Jumapili, 27 Julai 2025

Mungu anaposhika Kalamu!

 

Esta 3:8-11 “Basi Hamani akamwambia mfalme Ahasuero, Kuna taifa moja waliotawanyika na kukaa mahali mahali katikati ya mataifa walioko katika majimbo yote ya ufalme wako. Nao sheria zao zimefarakana na sheria za kila taifa; wala hawazishiki amri za mfalme; kwa hiyo haimpasi mfalme kuchukuliana nao. Basi, mfalme akiona vema, na iandikwe kwamba waangamizwe; nami nitalipa talanta kumi elfu za fedha mikononi mwao watakaosimamia shughuli hiyo, waziweke katika hazina ya mfalme. Ndipo mfalme alipoivua pete yake mkononi, akampa Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, adui ya Wayahudi. Kisha mfalme akamwambia Hamani, Hiyo fedha umepewa, na watu pia, fanya uonavyo vema.”

 


Utangulizi:

Mungu anaposhika kalamu ni usemi wa fumbo (Metaphor)  unaotumika kuelezea uwezo na utendaji wa Mungu katika kuamua mambo ya kitaifa, ulimwengu au mtu mmoja mmoja kuhusiana na mpango wake wa baadaye, Mungu ndiye mshika dau wa maisha ya kila mtu na anayeujua mwanzo na mwisho wa mtu au anayeamua kuwa hatima ya mtu itakuwaje, uweza wake huo hauwezi kuingiliwa wala kuathiriwa na mpango wowote wa kibinadamu wala Shetani, wakati wote yeye ndiye hubakia kuwa mwenye hatima ya mwisho wa kila mtu, familia, taifa na ulimwengu!, Hakuna mwanadamu, wala serikali wala ufalme wala mamlaka yenye uwezo wa kuamua hatima yako itakuwaje isipokuwa Mungu peke yake! Ni yeye peke yake ndiye anayetuwazia mema kwa sababu yeye ndiye aliye tuumba na kwa sababu hiyo anajua hatima yetu na sababu ya yeye kutuumba! Ameandika kila kitu kutuhusu hakuna wa kufuta.

Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.”

Kwa bahati mbaya wako watu duniani ambao hufiriki ya kuwa wao wanaweza kuamua hatima ya maisha yako au maisha yetu au kwamba hatima ya taifa letu iko mikononi mwao, na kwa sababu hiyo kwa kutumia nafasi waliyo nayo wakati mwingine wameweza kuingilia na kujaribu kuzuia au kuwakwamisha watu wengine katika mpango wa Mungu wakidhani kwa mawazo mafupi kuwa wao wanaweza kufanya hivyo, Lakini hatimaye Mungu huingilia kati na kubadilisha mambo ni mpango wake peke yake unaoweza kuhitimisha mambo kinyume na matarajio na mipango ya wanadamu ni wazo lake na shauri lake na kusudi lake pekee linaloweza kusimama.

Zaburi 33:8-11 “Nchi yote na imwogope Bwana, Wote wakaao duniani na wamche. Maana Yeye alisema, ikawa; Na Yeye aliamuru, ikasimama. Bwana huyabatilisha mashauri ya mataifa, Huyatangua makusudi ya watu. Shauri la Bwana lasimama milele, Makusudi ya moyo wake vizazi na vizazi.”

Leo basi tutachukua muda mfupi, kujifunza kwa kina na mapana ujumbe huu wa muhimu “Mungu anaposhika kalamu”na tutajifunza ujumbe huu kwa kuzingatia vipengele viwili muhimu vifuatavyo:-

·         Njama za kuharibiwa kwa hatima yako.

·         Mungu anaposhika kalamu.


Njama za kuharibiwa kwa hatima yako

Katika dunia hii iliyojaa iliyojawa na watu wenye chuki, uadui, uchawi, wivu, hasira, faraka uzushi, husuda, ulafi, tamaa mbaya, chuki zisizo hata na sababu majungu na fitina, kuharibiana na kuchafuana, kuwindana na kutafutana watu wanaweza kwa sababu au hata bila sababu kukutafutia namna ya kukutengenezea hatima mbaya, adui zako watatamani wakati wote wasikie unaharibikiwa na mambo yako hayaendi na wakati mwingine watakusudia uwe na hatima mbaya hata kinyume na mapenzi ya Mungu, watatamani kuona ndoto zako, maono yako na matamanio yako uliyopewa na Mungu hayatimii kwa mbinu na hila za kibinadamu, kwa hiyo unaweza kuwekewa mpango mkakati na watu ili wahakikishe ya kuwa mambo yako yanakwama, kama haya yanakukuta hilo sio jambo geni kwako wala kwetu, maandiko yanatutia moyo kuwa tusione kuwa ni ajabu tunapopatwa na changamoto za aina mbalimbali

1Petro 4:12-13 “Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio kati yenu, unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho. Lakini kama mnavyoyashiriki mateso ya Kristo, furahini; ili na katika ufunuo wa utukufu wake mfurahi kwa shangwe.”

Nyakati za Biblia walikuweko watu kama wewe na wanadamu kama wewe waliokutana na changamoto kama zako watu wakiwakusudia kuwakwamisha kwaajili ya maslahi yao au kwa sababu ya husuda ya kitu cha kiungu ambacho Mungu amekiweka ndani yako:-

1.       Yusufu – Mungu alimpa ndoto kubwa za maisha yake ya baadae,  na ya nduguze lakini sio hivyo tu alipata kibali kwa Mungu na kwa baba yake, Mungu alimpenda Yusufu na alikuwa pamoja naye, lakini pia baba yake alimpenda sana na Mungu alimpa Yusufu ndoto kuhusu hatima yake lakini hata hivyo nduguze walichukizwa na ndoto hizo na kuanza kula njama ya kutaka kumuangamiza.

 

Mwanzo 37:2-11 “Hivi ndivyo vizazi vya Yakobo. Yusufu, aliyekuwa mwenye miaka kumi na saba, alikuwa akichunga kondoo pamoja na ndugu zake; naye alikuwa kijana pamoja na wana wa Bilha, na wana wa Zilpa, wake wa baba yake. Yusufu akamletea baba yao habari zao mbaya. Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani. Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”

 

Ni jambo la kushangaza kwamba Yusufu alichukiwa na ndugu zake na sio kumchukia tu walimuhusudu walikuwa na wivu wenye uchungu mkubwa dhidi yake na kwa sababu ya ndoto zake walihakikisha wanaweka mkakati wa kummaliza ili waone ndoto zake zitatimiaje yaani walitaka kumuua!

 

Mwanzo 37:13-20 “Israeli akamwambia Yusufu, Je! Ndugu zako hawachungi kondoo katika Shekemu? Njoo, nikutume kwao. Akamwambia, Mimi hapa. Akamwambia, Enenda, basi, ukaone kama ndugu zako hawajambo, na kundi nalo li salama, ukaniletee habari. Basi akampeleka kutoka bonde la Hebroni, akafika Shekemu. Mtu mmoja akamkuta, naye alikuwa anazunguka-zunguka katika nyika; yule mtu akamwuliza, akisema, Unatafuta nini? Akasema, Nawatafuta ndugu zangu; tafadhali uniambie mahali wanakochunga. Yule mtu akasema, Wametoka hapa, maana niliwasikia wakisema, Twendeni Dothani. Basi Yusufu akawafuata ndugu zake akawakuta huko Dothani. Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake.”

 

Wanadamu bila kufahamu kuwa Mungu alikwisha kumuandikia mtumishi wake Yusufu kuwa atakuwa mkuu, wao walikuwa wakijaribu kuandika kinyume na kile ambacho Mungu alikuwa amekikusudia kwa Yusufu, ndugu yangu hayo unayoyapitia ni kuwa wanadamu wanataka kujaribu kuandika hitoria yako kinyume na kile ambacho Mungu amekikusudia katika maisha yako!

 

2.       Daniel – Alifanyiwa njama na Mawaziri wenzake  baada ya kuwa ameinuliwa sana na Mungu na kupata kibali kwa mfalme ambaye aliamua kumuweka juu sana katika madaraka ya nchi ya uhamishoni, Mawaziri wa kikaldayo walikuwa na mpango wa kuharibu hatima ya Daniel na kwa kuwa alikuwa na uadilifu walikosa sababu, wakaona watumie njama ya kuzuia maombi kwa Mungu aliye hai, jambo ambalo lingesababisha Daniel ashindwe na kupata sababu ya kumhukumu kwa hiyo mawaziri waliandika mswada na kuupitisha

 

Daniel 6:1-16 “Ilimpendeza Dario kuweka juu ya ufalme maliwali mia na ishirini, wawe juu ya ufalme wote; na juu yao akaweka wakubwa watatu, na Danieli alikuwa mmoja wao; ili maliwali hawa watoe hesabu kwao, mfalme asipate hasara. Basi Danieli huyo alipata sifa kuliko wakubwa na maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake; naye mfalme akaazimu kumweka juu ya ufalme wote. Basi mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za kumshitaki Danieli kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala hatia ndani yake. Ndipo wale watu wakasema, Hatutapata sababu ya kumshitaki Danieli huyo, tusipoipata katika mambo ya sheria ya Mungu wake. Basi wale mawaziri na maamiri wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia hivi, Mfalme Dario, uishi milele. Mawaziri wote wa ufalme, na manaibu, na maamiri, na madiwani, na maliwali wamefanya shauri pamoja ili kuweka amri ya kifalme; na kupiga marufuku, ya kwamba mtu ye yote atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme atatupwa katika tundu la simba. Sasa, Ee mfalme, piga marufuku, ukatie sahihi maandiko haya, yasibadilike, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi, isiyoweza kubadilika. Basi mfalme Dario akayatia sahihi maandiko yale, na ile marufuku. Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake. Ndipo wakakaribia, wakasema mbele ya mfalme katika habari ya ile marufuku ya mfalme; Je! Hukuitia sahihi ile marufuku, ya kwamba kila mtu atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme, atatupwa katika tundu la simba? Mfalme akajibu, akasema, Neno hili ni kweli, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi isiyoweza kubadilika. Basi wakajibu, wakasema mbele ya mfalme, Yule Danieli, aliye mmoja wa wana wa wale waliohamishwa wa Yuda, hakujali wewe, Ee mfalme, wala ile marufuku uliyoitia sahihi, bali aomba dua mara tatu kila siku. Basi mfalme aliposikia maneno haya alikasirika sana, akakaza moyo wake ili kumponya Danieli; akajitaabisha kumwokoa hata jua likachwa. Ndipo watu wale wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia mfalme, Ee mfalme, ujue ya kuwa ni sheria ya Wamedi na Waajemi, lisibadilike neno lo lote lililo marufuku, wala amri yo yote iliyowekwa na mfalme. Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya.”

 

3.       Wayahudi waliokuwa uhamishoni – Mungu alikuwa amewabarikia sana wayahudi waliokuwa utumwani, wao walikuwa na moyo ule ule wa kumcha Mungu wakiwa wamejifunza kwamba kupitia kuabudu miungu mingine wao walihukumiwa kwenda utumwani kwa hiyo wayahudi waliokuwa uhamishoni hawakutaka kuabudu sanamu wala mtu waliipeleka heshima yote kwa Mungu, Kwa sababu hiyo Hamani ambaye alikuwa amemchukia Modrekai kwa sababu alikuwa hainami mbele zake aliamua kupitisha mswada bungeni ili kwamba ipitishwe sheria ya kuwaangamiza wayahudi wote na hivyo waliandika mswada wa maangamizi

 

Esta 3:8-11 “Basi Hamani akamwambia mfalme Ahasuero, Kuna taifa moja waliotawanyika na kukaa mahali mahali katikati ya mataifa walioko katika majimbo yote ya ufalme wako. Nao sheria zao zimefarakana na sheria za kila taifa; wala hawazishiki amri za mfalme; kwa hiyo haimpasi mfalme kuchukuliana nao. Basi, mfalme akiona vema, na iandikwe kwamba waangamizwe; nami nitalipa talanta kumi elfu za fedha mikononi mwao watakaosimamia shughuli hiyo, waziweke katika hazina ya mfalme. Ndipo mfalme alipoivua pete yake mkononi, akampa Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, adui ya Wayahudi. Kisha mfalme akamwambia Hamani, Hiyo fedha umepewa, na watu pia, fanya uonavyo vema.”

 

Hata hivyo katika namna isiyoweze kuelezeka sheraia za waamedi na waajemi zilikuwa zikipitishwa haikuwa kitu rahisi kubatilisha isipokuwa tu kama Mungu ataingilia kati kwani sharia zao zikipita zimepita

 

Esta 8:8 “Basi waandikieni Wayahudi pia vyo vyote mpendavyo, kwa jina la mfalme, mkatie muhuri kwa pete ya mfalme; kwa kuwa andiko lililoandikwa kwa jina la mfalme na kutiwa muhuri kwa pete ya mfalme hakuna awezaye kulitangua.”

 

4.       Yesu Kristo – Ambaye alishitakiwa kwa husuda na wakuu wa makuhani ili tu kumsambaratisha na wakidhani kwa kufanya hizo njama watakuwa wamemmaliza kabisa, aliandikiwa hati ya hukumu ya kufa msalabani

 

Mathayo 27:17-20 “Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda. Na alipokuwa ameketi juu ya kiti cha hukumu, mkewe alimpelekea mjumbe, kumwambia, Usiwe na neno na yule mwenye haki; kwa sababu nimeteswa mengi leo katika ndoto kwa ajili yake. Nao wakuu wa makuhani na wazee wakawashawishi makutano ili wamtake Baraba, na kumwangamiza Yesu.”

 

Wakati mwingine adui zako watafanya njama na kukushambulia kwa hila na njia mbalimbali ilimradi tu wahakikishe kuwa wanakupoteza au wanaharibu hatima yako kama tunavyoona katika mifano hiyo hapo juu katika maandiko, ndugu msomaji wangu na msikilizaji wangu inawezekana kuwa mara kadhaa na wewe unaweza kuwa umekutana na changamoto za aina mbalimbali ambazo zote zinalenga kumaliza au kuharibu hatima yako au hata kukuua kwa makusudi yale yale ya kuua kitu cha kiungu ambacho kimewekwa ndani yako! Lakini hata hivyo uzoefu wa kimaandiko unaonyesha ya kuwa Mungu huingilia kati na kubadilisha mambo pale anaposhika kalamu yake. Mungu huwaacha wanadamu waandike miswada yao kisha yeye kama mfalme wa wafalme huitangua, Mungu anaposhika kalamu historia yote na matarajio yote ya adui hubatilika

Mungu anaposhika kalamu.

Mungu anaposhika kalamu maana yake Mungu anauwezo wa kubadili historia ya mambo, wanadamu na shetani wanapokusudia kuharibu na kusitisha kile kitu ambacho Mungu amekiweka ndani yako au kuharibu hatima yako na kukupakazia ubaya au kukukusudia ubaya Mungu anauwezo wa kubadili historia ya mambo mabaya na kuigeuza kujwa njema, au uwezo wa kubadili maji machungu kuwa matamu, anauwezo wa kuandika upya hatima yako ya familia yako na taifa lako na hata ulimwengu kwa ujumla, Mungu anauwezo wa kurejesha heshima ambayo imeharibiwa, ana uwezo wa kuharibu mipango mibaya ya adui na kuifanya kuwa myema au kupitia mpango huo mbaya akatokeza jambo jema kwa uwezo wake mkuu na kwa mkono wake wa nguvu ulionyooshwa

Warumi 8:28-30 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza.”

Yusufu aliyefanyiwa njama na kaka zake ili kwamba ndoto zake zisitimie Mungu aliitumia njia iiliyoonekana kuwa ya uchungu na ya kuumiza kuleta wokovu kwa taifa zima, Mungu alibadili hatima mbaya iliyokusudiwa na wanadamu kutimiza hatima yeke iliyokusudiwa na yeye Mungu anaposhika kalamu mambo hubadilika.  

Mwanzo 50:15-20 “Ndugu zake Yusufu walipoona ya kwamba baba yao amekufa, walisema, Labda Yusufu atatuchukia; naye atatulipa maovu yetu tuliyomtenda.  Wakapeleka watu kwa Yusufu, kunena, Baba yako alitoa amri kabla ya kufa kwake, akasema, Mwambieni Yusufu hivi, Naomba uwaachilie ndugu zako kosa lao na dhambi yao, maana walikutenda mabaya; sasa twakuomba utuachilie kosa la watumwa wa Mungu wa baba yako. Yusufu akalia waliposema naye. Nduguze wakaenda tena, wakamwangukia miguu, wakasema, Tazama, sisi tu watumwa wako. Yusufu akawaambia, Msiogope, je! Mimi ni badala ya Mungu? Nanyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia kuwa mema, ili itokee kuokoa taifa kubwa, kama ilivyo leo.”

Mungu aliingilia kati maswala ya Daniel ambaye alishitakiwa kwa hila na Mungu aliona wazi kuwa hakuwa na hatia na mfalme akabadili mawazo kwa kumtoa Daniel katika tundu la simba na kuwaingiza washitaki wake na familia zao Ni kitu gani kilitokea Mungu alposhika kalamu makanwa ya simba hayakumuweza Daniel na badala yake adui zake walishughulikiwa!

Daniel 6:21-27. “Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno. Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danieli katika lile tundu. Ndipo Danieli akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake. Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danieli, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu. Ndipo mfalme Dario akawaandikia watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, waliokaa juu ya uso wa dunia; Amani na iongezeke kwenu. Mimi naweka amri, ya kwamba katika mamlaka yote ya ufalme wangu watu watetemeke na kuogopa mbele za Mungu wa Danieli; maana yeye ndiye Mungu aliye hai, adumuye milele, na ufalme wake ni ufalme usioharibika, na mamlaka yake itadumu hata mwisho. Yeye huponya na kuokoa, hutenda ishara na maajabu mbinguni na duniani, ndiye aliyemponya Danieli na nguvu za simba.”

Mungu alishika kalamu na kuondoa mashitaka dhidi ya wayahudi waliokuwa uhamishoni na wakapewa mamlaka ya kujilinda na kuwafanyia lolote adui zao, ingawa tunaona kuwa Hamani alikuwa na mpango mbaya lakini Mungu alibadili mpango huo na hata msalaba ambao Hamani alikuwa amemuandalia Mordekai ukweli ni kuwa alisulubiwa yeye

Esta 8:7-11 “Mfalme Ahasuero akawaambia malkia Esta na Mordekai, Myahudi, kusema, Tazama, nimekwisha kumpa Esta nyumba yake Hamani, naye mwenyewe wamekwisha kumtundika juu ya mti, kwa sababu aliwatia mikono Wayahudi. Basi waandikieni Wayahudi pia vyo vyote mpendavyo, kwa jina la mfalme, mkatie muhuri kwa pete ya mfalme; kwa kuwa andiko lililoandikwa kwa jina la mfalme na kutiwa muhuri kwa pete ya mfalme hakuna awezaye kulitangua. Basi, waandishi wa mfalme wakaitwa pale pale, siku ya ishirini na tatu ya mwezi wa tatu, ndio mwezi wa Siwani; na kama vile Mordekai alivyoamuru, Wayahudi wakaandikiwa, pamoja na maakida na maliwali, na wakuu wa majimbo toka Bara Hindi mpaka Kushi, majimbo mia na ishirini na saba, kila jimbo kwa mwandiko wake, na kila taifa kwa lugha yake; na Wayahudi kwa mwandiko wao na kwa lugha yao. Akaandika kwa jina la mfalme Ahasuero, na kutia muhuri kwa pete ya mfalme, akazipeleka barua kwa matarishi, wamepanda farasi, wamepanda wanyama wepesi sana waliotumika kwa huduma ya mfalme, ndio waliozalishwa katika zizi la mfalme. Katika barua hizo mfalme aliwaruhusu Wayahudi wakusanyike katika kila mji na kuzisimamia maisha zao, kuangamiza, na kuua, na kulifisha jeshi lote la watu na la jimbo watakaowaondokea, wao na wadogo wao na wanawake; na kuyachukua mali yao kuwa nyara;”

Mungu alimfufua Yesu Kristo ambaye wazee walimshulubisha wakidhani ya kuwa wamemaliza hatima yake, walipomuua waliomba kwamba kaburi lake lilindwe na likawekwa na muhuri kuwa lisibadilike neno lolote katika kile ambacho kimeagizwa na askari waliwekwa kulinda lakini Yesu alifufuka siku ya tatu!

Matendo 3:14-18 “Bali ninyi mlimkana yule Mtakatifu, yule Mwenye haki, mkataka mpewe mwuaji; mkamwua yule Mkuu wa uzima, ambaye Mungu amemfufua katika wafu; na sisi tu mashahidi wake. Na kwa imani katika Jina Lake, jina lake limemtia nguvu mtu huyu mnayemwona na kumjua; na imani ile iliyo kwake yeye imempatia huyu uzima huu mkamilifu mbele yenu ninyi nyote. Basi sasa, ndugu, najua ya kuwa mliyatenda haya kwa kutokujua kwenu, kama na wakuu wenu walivyotenda. Lakini mambo yale aliyohubiri Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa, ameyatimiza hivyo.”

Mungu yule yule ambaye alibadilisha historia za watau wake hapo juu anauwezo wa kubadilisha historia yako, Mungu anaposhika kalamu anafungua ukurasa mpya katika maisha yako  na kusababisha kitu kipya katika maisha yako kitokee, haijalishi unapitia katika mapito gani, Wanadamu wote walikuwa wameandikiwa kifo na laana ya dhambi lakini kupitia kazi iliyofanywa na Bwana wetu Yesu Kristo pale msalabani Yesu amekuandikia habari mpya , ameifuta ile hati iliyoandikwa ya sheria iliyokuwa na shuhuda zetu na kesi iliyokuwa inatukabili ameigongomelea msalabani isiwepo tena ile hati ya kutuhukumu imefutwa, Mungu anaweza kukufanya kuwa kiumbe kipya leo kama uliandikiwa hukumu hati ya hukumu imefutwa, kama uliandikwa katika kitabu cha hukumu mambo yako ya kale yamepita na yamekuwa mapya leo, haijalishi wanadamu wamekusudia nini leo katika maisha yako nakuletea Yesu Kristo mzima mzima ambaye atayabadilisha maisha yako na kuyafanya upya, wale waliokuzomea na kukuandalia kaburi, wale waliokushitaki na kukuandikia hukumu, Yesu anabadilisha maisha yako anabadili hatima yako, hakuna mwanadamu mwenye hati miliki ya Mungu, Mungu ni wa wote ni Mungu wa wote wenye mwili, na Mungu akiishika kalamu na hubadili maisha yako kabisa na kukupa muelekeo mpya, Mungu anaposhika kalamu ndugu yangu kila kitu kitakuwa kipya tofauti na matarajio yako, Mungu anaposhika kalamu hakuna historia mbovu isiyoweza kubadilishwa, hakuna aliyechelewa sana asiyeweza kusawazishiwa, hakuna aliye na doa kubwa lisiloweza kufutika, hakuna aliyekatwa asiyeweza kuchipuliwa, hakuna aliyeachwa asiyeweza kurejezwa, Muda usingeliweza kutosha kukupa shuhuda za Ayubu ambaye shetani alifilisi kila kitu lakini Mungu aliposhika kalamu, Ayubu akawa tajiri mara mbili zaidi, Muda usingeliweza kutosha kuleta habari za Petro na Paulo na Sila ambao walitiwa gerezani na maadui zao wakitarajia kuwa watakuwa wamewaweza au kuwaweka kizuizini ili yamkini wawaangamize baadaye lakini Mungu aliposhika kalamu hali ilibadilika na mambo yakawa tofauti itakuwa hivyo pia kwako leo, katika maisha yako, katika  ndoa yako,  katika huduma yako, kwaajili ya watoto wako, kabila lako, jamii yako, taifa lako, ukoo wako, biashara zako, masomo yako, tumbo lako la uzazi na kadhalika, Ni swala la Muda tu Mungu anaposhika kalamu kila kitu huwa tofauti, waliosema hutoboi Mungu nanaposhika kalamu wataisoma namba, hakuna jambo lililogumu lisilowezekana kwa Mungu, Hatima yako iko mikononi mwa Mungu, hakuna mchawi, wala mganga wala mzimu, wale pepop, wala shetani. Wala jinni wala mtu yeyote yule anayeweza kukuandikia kinyume na kile Mungu amekiandika leo ni siku yako ya kuwekwa huru, ni siku ambayo Mungu ataweka sawa pale palipoyumba katika maisha yako Haleluyaaaa!

Dua!   

Ee Bwana mtumwa wako ninaomba! Katika jina la Yesu Kristo; nakusihi ushike kalamu sasa na kubadilisha maisha ya kila mmoja wetu na kuandika hatima mpya, andika hatima mpya ya ndugu yangu huyu, andika hatima mpya ya dada yangu huyu, andika hatima mpya ya familia zetu, andika hatima mpya ya huduma zetu, andika hatima mpya ya vizazi vyetu, andika hatima mpya ya taifa letu, andika ee Bwana tofauti na wanadamu walivyoandika, andika ee Bwana kwaajili ya jina lako tafakatifu, andika ee Bwana kupitia neema yako na upendo wako mkubhwa sana na wingi wa rehema zako tafadhali Bwana mwandikie kila mmoja wetu ukurasa mpya wenye kufaa kama ulivyokusudia toka mwanzo  namwombea kila mmoja anayesoma ujumbe huu katika jina la Mwanao Mpendwa Yesu Kristo ameeen!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Hakuna maoni: