Jumapili, 7 Juni 2020

Mkristo na Mitandao ya kijami



Luka 13:1-5Na wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichanganya damu yao na dhabihu zao.  Akawajibu akawaambia, Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo.” 







Utangulizi:


Ni muhimu kufahamu kuwa taarifa (Habari) ni moja ya nyenzo yenye kubwa sana yenye kubeba maana zinazoweza kujenga au kubomoa jamii, taarifa zina nguvu, zina nguvu zote mbili za kujenga au kubomoa, Mungu ndiye mwanzilishi wa taarifa, Alipomuumba mwanadamu alimpa taarifa ya namna na jinsi ya kuutawala ulimwengu alimweleza kama mtu huru namna anavyoweza kuutumia ulimwengu na alimuelekeza namna nzuri ya kuutumia ulimwengu lakini pia alimuonya kuwa kama atautumia ulimwengu vibaya angeweza kuleta madhara makubwa kwa maisha yake na jamii yake yaani kifo. Taarifa inaweza kuwa ndogo lakini kama ikitumika vibaya inaweza kuleta madhara makubwa sana kwa jamii kama njiti ya kiberiti inavyoweza kuchoma msitu mzima! 


Ni muhimu kufahamu kuwa nyakati za Biblia pia kulikuwa na namna ambavyo watu waliweza kupokea na kutoa taarifa kama unavyoweza kuona katika kifungu hiki


Luka 13:1-5Na wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichanganya damu yao na dhabihu zao.  Akawajibu akawaambia, Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo.” 


Yesu alikuwa amepokea taarifa au habari kuhusu Wagalilaya waliouawa vibaya na Pilato, na baada ya kupokea taarifa hizi tunaona namna Yesu alivyozitumia taarifa hizo sasa kuwafundisha watu wake somo kuhusu toba na pia akiunganisha na taarifa nyingine ya watu kumi walioangukiwa na mnara huko siloamu, Kutoa na kupokea taarifa ni haki ya kila jamii, Yesu aliitumia taarifa hii kwa sababu huenda aliamini au kulikuwa na namna ya uthibitisho kuwa chanzo cha taarifa alichokipokea kilikuwa ni chanzo cha kuaminika na kwa sababu hiyo taarifa alizozipokea zilikuwa na ukweli, na hivyo alizitumia kufundisha kama mfano kwa jamii iliyomzunguka, Unapochunguza kwa kina mafundisho ya Yesu Kristo utaweza kuona alikuwa na mifano mingi sana na alikuwa na stori nyingi sana na khadithi nyingi sana na nyingi alizitumia katika kuielimisha jamii na kuijenga kama jinsi Mungu anavyotaka.


Kutokana na kupanuka kwa technolojia leo hii kumekuweko na vyanzo vingi sana vya kupokea na kutoa habari, lakini ni jambo la kusikitisha sana kuwa jamii ya leo haizingatii uadilifu katika swala zima la kupokea na kutoa habari, Mfano mzuri ni tukio la hivi karibuni ambapo watangazaji/ waandishi wa habari wa TBC walifariki, lakini wakati huo huo kulikuwa na taarifa za kufariki kwa Mtangazaji wa shirika hilo wa habari za biashatra aliyeitwa “Gloria Maiko” aidha kabla ya kuenea kwa taarifa hii kuhusu kufa kwake ilienea taarifa kuwa Gloria anaumwa sana tena ana ugonjwa wa Corona, Mimi napenda habari, mimi ni mwana habari, mimi nimesoma Introduction to jounalism, napenda kupata taarifa kwa sababu huwa pia natoa taarifa yaani nazitumia kuijenga jamii, sio hivyo tu unaposoma chuo cha Biblia kwaajili ya kazi ya uchungaji hausomei Biblia pekee unaandaliwa pia kuwa mwana habari kwa sababu kanisa linaweza kuwa na gazeti, Kanisa linaweza kuandika vitabu, kanisa linaweza kuwa na televisheni, kanisa linaweza kuwa na radio, kanisa linaweza kuwa na ukurasa wa faceboo, instagram, blog na nyenzo nyingine za utoaji wa taarifa kwa hiyo lazima watu wa Mungu wawe na angalau ufahamu mdogo tu kuhusu upokeaji na utoaji wa habari, wakati huu nilisoma chanzo kingine kuhusu Gloria kinasema hivi ngoja nikinukuu


 TBC1 tuliwaonya kukusanyika siku ya msiba wa Marini Hassan hamkusikia! Haya leo Joseph Kambangwa mfanyakazi wenu kafa kwa corona na maziko ni kesho saa 4 huko huko Mloganzila! **Gloria Maiko (anatangazaga habari za biashara) yuko hoi ana dalili zote za corona! RIP Kambangwa  


mwisho wa kunukuu, angalia huyu ni mtu mwenye akili timamu, ni mtu ambaye jamii inamtegemea, jamii inaamini labda katika hiki alichokisema lakini je habari hii ilikuwa na malengo gani kwa jamii, ilikusudia nini kwa Gloria? Na kwa familia yake, je ilikuwa inajenga au inabomoa? Kwa sababu baada ya kuenea kwa Taarifa hii Gloria Maiko alijitokeza kwenye mitandao ya kijamii akithibitisha kuwa yeye yuko hai na wala haumwi! Lakini mwandishi anajisikiaje? Baada ya Gloria mwenyewe kutokea je wale walioeneza katika mitandao ya kijamii na kutoa salamu za astarehe kwa amani wanajisikiaje katika mioyo yao baada ya mtu mliyemzushia kifo kujitokeza na kuonyesha yuko hai, nimetoa tu mfano huu lakini Jambo hili limewahi kuwatokea wengi, hapa nchini hata Mheshimiwa Augustin Lyatonga Mrema alizushiwa mara kadhaa mpaka alipojitokeza na kuionya jamii kuwa yeye ni mzima na kuwa kuanzia sasa atawafungulia mashtaka watu wanaoanzisha uzushi huu, Huko ulaya mambo ya aina hii yako sana lakini kwa mujibu wa tamaduni zao, Lakini sisi ni Watanzania na wana Afrika Mashariki je mambo haya ni sawasawa? Je wale waliosomea uandishi wa habari jambo hili ni sawa katika utoaji wa taarifa na upokeaji, Je wale wanaozushia wenzao hujitokeza kuomba radhi? Je wanachukuliwa hatua gani je ni aina gani ya jamii tunaijenga ya watu wanaosema ukweli au jamii ya waongo? Mungu ametupa hekima na akili na maendeleo makubwa ya nyenzo za utoaji wa taarifa lakini ni muhimu zikatumika kwaajili ya utukufu wa Mungu, kwa wakristo tunaambiwa katika maandiko kwamba lolote tulifanyalo kwa neno au kwa tendo tulifanye kwa utukufu wa Mungu ona


 Wakolosai 3:17 “Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.” 


Swali kubwa ambalo kila mwana jamii anapaswa kujiuliza na kuhoji ni kuwa kama Yesu angekuwepo Duniani leo ni habari gani angeikubali na habari gani angeikataa na je angetumiaje mitandai ya kijamii, na sisi vilevile tujiulize je tunapopata habari ambazo hazina uhakika haziko sahihi, hazina utu, zina mitazamo hasi, zinaupendeleo, na kama ni za uongo wanaozitoa hawawajibishwi, habari hazina kiasi, na ziko kinyume na uadilifu je tungejisikiaje? Nafikiri wote tuna namna ambavyo tunatarajia jinsi habari au taarifa inavyopaswa kuwa! Mkurugenzi wa Maadili ya uandishi wa habari aitwaye Aidan White anasema ziko kanuni 400 ambazo wanahabari wanapaswa kuzizingatia lakini ziko kanuni 5 Muhimu zaidi ambazo kila mwandishi na mtoa habari anapaswa kuzifuata bila kushindwa 


1.       Ukweli na Uhakika (Accuracy) – “the quality or state of being correct or precise” Maana yake kila mtoa habari na mpokea habari na mtawanya habari au taarifa anapaswa kuhakikisha kuwa taarifa anayoitoa ina UKWELI na pia IMEHAKIKISHWA. Lakini pia kuzinagatia kuwa habari inaweza kuwa ya ukweli na imehakikishwa lakini swali je ni wakati muafaka kuitoa? Kwa sababu inaweza kuwa kweli na ya uhakika lakini wakati ukawa hauruhusu kuisema au mazingira yakawa hayaruhusu kusema !, tunapohubiri injili watu wa Mungu huwa hatuleti maneno ya kushawishi,  watu wanapaswa kuziamini habari njema na za kweli ili wapate kuamini na kuokolewa.


Isaya 53:1 ”Ni nani aliyesadiki habari tuliyoileta? Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani?  wale yenye ufundi wa kibinadamu tunapopeleka habari njema tunapeleka habari ambazo ni za kweli na zinathibitishwa na Roho Mtakatifu, ile Nguvu ya ukweli pekee inauwezo wa kuwaweka watu huru na kuiponya jamii. Nyakati za Biblia watu waliwahi kueneza habari za uongo kwaajili ya faida zao na hivyo ikafikiriwa kuwa Yesu aliibiwa na hakufufuka ona. 


Mathayo 28:12-15 “Wakakusanyika pamoja na wazee, wakafanya shauri, wakawapa askari fedha nyingi, wakisema, Semeni, ya kwamba wanafunzi wake walikuja usiku, wakamwiba, sisi tulipokuwa tumelala.Na neno hili likisikilikana kwa liwali, sisi tutasema naye, nanyi tutawaondolea wasiwasi.Basi wakazitwaa zile fedha, wakafanya kama walivyofundishwa. Na neno hilo likaenea kati ya Wayahudi hata leo”. Waandishi wa habari ni kama manabii wanapaswa kutia habari za ukweli na uhakika ona Kumbukumbu la Torati 18:22 “Atakaponena nabii kwa jina la Bwana, lisifuate jambo lile wala kutimia, hilo ndilo neno asilolinena Bwana; kwa kujikinai amelinena huyo nabii, usimwogope” 


Biblia liagiza kuwa kama nabii atatia taarifa na akadai taarifa hiyo imetoka kwa Mungu na kumbe sivyo yaani haikutimia yaani haina ukweli asiogopwe maana yake achukuliwe hatua, kwa hiyo kama watu wanaotoa habari na habari zao zikawa sio za uhakika torati inashauri wachukuliwe hatua katika agano la kale waliuawa, katika agano jipya  wanapaswa kuchukuliwa hatua, Yesu angelikuwepo leo hangeweza kukubalia habari ambayo haijathibitishwa haina ukweli na haijahakikishwa!  Habari zisizo za kweli zinaumiza mioyo ya watu na kubadili mtizamo wa mtu Habari za uongo zinasumbua na kuiumiza jamii Yakobo alilia na kuomboleza kwa miaka mingi sana baada ya kueletewa habari kuwa yusufu mwanae amekufa ona 


Mwanzo 37:31-35 “Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa.Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi. Wanawe wote, na binti zake wote, wakaondoka wamtulize, lakini akakataa kutulizwa, akasema, La! Nitamshukia mwanangu, nikisikitika, hata kuzimu. Baba yake akamlilia” 



Yusufu hakuwa amekufa kweli lakini wana wa israel walimdanganya baba yao naye akaamini kuwa mwanaye Yusufu amekufa lakini kumbe habari hii haikuwa sahihi Yakobo aliishi kwa huzuni kwa miaka 13 akiwa na mtazamo kuwa mwanaye amekufa, Ni mpaka watoto wake tena walipomletea habari kuwa mwanao Yusufu yuko hai ndipo Roho ya Yakobo ilipofufuka kwa furaha



Mwanzo 45: 25-28 . “Wakatoka Misri, wakafika nchi ya Kanaani kwa Yakobo, baba yao. Wakampasha habari, wakisema, Yusufu angali hai; naye ndiye mtawala katika nchi yote ya Misri. Moyo wake ukazimia, kwa sababu hakuwasadiki. Wakamwambia maneno yote ya Yusufu, aliyowaambia; na alipoona magari aliyoyapeleka Yusufu, ili kumchukua, roho ya Yakobo baba yao ikafufuka. Israeli akasema, Yatosha! Yusufu mwanangu angali hai; nitakwenda, nionane naye kabla sijafa.” 



Kumbe sasa tunaweza kufahamu kuwa habari inaweza kuhuisha au kuua kwa msingi huo ni vema wakristo wawe makini katika kutoa na kupeleka taarifa, Taarifa inauwezo wa kuua, Habari inaweza kuwa ya kweli lakini lazima pia inagaliwe namna unavyoipeleka kwa sababu ina nguvu inaweza kuua au kupoteza maisha ya mtu ona 


1Samuel 4:10-17 “Wafilisti wakapigana nao, Israeli wakapigwa, wakakimbia kila mtu hemani kwake; wakauawa watu wengi sana; maana katika Israeli walianguka watu thelathini elfu wenye kwenda vitani kwa miguu.Hilo sanduku la Mungu Likatwaliwa; na Hofni na Finehasi, wale wana wawili wa Eli, wakauawa. Basi, mtu mmoja wa Benyamini akapiga mbio kutoka mle jeshini akafika Shilo siku ile ile, hali nguo zake zimeraruliwa, na mavumbi kichwani mwake.  Alipofika, tazama, Eli alikuwa ameketi kitini pake kando ya njia, akingojea; maana moyo wake ulitetemeka kwa ajili ya sanduku la Mungu. Na yule mtu alipoingia mjini, akatoa habari, mji wote ukalia. Naye Eli aliposikia kelele za kile kilio, akasema, Maana yake nini kelele za kishindo hiki? Yule mtu akafanya haraka, akaenda, akamwambia Eli. Basi Eli umri wake umepata miaka tisini na minane; na macho yake yamepofuka hata asiweze kuona. Yule mtu akamwambia Eli, Mimi ndimi niliyetoka jeshini, nami leo hivi nimekimbia toka jeshini. Naye akasema, Yalikwendaje, mwanangu? Yeye aliyeleta habari akajibu, akasema, Israeli wamekimbia mbele ya Wafilisti, tena watu wengi sana wameuawa, hata na wana wako wawili, Hofni na Finehasi, wamekufa pia, na sanduku la Mungu limetwaliwa.” 


2.       Huru – Independence – yaani taarifa inapaswa kuwa ya haki isiyopendelea upande wowote, Kila mtoa habari na mpokea habari anapaswa kuwa na mtizamo wa haki, hapaswi kuwa mwenye kupendelea upande fulani, mfano kama ni kwa habari ya vyama vya siasa ni vema mtoa habari na mpokea habari wakawa hawana mtazamo wa kisiasa au mtazamo wa siasa zinazofungamana na upande fulani, taarifa itolewe kwa uwazi na kwa haki na ihaririwe kwa uwazi na kwa haki, Maandiko yanatufundisha wale wanaomuamini Yesu kuwa imani yetu katika Kristo isiwe kwaajili ya kupendelea watu 


Yakobo 2:1 “Ndugu zangu, imani ya Bwana wetu Yesu Kristo, Bwana wa utukufu, msiwe nayo kwa kupendelea watu unaona Yesu angelikuwepo leo hangeweza kupokea au kutoa habari inayomkandamiza mtu fulani haki ingesimama, Wako watu ambao wanaweza kutoa taarifa lakini kwaajili ya maslahi yao, kwa hiyo kanuni za kiandishi zinataka watu wasipeleka taarifa kwaajili ya faida yao ona pia 


Yuda 1:16 “Watu hawa ni wenye kunung'unika, wenye kulalamika, waendao kwa tamaa zao, na vinywa vyao vyanena maneno makuu mno ya kiburi, wakipendelea watu wenye cheo kwa ajili ya faida.”  Kila mpokea habari na mtuma habari hapaswi kuwa na upendeleo anapaswa kutenda haki kama hakimu Mambo ya walawi 19:15 “Msitende yasiyo haki katika hukumu, usimpendelee mtu maskini, wala kumstahi mwenye nguvu; bali utamhukumu jirani yako kwa haki.” Maandiko yanamtaka kila mmoja kutenda haki kuhukumu kwa haki agizo hili sio kwa mahakimu pekee bali na kwa wanaotoa taarifa na kupokea taarifa au kusambaza taarifa na 


Kumbukumbu la Torati 1:16-17 “Nikawaagiza wakati ule waamuzi wenu, nikawaambia, Sikizeni ninyi maneno kati ya ndugu zenu, mkaamue kwa haki kati ya mtu na nduguye, na mgeni aliye pamoja naye. Msitazame nafsi za watu katika hukumu; mwasikize wadogo na wakubwa sawasawa; msiche uso wa mtu awaye yote; kwa kuwa hukumu ni ya Mungu; na lile neno liwashindalo mniletee mimi, nami nitalisikiza.         


3.      Usiyo na Masalahi nayo – Impartiality kwa kiingereza neno hili maana yake “Impartiality is a principle of justice holding that decisions should be based on objective criteria, rather than on the basis of bias, prejudice, or preferring the benefit to one person over another for improper reasons“ yaani kanuni ya haki inayotaka maamuzi yafanyike kwa mujibu wa vigezo na sio kwa sababu mtu una masalahi fulani, au ukungu fulani unaotaka mtu mmoja anufaike dhidi ya mwingine kwa sababu zisizo sahihi, unapopokea au kutoa habari kwa makusudi maovu au kwa uependeleo kwa Mungu hufai kuwa mtu wa haki, Yesu angekuwepo leo kwa habari ya kupokea na kutoa habari angehukumu kwa haki Isaya 11:1-5Basi litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi yake litazaa matunda. Na roho ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha Bwana; na furaha yake itakuwa katika kumcha Bwana; wala hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake, na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya.Na haki itakuwa mshipi wa viuno vyake, na uaminifu mshipi wa kujifungia” Mtoa habari au mpokea habari anapaswa kuwa mwaminifu na kuwa mtu wa haki, wakati mwingine kwa sababu ya mitazamo fulani na hata kwaajili ya kupokea rushwa tumepokea au kutoa habari kwa maslahi ya upande fulani kwa sababu tunaletu jambo, Mungu hapendezwi na utaratibu huo na ndio maana hatua kali sana zinapaswa kuchukuliwa endapo itabainika mwandishi kuwa ana dalili za kupokea rushwa.


Nyakati za Kanisa la Kwanza stephano aliuawa kwa sababu ya maslahi ya watu, na sio kwa sababu alisema uongo Matendo 6:9-15 “Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano;  lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye. Hata wakashawishi watu waliosema, Tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu. Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi, wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati; maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahali hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa. Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso wake kuwa kama uso wa malaika.” Stephano alihukumiwa na kuuawa kwa sababu ya taarifa za uongo kwa masalahi ya watu wa dini kwa sababu hawakutaia kuambiwa ukweli, kila mpokea taarifa na mtuma taarifa anapaswa kyuhakikisha kuwa anatoa taarifa yenye kujenga jamii na sio kuua au kwa sababu ana maslahi nayo.


4.       Taarifa yenye kujali utu –  Sence of Humanity Ni muhimu kufahamu kuwa biblia inasema usiue kuua kuko kwa namna nyingi sana unaweza kuua kwa kutumia maneno, unamuua mtu kisiasa, umamuharibia mtu au unamchafua mtu huku ni kuua mpokea habari au mtoa habari anapaswa kuhakikisha kuwa anajali utu, ni dhambi kuandika, kupokea au kutoa habari yenye kudhuru, yenye kuharibu ubinadamu wa mtu, au yenye kumvunjia mtu heshima hatupaswi kutoa habari wala kusambaza habari au habari picha yenye kuharibu maisha ya wengine au kudhalilisha, watu wasiojua kutumia mitandao ya kijamii wanapiga picha hata za watu waliopata ajali mbaya na kuzisambaza katika mitandao ya kijamii, katika nchi nyingi zilizoendelea hata mwili wa Marehemu anapoagwa haupigwi picha, Picha ya marehemu inayoruhusiwa kuonekana ni ile ambayo wanafamilia wataiweka juu ya jeneza kwaajili ya kumbukumbu yake, nchi nyingi zawatu wasiostaraabika utaona mtu aliyepasuka kichwa kwa ajali, waliovunjika miguu, mtu mwenye ulemavu wa jabu na picha za kutisha sana zinarushwa kwenye mitandao ya kijamii, je umewahi kujiuliza kwanini mtu akipata ajali watu hutoa nguo zao na kuufunika mwili wa marehemu?  Ni kwaajili ya kujali utu, Mungu hawezi kukubali na kufurahia utu wa mtu udhalilishwe, kwa msingi huo kila mtoa habari na mpokea habari namsambazaji anapaswa mno sana kuzingatia utu, Yesu alikubali kifo cha aibu pale msalabani ili kutunza heshima ya mwanadamu, natarajia kuona jamii iliyostaarabika ambayo haitarusha picha ya marehemu yoyote akiwa na pamba puani, wala hata jeneza ikiwezekana na kama umefiwa weka picha ya aliyefariki ikiwa katika hali ya ubora na usiiwekee “X” muonyehse mtu enzi za ubora wake, sikitika kwa kumpoteza mtu huyo lakini usimdhalilishe nduguyo, aidha usisambaze wala usizikubali picha za watu walio katika hali mbaya za ajali, mwanadamu ameumbwa kwa sura na utukufu wa Mungu na lazima utu wa kila mtu uheshimiwe, hali kadhalika picha za ngono na zenye kuonyesha uchi ni mwiko kwa watu waadilifu, Mtu wa haki huwa hadhalilishi mtu mwingine. Mathayo 1:18-19Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri.” Mtu wa haki huwa hafanyi mambo kwa kusudi la kumuaibisha mtu mwingine hata kama mtu huyo ni kweli amefanya jambo hilo Yesu angekuwepo leo hangekubali kupokea au kutoa taarifa zinazodhalilisha utu wa mwanadamu ambao ni uumbaji wake.


5.       Kuwajibika – accountability - In ethics and governance, accountability is answerability, Maana yake kila mtoa habari na mpokea habari na msambaza habari wanapaswa kujua na kukubali kuwa wanawajibika kwa habari wanazotoa au kusambaza, kwa msingi huo kama utatoa habari na ikasababisha madhara au hata isiposababisha madhara ufahamu kuwa unatakiwa kuwa na utayari wa kuijibia kuitolea maelezo na kuwa tayari kuomba radhi ikiwa umekosea,  au kukubali kukosoelewa na kupokea maoni ya jamii kuhusiana na ulichokitoa au kukisema na ikiwezekana kuwa tayari kushitakiwa mahakamani na hata kufungwa na au hata kuuawa na wale watakaochukizwa na habari ulizozitoa Mfano 2Samuel 1:2-15 “hata siku ya tatu ikawa, tazama! Akaja mtu kutoka kambi ya Sauli, nguo zake zimeraruliwa, tena ana mavumbi kichwani mwake; basi, ikawa alipomfikia Daudi, akaanguka chini, akamsujudia. Daudi akamwambia, Umetoka wapi? Akamwambia, Nimeokoka katika kambi ya Israeli. Daudi akamwambia, Yalikwendaje? Tafadhali uniambie. Akajibu, Watu wamekimbia vitani, tena watu wengi wameanguka wamekufa; hata Sauli naye na Yonathani, mwanawe, wamekufa.Daudi akamwambia yule kijana aliyempa habari, Umejuaje ya kuwa Sauli na Yonathani mwanawe wamekufa?  Yule kijana aliyempa habari akasema, Nalikuwapo kwa nasibu juu ya kilima cha Gilboa, na tazama, Sauli alikuwa ameegemea fumo lake; na tazama, magari na wapanda farasi wanamfuatia kwa kasi. Naye alipotazama nyuma, akaniona, akaniita. Nikajibu, Mimi hapa. Akaniambia, U nani wewe? Nikamjibu, Mimi ni Mwamaleki. Akaniambia, Tafadhali simama karibu nami, ukaniue, maana shida imenipata; kwa sababu roho yangu ingali hai ndani yangu. Basi, nikasimama karibu naye, nikamwua, kwa sababu nalijua hakika ya kuwa hawezi kupona baada ya kuanguka; kisha nikaitwaa ile taji iliyokuwa kichwani mwake, na kikuku kilichokuwa mkononi mwake, nami nimevileta hapa kwa bwana wangu. Ndipo Daudi akashika nguo zake akazirarua na kadhalika watu wote waliokuwa pamoja naye; wakaomboleza, wakalia, wakafunga hata jioni, kwa ajili ya Sauli, na kwa ajili ya Yonathani mwanawe, na kwa ajili ya watu wa Bwana na kwa ajili ya nyumba ya Israeli; kwa sababu wameanguka kwa upanga. Naye Daudi akamwambia yule kijana aliyempa habari, Watoka wapi wewe? Akajibu, Mimi ni mwana wa mgeni, Mwamaleki. Daudi akamwambia, Jinsi gani hukuogopa kuunyosha mkono wako umwangamize masihi wa BWANA? Ndipo Daudi akamwita mmoja wa vijana, akamwambia, Mwendee, ukamwangukie. Basi akampiga hata akafa.”, kila habari unayoitoa ni muhimu kufahamu kuwa itakugharimu, Kijana huyu alitoa habari iliyoweza kudhuru maisha yake, yeye alifikiri atapata sifa kwa Daud lakini kifo cha Sauli na Jonathan haikuwa habari njema kwa Daud na hivyo kijana huyu aliuawa, habari zinaweza kugharimu maisha yetu mbele za Mungu na wanadamu, Yesu alisema kila neno lisilo na maana atakalolinena mwanadamu atatoa hesabu yake Mathayo 12:36-37Basi, nawaambia, Kila neno lisilo maana, watakalolinena wanadamu, watatoa hesabu ya neno hilo siku ya hukumu. Kwa kuwa kwa maneno yako utahesabiwa haki, na kwa maneno yako utahukumiwaYesu atakapokuja atawahukumu wazushi wote hapa aliwaonya watu waliokuwa wakitoa habari zisizo sahihi kuhusu utendaji wa Yesu Kristo, Yesu anatoa pepo kwa Roho wa Mungu wapotoshaji wakesema anatumia nguvu za mkuu wa pepo Baalzebub, lazima ieleweke wazi kuwa watoa habari watawajibika sio mbele za wanadamu tu na mbele za Mungu! Wote tunakumbuka kuwa Sababu ya kifo cha Yohana Mbatizaji na kuwekwa kwake gerezani kulitokana na kupokea habari na kuzitumia habari hizo kumkemea Mfalme Herode ona Mathayo 14:3-10 “Maana Herode alikuwa amemkamata Yohana, akamfunga, akamtia gerezani, kwa ajili ya Herodia, mke wa Filipo nduguye. Kwa sababu Yohana alimwambia, Si halali kwako kuwa naye. Naye alipotaka kumwua, aliwaogopa watu, maana walimwona Yohana kuwa nabii. Hata ilipofika sikukuu ya kuzaliwa kwake Herode, binti Herodia alicheza mbele ya watu, akampendeza Herode. Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba.  Naye, huku akichochewa na mamaye, akasema, Nipe hapa katika kombe kichwa cha Yohana Mbatizaji.  Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; akatuma mtu, akamkata kichwa Yohana mle gerezani.Watoa habari wengi sana wameuawa na kupotezwa na kufunguliwa mashitaka duniani kwa sababu ya utoaji habari, habari inaweza kuwa ya kweli na imethibitishwa lakini kama haikuzingatia kanuni hii ya kuwajibika basi inaweza pia kugharimu maisha yetu, mtoa habari mpokea habari na msambaza habari wanapaswa kuwa na uangalifu mkubwa sana namna wanavyopeleka habari


Hitimisho! 

Biola shaka kuna kitu umejifunza hapo sisi kama wakristo ndio chumvi ya ulimwengu napenda kila mmoja wetu aelimike na kukubalia kujifunza kuwa katika wakati huu wa utandawazi wakati ambapo kila mwanadamu anauwezo wa kutoa taarifa, kupokea taarifa na kusambaza taarifa ni Muhuhimu kwetu tukaacha kujisahau na kukumbuka kuwa ziko kanuni za neno la Mungu ambazo zinatuongoza jinsi na namna ya kuitumia mitandao hii ya kijamii, ninapohitimisha nataka kukukumbusha mambo kadhaa ya msingi yafuatayo:- 

a.       Tumia mitandao ya kijamii kuhudumu kwa neno la Mungu na kusambaza habri njema za Yesu

b.      Kumbuka kujitenga kwa muda na mitandao ya kijamii na kwenda kuomba, Yesu wakati mwingine aliacha makutano wengi sana na akajitenda kwenda kuomba.

c.       Kumbuka kuwakumbusha watu kutubu na kuishi maisha yanayompendeza Mungu, jitambue kuwa wewe ni mjenzi wa jamii na hivyo kabla ya kutoa habari tulizozipokea hakikisha kuwa zitakuwa zenye kujenga, kuonya kukemea kuelekeza na kukaribia kwa kusudi la mkujenga.

d.      Kumbuka kutia moyo mambo yaliyo mema kwa ku like na kuweka maoni yako na kukosoa vikali maovu na kuonyesha wazi jambo au kitu usichopendezwa nacho tumia neno la Mungu

e.      Tumia mitandao ya kijamii kudumisha uhusiano na kutafuta amani na watu wote na sio kuharibu, hakikisha nkuwa huondoki katika kusudi lako la matumizi ya mitandao, kama ni injili injili,

f.        Tumia mitandao ya kijamii kuonyesha semina, mikutano ya neno la Mungu na maswala muhimu ya kijamii onya karipia fundisha na jihadhari na matapeli, uwe makini na taarifa zako, maadui wanaweza kutumia taarifa zako kukudhuru wewe mwenyewe.

g.       Zingatia kanuni husika tulizojifunza na muombe Mungu ziwe kanuni muhimu katika maisha yako, asomaye na afahamu, ukiyajua hayo heri wewe ukiyatenda,

Na. Mchungaji Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye hekima
0718990796

Hakuna maoni: