Jumanne, 12 Novemba 2019

Usiudharau Msalaba!


Waebrania 12:2-3 “tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.”


Utangulizi:
Usiudharau Msalaba wa Yesu! Angalia iko nguvu ya ajabu na uwezo wa ajabu katika Msalaba, Msalaba unaweza kukupa ushindi dhidi ya changamoto zozote unazozipitia katika maisha, Ushindi mkubwa katika maisha yetu utapatikana kwa kitafakari kazi kubwa iliyofanya na Yesu Kristo pale Msalabani, wokovu kamili umekuja kwetu kupitia Msalaba na ndio maana ni muhimu sana kuutafakari , na kukumbuka kazi aliyoifanya Yesu Pale Msalabani

Paulo Mtume anaonyesha kuwa msalaba una nguvu, na kwa watu wanaopotea unaokana kuwa ni upuuzi lakini kwetu sisi tunaookolewa ni Nguvu ya Mungu angalia katika  1Wakoritho 1:18 “Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu.Ulimwengu unafahamu kuwa katika Historia Mfalme mmoja wa kipagani wa Rumi aliyejulikana kama CONSTANTINE akiwa pamoja na askari wake vitani tarehe 27/10/312 Baada ya Kristo, akiwa katika kambini Jeshini na wanajeshi wake aliona alama ya Msalaba upande wa juu wa jua na maandishi yaliyoansikwa kwa lugha ya Kiyunani, Lakini yanasomeka au yamepata umaatrufu zaidi katika Lugha ya KilatiniIN HOC SIGNO VINCES” Kwa kiinregreza “IN THIS SIGN YOU WILL CONQUERYaani kwa ishara hii Utashinda. Unaona kwa mujibu wa mwana historia maarufu wa karne ya tatu Askofu Eusebius wa Kaisaria anaeleza kuwa Contantine alikuwa akisonga mbele na jeshi lake  bila kutaja ni mahali ganina alipoangalia juu ya jua aliona msalaba unaong’ara  juuyake  yaliandikwa maneno hayo, inasemekana kuwa Contantine hakuwa ameelewa maana ya maono yale lakini usiku alipokuwa amelala aliona katika ndoto Yesu akimfafanulia kwamba anaopaswa kuitumia alama ya msalaba dhidi ya adui zake  na kuwa atapata ushindi, Tangu wakati huo wakristo wengi wa maeneo ya kilatini huutumia msalaba kama alama ya ushindi, wachezaji wa mpira wa miguu wanapoingia viwanjani hugusa uwanja na kuonyesha alama ya msalaba, alama ya msalaba ilipata umaarufu mkubwa kutokana na ushindi alioupata Contsntine ambaye baada ya ushindi wake aliifanya Roman kuwa himaya ya Kikristo.
Msalaba si jambo la kupuuzi ni ushindi wa maisha yetu, nilipokuwa nikitafakari kwamba ni jambo gani naweza kuzungumza na waomaji wangu na wasikilizaji wangu, Roho Mtakatifu aliniambia waaembie wasiudharau Msalaba, hii haina maana ya kuwa watu waubusu na kuuheshimu msalaba wenye sanamu ya Yesu hapana, maana yake ni lazima wakubali na kumtafakari Yesu mwenyewe aliyekubali kufa msalabani kwaajili yao/yetu.

Unapofungua Biblia yako katika injili ya Luka 23:35-43 tunapata habari za watu wawili wanaowakilisha jambo mmoja  watu wanaodharau kazi ya msalaba na wa pili watu wanaouheshimu msalaba watu hawa walikuwa karibu kabisa na Yesu aliyekuwa anasulubiwa hali kadhalika na wao walikuwa wakisulubiwa siku ile hebu tusome kwanza tuone
Luka 23:35-43 “Watu wakasimama wakitazama. Wale wakuu nao walikuwa wakimfanyia mzaha, wakisema, Aliokoa wengine; na ajiokoe mwenyewe, kama ndiye Kristo wa Mungu, mteule wake. Wale askari nao wakamfanyia dhihaka, wakimwendea na kumletea siki,  huku wakisema, Kama wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi, ujiokoe mwenyewe. Na juu yake palikuwa na anwani; HUYU NDIYE MFALME WA WAYAHUDI. Na mmoja wa wale wahalifu waliotungikwa alimtukana, akisema, Je! Wewe si Kristo? Jiokoe nafsi yako na sisi.Lakini yule wa pili akamjibu akamkemea, akisema, Wewe humwogopi hata Mungu, nawe u katika hukumu iyo hiyo? Nayo ni haki kwetu sisi, kwa kuwa tunapokea malipo tuliyostahili kwa matendo yetu; bali huyu hakutenda lo lote lisilofaa. Kisha akasema, Ee Yesu, nikumbuke utakapoingia katika ufalme wako. Yesu akamwambia, Amin, nakuambia, leo hivi utakuwa pamoja nami peponi.”
Unaweza kuona watu walimdharau Yesu pale msalabani, wakatoa maneno ya kejeli na kumfanyia mzaha walisema aliokoa wengine na ajiokoe mwenyewe hapa msalabani hususani kama yeye ndio masihi, aidha mhalifu mmoja aliyekuwa anasulubiwa pamoja na Yesu naye bila aibu alimtukana Yesu na kusema je wewe sio Kristo jiokoe nafsi yako na sisi, huyu aliupuuzia Msalaba na kujikuta yuko jehanamu milele na milele
Lakini yule muhalifu mwingine alikuwa na dalili kadhaa zilizomletea wokovu:-
a.       Alikuwa na Hofu ya Mungu Luka 23:40 alimuuliza mwenzake Je wewe humuogopi Mungu
b.      Alitambua kuwa yeye ni mwenye dhambi Luka 23:41 alimweleza mwenzake kuwa sisi tunasulubiwa kwa sababu ya maovu yetu na uhalifu wetu, hivyo tunapata kilicho halali yetu ni malipo ya maovu yetu  Lakini sivyo ilivyo kwa Yesu yeye yuko pale akiwa hata hatia
c.       Alimuamini Yesu kuwa anaweza kumuokoa Luka 23:42 alimwambia Yesu unikumbuke utakapokuja katika ufalme wako, Yeye aliamini kuwa Yesu huyu aliyetundikwa Msalabani ni mfalme na atatawala ilikuwa ni imani ya ajabu alikuwa na utambuzi kuwa msalaba sio mwisho wa maisha ya Yesu
d.      Mwisho Luka 23:42 alijiombea aweze kuokolewa alimwambia Yesu unikumbuke utakapokuja katika ufalme wako, jamaa alijitambua kuwa amefanya maovu mengi na kuwa hasathili chochote alijiombea rehema kwa Yesu palepale msalabani, huyu alikuwa ni kama mtu anayejua kuitumia nafasi aliyoipata katika dakika ya mwisho, ni kama timu iliyokuwa imekwisha kufungwa kisha ikasawazisha goli katika dakika ya nyongeza, Yesu alimjibu Lao utakuwa pamoja nani peponi
Unapopitia changamoto za iana yoyote, mitihani ya aina yoyote, mateso ya aina yoyote, majonzi ya aina yoyote, dhuluma ya aina yoyote machozi ya aina yoyote,kuonewa kwa namna yoyote, unyama wa aina yoyote, uonevu wa aina yoyote, majaribu ya aina yoyote, kucheleweshwa kwa aina yoyote, ni lazima ukumbuke na kuuangalia msalaba hapo ndipo palipo siri ya ushindi wako, ushindi wangu uko Msalabani, siogopi chochote Nauangalia msalaba kwa alama hii nitashinda kama alivyoshinda Mfalme Constantine, wewe nawe ni mshindi ni mshindi kupitia kazi iliyofanya na Yesu pale msalabani, mwangalie Yesu, katika mapito yako mwangalie Yesu , katika mateso yako mwangalie Yesu, katika ugumu wa maisha unaoupitia mwangalie Yesu, katika kesi yako na majonzi na mateso na njaa, na uchgu na kupungukiwa na aibu nadharau nakukataliwa na kutokufaanamakosa wewe mwangalie Yesu tu, na kwa kuiangalia kazi aliyoifanya pale msalabani wewe ni mshindi, Kumbuka Msalaba! Usiudharau!

Na Mkuu wa wajenzi mwenye hekima
Rev. Innocent Kamote.
 
0718990796.

Hakuna maoni: