Jumapili, 6 Julai 2025

Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!

 


1Timotheo 1:15-16 “Na neema ya Bwana wetu ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi. Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.”




Utangulizi:

Ni muhimu kujikumbusha kuwa Yesu Kristo mwana wa Mungu alikuja duniani kwa kusudi la kutafuta na kuokoa kile kilichopotea, Maisha yake na huduma yake pamoja na mafundisho yake yalileta mabadiliko makubwa sana ya kiroho na kijamii na uadilifu katika maisha ya watu wengi, mtu mmoja mmoja na jamii kwa ujumla.

Luka 19:2-10 “Na tazama, palikuwa na mtu, jina lake Zakayo, mkubwa mmoja katika watoza ushuru, naye ni tajiri. Huyu alikuwa akitafuta kumwona Yesu ni mtu wa namna gani, asiweze kwa sababu ya umati wa watu, maana ni mfupi wa kimo. Akatangulia mbio, akapanda juu ya mkuyu apate kumwona, kwa kuwa atakuja kuipitia njia ile. Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako. Akafanya haraka, akashuka, akamkaribisha kwa furaha. Hata watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi.Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne. Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Alipokuwa duniani Yesu alijichanganya na kuwaendea wenye dhambi kwa upendo heshima na kwa unyenyekevu mkubwa sana na kuwafanya wao wampende na kumkubali, aliyabadilisha maisha yao wakati mwingine wala sio kwa kuhubiri kwa nguvu bali kwa kuwaonyesha upendo na kuwajali hususani wale waliokuwa wamekataliwa na kuonekana kuwa hawafai, wapinzani wake wa kidini walimshutumu sana wakifiri ya kuwa alikuwa ni  nabii aliyekosa kiasi kwa kuwa alikaa na kula na kuongea na wenye dhambi, majibu yake kwa wapinzani wake yalikuwa yamejaa hekima neema na mshangazo mkubwa sana kwani pia yalionyesha kuwa alikuwa na ujuzi na mpango mkakati aliokuja nao ambao ni kuleta tiba kwa wenye dhambi ambao walikuwa wakitubu kwa njia nyepesi sana na kupokea muujiza mkubwa muujiza wa mabadiliko ya kitabia akijibainisha hivyo Yesu alisema

Luka 5:29-32 “Na Lawi akamfanyia karamu kubwa nyumbani mwake; palikuwa na mkutano mkuu wa watoza ushuru na watu wengineo waliokuwa wameketi chakulani pamoja nao. Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.”

Majibu yake Yesu na maneno yake na matendo yanadhihirisha wazi kuwa Yesu Kristo alikuja duniani akiwa na mpango na mkakati wa kuleta mabadiliko makubwa kwa jamii, Yesu anasifiwa kama mojawapo ya wanafalsafa wakubwa sana duniani lakini moja ya sifa yake kubwa inayomtofautisha na wanafalsafa wengine ni uwezo wake wa kubadilisha maisha ya watu, kwa muda wa miaka zaidi ya 2000 kumekuwepo na wanafunzi wengi sana wa Bwana Yesu na wanaoonyesha msimamo na mabadiliko makubwa ya kimaisha ya wale waliokutwa na mafundisho yake hii maana yake ni kwamba hata pamoja na kuwa amepaa mbinguni habari zake njema zimekuwa njema na dawa ya kipekee kwa jamii kwa hiyo ni wazi kuwa mtu yeyote ayayehitaji mabadiliko ya mtindo wa maisha na ikawa imeshindikana sehemu nyingine anamuhitaji Yesu,  na sisi nasi kama watumishi wake hatuna budi kumuuza Yesu kwa kumtangaza na kumuhubiri katika jamii kwaajili ya mabadiliko ya kweli ya jamii yetu “Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!”, tutajifunza somo hili Yesu kwa mabadiliko ya jamii kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Yesu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.

·         Mifano ya watu waliokutana na Yesu na kubadilika.

·         Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!.


Yesu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea

Kama tulivyoona katika utangulizi wa somo hili ya kuwa Yesu Kristo alikuja duniani akiwa na mpango mkakati ulio wazi ambao ni kuokoa kile kilichopotea, Kimsingi Yesu alikuja kusamehe watu dhambi na kuyabadili maisha yao kabisa, alitajwa mapema katika maandiko kwamba yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao na pamoja na matokeo hasi yaliyosababishwa na dhambi

Mathayo 1:21-23 “Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao. Hayo yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii akisema, Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi.”

Luka 19:9-10 “Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu.Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Watu wote duniani wanafahamu kuwa ni makosa kumteda Mungu dhambi na ndani ya mioyo yao wanajua na wako ambao wanajitahidi kwa jitihada zao za kidini na kiimani lakini wanashindwa, dhambi ni adui mkubwa wa mwanadamu analeta hatia na kuondoa ujasiri katika moyo, Dhambi pia inaweza ikakufanya uishi kinafiki bila kupenda, inatawala na kuwafanya watu kuwa watumwa. Dhambi ni adui yetu mkubwa kama alivyo shetani tu, tangu anguko la mwanadamu duniani asili ya mwanadamu imeathiriwa na dhambi na kwa sababu hiyo wanadamu hawawezi kufanya yale wanayoyapenda ikiwa ni pamoja na kumpendeza Mungu, umasikini wa kiroho  na ukosefu wa tumaini umeingia, uhusiano na Mungu umeingia mashakani na mwanadamu anapotea akijiona, Ni Yesu Kristo peke yake aliyekuja kurejesha tumaini hilo, Ni yeye pekee aliyekuja kuonyesha upendo wa Mungu kwetu  na kwa njia ya msalaba aliikamilisha kazi hiyo pana kwa sababu hiyo sasa mlango uko wazi kwa jamii nzima, waliokataliwa, walevi, wachawi, makahaba, wagonjwa, na jamii nzima inayotumikishwa bila kupenda tunapaswa kuitumia huruma ya Mungu wetu kwa kuukubali upendo wake na kazi yake aliyoifanya pale msalabani ili tusipotee, wajibu wetu mkubwa ni kumwamini na tukimwamini hatutapotea na badala yake tutakuwa na uzima wa milele.

Yohana 3:16-18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Mifano ya watu waliokutana na Yesu na kubadilika.

Alipokuwa duniani mwokozi Yesu Kristo alisababisha mabadiliko makubwa sana ambayo yanaendelea mpaka leo kila inapohubiriwa injili na watu wakaikubali, Yesu alikuwa Mwalimu wa kipekee ambaye hakufundisha tu bali mafundisho yake yalikuwa na nguvu na mamlaka yakiambatana na uwezo mkubwa wa kubadilisha maisha ya watu hata wale waliokuwa wagumu kufikika, Yesu alibadilisha kila mtu aliyekutana naye na akawapa maisha mapya na hapa iko mifano kadhaa:-

1.       Paulo mtume - alikuwa moja ya watu hatari sana mtu mwenye msimamo mkali katika dini yake aliyekuwa anaiona imani ya kikrito kama imani potofu na inayoharibu mila na tamaduni za kiyahudi kwa hiyo alitumia nguvu zake zote kuipinga na kuipiga vita imani hii, alisimamia mauaji ya Stephano, na kwa hiyari yake aliomba kibali kwa kuhani mkuu kuwafuatia na kuwakamata watu wote wa njia hii yaani (Waliookoka) na kuwaburuza na kuwatia ndani.

 

Matendo 7:16-18 “Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli.Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu.Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.”

 

Matendo 9:1-5 “Lakini Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana, akamwendea Kuhani Mkuu, akataka ampe barua za kuenda Dameski zilizoandikwa kwa masinagogi, ili akiona watu wa Njia hii, waume kwa wake, awafunge na kuwaleta Yerusalemu. Hata alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, mbona waniudhi? Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe.”

 

Mtume Paulo aliyekuwa wa ajabu na adui mkubwa sana wa ukristo alipokutana na Yesu mabadiliko makubwa sana yalitokea maishani mwake na uadui wake dhidi ya Yesu Kristo na kanisa lake ulifikia mwisho na badala ya kuhukumiwa kuuawa Yesu alimuamuru kuwa chombo chake cha kuihubiri injili na akawa mtu mwenye bidii na juhudi kubwa na kuleta mchango mkubwa sana katika jamii, yeye anakumbuka jinsi Mungu alivyomuokoa na baadaye maisha yake yakawa kielelezo kwa jamii ya wakati ule na sasa.

 

1Timotheo 1:154-16 “Na neema ya Bwana wetu ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi. Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.”

 

2.       Mwanamke msamaria – Alikuwa ni mwanamke ambaye ametengwa na jamii kwa sababu ya maisha yake ya aibu, hata muda wake wa kutembea na kwenda kuteka maji ulikuwa ni muda wa tofauti na wanawake wenzake kijijini, Yesu alipokutana naye alizungumza naye moja kwa moja na akaweza kushughulika na hali yake ya kiroho kimwili na kisaikolojia alimponya na kuitimiza kiu yake ya kuhitaji maji ya uzima, baada ya muda mfupi wa kukutana na Yesu na kuzungumza naye na kumfunulia yaliyokuwa yakiendelea moyoni mwake mwanamke huyu aligeuka muhubiri wa injili ambaye aliwavuta wengi kuja kwa Yesu maisha yake  yalibadilika na kupitia yeye jamii yake pia ilipata mwanga wa injili na giza likaondoka katika mji wao.

 

Yohana 4:3-42 “aliacha Uyahudi, akaenda zake tena mpaka Galilaya. Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria. Basi akafika kunako mji wa Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu mwanawe. Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita. Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe. Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.) Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu; basi umeyapata wapi hayo maji yaliyo hai? Je! Wewe u mkubwa kuliko baba yetu, Yakobo, aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akanywa maji yake, na wanawe pia, na wanyama wake? Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena;  walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka. Yesu akamwambia, Nenda kamwite mumeo, uje naye hapa. Yule mwanamke akajibu, akasema, Sina mume. Yesu akamwambia, Umesema vema, Sina mume; kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako; hapo umesema kweli. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii! Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia. Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli. Yule mwanamke akamwambia, Najua ya kuwa yuaja Masihi, (aitwaye Kristo); naye atakapokuja, yeye atatufunulia mambo yote. Yesu akamwambia, Mimi ninayesema nawe, ndiye. Mara hiyo wakaja wanafunzi wake, wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke; lakini hakuna aliyesema, Unatafuta nini? Au, Mbona unasema naye? Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akawaambia watu, Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo? Basi wakatoka mjini, wakamwendea. Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule. Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi. Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula?  Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake. Hamsemi ninyi, Bado miezi minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. Naye avunaye hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja. Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli, Mmoja hupanda akavuna mwingine. Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao. Na katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda. Basi wale Wasamaria walipomwendea, walimsihi akae kwao; naye akakaa huko siku mbili. Watu wengi zaidi wakaamini kwa sababu ya neno lake. Wakamwambia yule mwanamke, Sasa tunaamini, wala si kwa sababu ya maneno yako tu; maana sisi tumesikia wenyewe, tena twajua ya kuwa hakika huyu ndiye Mwokozi wa ulimwengu.”

 

Ushuhuda wa mwanamke msamaria unatukumbusha kazi ya Yesu ya kubadilisha jamii, na tunajifunza jinsi ambavyo hata mtu mmoja tu aliyedharauliwa na kukataliwa katika jamii na ambaye anaonekana hafai anaweza kabisa kubadilika na kusababisha mabadiliko makubwa kwa jamii, Yesu anabadilisha maisha, Yesu anabadilisha tabia, Yesu anabadilisha jamii.

 

3.       Mathayo yule mtoza ushuru – Watoza ushuru walikuwa  mojawapo ya kundi lililochukiwa na watu katika jamii ya wayahudi, kwanza wakihesabika kama wasaliti kwa sababu walitoza kodi watu wa taifa lao kwa niaba ya taifa la kigeni au la kikoloni la Warumi, lakini pia walionekana kama kundi la watu wenye kudhulumu au wezi kwa sababu walijikusanyia mali kwa dhuluma au kujitajirisha kwa fedha za haramu, kwa hiyo mafarisayo waliwaweka katika kundi moja la watu najisi na wasiofaa  na kudharaulika au kuonekana kama ni wadhambi ona

 

Luka 18:9-14 “Akawaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote. Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.”

 

Tofauti na mafarisayo ambao waliwabagua sana watoza ushuru na kujihesabia haki Yesu yeye aliwaendea na kuwafanya rafiki zake akila na kufurahi pamoja nao ili hatimaye awabadilishe maisha yao akiwepo Mathayo ambaye baadaye Yesu alimtumia kuandika injili

 

Mathayo 9:9-13 “Naye Yesu alipokuwa akipita kutoka huko aliona mtu ameketi forodhani, aitwaye Mathayo, akamwambia, Nifuate. Akaondoka, akamfuata. Ikawa alipoketi nyumbani ale chakula, tazama, watoza ushuru wengi na wenye dhambi walikuja wakaketi pamoja na Yesu na wanafunzi wake. Mafarisayo walipoona, waliwaambia wanafunzi wake, Mbona mwalimu wenu anakula pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Naye aliposikia, aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi. Lakini nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka; kwa maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi.”

Mifano hii inatuthibitishia na kutuonyesha ya kwamba ni Yesu peke yake anayeweza kuleta mabadiliko ya kweli katika jamii, na ni mabadiliko yanayoanzia moyoni na yasiyo na unafiki yanayotokana na njia yake ya kuuendea ulimwengu kwa upendo na huruma na nguvu za Mungu, kwa hiyo kupitia upendo wake huu aliweza kuwafikishia watu maisha mapya bila kutumia nguvu aliwagusa watu kwa neema yake na upendo wake  na kuwapa maisha mapya yaliyoathiri jamii zao, hakuna mtume wala nabii yeyote ambaye alikuwa au amakuwa na uwezo wa kuyabadili maisha ya watu wake na kuwafanya kuwa wema kama ilivyo kwa Bwana wetu Yesu Kristo!.

Kwa msingi huo tunajifunza ya kwamba hata sasa tunaweza kumpeleka Yesu kwa jamii na kumnadi kama biashara inayoweza kuleta mabadiliko ya kila aina katika maisha yetu, Yesu atabadilisha maisha ya watu kutoka kwenye uhalifu kuwa watu wema, kutoka kuwa wavuvi wa samaki kuwa wavuvi wa watu, kutoka kwenye kundi la kudharaulika kwenda kwenye kundi la kuheshimika na kutoka kwenye huzuni kwenda kwenye furaha, kanisa nini tunapaswa kukifanya ni kuuza bidhaa Yesu na kuitangaza kwa ajili ya mabadiliko ya jamii!, Kama alivyobadilisha wengine anaweza kumbadilisha yeyote  yule hata ambaye anaonekana kushindikana katika jamii, kama unaona ya kuwa jamii ni kama imekuchoka kwa maneno na matendo yako Jaribu Yesu Kristo leo na utafurahi

Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!

Katika jamii hii tuliyo nayo ambayo inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na ufisadi, ukosefu wa haki, dhuluma uhalifu, umasikini, unyonge, mmomonyoko wa maadili, kukata tamaa na msongo wa mawazo dunia inahitaji sana ujumbe wa Yesu Kristo ambao ndio pekee unaobaki kuwa tiba ya kweli ya changamoto hizi ni lazima tuwapelekee watu bidhaa hii na kuinadi kwao, Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii, ni yeye pekee ambaye anatoa mwaliko wa kuwapoza watu wote wenye kuelemewa na mizigo na kutoa ahadi ya kweli kwamba atawapumzisha!

Mathayo 11:28-30 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”

Yesu anauwezo wa kubadilisha mioyo ya wanadamu wote katika jamii mabadiliko ya watu kama mwanamke msamaria, mabadiliko ya watu walioshikilia dini zao kama Paulo na mabadiliko ya watu waliokataliwa na jamii kama kina Mathayo na Zakayo na mwanamke Msamaria,  tukiwakutanisha na watu wa jinsi hiyo na Yesu watapewa pumziko la kweli na maisha ya haki upendo na huruma zake

Kila mwanadamu aliyepoteza tumaini na kukata tamaa katika jamii na anayehitaji kushinda changamoto za kila siku za maisha ni aelewe na ajuzwe kuwa ni Yesu Kristo pekee anayeweza kurejesha matumaini hayo, yeye pekee huelekeza watu kuishi maisha ya haki na kutoa mwongozo wa maisha yanayoweza kubadilisha jamii, hutumii nguvu zako kubadilika Ni Yesu anatumia damu yake na neema yake na trehema zake kukubadilisha wewe unacho kihitaji ni Yesu tu!

Kwa hiyo ni lazima tumuhubiri Yesu na kumpeleka Yesu kwa jamii yenye changamoto za aina mbalimbali tunaelezwa kuwa nyakati za kanisa la kwanza wahubiri hawakuwa na ujumbe mwingine zaidi walimuhubiri Yesu Kristo hawakuhubiri watu wala madhehebu yao wala makanisa yao lakini walimuhubiri Yesu Kristo; Muhubiri Yesu tangaza bidhaa hii ieleze jamii Yesu Kristo kwa mabadiliko, tukitaka kuwapelekea watu furaha ya kweli wapelekee Yesu, wahubiri watu kuhusu Yesu waelekeze watu kwa Yesu, wape watu bidhaa iitwayo Yesu Kristo; Yesu ndio sera inayouzika kuliko sera nyingine hakuna mbadala  wa Yesu, Damu yake inatakasa, yeye mwenyewe yuko hai ameketi mkono wa kuume wa Mungu waelezee watu kuhusu Yesu; Yesu anaokoa, Yesu anaponya, Yesu anabadilisha maisha analeta tumaini, Yesu anatakasa, Yesu anasamehe, Yesu habadiliki, Yesu haukumu mtu,Yesu ni mwaminifu, Yesu amejaa neema na rehema na huruma hakua kama Yesu; Yesu ni yeye yule jana leo na hata milele, tumuuze Yesu, tumnadi yetu, Tangaza uza bidhaa Yesu kwa mabadiliko ya jamii

Matendo 8:5-8 “Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, AKAWAHUBIRI KRISTO. Na makutano kwa nia moja wakasikiliza maneno yale yaliyosemwa na Filipo walipoyasikia na kuziona ishara alizokuwa akizifanya. Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa. Ikawa furaha kubwa katika mji ule.” 

Yesu Kristo alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea, na ni kupitia maisha yake na huduma yake na kazi yake aliyoifanya pale msalabani alibadilisha maisha ya watu na anabadilisha maisha ya watu hata leo ikiwa jamii yoyote inahitaji Amani na furaha basi jamii hiyo inapaswa kumpokea Yesu, upendo wake, kujali kwake huruma yake na nguvu zake ziko kutusaidia jamii yetu kwa sasa inamuhitaji  Yesu zaidi kuliko kitu kingine chochote atawaokoa na kuwasamehe na kuwapoza mioyo yao na kuwaletea nyakati za kuburudishwa, na kuwapoza mioyo yao na kuishusha mizigo yao!

Zaburi 107:13-15 “Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao. Aliwatoa katika giza na uvuli wa mauti, Akayavunja mafungo yao. Na wamshukuru Bwana kwa fadhili zake, Na maajabu yake kwa wanadamu.”

2Wakorintho 5:17 “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.”

Haijalishi maisha yako yameharibiwa kwa kiasi gani, haijalishi ulirogwa kwa mchawi gani, haijalishi adui zako wametambikia kwa kiwango gani,  kutano moja tu na Bwana Yesu litabadilisha maisha yako na mabadiliko makubwa yatakuwa ushahidi kwako, unamuhitaji Yesu kwa mabadiliko ya maisha yako leo,  mpe Yesu maisha yako na hutakuwa mtu yule tena, maisha yoyote bila Yesu ni maisha yasiyokamilika,  maisha yoyote bila Yesu ni maisha yenye kusikitisha sana, Maisha yoyote bila Yesu ni maisha yenye upungufu, Kila mmoja wetu anamuhitaji Yesu, tunamuhitaji hata kwa ushindi wa vita zetu, tunamuhitaji pia kwaajili ya maisha yetu yajayo, tunamuhitaji katika ndoa zetu, kazini kwetu, biashara zetu, masomo yetu  na popote, yeye hubadilisha maisha! Jaribu leo!, omba sala hii pamoja nami endapo liko eneo katika maisha yako unahitaji mabadiliko! Tuombe!

Bwana kama iekupendeza wewe kutubadilisha sisi, Basi nakuomba tufanye kuwa mtu yule ambaye ungependa tuwe, tunatamani kubadilika, kwa sababu hiyo mpe neema kila mmoja kuwa vile upendavyo wewe, nakushukuru kwa sababu utawabadilisha wengi, hata Msomaji wangu na msikilizaji wangu utampa kuona wema wako, asante kwa sababu utafanya zaidi ya jinsi nilivyokuomba kwa unyenyekevu mkubwa katika jina la Yesu Kristo Amen!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni: