Jumamosi, 31 Machi 2018

Je Mtu akifa atakuwa hai tena?


Ayubu 14:13-14Laiti ungenificha kuzimuni, Ukanilinda kwa siri, hata ghadhabu zako zitakapopita, Na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka! Mtu akifa, je! Atakuwa hai tena? Mimi ningengoja siku zote za vita vyangu, Hata kufunguliwa kwangu kunifikilie.”

 Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele
 
Leo hii wakristo wote nchini wanaungana na wakristo wengine duniani kote pamoja na wayahudi kuadhimisha sikukuu ya Pasaka, kukumbuka tukio la kusulubiwa, kufa na kufufuka kwa Yesu Kristo kulikotokea miaka zaidi ya 2000 iliyopita, huku Wayahudi wakiadhimisha miaka zaidi ya 3000 Tangu walipoadhimisha Pasaka ya kwanza katika siku ya 15 ya mwezi wa Nisan kwa mujibu wa Kalenda ya kiyahudi  Hapo walipookolewa kutoka Misri.

Miaka mingi sana kabla ya kufufuka kwa Yesu, mtumishi wa Mungu Ayubu aliwahi kuuliza swali la msingi sana katika maisha ya mwanadamu, swali hili ni moja ya miongoni mwa maswali ya kifalsafa, swali hili liliulizwa kutokana na hoja zilizotolewa na watu wenye hekima mbali mbali waliokuja kumtia moyo ayubu na kujiuliza swali kwanini wanadamu wanateseka, swali kuhusu mateso hata leo limekuwa ni swali kubwa sana lenye mjadala mkubwa sana katika imani mbalimbali

·         Wahindu wanaamini mateso yanatokana na KARMA yaani kuishi kwa kutenda Mema wanaamini kama ukiishi vibaya utazaliwa kitu kibaya na utapata shida, na hivyo katika mzunguko wa maisha Mungu atakupa mabaya na utachelewa kufika NIRVANA yaani mbinguni kukaa na Mungu

·         Wabudha wanaamini kuwa mateso yanatokana na tamaa, yaani kama mwanadamu ataishi mbali na tamaa atakuwa ameingia NIRVANA hata kama bado yuko Duniani, hivyo wao hujifunza kuridhika na kujikana na kuitesa miili yao 

·         Waislam wanaamini kuwa mateso ni matokeo ya Kudra za mwenyezi Mungu, yaani ni mapenzi ya Mungu kwa kadiri ya majaliwa yake 

·         Wayahudi waliamini kuwa mtu anaweza kupata mateso kama matokeo ya dhambi zake au za wazazi wake kutokana na Mungu alivyoahidi kushuhulika na kizazi hata ta tatu na nne cha wampendao au wanaomchukiza

·         Wakristo swala kuhusu Mateso ni swala pana sana na linaweza kuwa na ufafanuzi mpana sana wa kwanini wanadamu wanateseka, hata hivyo Kiongozi mkuu wa wokovu wetu yaani Yesu alikamilishwa kwa njia ya mateso

Katika kitabu cha Ayubu ni wazi kuwa Ayubu pamoja na rafiki zake walikuwa wakijadili kuhusu Mateso na sio mateso ya kawaida bali mateso ya mtu aliyeishi kwa haki, Ayubu ambaye inasemekana kuwa aliihi maisha ya hali alikuwa anateseka sana na hakuwa amepata tiba, licha ya mali yake kuwa imetekekea, licha ya kuwa amepoteza watoto wake wote, pia alikuwa na majipu mabaya yaliyokuwa yakifumba na kufumbuka mwili mzima kutoka kichwani hata unyayoni, Ayubu na wenzake walikuwa wamejadili na kutafuta suluhu bila kupata ufumbuzi na hivyo Aybu alikuwa anatazamia kufa aliamini kuwa sasa hakuna tumaini lingine lililosalia zaidi ya kifo  tu, ndipo Ayubu akauliza katika hali yakukata tamaa

Kwamba mbona miti ikikatwa shina lake huchipuka? Na maji ya bahari hupwa na kujaa ni kama inaonekana kuwa viumbe hivyo vina matumaini lakini sivyo ilivyo kwa mwanadamu, inaonekama kama mtu akifa ni mwisho wa kila kitu na hakuna matumaini ya kurejea tena, Ayubu anamwambia Mungu kwa kuwa siku za mwanadamu za kuishi ni chache na zimejaa taabu, ni afadhali angewaacha tu bila kupata mateso maana hawatakuwako tena, Hata hivyo Ayubu alikuwa na imani kuwa iko namna atamuona Mungu tu hata kama mwili wake utaharibiwa alikuwa na imani kuwa macho yake yatamuona tu   

Ayubu 19: 25-27Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi.  Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivi, Lakini, pasipokuwa na mwili wangu nitamwona Mungu; Nami nitamwona mimi nafsi yangu, Na macho yangu yatamtazama, wala si mwingine. Mtima wangu unazimia ndani yangu.”   

Swali lililoulizwa na Ayubu Mungu aliwahi kumuuliza mtumishi wake Ezekiel katika namna nyingine,  

Ezekiel 37:1-3 “.Mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu, naye akanichukua nje katika roho ya Bwana, akaniweka chini, katikati ya bonde; nalo limejaa mifupa; akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama, palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! Nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana.  Akaniambia, Mwanadamu, je! Mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana MUNGU, wajua wewe”. 

Wakati huu taifa la Yuda lilikuwa limechukuliwa utumwani Babel na kila kitu iimeaharibiwa na kufa hakukuwa na matumaini ya uhai tena ndio maana swali hili lilikuwa Gumu kwa Ezekiel yeye alijibu tu kuwa Bwana unajua wewe! Mtu awaye yote anapopitia katika mateso na huzuni na kukata tamaa huwa anafikiri kuhusu kurejeshwa tena katika hali aliyokuwa nayo mwanzoni your Golden Age!

Mtume Yohana ndiye mtume aliyeteseka sana kuliko mitume wote, inasemekana aliwahi kuviringishwa katika yasi na kuwashwa moto lakini alitoka akiwa safi, aliwahi kuchemshwa katika pipala mafuta ya lami lakini alitoka akiwa hai, alishuhudia wenzake na wakrito wengine wakifa na kuawa kwa kuliwa na simba kuchomwa moto na kadhalika yeye kutokana na kushindikana kufa waliamua kumpeleka katika kisiwa cha Patmo ili akateseke huko maisha yalikuwa ni yenye kuhuzunisha na kukatisha tamaa, Yesu alimuona Yohana akiwa amekata tamaa na alimpa ujumbe mkubwa wa kutia moyo  

Yohana 1:17-18 “Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.”

Swali la muhimu la kujiuliza ni kwanini Yesu alijitambulisha kuwa yu hai yaani amefufuka? Ni muhimu kufahamu kuwa ujumbe muhimu kwa mtu ANAYETESEKA, ALIYEKATA TAMAA, na ALIYE KATIKA HALI YA KUFA ni UJUMBE WA UFUFUO Yesu alifahamu kuwa huu ndio ujumbe pekee unaoweza kumpa mtu tumaini Jipya!

Habari njema kwa ndoa iliyokufa sio kuolewa tena ni kurejea tena kwa furaha iliyotoweka na upendo uliotoweka katika ndoa yake.

Tunapoisheherekea pasaka na kukumbuka kufufuka kwa Bwana wetu Yesu ni ujumbe wa matumaini  kwamba Bwana Yesu alikufa na akafufuka na kuwa mauti haimuwezi na kuwa ni yeye ndiye mwenye funguo za mauti na kuzimu, ki msingi Yesu anajibu la swali la Ayubu kuwa mtu akifa atakuwa hai tena Yesu anajibu swali hili kuwa ndio mtu akifa anaweza kuwa hai tena na anatutangazia wazi kuwa yeye anazofunguo za mauti na kuzimu na hivyo anauwezo wa kufufua matumaini yaliyotoweka kwako, anauwezo wa kufufua huduma yako, anauwezo wa kurejesha watoto wako, ana uwezo wa kurejesha kila kilicho haribiwa na kuuawa na ibilisi, ana uwezo wa kurejesha na kufufua taifa linalomtumaini yeye, Pasaka hii mimi sihitaji habari nyingine yoyote nahitaji kusikia habari za matumaini ya kuwa Yesu Kristo yuko hai na ndiye mwenye Mamlaka ya kifo  na uzima na ana uwezo wa kufufua ndoto zetu, maisha yetu,  matumaini yetu, uzima wetu, mimi sihitaji waraka wa maaskaofu nahitaji kumuona mteteaji wangu akisimama kiunitetea dhidi ya kila aina ya unyonge na utumwa Pasaka ina uhusiano na ukombozi nahitaji kumuoja Yesu akinikomboa mimi na familia yangu na watu wangu na taifa langu hii ndio habari njema ya ujasiri kuwa mauti haina nguvu katika maisha yetu, imepoteza mamlaka ni yesu pekee mwenye mamlaka hiyo yeye atafufuka pamoja na mashaka yangu yeye atahuisha nafsi yangu!

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni: