Isaya 38:1-6 “Siku hizo Hezekia aliugua,
akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa
mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana
utakufa, wala hutapona. Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani,
akamwomba Bwana, akasema, Ee Bwana, kumbuka haya, nakusihi, kwamba nimekwenda
mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni
pako. Hezekia akalia sana sana. Ikawa, neno la Bwana likamjia Isaya, kusema,
Enenda ukamwambie Hezekia, Bwana, Mungu wa Daudi, baba yako, asema hivi, Mimi
nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama, nitaziongeza siku
zako, kiasi cha miaka kumi na mitano. Nami nitakuokoa wewe, na mji huu, na
mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji huu.”
Utangulizi:
Mojawapo ya njia ya kutuletea
neema kubwa sana kutoka kwa Mungu ni pamoja na njia ya maombi, wote tutakuwa
tunafahamu jinsi maombi yalivyo na nguvu kubwa sana, yana nguvu ya kuteremsha
rehema na neema kutoka kwa Mungu hata wakati tunapopitia changamoto za aina
mbalimbali katika maisha yetu, maombi yana uwezo wa kumfanya mwanamke aliye
tasa kuwa na watoto wengi, maombi yana uwezo wa kusababisha adui kupigwa na
ushindi kupatikana, maombi yana uwezo wa
kufungua utendaji wa miujiza na kuchochewa kwa karama, maombi yana uwezo wa
kubatilisha hukumu ya kifo na kurejesha uhai, maombi yana uwezo wa kugeuza
kesi, maombi yanauwezo wa kubatilisha kile Mungu amesema. Maombi yana uwezo wa
kufungua magereza za kimwili na kiroho, Mungu ametupa maombi kama njia ya
kufanya kazi na yeye na kumruhusu kufanya kazi duniani. Maombi yana nguvu
isiyoweza kuelezeka katika changamoto yoyote unayokutana nayo duniani wewe
tumia maombi.
Mathayo 7:7-11 “Ombeni, nanyi mtapewa;
tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye
hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Au kuna mtu yupi
kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa
nyoka? Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema,
je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?”
Sisi ndio wenye maamuzi ya mwisho
ya kuamua Mungu atafanya nini duniani kwa kutumia maombi, Hapa duniani sio eneo
la utawala wa Mungu, ni eneo ambalo Mungu amewapa wanadamu kutawala, yeye
utawala wake uko mbinguni, huko mapenzi yake yote hutimizwa kwa ukamilifu,
lakini sivyo ilivyo duniani, ili kumpa Mungu kibali cha kufanya mambo duniani
ni lazima tuombe, tunapoomba tunamruhusu Mungu kufanya yanayotakiwa yafanyike
duniani kama yanavyofanyika mbinguni.
Zaburi 123:1-3 “Nimekuinulia macho yangu,
Wewe uketiye mbinguni. Kama vile macho ya watumishi Kwa mkono wa bwana zao Kama
macho ya mjakazi Kwa mkono wa bibi yake; Hivyo macho yetu humwelekea Bwana,
Mungu wetu, Hata atakapoturehemu.”
Mwanzo 1:26-28 “Mungu akasema, Na tumfanye
mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu; wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa
angani, na wanyama, na nchi yote pia, na kila chenye kutambaa kitambaacho juu
ya nchi. Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba,
mwanamume na mwanamke aliwaumba. Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni,
mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na
ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”
Kupitia maombi tunaweza
kumfungulia Mungu njia ya kututendea mambo makubwa na magumu tusiyoyajua,
maombi yana uwezo mkubwa sana wa kubadilisha mambo na utendaji wa Mungu kutoka
katika maisha ya mtu binafsi mpaka maswala ya kitaifa na ulimwengu kwa ujumla,
tunapoomba tunamruhusu Mungu kuinguilia kati na kufanya jambo kwaajili yetu
hapa duniani, tunaruhusu utawala wa kimbingu kuleta msaada wa haraka duniani.
-
Maombi
yanaweza kumfanya tasa kuwa na watoto - Hana aliyekuwa mwanamke tasa,
alipitia machungu na mateso na mashutumu kutoka kwa mke mwenzake, alinyanyasika
hata pamoja na kupendwa sana na mumewe, lakini Penina mara kwa mara alimchokoza
na kumkumbusha hali yake ya kukosa mtoto jambo ambalo lilimsikitisha sana na
kumfanya kutembea kwa huzuni, Hana hata hivyo alifahamu kuwa njia pekee
inayoweza kubadilisha hali yake ni maombi, hivyo alimimina maombi yake mbele za
Mungu na hatimaye Mungu alisikia na kubadilisha hali yake aliyokuwa nayo,
kutoka hali ya utasa kuwa mama wa watoto wengi.
1Samuel 1:1-6 “Palikuwa
na mtu mmoja wa Rama, Msufi, wa nchi ya milima milima ya Efraimu, jina lake
akiitwa Elkana, mwana wa Yerohamu, mwana wa Elihu, mwana wa Tohu, mwana wa
Sufu, Mwefraimu naye alikuwa na wake wawili; jina lake mmoja akiitwa Hana, na
jina lake wa pili aliitwa Penina; naye huyo Penina alikuwa na watoto, lakini
Hana hakuwa na watoto. Na mtu huyo alikuwa akikwea kutoka mjini kwake mwaka kwa
mwaka, ili kuabudu, na kumtolea Bwana wa majeshi dhabihu katika Shilo. Na wale
wana wawili wa Eli, Hofni na Finehasi, makuhani wa Bwana, walikuwako huko. Hata
siku ile ilipofika Elkana alipotoa dhabihu, kumpa mkewe Penina sehemu, akawapa
na watoto wake wote, waume kwa wake, sehemu zao; lakini Hana humpa sehemu mara
mbili; maana alimpenda Hana, ingawa Bwana alikuwa amemfunga tumbo. Ila mwenzake
humchokoza sana, hata kumsikitisha, kwa sababu Bwana alikuwa amemfunga tumbo.”
1Samuel 1:10-20 “Naye
huyo mwanamke alikuwa na uchungu rohoni mwake, akamwomba Bwana akalia sana.
Akaweka nadhiri, akasema, Ee Bwana wa majeshi, ikiwa wewe utaliangalia teso la
mjakazi wako, na kunikumbuka, wala usinisahau mimi mjakazi wako, na kunipa mimi
mjakazi wako mtoto mume, ndipo mimi nitakapompa Bwana huyo mtoto siku zote za
maisha yake, wala wembe hautamfikilia kichwani kamwe. Ikawa, hapo alipodumu
kuomba mbele za Bwana, Eli akamwangalia kinywa chake. Basi Hana alikuwa akinena
moyoni mwake; midomo yake tu ilionekana kama anena, sauti yake isisikiwe; kwa
hiyo huyo Eli alimdhania kuwa amelewa. Ndipo Eli akamwambia, Je! Utakuwa mlevi
hata lini? Achilia mbali divai yako. Hana akajibu, akasema, Hasha! Bwana wangu,
mimi ni mwanamke mwenye roho ya huzuni, mimi sikunywa divai wala kileo, ila
nimeimimina roho yangu mbele za Bwana. Usimdhanie mjakazi wako kuwa ni mwanamke
asiyefaa kitu; kwa kuwa katika wingi wa kuugua kwangu na kusikitika kwangu
ndivyo nilivyonena hata sasa. Ndipo Eli akajibu, akasema, Enenda kwa amani; na
Mungu wa Israeli akujalie haja yako uliyomwomba. Naye akasema, Mjakazi wako na
aone kibali machoni pako. Basi huyo mwanamke akaenda zake, naye akala chakula,
wala uso wake haukukunjamana tena. Wakaondoka asubuhi na mapema, wakasali mbele
za Bwana, kisha wakarejea na kufika nyumbani kwao huko Rama; Elkana akamjua
mkewe Hana; naye Bwana akamkumbuka. Ikawa, wakati ulipowadia, Hana akachukua
mimba na kuzaa mtoto mwanamume; akamwita jina lake Samweli, akisema, Kwa kuwa nimemwomba
kwa Bwana.”
Tunajifunza hapa
kuwa maombi yana uwezo wa kubadilisha aibu kuwa heshima, yana uwezo wa kufumba
vinywa vya maadui zetu, yana uwezo wa kunyamazisha wanaotubeza, yana uwezo wa
kuifanya biashara yako kufanikiwa, mashamba kuzaa, mifugo yako kuongezeka,
maisha yako kujawa na mafanikio, Huduma yako kutendeka kwa kiwango na kanisa
lako linaloonekana kama tasa likawa kanisa lenye watu wengi, tunaweza
kubadilisha hali yoyote inayotukabili iwe ni chungu kuwa furaha, Hana
hakukubali kubakia vile alivyo lakini kwa kupitia maombi alibadilisha mwelekeo
wa maisha yake na kurejesha heshima yake kama mwanamke kamili kwa njia ya
maombi, Maombi yanaweza kubadilisha hatima yako na jina lako.
-
Maombi yanaweza
kutuletea ushindi vitani - Maandiko yanaonyesha kuwa watu waliookolewa wako
vitani, Paulo anasema kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama maana yake
hatuna adui wa kimwili sisi, wala hatuwezi kumuhesabu mwanadamu awaye yote kuwa
ni adui yetu, lakini adui zetu wako rohoni, ni mamlaka, ni falme ni wakuu wa
giza na majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho, hao tunaweza
kushughulika nao kwa njia ya kuomba peke yake, maombi yatatupa ushindi dhidi ya
nguvu za giza popote.
Waefeso 6:10-18 “Hatimaye,
mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote
za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu
sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa
giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. Kwa sababu
hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na
mkiisha kuyatimiza yote, kusimama. Basi simameni, hali mmejifunga kweli
viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa
Injili ya amani; zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza
kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu. Tena ipokeeni chapeo ya wokovu,
na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu; kwa sala zote na maombi mkisali kila
wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea
watakatifu wote;”
Ushindi wetu
hauwezi kupatikana kwa nguvu za mwili na akili za kibinadamu na ujanja ujanja
ushindi wetu utapatikana kwa kumualika Mungu katika vita zetu kupitia maombi,
wakati Musa alipokuwa jangwani wanaikabili Kanaani njiani waameleki walitokea
na wakapigana na Israel neno la Mungu linatuambia kuwa Musa na Haruni na Huri
walipanda mlimani na huko Musa
alinyoosha mikono yake kwa Mungu na Yoshua
na Israel walipata ushindi, Musa akishusha mikono Israel wanashindwa,
watumishi wa Mungu ili tuweze kuwa na ushindi tusikubali kushusha mikono yetu,
tuendelee kumuinulia Mungu mikono yetu na ushindi utakuwa upande wetu kwa
Dhahiri hapo tunajifunza nguvu ya maombi, kwamba tunaweza kupata ushindi.
Kutoka 17:10-13 “Basi
Yoshua akafanya kama Musa alivyomwambia, akapigana na Amaleki; na Musa na
Haruni na Huri wakapanda juu ya kile kilima. Ikawa, Musa alipouinua mkono wake,
Israeli walishinda; na alipoushusha mkono wake, Amaleki walishinda. Lakini
mikono ya Musa ilikuwa mizito; basi wakatwaa jiwe, wakaliweka chini yake
akalikalia. Haruni na Huri wakaitegemeza mikono yake, mmoja upande huu na mmoja
upande huu; mikono yake ikathibitika hata jua lilipokuchwa. Yoshua
akawaangamiza Amaleki na watu wake kwa ukali wa upanga.”
-
Maombi yanaongeza
nguvu wakati wa upinzani – Nyakati za kanisa la kwanza Mitume walipoanza
kuhubiri injili na kufanya miujiza, walikutana na upinzani, walikamatwa,
waliwekwa gerezani, waliadhibiwa na walitishwa na walikatazwa wasizungumze
lolote kwa jina la Yesu, kanisa lilipopata taarifa walijua ni namna gani
wanaweza kuendelea na injili, walijua dawa ni kuomba na walipoomba mahali pale
walipokuweko pakatikiswa wakajaa nguvu za Roho Mtakatifu na kazi ya Mungu ikaendelea
na neno la Mungu linaenea.
Matendo 4:21-31 “Nao
walipokwisha kuwatisha tena wakawafungua, wasione njia ya kuwaadhibu, kwa
sababu ya watu; kwa kuwa watu wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa hayo
yaliyotendeka; maana umri wake yule mtu aliyefanyiwa ishara hii ya kuponya
ulipita miaka arobaini. Hata walipofunguliwa, wakaenda kwa watu wao,
wakawapasha habari ya mambo yote waliyoambiwa na wakuu wa makuhani na wazee. Nao
waliposikia, wakampazia Mungu sauti zao kwa moyo mmoja, wakisema, Mola, wewe
ndiwe Mungu, ndiwe uliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo;
nawe ulinena kwa Roho Mtakatifu kwa kinywa cha babaetu Daudi, mtumishi wako,
Mbona mataifa wamefanya ghasia, Na makabila wametafakari ubatili? Wafalme wa
dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya
Kristo wake. Maana ni kweli, Herode na Pontio Pilato pamoja na Mataifa na watu
wa Israeli, walikusanyika katika mji huu juu ya Mtumishi wako mtakatifu Yesu,
uliyemtia mafuta, ili wafanye yote ambayo mkono wako na mashauri yako
yamekusudia tangu zamani yatokee. Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao;
ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono wako
kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu.
Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote
wakajaa Roho Mtakatifu, wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.”
-
Maombi
yanaweza kubadilisha mpango mbaya wa Serikali na wafalme – Mfalme Herode
alikuwa na mpango wa kuwaangamiza viongozi wa kanisa, na alimkamata Yakobo na
kumuua na alipoona imewapendeza wayahudi akamkamata na Petro ili naye amuuue vile
vile, maandiko yanatueleza kuwa Kanisa lilimuomba Mungu kwa bidii kwaajili ya
Petro aliyekuwa amefungwa na Mungu alijibu maombi kwa kumtuma malaika wake
aliyemtokea Petro gerezani na kumfungua, hakuna mlango wowote mgumu
utakaofungiwa au mnyororo wowote wa adui unaoweza kushindana na nguvu ya maombi,
maombi yana nguvu dhidi ya wafalme, Maombi yana nguvu dhidi ya serikali, na
yana nguvu dhidi ya magereza yoyote.
Matendo 12:5-11 “Basi
Petro akalindwa gerezani, nalo kanisa likamwomba Mungu kwa juhudi kwa ajili
yake. Hata wakati Herode alipotaka kumtoa, usiku ule ule Petro alikuwa analala
katikati ya askari wawili, amefungwa minyororo miwili; walinzi mbele ya mlango
wakailinda gereza. Mara malaika wa Bwana akasimama karibu naye, nuru ikamulika
mle chumbani, akampiga Petro ubavuni, akamwamsha, akisema, Ondoka upesi.
Minyororo yake ikamwanguka mikononi. Malaika akamwambia, Jifunge, kavae viatu
vyako. Akafanya hivyo. Kisha akamwambia, Jivike nguo yako, ukanifuate. Akatoka
nje, akamfuata; wala hakujua ya kuwa ni kweli yaliyofanywa na malaika; bali
alidhani kwamba anaona maono. Na walipopita lindo la kwanza na la pili, wakaja
hata mlango wa chuma wa kuingilia mjini, ukawafungukia wenyewe. Wakatoka nje,
wakapita katika njia moja; mara malaika akamwacha. Hata Petro alipopata fahamu
akasema, Sasa nimejua yakini ya kuwa Bwana amempeleka malaika wake na kunitoa
katika mkono wa Herode na katika kutazamia kote kwa taifa la Wayahudi.”
-
Maombi
yanaweza kufungua milango ya gereza – Paulo na Sila waliokuwa wakiihubiri
injili walipata matokeo makubwa sana na watu wengi waliokolewa lakini baada ya
kijakazi mmoja kutolewa pepo wa uaguzi bwana zake walikasirika na kuwafanyia
ghasia kubwa sana na hivyo mitume waliwekwa gerezani, na kufungwa katika
mikatale, tunaelezwa kuwa watu hawa waliimba na kumuomba Mungu usiku wa manane
na mara walipofanya hayo tunaelezwa kuwa kila kifungo cha magereza kiliachia
sio wao tu na wafungwa wote na matokeo makubwa ni kuwa hata mkuu wa gereza
aliokolewa na familia yake yote, tunajifunza kuwa hakuna kifungo chochote kiwe
cha kimwili, cha kiroho, cha gereza cha waganga wa kienyeji cha wachawi
kinachoweza kusimama mbele ya maombi, hakuna mtu yeyote awe askari awe mfungwa
ambaye maombi hayana nguvu za kumgusa, kuna nguvu ya ajabu katika kuomba kwa
sababu hiyo kanisa tusipuuzie kuomba kwa kila jambo tuombe, omba kila
unapokutana na changamoto yoyote ile omba omba omba!
Matendo 16:25-31 “Lakini
panapo usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia
nyimbo za kumsifu, na wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza. Ghafula pakawa
tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisika, na mara hiyo milango
ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa. Yule mlinzi wa gereza akaamka, naye
alipoona ya kuwa milango ya gereza imefunguka, alifuta upanga, akataka kujiua,
akidhani ya kuwa wafungwa wamekimbia. Ila Paulo akapaza sauti yake kwa nguvu,
akisema, Usijidhuru, kwa maana sisi sote tupo hapa. Akataka taa ziletwe,
akarukia ndani, akitetemeka kwa hofu, akawaangukia Paulo na Sila; kisha
akawaleta nje akasema, Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka?
Wakamwambia, Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako.”
-
Maombo
yanaweza kubadilisha mpango wa maangamizo – Mungu mwenyewe alikuwa amemtuma
Yona kwamba aende Ninawi na kuuonya mji ule na kuutangazia kuwa baada ya siku
40 ataungamiza, watu wa Ninawi na mfalme wao walipoambiwa kuhusu mpango huo
walimgeukia Mungu wakafunga na kuomba na kumshawishi Mungu kubadili hukumu na
Mungu akaghairi maangamizi aliyokuwa ameyakusudia, maombi ya toba yanaweza
kubadilisha hukumu ya Mungu ya kitaifa na ya mtu mmoja mmoja na kusababisha neema
na rehema za Mungu ziweze kumwagika kwetu.
Yona 3:4 -10 “Yona
akaanza kuuingia mji mwendo wa siku moja, akapaza sauti yake, akasema, Baada ya
siku arobaini Ninawi utaangamizwa. Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu;
wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata
aliye mdogo. Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti
chake cha enzi, akavua vazi lake, akajivika nguo za magunia, na kuketi katika
majivu. Naye akapiga mbiu, akatangaza habari katika mji wa Ninawi, kwa amri ya
mfalme na wakuu wake; kusema, Mwanadamu asionje kitu, wala mnyama wala makundi
ya ng'ombe, wala makundi ya kondoo; wasile, wala wasinywe maji; bali na
wafunikwe nguo za magunia, mwanadamu na mnyama pia, nao wakamlilie Mungu kwa
nguvu, naam, na wageuke, kila mtu akaache njia yake mbaya, na udhalimu ulio
mikononi mwake. Ni nani ajuaye kwamba Mungu hatageuka na kughairi, na kuiacha
hasira yake kali, ili msiangamizwe? Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha
njia yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema
atawatenda; asilitende.”
-
Maombi yana
uwezo wa kubatilisha tangazo la kifo – Katika kifungu chetu cha msingi cha
somo hili tunamuona nabii Isaya akitangaza mauti kwa Mfalme Hezekia, tangazo
hilo nabii Isaya alikuwa amepewa na Mungu, lakini Hezekia alilipuuzia tangazo
hilo na kugeukia ukutani aliomba kwa bidii na kwa kulia machozi na kumkumbusha
Mungu matendo yake ya rehema hata alipokuwa akiomba katikati ya kuomba kwake
Mungu alisema na nabii Isaya kwamba amemuongezea Hezekia miaka 15 ya kuishi
kwake, kumbe kupitia maombi tunaweza kukata rufaa kwa Mungu kwaajili ya tangazo
lolote la hukumu hata kama tangazo hilo au tamko hilo limetoka kwa Bwana
mwenyewe! Tunaweza kumsihi Mungu kwa rehema zake na akafanya kwa maombi
Isaya 38:1-6 “Siku
hizo Hezekia aliugua, akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa
Amozi, akaenda kwa mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya
nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona. Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza
uso wake ukutani, akamwomba Bwana, akasema, Ee Bwana, kumbuka haya, nakusihi, kwamba
nimekwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo
mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana. Ikawa, neno la Bwana likamjia
Isaya, kusema, Enenda ukamwambie Hezekia, Bwana, Mungu wa Daudi, baba yako,
asema hivi, Mimi nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama,
nitaziongeza siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano. Nami nitakuokoa wewe,
na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji huu.”
Hitimisho.
Tunajifunza hapo
kuwa hakuna jambo lolote lililo gumu lisiloweza kubadilishwa kwa maombi, kama
watumishi wa Mungu waliotutangulia waliweza kubatilisha maswala kadhaa wa
kadhaa katika maisha yao na huduma zao kupitia kuomba sisi nasi leo tunaweza
kuliitia jina la Bwana Mungu wetu asiye badilika ambaye ni yeye yule jana leo na
hata milele na tukashuhudia matokeo makubwa katika maisha yetu kwa sababu hiyo
tusiache kuomba tudumu katika maombi siku zote za maisha yetu
Wakolosai 4:2-3 “Dumuni
sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani; mkituombea na sisi
pia, kwamba Mungu atufungulie mlango kwa lile neno lake, tuinene siri ya
Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa”
Karibu na wewe, Mungu wangu, Karibu zaidi
Bwana wangu……
Na Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.
Maoni 1 :
Ameen Pastor
Chapisha Maoni