Jumapili, 13 Julai 2025

Asizimie moyo mtu!


1Samuel 17:32-36 “Daudi akamwambia Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi wako nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake. Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha haya mara nyingi mimi na wewe kama wanadamu huwa tunakutana na changamoto mbali mbali ambazo nyinginezo zinaweza kutuvunja moyo na kutukatisha tamaa, sio hivyo tu pia zinaweza kutuogopesha na kutufanya tupoteze kujiamini au hata kuamini kuwa Mungu anaweza kutusaidia tena, Katika Israel wakati fulani waliwahi kukutana na hali kama hii unayoipitia wewe, walikuwa katika vita na wafilisti, na katika jeshi la wafilisti alijitokeza mtu mmoja mkubwa sana mwenye nguvu na mwenye kutisha ambaye alizungumza maneno ya propaganda za kivita na kuwatia hofu sana wana wa Israel kiasi ambacho jeshi lote la Israel wakiongozwa na Sauli mfalme wao waliogopa na kuzimia moyo, Neno “Asizimie” katika Lugha ya kiebrania linasomeka kama “Nรขphal” ambalo kwa kiingereza ni “fall” limetumika hivyo mara 318 likimaanisha kuanguka, au kupoteza matumaini, au kushuka chini kutoka katika hali yake ya awali, kwa Kiswahili kuvunjika moyo yaani asivunjike moyo mtu awaye yote  unapokutana na changamoto.

1Samuel 17:1-11 “Wakati huo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwa vita, nao wakakusanyika huko Soko, ulio mji wa Yuda, wakatua kati ya Soko na Azeka, katika Efes-damimu. Naye Sauli na watu wa Israeli wakakusanyika, wakatua katika bonde la Ela, nao wakapanga vita juu ya hao Wafilisti. Wafilisti wakasimama juu ya mlima upande huu, na Waisraeli wakasimama juu ya mlima upande huu, napo palikuwa na hilo bonde katikati. Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. Na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana.”

Kutokana na maneno ya shujaa huyo wa wafilisti mwenye kutisha sana Israel waliogopa na kuzimia moyo, ni jambo la kawaida wakati mwingine kwamba linapotokea jambo la kutisha kutokana na propaganda za kishetani huwa tunasahau uweza wa Mungu na ukuu wake na kuitazama ile changamoto huku tukijiuliza kama tunaweza kutokaje katika changamoto hiyo, unajiuliza nitatoboa kweli au safari hii ndio nafariki, nitatokaje katika ugonjwa huu, nawezaje kukabiliana na deni hili kubwa namna hii, aibu inakaribia, nawezaje kutoka katika matatizo haya na kwa sababu ya utisho wa hali inayotuzunguka ni rahisi kwetu kuvunjika moyo au kuzimia moyo, Kijana mdogo sana katika Israel Daudi alisimama kwa ujasiri na kuwatia moyo taifa zima ya kuwa asizimie moyo mtu! Kwani yeye atapambana na hali inayowakabili kwa jina la Mungu wa Israel!. Leo kila changamoto unayokabiliana nayo, kila ukuta unaosimama kama kikwazo katika maisha yako, kila mlima na jaribu, na mateso, na ugonjwa na majini na mapepo na nguvu za giza zinazosimama kama changamoto katika maisha yako ambazo zimekufanya ukazimia moyo kwa jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai tunakwenda kukabiliana nazo na kuzisambaratisha kabisa haleluyaa Asizimie moyo mtu!.Tutajifunza somo hili Asizimie Moyo mtu kwa kuzuingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Sababu za watu kuzimia moyo!

·         Asizimie moyo mtu!

·         Kwanini asizimiye moyo mtu!

Sababu za watu kuzimia moyo!

Ni ukweli uliokuwa wazi kuwa Israel kama ilivyo kwa watu wengine walikuwa wamevunjika moyo na kuzimia kabisa kwa woga, mazingira waliokuwa wanakabiliana nayo, yalikuwa ni magumu na yenye kuogopesha sana, propaganda za kivita zilikuwa zimewatia hofu na kuwachosha, Goliath alikuwa akijitokeza kila siku asubuhi na jioni kwa siku 40 akiwatukana na kuwatisha sana, jambo lilolopelekea jeshi zima na mashujaa wakubwa wakiwepo kaka zake Daudi na mfalme Sauli kutishika na kufadhaika sana, Goliathi aliyatukana majeshi ya Israel waziwazi, hadharani kila mtu akishuhudia!

1Samuel 17:10-16 “Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana. Basi Daudi alikuwa mwana wa yule Mwefrathi, wa Bethlehemu ya Yuda, aliyeitwa jina lake Yese; naye huyo alikuwa na wana wanane; na yeye mwenyewe alikuwa mzee siku za Sauli, na mkongwe miongoni mwa watu. Nao wale wana watatu wa Yese waliokuwa wakubwa walikuwa wamefuatana na Sauli kwenda vitani, na majina ya hao wanawe watatu waliokwenda vitani ni haya, mzaliwa wa kwanza Eliabu, na wa pili wake Abinadabu, na wa tatu Shama. Naye huyo Daudi alikuwa mdogo wa wote; na hao watatu waliokuwa wakubwa wakafuatana na Sauli. Basi Daudi alikuwa akienda kwa Sauli na kurudi ili awalishe kondoo za baba yake huko Bethlehemu. Naye yule Mfilisti hukaribia asubuhi na jioni, akajitokeza siku arobaini.”

Sisi nasi katika maisha yetu tunaweza kufadhaika na kutishika na hata kuvunjika moyo kutokana na uhalisia wa changamoto, ni ukweli uliokuwa wazi kuwa Golitahi lilikuwa jitu kubwa lenye nguvu na uzoefu wa kivita, na jeshi lote la Israel lilimuogopa, yako mambo ambayo yakikupata wewe mwenyewe na hata wataalamu wanaweza kukubaliana kuwa ni jambo zito na kubwa, ikiwa una ukimwi, ikiwa una sukari, ikiwa umepatwa na kiharusi, ikiwa una kansa ya damu, ikiwa una changamoto ya ini, kansa, figo, changamoto za mfumo wa fahamu, umeme katika mwili, moyo na kadhalika ni magonjwa ya kutisha ambayo hata wataalamu wa afya wenyewe wanayaogopa na una historia yake namna na jinsi yalivyoua watu mbalimbali kwenye jamii yako, familia yako na hata majirani, changamoto za mikopo umiza, madeni ya aibu, kufilisika, hasara za namna mbalimbali, kutapeliwa fedha nyingi, kuporomoka kwa biashara, hali mbaya ya kiuchumi, kutokujitosheleza kwa mahitaji mbalimbali na umasikini wa kutisha vinaweza kuwa sababu ya kuzimia moyo, Sio hivyo tu maneno unayoyasikia kutoka upande wa upinzani au wa adui yako na wakati mwingine wanaweza hata kusema kuhusu Mungu wako kwamba tuone kama Mungu wake anaweza kumsaidia hivyo vyote vinaweza kukufanya ukazimia moyo, wakati unapokuwa katika changamoto kali na ngumu sana maneno ya adui zako yanaweza kukuumiza sana, na hata maneno ya wale watu usiowatarajia, kama wapendwa wenzetu, Yesu alipokuwa msalabani adui zale walisema pia kuhusu Mungu kwamba amemtegemea Mungu na amwokoe sasa Msalabani nasi tutamwamini maneno ya kuumiza!

Mathayo 27:40-43. “Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani.Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe. Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.”

Hatupaswi kamwe kukosa imani na kuvunjika moyo au kuzimia moyo wala kuyatazama mazingira na badala yake tunapaswa kumwangalia Mungu ambaye ni mkubwa kuliko changamoto yako, Daudi kamwe hakukubali kuwa na aibu ya kitaifa na wala hakukubali Mungu wake adhalilike na ndugu zake waaibike, akiwa amejaaa Imani, uzoefu, ujuzi kuhusu Mungu na ujasiri mkubwa ambao wengi walikuwa wameupoteza yeye alisema atapambana na hali hiyo na kwa sababu hiyo asizimie moyo mtu, usizimie moyo kwaajili ya ugonjwa wako, usizimie moyo kwaajili ya adui zako, usizimie moyo kwaajili ya umasikini wako, usizimie moyo kwaajili ya changamoto na matatizo ya kifamilia, haijalishi adui anatisha kwa kiwango gani sisi tutamjia kwa jina la Bwana Mungu wa Israel aliye hai.

Asizimie moyo mtu!

Wakati kila mtu akiwa ameingiwa na hofu fadhaa na kukata tamaa au kuzimia Moyo, Daudi alikuwa na mtazamo tofauti na wengine Yeye alikuwa amejifunza kuwa Mungu ni mkubwa kuliko changamoto ya aina yoyote ile, alikuwa amejifunza na kupata uzoefu na shuhuda namna na jinsi Mungu alivyompa ushindi dhidi ya  wanyama wakali wenye nguvu kuliko binadamu wanyama kama Dubu, Simba na kadhalika alitambua kuwa Mungu alikuwa pamoja naye hata alipokuwa akiwachunga kondoo wa baba yake na kwa sababu hiyo Golitahi kwake lilikuwa ni jambo dogo sana wala sio la kufadhaisha mtu na hivyo aliwapa tumani watu wote pamoja na mfalme Asizimie moyo mtu!

1Samuel 17:34-37 “Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai. Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe.”

Daudi aliamini kuwa sio kwa nguvu za kibinadamu atamkabili Goliath lakini ni kwa nguvu za Mungu na kwa msaada wa Mungu, alikumbuka shuhuda za ukuu wa Mungu na matendo yake na uaminifu wake, alitambua jinsi jina la Mungu linavyopaswa kutakaswa na kutukuzwa na alijua ya kuwa kwa jina hilo hakuna kinachoweza kusimama, alifahamu ya kuwa Mungu hawezi kutukanwa wala kudhalilishwa na jeuri na kiburi cha kibinadamu na kisha akakubali, Daudi alitambua kuwa kutukanwa kwa majeshi ya Mungu aliye hai ni kutukanwa kwa Mungu kwa hiyo alitaka kuitetea heshima ya Mungu, Daudi alitambua kuwa ushindi wake ni ushindi wa kitaifa na sio wa mtu mmoja na kuwa kushindwa kwa Goliathi ni kushindwa kwa wafilisti wote, Ni ukweli uliowazi katika ulimwengu wa roho vita ya Daudi na Goliati ilikuwa inawakilisha vita ya Yesu Kristo na Shetani, yule atakayeshindwa atakuwa mtumwa wa yule atakayeshindwa na watu wake na yule atakayeshinda atatawala yeye na watu wake kila mtu aliyeokoka ni mshindi kupitia ushindi wa Yesu Kristo, wakati Goliathi akiwa na kofia ya chuma na mabamba ya chuma kila mahali Daudi yeye hakuwa na kizuizi chochote na alikuwa na silaha laini yaani manati-kombeo na mawe matano tu laini

1Samuel 17:45-47.”Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya Bwana, naye atawatia ninyi mikononi mwetu.”

Wakati Goliathi alikuwa akitema propaganda tu na vitisho kwa kujiamini kwa kiburi na majivuno, Daudi alikuwa akizitamka shuhuda za Mungu na ukweli wa neno lake Mungu na uweza wake, ni ukweli ulio wazi kuwa siku ile Daudi alimpiga Goliathi na kwa kutumia upanga wa Goliathi mwenyewe alikata kichwa chake, tukio hili liliwapa nguvu Israel na waliwakimbiza wafilisti na kuwachinja kama walivyotaka na kujikusanyia nyara:-

1Samuel 17:48-52 “Ikawa, hapo Mfilisti alipojiinua, akaenda akamkaribia Daudi, ndipo Daudi naye akapiga mbio, akalikimbilia jeshi ili akutane na yule Mfilisti. Daudi akatia mkono wake mfukoni, akatwaa humo jiwe moja, akalitupa kwa kombeo lake, akampiga Mfilisti katika kipaji cha uso; jiwe hilo likamwingilia kipajini, akaanguka chini kifudifudi. Hivyo Daudi akamshinda yule Mfilisti kwa kombeo na jiwe, akampiga Mfilisti, akamwua; walakini Daudi hakuwa na upanga mkononi mwake. Ndipo Daudi akapiga mbio, akasimama juu ya Mfilisti, akautwaa upanga wake, akaufuta alani mwake, akamwua, akamkata kichwa kwa upanga huo. Nao Wafilisti walipoona ya kuwa shujaa wao amekufa, wakakimbia. Nao watu wa Israeli na wa Yuda wakainuka, na kupiga kelele, nao wakawafuata Wafilisti mpaka ufikapo Gathi, na mpaka malango ya Ekroni. Nao majeruhi wa Wafilisti wakaanguka kando ya njia iendayo Shaarimu, mpaka Gathi, na mpaka Ekroni.”  
           

Kwanini asizimiye moyo mtu!

Daudi alikuwa na ufahamu kuwa ushindi wake hautokani na yeye mwenyewe bali ushindi wake unatokana na Mungu, sisi nasi hatuna budi kufahamu kwamba ushindi wetu unapatikana kupitia Yesu Kristo ambaye alishinda kifo na mauti, ushindi wowote tulio nao na tutakaokuwa nao ni ushindi unaotokana na ushindi wake Kristo Yesu mwana wa Daudi.  

1Wakorintho 15:57 “Lakini Mungu na ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo.”

Maandiko yanatukumbusha tu kuwa hakuna changamoto kubwa kuliko Mungu wetu, kila mtu aliyeokolewa na anayemtegemea Mungu anapaswa kumtegemea Mungu na kumfanya kuwa ngao yake na kinga yake, tunapaswa kuwa na ujasiri na kuacha kupoteza matumaini, hatupaswi kamwe kuzimia moyo kama tumemfanya Bwana kuwa ngao yetu, hatupaswi kulia wala kufadhaika maana Mungu ndiye wokovu wetu, na ngome yetu na hakuna wa kutukaribia wala kutudhuru vyovyote vile!

Zaburi 27:1-3 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Maandiko yanatukumbusha kuwa Mungu hutumia mambo manyonge sana, wakati ambapo Goliath anaonekana kuwa na silaha bora, mkuki mkubwa na uzoefu mkubwa vitani, huku mwili wake umezingirwa na mambamba ya shaba Daudi alikuwa ni kijana mdogo, mzuri macho mekundu lakini alijikinga kwa jina la Mungu na kumfanya Mungu kuwa tumaini lake, hii inatukumbusha kuwa Mungu anaweza kutumia chochote na kumtumia mtu yeyote bila kujali hali yake, historia yake na muonekano wake wa nje, unyonge wake au kupuuzwa kwake, Mungu hutumia vilivyodharaulika!  

1Wakorintho 1:26-29 “Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.”

Maandiko yanatukumbusha kuwa Mungu ni mwaminifu na kuwa tunapokabiliana na changamoto za aina yoyote katika maisha yetu na tukumbuke namna na jinsi alivyotusaidia katika mambo mengine kumbuka matendo yake ya kale na hii itamuimarisha kila mmoja wetu kujua kuwa Mungu yule yule asiyebadilika aliyewasaidia baba zetu katika vita zao atajitokeza tena kwa namna nyingine kutusaidia

Zaburi 77:11-14 “Nitayakumbuka matendo ya Bwana; Naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote; Nitaziwaza habari za matendo yako. Ee Mungu, njia yako i katika utakatifu; Ni nani aliye mungu mkuu kama Mungu? Wewe ndiwe Mungu ufanyaye maajabu; Uliudhihirisha uweza wako kati ya mataifa.”

Ee Bwana usimuache msomaji wangu, na msikilizaji wangu na kila mtu duniani anayekutegemea wewe, usimwache akazimia moyo wakati wa taabu yake lakini umpe moyo wa ujasiri kama Daudi na nutupe ushindi katika vita zetu za maisha katika jina la Yesu Kristo amen!

Na. Rev Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 6 Julai 2025

Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!

 


1Timotheo 1:15-16 “Na neema ya Bwana wetu ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi. Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.”




Utangulizi:

Ni muhimu kujikumbusha kuwa Yesu Kristo mwana wa Mungu alikuja duniani kwa kusudi la kutafuta na kuokoa kile kilichopotea, Maisha yake na huduma yake pamoja na mafundisho yake yalileta mabadiliko makubwa sana ya kiroho na kijamii na uadilifu katika maisha ya watu wengi, mtu mmoja mmoja na jamii kwa ujumla.

Luka 19:2-10 “Na tazama, palikuwa na mtu, jina lake Zakayo, mkubwa mmoja katika watoza ushuru, naye ni tajiri. Huyu alikuwa akitafuta kumwona Yesu ni mtu wa namna gani, asiweze kwa sababu ya umati wa watu, maana ni mfupi wa kimo. Akatangulia mbio, akapanda juu ya mkuyu apate kumwona, kwa kuwa atakuja kuipitia njia ile. Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako. Akafanya haraka, akashuka, akamkaribisha kwa furaha. Hata watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi.Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne. Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Alipokuwa duniani Yesu alijichanganya na kuwaendea wenye dhambi kwa upendo heshima na kwa unyenyekevu mkubwa sana na kuwafanya wao wampende na kumkubali, aliyabadilisha maisha yao wakati mwingine wala sio kwa kuhubiri kwa nguvu bali kwa kuwaonyesha upendo na kuwajali hususani wale waliokuwa wamekataliwa na kuonekana kuwa hawafai, wapinzani wake wa kidini walimshutumu sana wakifiri ya kuwa alikuwa ni  nabii aliyekosa kiasi kwa kuwa alikaa na kula na kuongea na wenye dhambi, majibu yake kwa wapinzani wake yalikuwa yamejaa hekima neema na mshangazo mkubwa sana kwani pia yalionyesha kuwa alikuwa na ujuzi na mpango mkakati aliokuja nao ambao ni kuleta tiba kwa wenye dhambi ambao walikuwa wakitubu kwa njia nyepesi sana na kupokea muujiza mkubwa muujiza wa mabadiliko ya kitabia akijibainisha hivyo Yesu alisema

Luka 5:29-32 “Na Lawi akamfanyia karamu kubwa nyumbani mwake; palikuwa na mkutano mkuu wa watoza ushuru na watu wengineo waliokuwa wameketi chakulani pamoja nao. Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.”

Majibu yake Yesu na maneno yake na matendo yanadhihirisha wazi kuwa Yesu Kristo alikuja duniani akiwa na mpango na mkakati wa kuleta mabadiliko makubwa kwa jamii, Yesu anasifiwa kama mojawapo ya wanafalsafa wakubwa sana duniani lakini moja ya sifa yake kubwa inayomtofautisha na wanafalsafa wengine ni uwezo wake wa kubadilisha maisha ya watu, kwa muda wa miaka zaidi ya 2000 kumekuwepo na wanafunzi wengi sana wa Bwana Yesu na wanaoonyesha msimamo na mabadiliko makubwa ya kimaisha ya wale waliokutwa na mafundisho yake hii maana yake ni kwamba hata pamoja na kuwa amepaa mbinguni habari zake njema zimekuwa njema na dawa ya kipekee kwa jamii kwa hiyo ni wazi kuwa mtu yeyote ayayehitaji mabadiliko ya mtindo wa maisha na ikawa imeshindikana sehemu nyingine anamuhitaji Yesu,  na sisi nasi kama watumishi wake hatuna budi kumuuza Yesu kwa kumtangaza na kumuhubiri katika jamii kwaajili ya mabadiliko ya kweli ya jamii yetu “Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!”, tutajifunza somo hili Yesu kwa mabadiliko ya jamii kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Yesu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.

·         Mifano ya watu waliokutana na Yesu na kubadilika.

·         Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!.


Yesu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea

Kama tulivyoona katika utangulizi wa somo hili ya kuwa Yesu Kristo alikuja duniani akiwa na mpango mkakati ulio wazi ambao ni kuokoa kile kilichopotea, Kimsingi Yesu alikuja kusamehe watu dhambi na kuyabadili maisha yao kabisa, alitajwa mapema katika maandiko kwamba yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao na pamoja na matokeo hasi yaliyosababishwa na dhambi

Mathayo 1:21-23 “Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao. Hayo yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii akisema, Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi.”

Luka 19:9-10 “Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu.Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Watu wote duniani wanafahamu kuwa ni makosa kumteda Mungu dhambi na ndani ya mioyo yao wanajua na wako ambao wanajitahidi kwa jitihada zao za kidini na kiimani lakini wanashindwa, dhambi ni adui mkubwa wa mwanadamu analeta hatia na kuondoa ujasiri katika moyo, Dhambi pia inaweza ikakufanya uishi kinafiki bila kupenda, inatawala na kuwafanya watu kuwa watumwa. Dhambi ni adui yetu mkubwa kama alivyo shetani tu, tangu anguko la mwanadamu duniani asili ya mwanadamu imeathiriwa na dhambi na kwa sababu hiyo wanadamu hawawezi kufanya yale wanayoyapenda ikiwa ni pamoja na kumpendeza Mungu, umasikini wa kiroho  na ukosefu wa tumaini umeingia, uhusiano na Mungu umeingia mashakani na mwanadamu anapotea akijiona, Ni Yesu Kristo peke yake aliyekuja kurejesha tumaini hilo, Ni yeye pekee aliyekuja kuonyesha upendo wa Mungu kwetu  na kwa njia ya msalaba aliikamilisha kazi hiyo pana kwa sababu hiyo sasa mlango uko wazi kwa jamii nzima, waliokataliwa, walevi, wachawi, makahaba, wagonjwa, na jamii nzima inayotumikishwa bila kupenda tunapaswa kuitumia huruma ya Mungu wetu kwa kuukubali upendo wake na kazi yake aliyoifanya pale msalabani ili tusipotee, wajibu wetu mkubwa ni kumwamini na tukimwamini hatutapotea na badala yake tutakuwa na uzima wa milele.

Yohana 3:16-18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Mifano ya watu waliokutana na Yesu na kubadilika.

Alipokuwa duniani mwokozi Yesu Kristo alisababisha mabadiliko makubwa sana ambayo yanaendelea mpaka leo kila inapohubiriwa injili na watu wakaikubali, Yesu alikuwa Mwalimu wa kipekee ambaye hakufundisha tu bali mafundisho yake yalikuwa na nguvu na mamlaka yakiambatana na uwezo mkubwa wa kubadilisha maisha ya watu hata wale waliokuwa wagumu kufikika, Yesu alibadilisha kila mtu aliyekutana naye na akawapa maisha mapya na hapa iko mifano kadhaa:-

1.       Paulo mtume - alikuwa moja ya watu hatari sana mtu mwenye msimamo mkali katika dini yake aliyekuwa anaiona imani ya kikrito kama imani potofu na inayoharibu mila na tamaduni za kiyahudi kwa hiyo alitumia nguvu zake zote kuipinga na kuipiga vita imani hii, alisimamia mauaji ya Stephano, na kwa hiyari yake aliomba kibali kwa kuhani mkuu kuwafuatia na kuwakamata watu wote wa njia hii yaani (Waliookoka) na kuwaburuza na kuwatia ndani.

 

Matendo 7:16-18 “Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli.Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu.Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.”

 

Matendo 9:1-5 “Lakini Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana, akamwendea Kuhani Mkuu, akataka ampe barua za kuenda Dameski zilizoandikwa kwa masinagogi, ili akiona watu wa Njia hii, waume kwa wake, awafunge na kuwaleta Yerusalemu. Hata alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, mbona waniudhi? Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe.”

 

Mtume Paulo aliyekuwa wa ajabu na adui mkubwa sana wa ukristo alipokutana na Yesu mabadiliko makubwa sana yalitokea maishani mwake na uadui wake dhidi ya Yesu Kristo na kanisa lake ulifikia mwisho na badala ya kuhukumiwa kuuawa Yesu alimuamuru kuwa chombo chake cha kuihubiri injili na akawa mtu mwenye bidii na juhudi kubwa na kuleta mchango mkubwa sana katika jamii, yeye anakumbuka jinsi Mungu alivyomuokoa na baadaye maisha yake yakawa kielelezo kwa jamii ya wakati ule na sasa.

 

1Timotheo 1:154-16 “Na neema ya Bwana wetu ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi. Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.”

 

2.       Mwanamke msamaria – Alikuwa ni mwanamke ambaye ametengwa na jamii kwa sababu ya maisha yake ya aibu, hata muda wake wa kutembea na kwenda kuteka maji ulikuwa ni muda wa tofauti na wanawake wenzake kijijini, Yesu alipokutana naye alizungumza naye moja kwa moja na akaweza kushughulika na hali yake ya kiroho kimwili na kisaikolojia alimponya na kuitimiza kiu yake ya kuhitaji maji ya uzima, baada ya muda mfupi wa kukutana na Yesu na kuzungumza naye na kumfunulia yaliyokuwa yakiendelea moyoni mwake mwanamke huyu aligeuka muhubiri wa injili ambaye aliwavuta wengi kuja kwa Yesu maisha yake  yalibadilika na kupitia yeye jamii yake pia ilipata mwanga wa injili na giza likaondoka katika mji wao.

 

Yohana 4:3-42 “aliacha Uyahudi, akaenda zake tena mpaka Galilaya. Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria. Basi akafika kunako mji wa Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu mwanawe. Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita. Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe. Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.) Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu; basi umeyapata wapi hayo maji yaliyo hai? Je! Wewe u mkubwa kuliko baba yetu, Yakobo, aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akanywa maji yake, na wanawe pia, na wanyama wake? Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena;  walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka. Yesu akamwambia, Nenda kamwite mumeo, uje naye hapa. Yule mwanamke akajibu, akasema, Sina mume. Yesu akamwambia, Umesema vema, Sina mume; kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako; hapo umesema kweli. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii! Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia. Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli. Yule mwanamke akamwambia, Najua ya kuwa yuaja Masihi, (aitwaye Kristo); naye atakapokuja, yeye atatufunulia mambo yote. Yesu akamwambia, Mimi ninayesema nawe, ndiye. Mara hiyo wakaja wanafunzi wake, wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke; lakini hakuna aliyesema, Unatafuta nini? Au, Mbona unasema naye? Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akawaambia watu, Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo? Basi wakatoka mjini, wakamwendea. Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule. Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi. Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula?  Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake. Hamsemi ninyi, Bado miezi minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. Naye avunaye hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja. Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli, Mmoja hupanda akavuna mwingine. Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao. Na katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda. Basi wale Wasamaria walipomwendea, walimsihi akae kwao; naye akakaa huko siku mbili. Watu wengi zaidi wakaamini kwa sababu ya neno lake. Wakamwambia yule mwanamke, Sasa tunaamini, wala si kwa sababu ya maneno yako tu; maana sisi tumesikia wenyewe, tena twajua ya kuwa hakika huyu ndiye Mwokozi wa ulimwengu.”

 

Ushuhuda wa mwanamke msamaria unatukumbusha kazi ya Yesu ya kubadilisha jamii, na tunajifunza jinsi ambavyo hata mtu mmoja tu aliyedharauliwa na kukataliwa katika jamii na ambaye anaonekana hafai anaweza kabisa kubadilika na kusababisha mabadiliko makubwa kwa jamii, Yesu anabadilisha maisha, Yesu anabadilisha tabia, Yesu anabadilisha jamii.

 

3.       Mathayo yule mtoza ushuru – Watoza ushuru walikuwa  mojawapo ya kundi lililochukiwa na watu katika jamii ya wayahudi, kwanza wakihesabika kama wasaliti kwa sababu walitoza kodi watu wa taifa lao kwa niaba ya taifa la kigeni au la kikoloni la Warumi, lakini pia walionekana kama kundi la watu wenye kudhulumu au wezi kwa sababu walijikusanyia mali kwa dhuluma au kujitajirisha kwa fedha za haramu, kwa hiyo mafarisayo waliwaweka katika kundi moja la watu najisi na wasiofaa  na kudharaulika au kuonekana kama ni wadhambi ona

 

Luka 18:9-14 “Akawaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote. Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.”

 

Tofauti na mafarisayo ambao waliwabagua sana watoza ushuru na kujihesabia haki Yesu yeye aliwaendea na kuwafanya rafiki zake akila na kufurahi pamoja nao ili hatimaye awabadilishe maisha yao akiwepo Mathayo ambaye baadaye Yesu alimtumia kuandika injili

 

Mathayo 9:9-13 “Naye Yesu alipokuwa akipita kutoka huko aliona mtu ameketi forodhani, aitwaye Mathayo, akamwambia, Nifuate. Akaondoka, akamfuata. Ikawa alipoketi nyumbani ale chakula, tazama, watoza ushuru wengi na wenye dhambi walikuja wakaketi pamoja na Yesu na wanafunzi wake. Mafarisayo walipoona, waliwaambia wanafunzi wake, Mbona mwalimu wenu anakula pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Naye aliposikia, aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi. Lakini nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka; kwa maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi.”

Mifano hii inatuthibitishia na kutuonyesha ya kwamba ni Yesu peke yake anayeweza kuleta mabadiliko ya kweli katika jamii, na ni mabadiliko yanayoanzia moyoni na yasiyo na unafiki yanayotokana na njia yake ya kuuendea ulimwengu kwa upendo na huruma na nguvu za Mungu, kwa hiyo kupitia upendo wake huu aliweza kuwafikishia watu maisha mapya bila kutumia nguvu aliwagusa watu kwa neema yake na upendo wake  na kuwapa maisha mapya yaliyoathiri jamii zao, hakuna mtume wala nabii yeyote ambaye alikuwa au amakuwa na uwezo wa kuyabadili maisha ya watu wake na kuwafanya kuwa wema kama ilivyo kwa Bwana wetu Yesu Kristo!.

Kwa msingi huo tunajifunza ya kwamba hata sasa tunaweza kumpeleka Yesu kwa jamii na kumnadi kama biashara inayoweza kuleta mabadiliko ya kila aina katika maisha yetu, Yesu atabadilisha maisha ya watu kutoka kwenye uhalifu kuwa watu wema, kutoka kuwa wavuvi wa samaki kuwa wavuvi wa watu, kutoka kwenye kundi la kudharaulika kwenda kwenye kundi la kuheshimika na kutoka kwenye huzuni kwenda kwenye furaha, kanisa nini tunapaswa kukifanya ni kuuza bidhaa Yesu na kuitangaza kwa ajili ya mabadiliko ya jamii!, Kama alivyobadilisha wengine anaweza kumbadilisha yeyote  yule hata ambaye anaonekana kushindikana katika jamii, kama unaona ya kuwa jamii ni kama imekuchoka kwa maneno na matendo yako Jaribu Yesu Kristo leo na utafurahi

Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!

Katika jamii hii tuliyo nayo ambayo inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na ufisadi, ukosefu wa haki, dhuluma uhalifu, umasikini, unyonge, mmomonyoko wa maadili, kukata tamaa na msongo wa mawazo dunia inahitaji sana ujumbe wa Yesu Kristo ambao ndio pekee unaobaki kuwa tiba ya kweli ya changamoto hizi ni lazima tuwapelekee watu bidhaa hii na kuinadi kwao, Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii, ni yeye pekee ambaye anatoa mwaliko wa kuwapoza watu wote wenye kuelemewa na mizigo na kutoa ahadi ya kweli kwamba atawapumzisha!

Mathayo 11:28-30 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”

Yesu anauwezo wa kubadilisha mioyo ya wanadamu wote katika jamii mabadiliko ya watu kama mwanamke msamaria, mabadiliko ya watu walioshikilia dini zao kama Paulo na mabadiliko ya watu waliokataliwa na jamii kama kina Mathayo na Zakayo na mwanamke Msamaria,  tukiwakutanisha na watu wa jinsi hiyo na Yesu watapewa pumziko la kweli na maisha ya haki upendo na huruma zake

Kila mwanadamu aliyepoteza tumaini na kukata tamaa katika jamii na anayehitaji kushinda changamoto za kila siku za maisha ni aelewe na ajuzwe kuwa ni Yesu Kristo pekee anayeweza kurejesha matumaini hayo, yeye pekee huelekeza watu kuishi maisha ya haki na kutoa mwongozo wa maisha yanayoweza kubadilisha jamii, hutumii nguvu zako kubadilika Ni Yesu anatumia damu yake na neema yake na trehema zake kukubadilisha wewe unacho kihitaji ni Yesu tu!

Kwa hiyo ni lazima tumuhubiri Yesu na kumpeleka Yesu kwa jamii yenye changamoto za aina mbalimbali tunaelezwa kuwa nyakati za kanisa la kwanza wahubiri hawakuwa na ujumbe mwingine zaidi walimuhubiri Yesu Kristo hawakuhubiri watu wala madhehebu yao wala makanisa yao lakini walimuhubiri Yesu Kristo; Muhubiri Yesu tangaza bidhaa hii ieleze jamii Yesu Kristo kwa mabadiliko, tukitaka kuwapelekea watu furaha ya kweli wapelekee Yesu, wahubiri watu kuhusu Yesu waelekeze watu kwa Yesu, wape watu bidhaa iitwayo Yesu Kristo; Yesu ndio sera inayouzika kuliko sera nyingine hakuna mbadala  wa Yesu, Damu yake inatakasa, yeye mwenyewe yuko hai ameketi mkono wa kuume wa Mungu waelezee watu kuhusu Yesu; Yesu anaokoa, Yesu anaponya, Yesu anabadilisha maisha analeta tumaini, Yesu anatakasa, Yesu anasamehe, Yesu habadiliki, Yesu haukumu mtu,Yesu ni mwaminifu, Yesu amejaa neema na rehema na huruma hakua kama Yesu; Yesu ni yeye yule jana leo na hata milele, tumuuze Yesu, tumnadi yetu, Tangaza uza bidhaa Yesu kwa mabadiliko ya jamii

Matendo 8:5-8 “Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, AKAWAHUBIRI KRISTO. Na makutano kwa nia moja wakasikiliza maneno yale yaliyosemwa na Filipo walipoyasikia na kuziona ishara alizokuwa akizifanya. Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa. Ikawa furaha kubwa katika mji ule.” 

Yesu Kristo alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea, na ni kupitia maisha yake na huduma yake na kazi yake aliyoifanya pale msalabani alibadilisha maisha ya watu na anabadilisha maisha ya watu hata leo ikiwa jamii yoyote inahitaji Amani na furaha basi jamii hiyo inapaswa kumpokea Yesu, upendo wake, kujali kwake huruma yake na nguvu zake ziko kutusaidia jamii yetu kwa sasa inamuhitaji  Yesu zaidi kuliko kitu kingine chochote atawaokoa na kuwasamehe na kuwapoza mioyo yao na kuwaletea nyakati za kuburudishwa, na kuwapoza mioyo yao na kuishusha mizigo yao!

Zaburi 107:13-15 “Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao. Aliwatoa katika giza na uvuli wa mauti, Akayavunja mafungo yao. Na wamshukuru Bwana kwa fadhili zake, Na maajabu yake kwa wanadamu.”

2Wakorintho 5:17 “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.”

Haijalishi maisha yako yameharibiwa kwa kiasi gani, haijalishi ulirogwa kwa mchawi gani, haijalishi adui zako wametambikia kwa kiwango gani,  kutano moja tu na Bwana Yesu litabadilisha maisha yako na mabadiliko makubwa yatakuwa ushahidi kwako, unamuhitaji Yesu kwa mabadiliko ya maisha yako leo,  mpe Yesu maisha yako na hutakuwa mtu yule tena, maisha yoyote bila Yesu ni maisha yasiyokamilika,  maisha yoyote bila Yesu ni maisha yenye kusikitisha sana, Maisha yoyote bila Yesu ni maisha yenye upungufu, Kila mmoja wetu anamuhitaji Yesu, tunamuhitaji hata kwa ushindi wa vita zetu, tunamuhitaji pia kwaajili ya maisha yetu yajayo, tunamuhitaji katika ndoa zetu, kazini kwetu, biashara zetu, masomo yetu  na popote, yeye hubadilisha maisha! Jaribu leo!, omba sala hii pamoja nami endapo liko eneo katika maisha yako unahitaji mabadiliko! Tuombe!

Bwana kama iekupendeza wewe kutubadilisha sisi, Basi nakuomba tufanye kuwa mtu yule ambaye ungependa tuwe, tunatamani kubadilika, kwa sababu hiyo mpe neema kila mmoja kuwa vile upendavyo wewe, nakushukuru kwa sababu utawabadilisha wengi, hata Msomaji wangu na msikilizaji wangu utampa kuona wema wako, asante kwa sababu utafanya zaidi ya jinsi nilivyokuomba kwa unyenyekevu mkubwa katika jina la Yesu Kristo Amen!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima