Jumapili, 29 Juni 2025

Rahabu yule kahaba!


Yoshua 6:22-25. “Naye Yoshua akawaambia wale wanaume wawili walioipeleleza nchi, Ingieni katika nyumba ya yule kahaba, mkamtoe huyo mwanamke mwenyewe na vitu vyote alivyo navyo, kama mlivyomwapia. Basi wale vijana wapelelezi wakaingia, wakamtoa Rahabu, na baba yake, na mama yake, na ndugu zake, na vitu vyote walivyokuwa navyo, wakawatoa na jamaa zake wote pia; wakawaweka nje ya matuo ya Israeli. Kisha wakauteketeza mji kwa moto, na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake; bali fedha, na dhahabu, na vyombo vya shaba, na vya chuma, wakavitia katika hazina ya nyumba ya Bwana. Lakini Yoshua akamhifadhi Rahabu, yule kahaba, na watu wa nyumba ya baba yake, na vitu vyote alivyokuwa navyo; naye akakaa kati ya Israeli hata leo; kwa sababu aliwaficha wale wajumbe aliowatuma Yoshua ili kuupeleleza mji wa Yeriko.”




Utangulizi:

Hakuna mtu mbaya sana, wala hakuna mtu aliye mbali sana kiasi cha Rehema za Mungu kushindwa kumfikia na kuokolewa, Haijalishi mtu ametoka wapi na amefanya nini, Mpango wa Mungu uko pale pale kwamba yeye alikuja duniani kuwaokoa wenye dhambi na kwa sababu hiyo hashindwi kumbadilisha yeyote na kumtumia katika mpango wake mkuu, kimsingi Yesu Kristo ambaye ndiye mwokozi, hakuja duniani kuwaita watu wema bali alikuja kuwaita wenye dhambi na kuokoa wale waliopotea.

Luka 5:30-32 “Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.”

Luka 19:9-10 “Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu.Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Katika maandiko tunauona moyo wa Mungu, jinsi usivyokuwa na ubaguzi wala mipaka katika kuokoa, Mungu alimuingiza Rahabu yule kahaba katika mpango wake wa ukombozi kwa sababu ya Imani yake kwake, Yeye alimuamini Mungu na kuokolewa, licha ya kuwa na historia mbaya ya maisha ya nyuma, tunajifunza kuwa Mungu anaweza kumuokoa yeyote bila kujali historia ya maisha yake ya nyuma, kama alivyomuokoa Rahabu, Leo tutachukua muda basi kujifunza kwa habari ya Rahabu na kujifunza namna na jinsi ambavyo Mungu anaweza kukuokoa na wewe na kukuingiza katika mpango wake na makusudi yake ya ukombozi bila kujali unatokea wapi.

Tutajifunza ujumbe huu Rahabu yule kahaba kwa kuzingatia mambo ya muhimu yafuatayo!

·         Rahabu alikuwa mtu wa namna gani?

·         Mambo yaliyopelekea maisha ya Rahabu kubadilika

·         Kujifunza kutoka kwa Rahabu yule kahaba


Rahabu alikuwa mtu wa namna gani?

Kwa mujibu wa maandiko Rahabu aliyeishi mwaka wa 1481 Kabla ya Kristo alikuwa ni mwanamke kahaba wa kabila za kikanaani aliyeishi katika jiji la Yeriko, lililokuwako katika inchi ya ahadi, moja ya sifa kubwa inayomtambulisha Rahabu ilikuwa ni pamoja na kazi yake ya ukahaba, Neno Kahaba katika maandiko ya kiebrania linasomeka kama “Zânâh” Neno hilo kwa kiingereza ni Harlot au hookers au zona yaani Prostitute ambalo tafasiri yake ni mtu anayejishughulisha na kuuza mwili wake ili kujipatia fedha, au mtu anayetoa huduma ya tendo la ngono kwa kusudi la kujipatia fedha, Kwa hiyo Rahabu alikuwa ni mtu anayefanya biashara hiyo, sio hivyo tu, Rahabu pia alikuwa anamiliki nyumba ya wageni au nyumba ya kufanyia mapenzi maarufu kama danguro, kwa hiyo ilikuwa rahisi kwa wageni wa kila aina kufikia nyumbani mwake au kwenye nyumba yake ya wageni

Yoshua 2:1-3 “Yoshua, mwana wa Nuni, akawatuma watu wawili kutoka Shitimu kwa siri, ili kupeleleza, akawaambia, Enendeni mkaitazame nchi hii, na Yeriko. Wakaenda wakafika nyumbani kwa kahaba mmoja jina lake aliitwa Rahabu, wakalala huko. Mfalme wa Yeriko akaambiwa, kusema, Tazama, watu wawili wa wana wa Israeli wameingia humu leo usiku, ili kuipeleleza nchi. Mfalme wa Yeriko akatuma watu kwa Rahabu, akasema, Watoe watu wale waliokuja kwako, walioingia ndani ya nyumba yako, maana wamekuja ili kuipeleleza nchi.”

Utafiti wa hivi karibuni unaonyesha kuwa duniani kuna watu wapatao milioni 42 ambao wanajihusisha na biashara ya ukahaba na wengi wao ni wanawake, Ukahaba ni swala lililo kinyume na sheria katika inchi nyingi na linahesabika kama uhalifu, lakini hata hivyo biashara hii inashamiri hata katika maeneo ambayo ni vigumu sana kuamini kuwa yanaweza kuwa na ukahaba, mfano katika nchi ya Jordan ni rahisi kuona waziwazi wanawake wa kiarabu wakijiuza kwa watalii, katika mpango mkakati wa kuhubiri injili, Kanisa halina budi kuwa na Programu maalumu ya kujaribu kusaidia na kuwafikia makahaba au watu wanaojihusisha na biashara hii kwa injili, kwani wengine wamelazimika kuwa hivyo kutokana na kushindwa kuvumilia changamoto mbalimbali za kimaisha, Mungu alimuhurumia Kahaba huyu na kumuokoa na kumsamehe kabisa na kuolewa katika ukoo wa Yuda na hivyo kuingia katika mstari wa wanawake maarufu wanaotajwa katika ukoo wa Masihi

Mathayo 1:1-5 “Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa Isaka; Isaka akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yuda na ndugu zake;  Yuda akamzaa Peresi na Zera kwa Tamari; Peresi akamzaa Esromu; Esromu akamzaa Aramu; Aramu akamzaa Aminadabu; Aminadabu akamzaa Nashoni; Nashoni akamzaa Salmoni; Salmoni akamzaa Boazi kwa Rahabu; Boazi akamzaa Obedi kwa Ruthu; Obedi akamzaa Yese; Yese akamzaa mfalme Daudi. Daudi akamzaa Sulemani kwa yule mke wa Uria;”

Mambo yaliyopelekea maisha ya Rahabu kubadilika

Pamoja na changamoto aliyokuwa anakabiliana nayo Rahabu katika maisha yake kama kahaba, Kahaba huyu alikuwa na ufahamu mkubwa au ufahamu mpana jina lake Rahabu katika kiebrania linasomeka kama “Rāhāb” au “Rahav” ambalo maana yake mwenye ufahamu mpana au mwenye ufahamu mkubwa, kwa hiyo ni wazi kuwa Rahabu alikuwa ni mwanamke mwenye uelewa mkubwa sana na ufahamu mpana,upana wa ujuzi wake ulihifadhi siri nyingi sana na taarifa kubwa kama bahari. Rahabu alikuwa ni mtu mwenye taarifa nyingi tena zilizo sahihi, kwa hiyo mwanamke huyu vilevile alikuwa “informer” alikuwa ni mtu mwenye uwezo mkubwa wa kudukuu taarifa na ndio maana hata mfalme wa inchi alijua kuwa anaweza kupata taarifa sahihi za wapelekezi walioingia nchini mwake.

Yoshua 2:2-5 “Mfalme wa Yeriko akaambiwa, kusema, Tazama, watu wawili wa wana wa Israeli wameingia humu leo usiku, ili kuipeleleza nchi. Mfalme wa Yeriko akatuma watu kwa Rahabu, akasema, Watoe watu wale waliokuja kwako, walioingia ndani ya nyumba yako, maana wamekuja ili kuipeleleza nchi. Yule mwanamke akawatwaa wale watu wawili, akawaficha, akasema, Naam, wale watu walikuja kwangu, lakini sikujua walikotoka; ikawa kama wakati wa kufungwa lango la mji, kulipokuwa giza, watu wale wakatoka, wala sijui walikokwenda; wafuateni upesi, maana mtawapata.”

Kutokana na uwezo wake mkubwa wa kupata taarifa kahaba huyu alikuwa na taarifa zote za Wana wa Israel na matendo yote ya Mungu wao na alitambua kila kitu kuhusu Wayahudi na Mungu wao Tangu siku walipotoka Misri hivyo alikuwa na taarifa sahihi kuhusu Mungu huyu wa kweli na kuamini

a.       Alimwamini Mungu wa Israel - Yoshua 2:9-11 “ akawaambia wale wanaume, Mimi najua ya kuwa Bwana amewapa ninyi nchi hii, na ya kuwa hofu imetuangukia mbele yenu, na ya kuwa wenyeji wote wa nchi wanayeyuka mbele yenu. Maana tumesikia jinsi Bwana alivyoyakausha maji ya bahari ya Shamu mbele yenu, hapo mlipotoka Misri, tena mambo hayo mliyowatendea wafalme wawili wa Waamori waliokuwa huko ng'ambo ya Yordani, yaani, Sihoni na Ogu, mliowaangamiza kabisa. Na mara tuliposikia hayo mioyo yetu iliyeyuka, wala haukusalia ujasiri wo wote katika mtu awaye yote, kwa sababu yenu; kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, yeye ndiye Mungu, katika mbingu juu na katika nchi chini.”

               

b.      Alitaka Agano la ukombozi – Licha ya kuwa na taarifa nyingi na sahihi na pana kuhusu Waisrael na kuhusu Mungu wao, Rahabu pia alijua ni namna gani anaweza kuyaokoa maisha yake na familia yake, alitambua namna anavyoweza kujiepusha na maangamizi kwa sababu hiyo alifahamu namna na jinsi anavyoweza kujiweka salama kwa kuingia katika agano na Mungu wa Israel na watu wake kwa sababu hiyo aliwaomba wapelelezi wamuhakikishie wokovu wake na nyumba yote ya baba yake

 

Yosua 2:12-14 “Basi sasa, nawasihi, niapieni kwa Bwana, kwa kuwa nimewatendea ihisani, ya kwamba ninyi nanyi mtaitendea ihisani nyumba ya baba yangu; tena nipeni alama ya uaminifu; ya kwamba mtawaponya hai baba yangu na mama yangu, na ndugu zangu wanaume na wanawake, na vitu vyote walivyo navyo, na kutuokoa roho zetu na kufa. Wale wanaume wakamwambia, Uhai wetu badala ya uhai wenu, ikiwa hamwitangazi habari ya shughuli yetu hii; kisha itakuwa, wakati Bwana atakapotupa nchi hii, tutakutendea kwa ihisani na uaminifu.”

 

c.       Alionyesha Imani na matendo – Licha ya kumuamini Mungu wa Israel Rahabu aliwatendea mema wapelelezi wale kwa kuwaficha  na kuwaelekeza njia ya kutorokea aliwalinda na hakutaka kuwatoa kwa watu wanchi yake ili wauawe au kukamatwa, aliwatendea mema watu wa Mungu

 

Yoshua 2:15-16 “Ndipo akawashusha kwa kamba dirishani, maana nyumba yake ilikuwa katika ukuta wa mji; naye alikaa ukutani. Akawaambia, Enendeni zenu mlimani, wale wanaowafuatia wasije wakawapata; mkajifiche huko siku tatu hata wao wanaowafuatia watakaporudi; kisha enendeni zenu.           

 

Yakobo 2:25 “Vivyo hivyo na Rahabu, yule kahaba naye, je! Hakuhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo, hapo alipowakaribisha wajumbe, akawatoa nje kwa njia nyingine? Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa.”         

Kujifunza kutoka kwa Rahabu yule kahaba

Ni wazi kuwa mtu huyu hakuwa myahudi wala hakuwa mwenye metendo mema alikuwa kahaba, lakini Mungu alimuokoa kwa sababu alimuamini Mungu, Yesu Kristo amekuja duniani sio kwaajili ya watu Fulani maalumu, Mungu yuko tayari kumuokoa mtu yeyote wa kabila lolote na wa historia yoyote maadamu tu mtu huyo atamuamini Mungu aliye hai na kazi yake ya ukombozi kupitia mwanae mpendwa Yesu Kristo

Yohana 3:16 -18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Awaye yote akimuamini Yesu Kristo, ataokolewa bila kujali kuwa anatokea katika historia gani, wala Mungu haangalii makosa yetu ya zamani na badala yake anatazama moyo uliobadilika kumuelekea yeye, Mungu alimuinua Kahaba Rahabu na kumpeleka juu sana hata kuwa sehemu ya ukoo wa Yesu Kristo, wakati mwingine kuonelewa kwako sana na ibilisi kunadhihirisha wivu mkubwa sana alio nao kwako endapo Mungu angekutana na wewe

Wokovu na haki ya Mungu sio vitu vinavyopatikana kwa jitihada na matendo ya kibinadamu, bali Imani katika Mungu na neema anayoitoa yeye, neema hii inaweza kwenda kwa yeyote yule bila kujali historia yake.

Waefeso 2:8-9. “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.”

No one is too special to meet the Grace of God, Hakuna mtu ambaye yeye anaweza kudai kuwa ni maalumu sana mpaka aweze kupokea neema ya Mungu, ni Imani yako kwake tu ndiyo inayoweza kumgusa na akabadilisha maisha yako, huna lolote unaloweza kulifanya ukampendeza yeye, zaidi ya kuamini. Usihuzunike kwa sababu labda umewahi kupitia historia mbaya zaidi ya maisha yasiyofaa ambayo labda unaweza kudhania kuwa kwajili ya hayo hustahili kuhurumiwa na Mungu, lakini nakutangazia kuwa haijalishi umepitia maisha mabaya kiasi gani, Rahabu ni ishara ya kuwa hata wewe unaweza kupokelewa na Mungu na historia ya maisha yako ikabadilika, ukamtangaza Kristo.

2Wakorintho 5:17 “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.”

Yeriko ulipoharibiwa Rahabu pamoja na familia yake na nyumba ya baba yake waliokolewa wote kwa sababu ya Imani na agano lile aliloapiwa na Wapelelezi katika inchi ya Kanaani, Mungu alikuwa mwaminifu kwa ahadi zake, na watu wake walikuwa wamejifunza kusimamia viapo vyao kwani Yoshua alikumbuka kuwa yuko mtu ambaye hastahili kuangamizwa kwa sababu amemuamini Mungu wa Israel na ana agano na Mungu wa Yakobo!

Yoshua 6:22-25 “Naye Yoshua akawaambia wale wanaume wawili walioipeleleza nchi, Ingieni katika nyumba ya yule kahaba, mkamtoe huyo mwanamke mwenyewe na vitu vyote alivyo navyo, kama mlivyomwapia. Basi wale vijana wapelelezi wakaingia, wakamtoa Rahabu, na baba yake, na mama yake, na ndugu zake, na vitu vyote walivyokuwa navyo, wakawatoa na jamaa zake wote pia; wakawaweka nje ya matuo ya Israeli. Kisha wakauteketeza mji kwa moto, na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake; bali fedha, na dhahabu, na vyombo vya shaba, na vya chuma, wakavitia katika hazina ya nyumba ya Bwana. Lakini Yoshua akamhifadhi Rahabu, yule kahaba, na watu wa nyumba ya baba yake, na vitu vyote alivyokuwa navyo; naye akakaa kati ya Israeli hata leo; kwa sababu aliwaficha wale wajumbe aliowatuma Yoshua ili kuupeleleza mji wa Yeriko.”     

Wokovu ni zawadi ya Mungu kwa watu wote, Mungu hana upendeleo, hatupaswi kujivunia wokovu na kujifikiri kuwa sisi ni watu maalumu sana kuliko wengine, Mungu ni Mungu wa wote wenye mwili anaweza kumuokoa yeyote na anaweza kumuinua yeyote ana anaweza kumtumia yeyote, wapelelezi hawakuweza kabisa kumdharau Rahabu kwa sababu ya ukahaba wake na maisha yake yaliyopita badala yake walimuheshimu na kumsikiliza, na walifuata maelekezo yake. Mungu alimhamisha Rahabu kutoka katika maisha ya dhambi kwenda katika historia ya ukombozi wa mwanadamu, ni kupitia rehema za Mungu, na neema yake yeye anaweza kuwafikiwa watu wote na wa jinsia zote na imani zote duniani, hupaswi kujikinai na kujifikiri kuwa wewe ni mtu asiyefaa, badala yake mtazame yule tu awezaye kuokoa, haki yetu haihesabiwi na wanadamu, haki yetu inahesabiwa na Mungu na hakuna mwanadamu yeyote mwenye mamlaka ya kutushitaki

Zaburi 130:3-4 “Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha, Ili Wewe uogopwe.”

Warumi 8:33-34 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.”        

Na. Rev. Innocent Mkombozi bin Samuel bin Hamza bin Jumaa bin Athumani bin Salim Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

Hakuna maoni: