Mathayo 17:14-21 “Nao walipoufikia mkutano,
mtu mmoja akamjia, akampigia magoti, akisema, Bwana, umrehemu mwanangu, kwa
kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara
nyingi majini. Nikamleta kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya. Yesu akajibu,
akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata
lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. Yesu akamkemea pepo,
naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile. Kisha wale wanafunzi
wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema Mbona sisi hatukuweza kumtoa? Yesu
akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia,
Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa
uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu. [Lakini
namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.]”
Utangulizi:
Katika kifungu chetu cha msingi
wa maandiko leo, tunakutana na kisa chenye kushangaza sana ambapo wanafunzi wa
Yesu walishindwa kumsaidia kijana aliyekuwa anateswa na pepo wa kifafa, Baba wa
kijana alileta mashitaka hayo kwa Yesu kwamba kijana wake amekuwa akisumbuliwa
na pepo hao wa kifafa ambao wakati mwingine wamemtupa kijana wake katika maji
na katika moto, na alipomleta kwa wanafunzi wake wao walishindwa kumtoa, Ndipo
Yesu kwa uchungu mkubwa alitoa agizo lenye uzito “Mleteni huku Kwangu” agizo hili sio agizo la kawaida ni mamlaka ya
kiroho yenye maana pana kwa kila mtu anayetafuta msaada wa kweli.
Mleteni Kwangu!
Ni muhimu kufahamu kuwa ni swala
la kawaida kwamba kila mwanadamu anapopatwa na shida au changamoto zozote zile
zikiwepo changamoto za kiafya huwa anatafuta msaada, na wakati mwingine
wanadamu huwa na tabia ya kupeana taarifa wapi pa kwenda ili changamoto zako ziweze
kutatuliwa, Baba wa kijana huyu anaonekana wazi kukosa Amani kwaajili ya afya
ya mtoto wake ambaye alikuwa anasumbuliwa na Pepo wa kifafa, na huenda
alihangaika sehemu nyingi sana kwaajili ya kujaribu kutatua hali ya kiafya
iliyokuwa ikimkabili kijana wake, hatimaye huenda alisikia habari za Yesu,
lakini wakati huu Yesu alikuwa mlimani pamoja na Petro na Yakobo na Yohana
wanafunzi wengine walibaki, Mzee huyu aliwakabidhi wanafunzi wa Yesu changamoto
za mwanae na wanafunzi walishindwa kushughulika nayo, Yesu alipofika baba wa
kijana alitoa taarifa kwa Yesu na ndipo Yesu alipotoa amri “Mleteni huku kwangu”
Kwanini aletwe kwa Yesu?
Watu wengi sana wanapopatwa na
changamoto za namna mbalimbali kwa kawaida huwa hawampi Yesu nafasi ya Kwanza,
na badala yake huanza kutumia akili zao za kawaida na za kibinadamu katika
kutatua changamoto zinazowakabili na Yesu huwa anapewa nafasi ya mwisho, hii
sio tu kwa wanadamu wa siku za leo, bali hata wakati Bwana Yesu alipokuwa
duniani bado wako watu waliokuwa na changamoto mbalimbali walianza kupeleka
changamoto zao kwa matabibu mbalimbali na kuingia gharama kubwa
Marko 5:25-29 “Na mwanamke mmoja mwenye
kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, na kuteswa mengi kwa mikono ya
matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo,
bali hali yake ilizidi kuwa mbaya aliposikia habari za Yesu, alipita katika
mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake;maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake
tu, nitapona. Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, naye akafahamu mwilini
mwake kwamba amepona msiba ule”
Inawezekana umekuwa ukipitia
changamoto za aina mbalimbali kama mwanadamu katika maisha yako ya kawaida, ni
desturi na jambo la kawaida sana wanadamu kuomba ushauri kwa wanadamu wenzao na
kuelezewa kuwa wajaribu hiki au kile, nenda hospitali hii au ile kamuone
mwanasaikolojia huyu au yule, kamuone daktari huyu au yule, nenda kwa mganga
huyu au yule, changamoto yako hii yuko mama mmoja huyo ni kiboko, changamoto
yako hii inangekuwa kule Sumbawanga ingeshughulikiwa, tatizo lako hili
lingekuwa kule Kwamsisi ni jambo dogo tu, changamoto yako hii ingekuwa kule
Lamu - Mombasa sharifu angekusomea, hili tatizo lingepelekwa kule Korogwe kwa Semangube
lingekuwa kama chai tu, hii kitu kuna wazee kule Kigombe Muheza inaisha na
kadhalika na kadhalik wanadamu wanaweza kukupa ushauri wa kupeleka matatizo
yako huku na kule na ukasumbuka sana kwaajili ya kutafuta uzima, na
ikakugharimu sana, Mzee huyu ambaye alihangaika vile vile kwaajili ya kijana
wake alipeleka changamoto yake huku na kule hospitali za kawaida zilishindwa,
hospitali za rufaa zilishindwa na sasa akawaona wanafunzi wa Yesu ambao nao
vile vile walishindwa!
·
Wanafunzi
wa Yesu walishindwa – Bado walikuwa wanajifunza, Yesu alikuwa amewapa amri
na mamlaka juu ya pepo, lakini walikosa namna na jinsi ya kuachilia nguvu za
Mungu na kuitumia mamlaka hiyo kutoa Pepo, hii ni kwa sababu waliogopa,
walishindwa kuamini na pia walikosa maisha ya kufunga na kuomba na hivyo
mamlaka yao ilikuwa chini, Yesu aliwajulisha kuwa Pepo wana mamlaka za kijeshi
na Pepo wa kifafa (aina hii) wana daraja la juu katika mamlaka za kipepo za
kuwatesa wanadamu na kuwa wanaweza kutolewa kwa maisha ya kufunga na kuomba
Luka 10:17-19. “Ndipo
wale sabini waliporudi kwa furaha, wakisema, Bwana, hata pepo wanatutii kwa
jina lako. Akawaambia, Nilimwona Shetani, akianguka kutoka mbinguni kama umeme.
Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na nge, na nguvu zote za yule adui,
wala hakuna kitu kitakachowadhuru.”
Mathayo 17:17-21 “Yesu
akajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi
hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. Yesu akamkemea
pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile. Kisha wale wanafunzi
wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema Mbona sisi hatukuweza kumtoa? Yesu
akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia,
Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa
uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu. [Lakini
namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.]”
Maisha duni ya
kufunga na kuomba, pamoja na upungufu wa Imani ya wanafunzi wa Yesu ilikuwa ni
sababu ya kushindwa kwao kuwaamuru pepo hawa wa kifafa kumuachia kijana na
kumuweka huru Yesu aliwajulisha baadae tatizo lililokuwako, kwa hiyo
walishindwa kumsaidia, na mzazi aliwashitaki kwa Yesu.
·
Wanafunzi
wa Yesu walikuwa wanadamu – watu wengi sana wanapokuwa na changamoto za
aina mbalimbali katika maisha katika akili zao kichwani kwanza huanza kuwafikiri
wanadamu, wanafikiria mtu atakayewapa muunganiko “connection” mtu wa
kuwaunganishia, wanaelekeza mawazo yao na kuwategemea wanadamu na kama ilivyo
ada Mungu anakuwa chagua la mwisho
Yeremia 17:5-8 “Bwana
asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa
kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana. Maana atakuwa kama fukara nyikani,
Hataona yatakapotokea mema; Bali atakaa jangwani palipo ukame, Katika nchi ya
chumvi isiyokaliwa na watu. Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, Ambaye Bwana
ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, Uenezao
mizizi yake karibu na mto; Hautaona hofu wakati wa hari ujapo, Bali jani lake
litakuwa bichi; Wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, Wala hautaacha
kuzaa matunda.”
·
Yesu
ndiye suluhisho – Ziko shida ambazo madaktari wa kawaida hawawezi
kushughulika nazo, ziko changamoto ambazo wanadamu hawawezi, ziko changamoto
ambazo huwezi kuzidhibiti kwa mifumo ya kidini na kiserikali wala kwa uzoefu
wako na maarifa yako bila kumkaribia Yesu Mwenyewe!
Yeye peke yake
ndiye mwenye mamlaka yote mbinguni na duniani, hata wenye mamlaka na waliopewa
mamlaka wanahitaji kumtegemea Yesu kila wakati, Yesu anapoagiza mleteni huku
kwangu alikuwa anatualika wote kwamba changamoto yoyote kubwa au ndogo
inayokukabili yeye anaweza kushughulika nayo, yeye ndiye mwenye mamlaka yote,
jina lake lina kibali kila mahali, yeye ni mwisho wa matatizo zote, na kuwa
kwake hakuna jambo lisilowezekana, hakuna linaloshindikana kwake, kila kitu
ambacho kimeshindikana kipelekwe kwa Yesu, peleka watoto walioshindikana,
peleka mke aliyeshindikana, peleka mume aliyeshindikana, peleka magonja na
shida na changamoto zote zilizoshindikana kwa sababu Yesu sio wa kawaida !
Mathayo 28:18 “Yesu
akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”
Ufunuo 1:8 “Mimi
ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, asema Bwana Mungu, aliyeko na aliyekuwako
na atakayekuja, Mwenyezi.”
Wafilipi 2:9-11 “Kwa
hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina;
ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani,
na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa
utukufu wa Mungu Baba.”
Hakuna mafanikio
ya kweli unayoweza kuyapata nje ya Yesu Kristo, yeye ndiye mwenye mamlaka yote,
yeye ndiye mwanzo na mwisho Alfa na Omega, yeye kwa jina lake kila kitu
kitapiga goti kiwe cha kuzimu, duniani au mbinguni, kila kitu kimetiishwa chini
yake, mapepo yametiishwa chini yake magonjwa yametiishwa chini yake roho wote
wachafu, falme mamlaka wakuu wa giza na majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu
wa roho yametiishwa chini yake, hakuna shida ambayo yeye hawezi kuitatua, maarifa
yako yanaweza kushindwa wagaganga wako wanaweza kushindwa, washauri wako
wanaweza kukwama, dini yako inaweza kukwama, wanasaikolojia wako wanaweza
kushindwa kukukwamua Lakini Yesu anasema na kutoa mwaliko leo Mleteni huku
kwangu, Yako mambo katika maisha yako huwezi kuyashughulikia, unahangaika kwa
sababu hujawahi kujaribu kwa Yesu, sikiliza mwito wa Mwana wa Mungu yeye
anasema Mleteni huku kwangu, ni mke aliyeshindikana kwa ukorofi, mleteni huku
kwangu, ni mtoto aliyeshindikana kwa ukorofi mleteni huku kwangu, ni mume
aliyetekwa na makahaba mleteni huku kwangu, ni mlevi aliyepindukia kila mtu
amemkataa mleteni huku kwangu, ni huduma yako haieleweki, mleteni huku Kwangu,
ni magonjwa madakatari wameshindwa mleteni huku kwangu, ni mwenye nyumba
mkorofi mleteni huku kwangu, ni bosi mwenye gubu mleteni huku kwangu, ni shida
ya aina yoyote imekushika kooni Yesu anatoa mwaliko mleteni huku kwangu Yesu habadiliki uwezo wake wa kutoa msaada
bado uko pale pale yeye ni yeye yule jana leo na hata milele na hakuna jambo
lililo gumu la kumshinda yeye.Hebu twende mbele za Bwana na kupeleka mahitaji yetu
yote yaliyoshindikana kwake yeye ni mwema atatusaidia.
Waebrania 13:8 “Yesu
Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele.” Luka 1:37 “kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.”
Fanya uamuzi leo, wa kumkabidhi Yesu lolote
linalokusibu na lolote libnalokusumbua katika maisha yako
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni