Jumapili, 1 Machi 2026

Umuhimu wa kutunza siri!


Mithali 11:12-14 “Asiye na akili humdharau mwenziwe; Bali mtu aliye na ufahamu hunyamaza. Mwenye kitango akisingizia hufunua siri; Bali mwenye roho ya uaminifu husitiri mambo. Pasipo mashauri taifa huanguka; Bali kwa wingi wa washauri huja wokovu.”



tangulizi:

Kutunza siri ni mojawapo ya jambo la msingi na la muhimu sana katika jamii, siri zinatunzwa kwa sababu ya kuheshimu utu wa mtu, kujenga jamii, kulinda taifa, kutunza na kuonyesha uaminifu, kuudumisha mahusiano, kuepuka kuleta migogoro, kutunza taarifa nyeti na za muhimu, kulinda usalama wa taifa, kulinda heshima ya mtu, kulinda jamii serikali, taasisi au watu dhidi ya madhara mbalimbali, aidha siri hutunzwa kwa makusudi ya kuepusha kumuharibia mtu, kumuaibisha mtu, kusababisha mtu ahukumiwe na jamii, au kukataliwa na jamii, au kutunza ubora wa taarifa za mtu, kutunza siri ni heshima na siri inaweza pia kutunza uhai wa mtu na kuonyesha ukomavu wa Msiri.

Mathayo 1:18-19 “Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri.”

Kutunza siri ni kiwango cha juu sana cha uadilifu, mtu anapokueleza siri yake maana yake amekuamini, kutunza siri wakati mwingine kunasaidia kutunza uhusiano, kunazuia kusambaa kwa taarifa za mafununu, na kunawalinda wengine au taifa au kanisa kupata madhara na kunatunza heshima ya wengine, utunzaji wa siri unawapa watu maisha unampa mtu ujasiri wa kuendelea na maisha mengine na kujiamini, hakuna fani yeyote ile ambayo haina siri, Madaktari na wauguzi wanaapa kutunza siri za wagonjwa, Magereza kuna siri, Polisi kuna siri, waalimu wana siri, wachungaji wanapaswa pia kutunza siri lakini serikalini pia kuna siri, vyombo vyote vya ulinzi na usalama na fani za upelelezi wakati mwingine katika mazingira fulani hasa ya kichunguzi wanapaswa kuwa na siri.

Leo tutachukua muda basi kujifunza somo hili muhimu sana katika maisha, Umuhimu wa kutunza siri na tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya neno siri

·         Umuhimu wa kutunza siri

·         Hatari za kutoa siri


Maana ya neno siri

Mithali 25:7-9 “Kwa maana ni heri kuambiwa, Njoo huku mbele; Kuliko kuwekwa nyuma machoni pa mkuu. Yale uliyoyaona kwa macho, Usitoke nje kwa haraka ili kuyashindania; Usije ukakosa kujua la kutenda hatimaye, Mwenzako atakapokuwa amekuaibisha. Ujitetee na mwenzako peke yake; Bali usiifunue siri ya mtu mwingine;”

Neno la Mungu linaonya na kuagiza juu ya kutokuifunua siri ya mtu mwingine, kimsingi neno la Mungu linatufundisha kuwa hapa duniani ziko siri au yako mambo ambayo kimsingi kama yatawekwa wazi yote yanaweza kusababisha madhara makubwa katika jamii kwa hiyo sio kila jambo linaweza kuwekwa wazi, hii ni kuanzia katika ngazi ya ndoa na familia mpaka ngazi ya taifa sasa basi tunapotaka kujifunza somo hili umuhimu wa kutunza siri kwanza ni muhimu kwetu kuelewa maana ya neno siri, Siri ni nini hasa kwa mujibu wa tafasiri za kibiblia.

Neno SIRI Katika Biblia ya Kiebrania linasomeka kama neno “Sôd” au “Sâthar” Neno hili limejitokeza katika biblia ya KJV mara 82 likitajwa katika kiingereza kama neno “Hide”, mara 72, “Secret” mara 4 “Close” mara 2, “Conceal” mara 1 na “Variant” mara 1 “Absent” 1 na “Surely” mara 1 kwa hiyo neno siri maana yake ni Mazungunzo au maandishi au maneno au sauti, au taarifa zilizofichwa, ni taarifa za siri, ni taarifa zilizofungwa, au taariza zinazolindwa, au zisizotakiwa kuwekwa wazi, zisizotakiwa kufunuliwa, kwa kiyunani ni “Mystērion” sawa na neno la kiingereza “mystery  yaani mambo ambayo hayajawekwa wazi, mambo ambayo yamefichwa aidha na Mungu au Serikali au na mtu binafsi. Kuficha, kufunga mdomo, kufanya kazi chini ya njia za kificho “undercover”, kuendesha chini chini, usiri.

Kumbukumbu 29:29 “Mambo ya siri ni ya Bwana, Mungu wetu; lakini mambo yaliyofunuliwa ni yetu sisi na watoto wetu milele, ili tuyafanye maneno yote ya sheria hii.”

Kwa hiyo jambo linapokuwa siri maana yake limekusudiwa kubaki kati ya mtu ama kundi fulani tu, na halipaswi kujulikana na wengine ama linabaki na mtu fulani bila mtu huyo kuliweka wazi kwa wengine, siri ni jambo la ndani, linaishia huko huko,  hulitangazwi, au huwezi kulisema kabla ya wakati, au halipaswi kusemwa kwa yeyote wala kujulikana na wakati mwingine ili kulitunza linaweza kuhusisha kiapo, swala linalopaswa kuheshimiwa na kusitiriwa isipokuwa kwa idhini tu, Mungu ni msiri kwa hiyo usiri ni tabia ya uadilifu, fikiria kama Mungu angeamua kuweka wazi mambo ya kila mtu duniani ingekuwaje? Au fikiria kama mitandao ya kijamii au ya simu za mkononi ikiamua kuweka wazi au kuutangazia umma kila ulichowasiliana kwa maneno au kwa maandishi je unadhani ingekuwaje kwa hiyo utakubaliana na maandiko kuwa kuficha siri ni kwaajili ya utukufu wa Mungu pia na ni uadilifu wa hali ya juu.

Mithali 25:2-3. “Ni utukufu wa Mungu kuficha jambo; Bali ni utukufu wa mfalme kuchunguza jambo. Mbingu huenda juu sana, na nchi huenda chini; Lakini mioyo ya wafalme haichunguziki.”

Umuhimu wa kutunza siri.

Nadhani mpaka sasa baada ya kuwa umefahamu maana ya siri vilevile utakuwa umeanza kuelewa umuhimu wa kutunza siri na hatari ya kuvujisha siri, siri zinaweza kuwa na maana kubwa sana endapo zitatunzwa na vilevile zinaweza kuwa na madhara makubwa sana endapo zitawekwa wazi, siri zinalinda usalama wa ndoa, usalama wa jamii, usalama wa mtu, usalama wa taasisi na usalama wa taifa, na kadhalika, kwa ujumla kutunza siri kuna uhusiano wa moja kwa moja na maswala ya uadilifu, chukulia kuwa umeugua jipu sehemu za siri, na muuguzi akakutibu kwa kulipasua jipu lako, kisha baada ya kukuhudumia habari za maumbile yako na utupu wako zikawa nimeenea mtaani? Au chukulia kuwa umekwenda kuungama na kutubu kwa mchungaji fulani, kisha baada ya muda habari za maungamo yako na toba yako zikawa zimeanikwa nje ya ofisi, au Serikali imetengeneza mitihani kwaajili ya darasa fulani kwa nchi nzima kisha mtihani wa somo fulani ukavuja kabla ya wakati wake  na labda watahiniwa wako milioni moja nukta mbili 1.2 nchi nzima kwa mwaka huo, Baraza la mitihani litatakiwa kuubadilisha mtihani huo kwa nchi nzima na kuuchapa tena na kuusambaza tena kwa wakati, unadhani serikali itapata hasara kiasi gani kwa mtihani mmoja kuvuja? Ambao ulifungwa usijulikane kabla ya wakati wake?  hapo ndipo tunapoelewa na kufahamu kuwa kutunza siri ni swala nyeti sana, hata katika ngazi ya familia na ndoa, chukulia kila unachokifanya mkeo anakwenda kukielezea kwa mama yake yaani mama mkwe wako kwa undani kabisa kisha ukakisikia utajisikiaje?, kuna mambo yakiwa siri yanaleta manufaa kwa jamii, chukulia kijana amebakwa au kulawitiwa kisha akatajwa wazi kwa jina lake halisi na akapigwa picha zake na zikawa wazi au jina lake likatajwa kama lilivyo katika vyombo vya habari, je hakuna madhara kwa makuzi ya huyo kijana? Na jamii yake je itakuwaje kesho yake na maisha yake hapo ndipo tunapopata ujuzi na hekima ya umuhimu wa kutunza siri, inawezekana katika maisha haya kuna mambo ambayo wewe hungependa yafunuliwe au watu wayajue kwa sababu yanaweza kukuaibisha au kufanya wewe upotee au kuchukua maamuzi mabaya sana ambayo hungeyachukua kama siri isingeliwekwa wazi aidha mambo hayo umeyafanya au umefanyiwa kila mwanadamu anayo siri fulani kwa hiyo siri ni sehemu ya maisha ya mwanadamu kwa hiyo yako mambo ambayo kila mwanadamu hangependa hata yeye mwenyewe kuyakumbuka au kukumbushwa,  kwa hiyo siri ina umuhimu katika maisha ikitunzwa, kufichua siri kulileta laana kwa Kanaani mtoto wa Hamu kwa sababu baba yake yaani Nuhu alipokunywa mvinyo akalewa na alipokaa uchi yeye hakuitunza siri na badala yake akaianika kwa kila mtu Nuhu alipoamka usingizini alimlaani aliyetoa siri na aliwabariki walioficha siri, Hakuna anayependa kuanikwa

Mwanzo 9:20-27 “Nuhu akaanza kuwa mkulima, akapanda mizabibu; akanywa divai, akalewa; akawa uchi katika hema yake. Hamu, baba wa Kanaani, akauona uchi wa baba yake, akawaeleza ndugu zake wawili waliokuwa nje. Shemu na Yafethi wakatwaa vazi, wakalitanda mabegani mwao wote wawili, wakaenda kinyumenyume, wakaufunika uchi wa baba yao; na nyuso zao zilielekea nyuma, wala hawakuuona uchi wa baba yao. Nuhu akalevuka katika ulevi wake, akajua mwana wake mdogo alivyomtendea. Akasema, Na alaaniwe Kaanani; Atakuwa mtumwa kabisa kwa ndugu zake. Akasema, Na atukuzwe BWANA, Mungu wa Shemu; Na Kaanani awe mtumwa wake.Mungu akamnafisishe Yafethi, Na akae katika hema za Shemu; Na Kaanani awe mtumwa wake.”

-          Kutunza siri ni ishara ya ukomavu, uadilifu na uaminifu – Mtu yeyote mkomavu wa busara na mkomavu wa kiroho anawajibu wa kuwa mtu wa kutunza siri, Kimsingi hata Mungu mwenyewe huweka siri zake kwa watu waminifu, kibiblia mtu asiyetunza siri huitwa mtu asiye na akili, wasiotunza siri katika jamii hupewa majina ya dharau na kutokuheshimika, huitwa wambeya, huitwa watu wasio na kifua, huitwa watu wenye friji haligandishi.

Mithali 11:12-13 “Asiye na akili humdharau mwenziwe; Bali mtu aliye na ufahamu hunyamaza. Mwenye kitango (Msengenyaji) akisingizia hufunua siri; Bali mwenye roho ya uaminifu husitiri mambo.”

-          Kutunza siri ni ishara ya kuwa mtu wa haki  - Maandiko yanamtaja Yusufu mumewe Mariamu mama yake Yesu kuwa alikuwa mtu wa haki, yeye alikuwa na ukomavu ya kuwa kila mwanadamu anakosea na hakuna mtu mkamilifu, alimpenda sana Mariamu na alipokuwa amemchumbia aligundua kuwa ana mimba, kwa mujibu wa torati ya Musa kama sio ufafanuzi wa Malaika kuwa ilikuwa mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, Mariamu alipaswa kutolewa kuulizwa na kupigwa mawe kwa dhambi ya zinaa, lakini Yusufu hakutaka Mariamu aaibishwe na pia alifikiri sana kuhusu maisha ya Mariamu na mwanae aliona aache maisha yaendelee yeye angeliweza kuoa mke mwingine, watu wasio na haki huaibisha wengine kwa kuanika wazi siri zao na kuwadhalilisha wengine.

Mathayo 1:18-21. “Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri.Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao.”

-          Kutunza siri kunadumisha mahusiano – Watu wanaotunza siri katika jamii wanaheshimika sana lakini wale wasiotunza siri wanaitwa hawana akili, wapumbavu, katika jamii yetu sisi wanaitwa wambeya, kuti kavu au watu ambao wana friji bovu, yaani friji lisilogandisha, ni nani atakufurahia kama anakuelezea mambo yake kisha unakwenda kumuanika, hii imekuwako hata makanisani, unamwamini mtu fulani unakwenda kukiri na kuungama dhambi zako kwake kesho kutwa anakuanika na kukutoa kwenye bomba, mnakwenda kupatanisha ndoa yenu kesho kutwa unatolewa mfano kwenye mahubiri, ukitunza siri za watu utaheshimiwa, kwa kuwa unatunza mahusiano mazuri ya watu kinyume cha hapo unaweza kusababisha fitina na mafarakano katika jamii

Mithali 25:8-9 “Usitoke nje kwa haraka ili kuyashindania; Usije ukakosa kujua la kutenda hatimaye, Mwenzako atakapokuwa amekuaibisha. Ujitetee na mwenzako peke yake; Bali usiifunue siri ya mtu mwingine;”

-          Kutunza siri kunakufanya uaminiwe na Mungu – Kuna mambo mengi sana ambayo Mungu aliyaweka wazi kwa Mariamu kuhusu mtoto Yesu na kama Mariamu asingelikuwa na kifua, Yesu angehujumiwa mapema sana Lakini Mariamu alikuwa mtu wa siri aliweka mambo moyoni, wakati mwingine Mungu hukufunulia jambo fulani ambalo labda unatakiwa kuliombea au ni maono ya siku zijazo na kwa sababu hiyo hayapaswi kusemwa, lakini kwa bahati mbaya ili watu wajionyeshe kuwa wao ni maalumu sana wanaweka wazi maono hayo badala ya kuyaweka moyoni na wamejikuta wanapoteza hata huduma zao au wanachukiwa kwa sababu ya kuropoka ropoka hivyo, Marimau alitunza moyoni mwake, maana yake alikuwa na siri kuhusu mambo makuu ya mwanaye yaani Yesu

Luka 2:15-19 “Ikawa, malaika hao walipoondoka kwenda zao mbinguni, wale wachungaji waliambiana, Haya, na twendeni mpaka Bethlehemu, tukalione hilo lililofanyika, alilotujulisha Bwana. Wakaenda kwa haraka wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule mtoto mchanga amelala horini. Walipomwona wakatoa habari waliyoambiwa juu ya huyo mtoto.Wote waliosikia wakastaajabu kwa hayo waliyoambiwa na wachungaji. Lakini Mariamu akayaweka maneno hayo yote, akiyafikiri moyoni mwake.”

-          Kutunza siri kunaepusha migogoro, mafarakano na hasara – watu wasioweza kuficha siri husababisha migogoro, mafarakano na hasara, daraja la chuki hujengeka kati ya watu waliowekwa wazi siri zao na aliyeweka wazi siri, usalama wa ndoa, familia, na hata taifa na taasisi, unaweza kuyumbishwa sana endapo watu watatoa siri na ndio maana wakati mwingine ili kutunza siri hizo viapo vinahusika katika kuhakikisha kuwa mtu ana apa kwa imani yake ili kutunza siri, hata hivyo kwa bahati mbaya wanadamu wanapenda umbeya na mtu akiwa na kitu moyoni hudhani kuwa akikitoa ndio atapata umaarufu kumbe anajivunjia heshima usitoe siri za watu.

Mithali 16:27-28 “Mtu asiyefaa kitu huchimba shimo la madhara; Katika midomo yake mna moto uteketezao. Mtu mshupavu huondokesha fitina; Na mchongezi huwafarakanisha rafiki.”

-          Kutunza siri kunahifadhi Usalama wa taifa na nchi – Serikali ina mambo nyeti, yanayohusu utunzaji wa nyaraka, ulinzi na usalama, mipango mikakati ya kitaifa, Serikali ina siri za kiusalama, siri za kiuchunguzi, siri za maamuzi ya ndani, na siri za watu,  siri hizo lazima zilindwe kwa sababu zinahusisha ustawi wa wengi na zinaweza kuleta madhara makubwa endapo zitavuja, sasa kama mambo yatavuja usalama wa nchi raia na viongozi unaweza kuwapo hatarini,  kwa hiyo kama u mfanya kazi katika sekta ya umma au serikalini na katika taasisi yoyote ile basi unapaswa kuwa na uwezo wa kutunza siri kwa kuheshimu mamlaka zilizoko, aidha watu wanaofanya kazi za za kikatibu au kwenye steshenari wanapaswa kuwa wasiri wa nyaraka za watu kwa uaminifu unapoapishwa usifanye tofauti na kiapo chako kiapo ni nadhiri hivyo ukishindwa kutimiza nadhiri umefanya upumbavu, kuweka nadhiri maana yake ni kujifunga au kuweka kiapo ya kuwa utafanya jambo kwa jina la Bwana hivyo kutokutimiza ahadi yako kwa Mungu kunaweza kukuponza, tafadhali sana hakikisha unatunza siri za kazini kwako, taifa lako na familia yako, rafiki zako, ndugu zako na kadhalika.

Kumbukumbu 23:21-23 “Utakapoweka nadhiri kwa Bwana, Mungu wako, usiwe mlegevu katika kuiondoa; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, hataacha kuitaka kwako; nayo hivi itakuwa dhambi kwako. Lakini ukijizuia usiweke nadhiri, haitakuwa dhambi kwako. Yaliyotoka midomoni mwako yashike kuyafanya; kwa mfano wa ulivyomwekea nadhiri Bwana, Mungu wako, ni sadaka ya hiari uliyoahidi kwa kinywa chako.”

Muhubiri 5:4-6 “Wewe ukimwekea Mungu nadhiri, usikawie kuiondoa; kwa kuwa yeye hawi radhi na wapumbavu; basi, uiondoe hiyo uliyoiweka nadhiri. Ni afadhali usiweke nadhiri, Kuliko kuiweka usiiondoe. Usikiache kinywa chako kuukosesha mwili wako; wala usiseme mbele ya huyo malaika ya kwamba umepitiliwa; kwani Mungu akukasirikie sauti yako, na kuiharibu kazi ya mikono yako?              

-          Kutunza siri ni kuvuta muda mpaka baada ya wakati – Kuna siri ambazo haziwezi kufunuliwa kwa wakati fulani ili kuepusha madhara, na zinaweza kufunuliwa wakati muafaka ukifika ili mambo yasiharibike, kwa mfano mtihani unakuwa ni nyaraka ya siri kabla haujafanyika na siri ya mtihani huishia katika chumba cha mtihani na kisha karatasi za majibu hugeuka kuwa nyaraka ya siri mpaka mtihani utakaposahihishwa, baada ya majibu siri ya mtihani humalizika na mitihani hugeuka kuwa mitihani iliyopita maarifu kama Past papers, Yohana mbatizaji alipotaka kuzaliwa ililazimika baba yake kuwa bubu kwanza mpaka kijana alipozaliwa ndipo siri ilipowekwa wazi,kuwa alitokewa na malaika, tunajifunza hapo kuwa kuna mambo mengine hayapaswi kusemwa kwanza mpaka wakati wake utakapofika ndipo inapoweza kuwekwa wazi kwani mtu anaweza kuropoka kwa kiwewe kabala ya wakati, Malaika alijua kuwa Zekaria anaweza kuropoka maneno ya kutikuwa na imani hivyo mbingu zilitaka awe kimya mpaka mtoto alipozaliwa kwa hiyo nabii Zekaria alikuwa bubu mpaka Yohana alipozaliwa.

Luka 1:5-20 “Zamani za Herode, mfalme wa Uyahudi, palikuwa na kuhani mmoja, jina lake Zakaria, wa zamu ya Abiya, na mkewe alikuwa mmojawapo wa uzao wa Haruni, jina lake Elisabeti. Na wote wawili walikuwa wenye haki mbele za Mungu, wakiendelea katika amri zote za Bwana na maagizo yake bila lawama.Nao walikuwa hawana mtoto, maana Elisabeti alikuwa tasa, na wote wawili ni wazee sana. Basi ikawa, alipokuwa akifanya kazi ya ukuhani katika taratibu ya zamu yake mbele za Mungu, kama ilivyokuwa desturi ya ukuhani, kura ilimwangukia kuingia katika hekalu la Bwana ili kufukiza uvumba. Na makutano yote ya watu walikuwa wakisali nje saa ya kufukiza uvumba. Akatokewa na malaika wa Bwana, amesimama upande wa kuume wa madhabahu ya kufukizia. Zakaria alipomwona alifadhaika, hofu ikamwingia. Lakini yule malaika akamwambia, Usiogope, Zakaria, maana dua yako imesikiwa, na mkeo Elisabeti atakuzalia mtoto mwanamume, na jina lake utamwita Yohana. Nawe utakuwa na furaha na shangwe, na watu wengi watakufurahia kuzaliwa kwake. Kwa sababu atakuwa mkuu mbele za Bwana; hatakunywa divai wala kileo; naye atajazwa Roho Mtakatifu hata tangu tumboni mwa mamaye. Na wengi katika Waisraeli atawarejeza kwa Bwana Mungu wao.Naye atatangulia mbele zake katika roho ya Eliya, na nguvu zake, ili kuigeuza mioyo ya baba iwaelekee watoto, na kuwatilia waasi akili za wenye haki, na kumwekea Bwana tayari watu waliotengenezwa.  Zakaria akamwambia malaika, Nitajuaje neno hilo? Maana mimi ni mzee, na mke wangu ni mkongwe wa siku nyingi. Malaika akamjibu akamwambia, Mimi ni Gabrieli, nisimamaye mbele za Mungu; nami nimetumwa niseme nawe, na kukupasha habari hizi njema. Na tazama! Utakuwa bubu, usiweze kusema, mpaka siku ile yatakapotukia hayo, kwa sababu hukuyasadiki maneno yangu; nayo yatatimizwa kwa wakati wake.”

Habakuki 2:2-3 “Bwana akanijibu, akasema, Iandike njozi ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili aisomaye apate kuisoma kama maji. Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia.”

Hatari za kutoa siri.

Nadhani kama umefuatilia vizuri somo hili hatua kwa hatua utakuwa unaona pia madhara ya kutoa siri au hatari za kutoa siri, kutoa siri za mtu kunaweza kusababisha madhara makubwa na hata kusababisha kifo, watu wote duniani wana siri zinaweza kuwa siri nzuri au zinaaweza kuwa siri mbaya, kutoa siri kunaweza kukugharimu sana maisha yako, kunaweza kukujenga au kunaweza kukuharibu  na kunaweza kukubomoa, kwa hiyo mtu anapotaka kutoa siri ni lazima ajiulize mara mbilimbili anaitoa kwa nani na kwa manufaa gani na kama umeapishwa kutokutoa siri basi usizitoe kwa usalama wako, kwa nini usitoe siri?.

-          Kutoa siri ni ishara ya kukosa uaminifu na uadilifu – Ulimwamini mtu ukampa siri yako kisha yeye akaamua kukuanika na kuitoa ni Ishara ya kuwa mtu huyu sio mwaminifu na hana uadilifu, anapoitoa siri hiyo inaweza kuyagharimu maisha yako, usalama wako na hata kusababisha kifo, huu ni usaliti wa hali ya juu, sawa tu na jinsi Yuda alivyowaongoza watu waliokuja kumkamata Yesu, kwa sababu alijua kuwa Yesu atakuwa eneo gani na sehemu gani, anapatikana wapi na mida gani na akawaongoza maadui, wa Yesu mpaka kwenye bustani ya Geththemane. Watu wengi wamedhuriwa na wale waliowaamini, waliodhani kuwa watawatunzia siri zao hao hao ndio wakawa sababu ya uharibifu na maumivu mengi katika maisha, kwa hiyo tunajifunza pia usimpe siri yako mtu ambaye bado hujamuelewa, mtu anayeweza kukudhuru ni yule ambaye anakujua nje ndani ndani nje lakini sio hivyo tu Shetani hupenda kuwatumia watu wanaotujua vema ili kukuharibia maisha yako na kukuletea uhungu mkubwa katika maisha kwa hiyo usimuamini kila mtu wala usitoe siri yako kwa kila mtu, na kama unajua mambo ya mtu usiyatoe mpaka kwa idhini yake au umuone yeye mwenyewe kwanza ili kupata uhakika.

Zaburi 41:9 “Msiri wangu tena niliyemtumaini, Aliyekula chakula changu, Ameniinulia kisigino chake.”

Luka 22:47-48 “Basi alipokuwa katika kusema, tazama, mkutano wa watu, na yule aitwaye Yuda, ambaye ni mmoja wa wale Thenashara, amewatangulia. Akamkaribia Yesu ili kumbusu.Yesu akamwambia, Yuda, wamsaliti Mwana wa Adamu kwa kumbusu?

-          Kutoa siri kunaweza kusababisha madhara na hasara kwa wengine na taifa – Ziko siri ambazo zikitolewa zinaweza kuwa na madhara makubwa kwa mtu, watu au taifa na kusababisha hasara, upotevu na uharibifu au uvunjifu wa mahusiano, kama kifua chako hakiwezi kustahimili kutunza vitu basi ni muhimu kwako ukafanya tathimini kwanza kabla ya kuropoka unayotaka kuyaropoka, Samsoni alitoa siri yake kwa mwanamke wa kifilisti aliyekuwa mpelelezi ambaye aliweza kusababisha madhara kwa Samsoni na kuharibu maisha yake na huduma.

Waamuzi 16:15-21 “Mwanamke akamwambia, Wawezaje kusema, Nakupenda; na moyo wako haupo pamoja nami? Umenidhihaki mara hizi tatu, wala hukuniambia asili ya nguvu zako nyingi. Ikawa, kwa vile alivyomsumbua kwa maneno yake kila siku, na kumwudhi, roho yake ikadhikika hata kufa.Ndipo alipomwambia yote yaliyokuwa moyoni mwake, akamwambia, Wembe haukupita juu ya kichwa changu kamwe; maana mimi nimekuwa Mnadhiri wa Mungu, tangu tumboni mwa mama yangu; nikinyolewa, ndipo nguvu zangu zitanitoka, nami nitakuwa dhaifu, nitakuwa kama wanadamu wenzangu. Delila alipoona ya kuwa amemwambia yote yaliyokuwa moyoni mwake, akatuma mtu akawaita wakuu wa Wafilisti, akisema, Njoni huku mara hii tu, maana ameniambia yote aliyo nayo moyoni mwake. Ndipo wakuu wa Wafilisti wakamwendea wakachukua ile fedha mikononi mwao.Naye akamlaza usingizi magotini pake. Kisha akamwita mtu akavinyoa vile vishungi saba vya nywele za kichwa chake; akaanza kumsumbua, nguvu zake zikamtoka. Kisha akasema, Samsoni, Wafilisti wanakujia. Akaamka katika usingizi wake, akasema, Nitakwenda nje kama siku nyingine, na kujinyosha. Lakini hakujua ya kuwa Bwana amemwacha. Wafilisti wakamkamata, wakamng'oa macho; wakatelemka naye mpaka Gaza, wakamfunga kwa vifungo vya shaba; naye alikuwa akisaga ngano katika gereza.”

-          Kutoa siri kunaweza wakati mwingine kusababisha kumkosea Mungu – Yako mambo ambayo Mungu anaweza kuyafunua kwako au kuyaeleza kwako kama siri na wakati wake ukawa bado, na kama utalisema kabla ya wakati unaweza kuharibu mambo, na kuvuruga mpango wa Mungu, kwani Mungu anao Muda maalumu labda wa kufunuliwa kwa jambo hilo, jua basi ni wakati gani wa kusema na ni wakati gani wa kunyamaza.

Mathayo 17:9 “Na walipokuwa wakishuka mlimani, Yesu aliwaagiza, akasema, Msimwambie mtu ye yote habari ya maono hayo, hata Mwana wa Adamu atakapofufuka katika wafu.”

Muhubiri 3:1-7 “Kwa kila jambo kuna majira yake, Na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu. Wakati wa kuzaliwa, na wakati wa kufa; Wakati wa kupanda, na wakati wa kung'oa yaliyopandwa; Wakati wa kuua, na wakati wa kupoza; Wakati wa kubomoa, na wakati wa kujenga; Wakati wa kulia, na wakati wa kucheka; Wakati wa kuomboleza, na wakati wa kucheza; Wakati wa kutupa mawe, na wakati wa kukusanya mawe; Wakati wa kukumbatia, na wakati wa kutokumbatia; Wakati wa kutafuta, na wakati wa kupoteza; Wakati wa kuweka, na wakati wa kutupa; Wakati wa kurarua, na wakati wa kushona; Wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena;”

-          Kutoa siri kunaweza kusababisha fedheha – Kutoa siri kunaweza kumsababishia mtu mwingine fedheha au wewe unayetoa siri ukajikuta unafedheheka, kutunza siri ni hekima uaminifu na heshima unapokuwa mwaminifu kutunza siri utaaminiwa sio tu na wanadamu bali hata Mungu pia,

Mithali 13:2-3 “Mtu atakula mema kwa matunda ya kinywa chake; Bali nafsi ya mtu haini itakula jeuri.Yeye alindaye kinywa chake huilinda nafsi yake; Bali afunuaye midomo yake atapata uharibifu.”

Yakobo 3:2-5 “Angalieni, twatia lijamu katika vinywa vya farasi, ili wamtii, hivi twageuza mwili wao wote. Tena angalieni merikebu; ingawa ni kubwa kama nini, na kuchukuliwa na pepo kali, zageuzwa na usukani mdogo sana, ko kote anakoazimia kwenda nahodha. Vivyo hivyo ulimi nao ni kiungo kidogo, nao hujivuna majivuno makuu. Angalieni jinsi moto mdogo uwashavyo msitu mkubwa sana.”

-          Kutoa siri kunaharibu uhusiano na kubomoa kuaminika – Mithali 17:9 “Afunikaye kosa hutafuta kupendwa; Bali yeye akashifuye neno hutenga rafiki.” Una rafiki umemuamini unajifunua kwake na kumueleza kila kitu chako kisha kesho unasikia habari zimeenea mtaani, ni wazi kuwa kama hukutaka siri hiyo ifunuliwe kwa watu, kutasababisha mafarakano mgawanyiko na maumivu lakini pia kuvunjika kwa urafiki na uhusiano, kimsingi mtu anapotoa siri zako pia ni kama anatangaza kuwa hakupendi na anakuchukia, neno la Mungu linasema upendo husitiri wingi wa dhambi, kama mtu unampenda hutapenda kuweka wazi mambo yake hata kama ni mabaya kwa hiyo kuanika siri za mtu ni ishara ya kuwa unamchukia mtu huyo, ziko kanuni kwa mfano ambazo haziwezi kutolewa bila kibali cha wenyewe? Kanuni kwa mfano za kutengeneza Cocacola, au Colgate na kadhalika ni siri ya viwanda husika hata katika bidhaa ndogo ndogo watu wana kanuni zao mpaka za kutengeneza maandazi n.k.

1Petro 4:8 “Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi.”

-          Kutoa siri ni kujivunjia heshima – wengi wa watu wanaotoa siri Fulani wanadhani watapata heshima lakini badala yake wanajivunjia heshima, neno la Mungu linasema watu watakaposikia hawatamdharau uliyemtolea siri badala yake utadharauliwa wewe uliyetoa siri, unatoa siri kwa lengo gani? Ni ili mtu asikubalike? ni ili kumchafua mtu? Ni ili wewe uonekane kuwa ni mtu maalumu sana

Mithali 18:6-8 “Midomo ya mpumbavu huingia katika fitina, Na kinywa chake huita mapigo. Kinywa cha mpumbavu ni uharibifu wake, Na midomo yake ni mtego wa nafsi yake. Maneno ya mchongezi ni kama vitoweo; Nayo hushukia pande za ndani za tumbo.”

Neno la Mungu linakutaka kama una neno na mtu muitane ninyi wenyewe na kuyamaliza wenyewe, kwa hiyo unaposikia neno kuhusu mtu mwite yeye mwenyewe kwa ufafanuzi na maonyo na mkilelewana umempata nduguyo mpaka ikishinidkana basi unaweza kumuhesabu kama mtu asiye na lolote

Mathayo 18:15-17 “Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo. La, kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru.”

-          Kutoa siri katika mapenzi ya Mungu – Katika mazingira Fulani mtu anaweza kutoa siri katika mapenzi ya Mungu japo sio hekima kufanya hivyo kwani kunaweza kuhatarisha maisha yako lakini watu wa Mungu wakati mwingine tunapaswa kuwa waaminifu hata kufa, Hatuwezi kufumbia macho uovu, Serikali au taasisi zinazoongozwa na watu, na watu hawa wana Imani na wakati mwingine watu wanaweza kuwa waovu, kama kutakuwa na Rushwa, ufisadi, wizi wa kura, uonevu mauaji, na vitendo vyovyote vile vinavyopingana na haki za binadamu na mambo yote yanayohusisha dhambi na uovu na mambo hayo yako kinyume na mapenzi ya Mungu. Utamuomba Mungu na utatumia hekima au utaratibu wa kisheria, si kwa fujo wala uasi utaionya na kukemea serikali au kutoa taarifa zenye ushahidi juu ya uovu wote unaofanywa na serikali au viongozi wake lakini sio kwa tamaa chuki au uzembe au kwa kusudi la kumchafua mtu, au kutaka sifa, kemea uovu huo, ingawa inaweza kugharimu maisha yako

Matendo 5:26-29 “Ndipo yule jemadari akaenda pamoja na watumishi, wakawaleta, lakini si kwa nguvu, kwa maana waliogopa watu wasije wakawapiga kwa mawe. Walipowaleta, wakawaweka katika baraza. Kuhani Mkuu akawauliza, akisema, Je! Hatukuwaamuru ninyi kwa nguvu, msifundishe kwa jina hili? Nanyi, tazameni, mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu, na mnataka kuileta damu ya mtu yule juu yetu. Petro na mitume wakajibu, wakisema, Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”

Mathayo 14:3-4 “Maana Herode alikuwa amemkamata Yohana, akamfunga, akamtia gerezani, kwa ajili ya Herodia, mke wa Filipo nduguye. Kwa sababu Yohana alimwambia, Si halali kwako kuwa naye.”

Serikali ina haki ya kulinda siri na kuadhibu wale wanaozivunja kwa mujibu wa sheria, lakini serikali haina mamlaka ya kumuua mtu kwa kosa la kuvujisha siri, Mungu anachukizwa na mauaji yanayofanywa kwa jina la kimamlaka kwa sababu uhai ni mali ya Mungu kwa hiyo hakuna mtu mwenye haki ya kuondoa uhai wa mwingine, Mtu akivunja kiapo cha utoaji siri ataadhibiwa kwa mujibu wa sheria ziliowekwa kwa haki, lakini swala la hukumu ya kifo sio haki ya mwanadamu kwa sababu uhai wa mtu ni mali ya Mungu, Uhai ni mali ya Mungu.

Narudia tena ni makosa kutoa siri hata  hivyo si halali kumuua mtu kwa sababu ya kutoa siri na badala yake mtu aliyetoa siri au atakayetoa siri anaweza kushitakiwa kwa kanuni za haki za binadamu, swala la uhai wa binadamu liko mikononi mwa Mungu yeye ndiye mwamuzi mwenye haki, hivyo serikali yoyote ile hairuhusiwi kumuua mtu kwa sababu ametoa siri, badala yake adhabu za kisheria zinapaswa kuchukua mkondo wake hasa kama amehatarisha usalama wa taifa lakini kimaandiko uhai ni mali ya Mungu na hakuna mtu anatakiwa kufa kwa hilo

Yakobo 4:11-12 “Ndugu, msisingiziane; amsingiziaye ndugu yake, au kumhukumu ndugu yake, huisingizia sheria na kuihukumu sheria. Lakini ukiihukumu sheria, huwi mtenda sheria, bali umekuwa hakimu.Mtoa sheria na mwenye kuhukumu ni mmoja tu, ndiye awezaye kuokoa na kuangamiza. U nani wewe umhukumuye mtu mwingine?

Wewe mwenyewe pia unayo haki ya kuweka dhambi zako wazi na kuziungama mbele za Mungu endapo umemkosea Mungu huko utaeleza siri zako na Mungu ni mwaminifu atakupa rehema, kwa sababu kama tunaishi kwa unafiki Mungu sio mnafiki siku ya hukumu ataleta hukumuni kila jambo na kila tendo la siri  

Mithali 28:13 “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; Bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.”

1Yohana 1:8-10 “Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu. Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.Tukisema kwamba hatukutenda dhambi, twamfanya Yeye kuwa mwongo wala neno lake halimo mwetu.”

Muhubiri 12:14 “Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.”          

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 22 Februari 2026

Kombeo la Daudi!


1Samuel 17:38-40. “Ndipo Sauli akamvika Daudi mavazi yake ya vita, akamtia chapeo cha shaba kichwani, akamvika dirii. Naye Daudi akajifunga upanga juu ya mavazi yake, akajaribu kwenda; maana alikuwa hajavijaribu. Daudi akamwambia Sauli, Siwezi kwenda na vitu hivi, maana sikuvijaribu. Basi Daudi akavivua. Akaichukua fimbo yake mkononi, akajichagulia mawe laini matano katika kijito cha maji, akayatia katika mfuko wa kichungaji aliokuwa nao, maana ni mkoba wake, na kombeo lake alikuwa nalo mkononi mwake, akamkaribia yule Mfilisti.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha yetu duniani wakati mwingine adui zetu watatulazimisha kuingia katika vita hata kama sisi ni watu wa Amani, na ni muhimu kwetu kujua kuwa sisi ni askari wa Yesu Kristo kwa hiyo tuwapo duniani tunapigana, tunapigana vita vita inayoonekana na isiyoonekana na kwa sababu hiyo ni lazima kila mmoja wetu apigane vita vilivyo vizuri na kuilinda Imani, Paulo mtume alipokuwa anahitimisha kazi yake ya injili duniani alitoa taarifa kuwa amevipiga vita vizuri.

2Timotheo 4:7-8 “Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda; baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.”

Katika vita zetu duniani ni lazima tuelewe kuwa Mungu ndiye anayetufundisha vita na kwa sababu hiyo ni muhimu kwetu kuwa makini na kujifunza kutoka kwake namna na jinsi tunavyoweza kupigana vita hizo ili tuweze kushinda.

2Samuel 22:33-35 “Mungu ndiye ngome yangu yenye nguvu; Naye huwaongoza wakamilifu katika njia yake. Huifanya miguu yangu kuwa kama ya kulungu; Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. Ananifundisha mikono yangu vita; Hata mikono yangu yaupinda upinde wa shaba.”

Zaburi 18:31-34 “Maana ni nani aliye Mungu ila Bwana? Ni nani aliye mwamba ila Mungu wetu? Mungu ndiye anifungaye mshipi wa nguvu, Naye anaifanya kamilifu njia yangu. Miguu yangu anaifanya kuwa ya kulungu, Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. Ananifundisha mikono yangu vita, Mikono yangu ikaupinda upinde wa shaba.”

Zaburi 144:1-2 “Na ahimidiwe Bwana, mwamba wangu, Anifundishaye mikono yangu vita, Vidole vyangu kupigana. Mhisani wangu na boma langu, Ngome yangu na mwokozi wangu, Ngao yangu niliyemkimbilia, Huwatiisha watu wangu chini yangu.”    

Mungu huwafundisha watu wake vita na namna ya kupigana kwa jina la Bwana na kupata ushindi katika maisha yetu, Moja ya watu waliokuwa na uhodari katika vita ni pamoja na Daudi na watakatifu waliotutangulia wao walikuwa hodari katika vita kwa sababu Mungu aliwafundisha namna ya kupigana kwa usahihi katika maisha haya ya mapigano dhidi ya adui yetu mkuu ambaye ni shetani, maandiko yanawataja kuwa walikuwa hodari katika vita, sisi nasi Mungu na atupe kuwa hodari katika vita sawasawa na mapenzi yake katika jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai

Waebrania 11:32-33 “Nami niseme nini tena? Maana wakati usingenitosha kuleta habari za Gideoni na Baraka na Samsoni na Yeftha na Daudi na Samweli na za manabii; ambao kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba, walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga. Walitiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya wageni.”

Leo tutachukua muda kujifunza kutoka kwa Daudi jinsi Mungu alivyoweza kumtumia kuleta ushindi mkubwa kwa watu wa Taifa lake dhidi ya wafilisti kwa kutumia silaha duni na dhaifu maarufu kama kombeo, na tutajifunza somo hili Kombeo la Daudi kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-

·         Ufahamu kuhusu Kombeo

·         Kombeo la Daudi

·         Kanisa na kombeo la Daudi.


Ufahamu kuhusu Kombeo.

Mojawapo ya silaha ya zamani sana ambayo ilitengenezwa kwa kamba zilizofumwa vizuri au ngozi na kuwekewa kifuko cha ngozi katikati kwaajili ya kuwekea jiwe kisha kuzungushwa na kuliachia jiwe kwa kasi kubwa na kwa ufundi wa kulenga shabaha ni pamoja na kombeo, Kombeo kama silaha iliyotumiwa na Daudi kuleta ushindi dhidi ya Goliath sasa ina umri wa miaka kama 3000, silaha hiyo maarufu kwa lugha ya kiebania kama “Kela David”  au “Qela David” na kwa kiingereza “David Sling” Kiswahili inaweza kuitwa “Kombeo la Daudi” au “Manati ya Daudi”, ni silaha duni na ya zamani sana iliyotumiwa na watu masikini wasiokuwa na uwezo hata wa kununua panga au mkuki, ndiyo silaha iliyotumiwa na Daudi kumuua Goliathi kwa jina la Bwana wa majeshi Mungu wa Israel, jina lingine la kombeo ni teo.

1Samuel 17:43-45 “Mfilisti akamwambia Daudi, Je! Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu yake.Mfilisti akamwambia Daudi, Njoo huku kwangu; nyama yako nitawapa ndege wa angani na wanyama wa mwituni. Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.”

Ni ukweli uliowazi kuwa  ushindi wa Daudi dhidi ya Goliath haukusababishwa na kombeo pekee bali Mungu alihusika nyuma ya ufundi, Imani na ujasiri wa Daudi, Daudi mwenyewe alikuwa na uelewa kamili kuwa Bwana angemtia Goliath katika mikono yake akiwa na uhakika kuwa Mungu haokoi kwa upanga wala mkuki bali kwa nguvu zake.

1Samuel 17:45-47 “Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya Bwana, naye atawatia ninyi mikononi mwetu.”

Maneno  haya ya Daudi yanathibitisha kuwa kulikuwa na zaidi ya kombeo katika vita ile, watu wakati mwingine tunaweza kusema kuwa kombeo la Daudi pia linaweza kuitwa “kombeo la Bwana”, Mungu alihusika kwa asilimia zote kusababisha muujiza ule kupitia silaha duni na ya chini na ya kimasikini sana, Wakristo wakati mwingine tumepambana na maswala magumu sana duniani, na wakati mwingine na watu wakubwa sana  wenye nguvu, wenye akili, wenye utajiri na uwezo, wasemaji wazuri kuliko sisi lakini tunaweza kuwaangusha chini kwa silaha zetu duni na zenye kudharaulika endapo tutazitumia silaha hizo vema, ingawa silaha  za vita vyetu si za mwili lakini tunaelezwa katika maandiko kuwa zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome na kila kitu kinachijiinu kinyume na Mungu.

2Wakorintho 10:4-6 “(maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome ;) tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo; tena tukiwa tayari kupatiliza maasi yote, kutii kwenu kutakapotimia.”

Pamoja na uduni wa kombeo moja ya sifa kubwa ya kombeo ilikuwa ni ni silaha ambayo kamwe haiko kwenye kundi la silaha ya kubahatisha na wale waliojifunza kuitumia wanakiri kuwa inapiga kwa ustadi na kwa umakini mkubwa, kwa hiyo Daudi alikuwa na uzoefu wa siri wa matumizi ya silaha hiyo ambayo aliitumia pia kuua dubu na simba kabla ya kujitokeza hadharani, wapendwa silaha za rohoni kama ukizitumia kwa ustadi zinalenga pale pale na kumaliza kabisa nguvu za adui bila kubahatisha, Kufunga na kuomba na matumizi sahihi ya neno la Mungu hakujawai hata siku moja kuwa kitu cha kubahatisha kama unataka kumpiga adui kwa usahihi basi tumia silaha hizo kwa usahihi.

Wajibu wa kutokuogopa silaha nzito:

Neno la Mungu limeonya kuwa hatupaswi kuogopa silaha za upande wa adui hata kama zitaonekana kuwa na ubora na manufaa kuliko silaha zetu, hatupaswi kuogopa farasi, wala magari ya vita, wala jeshi kubwa, Mungu amesema katika neno lake havipaswi kuogopewa, tunapoingia katika uwanja wa vita vya kiroho kamwe tusiogope nguvu za kibinadamu, wala teknolojia ya vita, wala ufundi wa maneno, wala takwimu ya jeshi kubwa wala uzoefu na ujuzi wa maadui, Mungu alitaka watu wake wamtegemee yeye tu yeye mwenyewe ndiye vita yetu, Mungu haokoi kwa wingi,

Kumbukumbu 20:1-4 “Utokapo kwenda vitani kupigana na adui zako, na kuona farasi, na magari, na watu wengi kuliko wewe, usiwaogope; kwa kuwa Bwana Mungu wako, yu pamoja nawe, aliyekukweza kutoka nchi ya Misri. Na iwe, msongeapo mapiganoni, kuhani na akaribie na kusema na watu, awaambie, Sikizeni, enyi Israeli, hivi leo mwasongea mapiganoni juu ya adui zenu mioyo yenu na isizime; msiche, wala msiteteme, wala msiingiwe na hofu kwa ajili ya wao; kwa maana Bwana, Mungu wenu, ndiye awaandamaye kwenda kuwapigania juu ya adui zenu, ili kuwaokoa ninyi.”

Kumbukumbu 17:16 “Ila asifanye farasi wake kuwa wengi, wala asiwarudishe watu Misri, ili apate kufanya farasi kuwa wengi; kwa kuwa Bwana amewaambia, Tangu sasa msirudie tena njia ile.”

Yoshua 11:1-11 “Kisha ikawa, hapo huyo Yabini, mfalme wa Hazori, aliposikia habari ya mambo hayo, akatuma mjumbe aende kwa Yobabu, mfalme wa Madoni, na kwa mfalme wa Shimroni, na mfalme wa Akshafu, na hao wafalme waliokuwa upande wa kaskazini, katika nchi ya vilima, na katika Araba upande wa kusini wa Kinerethi, na katika Shefela, na katika nchi zilizoinuka za Dori upande wa magharibi, na kwa Mkanaani upande wa mashariki, na upande wa magharibi, na kwa Mwamori, na Mhiti, na Mperizi na Myebusi katika nchi ya vilima, na kwa Mhivi pale chini ya Hermoni katika nchi ya Mispa. Nao wakatoka nje, wao na jeshi zao zote pamoja nao, watu wengi mno, kama mchanga ulio ufuoni mwa bahari kwa wingi, pamoja na farasi na magari mengi sana. Wafalme hao wote wakakutana pamoja; wakaenda na kupanga mahema yao pamoja hapo penye maji ya Meromu, ili kupigana na Israeli. Bwana akamwambia Yoshua, Usiche wewe kwa ajili ya hao; kwani kesho wakati kama huu nitawatoa hali wameuawa wote mbele ya Israeli; utawatema farasi zao, na magari yao utayapiga moto. Basi Yoshua akaenda, na watu wote wa vita pamoja naye, ili kupigana nao hapo penye maji ya Meromu ghafula; wakawaangukia. Bwana akawatia mkononi mwa Israeli, nao wakawapiga, na kuwafukuza hata kufikilia Sidoni ulio mkuu, na hata kufikilia Misrefoth-maimu, tena hata kufikilia bonde la Mispa upande wa mashariki; wakawapiga hata wasiwasaze hata mtu mmoja aliyesalia. Yoshua akawafanyia vilevile kama Bwana alivyomwamuru; akawatema farasi zao, na magari yao akayapiga moto.”

Wakati wote Mungu alifanya vita na adui za watu wake katika namna ya kushangaza sana, na Mungu aliwaonya watu wake kutokuzitumainia silaha za kimataifa na za kifalme, aliwataka watu wake kumtegemea yeye, aliwataka watu wake wawe na ujuzi kuwa sio wingi wa farasi unaookoa, wala sio wingi wa watu unaookoa wala sio ukubwa wa jeshi, tena aliwataka hata wasiombe msaada wa kivita kwa majirani hasa Misri  na hata wakiteka mateka aliwambia farasi zao wazikate mishipa na magari yao ya vita wayachome moto, Mungu anajua kuwa ziko silaha zizisooenakana kwa macho na hata zile zinazoonekana kwa macho na zikadharauliwa na kuonekana kuwa ni silaha duni, Ni ukweli ulio wazi, kuwa Mungu anazitumia nyuma ya mambo kufanya mambo makubwa ya kutisha na kushangaza, Mungu hakutaka watu wajisifie wingi na uwezo wao alitaka watu waelewe na wajue ya kuwa ushindi unatoka kwa Mungu.

Waamuzi 7:1-2 “Kisha Yerubaali, yaani Gideoni, na watu wote waliokuwa pamoja naye wakaondoka na mapema, wakapiga kambi yao karibu na kijito cha Harodi; na kambi ya Midiani ilikuwa upande wao wa kaskazini, karibu na mlima wa More, bondeni. Bwana akamwambia Gideoni, Watu hawa walio pamoja nawe ni wengi mno hata nikawatie Wamidiani katika mikono yao, wasije Israeli wakajivuna juu yangu wakisema, Mkono wangu mwenyewe ndio ulioniokoa.”

Mungu aliwapunguza wanajeshi waliotoka na Gideoni kutoka 32,000 hadi kufikia mia tatu 300 na alimkataza Gideoni kusudi Israel wasijivunie kuwa ushindi walioupata umetokama na wingi wao, katika vita za Bwana wingi haumtishi, wala hauhusiki na wokovu wake, Mungu aweza kutumia silaha duni na watu wachache kusababisha ushindi kwa utukufu wake na kwaajili ya jina lake ili sifa na utukufu zielekezwe kwake!

Zaburi 33:16-17 “Hapana mfalme aokokaye kwa wingi wa uwezo, Wala shujaa haokoki kwa wingi wa nguvu. Farasi hafai kitu kwa wokovu, Wala hamponyi mtu kwa wingi wa nguvu zake.”

Zaburi 20:6-7 “Sasa najua kuwa Bwana amwokoa masihi wake; Atamjibu kutoka mbingu zake takatifu.Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu.” 

Isaya 31:1-3 “Ole wao watelemkao kwenda Misri wapate msaada, na kutegemea farasi; watumainio magari kwa kuwa ni mengi, na wapanda farasi kwa kuwa ni hodari sana; lakini hawamwangalii Mtakatifu wa Israeli, wala hawamtafuti Bwana! Lakini yeye naye ana akili, naye ataleta uovu, wala hatayatangua maneno yake; Bali ataondoka juu ya nyumba yao watendao mabaya, na juu ya msaada wa hao watendao maovu. Basi Wamisri ni wanadamu wala si Mungu, na farasi zao ni nyama wala si roho; na Bwana atakaponyosha mkono wake, yeye asaidiaye atajikwaa, na yeye asaidiwaye ataanguka, nao wote pamoja watakoma.”

Isaya 54:15-17 “Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako.Tazama, nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba mharibu ili aharibu. Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”                 

Kombeo la Daudi

Daudi alikuwa na ujuzi fulani kuhusu Mungu na maagizo yake katika Torati. Alikuwa amekwisha kujifunza kuwa Mungu haokoi kwa upanga wala mkuki, alikuwa na ujuzi kuwa Mungu haokoi kwa kutumia wingi, kwa hiyo alipomwendea adui yake alikuwa na mkoba wa ngozi na ndani yake alikuwa amekunja kombeo yake na alikuwa na mawe matano laini kutoka mtoni, yanaitwa mawe laini kwa sababu yalikuwa na uduara flani yaani yasiyoweza kukata au kuumiza kutokana na kudongoroshwa katika maji, lakini yalikuwa magumu sana, Wakati Goliath alikuwa na vifaa vya kisasa  vya vita, na katika Israel ni mfalme Sauli tu na mwanae Jonathan ndio waliokuwa na uwezo wa kumiliki upanga, watu wengine wote walikuwa na silaha duni na za kimasikini, Daudi alikuwa anatambua kuwa vita ni ya Bwana na kuwa Bwana angewaliwapigania watu wake kwa hiyo Kombeo la Daudi ilikuwa ni silaha inayoonekana ya Mungu asiyeonekana, kulikuwa na kitu cha ziada katika kombeo la Daudi, yeye alionekana ameshika fimbo tu mpaka pale alipoichomoa kombeo lake na kuchagua jiwe laini na adui alisambaratishwa kwa uwezo wa jina la Bwana kupitia jiwe lile moja tu kati ya mawe matano aliyokuwa ameyachagua, kwanini Daudi alikuwa na uhakika wa silaha ile duni kumpa ushindi mkubwa usiokuwa wa kawaida?

-          Daudi alikuwa amefundishwa kupigana, Mungu alimfundisha Daudi vita na matumizi ya silaha zile duni na zikaonyesha uwezo mkubwa akiwa nyikani, wakati akiwa anachunga kondoo wa baba yake alikuwa amekwisha kujifunza kutumia kombeo, na aliona kombeo ikiwashughulikia Dubu na Simba wanyama ambao ni wakali, aliweza kupambana nao na Mungu akimsaidia, Mungu alimuokoa na wanyama hao wakali

 

1Samuel 17:34-37 “Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai. Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe.”

 

-          Daudi hakutegemea silaha za kifalme, Kulikuwa na nyakati ambapo wafilisti walihodhi teknolojia ya usindikaji vyuma kwa kusudi la kuwazuia Waisrael wasitengeneze silaha, hii ilikuwa mbinu ya kimkakati ya adui ya kuwafanya Israel wawe dhaifu na tegemezi, kwa hiyo watu walioweza kumiliki silaha za vyuma walikuwa ni wafalme au watu matajiri sana wenye kipato cha hali ya juu, kwa hiyo mtu kama Daudi hakuwa na uwezo wa kumiliki silaha za chuma wala hakuwa na ujuzi katika hizo, ilikuwa mtu akitaka kunoa hata jembe ni lazima aende kwa wafilisti, kwa hiyo uhodari wa vita ulikuwa ni katika matumizi ya kombeo, fimbo mawe na vifaa vya shambani, wafilisti walitaka kuwanyima Israel maarifa na dhana za mapigano  ili kujihakikishia ushindi

 

1Samuel 13:19-22 “Basi, hakuonekana mhunzi ye yote katika nchi yote ya Israeli; kwa kuwa Wafilisti walisema, Waebrania wasije wakajifanyizia panga au mikuki; lakini Waisraeli wote hushuka kwa Wafilisti, ili kunoa kila mtu jembe lake, na mundu wake, na shoka lake, na sululu yake; ila walikuwa na tupa za kunolea sululu, na miundu, na mauma, na mashoka; na kwa kuinoa michokoo. Hivyo ikawa, siku ya vita, haukuonekana mkononi mwa mtu ye yote, miongoni mwa watu waliokuwa pamoja na Sauli na Yonathani, upanga wala mkuki; isipokuwa Sauli mwenyewe na mwanawe Yonathani walikuwa navyo.”

 

-          Daudi alikuwa na ufahamu kuwa vita ni ya Bwana, Daudi alikuwa na uelewa wa wazi kuwa wao walikuwa na silaha duni, na walinyimwa teknolojia na hata utengenezaji wa silaha za vita za chuma, watu waliokuwa na silaha katika Israel ni Sauli na mwanae Jonathani, hivyo Daudi aliweka tumaini lake lote kwa Mungu, alielewa kuwa kombeo ilikuwa ni silaha duni sana na haikuwa na mchango wowote kwa mtu ambaye amejivika vyuma mwili mzima lakini alielewa kuwa Mungu angekuwa nyuma ya kombeo na angeliongoza jiwe kupita popote palipo wazi hata kama ni kwenye jicho kwani alijifunza kuwa kombeo lililoongozwa na Bwana halitakosa kulenga shabaha, na mkuki na upanga kama Bwana hayuko navyo haziwezi kuwa silaha za kutisha kwake, watu waliojifunza kutumia kombeo au teo walikuwa na uwezo wa kuitumia kwa usahihi sana tangu nyakati za waamuzi watumiaji wa kombeo walikuwa wanauwezo wa kulenga hata unywele kwa jiwe  na wasikose shabaha kwa hiyo usahihi wa matumizi ya kombeo ulikuwa wa uhakika kwa kiwango cha juu, sana na kwa sababu hiyo Daudi hakuidharau silaha yake ndogo na duni akijua kuwa Mungu ataitumia  

 

1Samuel 17:45   Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.”

 

Waamuzi 20:14-16 “Lakini wana wa Benyamini wakakutanika huko Gibea kutoka katika miji yao, ili watoke kwenda kupiga vita juu ya wana wa Israeli. Hao wana wa Benyamini walihesabiwa siku ile kutoka hiyo miji, watu waume ishirini na sita elfu waliotumia upanga, zaidi ya hao waliokaa Gibea, ambao walihesabiwa watu wateule mia saba. Katika watu hao wote walikuwako watu waume mia saba waliochaguliwa, wenye shoto; kila mmoja alikuwa anaweza kuutupia unywele mawe kwa teo, wala asikose.”

 

Ni kutokana na umahiri wa silaha hii leo hii Idara ya ulinzi ya Israel Israel Defense Force (IDF) wameendeleza silaha ya kisasa kabisa inayoitwa kwa jina hili la kombel la Daudi “David’s Sling” ambayo ilianza kutumika kijeshi mwaka 2017 ikiwa na uwezo wa kuingilia kati na kuharibu mifumo ya ushambuliaji ya maadui kama wakitumia ndege, drones, na mabomu ya mashambulizi ya kisasa Ballistics missiles za uwezo wa aina mbalimbali kuanzia kilomita 40 mpaka 300 katika mifumo ya kivita ya kisasa ya israel      

Kanisa na kombeo la Daudi.

Mungu katika mpango wake hata leo bado ameendelea kulifundisha kanisa lake na kulihimiza, kuendelea kuweka tumaini letu kwake katika maeneo yote, Pamoja na maendeleo ya kitaaluma na teknolpojia iliyoko leo na mpanuko mkubwa wa elimu Bado Mungu anataka tumpe yeye kipaumbele na katika nguvu zake na hekima ya Mungu kuliko nyenzo za kisasa zilizoko duniani, kuhudumu kwetu na kufundisha kwetu na kuhubiri kwetu kamwe kusiangukie katika hekima ya kibinadamu bali tuendelee kuzitegemea nguvu za Mungu katika maisha yetu yote Paulo mtume alikuwa msomi, mwanasheria mkubwa na mwanafalsafa aliyebobea hata hivyo, alimtegemea sana Mungu katika huduma yake kuliko Elimu yake  na uwezo wake wa kushawishi, Mungu hutumia Imani  yetu katika jina lake na upako  hata kuliko vyeti vyetu vya kitaaluma, sio vibaya kuwa na taaluma lakini tusisahahu upako una sehemu muhimu katika maisha yetu ya huduma na utumishi, jumbe zangu zote zinatokana na muongozo wa Roho Mtakatifu kwanza kisha taaluma hufuata baadae katika maandalizi, lakini Mungu Roho Mtakakatifu ni namba moja kwangu.

1Wakorintho 2:4-5 “Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.”   

Paulo mtume alikuwa na ujuzi ya kuwa Mungu anaweza kuwatumia wenye cheo na wenye hekima ya dunia hii, lakini alitahadharisha kuwa Mungu huyatumia mambo manyonge na madhaifu na yaliyodharauliwa, na wadhaifu, kwa sababu Mungu hataki watu wajisifie mbele zake kwa sababu ya uwezo wa kibinadamu, bali kwaajili ya jina lake.

1Wakorintho 1:26-29 “Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.”

Paulo alikuwa na ujuzi ya kuwa Mungu anaweza kumtumia mtu kwa rehema zake na neema yake tu na ya kuwa juhudi za kibinadamu haina mchango wowote katika kutupatia kibali cha Mungu, wala jitidaha za kibinadamu hazina mchango wa kuleta rehema za Mungu kwetu wala matakwa yetu

Warumi 9:10-16 “Wala si hivyo tu, lakini Rebeka naye, akiisha kuchukua mimba kwa mume mmoja, naye ni Isaka, baba yetu,(kwa maana kabla hawajazaliwa wale watoto, wala hawajatenda neno jema wala baya, ili lisimame kusudi la Mungu la kuchagua, si kwa sababu ya matendo, bali kwa sababu ya nia yake aitaye), aliambiwa hivi, Mkubwa atamtumikia mdogo. Kama ilivyoandikwa, Nimempenda Yakobo, bali Esau nimemchukia.Tuseme nini basi? Kuna udhalimu kwa Mungu? Hasha! Maana amwambia Musa, Nitamrehemu yeye nimrehemuye, nitamhurumia yeye nimhurumiaye. Basi, kama ni hivyo, si katika uwezo wa yule atakaye, wala wa yule apigaye mbio; bali wa yule arehemuye, yaani, Mungu.”

Neno la Mungu linatufundisha kuwa kuna namna ambapo Mungu asipohusika kwenye jambo lolote hata tujihusishe vipi jambo hilo haliwezi kuwa na maanikio bila ya mkono wake   na jambo hili ndio liko kwenye siri ya kombeo la Daudi           

Zaburi 127:1 “Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure.”  

Yohana 15:4-5 “Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote.”

Tunajifunza kuacha kuzitegemea Pesa kuliko Mungu kuingilia kati maswala yetu, kuacha kutegemea miundo mbinu bila kumruhusu Roho Mtakatifu katika shughuli zetu, kuacha kutegemea wingi wa watu kuliko uwepo wa Mungu, tulitegemee neno la Mungu kama upanga wa roho kwaajili ya ushindi katika maisha yetu, tuyategemee maombi yetu kuleta matokeo kuliko akili zetu na tumtegemee Mungu kwa Imani hata katika mambo madogo yasiyotatrajiwa, tutumie kile ambacho Mungu amekiweka ndani yetu kwa utukufu wake na tunataona ushindi mkubwa katika maisha yetu na hilo ndio kombeo la Daudi, Bila uwepo wa Mungu kombeo lisingeweza kuwa sababu ya ushindi wa Daudi.

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 15 Februari 2026

Sauti ya kijana huko jangwani!


Mwanzo 21:14-20 “Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia. Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana. Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde.”




Utangulizi:

Kama kuna mojawapo ya matukio magumu sana duniani ni pamoja na tukio la kukataliwa na baba yako aliyekuzaa, maumivu ya kukataliwa na baba yanaweza kusababisha jeraha lisiloweza kukoma, hofu, kukosa kujiamini na kutelekezwa, jambo ambalo linaweza kupunguza kwa kiwango kikubwa uwezo wa kuwaamini watu, lakini pia linaweza kusababisha msongo wa mawazo, kushindwa kujitambua na kutokujitosheleza, inahitajika nguvu ya ziada sana kuweza kuwa kawaida na kuishinda hali ya kukataliwa, Lazima uwe na kitu cha ziada kuweza kujijenga kuwa unastahili na kujikomboa kutoka katika maumivu hayo ya kihisia kwani hali hii inazalisha hali ya kutaka  kujithibitisha.

Haya ndiyo yaliyomkuta Ishmael baada ya kufukuzwa nyumbani kwa baba yake ambaye kimsingi alikuwa tajiri sana wa mifugo fedha na dhahabu, lakini inaelezwa kuwa Ishamel na mama yake walitolewa mikono mitupu, wakipewa maji na mkate tu na hawakuwa hata na mtu wa kuwasindikiza, wala hawakuwa na chakula hata cha akiba, bali tupu.

Mwanzo 13:21-3 “Abramu akapanda kutoka Misri, yeye, na mkewe, na kila alichokuwa nacho, na Lutu pamoja naye, mpaka kusini. Naye Abramu alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu. Akaendelea kusafiri kutoka kusini mpaka Betheli, mahali pale palipokuwapo hema yake kwanza kati ya Betheli na Ai;”

Abrahamu alikuwa ni mtu aliyefanikiwa sana, alikuwa na makundi makubwa ya mifugo, wasimamizi, wafanyakazi, utajiri mkubwa wa fedha na dhahabu, lakini alikuwa ni mtu mwenye jeshi kali lililoweza kupigana vita na wafalme wakubwa katika vita, na moja ya vita maarufu aliyopigana na kuteka nyara ni vita iitwayo “opereshini Lutu”, ambapo alikwenda kupigana kumuokoa Lutu, Jeshi hilo lilikuwa na makomandoo 318 ambao walikuwa wamefunzwa vizuri  

Mwanzo 14:5-16 “Na mwaka wa kumi na nne akaja Kedorlaoma na wafalme waliokuwa pamoja naye, wakawapiga Warefai katika Ashteroth-karnaimu, na Wazuzi katika Hamu, na Waemi katika Shawe-kiryathaimu,na Wahori katika mlima wao Seiri, mpaka Elparani iliyo karibu na jangwa. Kisha wakarudi wakaja mpaka Enmisfati, ndio Kadeshi, wakapiga nchi yote ya Waamaleki, na Waamori waliokaa Hasason-tamari. Mfalme wa Sodoma, na mfalme wa Gomora, na mfalme wa Adma, na mfalme wa Seboimu, na mfalme wa Bela, ndio Soari, wakatoka wakapanga vita panapo bonde la Sidimu; wapigane na Kedorlaoma mfalme wa Elamu, na Tidali mfalme wa Goimu, na Amrafeli mfalme wa Shinari, na Arioko mfalme wa Elasari, wafalme wanne juu ya wale watano. Na bonde la Sidimu lilikuwa limejaa mashimo ya lami. Nao wafalme wa Sodoma na Gomora wakakimbia, wakaanguka huko, nao waliosalia wakakimbia milimani. Wakachukua mali zote za Sodoma na Gomora na vyakula vyao vyote, wakaenda zao. Wakamtwaa Lutu, mwana wa nduguye Abramu, aliyekaa huko Sodoma, na mali yake, wakaenda zao. Mtu mmoja aliyeponyoka akaenda, akampasha habari Abramu Mwebrania; naye amekaa panapo mialoni ya Mamre, yule Mwamori, ndugu ya Eshkoli, na ndugu ya Aneri, na hao walikuwa wamepatana na Abramu. Abramu aliposikia ya kwamba nduguye ametekwa mateka, akawapa silaha vijana wake, waliozaliwa katika nyumba yake, watu mia tatu na kumi na wanane, akawafuata mpaka Dani. Akajipanga apigane nao usiku, yeye na watumwa wake, akawapiga, akawafukuza mpaka Hoba, ulioko upande wa kushoto wa Dameski. Naye akarudisha mali zote, akamrudisha na Lutu nduguye na mali zake, na wanawake pia, na watu.”

Kwa hiyo unapata picha jinsi Abrahamu alivyokuwa mtu mkubwa sana mwenye uwezo mwingi na utajiri na mtu mwenye kumiliki Jeshi lake binafsi, na alipigana na wafalme zaidi ya watano na kuwashinda na kumrejesha Lutu na familia yake nyumbani na mifugo na mali zake sasa anamfukuza mtoto wa kumzaa mwenyewe tena mikono mitupu! Kwa mujibu wa  vitabu vya mafafanuzi ya kiyahudi na tamaduni zake viitwavyo “Talmudi” na “Midrashi” vinaeleza hivi kwa lugha ya kiingereza kuhusu Ishamel “Ishmael’s experience upon being sent away by Abraham was one of severe trauma, desperation and existential abandonment” kwa tafasiri yangu isiyo rasmi wanasema swala la kufukuzwa kwa Ishmael na Abrahimu lilikuwa ni mojawapo ya tukio baya, la kusikitisha, na kutelekezwa kikatili, kusikokuwa kwa kawaida” mtu tajiri mwenye uwezo mkubwa usiokuwa wa kawaida anamtoa mtoto wake wa kumzaa mikono mitupu bila kujali hali yake ya baadaye itakuwaje hata kama alizaliwa na mjakazi!

Mgogoro ulianza wakati Sara alipomshuhudia Ishmael akimdhihaki Isaka siku ile alipofanyiwa ibada ya shukurani kwaajili ya muujiza ule mkubwa wa kuzaliwa kwake Isaka na kuachishwa kunyonya

Mwanzo 21:6-10 “Sara akasema, Mungu amenifanyia kicheko; kila asikiaye atacheka pamoja nami. Akasema, N'nani angemwambia Ibrahimu, Sara atanyonyesha wana? Maana nimemzalia mwana katika uzee wake. Mtoto akakua, akaachishwa kunyonya; Ibrahimu akafanya karamu kuu siku ile Isaka alipoachishwa kunyonya. Sara akamwona yule mwana wa Hajiri Mmisri, ambaye alimzalia Ibrahimu, anafanya dhihaka. Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka.”

Jambo hili halikumfurahisha Abraham, hata hivyo Mungu alimwambia Abrahamu afanye kile ambacho Sara ameagiza

Mwanzo 21:11.-12 “Na neno hilo lilikuwa baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya mwanawe. Mungu akamwambia Ibrahimu, Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa.”

Jambo hili linamuweka Ishmael na mama yake katika wakati mbaya sana sasa wanapitia hali ngumu na ya uchungu sana, tutaliangalia somo hizi Sauti ya kijana Jangwani kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maumivu ya kukataliwa

·         Sauti ya kijana huko jangwani

·         Mungu anamkumbuka kijana huko jangwani

Maumivu ya kukataliwa

Tunawaona Ishmael na mama yake wakiwa jangwani maji yanawaishia na mkate unamalizika hali ya mauti sasa ndiyo inayomzunguka mtoto, akiwa ni kijana wa miaka 16 tu ambaye alilelewa maisha ya kudekezwa kama mtoto pekee nyumbani ghafla maisha yanabadilika na anatupwa jangwani, moyoni ana maumivu makali ya kutupwa na kukataliwa anajiona kama mtu asiye na bahati na ambaye amesalitiwa na baba yake na sio hivyo tu ametelekezwa, Ishmael na mama yake wanachanganyikiwa wamefukuzwa nyumbani nani kama wanatakiwa kuja kufia jangwani.

Mwanzo 21:14-16 “Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia.”  

Maji yamekwisha chakula pia kimeisha ni jambo la kushangaza kuwa wanatupwa hata bila ya chakula cha akiba na wanapotelea katika jangwa anakabiliwa na kiu anachoka na wamekuwa dhaifu, mama yake anamuweka katika kichaka cha nyikani anakimbia mbali ili asimuone mtoto wake anapokata roho ana wasiwasi na hofu ya kuona mauti ikimmaliza mwanae

Kijana anajutia kumdhihaki Isaka anatambua kosa lake ambalo sasa linamletea mateso, anakuwa imara na anapokea mabadiliko toba yake inaonekana kwa ushahidi kuwa alimalizana vizuri na baba yake kwani alielewa upumbavu wake na sasa alimuheshimu Isaka kwa mujibu wa masimulizi ya marabi wa kiyahudi “Rabbinic tradition” (Genesis Rabbah) adhabu hii ilileta toba na mabadiliko makubwa kwani alikuja kumzika baba yake kwa heshima akiwa na Isaka ona:-

Mwanzo 25:8-10. “Ibrahimu akafariki, naye akafa katika uzee mwema, mzee sana, ameshiba siku, akakusanyika kwa watu wake. Isaka na Ishmaeli wanawe wakamzika katika pango ya Makpela, katika shamba la Efroni bin Sohari Mhiti, lielekealo Mamre. Katika lile shamba alilolinunua Ibrahimu kwa wazawa Hethi, huko ndiko alikozikwa Ibrahimu na Sara mkewe.”

Ndugu yangu kutelekezwa hakumaanishi kuwa umefika mwisho wa maisha, kutelekezwa hakumaanishi kuwa Mungu amemalizana na wewe watu wanaweza kukukataa na kukutelekeza lakini Mungu kamwe hawezi kufanya hivyo, Mikono yake bado iko wazi na anaweza kukupokea, Jangwa ndilo linalomfanya mtu kuwa imara na kuacha upumbavu wake, Jangwa lilikuwa eneo la somo kwa Ishmael, alijifunza kusamehe hakumuwekea kinyongo baba yake  Mungu aliisikiliza sauti yake kule jangwani  na alikuwa amemuandalia kisima kizuri cha maji ambayo yangeokoa uhai wake na kumfanya kuwa kijana shujaa,

Zaburi 34:6-9 “Maskini huyu aliita, Bwana akasikia, Akamwokoa na taabu zake zote.Malaika wa Bwana hufanya kituo, Akiwazungukia wamchao na kuwaokoa. Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini. Mcheni Bwana, enyi watakatifu wake, Yaani, wamchao hawahitaji kitu.”

Sauti ya kijana huko jangwani

Mwanzo 21:17-21 “Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana. Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde. Akakaa katika jangwa la Parani; mama yake akamtwalia mke katika nchi ya Misri.”

Jina Ishmael maana yake Mungu amesikia kilio changu, Mungu alisikia kilio cha mtoto, Mungu sio dhalimu hata pale inapoonekana kuwa ndoto zako zimezikwa na unabii kukuhusu umefukiwa katika mchanga, Mungu ataendelea kuwa mwaminifu kwa watu wake na neno lake mbingu ziliitikia sauti jangwani, kijana kweli alikuwa amefukuzwa nyumbani lakini hakuwa amefukuzwa kutoka kwenye uwepo wa Mungu, Mungu alimwambia Hajiri usiogope, na Mungu aliyafunua macho yake na akaona kisima chenye maji, kisima ambacho kimsingi kilikuwapo pale  tayari, watu wengi sio kuwa Mungu amewaacha bali watu wengi wamefungwa macho wasione fursa na ndio maana wanalia, Ni kazi ya Roho wa Mungu kukufunulia fursa, hauna sababu ya kulia lakini unapaswa kuinua macho yako uone.

Unaweza kukataliwa, kuteswa na kufukuzwa na hata kuwekwa nje ya mtandao “Systems” unaweza kutupwa na baba yako wa kiroho kabisa na unaweza usijaliwe na wale waliotakiwa kukujali lakini hili ndio tunalojifunza kuwa kama Mungu nanaweza kusikia kilio jangwani taabu yako haiwezi kunyamaziwa mbinguni, inaweza kunyamaziwa na wanadamu lakini Mungu hawezi kunyamaza, unaweza kufukuzwa, unaweza kuwa na kiu na unaweza hata kusahaulika , lakini Mungu hawezi kuacha kukusikia, utembeleo wa malaika hauzuiliki na hali, na uhakika wa maisha yako ya baadae uko mikononi mwa Mungu, maji yanaweza kuisha, mkate unaweza kumalizika, milango inaweza kufunga na watu wanaweza kukaa kimya lakini Mungu anayemsikiliza Ishmael yuko hata leo yeye hatakuacha ufie jangwani atakufunulia macho yako na atakuelekeza nini cha kufanya, Mungu alikuwa pamoja na Ishamel Mungu hana upendeleo haijalishi wewe ni wa mwanamke muungwana au wa mjakazi.

Mungu anamkumbuka kijana huko jangwani

Mungu alikumbuka agano lake alilolifanya na mama yake kuhusu kijana aliahidi kuwa angemfanya taifa kubwa na kwa sababu hiyo kufa jangwani haukuwa mpango wa Mungu, Mungu alikumbuka mpango wake na Mungu alisikia kilio cha Ishmael Mungu akamkumbuka kijana huko jangwani!

Mwanzo 16:6-11 “Naye Abramu akamwambia Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako. Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake. Malaika wa BWANA akamwona kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika njia ya kuendea Shuri. Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi, nawe unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai. Malaika wa BWANA akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono yake. Malaika wa BWANA akamwambia, Hakika nitauzidisha uzao wako, wala hautahesabika kwa jinsi utakavyokuwa mwingi. Malaika wa BWANA akamwambia, Tazama! Wewe una mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Ishmaeli, maana BWANA amesikia kilio cha mateso yako.”

Mungu alizungumza na Hajiri wakati wa changamoto, Mungu huleta ufumbuzi wakati wa changamoto, Mungu alimwambia asiogope, na Mungu alimfunulia macho kuona kisima cha maji, Mungu alikuwa ameahidi kumfanya Ishamel kuwa taifa kubwa na Ishamel akawa mkuu mno na wafalme 12 walitokea katika viuno vyake

Mwanzo 25:12-17 “Hivi ndivyo vizazi vya Ishmaeli, mwana wa Ibrahimu, ambaye Hajiri, Mmisri, mjakazi wa Sara, alimzalia Ibrahimu. Na haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kwa majina yao, na kwa vizazi vyao. Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli, ni Nebayothi, na Kedari, na Abdeeli, na Mibsamu, na Mishma, na Duma, na Masa, na Hadadi, na Tema, na Yeturi, na Nafishi, na Kedema. Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ni majina yao, katika miji yao, na katika vituo vyao, maseyidi kumi na wawili kwa kufuata jamaa zao. Na hii ndiyo miaka ya maisha ya Ishmaeli, miaka mia na thelathini na saba. Akakata roho, akafa, akakusanyika kwa watu wake.”

Mungu ndiye anayeshikilia maisha yako, mipango yako iko katika mikono yake tangu kuwekwa kwa misingi ya ulimwengu, hakuna bahati mbaya yeye ni muumba mwenye upendo, kila mtu duniani yuko katika mpango wake na ni yeye ndiye anayeziongoza njia zako, na makusudi yake kwako atayatimiza mwenyewe katika mpango wake haijalishi ni vikwazo gani utakutana navyo au ni giza gani liko mbele yako hiyo haimaanishi kuwa Mungu amekuacha ni swala la kufumba na kufumbua tu amini mchakato wa Mungu “trust the process” yeye atakulinda, atakuongoza atakuweka katika njia iliyo sahihi, hakuna anayeweza kuuzuia mpango wake wala makusudi yake, Mungu anaweza kuwainua watu kwaajili yako na wakakutendea mema watakusaidia kulifikia kusudi lako haijalishi watu wamekuchezea kiasi gani lakini Mungu ni mwenye nguvu kuliko wao, Je uko kwenye jangwa gani? Mungu anaisikia sauti yako, hutafia jangwani yeye bado hajamalizana na wewe, Mungu ana ahadi na wewe na ni lazima aitimize!

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima