Jumapili, 14 Septemba 2025

Urithi wa Mtoto wa kike!


Hesabu 27:1-4 “Wakati huo wakakaribia hao binti za Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, wa jamaa za Manase mwana wa Yusufu; na majina ya hao binti za Selofehadi ni haya; Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. Nao wakasimama mbele ya Musa, na mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya wakuu, na mkutano wote, mlangoni pa hema ya kukutania, wakasema, Babaetu alikufa nyikani, naye hakuwamo katika mkutano wa hao waliojikutanisha kinyume cha Bwana katika mkutano wa Kora; lakini akafa katika dhambi zake mwenyewe; naye alikuwa hana wana wa kiume. Kwa nini basi jina la babaetu kufutwa katika jamaa zake kwa sababu alikuwa hana mwana wa kiume? Tupe sisi urithi pamoja na ndugu zake babaetu.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika Jamii nyingi zamani na hata siku hizi, Mwanamke hakupewa nafasi kubwa katika urithi wa mali za baba yake hususani ardhi, Kulikuwa na sheria na mila nyingi zinazompa upendeleo mtoto wa kiume na kumpuuzia mtoto wa kike, Hapa Masaini Loiborosoit A, Wilayani Simanjirio, Mkoani Manyara niliko pia nimeikuta mila hii miongoni mwa jamii ya Kimaasai, Mila, Desturi na Sheria kama hii vilevile lilikuweko katika jamii ya Kiyahudi wakati wa Torati ya Musa, Lakini kupitia mabinti jasiri sana wana wa SELOFEHADI  yaani Mala, Noa, Hogla, Milka na Tirsa  wao waliwahi kutoa hoja mbele ya Musa na kuhani mkuu Eleazari na kisha hoja ikapelekwa kwa Mungu na Mungu akalazimika kubadilisha sheria na kutoa kibali kwamba watoto wa kike wana haki ya kurithi kama ilivyo kwa watoto wa kiume, ujasiri wao na uthubutu wao wa kuweza kumkabili Musa na hatimaye Mungu kubadili sheria kwaaji yao unaonyesha kuwa mabinti hawa walikuwa na ujasiri usiokuwa wa kawaida “uncommon boldness” katika tafiti zangu wakati wa maandalizi ya somo hili nilimuona mtu mmoja akiwaita mabinti hawa “Change Makers” yaani waleta mabadiliko, Hoja yao ilikuwa na mashiko jambo lililopelekea Mungu kubadili sheria kwaajili ya watoto wa kike

Hesabu 27:5-8 “Basi Musa akaleta neno lao mbele ya Bwana Bwana akanena na Musa, na kumwambia, Hao binti za Selofehadi wananena lililo haki; kweli utawapa milki ya urithi pamoja na ndugu za baba yao; nawe utawapa urithi wa baba yao. Kisha utanena na wana wa Israeli, na kuwaambia, Mtu akifa, naye hana mwana wa kiume, ndipo utampa binti yake urithi wake.”

Leo basi tutachukua muda kujifunza kwa njia ya uchambuzi somo hili Urithi wa Mtoto wa kike kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

 

·         Sheria isiyozingatia haki

·         Kuvunjwa kwa sheria isiyozingatia haki

·         Urithi wa mtoto wa kike

                 

Sheria isiyozingatia haki

Sheria ya Musa pamoja na Mila nyingi na Desturi za zamani zilikuwa zimezoeleka ya kwamba urithi wa mali pamoja na ardhi ulikuwa unaelekezwa kwa watoto wa kiume pekee, mtoto wa kiume wa kwanza akipokea urithi mara dufu yaani mara mbili kuliko wengine na wengine kwa kadiri ya sehemu zao, watoto wa kike hawakuhesabiwa, na kuwa kama mtu angefariki dunia bila kuwa na mtoto wa kiume basi mali zake zingerithiwa na Ndugu zake wa karibu na mabinti wangeolewa tu na kuwa na jina la familia nyingine, kimsingi pia wangeachwa bila kurithi lolote

Kumbukumbu 21:15-17 “Akiwa mtu yuna wake wawili, mmoja ampenda, mmoja hampendi, nao wamemzalia watoto, ampendaye na asiyempenda wote wawili; na yule mzaliwa wa kwanza akiwa ni wa mke asiyependwa; ndipo itakapokuwa ya kwamba siku atakayowarithisha wanawe alivyo navyo, asimweke mwana wa ampendaye kuwa mzaliwa wa kwanza mbele ya mwana wa asiyempenda, naye ndiye mzaliwa wa kwanza huyu; lakini amkubali mzaliwa wa kwanza mwana wa yule asiyempenda, kwa kumpa mafungu mawili katika vyote alivyo navyo; kwa maana ndiye mwanzo wa nguvu zake; haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake yeye.”

Kwa hiyo Mwanzoni Mila na Desturi na Sheria za Kiebrania hazikuwa zimemfikiria hata kidogo mtoto wa kike, Sheria hii ilikuwa ni Sheria isiyozingatia haki, ilisababisha huzuni kwa mabinti kwani mali hususani ardhi ya baba yao ingekwenda kwa ndugu zake na wao wangeachwa mikono mitupu, Binti za wana wa Selofehadi yaliwakuta haya, na bila shaka waliyafikiri kwa kina na kuona kuwa hakuna haki hapo na sheria hiyo ni kandamizi kwao wakadai haki hiyo

Hesabu 27:1-4 “Wakati huo wakakaribia hao binti za Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, wa jamaa za Manase mwana wa Yusufu; na majina ya hao binti za Selofehadi ni haya; Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. Nao wakasimama mbele ya Musa, na mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya wakuu, na mkutano wote, mlangoni pa hema ya kukutania, wakasema, Babaetu alikufa nyikani, naye hakuwamo katika mkutano wa hao waliojikutanisha kinyume cha Bwana katika mkutano wa Kora; lakini akafa katika dhambi zake mwenyewe; naye alikuwa hana wana wa kiume. Kwa nini basi jina la babaetu kufutwa katika jamaa zake kwa sababu alikuwa hana mwana wa kiume? Tupe sisi urithi pamoja na ndugu zake babaetu.”

Mabinti wa Selofehadi walihuzunika kuona kwakuwa baba yao hakuwa na mtoto wa kiume, basi ndugu zake baba yao wangerithi mali na ardhi yake na mabinti zake wakiepo wangeachwa bila kitu, lakini baada ya kuchukua hatua za kijasiri na kumkabili Musa na Musa akamuuliza Mungu huo ukawa mwisho wa sheria kandamizi dhidi ya wanawake.

Tunajifunza kutoka kwa Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa kwamba tunaweza kubadili lolote lisilo la haki kwa ujasiri na lolote lililo kandamizi kwa njia ya maombi na Mungu akasikiliza, Sheria na Kanuni yoyote iliyokinyume na lile tunalolihitaji na linalosimama kama haki yetu mbele za Mungu inaweza kuingiliwa kati kwa Sheria ya Kanuni ya kuomba kwa Mungu, Mabinti hawa kwa imani na ujasiri walimkabili Musa na Musa aliomba kwa Mungu na Mungu akabadili sheria, tunaweza kuomba lolote kwa jina la Yesu kwenda kwa Baba yetu wa Mbinguni na kubadilisha Sheria na Kanuni, Mila na Desturi kandamizi na uhuru wetu ukapatikana katika jina la Yesu Kristo.

Kuvunjwa kwa sheria isiyozingatia haki

Habari ya mabinti hawa inatufundisha kuwa tunaweza kubadili sheria, endapo tu tutasimama katika haki, na tunajifunza ya kuwa maombi yana nguvu ya kubadili sheria mila na desturi ambazo hazitutendei haki katika ulimwengu wa roho na mwili, wakati habari hii ikizungumzia kubadilishwa kwa sheria iliyopelekea wasichana au wanawake katika familia kuwa na haki ya kisheria ya kurithi, lakini tunajifunza pia kuwa tunaweza kubadili sheria za mila na desturi za aina yoyote ile kwa njia ya maombi ikiwa sheria hiyo au mila hizo au kanuni hizo hazijazingatia haki

Esta 4:15-16 “Basi Esta akawatuma ili wamjibu Mordekai, Uende ukawakusanye Wayahudi wote waliopo hapa Shushani, mkafunge kwa ajili yangu; msile wala kunywa muda wa siku tatu, usiku wala mchana, nami na wajakazi wangu tutafunga vile vile; kisha nitaingia kwa mfalme, kinyume cha sheria; nami nikiangamia, na niangamie.”  

Daniel 6:10-26 “Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu ;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake. Ndipo wakakaribia, wakasema mbele ya mfalme katika habari ya ile marufuku ya mfalme; Je! Hukuitia sahihi ile marufuku, ya kwamba kila mtu atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme, atatupwa katika tundu la simba? Mfalme akajibu, akasema, Neno hili ni kweli, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi isiyoweza kubadilika. Basi wakajibu, wakasema mbele ya mfalme, Yule Danieli, aliye mmoja wa wana wa wale waliohamishwa wa Yuda, hakujali wewe, Ee mfalme, wala ile marufuku uliyoitia sahihi, bali aomba dua mara tatu kila siku. Basi mfalme aliposikia maneno haya alikasirika sana, akakaza moyo wake ili kumponya Danieli; akajitaabisha kumwokoa hata jua likachwa. Ndipo watu wale wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia mfalme, Ee mfalme, ujue ya kuwa ni sheria ya Wamedi na Waajemi, lisibadilike neno lo lote lililo marufuku, wala amri yo yote iliyowekwa na mfalme. Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danieli. Kisha mfalme akaenda nyumbani kwake, akakesha usiku kucha, akafunga; na vinanda havikuletwa mbele yake; na usingizi wake ukampaa. Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba.Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno. Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danieli katika lile tundu. Ndipo Danieli akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake. Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danieli, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu. Ndipo mfalme Dario akawaandikia watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, waliokaa juu ya uso wa dunia; Amani na iongezeke kwenu. Mimi naweka amri, ya kwamba katika mamlaka yote ya ufalme wangu watu watetemeke na kuogopa mbele za Mungu wa Danieli; maana yeye ndiye Mungu aliye hai, adumuye milele, na ufalme wake ni ufalme usioharibika, na mamlaka yake itadumu hata mwisho.”              

Tunaona katika mifano kadhaa hapo juu ya kuwa maombi yana uwezo wa kuingilia kati sheria za kawaida na mila za kawaida na hata za Mungu na kubadilisha mambo, mabinti hawa wenye ujasiri waliomkabili Musa kwa maombo yao na ufuatiliaji waliweza kusababisha mabadiliko ya sheria, walimrudisha Musa kwa Mungu na Mungu akafanya mabadiliko ya sheria kwaajili yao na wengine hata leo, kwa tukio lao Mungu alibadili kanuni na kuamua kuwapa haki

Luka 18:1-7 “Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa. Akasema, Palikuwa na kadhi katika mji fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu. Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu. Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu,lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima.Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao?

Mungu atampa haki yake kila mtu anayemkomalia katika maombi, Mungu aliwapa haki mabinti wa Selofehadi ya Kuwa kama mtu akifa bila mwana wa kiume basi urithi wake utapewa binti zake, asipokuwa na binti au mwana wa kiume basi watepea ndugu zake walio karibu na sheria hii ikawa agizo la kudumu kwa Israel hata leo, haya yakawa mapinduzi makubwa na ya kipekee kwa sababu kupitia wao na kwa mara ya kwanza katika mila na desturi za Kiyahudi wanawake walihesabika kuwa warithi halali wa mali na ardhi ya baba zao. Sio hivyo tu Mungu aliongezea baadaye kwamba ili mali hizo zisitawanyike kutoka kwenye kabila lao basi mabinti hao waolewe ndani ya koo zao ili urithi usihame kutoka kabila moja hadi lingine na hii haikuwanyima haki ya kurithi bali ilihifadhi urithi ule ndani ya ukoo na ndani ya kabila husika bila kutawanyika kwa jina na mali za Muhusika

Hesabu 36:1-10 “Kisha wale wakuu wa nyumba za mababa ya jamaa ya wana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, katika jamaa za wana wa Yusufu, wakakaribia, na kunena mbele ya Musa, na mbele ya wakuu walio juu ya nyumba za mababa ya wana wa Israeli; wakasema, Bwana alimwagiza bwana wangu awape wana wa Israeli nchi kwa kupiga kura iwe urithi wao; tena bwana wangu aliagizwa na Bwana awape binti za Selofehadi ndugu yetu huo urithi wa baba yao. Wakiolewa na watu wa wana wa hizo kabila nyingine za wana wa Israeli, ndipo urithi wao utatwaliwa na kuondolewa katika urithi wa baba zetu, na hiyo kabila watakayotiwa ndani yake itaongezewa urithi wao; basi urithi huo utaondolewa katika kura ya urithi wetu. Tena itakapokuwapo hiyo yubile ya wana wa Israeli, ndipo urithi wa hiyo kabila ambayo wamekuwa ndani yake utaongezewa huo urithi wao; hivyo urithi wao utaondolewa katika urithi wa kabila ya baba zetu. Basi Musa akawaagiza wana wa Israeli kama neno la Bwana lilivyokuwa, akasema, Kabila ya wana wa Yusufu imenena yaliyo haki. Bwana ameagiza neno hili katika habari ya binti za Selofehadi, akasema, Na waolewe na waume wawapendao; lakini na waolewe katika jamaa ya kabila ya baba zao. Hivyo hapana urithi wo wote wa wana wa Israeli utakaotoka kabila hii kwenda kabila hii; kwa kuwa wana wa Israeli watashikamana kila mtu na urithi wa kabila ya baba zake. Na kila binti atakayemiliki urithi katika kabila yo yote katika wana wa Israeli, ataolewa katika jamaa moja ya kabila ya baba yake, ili wana wa Israeli wapate kumiliki kila mtu urithi wa baba zake. Hivyo hapatakuwa na urithi uwao wote utakaotoka kabila hii kwenda kabila hii; kwa kuwa kabila za wana wa Israeli zitashikamana kila mmoja na urithi wake mwenyewe. Basi hao binti za Selofehadi wakafanya kama Bwana alivyomwagiza Musa;”

Urithi wa mtoto wa kike

Moja ya fundisho lingine la msingi na la Muhimu tunalojifunza kutoka kwa mabinti wa Selofehadi ni kuwa tunajifunza namna Mungu anavyotaka sheria ya urithi wa mtoto wa kike kuzingatiwa, Ni kama neno la Mungu olinatoa wito kwa jamii kutokuwapuuzia watoto wa kike katika maswala mbalimbali ya kijamii, Kamwe jamii haipaswi kufikiri kuwa Mwanamke ni kiumbe wa daraja la chini, Haki zao zimendikwa katika Torati na zimethibitishwa na Mungu mwenyewe. Jamii inapaswa kuondoa dhana potofu ya kufikiri kuwa mwanamke hastahili urithi na kupingana na hilo ni kupingana na mpango wa Mungu, watoto wa kike wapewe kila wanachistahili katika familia zao, ikiwa ni pamoja na kuwaelimisha, kupinga ukatili na ubaguzi wa kijinsia, kutokuwatahiri wanawake na yote yanayowanyima haki kutokana na maumbile yao na kuwa jamii inapaswa kuacha mila na desturi za kizamani ambazo ni kandamizi.

Katika nyakati za agano jipya Mwanamke ana haki na mwanaume, Mtumwa na muajiri, Myahudi na Myunani wote wana haki sawa za kiroho, Kwa hiyo anapomuamini Yesu wote wanaonekana kuwa wamoja katika Kristo

Wagalatia 3:27-29 “Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo. Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu. Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.”

Habari ya mabinti wa Selofehadi ni fundisho la kipekee kwamba Mungu ni mtetezi wa haki ya wote walio dhaifu na wanyonge na wale wanaokandamizwa katika jamii, ni somo kwamba Mungu hakubaliani na mila na desturi zinazowanyima haki wengine kwa sababu fulani fulani, kila mwanadamu ana nafasi yake na heshima yake mbele za Mungu na kila mwanadamu anastahili kushiriki Baraka zote za Mungu, Urithi wa mwanamke ni agizo la Mungu na sio upendeleo, Lakini ili urithi ubaki katika kabila lao na jina la baba yao lisipotee waliolewa na binamu zao, kimsingi baadaye watoto hao mabinti walikabidhiwa urithi ulioahidiwa na Musa mtumishi wa Mungu katika nchi ya Mkanaani

Yoshua 17:3-4 “Lakini Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, hakuwa na wana waume ila binti; na majina ya hao binti zake walikuwa wakiitwa Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. Nao wakakaribia mbele ya Eleazari, kuhani, na mbele ya Yoshua, mwana wa Nuni, na mbele ya mashehe, wakasema, Bwana alimwamuru Musa kutupa sisi urithi kati ya ndugu zetu; basi kwa kuiandama hiyo amri ya Bwana akawapa urithi kati ya ndugu za baba yao.”

Desturi ya kuwanyima watoto wa kike urithi hususani wa Ardhi imeleta mafarakano katika jamii nyingi duniani, ni Sheria,  Mila na Desturi ambayo imeleta ubaguzi wa kijinsia, lakini hiki ambacho Mungu alikifanya baada ya mabinti wa Selofehadi kimeleta mtazamo mpya wa kijamii na usawa wa kijinsia, hivyo sio tu swala la ardhi lakini watoto wasomeshwe na wasiozwe katika hali ya utoto, lakini wajaliwe na kutunzwa na kuhudumiwa kama watoto wengine, Katika sheria za kislamu watoto wa kike hupewa urithi japo ni nusu ya kile wanapewa wanaume, Lakini wale wenye mila mbovu zinazo-mbagua mtoto wa kike wafahamu tu kuwa Mungu anawathamini nao vilevile kama anavyothamini watoto wa kiume hivyo ni wakati sasa kwa jamii kubadilika ni wakati wa mabunge kutunga sheria zenye kuzingatia uaswa wa kijinsia na kuondoa mila potofu na kandamizi katika jamii na kuachia zile zenye manufaa  

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Jumapili, 7 Septemba 2025

Chembe ya ngano isipoanguka!


Yoahana 12:23-25 “Naye Yesu akawajibu, akasema, Saa imefika atukuzwe Mwana wa Adamu. Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.”



Utangulizi:

Leo tunachukua muda kiasi kutafakari maneno ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyoyasema karibu na mwishoni kabisa mwa huduma yake Duniani, Yesu alikuwa ametembelewa na kundi kubwa la jamii ya watu wasiokuwa wayahudi, yaani Wayunani ambao kimsingi nao walikuwa na kiu na hamu na shauku ya kupata huduma ya Bwana wetu Yesu Kristo, Yesu anaiona shauku yao kama hitaji kubwa sana la kiroho kwa jamii ya watu wote duniani kama watu wanaomuhitaji Mungu na Mwokozi katika maisha yao, Hata hivyo kuhudumia jamii ya watu wote duniani kwa vyovyote vile kungemlazimu kutimiza mapenzi ya Mungu ya kufa msalabani ili aweze kuwa fidia ya wengi kama yanenavyo maandiko:-

Yohana 3:16 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”

Luka 2:34-35 “Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. Nawe mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi.”

Akifafanua juu ya mauti yake huku akiunganisha na mafundisho yahusuyo kujikana nafsi, Yesu anatumia mfano wa wakulima wa ngano ili kufafanua kanuni ya kiroho ya kuleta mafanikio na kuzaa matunda mengi inavyogharimu maisha ya waanzilishi ili kuleta uzima kwa wengi au kwa ulimwengu na ndipo anapotumia mfano wa Chembe ya ngano (Yaani mbegu ya ngano) kwamba ili iweze kutoa mazao mengi ni lazima ife na kuzikwa na inapoota yaani kufufuka inasababisha mazao mengi sana.

Tutajifunza ujumbe huu Chembe ya ngano isipoanguka kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-


·         Maana ya kuanguka kwa chembe ya ngano.

·         Chembe ya ngano isipoanguka!.

·         Faida za kuanguka kwa chembe ya ngano.


Maana ya kuanguka kwa chembe ya ngano.

Ni muhimu kufahamu kuwa Pamoja na ukulima wa zabibu, ufugaji wa wanyama wa aina mbalimbali,kama kondoo, mbuzi na ng’ombe, watu wa mashariki ya kati hususani Israel na baadhi ya waarabu ni watumiaji wazuri sana wa ngano kwaajili ya chakula na hasa mikate, sasa ili Yesu aweze kueleweka vizuri katika jamii yake alitumia mifano ya vitu vya karibu na vilivyozoeleka katika jamii yake ili aweze kuwasilisha ujumbe wa kiroho wenye maana inayoeleweka kwa watu wake, Yesu hapa anatumia mfano wa chembe ya ngano (yaani mbegu ya ngano) ambayo ili iweze kuzaa matunda mengi zaidi hutupwa au kuzikwa shambani na kisha inakufa katika udongo au ardhini na inapofufuka/kuota kama mmea na kuzaa inazalisha matunda au mbegu nyingine bora zaidi hii ndio kanuni ya kilimo.

Yohana 12:24 “Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi.”

·         Chembe ya ngano kwa kiyunani (Greek) inaitwa “ho kokkos tou sitou” kwa kiingereza “a grainof wheat”  ikimaanisha mbegu ya ngano

·         Kuanguka  kwa kiyunani (Greek) linatumika neno Piptō linalomaanisha kuanguka chini kwa hiyari, au kuangushwa kwa kusudi au kupanda

·         Kufa  kwa kiyunani (Greek) linatumika neno apothnēskō linalomaanisha kufa kimwili au kufa kwa hiyari yaani kwa kiingereza “Self- denial” “Self-sacrificial” kujitoa dhabihu, kujikana au kujikataa au kujitoa sadaka.

Waebrania katika mtazamo wao kuhusu mbegu siku zote waliamini ndani ya mbegu kua kuna UZIMA, URITHI, na KIZAZI, walikuwa wanatambua kuwa uhai hauwezi kuendelea bila ya kuwako kwa mbegu, lakini ili mbegu iweze kuendeleza uhai na uzima na urithi na kizazi ni lazima mbegu hiyo itolewe kutoka kwenye kuhifadhiwa na itupwe katika moyo wa ardhi, kisha ife na izikwe na kuchipuka ndipo iweze kuendeleza kizazi kwa hiyo mbegu katika mukthadha wa wayahudi inaitwa ZERA ikimaanisha UZAO 

Mwanzo 22:12-18 “Malaika wa BWANA akamwita Ibrahimu mara ya pili kutoka mbinguni akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”

Yesu alikuwa anatambua kwamba ni lazima ajidhabihu yeye mwenyewe kwaajili ya kuufikia ulimwengu, alifahamu wazi kuwa yeye hakuja kwaajili ya wayahudi pekee, bali alikuja kwaajili ya ulimwengu mzima, alifahamu kuwa anahitajika sio na wayunani pekee bali na ulimwengu mzima na kwa sababu hiyo, kujidhabihu kwaajili ya ulimwengu mzima kungerahisisha ukombozi utakaozaa matunda kwa Mungu wetu yaliyo mengi, Lakini wakati huo huo Yesu aliwataka wanafunzi wake wote ikiwa ni pamoja na wewe na mimi kuwa na ufahamu ya kuwa maisha ya uanzilishi wa kitu chchote yanahusisha kujitoa na kujidhabihu na matunda yake yangelikuja kuonekana mbeleni!, Yeye kama Uzao wa Ibrahimu ilikuwa ni lazima ajitoe sadaka yeye mwenyewe kwa hiyari ili mataifa yote waweze kubarikiwa

Tito 2:11-14 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa; tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu; ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi yote, na kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema.”

Waefeso 5:1-2 “Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; mkaenende katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato.”

Maandiko hayo yanadhihirisha wazi kuwa kusulubiwa kwa Yesu Kristo halikuwa tukio la kupangwa na wazee na wakuu wa makuhani, lakini lilikuwa ni tukio la Yesu Kristo mwenyewe kujidhabihu na kukubali kufa na kufufuka kutoka kwa wafu ili atukomboe wanadamu, Yeye alikuwa  ni chembe ya ngano ambayo ilikuwa lazima ianguke ili kusababisha mazao mengi sana duniani.                      

Chembe ya ngano isipoanguka!.

Yoahana 12:23-25 “Naye Yesu akawajibu, akasema, Saa imefika atukuzwe Mwana wa Adamu. Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.”

Yesu anatumia msemo huu  wa chembe yaani mbegu ya ngano kama mfano (Metaphor)  kuonyesha kuwa mbegu ili iweze kuleta mavuno mengi sana ni lazima ianguke, izikwe ardhini kisha inapochipuka yaani kuota na kustawi inaleta mavuno makubwa sana, kanuni hii ni kanuni ya kilimo lakini ni kanuni ya kiroho na kanuni ya kawaida katika maisha.

Yesu anaonyesha kuwa wakati mwingine ili mtu aweze kuzaa matunda, hakuna budi watu wajikane nafsi na kujidhabihu kama yeye, lakini sio hivyo tu kuishi maisha ya kumfuata Yesu na kumpendeza vile vile kunahitaji kujikana nafsi, Ni lazima ujikane ili uweze kuishi maisha matakatifu nay a mfano, bila kujikana ni ngumu kuona mazao

Luka 9:22-25 “akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka. Akawaambia wote, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha. Kwa kuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, au kujipoteza mwenyewe?

Chembe ya ngano isipoanguka hakuna lolote linaloweza kutokea, watu wasipojidhabihu na kujioa hakuwezi kutokea mabadiliko yoyote chanya katika jamii, mambo mengi tunayoyaona duniani na kuyafurahia wakati mwingine yamegharimu maisha ya watu wengine lakini wengi wanafaidika leo kutokana na kuumia kwa watu wengine, hususani waanzilishi wa mambo, Imani, mataifa, ustawi, uanzishwaji wa taasisi yoyote ile, upatikanaji wa Amani na kadhalika, huwa haviwezi kupata usitawi bila watu kujikana, kujiyoa na kujidhabihu, maisha ya kujitoa kwaajili ya jamii yanaweza kuumiza wachache lakini yakanufaisha wengi, Leo hii tunaushangilia wokovu na kujivunia lakini yaligharimu maisha ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo aligharimika pale msalabani na kwa kupigwa kwake tumepona

Marie Curie ambaye ni mgunduzi wa tiba ya kutumia mionzi (Radiation in Medicine) alifariki dunia tarehe 04 Julai 1934 huko ufaransa akiwa na miaka 66, Mwanamke huyu aliyekuwa mwanasayansi alihatarisha maisha yake hata kufa baada ya kuathiriwa na mionzi hiyo alipokuwa anafanya kazi za kitafiti na matumizi ya tiba ya mionzi ya (radium and Plonium) ambayo leo imekuwa msaada mkubwa sana katika tiba ya kiuchunguzi ya mionzi kama X-Rays

Katika maisha wakati mwingine mambo hayawezi kutokea mpaka watu wengine wamesimama kidete na kuhatarisha maisha yao au hata kufa kwaajili ya kusababisha mabadiliko yatokee, Mahatma Gandhi alijitoa maisha yake kusababisha nchi ya India kupata uhuru wake  kutoka kwa waingereza akianzisha harakati za kuandamana bila kufanya ghasia, akivumilia vifungo mbalimbali na hata wakati mwingine aliacha kula yaani akifunga na kujinyima ili haki za kibinadamu zipatikane  katika India inayofurahia matunda ya uhuru huo leo.

Wakristo, na watumishi wa Mungu katika mazingira mbalimbali, tunapaswa kuelewa Yesu alikuwa anamaanisha kwamba bila wengine kujitoa muhanga, maisha yao, fedha zao, starehe zao, mifungo yao, kesha zao, maisha ya familia zao, haki, na injili haiwezi kuwafikia watu wa Mungu, umasikini hauwezi kuondoka, unyonge hauwezi kuisha, ukandamizwaji hauwezi kukomeshwa, udhalimu hauwezi kutokomea, maovu yataendelea kuongezeka, amani haiwezi kupatikana, ubaguzi hauwezi kuisha, upendeleo hauwezi kuisha, haki haiwezi kupatikana, na uhuru wa kweli hauwezi kupatikana bila baadhi ya watu kujitoa dhabihu yaani  Chembe ya ngano isipoanguka! Inabakia ile ile!

Faida za kuanguka kwa chembe ya ngano.

Kuanguka kwa chembe ya ngano ni kujitoa au kujidhabihu kwaajili ya Mungu, Neno la Mungu linatueleza kuwa kujitoa ndio dhabihu iliyo hai, takatifu na ya kupendeza, kama mtu anataka kumpendeza Mungu basi ni lazima akubali kujitoa, au kujidhabihu, Kwa nini Mungu alipendezwa na Yesu Kristo hata kujivunia kuwa huyu ndiye mwanangu mpendwa ninayependezwa naye? Sababu kubwa ni kuwa Yesu alijitoa yeye mwenyewe

Warumi 12:1 “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana.”

Wafilipi 2:6-11 “ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

Mwanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo ni yule anayejitoa, unapodai kuwa unamfuata Yesu lakini hujitoi maana yake ni sawa na kuwa hauufuati mfano wake, Yeye mwenyewe anamkana kila mtu anayedai kuwa anamfuata yeye lakini hataki kuteseka kwaajili ya Kristo! Kimsingi huwezi kuwa mwanafunzi wa Yesu kama hutaki kugharimika na kumfuata

Luka 14:27 “Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.”

Kila anayejikana kwaajili ya Yesu Kristo na jamii nafsi yake haitapotea kwani atalipwa uzima wa milele, tunapojitoa na kujidhabihu hata kufa kwaajili ya wengine/kifo au mauti yako inayotokana na kujidhabihu haiwi mwisho badala yake unakuwa mwanzo wa uzima na maisha mapya yenye Baraka nyingi na yenye kukuzalia matunda

Isaya 53:5-11 “Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote. Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake. Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu. Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala hapakuwa na hila kinywani mwake. Lakini Bwana aliridhika kumchubua; Amemhuzunisha; Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi, Ataona uzao wake, ataishi siku nyingi, Na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake; Ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika. Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki Atawafanya wengi kuwa wenye haki; Naye atayachukua maovu yao.”     

Yoahana 12:25-26 “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele. Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu.”

Hitimisho.

Kuishi maisha matakatifu kunahitaji kujikana, kuishi kwaajili ya Kristo kunahitaji kujikana, kuwatumikia watu kunahitaji kujikana, kuanzisha kazi mpya kunahitaji kujikana, kufanya umisheni kunahitaji kujikana, kumtumikia Mungu kunahitaji kujikana, kufanya uinjilisti kunahitaji kujikana, kuimba kwaya kunahitaji kujikana, kuomba kunahitaji kujikana, kukesha kunahitaji kujikana, kila kitu duniani na mafanikio yoyote yale duniani hayawezi kuja kama hatuna kujikana, kuleta maendeleo kunahitaji kujikana, bila kujikana katika jambo lolote lile hakuwezi kuwako na matunda yanayokusudiwa, mwanafunzi ili afaulu mitihani yake anahitaji kujikana, kusoma kunahitaji kujikana, biashara inahitaji kujikana, kilimo kinahitaji kujikana maendeleo yoyote yake yanahitaji kujikana hali kadhalika maisha ya kiroho yanahitaji kujikana hii ndio kanuni ya mafanikio, ni lazima chembe ya ngano ianguke, isipoanguka inabakia ile ile, lakini ikifa ikizikwa inatoa mazao mengi sana hii ni kanuni ya wokovu, ni kanuni ya kiroho na ni kanuni ya maisha,  na ni kanuni ya kuleta mafanikio makubwa duniani chembe ya ngano isipoanguka ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi, Ni dua yangu na maombi yangu wasomaji wangu na wasilikizaji wangu tujitoe kwaajili ya kazi ya Mungu kabla ya kuangalia faida zetu binafsi.               

1Wakorintho 15:36-38 “Ewe mpumbavu! Uipandayo haihuiki, isipokufa; nayo uipandayo, huupandi mwili ule utakaokuwa, ila chembe tupu, ikiwa ni ya ngano au nyingineyo; lakini Mungu huipa mwili kama apendavyo, na kila mbegu mwili wake.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima.

+255718990796