2Wafalme 5:1-5 “Basi Naamani, jemadari wa jeshi la mfalme wa Shamu, alikuwa mtu mkubwa mbele ya bwana wake, na mwenye kuheshimiwa, kwa sababu kwa mkono wake Bwana alikuwa amewapa Washami kushinda; tena alikuwa mtu hodari wa vita; lakini alikuwa mwenye ukoma. Na Washami walikuwa wametoka vikosi, wakachukua mfungwa mmoja kijana mwanamke kutoka nchi ya Israeli; naye akamhudumia mkewe Naamani. Akamwambia bibi yake, Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! Maana angemponya ukoma wake.”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kwamba mojawapo
ya nafasi ya Muhimu sana katika utumishi wa Mungu ni pamoja na kupata nafasi ya
kuwa mfanyakazi wa ndani katika nyumba ya Mchungaji au mtumishi awaye yote wa
Mungu, hii ni nafasi ya kipekee sio tu ya kupata neema ya kuwahudumia watumishi
wa Mungu lakini pia ya kupitia kujifunza kwa namna ya kipekee na kushuhudia
maisha ya utumishi wa watu wa Mungu na kujiletea baraka na heshima kutoka kwa Mungu, hii ni kwa sababu
neno la Mungu limesema yeye amuhudumiaye nabii kwa kuwa ni nabii atapata
thawabu ya nabii.
Mathayo 10:40-42 “Awapokeaye ninyi,
anipokea mimi; naye anipokeaye mimi, ampokea yeye aliyenituma. Ampokeaye nabii
kwa kuwa ni nabii, atapata thawabu ya nabii; naye ampokeaye mwenye haki kwa
kuwa ni mwenye haki, atapata thawabu ya mwenye haki. Na mtu awaye yote
atakayemnywesha mmojawapo wa wadogo hawa ngaa kikombe cha maji ya baridi, kwa
kuwa ni mwanafunzi, amin, nawaambia, haitampotea kamwe thawabu yake.”
Wafanyakazi wa ndani katika
nyumba za watumishi wa Mungu wanahitaji maelekezo maalumu ili waweze kutambua
wajibu wao na baraka ambazo Mungu amezikusudia kwao, wasipoelekezwa vema
wanaweza kutumika kinyume na mapenzi ya Mungu na kusababisha changamoto kubwa
za kihuduma kwa mtu wa Mungu na hata na kanisa lake kwa ujumla na huduma ya
Mchungaji na mama Mchungaji, Ni lazima watumishi wa ndani katika nyumba za
wachungaji watambue kuwa kazi yao ni huduma kamili na ni ibada kamili mbele za
Mungu na kwa sababu hiyo wanapaswa kuifanya kwa moyo na ni nafasi ya kipekee
sana na kwa sababu hiyo hawapaswi kuichukulia kama nafasi isiyo ya heshima, wao
wanaweza kuyatumia mazingira ya kiroho yapatikanayo katika nyumba ya mtumishi
wa Mungu kama njia ya Baraka kubwa katika maisha yao.
Kwa msingi huo leo tutachukua
Muda kujifunza maswala ya msingi ambayo wafanyakazi wa ndani katika nyumba za
watumishi wa Mungu wanaweza kuyaishi ili waweze kuwa Baraka katika mwili wa
Kristo na kwa kanisa la Mungu bila kusababisha madhara katika nyumba za
watumishi wa Mungu na huduma walizoaminiwa na Mungu katika maisha yao. Huduma
ya kichungaji inapaswa kulindwa na kwa sababu hiyi mtenda kazi wa ndani ni moja
ya walinzi wa huduma ya kichungaji, ni walinzi wa madhabahu iliyo hai yaani
moyo na maisha ya Mchungaji.
1.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji ni watenda kazi pamoja na mtumishi wa Mungu.
Inapotokea kuwa
kwa njia yoyote ile umepata nafasi ya kuishi katika nyumba ya Mchungaji au
nabii, Mtume na kadhalika kwaajili ya kazi za ndani ni lazima utambue kuwa wewe
ni mtumishi wa Mungu katika nafasi uliyo nayo, kwa sababu umepata neema ya kumtumikia
Mungu pamoja na mtumishi wake na familia yake, na kwa sababu hiyo kazi yako sio
kazi ya kawaida bali ni ibada mbele za Mungu na Mungu atakubariki endapo
utaifanya kazi hiyo kwa uaminifu na uchaji wa Mungu, kwa hiyo fanya kazi hiyo
kama sehemu ya utumishi wako kwa Mungu na kamwe acha kujifikiri kuwa u mtumwa
au mjakazi.
Wakolosai 3:23-24 “Ninyi
watumwa, watiini hao ambao kwa mwili ni bwana zenu, katika mambo yote, si kwa
utumwa wa macho, kama wajipendekezao kwa wanadamu, bali kwa unyofu wa moyo, mkimcha
Bwana. Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana, wala si kwa
wanadamu,mkijua ya kuwa mtapokea kwa Bwana ujira wa urithi. Mnamtumikia Bwana
Kristo.”
Nimeishi na
wasichana wa kazi wengi katika maisha yangu na wengi wa wale waliokaa na mimi
vizuri Mungu aliwabariki na waliolewa na sasa wana nyumba zao na wanaishi
maisha mazuri na yenye utulivu, nay a kuvutia sana, vijana wengi waliamini kuwa mambinti hao wako
salama na wote waliooa kutoka katika
nyumba za wachungaji hawakuwahi kujutia hii ni moja ya Baraka kubwa, wakati
mwingine kutokana na kuishi katika utumishi wa Mtumishi wa Mungu, Mungu
amewafanya wafanyakazi katika nyumba za watu wa Mungu kuja kuwa na huduma ya
kitumishi vile vile na wengi wameinuliwa kutoka kuwa watumishi wa ndani na hata
kuwa mama wachungaji, mama maaskofu na kadhalika
Roho ya utumishi
wa Mungu imewahi kuwakalia wale waliokuwa watumishi wa watumishi wa Mungu, hii
ni kwa sababu watumishi wa waliokuwa watumishi wa Mungu wanajua mapito na
mateso yote ambayo Bwana zao waliyapitia kwa hiyo haishangazi kuona Mungu
akijitwalia viongozi kutoka wale waliokuwa wakifanya kazi kama za utumwa tu,
kimsingi wakati mwingine huwezi kuwa mtumishi wa Mungu kabla ya kuwa mtumishi
wa mwanadamu.
Kutoka 3:1-4 “Basi
huyo Musa alikuwa akilichunga kundi la Yethro mkwewe, kuhani wa Midiani;
akaliongoza kundi nyuma ya jangwa, akafika mpaka mlima wa Mungu, hata Horebu.
Malaika wa BWANA akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti;
akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea.
Musa akasema, Nitageuka sasa, niyaone maono haya makubwa, na sababu kijiti hiki
hakiteketei. BWANA alipoona ya kuwa amegeuka ili atazame, Mungu akamwita kutoka
katikati ya kile kijiti, akasema, Musa! Musa! Akasema, Mimi hapa.”
Hesabu 11:28-29 “Yoshua
mwana wa Nuni, mtumishi wa Musa tangu ujana wake, akajibu akasema, Ee bwana
wangu Musa, uwakataze. Musa akamwambia, Je! Umekuwa na wivu kwa ajili yangu;
ingekuwa heri kama watu wote wa Bwana wangekuwa manabii na kama Bwana angewatia
roho yake.”
Yoshua 1:1-3 “Ikawa
baada ya kufa kwake Musa, mtumishi wa Bwana, Bwana akamwambia Yoshua, mwana wa
Nuni, mtumishi wa Musa, akasema, Musa mtumishi wangu amekufa; haya basi,
ondoka, vuka mto huu wa Yordani; wewe na watu hawa wote, mkaende hata nchi
niwapayo wana wa Israeli.Kila mahali zitakapopakanyaga nyayo za miguu yenu,
nimewapa ninyi, kama nilivyomwapia Musa.”
Ni jambo la
kushangaza kuwa Musa alikuwa akifanya kazi ya kulichunga kund la Yethro mkwewe
ambaye alikuwa kuhani wa Midian, Lakini Mungu alimuita Musa akiwa katika hali
ya kumtumikia mkwewe na kufanya kazi hiyo ambayo kimtazamo ilionekana ni kama
kazi ya chini sana, Yoshua alikuwa mtumishi wa Musa na baadaye Musa alipokufa
Yoshua ndiye aliyekuwa kiongozi mkubwa aliyewaingiza Israel katika inchi ya
mkanaani hii inaweza isiwe kanuni lakini
inatufunza Mungu anajali utumishi wako dhidi ya watumishi wake.
2.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji ni lazima wajifunze kuwaheshimu wachungaji
na familia zao.
Kila anayefanya
kazi katiia nyumba ya mtumishi wa Mungu ni lazima awe na uelewa kuwa watumishi
hao wa Mungu wanahitaji kuheshimiwa sana wao pamoja na familia zao, Mchungaji
au nabii au mtume ni mtu aliyeitwa na Mungu na ni mtu anayestahili heshima yeye
pamoja na mkewe pia na watoto wao, kwa
sababu hiyo kila anayefanya kazi ndani ya nyumba za watumishi wa Mungu anapaswa
kujiheshimu, ni marufuku kuutumia udhaifu wa mke wa Mchungaji kama nafasi ya kutaka
kumvunjia Heshima mama Mchungaji na au mchungaji, Moja ya mgogoro mkubwa
uliompata Sara na Hajiri hata kufikia ngazi ya kuanza kutesana ni pamoja na Hajiri
kuanza kumdharau Bibi yake.
Mwanzo 16:6-9 “Naye
Abramu akamwambia Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo
jema machoni pako. Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake. Malaika wa
BWANA akamwona kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika
njia ya kuendea Shuri. Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi,
nawe unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai.
Malaika wa BWANA akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono
yake.”
Wafanyakazi wa
ndani watapaswa kuishi na mke wa mchungaji vizuri na kujiepusha na migogoro
isiyo na msingi, aidha wao ni waajiriwa wa mwanamke na kamwe halitakuwa jambo
lenye kupendeza Mchungaji kujihusisha na malipo ya mshahara wa mfanyakazi,
wafanyakazi wa ndani wanapaswa kuheshimu mamlaka ya kiroho ya kichungaji sawa
tu na ilivyo Kanisani na nyumbani pia.
1Timotheo 5:17 “Wazee
watawalao vema na wahesabiwe kustahili heshima maradufu; hasa wao wajitaabishao
kwa kuhutubu na kufundisha.”
Aidha kila
msichana wa kazi katika nyumba ya mtumishi wa Mungu anapaswa kuwa kielelezo kwa
kuishi maisha matakatifu na yaliyo kielelezo kwani watu wanaitazamia nyumba ya
mchungaji kuwa kielelezo, wako mambinti wengi katika nyumba za watumishi wa
Mungu ambao wametia aibu kwa kuishi maisha yasiyokuwa na kielelezo na kwa
sababu hiyo kusababisha maswali yasiyoyokuwa na majibu, wengine walipata
ujauzito na wakarudhishwa makwao huku washirika wakibaki na maswali kwamba
waliwezaje kufanya matukio ya aina hiyo ili hali wanaishi katika nyumba za watu
wa Mungu, huku ni kufanya uchafuzi wa kimazingira na kuleta shaka juu ya
usimamizi wa huduma ya kichungaji kwani Mchungaji na mama Mchungaji wana wajibu
wa kuisimamia nyumba ya Mchungaji ili iwe kielelezo kwa waamini.
1Timotheo 3:4-5 “mwenye
kuisimamia nyumba yake vema, ajuaye kutiisha watoto katika ustahivu; (yaani,
mtu asiyejua kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje Kanisa la Mungu?) ”
3.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji ni lazima wawe kielelezo katika Uadilifu,
Nidhamu na kutunza siri za nyumbani
Ukiacha kuwa ni
jukumu la kila mfanyakazi wa ndani katika nyumba ya Mchungaji kuishi maisha
yaliyo kielelezo na ya uadilifu na nidhamu, pia kila msichana wa kazi katika
nyumba za watumishi wa Mungu anapaswa kuwa mstari wa mbele katika kutunza siri
za changamoto zinazojitokeza katika nyumba ya mtumishi wa Mungu, Nyumbani
Mchungaji ni Baba, ni Mume na ni
kiongozi wa familia, lakini sio hivyo tu Nyumba ya mchungaji ina mapito mengi,
wanaweza kulala na njaa, kufunga, kula vibaya yaani chakula kisicho na hadhi,
kupungukiwa na kadhalika pia Mchungaji anao ndugu na jamaa ambao wanaweza kuwa
hawajaokoka, hivyo watendakazi nyumbani kwa mchungaji hupita mapito hayo pamoja
na familia ya Mchungaji na kwa sababu hiyo wakati mwingine usiri unahitajika
kuhusiana na mapito hayo, Ni lazima mfanyakazi wa ndani katika nyumba ya
mchungaji awe mwaminifu kwa kila linaloendelea nyumbani, hupaswi kulianika nje?
Usieneze siri ya matatizo au mapito ya ndani ya nyumba ya mchungaji, hakikisha
kuwa washirika wengine hawatengenezi nafasi ya udadisi ya kutaka kujua
yanayoendelea katika nyumba ya mchungaji wewe endelea kuwa mwaminifu na kufanya
kazi kwa heshima, usafi na kwa moyo acha kueneza fitina hususani kati ya nyumba
ya mchungaji na washirika wake, waache waguswe wenyewe kuihudumia nyumba ya
Mchungaji na usiwaeleze watu kabisa hata kama mmeshinda na njaa. Aidha kama
kuna jambo watu wanajaribu kulidadisi kuhusu Mchungaji au mama Mchungaji
waelekeze watu kuwaona wasemaji wa familia ya Mchungaji na wewe baki kama mtu
usiyejua kinachoendelea!
Mithali 11:13 “Mwenye
kitango akisingizia hufunua siri; Bali mwenye roho ya uaminifu husitiri mambo.”
Mithali 25:2 “Ni
utukufu wa Mungu kuficha jambo; Bali ni utukufu wa mfalme kuchunguza jambo.”
Aidha ishi na
watoto wa Mtumishi wa Mungu sawa na makusudi ambayo kwayo watoto hao
wamezaliwa, wewe kama yaya wa watoto wa Mchungaji usijihusishe katika
kuwapandikizia watoto wa Mchungaji uharibifu, lilikuwa ni jambo la kusikitisha
kuwa Hajiri yeye alianza kumnyanyasa Isaka na akiwa na mwanae Ishmael walianza
kutumiwa na shetani kumdhihaki Isaka na kumfanya mtoto yule wa ahadi
asiyafurahie maisha nyumbani kwao jambo lililompelekea Sara kuamuru kutimuliwa
kwa mjakazi na mwanae.
Mwanzo 21:8-12 “Mtoto
akakua, akaachishwa kunyonya; Ibrahimu akafanya karamu kuu siku ile Isaka
alipoachishwa kunyonya. Sara akamwona yule mwana wa Hajiri Mmisri, ambaye
alimzalia Ibrahimu, anafanya dhihaka. Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, Mfukuze
mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu,
Isaka. Na neno hilo lilikuwa baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya
mwanawe. Mungu akamwambia Ibrahimu, Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa
ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti
yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa.”
Aidha uzembe
uliowahi kufanya na yaya wa Yonathan mwana wa Sauli kwa kijana wake
Methiboehseth ulisababisha ulemavu usio wa lazima kwa mtoto wa Mtumishi wa
Mungu Yonathan, kwa hiyo hata yaya katika nyumba za watumishi wa Mungu anapaswa
kuwa mtu mwangalifu kwa familia ya Mchungaji, watoto wke mkewe na nduguze na
kuchukua tahadhari za kutokuwasababishia matatizo au changamoto watumishi wa
Mungu zikiwemo changamoto za kiafya!
2Samuel 4:4 “Naye
Yonathani, mwana wa Sauli alikuwa na mwana aliyekuwa na kilema cha miguu.
Alikuwa amepata miaka mitano, habari za Sauli na Yonathani zilipofika Yezreeli,
na yaya wake akamchukua akakimbia ikawa, alipokimbia kwa haraka, huyo mtoto
akaanguka, akawa kilema. Na jina lake aliitwa Mefiboshethi.”
4.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji ni lazima waishi kwa kutumia fursa za
kiroho zinazopatikana katika nyumba ya mtumishi
Kuishi na
watumishi wa Mungu kwa uzuri ubora na uaminifu kunaleta Baraka kubwa sana
kutokana na utendaji wako uliotukuka wewe unaweza kufanikisha watumishi wa
Mungu kuhudhuria ibada kwa wakati huku wakiwa wameshiba, kuwapikia chakula
bora, kuitumia nafasi ya kufunga kwao na kuomba kukua kiroho, kuhudhuria ibada
pamoja nao na kujifunza maisha ya utumishi, kwa ujumla ni Baraka kubwa sana
kuwatumikia watumishi wa Mungu wale waliotumika kwa uaminifu walipata Baraka na
wale walioshindwa kuwa waaminifu walipata madhara kwa sababu hiyo wewe itumie
nafasi ya kuishi kwa mchungaji kwa nia njema, usikubali kuwaacha watumishi wa
Mungu kwa sababu zozote zile hata wanapopitia changamoto wewe ni lazima uwe mtu
wa kwanza kusimama nao
2Wafalme 2:9-15 “Hata
ikawa, walipokwisha kuvuka, Eliya akamwambia Elisha, Omba kwangu lo lote
utakalo nikutendee, kabla sijaondolewa kwako. Elisha akasema, Nakuomba, sehemu
maradufu ya roho yako na iwe juu yangu. Akasema, Umeomba neno gumu; lakini,
ukiniona nitakapoondolewa kwako, utalipata; la hukuniona, hulipati. Ikawa,
walipokuwa wakiendelea mbele na kuongea, tazama! Kukatokea gari la moto, na
farasi wa moto, likawatenga wale wawili; naye Eliya akapanda mbinguni kwa upepo
wa kisulisuli. Naye Elisha akaona, akalia, Baba yangu, baba yangu, gari la
Israeli na wapanda farasi wake! Asimwone tena kabisa; akashika mavazi yake
mwenyewe, akayararua vipande viwili. Kisha akaliokota lile vazi la Eliya
lililomwangukia, akarudi, akasimama katika ukingo wa Yordani. Akalitwaa lile
vazi la Eliya lililomwangukia, akayapiga maji, akasema, Yuko wapi Bwana, Mungu
wa Eliya? Naye alipoyapiga maji, yakagawanyika huku na huku, Elisha akavuka.Na
hao wana wa manabii, waliokuwako Yeriko wakimkabili, walipomwona, walisema,
Roho ya Eliya inakaa juu ya Elisha. Wakaja kuonana naye, wakainama kifudifudi
mbele yake.”
Elisha alikuwa
ni mtumishi binafsi wa Eliya, alitumika kwa uaminifu mpaka dakika ya mwisho,
jambo hili lilimletea Baraka kubwa sana wakati wa kuagana ulipofika kwa kweli
Eliya alikuwa amekusudia kumbariki Elisha na Elisha aliomba sehemu maradufu ya
roho ya Eliya imkalie juu yake na kwa kweli Mungu alifanya hivyo na wote
waliokuwa wakimtambua Elisha kama mtumishi wa Eliya walimuinamia mpaka nchi
wakijua kuwa Roho ya Eliya inakaa juu ya Elisha
Wakati Elisha
akiwa anafaidika na utumishi wake mambo yalikuwa kinyume kwa Gehazi ambaye
aliweka maslahi yake mbele na kutokufuata maelekezo ya Bwana wake na kwa sababu
hiyo aliambulia kuwa na ukoma siku zote za maisha yake
2Wafalme 5:20-27 “Lakini
Gehazi, mtumishi wa Elisha mtu wa Mungu, akasema, Tazama, bwana wangu
amemwachilia huyo Naamani Mshami, asivipokee mikononi mwake vile vitu
alivyovileta; kama Bwana aishivyo, mimi nitamfuata mbio, nipokee kitu kwake.
Basi Gehazi akamfuata Naamani. Naye Naamani, alipoona mtu apigaye mbio anakuja
nyuma yake, alishuka garini amlaki, akasema, Je! Ni amani? Akasema, Amani.
Bwana wangu amenituma, kusema, Tazama, sasa hivi wamenijia kutoka milimani mwa
Efraimu vijana wawili wa wana na manabii; uwape, nakuomba, talanta ya fedha, na
mavazi mawili. Naamani akasema, Uwe radhi, ukatwae talanta mbili.
Akamshurutisha, akafunga talanta mbili za fedha ndani ya mifuko miwili, na
mavazi mawili, akawatwika watumishi wake wawili; nao wakayachukua mbele yake.
Naye alipofika kilimani, alivitwaa mikononi mwao, akaviweka nyumbani; akawaacha
wale watu kuondoka, nao wakaenda zao. Lakini yeye akaingia, akasimama mbele ya
bwana wake. Elisha akamwambia, Watoka wapi, Gehazi? Akanena, Mtumwa wako
hakuenda mahali. Akamwambia, Je! Moyo wangu haukuenda na wewe, hapo alipogeuka
yule mtu katika gari ili akulaki? Je! Huu ndio wakati wa kupokea fedha, na
kupokea mavazi, na mashamba ya mizeituni, na mizabibu, na kondoo, na ng'ombe,
na watumwa, na wajakazi? Basi ukoma wa Naamani utakushika wewe, na wazao wako
hata milele. Naye akatoka usoni pake mwenye ukoma kama theluji.”
Kutokuitumia
fursa ya kiroho ya kuishi na watumishi wa Mungu kunaweza kutuletea laana na
wazao wetu, lakini tukiwa na akili na kujua mapenzi ya Mungu neema ya Mungu
itatuinua na watumishi hao wa Mungu watatuachia Baraka kubwa sana katika maisha
yetu, kama ukiitambua siri ya kuishi na watumishi wa Mungu na ukajua Baraka
zinazopatikana kwa kweli utasema kama Daudi kuwa siku moja katika nyua zako ni
bora kuliko siku 1000, kuitumikia nyumba ya mtumishi wa Mungu ni kuitumikia
madhabahu ya Bwana
Zaburi 84:10 “Hakika
siku moja katika nyua zako Ni bora kuliko siku elfu. Ningependa kuwa bawabu
nyumbani mwa Mungu wangu, Kuliko kukaa katika hema za uovu.”
5.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji ni lazima waitumie nafasi ya kuishi kwa
maombi na neno la Mungu
Kupata nafasi ya
kuishi katika nyumba ya mtumishi wa Mungu kusikufanye wewe kubweteka na kuishi
maisha ya kiburi na majivuno, badala yake lazima uitumie nafasi hiyo kwa kuishi
kwa maombi huku ukiwa mtu uliyejaa neno la Mungu, lazima mtu anayeishi katika
nyumba ya mchungaji awe msikilizaji na mtendaji mzuri wa neno la Mungu, huku ukiwa
kielelezo cha maisha ya kiroho, kushiriki ibada na mafundisho na hata kuandika
notes, watu wanaokaa kwa mchungaji hawachukuliwi kuwa watu wa kawaida kwa hiyo
ni lazima uwe kielelezo.
Kutoka 33:11 “Naye
BWANA akasema na Musa uso kwa uso, kama vile mtu asemavyo na rafiki yake. Kisha
akageuka akarejea hata maragoni; bali mtumishi wake Yoshua, mwana wa Nuni, naye
ni kijana, hakutoka mle hemani.”
Mathayo 4:4 “Naye
akajibu akasema, Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno
litokalo katika kinywa cha Mungu.”
6.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji ni lazima kuitumia nafasi ya kuishi kwa
Mchungaji kama sehemu ya huduma na Upendo kwa wengine.
Kufanya kazi
katika nyumba ya Mchungaji kunahitaji hekima, uvumilivu na upendo kwa wengine
lakini zaidi sana kwa Mchungaji, wachungaji wakati mwingine hukosa nafasi ya Mapumziko
mfanyakazi katika nyumba ya Mchungaji anapaswa kuwa na hekima sio kila wakati
utamwamsha mchungaji au kuwakaribisha wageni katika nyumba yake, utawahoji
wageni kwa hekima na upendo iwapo wana ahadi ya kukutana na Mchungaji nyumbani
kwake au ofisini, Afya ya Mchungaji ni lazima ilindwe kwa gharama yoyote, muda
wake binafsi na Mungu, muda wake wa kujiandaa kwaajili ya neno la Mungu,
utulivu wake kula kwake na mapumziko yake kwa hiyo ni wajibu wa mfanyakazi
katika nyumba ya Mchungaji ni kusimamamia ratiba za mtumishi wa Mungu badala ya
kumwamsha kila anapokuja mtu yoyote na hata matapeli tu kwa hiyo tunaaswa kuwa
na huduma na moyo wa upendo lakini tukiyanusuru na kuyalinda maisha ya mtumishi
wa Mungu yasiiingiliwe kama mtu atakavyo
Wagalatia 5:13-14 “Maana
ninyi, ndugu, mliitwa mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata
mwili, bali tumikianeni kwa upendo. Maana torati yote imetimilika katika neno
moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako kama nafsi yako.”
7.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji ni lazima wafanyike Baraka katika nyumba ya
Mchungaji.
Katika mstari wa
msingi wa somo hili nimenukuu habari za binti mmoja kijakazi katika nyumba ya
Naamani ambaye alichukuliwa mateka huko Syria, lakini binti huyu aligeuka
Baraka kubwa kwa sababu kupitia yeye na imani yake Bwana wake aliponywa ukoma
wake, mfanyakazi huyu alichukuliwa mateka kutoka Israel lakini jambo la
kushangaza hajawahi kuweka kinyongo chochote alikubali maisha ya ujakazi na
utumwa huku akiwa mwaminifu kwa Bwana wake huku akimtakia afya njema na
mafanikio zaidi, Naaman tunaelezwa kuwa alikuwa mzuri sana kwani jina Naaman
maana yake ni mzuri lakini alipougua ukoma hali yake iliharibika na sasa
kijakazi huyu anamtakia bibi yake na bwana wake furaha ya kweli kwa kujali afya
ya Naamani
2Wafalme 5:1-5 “Basi
Naamani, jemadari wa jeshi la mfalme wa Shamu, alikuwa mtu mkubwa mbele ya
bwana wake, na mwenye kuheshimiwa, kwa sababu kwa mkono wake Bwana alikuwa
amewapa Washami kushinda; tena alikuwa mtu hodari wa vita; lakini alikuwa
mwenye ukoma. Na Washami walikuwa wametoka vikosi, wakachukua mfungwa mmoja
kijana mwanamke kutoka nchi ya Israeli; naye akamhudumia mkewe Naamani.
Akamwambia bibi yake, Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko
Samaria! Maana angemponya ukoma wake.”
Kila mfanyakazi
katika nyumba ya mtumishi wa Mungu anapaswa kuwa sababu ya Baraka na uponyaji
wa nyumba ya mtumishi badala ya kutumika kama ajenti wa shetani na kusababisha
maafa na anguko la mtumishi wa Mungu au huduma yake, aidha kuwa na moyo wa
shukurani na subira kuacha tamaa, wivu na kutokuyatenda majukumu yako
ipaswavyo, binti yule wa kiyahudi alikuwa mwaminifu na mwenye moyo wa kweli
kwani licha ya kuwa alikuwa amechukuliwa mateka lakini alikuwa ni mtu
aliyethamini utumishi wa Naamani na kutamani kama angeponywa ukoma wake,
alikuwa na imani kubwa kwani haijawahi kusikika kokote kuwa mtu amewahi
kuponywa ukoma wake lakini yeye alimuamini Elisha na kusaidiki kuwa bwana wake
anaweza kupata msaada Endapo angekutana na mtu wa Mungu na ikawa hivyo kwani
Naamani aliponywa na sio mwili wake tu na alimuamini Mungu wa Israel hata
ushindi wake ulitokana na Mungu wa Israel
8.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji ni lazima wavae kwa kujisitiri
Kama mtumishi wa
Mungu ndani ya nyumba ya mchungaji hakikisha kuwa unavaa kwa heshima na
kujisitiri, haiwezekani unakaa katika nyumba ya Mtu wa Mungu kisha ukawa unavaa
mavazi ya kikahaba na kutumika kama chombo cha ibilisi kwaajili ya kumaliza
huduma ya kichungaji swala hilo halitaleta Baraka kwako na kwa mwili wa Kristo,
acha kujifikiri mwenyewe na starehe zako na baadala yake fikiri kuhusu faida za
mwili wa Kristo na ufalme wa Mungu.
1Timotheo 2:9-10 “Vivyo
hivyo wanawake na wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na
moyo wa kiasi; si kwa kusuka nywele, wala kwa dhahabu na lulu, wala kwa nguo za
thamani; bali kwa matendo mema, kama iwapasavyo wanawake wanaoukiri uchaji wa
Mungu.”
Mithali 7:10-18 “Na
tazama, mwanamke akamkuta, Ana mavazi ya kikahaba, mwerevu wa moyo; Ana kelele,
na ukaidi; Miguu yake haikai nyumbani mwake. Mara yu katika njia kuu, mara
viwanjani, Naye huotea kwenye pembe za kila njia. Basi akamshika, akambusu,
Akamwambia kwa uso usio na haya, Kwangu ziko sadaka za amani; Leo hivi
nimeziondoa nadhiri zangu; Ndiyo maana nikatoka nikulaki, Nikutafute uso wako
kwa bidii, nami nimekuona. Nimetandika kitanda changu, magodoro mazuri, Kwa
matandiko ya Kimisri yenye mistari. Nimetia kitanda changu manukato, Manemane
na udi na mdalasini. Haya, na tushibe upendo hata asubuhi, Tujifurahishe nafsi
zetu kwa mahaba.”
9.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji wasijaribu kuwa mrithi wa mama Mchungaji
Hakuna sheria
inayokataza Mchungaji kumuoa binti wake wa kazi endapo itatokea Mungu ametaka
iwe hivyo, hata hivyo litakuwa ni jambo lenye kuchukiza na kuleta utata mkubwa
sana endapo itatokea unaolewa na Mchyhungaji baada ya mama Mchungaji, maandiko
yanaonyesha kuwa ni chukizo kwa mjakazi kumrithi bibi yake, Muombe Mungu akupe
mumeo na usijihusishe na maisha ya Mchungaji wale mke wake hata kama
uliyasoma madhaifu yake, watmishi wa
Mungu tafadhali Mungu akupe hekima usilitupia jicho lako kwa binti wa kazi yeye
na awe kama moja ya mabinti zako tu nyumbani, Mwandishi wa kitabu cha Mithali
alionyesha kuwa kuoa housegirl ni
jambo lisilovumilika na linaweza kutetemesha nchi
Mithali 30:21-23 “Kwa
ajili ya mambo matatu nchi hutetemeka, Naam, kwa ajili ya manne haiwezi
kuvumilia. Mtumwa apatapo kuwa mfalme; Mpumbavu ashibapo chakula; Mwanamke
mwenye kuchukiza aolewapo; Na mjakazi aliye mrithi wa bibi yake.”
10.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji Wanaweza kumjua Mchungaji vema zaidi kuliko
watu wengine wote
Watumishi wa
ndani katika nyumba ya Mchungaji wanauwezo wa kumjua Mchungaji na mahitaji yake
vema zaidi kuliko watu wengine, Nyakati za kanisa la kwanza wakati Mchungaji
Yakobo na Petro walipokuwa wamekamatwa, na Yakobo akauawa na Herode ni ukweli
uliokuwa wazi kuwa kanisa lilimuomba Mungu kwa bidii sana lakini hata hivyo
hawakuwa na Imani kuwa Mungu angefanya muujiza, Hata hivyo Mungu alimtuma
malaika akamfungua Petro Gerezani na hata alipokuwa akigonga mlango mtu
aliyetambua kuwa Petro anagonga mlango alikuwa ni Roda mfanyakazi wa ndani
katika nyumba ya Mariamu mama yake Yohana, binti huyu kwa furaha aliacha kufungua
mlango na kuwapasha wote kuwa Petro anagonga mlango, hata hivyo kila mmoja
katika kanisa walifikiria kuwa binti huyo ana wazimu ni kichaa, hayuko
sawasawa, lakini ni ukweli ulio wazi
yeye ndiye aliyekuwa sahihi kuliko watu wote, moyo wake upendo na Imani yake
kwa Mungu ilimfanya kuwa na mtazamo tofauti na watu wengine wote yeye alimjua
Petro vizuri na hata sauti yake na alipogonga pia alikuwa anajua namna Petro
anavyogonga mlango wa nyumba
Matendo 12:11-16 “Hata
Petro alipopata fahamu akasema, Sasa nimejua yakini ya kuwa Bwana amempeleka
malaika wake na kunitoa katika mkono wa Herode na katika kutazamia kote kwa
taifa la Wayahudi. Na alipokuwa akifikiri haya akafika nyumbani kwa Mariamu,
mamaye Yohana, ambaye jina lake la pili ni Marko; na watu wengi walikuwa
wamekutana humo wakiomba. Naye alipobisha kilango cha lango, kijakazi, jina
lake Roda, akaja kusikiliza. Alipoitambua sauti ya Petro, hakukifungua lango,
kwa ajili ya furaha, bali alipiga mbio, akaingia ndani akawaambia kwamba Petro
anasimama mbele ya lango. Wakamwambia, Una wazimu. Lakini yeye akakaza sana,
akasema ya kwamba ndivyo hivyo. Wakanena, Ni malaika wake. Petro akafuliza
kugonga, hata walipokwisha kumfungulia wakamwona, wakastaajabu.”
Hii
inatukumbusha na kutufundisha kuwa watumishi wa ndani katika nyumba ya
Mchungaji wanaweza kuwa na ufahamu mkubwa na wa kina kumuhusu mtumishi wa Mungu
nahata kumjua Mungu na utendaji wake kuliko mtu mwingine yeyote na Mungu
amewapa wao neema ya kutambua mwenendo na uhitaji wa Mchungaji wakati mwingine kuliko
wengine katika kanisa, na tunakumbushwa hapa kuwa hatupaswi kuwafikiria kuwa ni
wenye wazimu hata kidogo, na kuwapuuzia au kuipuuzia mitazamo yao ya kiroho
11.
Watumishi
wa ndani katika nyumba ya mchungaji ni lazima wawe waaaminifu kwa mama
Mchungaji
Ruthu ni mfano
wa kuigwa kwa uaminifu wake aliokuwa nao kwa Mkwewe, alisimama na mkwewe katika
mazingira yaliyokuwa magumu sana na kujionyesha kuwa mwaminifu hata kwa gharama
yoyote, Yeye alikuwa ni Mmoabu na hakukuwa na kitu cha kupoteza endapo
angemuacha Naomi lakini alisimama na mkwewe katika mazingira magumu sana ambo
lililomletea sifa za kipekee na faraja kubwa sana hapo baadaye, simama na mama
Mchungaji katikamhali zote iwe njema au mbaya usikubali kumuacha mama Mchungaji
isipokuwa kama utaolewa na kuwa na majukumu yako mengine yanayokulazimu
Ruthu 1:16-18 “Naye
Ruthu akasema, Usinisihi nikuache, Nirejee nisifuatane nawe; Maana wewe uendako
nitakwenda, Na wewe ukaapo nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, Na Mungu
wako atakuwa Mungu wangu; Pale utakapokufa nitakufa nami, Na papo hapo
nitazikwa; Bwana anitende vivyo na kuzidi, Ila kufa tu kutatutenga wewe
nami.Basi alipomwona kuwa amekaza nia yake kufuatana naye, aliacha kusema naye.”
Ufunuo 2:10 “Usiogope
mambo yatakayokupata; tazama, huyo Ibilisi atawatupa baadhi yenu gerezani ili
mjaribiwe, nanyi mtakuwa na dhiki siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufa, nami
nitakupa taji ya uzima.”
Hitimisho:
Wafanyakazi wa ndani hasa katika
nyumba za watumishi wa Mungu wameitwa kuwa mabalozi wa Baraka za Mungu, kwa
Imani yao, mwenendo na tabia zao, kamwe hatuwatarajii wao kuwa sababu ya
kusambaratika kwa huduma za wachungaji au kusababisha kero na ugomvi katika
nyumba ya Mchungaji, haipendezi wao kuwa sababu ya dharau, na uchonganishi kati
ya huduma ya Mchungaji na washirika wake, somo hili linatoa mwanga tu wa namna
na jinsi iwapaswavyo kuishi kwaajili ya Mungu na wala si kwaajili yao, aidha na
kuwaonyea ili kwamba waache kutumika kama chombo cha shetani na badala yake
waweze kutumika kuiinua huduma ya kichungaji na kuiweka kwenye heshima
inayostahili, ni imani yangu kuwa kama unafanya kazi katika nyumba za watumishi
wa Mungu hutakata tamaa na kujidharau na kujifikiri kuwa huna maana nataka
nikutie moyo ili ujue ya kuwa Mungu anakuzingatia sana anajua umuhimu wako katika
kuitumikia familia ya mtumishi wake!
Wengi wa waliofanya kazi katika
nyumba za watumishi wa Mungu kamwe Mungu hakuwahi kuwapuuzia kwani wengine
alijifunua kwao na kuwabariki na wengine walimuona Mungu hata pale walipopita
katiia changamoto ngumu Mungu aliwatokea
Wakati Sara alipomtendea vibaya
Hajiri malaika wa Bwana hawakumuacha Hajiri na badala yake walimuelekeza njia
sahihi ya kufanya na kuyalinda maisha yake na ya mtoto wake, Mungu hajawahi
kuwadharau wajakazi na kuwaona kama watu wasio na maana na badala yake
aliwahusisha katika Baraka zake alizozikudsudia sawa na nyumba za watumishi
wake
Mwanzo 16:6-11 “Naye Abramu akamwambia
Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako.
Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake. Malaika wa BWANA akamwona
kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika njia ya
kuendea Shuri. Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi, nawe
unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai.
Malaika wa BWANA akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono
yake. Malaika wa BWANA akamwambia, Hakika nitauzidisha uzao wako, wala
hautahesabika kwa jinsi utakavyokuwa mwingi.Malaika wa BWANA akamwambia,
Tazama! Wewe una mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake
Ishmaeli, maana BWANA amesikia kilio cha mateso yako.”
1Timotheo 4:12 “Mtu awaye yote asiudharau
ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na
katika upendo na imani na usafi.”
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote
Maoni 1 :
AMEEN Pastor, somo zuri Mungu akubariki
Chapisha Maoni