Jumapili, 27 Desemba 2020

Familia takatifu !

Andiko la Msingi: Luka 2:41-49 “41. Basi, wazee wake huenda Yerusalemu kila mwaka, wakati wa sikukuu ya Pasaka. 42. Na alipopata umri wake miaka kumi na miwili, walipanda kama ilivyokuwa desturi ya sikukuu; 43. na walipokwisha kuzitimiza siku, wakati wa kurudi kwao, yule mtoto Yesu alibaki nyuma huko Yerusalemu, na wazee wake walikuwa hawana habari. 44. Nao wakadhani ya kuwa yumo katika msafara; wakaenenda mwendo wa kutwa, wakawa wakimtafuta katika jamaa zao na wenzao; 45. na walipomkosa, wakarejea Yerusalemu, huku wakimtafuta. 46. Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali. 47. Nao wote waliomsikia walistaajabia fahamu zake na majibu yake. 48. Na walipomwona walishangaa, na mama yake akamwambia, Mwanangu, mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni.49. Akawaambia, Kwani kunitafuta? Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu?”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa mara baada ya sikukuu ya krismas Kanisa huwa linasheherekea siku ya familia takatifu, Tayari Yesu Kristo amezaliwa na tayari imekuwa familia kamili, Yenye baba, Mama na mtoto, hii sasa ni familia ya watu wanaomcha Mungu, Familia ndio asili ya kila kitu, hakuwezi kuwa na taifa pasipo familia, hakuwezi kuwa na kabila pasipo familia, hatuwezi kuwa na viongozi wazuri wasiotoka katika familia, hatuwezi kuwa na watetea haki, waamuzi, wanamapinduzi,  manabii, na wachungaji ambao kwa namna moja ama nyingine hawajatokana na familia, hivyo familia ndio taasisi ya kwanza kabisa kabla ya kuweko kwa taasisi nyingine, Kwa msingi huo basi ili tuweze kuwa na kila jambo zuri, lazima jambo hilo lianzie katika familia, Leo tutachukua muda kujifunza namna familia ya Yesu, ambayo ilimjumuisha Mariamu, mama yake na Yusufu Baba yake mlezi na kijana mtoto Yesu. Hii ilikuwa ni familia ambayo imeleta Baraka kubwa sana duniani na hivyo kuna mambo ya kujifunza

1.       Hakuna familia isiyokuwa na Changamoto.

Ni muhimu kufahamu kuwa kila familia inapitia changamoto zake, Familia ya Yesu ilipitia changamoto za aina mbalimbali, Lakini kutokana na kumtanguliza Mungu, Mungu aliwatoa katika changamoto hizo:-

 

a.       Walipitia katika umasikini uliokithiri ;-

 

Kabla ya Yesu kuzaliwa ni wazi kabisa kuwa Yusufu na Mariamu hawakuwa na uchumi mzuri, walikuwa na ukata, usafiri waliotumia ulikuwa usafiri wa punda,  sadaka walizokuwa wakitoa Hekaluni ilikuwa ni njiwa wawili ambayo ni sadaka ya chini mno iliyotolewa na watu waliokuwa masikini, Hata hivyo umasikini huu haukuwa sababu ya manung’uniko kwao, wala sababu ya kuiba, au kutapeli, au kukopa na kutokurudisha, au kuomba omba, waliweza kuvumilia na kuendelea kumtegemea Mungu huku wakifanya kazi kwa bidii, Maisha yao yalibadilika baadaye baada ya sadaka ya Mamajusi waliotoa dhahabu, uvumba na manemane hivyo ndio viliweza kuibadili hali ya familia hii iliyomtegemea Mungu, Wakristo lazima tujifunze kuwa wavumilivu na kuusubiri wakati wa Mungu wa kutufanikisha bila kupitia short cut kwani Mungu ana majira na nyakati za kutubariki, Familia hii ilivumilia magumu na changamoto walizozipitia mpaka Mamajusi walipotoa zawadi zilizowatajirisha sana ona

Mathayo 2:10-12 “10. Nao walipoiona ile nyota, walifurahi furaha kubwa mno. 11. Wakaingia nyumbani, wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye, wakaanguka wakamsujudia; nao walipokwisha kufungua hazina zao, wakamtolea tunu; dhahabu na uvumba na manemane. 12. Nao wakiisha kuonywa na Mungu katika ndoto wasimrudie Herode, wakaenda zao kwao kwa njia nyingine.”


Tunaimba kwamba mjini mwaka mfalme Daudi palikuwa zizi nyoge... Yesu alizaliwa katika hali ya unyonge lakini maisha ya uvumilivu na subira ilibadilisha maisha ya familia yake na wakawa sasa wana uwezo wa kwenda Misri na kuishi huko kwa muda wakijikimu maisha yao, Lazima kila familia iwe na uvumilivu, usijilinganisha na watu wengine mtegemee Mungu, na Mungu atawabariki

 

b.      Walimsikiliza Mungu (Walitii mapenzi ya Mungu):-

 

 

Familia takatifu lazima iwe na uwezo wa kumsikiliza Mungu, Kumsikiliza Mungu ni kulisikiliza neno lake, kusikiliza watumishi wake na kuhudhuria ibada, Familia hii iliweza kudumu kwa sababu ilikuwa familia ya wazazi ambao wote walikuwa na uwezo wa kumsikiliza Mungu, kuliko kusikiliza maneno ya watu wa mtaani, Yusufu alipoona Mariamu ana Mimba biblia inasema aliamua kumuacha kwa siri! Unaona lakini mapema sana Malaika wa Bwana alimuonya Yusufu asimuache mariamu mkewe, ona katika

Mathayo 1:19-21 “19. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri. 20. Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. 21. Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao.

Unaona Kama Yusufu angekuwa ni mwenye kusikiliza maneno ya watu wa mitaani ndoa yake ingevunjika mapema na familia hii isingekuwa Baraka kwa dunia, Familia takatifu ni lazima iwe familia inayosikiliza maneno ya Mungu na kufuata uongozi wa Mungu, ni kwa kujua unyenyekevu na usikivu wa Yusufu, Mungu alisema na Yusufu tena kupitia malaika wake ili kukimbilia Misri na kuyalinda au kuyatunza maisha ya Yesu asiuawe na Herode ona 

Mathayo 2:13-14 “13. Na hao walipokwisha kwenda zao, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize. 14. Akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku, akaenda zake Misri;

Unaona ni maisha ya usikivu wa Yusufu ulioweza kumfanya Mariamu na mtoto Yesu kuwa salama kule misri na kuepuka kifo kutoka kwa Herode, Leo hii familia nyingi zinaharibika na watoto wanaenea mitaani wakipoteza muelekeo, au hata wakikosa kusoma kwa sababu ya wazazi waliokosa usikivu kwa Mungu na kwa wazazi, vijana wengi wanaishi vile wanavyojisikia na kujibu kile wanachojisikia na hata wazazi wamekosa kuwa mfano bora kwa kuigwa na watoto wao kwa sababu ya kutikumcha Mungu, Yusufu, na Mariam na Yesu walikuwa ni familia ya mfano katika kumcha Mungu.

 

c.       Walimuabudu Mungu;’-

 

Mstari wa msingi tuliousoma unasema “Basi, wazee wake huenda Yerusalemu kila mwaka,” Unajua maana yake nini hawakukosa ibada kuu katika hekalu lililokuwako Yerusalem, wazee wake maana yake wazazi wake kila mwaka walikwenda Hekaluni kusali na hawakuenda wenyewe walikwenda na vijana wao akiwemo Yesu, wao wenyewe walimuabudu Mungu lakini waliwafundisha watoto wao kumuabudu Mungu na kumpenda jambo hili lilijenga uhusiano mkubwa wa Yesu na Mungu baba wa Mbinguni, kiasi ambacho licha ya Yesu kuwaheshimu wazazi wake alimuona Mungu baba wa Mbinguni kuwa baba yake

Luka 2:48-49 “48. Na walipomwona walishangaa, na mama yake akamwambia, Mwanangu, mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni. 49. Akawaambia, Kwani kunitafuta? Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu?

tuwafunze watoto wetu wajue kuwa japo sisi ni wazazi wao lakini wanaye baba wa Mbinguni wamsikilize, wamtiii wampende wamuabudu familia takatifu lazima wajijenge tabia ya kuabudu. Kuimba, kuomba, kusoma neno la Mungu na kuhudhuria makusanyiko ya ibada na kujifunza na kudumisha uhusiano na Mungu ni jukumu la kila familia kuhimizana na kutiana moyo, kumuheshimu Mungu.

 

d.      Walipeleka watoto shule

 

Katika desturi za kiyahudi kijana aliyefikisha miaka 12 alikuwa tayari amefunzwa kuijua Torati na kufanya kazi za kujitegemea, wengine walijivunza uvuvi, wengine ukulima, wengine ujenzi na wengine kushoma mahema kama Paulo mtume, Yesu alikuwa na ujuzi wa torati na alikuwa amejifunza ujenzi “Carpenter” hii iliwajengea watoto uwezo wa kujiamini na kukabiliana na changamoto mbalimbali za maisha Hivyo Yesu alijengewa kupenda kujifunza na alikuwa msikivu kwa walimu wake na alikuwa mdadisi aliuliza maswali ona

“Luka 2:45-47 45. na walipomkosa, wakarejea Yerusalemu, huku wakimtafuta. 46. Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali. 47. Nao wote waliomsikia walistaajabia fahamu zake na majibu yake.”

Familia takatifu na iliyo njema inapaswa kuhakikisha kuwa watoto wao wanapata Elimu nzuri, na wanakuwa na uwezo wa kujitegemea wanaweza kufanya kazi mbalimbali, na wanakuwa na ujuzi wa maadili na sheria za ukoo na familia zao, leo hii tunaona kuna mmomonyoko mkubwa wa uadilifu lakini ni kwa sababu tatizo kubwa limeanzia katika ngazi ya familia, wazazi wanapaswa kuwa kitu kimoja na kuhakikisha kuwa wote kwa pamoja wanawajengea watoto uwezo wa kijitegemea ili watoto hao wasigeuke kuwa mzigo kwetu endapo hatutawaandaa vema Yesu alijengewa uwezo mkubwa sana na hatimaye akawa Mwalimu mwema alikuwa na wanafunzi 12 maalumu na wanafunzi wengine wengi, aliuitwa RABBI yaani Mwalimu, uwezo wake mkubwa wa kufundisha ulitokana na uwezo wake mkubwa wa kujifunza, kawaulize walimu hakuna Mwalimu mzuri ambaye sio mwanafunzi mzuri, Lazima tuwajengee uwezo wa kielimu watoto wetu

 

e.      Waliwalea watoto wao katika uadilifu

 

Tunasoma hivi katika Luka 2:52 “Naye Yesu akazidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.

Swali jepesi la kujiuliza je watoto wetu leo na familia zetu leo zinampendeza Mungu na wanadamu? Tunaambiwa Yesu alizidi kukua akiwa na hekima lakini vilevile akimpendeza Mungu na wanadamu, Je tunampendeza Mungu na wanadamu, hii haiwezi kutokea kama hatutakuwa chuo cha maadili kwa vijana wetu, ni muhimu kuwafunza watoto wetu, na kuwalea katika uadilifu, tikifanya hivi tutakuwa na watoto wenye muelekeo thabiti katika taifa letu, leo hii tujnashuhudia mmomonyoko mkubwa waa maadili lakini sababu kubwa ni kuanzia ngazi ya familia kutokujali uadilifu na mwenendo mwema kwa watoto wetu.

 

f.        Walijali Ndugu jamaa na kule walikozaliwa/kulelewa

 

“Human being is a social being” Mungu hakutuuumba tuishi kama kisiwa, aluiposema si vema mtu huyu awe peke yake alimaanisha wanadamu tunahitajiana wakati mwingine ili uweze kujengeka unapaswa kuwa na muda wa kusikiliza wengine na hapo ndipo tunapoweza kujengwa na kukua au kutiana moyo, Mariam alipopata ujauzito wa ajabu malaika alimueleza kuwa jamaa yako  Elizabeth pia ana mimba ya mtoto wa kiume, kusudi kubwa ilikuwa ili Mariamu aweze kutiwa moyo kustahimili kile kilichomtokea hivyo Mariamu alimtembela Elizabeth ona

Luka 1:36-44 “36. Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; 37. kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu. 38. Mariamu akasema, Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema. Kisha malaika akaondoka akaenda zake. 39. Basi, Mariamu akaondoka siku hizo, akaenda hata nchi ya milimani kwa haraka mpaka mji mmoja wa Yuda, 40. akaingia nyumbani kwa Zakaria akamwamkia Elisabeti. 41. Ikawa Elisabeti aliposikia kule kuamkia kwake Mariamu, kitoto kichanga kikaruka ndani ya tumbo lake; Elisabeti akajazwa Roho Mtakatifu; 42. akapaza sauti kwa nguvu akasema, Umebarikiwa wewe katika wanawake, naye mzao wa tumbo lako amebarikiwa. 43. Limenitokeaje neno hili, hata mama wa Bwana wangu anijilie mimi? 44. Maana sauti ya kuamkia kwako ilipoingia masikioni mwangu, kitoto kichanga kikaruka kwa shangwe ndani ya tumbo langu.


Unaoma Mariamu anamtembelea Elizabeth anajifunza mambo mablimbali kutoka kwa mwanamke mzee mwenye uzoefu wa kutembea na Mungu, na hivyo anajifunza mambo mbalimbali Mariamu kutoka kwa watu wa rika linguine je leo hii wanawake watu wazima huwafunza wanawake vijana ? je watu hutembeleana nyakati  za leo? Je watu hutembelea kule walikozaliwa au kulelelwa familia zenye upendo hutembeleana Yesu pia alitembelea Nazareth kule alikolelewa na kuwafundisha mambo makubwa ya Mungu ona

Luka 4:16-21 “16. Akaenda Nazareti, hapo alipolelewa; na siku ya sabato akaingia katika sinagogi kama ilivyokuwa desturi yake, akasimama ili asome.17. Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, 18. Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, 19. Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa. 20. Akakifunga chuo, akamrudishia mtumishi, akaketi; na watu wote waliokuwamo katika sinagogi wakamkazia macho. 21. Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu.


Yesu alienda Nazareth kule alikolelewa, Ni muhimu kukumbuka na nyumbani, watu wengi sana wanapofanikiwa hawakumbuki nyumbani, watu wengi wa Tanga waliosoma zamani walitawanyika huko na huko na kusaidia watu wengine na kuwaelimisha lakini waliisahau Tanga,  wabunge wengi  hukumbuka nyumbani wajkati wa kupiga kura, Yesu pamoja na umaarufu wake wote na alikuwa Mungu hakuweza kusahau kule alikolelewa, tunawashangaa wachaga tu wanapoenda nyumbani msimu wa sikukuu, hebu na sisi tujifunze na kukumbuka kuenda kule tulikolelelwa na kukulia na kuwa Baraka kwao pia

Tuwe tayari kujitoa kwa wengine

Kusudi kubwa la Yesu kuzaliwa ni ili awaokoe watu wake na dhambi zao Yusufu alielezwa hili mapema ona

Mathayo 1:20-21 “20. Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. 21. Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao.”


Yusufu alielezwa mapema kuwa Yesu ni mwokozi, familia ina wajibu wa kulea vijana na kukuza viongozi ambao watakuwa faida si kwaajili yao tu bali kwaajili ya ulimwengu mzima Mariamu pia alijulishwa kuwa mtoto wake sio wake pekee bali amewekwa kwaajili ya wenginona

Luka 2:34-35 “34. Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. 35. Nawe mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi.

  
Ilikuwa wazi kuwa Mungu aliwaamini Mariamu na Yusufu kuwa walezi wa kiongozi mkubwa ambaye atakuwa Baraka kubwa kwa ulimwengu ni mwokozi wa ulimwengu, kama familia hatuna budi kuwatunza wanafamilia wote na kuwasaidia kutimiza ndoto zao ili makusudi yote ya Mungu yapate kutimizwa ndani mwao, nani ajuaye kuwa mtoto uliyembeba ni Raisi ajaye, ni Mwalimu ajayem, ni daktari ajaye, Mungu ana makusudi na kila aliyezaliwa na hakunanayezaliwa kwa bahati mbaya hivyo tuendelee kuwa na ustawi katima familia zetu ili Mungu ajiinulie watumishi wake kutioka katika familia zetu watakaokuwa Baraka kwa wengine

Yohana 13:17 “Mkiyajua hayo heri ninyi mkiyatenda!”

Bwana Mungu awabariki na kuwafadhili tunapoadhimisha siku ya familia takatifu katika jina la Baba na Mwana na Roho Mtakatifu amina

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!

0718990796

Hakuna maoni: