Jumatatu, 29 Mei 2023

Jipe moyo; inuka anakuita!


Marko 10:46-50 “Wakafika Yeriko; hata alipokuwa akishika njia kutoka Yeriko, pamoja na wanafunzi wake, na mkutano mkubwa, mwana wa Timayo, Bartimayo, yule mwombaji kipofu, alikuwa ameketi kando ya njia. Naye aliposikia ya kwamba ni Yesu Mnazareti, alianza kupaza sauti yake, na kusema, Mwana wa Daudi, Yesu, unirehemu. Na wengi wakamkemea ili anyamaze, lakini alizidi kupaza sauti, Mwana wa Daudi, unirehemu. Yesu akasimama akasema, Mwiteni. Wakamwita yule kipofu, wakamwambia, Jipe moyo; inuka, anakuita.  Akatupa vazi lake, akaruka, akamwendea Yesu.”


Utangulizi:

Moja ya stori zenye mvuto mkubwa sana katika maandiko ya neno la Mungu (Biblia) ni pamoja na stori ya kuponywa kwa kipofu Batimayo, Katika stori hii kuna mambo mazuri sana ya msingi yakujifunza lakini kwa bahati mbaya wakati mwingine tunakosa kuyagundua mambo hayo, kuna kitu kikubwa na cha ziada cha kujifunza katika mwenendo mzima wa stori hii ukiacha uponyaji wenyewe! Lakini kuna mambo ya msingi ambayo Kristo anatufundisha kupitia tukio hili, kipofu mwenyewe na jamii ya watu waliokuwa wana mzunguka na kisha tutaweza kujiona sisi wenyewe tunapokuwa katika uhitaji, tabia ya uungu katika kushughulika na changamoto zetu na tabia ya watu wakati wa changamoto zetu, Bwana ampe neema kila mmoja wetu kuwa na macho ya rohoni tunapojifunza somo hili katika jina la Yesu Kristo amen!, tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-

*      Dhana potofu wakati wa changamoto!

*      Tabia ya Mungu wakati wa changamoto

*      Mambo ya kujifunza kutoka kwa Batimayo 

Dhana potofu wakati wa changamoto!

Stori ya uponyaji wa kipofu Batrimayo inaenda pamoja na ukweli kuwa mwandishi alikusudia chini ya uwongozi wa Roho Mtakatifu kutufungua macho, ili hatimaye tuweze kuona moja ya changamoto iliyojengeka katika jamii ya watu wanayoyajua maandiko kama ilivyokuwa kwa wayahudi dhana hii iko hata leo, hii ni ile dhana ya kufikiri kuwa kila changamoto inayomtokea mtu katika maisha yake imesababishwa na dhambi, katika kipindi cha muujiza huu kulikuwa na dhana potofu miongoni mwa wayahudi ya kuwa watu wenye changamoto kama hii ya kipofu Batrimayo labda huenda imesababishwa na dhambi, aidha ya mtu mwenyewe au wazazi wake kwa hiyo analipia, hivyo mtu kama Batrimayo licha ya kuwa na tatizo la upofu lakini vilevile alikuwa amekataliwa na jamii kwa kufikiri ya kuwa anastahili kubaki katika hali kama hiyo kwa vile yeye au wazazi wake wanalipia hali anayoipitia ona

Yohana 9:1-3 “Hata alipokuwa akipita alimwona mtu, kipofu tangu kuzaliwa. Wanafunzi wake wakamwuliza wakisema, Rabi, ni yupi aliyetenda dhambi, mtu huyu au wazazi wake, hata azaliwe kipofu? Yesu akajibu, Huyu hakutenda dhambi, wala wazazi wake; bali kazi za Mungu zidhihirishwe ndani yake.”

Unaona? Ni ukweli ulio wazi kitheolojia kuwa dhambi ina changamoto zake inazoweza kusababisha majanga katika maisha yetu, lakini ni muhimu kuweka uwiano kuwa sio kila changamoto inaweza kuwa na uhusiano na dhambi, hapo wanafunzi pamoja na jamii walihesabu watu waliokuwa vipofu walikuwa na laana Fulani au malipo Fulani kutokana na dhambi walizozifanya, sio hivyo tu hata kulipotokea majanga ya asili yaliyosababisha tatizo katika jamii Fulani haraka sana ilifikiriwa kuwa huenda ni kwaajili ya dhambi nyingi huku wale walio salama wakidhani wako sawa na Mungu ona mfano

Luka 13:1-5 “Na wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichanganya damu yao na dhabihu zao.  Akawajibu akawaambia, Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo.  Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo.”

Unaweza kuona! majanga yanapotokea na kuwapata watu haimaanishi kuwa wale waliopatwa na majanga ni waovu kuliko wale waliokuwa salama dhana hii Yesu alikuwa akiifundisha na kuwaelekeza watu kuwa wanapaswa kumzalia bwana matunda na kuacha kufikiri kuwa changamoto wanazozipitia watu wengine zimetokana na dhambi, Yesu alionyesha kuwa hitaji la toba ni hitaji la kila mmoja na hitaji la kuzaa matunda ni la kila mmoja na hivyo majanga yanaweza yasiwe na uhusiano wa moja kwa moja na hali ya dhambi au kiroho cha mtu husika

Ni katika dhana hiyo hiyo tunaona kuna jambo ambalo lilijitokeza hali kadhalika wakati wa uponyaji wa kipofu Batimayo wakati kipofu huyu alipokuwa anamuita Yesu na ikaonekana kana kwamba Yesu anapita au kama hajali makutano waliokuwa wakifikiri vibaya waliona kuwa Kipofu huyo anatakiwa kupambana na hali yake na kuwa hapaswi kumsumbua Yesu wala Yesu hajali hali yake, Maandiko yanatutaarifu kuwa wakati Yesu anapita na kipofu huyu anapaaza sauti yake kumuita makutano walimweleza wazi kwa kumkemea anyamaze ni kama walikuwa wanamwambia acha usumbufu wako, Yesu hawezi kushughulika na watu kama wewe pambana na hali yako ona

Marko 10:46-48a “Wakafika Yeriko; hata alipokuwa akishika njia kutoka Yeriko, pamoja na wanafunzi wake, na mkutano mkubwa, mwana wa Timayo, Bartimayo, yule mwombaji kipofu, alikuwa ameketi kando ya njia. Naye aliposikia ya kwamba ni Yesu Mnazareti, alianza kupaza sauti yake, na kusema, Mwana wa Daudi, Yesu, unirehemu. Na wengi wakamkemea ili anyamaze,…..

Unaona kutokana na dhana ya kufikiri kuwa watu wenye ulemavu na changamoto mbalimbali na hata walio na magonjwa ni kama wanaadhibiwa na Mungu kwaajili ya dhambi zao au za wazazi wao au babu zao na kadhalika kwa hiyo maandiko yanaonyesha kuwa wengi wakamkemea acha kelele zako, acha ujinga acha usumbufu hana mpango na wewe pambana na hali yako katika lugha ya kiingereza tunaweza kusema hivi “A BLIND BEGGAR WAS HUSHED BY THE CROWD” ni kama sio kunyamazishwa tu bali kunyamazishwa kwa ukali,kunyamazishwa kwa kunyanyaswa, ni ili unyamaze, ukae kimya usisumbue, uache fujo tulia, shiiiiii, funga domo lako, nyamaza! Katika hali moja ama nyingine katika maisha yetu inawezekana tumewahi kunyamazishwa katika namna ya ukali kama ilivyotokea kwa kipofu Batrimayo, unaonywa kuto kudai chochote kunyamaza na kulazimika kupitia au kipitishwa katika hali ambayo watu wanataka, ni katika hali kama hiyo Batimayo alikuwa anakutana na kipingamizi kikubwa cha kubakizwa katika hali ileile na jamii, hawataki asonge mbele wanaona kama wale walio na miguu na macho wao ndio wanaostahili, kuendelea mbele na Yesu na sio watu hovyo na wenye kutupwa na kudharaulika kama kipofu Batrimayo!  Jambo moja kubwa la msingi ni kuwa yeye aliendelea kupaza Sauti akimuita Yesu! Akihitaji rehema zake !

Tabia ya Mungu wakati wa changamoto!

Ni muhimu kufahamu kuwa katika mchakato mzima wa uponyaji wa Batimayo Yesu alionekana kama anapita na ni kutokana na hali hii nadhani hata makutano waliomkemea Batimayo walikuwa wanadhani kuwa hata Yesu hakuwa anajali hali aliyokuwa anaipitia kipofu, Yesu ni mwana wa Mungu kufikiri ya kuwa Yesu hangemjali Batimayo ni kufikiri vibaya, kufikiri kuwa Mungu hatujali ni fikra mbaya, ambayo iko kinyume na ukweli kuhusu wema wa Mungu, wakati tunapoliitia jina lake na kuhitaji rehema zake na kuona kama amekawia kuitikia na kudhani kuwa hajishughulishi tena na mambo yetu ni dhana isiyofaa kitu kabisa; Mungu ni mwema wakati wote maandiko yanatuthibitishia wazi ya kuwa anajishughulisha sana na mambo yetu ona

1Petro 5:6-7 “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.”

Tofauti na mawazo ya Mwanadamu Yesu alikuwa anapita huku anamwazia mema kipofu Batrimayo, kimsingi hata kupita njia ile ilikuwa ni maalumu sana kwa Batimayo wala sio kwaajili ya umati uliokuwa unamfuata, Ni huyu kipofu ndiye aliyekuwa amelengwa na Yesu siku ile kwanini unawezaje kujua ? Yesu alisimama na alisimama maalumu kwaajili ya huyu mtu mtu dhaifu, aliyekataliwa katika jamii na kudharauliwa masikini asiye na msaada, Yesu alimjua alijua historia yake alifahamu mahitaji yake kamwe hangeweza kumpita, wale watu kimsingi ndio waliokuwa vipofu hawakuweza kujua imani ya Batrimayo wala hawakuweza kujua namna Mungu anavyoshughulika na mahitaji ya watu wake.  Mungu ana njia zake na namna yake jambo jema hapa ni kuwa watu hawakumlaumu Yesu kama wakati alipokuwa amelala katika boti ambapo wanafunzi walimlaumu kuwa Mwalimu si kitu kwako kuwa tunaangamia? Na ni tofauti kiasi na alivyokuwa akishughulika na mwanamke aliyekuwa akitoka na damu kwa kumgusa katika upindo, wanafunzi walimshanga kuwa tunazungukwa na umati mkubwa je si rahisi kwako kuguswa rabbi? Hapa Yesu alisimama na kuamuru kuwa mwiteni! kuna kitu kimejificha hapa kwenye neno YESU AKASIMAMA katika lugha ya kiyunani kusimama kwa Yesu nenola kiyunani linalotumika ni  HISTEMI  ambalo ni neno lililovutwaa kutoka kwenye neno la kiyunani STAO  katika lugha nzuri ya kuelewa kusimama kwa Yesu hapa neno la kiingereza linaloweza kutumika hapa ni ESTABLISH STAND STILL, kwa hiyo neno STAO ni sawa na neno STAND na neno HISTEMI ndio ESTABLISH STAND STILL  kwa hiyo kwa Kiswahili kizuri ni kuwa YESU AKATAFUTA MAHALI PAZURI PANAPOFAA KUSIMAMA, hivyo kimsingi sio kuwa Yesu alikuwa amekusudia kumpita Batimayo lakini Yesu alikuwa anatafuta mazingira mazuri ya kusimama na kipofu ili aweze kumuhudumia vizuri, Haleluya!  Mwandishi maarufu wa karne za mwanzoni mwa kanisa Mtakatifu Jerome anaeleza kuwa Mazingira ya Yeriko ni yenye miamba na mawe ambayo yangeweza kusababisha kujikwaa au kuanguka  hivyo ni kweli kuwa Yesu alikuwa anaangalia mazingira mazuri ya kusimama na mtu asiyeona ili waweze kuzungumza vizuri  na kwa kufanya hivi alikuwa akiitimiza sharia ya Musa katika

Walawi 19:14 “Usimlaani kiziwi, wala usitie kwazo mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako; Mimi ndimi BWANA.”

Unaona wakati Mungu anaandaa mazingira mazuri ya kushughulika na mtu huyu duni mwenye imani na utambuzi mkubwa kuwa Yesu ni mwana wa Daudi, jambo ambalo linaonyesha wazi kuwa Batimayo alikuwa ameamini kuwa Yesu ni Masihi, Unadhani Yesu angemuachaje?  Yanenaje maandiko? na kila amwaminiye hatatahayarika!  katika wakati huo tayari watu wameshapata dhambi kwa kufikiri kuwa (Yesu) Mungu alikuwa hamjali na wala hakuwa na mpango naye, au kusaidia kumnyamazisha Batrimayo.  Mungu alikuwa anaandaa mazingira, acha kuimba usinipite mwokozi, yeye huwa hampiti Mtu mwenye uhitaji na anayemuamini na watu wanyamaze kimya wakati Bwana anashughulika na watu wake maana unaweza kujikuta unatengeneza dhambi wakati Kristo anaandaa mazingira mazuri ya kusema na mtu wake, kwa muda sahihi na mahali sahihi ili akutane na mahitaji yake, watu wale wale waliokuwa wakimkemea na kumwambia nyamaza ni hao hao waliomwambia changamka jipe moyo inuka anakuita, Kwa kawaida kuna watu wengi sana vipofu walioponywa na Yesu lakini hawakutajwa kwa majina yao Huyu alikuwa anatupa somo muhimu sana ndio maana anatajwa kwa jina lake alimuamini Yesu kuwa ni Masihi, Yesu alitengeneza mazingira ya kuzungumza na mtu huyu muhimu kwake kuliko wote wakati wao walikuwa wakimuona hana maana hana faida, Yesu aliwafunga mdomo nao wakamwambia jipe moyo inuka anakuita haleluya ! Yesu ni Mungu mwenye moyo wa ajabu na huruma sana! Anajali, alimjali.

Mambo ya kujifunza kutoka kwa Batimayo

Kuna mambo mengi ya kujifunza kutoka katika muujiza huu yako mengi, habari hii inatufunza mengi kwanza wako marafiki au watu ambao sio wazuri kwetu na wasiotutakia mema wanataka tusifanikiwe na tubaki katika hali ile ile tuliyo nayo, watatusaidia kutoa majibu ambayo wala sio majibu ya Mungu,  wanatuzuia kwenda kwenye mwelekeo sahihi wakijua wazi kabisa kuwa ndio mwelekeo wa mafanikio yetu, je unadhani watu wale walikuwa hawajui kuwa Yesu anaponya vipofu? Unadhani walikuwa hawajui kuwa Yesu ameponya vipofu wengi sana? Na je unadhani walikuwa hawaoni ya kuwa Batrimayo ni Kipofu na unadhani walikuwa hawajui kuwa siku ile ilikuwa siku nzuri sana kwa Batrimayo kuponywa kwa vile Yesu alikuwa Yeriko siku ile?  Kumbuka watu ni wale wale ambao tunapolia wanatuambia nyamaza,  ashukuriwe Mungu na aendelee kuwatunza kwani Mungu atageuza mambo hao hao waliokuwa wakikuambia nyamaza ndio watakaokuja kusema jipe moyo inuka anakuita ! Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa Batrimayo!

Usikubali mtu yeyote akunyamazishe au akuhesabu kuwa wewe ni wa kutupwa wakati Yesu Kristo amekuja kwaajili yako. Batrimayo ashukuriwe Mungu hakuwajali watu wanamwambia nini yeye aliendelea kumtazama Yesu tu na kulilia Rehema kutoka kwa Masihi mwana wa Mungu!

Uhusiano wako na Yesu ni wa tofauti haufannani na wa mwingine wengine wanafikiria kuwa hakujali! wewe endelea kumtazama kama mwenye kujali na utangundua kuwa kumbe yuko kwaajili yako

Linapokuja swala la wewe na maisha yako na Mungu usiangalie umati unasemaje, Mungu haabudiwi kwa mkumbo uwe na msimamo wako wa kipekee kuhusu Mungu, Batrimayo kwake Yesu ni mwana wa Daudi nani pekee mwenye kutoa rehema

Watumishi wa Mungu ni lazima waandae mazingira mazuri kwaajili ya huduma za uponyaji, nguo za kuwafunika wanaoangushwa na mapepo, wahudumu watakaosaidia kuwahifadhi wanaodondoshwa, mazingira yatakayosaidia kutunza usafi wao na kadhalika Yesu hakutaka Batrimayo ajikwae kwenye mawe alitafuta mazingira mazuri.

Mungu habadiliki, yeye ni yule yule jana, leo na hata milele, yeye ndiye mwenye kipimo cha wema wetu, matendo yetu yawe sawa na kile anachotuelekeza yeye na sio kwenye dhana za watu na yale wanayoyafikiri, wakatim Batrimayo akiwa katika changamoto hii ni ukweli ulio wazi kuwa walioelewana Lugha pale alikuwa Yesu mwenyewe na Batrimayo wengine walitoka kappa, ninapopita katika mapito ninayoyapitia na hali yoyote ile ninayoipitia anayeweza kunielewa vizuri mi Mungu na mimi ninayeipitia ile hali ninyi wengine kaa kimya msininyamazishe ninapomtafuta Bwana wangu, msininyamazishe ninapopiga kelele wala Mungu wangu hanipiti anaaandaa mazingira salama na ya utulivu nipige naye stori nimueleze ninayo yahitaji ana rehema hataniacha yatima hali hii baadaye utakuja kugundua kuwa kumbe mimi na Yesu tunaelewana vizuri sana kuliko umati huu.  Yawezekana unapitia katika changamoto kadhaa wa kadha na unadhani Yesu amekupita au hakujali na watu wanapata nafasi ya kukudhihaki wanatamani ubakie katika hali hiyo hiyo, hawataki ukutane na Yesu akusaidie nataka nikuambie wewe endelea kupiga kelele na kumwambia mwana wa Daudi unirehemu, ususeme usinipite mwokozi kwani yeye hapiti mtu anayemwangalia na kumlilia Rehema zake naye ataandaa mazingira na watu wale wale wanaosema nyamaza watapiga kelele Jipe moyo inuka anakuita! haleluyaa

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!



Hakuna maoni: