Ijumaa, 9 Mei 2025

Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!


Kumbukumbu 33:24-27 “Na Asheri akamnena, Na abarikiwe Asheri kwa watoto; Na akubaliwe katika nduguze, Na achovye mguu wake katika mafuta. Makomeo yako yatakuwa ya chuma na shaba; Na kadiri ya siku zako ndivyo zitakavyokuwa nguvu zako. Hapana aliyefanana na Mungu, Ee Yeshuruni, Ajaye amepanda juu ya mbingu ili akusaidie. Na juu ya mawingu katika utukufu wake. Mungu wa milele ndiye makazi yako, Na mikono ya milele i chini yako. Na mbele yako amemsukumia mbali adui; Akasema, Angamiza.”




Utangulizi:

Moja ya tahadhari inayotolewa kwa wahubiri wa neno la Mungu ni pamoja na kuhakikisha kuwa tunalitumia neno la Mungu kwa halali, Neno la Mungu linatahadharisha kuwa walimu wa neno la Mungu watapata hukumu iliyokubwa zaidi, kwa sababu hiyo ni muhimu kwa kila mtafasiri wa neno la Mungu kulitafasiri kwa halali neno la kweli ili watu wa Mungu wasipotoshwe na kujikuta wakipotezwa kwa kutokuwa na maarifa ya kuifahamu kweli ya neno la Mungu, na kanuni zake za kulitafasiri! Neno la Mungu likitafasiriwa kwa usahihi linaleta mwelekeo sahihi kwa watu wa Mungu. Tafasiri sahihi na njema kwa neno la Mungu huwajengea watu makuzi sahihi ya kiroho, kuikulia Imani sahihi na kujenga uhusiano imara na Mungu na kujiepusha na matumizi mabaya ya maandiko yatakayopelekea kuzuka kwa Imani potofu au Imani za kizushi na kuwafanya wadamu wasitimize kusudi sahihi la Mungu katika maisha yao!

2Timotheo 2:14-15 “Uwakumbushe mambo hayo, ukiwaonya machoni pa Mungu, wasiwe na mashindano ya maneno, ambayo hayana faida, bali huwaharibu wasikiao. Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.”         

Yakobo 3:1-2 “Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa mtapata hukumu kubwa zaidi. Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”

Kwa msingi huo basi leo nataka tuchukue muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu tafasiri ya Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta! Ili kwamba kila mwanafunzi wa Yesu Kristo aweze kuwa na ufahamu wa kutosha  na uliosahihi kuhusu fundisho linaloendelea mitaani ambapo kumekuwako na watumishi wa Mungu wanaowakanyagisha watu mafuta wakifikiri kuwa kwa kufanya hivyo wanaweza kusababisha mabadiliko ya maisha ya watu kiroho, kiuchumi na kimwili jambo ambalo sio sahihi,  na wakristo wengi sana wasomi kwa wasio wasomi lakini wasio na ujuzi kuhusu neno la Mungu wameshawishika kukanyaga mafuta halisi kwa kutumia tafasiri isiyo halisi ya neno la Mungu, tutajifunza somo hili Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta! Kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuafuatayo:-

 

·         Umuhimu wa kuzingatia kanuni za kutafasiri maandiko.

·         Tafasiri halisi ya Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!

·         Jinsi ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!

 

Umuhimu wa kuzingatia kanuni za kutafasiri maandiko.

Moja ya changamoto kubwa inayolikumba kanisa la Mungu katika nyakati za leo ni pamoja na kuweko kwa kundi kubwa la mashambulizi ya mafundisho ya uongo ambayo yamekuwa mwiba na usumbufu mkubwa katika kanisa la Mungu kwa miaka mingi, unaweza ukalichukulia swala hili kuwa ni swala la kawaida, lakini ni ukweli usioweza kupingika kuwa Mungu hafurahii watu wanaojitafasiria neno lake kama wapendavyo, Biblia ni kitabu cha Heshima kubwa sana ni neno la Mungu na kwa sababu hiyo haipendezi hata kidogo kila mtu tu akijitafasiria maandiko kama apendavyo kamwe huo sio mpango wa Mungu, Roho Mtakatifu ndiye mwandishi mkuu wa Biblia na bila shaka hangeweza kufurahia watu wajitafasirie neno lake kama watakavyo tu kwa mapenzi yao wenyewe!

2Petro 1:19-21 “Nasi tuna lile neno la unabii lililo imara zaidi, ambalo, mkiliangalia, kama taa ing'aayo mahali penye giza, mwafanya vyema, mpaka kutakapopambazuka, na nyota ya asubuhi kuzuka mioyoni mwenu. Mkijua neno hili kwanza, ya kwamba hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu. Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu.”

Mungu anachukizwa sana pale watu wanaposema kile ambacho yeye hajawahi kukisema, nakumbuka niliwahi kuwa na Muhasibu ambaye alikuwa akiandika jina langu katika namna ambayo mimi mwenyewe sikuwahi kuitwa hivyo, Mimi naitwa INNOCENT SAMUEL KAMOTE Lakini muhasibu wangu yeye alikuwa akiandika jina langu INNOCENT SAMWELI KAMMTTE  nililalamika mara kadhaa kuwa Jina langu unavyoliandika sivyo linavyopaswa kuwa lakini hata hivyo hakujali na aliendelea kuliandika jina langu katika namna hiyo hiyo aliyokuwa anataka yeye, mimi sio mwepesi wa hasira lakini hata hivyo nilianza kumtafasiri vibaya muhasibu huyu aliyekazania kuliandika jina langu katika namna anayoitaka yeye hata pamoja na kumuonyesha vitambulisho vyangu vilivyo na jina sahihi,yeye aliendelea kuliandika jina langu katika namna hiyo hiyo aliyoikubali yeye na hakukubali masahihisho, kimsingi nilianza kumchukia na kumuona kama mtu mwenye nia ovu kwa maslahi yangu kwani nafahamu kuwa dosari katika jina la mtu hasa ikiachwa hivyo katika documents muhimu linaweza kuwa na athari kubwa sana baadaye utakapohitajika kuthibitisha uhalisi wa mtu anayetajwa hapo na ukweli kuhusu jina lako, sio hivyo tu nilianza kuingia shaka kuhusu elimu yake na aidha akili zake, kwa hiyo sikuwa namfurahia tena, na alipoteza umuhimu wake kwangu, katika maumivu kama hayo ni ukweli ulio wazi kuwa Mungu anachukizwa sana watu wanapomnukuu vibaya tofauti na maana aliyokuwa anaikusudia kwenye neno lake, Mungu anataka neno lake lisemwe kwa uaminifu na kama mtu hataki aache, Mungu hataki kusingiziwa kwamba amesema kitu ambacho yeye hakukisema, iwe ni kwa misingi ya ndoto wala mafunuo anataka atendewe haki katika tafasiri halali kwa neno lake ili watu wake wasipotoshwe ona  

Yeremia 23:25-32.“Nimesikia waliyoyasema manabii wanaotabiri uongo kwa jina langu, wakisema, Nimeota ndoto; nimeota ndoto. Je! Mambo hayo yatakuwa katika mioyo ya manabii wanaotabiri uongo hata lini, manabii hao wenye udanganyifu katika mioyo yao wenyewe? Wanaodhania ya kuwa watawasahaulisha watu wangu jina langu kwa ndoto zao, wanazomhadithia kila mtu jirani yake, kama vile baba zao walivyolisahau jina langu, kwa ajili ya Baali. Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema Bwana. Je! Neno langu si kama moto? Asema Bwana; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande? Basi kwa sababu hiyo mimi ni juu ya manabii hao, asema Bwana, wanaompokonya kila mtu jirani yake maneno yangu. Tazama, mimi ni juu ya manabii, asema Bwana, wanaotumia ndimi zao na kusema, Yeye asema, Tazama, mimi ni juu ya hao wanaotabiri ndoto za uongo, asema Bwana, na kuzisema, na kuwakosesha watu wangu kwa uongo wao, na kwa majivuno yao ya upuzi, lakini mimi sikuwatuma, wala sikuwapa amri; wala hawatawafaidia watu hawa hata kidogo, asema Bwana.”

Kwa msingi huo hatuwezi kulichezea neno la Mungu na kuruhusu litafasiriwe vyo vyote vile kama watu wanavyotaka, ziko kanuni zinazoongoza tafasiri halali kwa neno la Mungu, katika karne ya 20 wa NAZI wa Ujerumani waliona kuwa kuna uhalali wa kuwaangamiza wayahudi na kuwaua kwa sababu walitumia andiko la Mathayo 27:24-25 vibaya:-

Mathayo 27:24-25 “Basi Pilato alipoona ya kuwa hafai lo lote, bali ghasia inazidi tu, akatwaa maji, akanawa mikono yake mbele ya mkutano, akasema, Mimi sina hatia katika damu ya mtu huyu mwenye haki; yaangalieni haya ninyi wenyewe. Watu wote wakajibu wakasema, Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu.”

Tafasiri yoyote mbaya ya kimaandiko inaweza kuleta matokeo mabaya yasiyokusudiwa katika jamii wala yasiyo sawa na mapenzi ya Mungu, kama kila mwanadamu anapenda kunukuliwa vizuri basi Mungu anapenda kunukuliwa vizuri zaidi. Katika mtindo kama huo Madaktari wanafahamu athari zinazoweza kutokea endapo mtu atazidishiwa dozi au kupewa dozi chini ya kiwango wakati wa kumtibu mgonjwa kufanya hivyo kunaweza kusababisha madhara ya usugu wa dawa au kumuumiza mgonjwa, kadhalika neno la Mungu linaagizwa litafasiriwe kwa halali na sio kwa maslahi ya mtu na mafunuo yake au ndoto zake, sio kila mtu ana sifa ya kuwa mtafasiri wa maandiko, na sio kila mtu anaweza kuelewa neno la Mungu bila msaada wa mtu mwingine, na wako watu Mungu amewaweka ili waifanye kazi hiyo ya kuelewesha wengine neno la Mungu ili malengo yake yaweze kufikiwa. Kwa hiyo usipuguze wala kuongeza neno.

Matendo 8:29-35 “Roho akamwambia Filipo, Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo. Basi Filipo akaenda mbio, akamsikia anasoma chuo cha nabii Isaya; akanena, Je! Yamekuelea haya unayosoma? Akasema, Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza? Akamsihi Filipo apande na kuketi pamoja naye. Na fungu la Maandiko alilokuwa akilisoma ni hili, Aliongozwa kwenda machinjoni kama kondoo, Na kama vile mwana-kondoo alivyo kimya mbele yake amkataye manyoya, Vivyo hivyo yeye naye hafunui kinywa chake. Katika kujidhili kwake hukumu yake iliondolewa. Ni nani atakayeeleza kizazi chake? Kwa maana uzima wake umeondolewa katika nchi. Yule towashi akamjibu Filipo, akasema, Nakuomba, nabii huyu; asema maneno haya kwa habari ya nani; ni habari zake mwenyewe au za mtu mwingine? Filipo akafunua kinywa chake, naye, akianza kwa andiko lilo hilo, akamhubiri habari njema za Yesu.”

Kumbukumbu 4:1-2 “Na sasa, Ee Israeli, zisikilizeni amri na hukumu niwafundishazo, ili mzitende; mpate kuishi na kuingia na kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wa baba zenu. Msiliongeze neno niwaamurulo wala msilipunguze, mpate kuzishika amri za Bwana, Mungu wenu, niwaamuruzo.”  

Wakati mwingine ili mtu aelewe neno la Mungu anahitaji kuongozwa na wale ambao Mungu ameweka neema maaalumu ya kuwa wakufunzi wa neno la Mungu, kumbuka sisi ni wanafunzi wa Yesu na tunapaswa kujifunza kila iitwapo leo, tukiwa na moyo wa unyenyekevu na kuweka kiburi pembeni Mungu anaweza kutufundisha njia yake kwa usahihi zaidi.

Matendo 18:24-28 “Basi Myahudi mmoja, jina lake Apolo, mzalia wa Iskanderia, mtu wa elimu, akafika Efeso; naye alikuwa hodari katika maandiko. Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; na kwa kuwa roho yake ilikuwa ikimwaka, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi habari za Yesu; naye alijua ubatizo wa Yohana tu. Akaanza kunena kwa ujasiri katika sinagogi; hata Prisila na Akila walipomsikia wakamchukua kwao, wakamweleza njia ya Bwana kwa usahihi zaidi. Na alipotaka kuvuka bahari aende mpaka Akaya, ndugu wakamhimiza, wakawaandikia wale wanafunzi wamkaribishe, naye alipofika akawasaidia sana wale waliokwisha kuamini kwa neema ya Mungu. Kwa maana aliwashinda Wayahudi kabisa kabisa mbele ya watu wote, akionyesha kwa maneno ya maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo.”

Kwa hiyo wakristo tunakubaliana kuwa mtu anaweza kusoma neno la Mungu na asielewe bila uongozi, na pia mtu anaweza kuwa muhubiri lakini asihubiri kwa usahihi kama hajafundishwa vizuri na tunakubaliana kuwa maandiko yana kanuni zake katika kulitafasiri neno la Mungu ili yamkini liweze kutendewa haki katika tafasiri zake na kutumika kwa halali jambo ambalo linamfurahisha Mungu pia, tusiruhusu kitabu chetu kitakatifu kikatafasiriwa kama apendavyo mtu tu kwa mapenzi yake mwenyewe bali sawa na kanuni za kiungwana na kiungu sawasawa na mapenzi ya Mungu.  Kwa sababu hiyo ziko kanuni rahisi kumi zinazoongoza watu wa Mungu katika kutafasiri maandiko na ingawa hatutakuwa na muda wa kuzifafanua sana kwa undani lakini zinaweza kukupa mwanga wa namna ya kusimamia tafasiri njema na sahihi ya maandiko:-

1.       Lazima mtafasiri wa maandiko awe na Kanuni ya utii (The Principle of Obidience) – hii ni kanuni ya dhamiri njema, mtafasiri wa maandiko lazima ahakikishe kuwa ana moyo wenye dhamiri njema na kuwa mpango wake ni kumtii Mungu,  na kumtumikia kwa dhati, Kila mwanadamu mwenye utii kwa mapenzi ya Mungu na mwenye dhamiri njema Mungu humsaidia muelekeo wake wa moyo kuwa na uweza wa kuifahamu kweli na hata akikosea kwa sababu alikuwa na dhamiri safi rehema za Mungu huwa juu yake, kwa sababu Mungu akiiangalia nia yake anaona kuwa ni mtu mwenye mapenzi mema, Mungu hawezi kuwa radhi na mtu anayekusudia mabaya wakati wanapotaka kulitafasiri neno la Mungu, hata hivyo utii na dhamiri njema havitoshi peke yake vinaweza kutosha kwa Mungu anayechunguza mioyo lakini havitoshi kwetu kwa sababu tutajuaje kuwa ulikuwa na dhamiri njema iwapo fundisho lako limesababisha upotofu miongoni mwa jamii? Kwa hiyo kanuni ya utii inaweza kukuweka salama kwa Mungu tu lakini haikuachi salama kwetu sisi tuliosomea utaalamu wa kutafasiri maandiko haikuweki salama  kwa sababu neno la Mungu linasema Moyo una ugonjwa wa kufisha

 

Yeremia 17:9-10 “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua? Mimi, Bwana, nauchunguza moyo, navijaribu viuno, hata kumpa kila mtu kiasi cha njia zake, kiasi cha matunda ya matendo yake.”

 

Kwa hiyo wakristo wana haki ya kuyachunguza maandiko ili waone kama kile kinachohubiriwa na kusemwa ni kitu sahihi ama hapana! Hapo haijalishi anayehubiri ni nani na ana mamlaka gani lazima tumpime katika maandiko ili tuone yale anayotupa ndio mapenzi ya Mungu hasa, kinyume cha hapo tutakuwa tumekosa uungwana, watu wa Beroya hawakuwahi kujali kuwa Paulo ana mafunuo gani laiki waliyachunguza maandiko wajionee wenyewe kama mambio ndivyo yalivyo, usiamini katika moyo wa mtu.

 

Matendo 17:10-11 “Mara hao ndugu wakawapeleka Paulo na Sila usiku hata Beroya. Nao walipofika huko wakaingia katika sinagogi la Wayahudi. Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”                                

 

2.       Lazima mtafasiri wa neno la Mungu awe na uelewa kuhusu Kanuni ya uvuvio (The Principle of Inspiration) – hii ni kanuni inayomsaidia kujua kuwa kila andiko lenye pumzi ya Mungu linafaa kwa mafundisho, kwa hiyo tunaweza kuwafundisha watu neno la Mungu kwa njia nyepesi tu na kama tuna mapenzi mema tutawaelekeza watu wake katika mapenzi yake kwa kutumia neno la Mungu  kwa sababu lijna pumzi ya Mungu

 

2Timotheo 3:16-17 “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”

 

Kanuni hii haitoshi ingawa kuna ukweli kuwa kila andiko lenye pumzi ya Mungu linafaa kwa mafundisho, lakini maandiko yanahitaji ulinganifu wa kina na ndio maana shetani pia alipoona Yesu anatumia maandiko naye akayatumia lakini si kwa nia nzuri kwa hiyo uko ulinganifu maalumu unaohitajika katika kujua andiko fulani linatumikaje na kwa wakati gani

 

Mathayo 4:5-7 “Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mji mtakatifu, akamweka juu ya kinara cha hekalu,akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake; Na mikononi mwao watakuchukua; Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.Yesu akamwambia, Tena imeandikwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako.”

 

3.       Lazima mtafasiri wa Maandiko pia awe na uelewa kuhusu Historia  na mazingira ya andiko (Mukhtadha) (Principle of Historical Context) – hapa mtafasiri anapaswa kujifunza historia ya Mazingira yanayozunguka andiko husika mfano historia ya mji wa Korintho, lugha zao, wakati ambapo neno linaandikwa, tamaduni zao, jamii yao na kadhalika , sio hivyo tu lazima mtafasiri aelewe kitu kilichoandikwa au kusemwa pamoja na maneno yote na maana zake zinazozunguka andiko husika, mazingira yaliyopelekea kutamkwa kwa maneno hayo huo ndio muktadha,  tafasiri hii inakulazima uwe msomi ili uweze kujua lugha za wakati ule, tamaduni za wakati ule, jamii ya wakati ule, na jinsi tunavyoweza kulitumia andiko hilo kwa sasa, lazima uwe na kamusi au ujuzi wa lugha za asili kwaajili ya kupata maana sahihi iliyokusudiwa na mwandishi

 

4.       Lazima mtafasiri aweze pia kufanya uchunguzi wa kimaandiko yaani “ajue yaliyomo” lugha zilizotumika misamiati iliyotumika na maana ya maneno yanayotumika,- (Principle of content) mfano lugha hiyo ni ya namna gani, maneno yake yana maana gani anaweza pia kwenda kwenye lugha za asili kama kiebrania, kiaramu, kiyunani na kilatini ili kupata matumizi ya lugha halisi ya wakati ule na jinsi inavyoweza kutumika katika wakati wa sasa, lazima uchunguze kuwa lugha hiyo ni ya kimafumbo au ya kawaida inaweza kutafasiriwa kama kawaida au inaweza kuwa fumbo? Na madhara gani yanaweza kujitokeza, ni lazima uwe na ujuzi kuhusu kitabu unachotaka kukitafasiri kama ni cha kinabii, kimashairi, kihistoria, sheria, nyaraka, au injili na msemaji alikuwa akizungumza na jamii ya watu wa aina gani, kwa wakati gani, kwa tamaduni gani na inaweza kutuhusu vipi sisi katika nyakati za leo, Lazima uwe na ujuzi kuhusu stori nzima, somo zima, wazo zima, mpangilio mzima, mtiririko mzima na nia nzima ya mwandishi na yote yaliyomo kabla na baada ya andiko husika.    

 

5.       Lazima mtafasiri pia wakati mwingine achukue “lugha rahisi” tu iliyoko kama ilivyo bila kutumia utaalamu kutafasiri japo kwa kufanya hivyo mtafasiri anaweza anaweza kujikuta yuko katika wakati mgumu kwa sababu sio kila lugha iliyotumika inaweza kuwa na maana hizo, ziko lugha za mficho, za kimashairi, za kimafumbo, za kinabii, na kadhalika  (The principle of simplicity) ziko Lugha au maana katika biblia ambazo hazihitaji tafasiri yoyote kwa hiyo ukizichukulia kama zilivyo bila kutafasiri unakuwa salama, huitaji kuyafanya mambo kuwa magumu, lakini yako maandiko ambayo yanahitaji kutokuchukuliwa kirahisi au kama yalivyo mfano:-

 

-          Jicho lako likikukosesha ling’oe – Mathayo 18:8-9 “Basi mkono wako au mguu wako ukikukosesha, ukate ukautupe mbali nawe; ni afadhali kuingia katika uzima hali umepungukiwa na mkono au mguu, kuliko kuwa na mikono miwili au miguu miwili, na kutupwa katika moto wa milele. Na jicho lako likikukosesha, ling'oe, ukalitupe mbali nawe; ni afadhali kuingia katika uzima una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum ya moto.”

 

-          Je unaweza kulichukua andiko hilo hapo juu na kulitafasiri kama lilivyo? Je andiko hilo ni la kawaida au ni la kimafumbo? Sasa ukichukulia kila kitu kama kilivyoandikwa hutaweza kupata tafasiri sahihi ya andiko hilo hali kadhalika   neno na “Na achovye mguu wake katika mafuta”.  Haliwezi kuchukuliwa katika maana yake nyepesi au rahisi kama ilivyo hiyo ilikuwa lugha inayohitaji ufafanuzi, ukiichukulia kama ilivyo wajinga watakanyaga mafuta

 

6.       Lazima mtafasiri pia ajifunze kufanya ulinganifu wa kimaandiko (The Principle of Harmonisation) yaani ili uweze kufanya fundisho kutoka katika andiko basi andiko hilo liwe na mashahidi wawili au watatu, ni lazima ufanye ulinganifu wa fundisho unalotaka kulitengeneza kutoka katika ushahidi wa maandiko mengine (Combination of scriptures references) Biblia imekaa katika mfumo unaotegemeana sana kwa sababu hiyo huwezi kuchomoa uzi mmoja wa nguo kisha ukadai kuwa hii ni nguo, nguo kamili ni mfungamano wa nyuzi nyingi zinazoifanya nguo kuwa nguo kwa hiyo mzani wako wa ulinganifu wa maandiko utakusaidia kuwa na fundisho sahihi  na hupaswi kusingizia kila kitu kuwa kimetokana na ufunuo wa kiungu

 

Isaya 28:9-10 “Atamfundisha nani maarifa? Atamfahamisha nani habari hii? Je! Ni wale walioachishwa maziwa, walioondolewa matitini? Kwa maana ni amri juu ya amri, amri juu ya amri; kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni; huku kidogo na huku kidogo.”

 

2Wakorintho 13:1 “Hii ndiyo mara ya tatu ya mimi kuja kwenu. Kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno litathibitishwa.”

Kumbukumbu 19:15 “Shahidi mmoja asimwinukie mtu awaye yote kumshuhudia kwa uovu wo wote, wala kwa dhambi yo yote, katika makosa akosayo yo yote; jambo na lithibitishwe kwa vinywa vya mashahidi wawili, au watatu.”

 

7.       Lazima uwe na utaalamu wa kutosha kuhusu ulinganifu wa maswala ya agano la kale na agano jipya, (The Principles of Covenants) uwe na ufahamu kuwa ni mafundisho gani hasa yaliweza kuwahusu watu wa agano la kale na kwa wakati gani na  wale wa agano jipya, sheria zipi zilifaa kwa wakati ule na zipi hazifai kwa wakati huu na ni yapi mapenzi ya Mungu hasa kwa wakati wetu

 

Matendo 17:30-31 “Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu. Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.”            

8.       Lazima uwe na utaalamu wa kujua ni mambo gani hasa yametimizwa katika ufalme wa Mungu na yale ambayo bado hayajatimizwa, Kanuni za ufalme wa Mungu (The Principle of the Kingdom) yako maswala kadhaa katika maswala yahusuyo ufalme wa Mungu ambayo yametimizwa na ambayo bado, kwa hiyo mtaalamu wa neno la Mungu anapaswa kuwa na uelewa huo.

 

9.       Lazima mtaalamu wa kutafasiri maandiko awe na ujuzi wa kina na wa kutosha kuhusu kutafasiri mifano ya ufalme wa Mungu (The Principle of Parables) mifano ya ufalme wa Mungu ina kanuni zake na taratibu zake na inabeba maana moja kubwa iliyokusudiwa na hivyo huwezi kuitafasiri kama unayefanya uchambuzi

 

10.   Lazima mtaalamu wa neno la Mungu awe na ujuzi wa kina kuhusu maswala ya unabii, (The Principle of Prophecy) ajue kuwa ni unabii gani umeshatimizwa na upi ambao bado haujatimizwa ili kujua ni namna gani anaweza kuyaweka sawa maswala ya kinabii asikosee au kwenda kinyume na zile kanuni za kimungu na ile tabia za unabii kujirudia kwa mfumo za zaidi ya mara moja.

Hizo hapo juu ni kanuni kumi muhimu zinazomuongoza mtafasiri wa maandiko kulitafasiri neno la Mungu kwa halali, sina muda mkubwa sana wa kuzielezea hapa kwa  kina lakini zinapatikana katika somo maalumu la kitheolojia linalohusika na namna na jinsi ya kuyatafasiri maandiko kwa halali somo hilo kitaalamu katika vyo vya Biblia linaitwa the “Principles of Biblical interpretations”  au “Hermaneutics”  the sientifical study of the methodological principles of interpretation of the Bible kwa Kiswahili hizo ni sayansi za ufundi na njia au kanuni za kimatumizi katiika kutafasiri maandiko au Biblia,  kwa hiyo watumishi wa Mungu wanaokuwa wameitwa na Mungu na kukubali kwenda katika vyuo vya Biblia hufundishwa masomo hayo kwa kusudi au lengo la kupunguza changamoto za kutafasiri vibaya maandiko, Uchungaji hausomewi, lakini yeye aliyeitwa anapaswa kuupeleka witio wake katika vyuo vya Biblia kwa walimu kwa kusudi la kuunoa wito wako ili uyatumie maandiko kwa halali au kwa mujibu wa kanuni kwa hiyo mtu anyezingatia kanuni hizo sasa anakuwa katika nafasi nzuri sasa ya kulitendea haki neno la Mungu kwa kuitafasiri Biblia katika njia iliyo njema, hairuhusiwi kutengeneza maana yako ya kibiblia kisha ukalisingizia andiko, to guide in “EISOGESIS”  na badala yake unatakiwa kutafuta maana iliyokusudiwa na mwandishi na kuiweka wazi kwa jamii unayoifundisha to guide out “EXEGESIS” wale wanaotafuta maana iliyokusudiwa na mwandishi kwa wakati wake kisha wakatafuta namna ya kuitumia maana ile kwa wakati huu wa sasa wako salama kabisa katika kulitafasiri neno la Mungu kwa usahihi, kwa hiyo tafasiri ya maandiko ni sayansi na sio swala la kukurupuka tu!

Sasa baada ya kujenga msingi huo wa ufahamu nataka twende moja kwa moja tukaaangalie sasa tafasiri ya kimaandiko kuhusu “Tafasiri halisi ya Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!” je andiko hili lilimaanisha nini kwa wakati wa Musa na linaweza kutafasiriwa vipi na linaweza kutendewa kazi katika mazingira yapi? Katika wakati wetu wa leo?

Tafasiri halisi ya Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!

Ni muhimu kwanza kufahamu kuwa andiko la msingi linatoka katika Kumbukumbu 33:24-25 “Na Asheri akamnena, Na abarikiwe Asheri kwa watoto; Na akubaliwe katika nduguze, Na achovye mguu wake katika mafuta. Makomeo yako yatakuwa ya chuma na shaba; Na kadiri ya siku zako ndivyo zitakavyokuwa nguvu zako.”

Andiko hili kwa asili linatokana na lugha ya kiebrania kwa sababu ndio lugha ya asili iliyotumika kuandikia agano la kale tofauti na agano jipya ambalo kimsingi liliandikwa kwa lugha ya kiyunani sasa basi katika lugha ya kiebrania andiko hilo linasomeka namna hii:-

Âshr âmar âshr bârak bn râtsâh âch ţâbal regel shemen “24 âshr âmar âshr bârak bn râtsâh âch ţâbal regel shemen” kwa kiingereza ingetakiwa kusomeka Of Asher he said May Asher be most blessed of sons, may he be favorite among his brothers and bathe his feet in oil

KJV inasomeka hivi “And Asher he said, Let Asher be blessed with children; let him be acceptable to brethren, and let him dip his foot in oil”

SUV inasomeka hiviNa Asheri akamnena, Na abarikiwe Asheri kwa watoto; Na akubaliwe katika nduguze, Na achovye mguu wake katika mafuta.

Kwa asili andiko hili limetokana na Musa nabii ambaye alikuwa akitamka Baraka za aina mbalimbali kwa makabila 12 ya Israel sawa tu na jinsi Yakobo baba yao alivyowatabiria watoto wake kuhusu maswala yatakayowapata siku za mwisho kwa hiyo haya yalikuwa ni maneno ya kinabii  kutoka kwa Musa akiongezea yale yaliyotoka kwa Yakobo ona

Mwanzo 49:1-2 “Yakobo akawaita wanawe, akasema, Kusanyikeni, ili niwaambie yatakayowapata siku za mwisho. Kusanyikeni, msikie, enyi wana wa Yakobo, Msikilizeni Israeli, baba yenu.”

Mwanzo 49:20 “Asheri, chakula chake kitakuwa kinono, Naye atatoa tunu za kifalme.” Kimsingi Musa alikuwa akijazilizia Baraka zilizokuwa zimetamkwa na Baba yao Israel kwa kabisa zote 12 za wana wa Israel lakini linapokuja swala la kabila la Asheri inaonekana wazi kuwa Musa pamoja na Yakobo walikuwa wanalizungumzia kabila hili kama kabila ambalo Bwana angelibariki sana  kwa hiyo maneno “Thy feet in the oil or and let him dip his foot in Oil” au kwa KiswahiliNa achovye mguu wake katika mafutayana maana ya kinabii inayoashiria kuwa kabila la Asheri katika Israel ni kabila ambayo imetamkiwa kutembea katika utajiri mkubwa sana kwa chakula na tunu au madini  hiyo lugha inayotumika hapo ni lugha ya kinabii au pia inaweza kuitwa (figurative language) au figurative expression, yaani lugha ya mficho au lugha ya kimafumbo inayoashiria kuwa Asheri litakuwa ni kabila litakalokanyaga mafanikio makubwa sana, Asheri watakuwa una utajiri mkubwa wa mafuta ya mzeituni.

Nyakati za agano la kale mtu aliyekuwa anamiliki mafuta hasa yaliyotokana na mzeituni, alikuwa ni mtu ambaye anaweza kutengeneza fedha nyingi sana na kuwa vizuri kiuchumi, kwa nyakati zile, kwa hiyo lugha kubwa ya mafanikio na utajiri pia ililinganishwa na wingi wa mafuta ya mizeituni ambao mtu aliweza kuwa nao kama mtu angekuwa na mafuta ya kutosha angeweza kuyamudu maisha yake na kuondokana kabisa na madeni au kupoteza mali na rasilimali alizokuwa nazo, kuchovya mguu katika mafuta kulimaanisha ni kuwa juu ya Baraka zilizopitiliza, kabila la Asheri wanabarikiwa kuwa kabila lenye mafanikio na utajiri unaomwagika, pia mbaraka huu uliashiria kuwa mipaka ya kabila la Asheri itakuwa ni mipaka inayozingirwa na utajiri wa ardhi yenye rutuba na yenye kustawi mizeituni kwa wingi jambo ambalo litawapa utajiri wa mafuta. Kwa hiyo kuchovya mguu wake katika mafuta kunamaanisha kutembea katika mafanikio na maisha ya starehe, mafuta yalikuwa ni ishaya ya mafanikio makubwa nyakati za zamani kwa ichi za mashariki ya kati, ukibarikiwa kuwa uchovye mguu wako katika mafuta maana yake Mungu akufanikishe kwa njia rahisi na isiyo ya taabu.

2Wafalme 4:1-7 “Basi, mwanamke mmoja miongoni mwa wake za wana wa manabii alimlilia Elisha, akasema, Mtumishi wako mume wangu amekufa; nawe unajua ya kuwa mtumishi wako alikuwa mcha Bwana; na aliyemwia amekuja ili ajitwalie wana wangu wawili kuwa watumwa. Elisha akamwambia, Nikufanyie nini? Niambie; una kitu gani nyumbani? Akasema, Mimi mjakazi wako sina kitu nyumbani, ila chupa ya mafuta. Akasema, Nenda, ukatake vyombo huko nje kwa jirani zako wote, vyombo vitupu; wala usitake vichache. Kisha uingie ndani, ukajifungie mlango wewe na wanao, ukavimiminie mafuta vyombo vile vyote; navyo vilivyojaa ukavitenge. Basi akamwacha, akajifungia mlango yeye na wanawe; hao wakamletea vile vyombo, na yeye akamimina.Ikawa, vilipokwisha kujaa vile vyombo, akamwambia mwanawe, Niletee tena chombo. Akamwambia, Hakuna tena chombo. Mafuta yakakoma.Ndipo akaja akamwambia yule mtu wa Mungu. Naye akasema, Enenda ukayauze mafuta haya, uilipe deni yako; nayo yaliyosalia uyatumie wewe na watoto wako.”

Mtu alipokuwa amebarikiwa sana nyakati za agano la kale mafanikio yalionekana ni kama kukanyaga siagi au kumiminiwa mito ya mafuta, wakati huo ulikuwa unaitwa wakati wa ustawi mkubwa sana mfano Ayubu alipokuwa amebarikiwa sana kabla ya mapito yake alizikumbuka nyakati zake za Baraka kubwa na kuzitaja kama nyakati za kukanyaga siagi au kuoshwa hatua zako kwa siagi ona

Ayubu 29:4-6 “Kama nilivyokuwa katika siku zangu za kukomaa, Hapo siri ya Mungu ilipokuwa hemani mwangu; Wakati Mwenyezi alipokuwa akali pamoja nami, Nao watoto wangu walipokuwa wakinizunguka; Wakati hatua zangu zilipokuwa zikioshwa kwa siagi, Nalo jabali liliponimiminia mito ya mafuta!

Kwa hiyo katika andiko la msingi ni muhimu kila mwanafunzi wa maandiko akawa na uelewa kuwa hakuna mahali maaandiko yameagiza au kutoa amri au agizo la kukanyaga mafuta, andiko hili ni sehemu kamili ya maneno ya Baraka ya Musa kwa kabila kadhaa za Israel kabla ya kufa kwake, Musa alikuwa akifanya hivyo kama kiongozi wa kiroho kama ilivyokuwa kwa Israel au Yakobo ambaye ilipofika saa yake ya mwisho pia aliwaita watoto wake na kuwatamkia Baraka  kwa hiyo maneno  naNa achovye mguu wake katika mafuta yana uhusiano na Baraka ya moja kwa moja kwa kabila la Asheri  na ni lugha ya kinabii inayohusiana na mafanikio yao utajiri mkubwa ambao Mungu amewapa Kabila la Asheri, kabila hili lilibarikiwa sana kimwili, na kiroho na kwa maelezo ya marabi wa kiyahudi ni kuwa kabila hili pia lilikuwa na wanawake wazuri na waliokuwa na adabu na wala hawana maringo, kabila hili lilibarikiwa kwa utajiri, mafanikio na ongezeko kubwa lakini pia walibarikiwa kama watu ambao hawapigiki kirahisi vitani  na watakuwa na ulinzi wa uhakika Makomeo yako yatakuwa ya chuma na shaba  Asheri litakuwa ni kabila la watu wenye mafanikio makubwa sana na wingi wa mafuta unaashiria utajiri mkubwa sana wa Ardhi yenye kuzalisha mizeituni kwa wingi bna ambay ingewabeba kiuchumi.

Mafuta ya mzeituni nyakati za Biblia ilikuwa ni bidhaa adimu na ya thamani sana, mafuta yalitumika kwa kupikia, kuwashia taa, kutibu, kujipaka na kwa sababu mbali mbali kwa hiyo kabila hili kuwabarikiwa kiasi cha kukanyaga mafuta kulimaanisha wingi wa utajiri wa bidhaa hii adimu waliyokuwa nayo, kukanyaga mafuta au zabibu pia kulikuwa na maana ya kuendesha mtambo wa kukamulia Mafuta au zabibu kwaajili ya mvinyo, Mashine ya kutengenezea Zabibu au Mafuta ya mzeituni ilitengenezwa kwa mawe makubwa mawili ambapo jiwe moja kubwa lilikaa chini na jiwe moya lilikuwa juu na lile la juu lingesukumwa ili kusaga zaituni zilizovunwa na kuoshwa vizuri kisha zilikamuliwa katika mashinde (Shinikizo) na hivyo kuendesha mashine ya kukamua mafuta au Zabibu kwaajli ya juisi ya zabibu pia kuliitwa kukanyaka shinikizo

Isaya 63:1-2. “Ni nani huyu atokaye Edomu, Mwenye mavazi ya kutiwa damu kutoka Bosra? Huyu aliye na nguo za fahari, Anayekwenda katika ukuu wa uweza wake? Kwani mavazi yako kuwa mekundu, Na nguo zako kama za mtu akanyagaye zabibu? Nalikanyaga shinikizoni peke yangu; Wala katika watu hakuwapo mtu pamoja nami; Naam, naliwakanyaga kwa hasira yangu, Naliwaponda kwa ghadhabu yangu; Na mavazi yangu yametiwa madoa kwa damu yao, Nami nimezichafua nguo zangu zote.”          

Unaona kukanyaga Zabibu hapo maana yake ni kusaga zabibu kwaajili ya kupata juisi ya zabibu, na kukanyaga mafuta ya zeituni ni kukanyaga shinikio (Mashine za kizamani) za kukamulia mafuta ua mizabizu, kwa hiyi utaweza kuona kama Mungu alikuwa anamaaisha kuchovya mguu katika mafuta ni tukio halisi basi kukanyaka Zabibu nalo lingekuwa ni tukio halisi unaelewa?

 

Kwa hiyo Kabila la Asheri linatamkiwa na Musa kuwa kabila lenye wingi wa mafanikio na utajijiri wa mafuta ya zeituni na watu wasiopigika kirahisi, kabila la Asehri walikuwa na sifa njema sana nyakati za biblia kimwili na kiroho maana walitabiriwa kukubalika pia na kupata kibali kwa ndugu zao wakati Yesu alipokuwa anazaliwa mwanamke mmoja mcha Mungu aliyekuwa wa kiroho sana mwenye umri mkubwa sana na tabia njema na uvumilivu alijitokeza pia kutoa unabii kumuhusu Yesu Kristo mwanamke huyu maarufu alitokea kabila la Asheri ona

Luka 2:36-38 “Palikuwa na nabii mke, jina lake Ana, binti Fanueli, wa kabila ya Asheri, na umri wake ulikuwa miaka mingi, alikuwa amekaa na mume miaka saba baada ya uanawali wake. Naye ni mjane wa miaka themanini na minne; haondoki katika hekalu, ila huabudu usiku na mchana kwa kufunga na kuomba. Huyu alitokea saa ile ile akamshukuru Mungu, na wote waliokuwa wakiutarajia ukombozi katika Yerusalemu akawatolea habari zake.”

Kwa sababu hiyo ni muhimu wakristo wakawa na uelewa kuwa hakuna agizo la kibiblia la aina yoyote lile linaloamuru wanadamu wakanyage mafuta, hii ilikuwa ni lugha ya kinabii ya kumtakia mtu mafanikio hata kama utakuwa ulikanyaga mafuta mahali na ukaona mafanikio fulani kumbuka tu kuwa Mungu aliweza kukuhurumia tena alikuhurumia kwa sababu ya ujinga wako na kwa kufilisika kwako kimawazo na kwa tafasiri mbovu za kibiblia, na kwa sababu ya jina lake ambalo lilitajwa huko lakini, andiko hilo halina uhusiano wowote na kukanyaga mafuta kunakofanywa na watumishi kadhaa leo.  Maandiko hayajakakataza mtu kupakwa mafuta miguuni baada ya kunawa au kuoga, lakini hilo sio agizo la kibiblia kwamba tukanyage mafuta, Nayaweka haya hadharani kwa sababu nimeagizwa kuihubiri kweli, nimeagizwa kuwafungua watu akili ili watoke gizani na kumgeukia Yesu Kristo mzima mzima sawa sawa na mapenzi yake nimeagizwa kuweka kweli ya Mungu kwa uwazi kwa kusudu la kuleta uelewa ulio wazi ili watu waifahamu kweli na kweli iwaweke huru maandiko yanaonyesha wazi kuwa wakati wa Yoshua alipopiga kura ya kugawa ardhi watu wa kabila la Asheri walipata inchi yenye utajiri mkubwa wa madini pamoja na ustawi wa miti ya mizeituni na chakula cha kutosha, kwa hiyo unabii kuhusu kubarikiwa kwa kabila hilo la Asheri ulitimizwa!

Yoshua 19:24-31 “Kisha kura ya tano ilitokea kwa ajili ya kabila ya wana wa Asheri kwa kuandama jamaa zao. Na mpaka wao ulikuwa ni Helkathi, na Hali, na Beteni, na Akishafu; na Alameleki, na Amadi, na Mishali; nao ukafikilia hata Karmeli upande wa magharibi, tena ulifikilia hata Shihor-libnathi; kisha ukazunguka kuelekea maawio ya jua mpaka Beth-dagoni, nao ukafikilia hata Zabuloni, tena mpaka bonde la Iftaeli upande wa kaskazini hata Bethemeki na Neyeli; kisha ukatokea hata Kabuli upande wa kushoto; na Ebroni, na Rehobu, na Hamoni, na Kana, hata kufikilia Sidoni mkuu; kisha mpaka ulizunguka kuelekea Rama, na mji wa Tiro ulio na boma; kisha mpaka ulizunguka kuelekea Hosa; na matokeo yake yalikuwa baharini katika nchi ya Akzibu; na Uma pia, na Afeka, na Rehobu; miji ishirini na miwili, pamoja na vijiji vyake.Huu ndio urithi wa kabila ya wana wa Asheri kwa kuandama jamaa zao; miji hii pamoja na vijiji vyake.”

Tafasiri ya Kabila la Asheri kuchovya mguu wao katika mafuta inaweza kutafasiriwa leo kama kutembea katika Baraka za Mungu, kubarikiwa na kupata kibali kiroho, kiuchumi na wingi wa mafanikio, kufurahia neema ya Mungu na kuwa na mapito yasiyo na taabu na masumbufu, lakini kamwe andiko hilo haliwezi kutafasiriwa kama lisemavyo moja kwa moja kwa kufanya hivyo ni kufanya mambo ya kijinga kwani mnakanyaga chakula, kukanyaga chakula kunaleta laana kubwa sana  kwa hiyo Mwandishi au Musa hakuagiza watu wakanyage chakula au wakanyage mafuta mwandishi hajawahi kukusudia hivyo! Msipoelewa maneno ya Mungu mtakanyagishwa mpaka ugali, Bwana ampe neema kila mmoja kutembea katika Baraka za Mungu kama kabila ya Asheri katika jina la Yesu Kristo amen!

Jamani swala la kuchovya mguu katika mafuta tafasiri yake sio kukanyaka mafuta halisi, hii ni lugha ya kimafumbo yenye maana kuwa kabila la Asheri watafanikiwa sana kwa utajiri mwingi utakaopatikana kwao naomba ieleweke kwa njia hiyo!

Naomba niseme kwa kiingereza hapa labda nitaeleweka pia

My brothers and Sisters the phrase is not a literal instruction to dip feet in oil, but rather a metaphor for the tribe of Asher’s Prosperity and abundance of resouces available to them I beg to be understood in that way!

Jinsi ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!

Kuchovya mguu wako katika mafuta maana yake ni kutembea katika Baraka za Mungu, matokeo ya kutembea katika Baraka za Mungu sio tukio linalokuja kama kufumba na kufumbua bali ni mchakato unaotokana na mtindo wa maisha ya kila siku, unaoendana na utii kwa Mungu. Badala ya kuwakanyagisha watu chakula watumishi wa Mungu wawafundishe watu jinsi ya kutembea katika Baraka za Mungu na kutembea katika Baraka za Mungu kuna kanuni zake.

Wakati Musa au Yakobo anawabariki kabla la Asheri kumbuka kuwa alikuwa amewasoma mtindo wao wa maisha tabia na mwenendo wao kwa Bwana, Imani yao, ushirika wao na kujitoa kwao katika maisha ya kila siku na safari ya kila siku ya maisha yao kwa hiyo Yakobo alipofikia mwisho aliwatabiria Asheri na Musa naye alipokuwa anafikia mwisho aliwatabiria Asheri Baraka nyingi sana kwa hiyo mtu awaye yote anayetaka Baraka za Mungu atapaswa kukanyaga katika kanuni za Mungu kwa kufanya yafuatayo katika maisha yake ya siku zote:-

1.       Ishi maisha ya utii kwa neno la Mungu – Baraka za Mungu huja kwetu pale tunapotii, huenda Musa alikuwa amewaangalia sana wana wa Asheri na kubaini kuwa walikuwa watii katika sheria za Mungu na sheria ya Mungu ilikuwa na ahadi kwamba kama mtu ataisikiliza sauti ya Bwana Mungu wake na kuyatunza maagizo yake basi Mungu angeamuru Baraka zije juu ya mtu huyu au kabila hiyo, utii wetu kwa Mungu katika mambo yote hata madogo madogo utawapelekea watu kufurahia matunda ya utii huo.

 

Kumbukumbu 28:1-2 “Itakuwa utakaposikia sauti ya Bwana, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo Bwana, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani; na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya Bwana, Mungu wako.”

 

Isaya 1:19-20 “Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi; bali kama mkikataa na kuasi mtaangamizwa kwa upanga; maana kinywa cha Bwana kimenena haya.”      

 

2.       Ishi maisha  ya Imani – Mwamini na kumtegemea Mungu, hakuna namna iwayo yote mtu anaweza kuishi kwa imani bila kutii na kutegemea, tunaelezwa kuwa Mungu alimuahidi Ibrahimu Baraka lakini ili Baraka hizo ziweze kumjilia Ibrahimu yeye alimuamini Mungu na kutii na ikahesabiwa kwake kuna na haki, hakuna namna yoyote ile ambayo tunaweza kumpendeza Mungu pasipo Imani

 

Mwanzo 12:1-4 “BWANA akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka; nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa. Basi Abramu akaenda, kama BWANA alivyomwamuru; Lutu akaenda pamoja naye. Naye Abramu alikuwa mtu wa miaka sabini na mitano alipotoka Harani.”

 

Waebrania 11:6 “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”

 

Yeremia 17:5-8 “Bwana asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana. Maana atakuwa kama fukara nyikani, Hataona yatakapotokea mema; Bali atakaa jangwani palipo ukame, Katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu. Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, Ambaye Bwana ni Tumaini Lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, Uenezao mizizi yake karibu na mto; Hautaona hofu wakati wa hari ujapo, Bali jani lake litakuwa bichi; Wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, Wala hautaacha kuzaa matunda.

 

3.       Ishi maisha ya utoaji – hakikisha kuwa unatoa kwa ukarimu na sio kwa sheria maandiko yanaonyesha kuwa Mungu huwabariki watu wake wote wanaotoa kwa moyo wa upendo na kwa ukarimu unapokuwa na moyo wa kuwasaidia wengine Mungu huamuru Baraka zake zikujie.

 

Matendo 20:34-35 “Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”            

 

Luka 6:38 “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.”                                        

Hitimisho:

Kutembea katika Baraka za Mungu ni matokeo ya maisha endelevu yenye kudumisha uhusiano wako na Mungu, kumpenda Mungu kwa moyo wako wote, kumtii na kumtumikia huku ukiendelea kumuamini, Mungu sio mchoyo kwani yeye amekusudia kumbariki kila mtu na yuko tayari kumimina Baraka zake katika maisha yako ili hatimaye wewe nawe uchovye mguu wako katika mafuta yaani utembee katika Baraka za Mungu, wakristo ni lazima wakumbuke kuwa hakuna njia ya mkato, lakini iko njia ya mchakato, usikubali kudanganywa hata kama watu wanayatumia maandiko, kama kukanyaka mafuta ingekuwa ni njia halisi ya kibiblia ya kufunguliwa na kupata Baraka za Mungu wengi tungekanyaga mafuta hayo, lakini je tangu umenza kukanyaga mafuta halisi kuna badiliko lolote la kiroho, kiafya au kiuchumi? Watumishi wa Mungu tuamke na kutembea katika nuru kwani saa ya kutoka gizani imekwisha kuwadia asomaye na afahamu!, iwapo kukanyaga mafuta lingekuwa agizo halisi la kimaandiko, mitume wa Bwana wangefanya hivyo, na Yesu angeagiza hivyo, na ingekuwa rahisi tu tungekanyaga mafuta na kupata mafanikio lakini hakuna njia ya mkato kwa Mungu kanyaga njia halisi za mapenzi yake na utafanikiwa, kama bado hujamwamini Yesu tafuta kwanza ufaome wake na haki yake na mengine yote mtazidishiwa jiulize  je ni wapi Yesu ameagiza katika agano jipya? Tuchovye mguu katika mafuta?  Je Yesu alipowaosha wanafunzi wake miguu alikuwa akimaanisha na sisi tuoshane miguu? La hasha alikuwa akijibu swali la wanafunzi wake ni yupi aliye mkubwa na akajibu kwa vitendo ni yule atumikaye au anayewahudumia wengine, hebu tulitendee haki neno la Mungu na tusikubali kudanganyika kila tunachofundishwa duniani tuhoji na tujiulize kikoje katika maandiko na je ndivyo kilivyo? Imekuwaje wakristo wa kipindi hiki ambao ni wasomi na maarifa nyameongezeka wanadanganyika kwa njia rahisi? Do you think that to think critical is sin? Je unafikiri kwamba kufikiri kwa kuhoji au kujiuliza ni dhambi? Amka kuanzia sasa na jaribu kila fundisho au roho uone kama ndivyo ilivyo, Mafundisho huwa yana roho nyuma yake

Yohana 6:63 “Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima.”

1Yohana 4:1-4 “Wapenzi, msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani. Katika hili mwamjua Roho wa Mungu; kila roho ikiriyo kwamba Yesu Kristo amekuja katika mwili yatokana na Mungu. Na kila roho isiyomkiri Yesu haitokani na Mungu. Na hii ndiyo roho ya mpinga Kristo ambayo mmesikia kwamba yaja; na sasa imekwisha kuwako duniani. Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia.”

                                 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Ameen Pastor Asante kwa Kutufungua akili...! Mungu akubariki