo, na utoke moto katika mti wa miiba na kuiteketeza mierezi ya Lebanoni.

Moja ya mahitaji makubwa ya wanadamu na watu wa Mungu kokote duniani ni kuwa na “ KIONGOZI MTUMISHI”   Viongozi watumishi ni watu wanaojishughulisha na kutoa huduma yenye kuwafanya watu waliokataliwa kuwa na Heshima na kamwe wao wenyewe hawajishughulishi na kuitafuta heshima, Dunia ya leo ina tatizo kubwa sana la aina hii ya viongozi ni adimu mmno na hawapatikani kirahisi

                                                         Mti wa Mzabibu katika Israel

Kitabu cha waamuzi ni kitabu cha uongozi wa mpito kutoka Yoshua kuelekea kuwa na Wafalme, Katika kipindi hiki Mungu mwenyewe aliwaongoza Israel akitumia viongozi walioitwa waamuzi hawa walikuwa mahakimu na viongozi wa kijeshi na washauri wa taifa viongozi hawa waliinuliwa na Mungu mwenyewe kwa nyakati tofautitofauti
Katika kisa tulichokisoma leo katika Mistari ile pale Juu kuna maswala mengi muhimu ya kujifunza kuhusu kanuni za uongozi wa kawaida na kiroho hasa kupitia Muamuzi aliyeitwa Abimeleki
1.       Uongozi hautafutwi kwa fitina na tamaa (Waamuzi 9:1-6)
Biblia inatufundisha kuwa katika maswala ya uongozi wa kawaida na wa Kiroho namna mtu anavyoingia au anavyotafuta namna ya kuingia madarakani inatupa ishara za msingi sana na kutuelekeza kuwa namna anavyoingia ndivyo atakavyotoka
Uongozi wa Kiroho na wa kawaida unatoka kwa MUngu na kwa kawaida hauendani na matakwa ya kibinadamu, Abimeleki aliingia Madarakani kwa tama yake mwenyewe na sio kwa mapenzi ya Mungu, aliingia kwa mauaji ya kuua ndugu zake, Kwa ujuzi wa hali ya juu na Hekima watu waelewa huwa hawatamani madaraka ya juu na mara nyingi hukataa majukumu ya kiutawala sikun zote Mungu anapowaita, hawathubutu hata kidogo kuyachukua kwa nguvu, kwa hila au kwa kampeni chafu au kwa kusukumwa kwa mtu mwingine ili wao waingie (1Samuel 24:1-6,26:7-11). Daudi alikuwa na uelewa wa hali ya juu sana , kuwa aina yoyote ya kutwaa uongozi kwa fitina utakufanya uishie kwa fitina Abimeleki hakuielewa kanuni hii lakini akiongozwa na tama na uchu wa madaraka na utukufu wa wanadamu alikuwa radhi kuua wengine ili yeye awe Kiongozi, Msomaji wangu mpendwa Je hujawahi kuona watu wa aina hii ambao walipokuwaq nje ya uongozi na hata walipoingia madarakani hawana kazi nyingine zaidi ya kuchafua, kuponda na kuharibu watu wengine ili wao waonekane kuwa Bora zaidi? Viongozi wa aina hii hugombana na kila mtu hata wale ambao hawawawazii mabaya wao huwaponda na kuwaua!
2.       Watu wenye Hekima hawatafuti Utawala (Waamuzi 9:7-15)
Maneno ya Yotham na mfano wake unatufundisha kanuni nyingine kubwa sana za huduma za uongozi wa kawaida na Kiroho Daniel 4:17 Utawala hutoka kwa Mungu na Mungu huwapa watu wanyenyekevu!
Jothamu alitoa mfano wa miti iliyokataa uongozi
a.       Mzeituni  Waamuzi 9:8-9 Mti -uliohusika kupaka watu mafuta
b.      Mtini Waamuzi 9: 10-11 ulitumika kufunika uchi kwa Adamu na Eva na matunda
c.       Mzabibu Waamuzu 9: 12-13 Uponyaji na kuchangamsha mwili na Roho
Miti hiiyohapo juu ilitumika kuleta Heshima kwa wanadamu na ilikataaa maswala ya utawala, ni miti iliyotumika kuleta heshima kwa wanadamu na iliridhika na kazi hizo, miti hii ni kimbilio na imetumika kurejesha heshima kwa wanadamu
kinabii miti hii huzungumzia

  • 1. Mzeituni- wokovu wa Israel Warumi 11
  • 2. Mtini Taifa la Israel Mathayo 24
  • 3. Mzabibu - Hali ya kiroho ya Israel Isaya 5

Baba yake Abimeleki Gideon aliwaokoa watu waliokuwa wamegandamizwa katika utumwa wa wamidian, waliokuwa wamegandamizwa kwa uchungu, alitumwa na Mungu kuwakomboa Waamuzi 6:11-14, Baada ya kuifanya kazi hiyo na kuitimiza watu walitaka kumfanya kuwa Mfalme lakini alikataa Waamuzi 8:22-23 Gideoni alielewa kuwa Jukumu lake kubwa ni kuwaletea wanadamu Heshima na sio kuwatawala alijua kuwa swala la utawala ni la Mungu, yeye alikuwa ni mfano wa Miti ile yenye hekima
3.       Kutiwa mafuta kwa mti wa Miiba Waamuzi 9:14-15
Baada ya miti mingine kukataa utawala Mti wa miiba (Abimeleki) aliamua kutawala sawa na mfano wa Yotham waamuzi 6:14
Mti wa miiba kihistoria ni mti wa laana, ulikuja duniani kama matokeo ya dhambi na kama adhabu kwa wanadamu walioasi ni mti usio na matunda yenye manufaa kwa wanadamu, ni mti unaojinufaisha wenyewe, hauwezi hata kutoa kivuli lakini unajiamini, una majigambo na kiburi na haujali kuwa unatoa shida kwa wengine na hudhalilisha wanadamu, wakati wa Kusulubiwa kwa Yesu Mti wa Miiba ulitumika kumuumiza Kristo kichwani na kumdhalilisha kama mfalme asiyena utukufu kwa wayahudi, Mti wa miiba ukichomwa moto huwaka kwa haraka sana na kusababisha madhara kwa miti yote
Taifa na kanisa ni lazima liwe makini na aina hii ya viongozi, kwamba tunachagua na kuweka viongozi wa aina gani ni lazima tumuombe Mungu atupe viongozi watakaotujali na kurudisha heshima ya wanadamu
Yesu Kristo ni Mfano katika Viongozi wakubwa sana Duniani
·         Hakuhitaji Kanisa ili awe Mchungaji nalikuwa Mchungaji tayari
·         Hakuhitaji Darasa ili awe mwalimu lakini watu walimsikiliza
·         Hakupokonya Hospitali ili awe mganga mkuu lakini watu walimfuata ili awaponye
·         Hakupindua ufalme wa Mtu lakini watu walitaka kumfanya kuwa mfalme na ndivyo alivyo
·         Kiongozi mzuri hawi mzuri anapokuwaq madarakani, ni kiongozi tu hata asipokuwa madarakani
·         Kiongozi mwema wakati wote huwa ni kimbilio la wanyonge na wenye madeni 1samuel 22:1-2
·         Kristo yesu alikuja Duniani kuleta Heshima kwa wanadamu waliokataliwa na kudharaulika, hakuwa na ubaguzi na watu walimpenda
Viongozi ambao ni mti wa miiba huendeleza mafarakano chuki na wivu na kila mtu huwa mbaya kwake hata wale waliomuunga mkono huwageuka na kuwajeruhi
Kila mtu na ajipime mwenyewe kuwa Yeye ni kiongozi wa aina gani na uhusiano wako na wanaokuzunguka ukoje jihoji je unaua wengine na kuwabomoa kwa maneno eti ili wewe uonekane kuwa Bora zaidi? Una wivu wenye uchungu? Unapenda Heshima na hutaki kushughulishwa na mabo manyonye ? Mungu atupe neema ili tusiwe kama mti wa Miiba katika jina la Yesu
Mkuu wa Wajenzi Mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote.
0718990796

Hakuna maoni: