Jumamosi, 27 Desemba 2025

Kupata na kujuta!

 


1Timotheo 6:6-10 “Walakini utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.”




Utangulizi

Bila shaka umewahi kushuhudia katika maisha haya kama mwanadamu kuwa unaweza kuwa na hamu au shauku ya kupata kitu fulani na ukapambana mpaka ukakipata na baada ya kuwa umekipata ukaanza kujuta moyoni, Hali hii inaweza ikatokea mara baada ya kufanya maamuzi kadhaa katika maisha yetu kisha baada ya maamuzi hayo unasikia hisia za majuto, unajiona kama umefanya maamuzi duni, ya kijinga na kipumbavu au kama umefanya makosa ya kiufundi umekosea malengo, au hujafanya maamuzi sahihi, wakati mwingine maamuzi ya aina hiyo yanaweza kuleta uchungu na hisia hasi na kuathiri afya na maendeleo ya mtu, kimwili, kiroho na kisaikolojia, ingawa kujuta pia kunaweza kujenga hisia chanya na kumfanya mtu kufanya maamuzi mazuri baadaye, maa na yake ni nini?, si kila kitu tunachikitaka na kufanikiwa kukipata duniani kinaweza kutuletea furaha, viko vitu vingine tunaweza tukavitamani sana lakini baada ya kuvipata vinaweza kuwa chanzo cha maumivu makubwa na huzuni na majuto, vitu hivyo inaweza kuwa mali, fedha, vyeo, mahusiano na kadhalika ambavyo tumevipigania kuvipata kwa shauku/tamaa lakini baadaye vinatuletea maumivu.

Yakobo 4:3 “Vita vyatoka wapi, na mapigano yaliyoko kati yenu yatoka wapi? Si humu, katika tamaa zenu zifanyazo vita katika viungo vyenu? Mwatamani, wala hamna kitu, mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata. Mwafanya vita na kupigana, wala hamna kitu kwa kuwa hamwombi! Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu. Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”

Watu wengi sana duniani wametamani sana kupata mali, vyeo, na hata mahusiano Fulani kwa tamaa zao, lakini baadaye walijuta na kulia machozi, ni muhimu sana kupata lolote tunalolitamani katika mapenzi ya Mungu na sio kwa tamaa ya kibinadamu, sio kila kitu tunachokitaka duniani kinaweza kutupa raha, na furaha, vingine vinaweza kutuletea maumivu, uchungu na majuto, mengi, wengi wamejilaumu wenyewe, kujikosoa na kujisikia vibaya au kukata tamaa kwa sababu ya hali hii “Getting and regretting” yaani kupata na kujuta kisaikolojia tendo hili linaitwa “Cognitive dissonance” ambalo ni tendo la kukosa raha, baada ya mambo kwenda kinyume na ulivyoamini!

Leo kwa msingi huo tutachukua muda kujifunza somo hili Kupata na kujuta kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-

·         Maana ya kupata na kujuta

·         Kupata na kujuta.

·         Jinsi ya kupata katika mpango wa Mungu


Maana ya kupata na kujuta

Kupata na kujuta ni tendo la kupata huzuni, kukata tamaa, kupata masononeko katika akili yanayokuja baada ya kupata jambo fulani ambalo ulitarajia kuwa litakupa furaha lakini ukajutia kuwa haikuwa kama ulivyokuwa unafikiri, na ukatamani kama ungelifanya vinginevyo, hii ni mojawapo ya sehemu ya kawaida katika maisha ambayo imewakumba watu wengi, aidha baada ya kupata nafasi fulani nzuri na kushindwa kuitumia au kupata nafasi fulani wakaitumia lakini isilete furaha au matarajio uliyoyafikiri, tendo hilo kisaokolojia linaitwa Cognitive dissonance – Psychological conflict resulting from incongruous beliefs and attitudes held simultaneously, kwa Kiswahili tunaweza kusema Majuto ni Matokeo ya mgogoro wa kisaikolojia unaotokana na kutokuenda sawa kwa kile ulichikiamini au kukitarajia sawa na mtazamo ulioufikiria, Kwa Kiebrania linatumika neno “Nâcham” naw- kham kimatamshi,  kwa kiingereza to sigh – physical and emotional response to strong feeling like grief, regret, repent Kwa mfano Mungu alipomuumba mwanadamu, aliatarajia wanadamu wataishi kwa shukurani na utii kwa Mungu, lakini badala yake  wanadamu wakaanza kuishi tofauti na kile Mungu alichokuwa amekitarajia kwa hiyo Mungu alijuta, aidha Mungu alijuta pia alipomtawaza Sauli akijua kuwa atatii yote anayomwagiza, lakini Sauli alirudi nyuma asifuate aliyoagizwa na Mungu

Mwanzo 6: 1-6 “Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua. BWANA akasema, Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye naye ni nyama; basi siku zake zitakuwa miaka mia na ishirini. Nao Wanefili walikuwako duniani siku zile; tena, baada ya hayo, wana wa Mungu walipoingia kwa binti za binadamu, wakazaa nao wana; hao ndiyo waliokuwa watu hodari zamani, watu wenye sifa. BWANA akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. BWANA akaghairi kwa kuwa amemfanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo.”

1Samuel 15:10-11 “Ndipo neno la Bwana likamjia Samweli, kusema, Najuta kwa sababu nimemtawaza Sauli awe mfalme; maana amerudi nyuma, asinifuate, wala hakufanya nilivyomwamuru. Samweli akasikitika, akamlilia Bwana usiku kucha.”                

Katika maandiko yote hayo lugha ya kiebrania inayotumika ni “Nâcham” ikimaanisha kuwa Mungu alijuta baada ya kuwa alifanya jambo kwa nia njema lakini baadaye hakupata matokeo kama yale aliyokuwa ameyaamini au kuyategemea au kuyatarajia huu ni mfano sasa wa kupata na kujuta, Katika maisha, kupata na kujuta kumewatokea watu wengi sana na kunaendelea kuwatokea, Bwana ampe neema kila mmoja wetu asitembee katika maisha ya majuto na badala yake aweze kufurahia maisha, Mungu akupe akili hizo na ufahamu huo, isitokee ukaja kujuta katika maisha yako Ameeeeen

Kupata na kujuta.

Kila mwanadamu anapaswa kuwa makini sana katika maeneo yote ya maamuzi katika maisha yake kwani kanuni inayotumika hapo ndiyo ambayo inaweza kutuletea furaha au majuto, endapo maamuzi yetu yatafanyika yakiwa yanaongozwa na tamaa na misukumo ya kibinadamu bila kuzingatia ua kufikiri sana katika upana wake kwa njia za kiungu na kutimiza mapenzi ya Mungu tunaweza kujikuta tunaingia katika kundi la watu wanaojuta katika maisha yao, Neno llinatuasa:-

Mithali 3:5-7 “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako; Mche Bwana, ukajiepushe na uovu.”   

Maandiko yanaonyesha kuwa wako watu wengi sana ambao walitazama kitu kwa mitazamo yao na kukitamani lakini bila kuzingatia mapenzi ya Mungu na wakapata lakini walijuta sana baadaye

-          Hawa – Mwanzo 3:6-7 “Mwanamke alipoona ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa, basi alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala. Wakafumbuliwa macho wote wawili wakajijua kuwa wa uchi, wakashona majani ya mtini, wakajifanyia nguo.”

 

Adamu na Hawa walijutia sana katika maisha yao na vizazi vyao swala zima la kutokumtii Mungu na kufuata mapenzi yao kwa kula mti waliokatazwa na Mungu, wao waliutamani ule mti na katika fikira zao walifikiri wanaweza kupata furaha wakala kwa tamaa ya kufanana na Mungu, na kwa masikitiko makubwa wakagundua kuwa wameingia matatizoni na wamekuwa uchi kabisa, uamuzi wao uliwapa kujuta siku zote za maisha yao kupata na kujuta

 

-          Lutu – alifanya uamuzi wa kuchagua kuishi katika bonde la Sodoma ambalo kwa macho ya kawaida liloonekana kuwa kama bonde la Mungu, ardhi ilikuwa nzuri yenye kuvutia na akaamua kuishi huko nadhani pia alioa huko, alipata lakini alitoka na majuto kwani alipoteza kila kitu alichokuwa nacho na hata mkewe pia na kujikuta akiishi katika pango akiwa masikini na asiyekuwa na kitu, na kuishia katika uvunjifu mkubwa wa kimaadili uliochagiwa bintize.

 

Mwanzo 13:10-13 “Lutu akainua macho yake, akaliona Bonde lote la Yordani, ya kwamba lote pia lina maji, kabla BWANA hajaharibu Sodoma na Gomora, lilikuwa kama bustani ya BWANA, kama nchi ya Misri hapo unapokwenda Soari. Basi Lutu akajichagulia Bonde lote la Yordani; Lutu akasafiri kwenda upande wa mashariki; wakatengana wao kwa wao. Abramu akakaa katika nchi ya Kanaani, na Lutu akakaa katika miji ya lile Bonde; akajongeza hema yake mpaka Sodoma.Lakini watu wa Sodoma walikuwa wabaya, wenye kufanya dhambi nyingi sana juu ya BWANA.”

 

Mwanzo 19:26-30 “Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi. Ibrahimu akatoka asubuhi kwenda mahali aliposimama mbele za BWANA, naye akatazama upande wa Sodoma na Gomora na nchi yote ya hilo Bonde, akaona, na tazama, moshi wa nchi ukapanda, kama moshi wa tanuru. Ikawa Mungu alipoiharibu miji ya Bondeni, Mungu akamkumbuka Ibrahimu, akamtoa Lutu katika maangamizi alipoiangamiza miji hiyo aliyokaa Lutu.Lutu akapanda kutoka Soari akakaa mlimani, na binti zake wawili pamoja naye, kwa sababu aliogopa kukaa katika Soari. Akakaa katika pango, yeye na binti zake wawili.”

 

-          Amnoni mwana wa Daudi alimpenda sana Tamari binti ya baba yake alimpenda sana mpaka akawa anakonda na kuumwa, alimtamani sana alimpenda mno ndio maandiko yanavyotueleza mpaka akapanga mikakati ya kumpata kwa hila, hata hivyo baada ya kumpata tu neno la Mungu linasema alimchukia machukio makuu sana kuliko yale mapenzi aliyokuwa amempenda kwanza jambo hili lilimfanya apate lakini ajute

 

2Samuel 13:11-19 “Naye alipokwisha kuileta karibu naye, ili ale, Amnoni akamkamata, akamwambia, Njoo ulale nami, ndugu yangu. Naye akamjibu, La, sivyo, ndugu yangu, usinitenze nguvu; kwani haifai kutendeka hivi katika Israeli; usitende upumbavu huu. Nami nichukue wapi aibu yangu? Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu wa Israeli. Basi, sasa, nakusihi, useme na mfalme; kwa maana hatakukataza kunioa. Walakini yeye hakukubali kusikiliza sauti yake; naye akiwa na nguvu kuliko yeye, akamtenza nguvu, akalala naye. Kisha Amnoni akamchukia machukio makuu sana; kwa kuwa machukio aliyomchukia yakawa makuu kuliko yale mapenzi aliyokuwa amempenda kwanza. Amnoni akamwambia, Ondoka, nenda zako. Naye akamwambia, Sivyo, kwa kuwa mabaya haya ya kunitoa ni makuu kuliko yale uliyonitendea. Lakini alikataa kumsikiliza. Ndipo akamwita mtumishi wake aliyemtumikia, akasema, Mtoe sasa mwanamke huyu kwangu, ukafunge mlango nyuma yake. Naye alikuwa amevaa kanzu ndefu; kwa kuwa kwa nguo hizo huvikwa binti za mfalme waliokuwa wanawali. Ndipo mtumishi wake akamleta nje, akafunga mlango nyuma yake. Naye Tamari akatia majivu kichwani mwake, akairarua hiyo kanzu ndefu yake aliyoivaa, akaweka mkono kichwani akaenda zake huku akilia kwa sauti.”

 

 

-          Yuda Iskariote – alitamani sana fedha, alifahamu au kudhani ya kuwa anaweza kumsaliti Yesu Kwa vipande 30 vya fedha, akidhani kuwa labda Yesu angeliponyoka katika mikono ya adui zake, hakufikiri kwa kina zaidi ya tamaa zake lakini baadaye alijutia sana umauzi wake alizitupa fedha hizo na kwenda kujinyonga, kupata fedha sio kubaya lakini kutafuta fedha nje ya mapenzi ya Mungu au kufanya mambo kwa tamaa ni jambo baya sana linaloweza kutuletea majuto, Kwa hiyo Yusa alifanikuwa kupata fedha kwa kumsaliti yetu Lakini alijutia

 

Mathayo 26:14-16 “Wakati huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa makuhani, akasema, Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha. Tokea wakati huo akawa akitafuta nafasi apate kumsaliti.”

               

Mathayo 27:1-5 “Na ilipokuwa asubuhi, wakuu wa makuhani wote na wazee wa watu wakafanya shauri juu ya Yesu, wapate kumwua; wakamfunga, wakamchukua, wakampeleka kwa Pilato aliyekuwa liwali. Kisha Yuda, yule mwenye kumsaliti, alipoona ya kuwa amekwisha kuhukumiwa, alijuta, akawarudishia wakuu wa makuhani na wazee vile vipande thelathini vya fedha, akasema, Nalikosa nilipoisaliti damu isiyo na hatia. Wakasema, Basi, haya yatupasani sisi? Yaangalie haya wewe mwenyewe. Akavitupa vile vipande vya fedha katika hekalu, akaondoka; akaenda, akajinyonga.”

Kusudi la Mungu ni kumtunza mwanadamu na maumivu mengi, kumlinda mwanadamu dhidi ya tamaa, kumkumbusha mwanadamu ya kuwa anapaswa sana kumtegemea Mungu katika maamuzi yake yote na njia zake zote, wanadamu wengi sana waliookoka na wale wasiookoka wamejikuta katika madhara makubwa kwa sababu ya kuongozwa na tamaa na matakwa yao wenyewe, ni vema kila unapofika wakati wa kufanya maamuzi watu wakawa wanautafuta uso wa Mungu kwa bidii ili kuyapata mapenzi ya Mungu badala ya kuzifuata njia zetu wenyewe ambazo baadaye zinaweza kutuletea majuto, Neno la Mungu linayo maelekezo ya kutosha ya namna ya kupata yale tuyatakayo katika mapenzi ya Mungu na ikiwa hivyo katika maisha yetu tutaepuka kwa kiwango kikubwa kujuta.

Mithali 14:12-14 “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti. Hata wakati wa kucheka moyo huwa na huzuni; Na mwisho wa furaha ni uzito wa moyo. Ageukaye moyoni hushiba njia zake mwenyewe; Na mtu mwema ataridhika nafsini mwake.”

Jinsi ya kupata katika mpango wa Mungu

Maisha yamejaa majuto mengi sana wako watu wanajuta kwa sababu mbalimbali katika maisha walipata lakini wanajuta, ukifanya utafiti, wako watu wamechoka mno mioyo yao imejaa simamzi na uchungu kwa sababu walipata au walifanya jitihada za kupata lakini wanajuta kwa namna moja ama nyingine, yale waliyoyapigania ili wapate yalileta majuto badala ya furaha, yale yaliowapotezea muda mwingi sana wakawekeza huko yakawalipa mabaya wasiotarajia, sasa wanajuta, wako wanaojuta kwa sababu, Walipopata kazi, walifanya kazi kwa bidii na kwa kujituma sana lakini hawakutoa muda wa kutosha kwa familia zao, marafiki zao na ndugu na jamaa, wakati wote walikuwa bize na kazi zao lakini walipojikuta wako vitandani na wanakaribia kufa walijuta kwa sababu kazi walizipata  na fedha walizipata lakini walijikuta wanafanya kazi sana na kutumia masaa mengi makazini na wakakosa wakati muhimu wa kuwa na familia zao, nahata kuwaweka sawa watoto wao, wanakuja kubaini watoto wamepotoka, wamekuwa bila upendo wa baba na mama,

Wako waliokataa wachumba zao kwa sababu walichelewa kuwaoa kwa sababu ya umasikini, nitamsubiria mpaka lini, mtu akaamua kuolewa na kijana aliyejitokeza kwa sababu ana kazi nzuri na gari nzuri, na pesa bila kujiuliza alivipataje lakini baada ya maisha kuendelea maisha yalitoa majibu tofauti, walipoteza upendo wa dhati kwa sababu ya vitu vinavyoonekana kwa muda sasa wanajuta

Wako watu ambao hawakuishi maisha yao halisi, na badala yake waliishi maisha ya kuigiza, wakitaka kuwafurahisha wengine walifurahia kusifiwa na kutambuliwa na watu, hawakuchagua ndoto zao walichagua ndoto za wazazi wao, hawakuchagua waume au wake waliowapenda wakachagua wale waliopendekezwa kwao na wachungaji, mabosi wao na vinginevyo, hawakuchagua kazi zao na fani zao walichagua kile dunia inakitaka kwaajili yao na wakawekeza muda wao huko na sasa wanajuta

Wako watu ambao wanajuta kwa sababu hawakuwa na muda wa kutunza afya zao, waliishi maisha ya hovyo, mabaya, hawakuwa na muda wa kutengeneza na watu, waliharibu mahusiano, na watu, familia zao na kupuuzia mapatano, na sasa wanajuta, wako waliopuuzia  muda wa kulala, muda wa kufanya mazoezi, walikunywa misoda na mavitu ya Super-market na sasa wanagundua kuwa wameharibu kila kitu wana huzuni kwa sababu hawakufanya mazoezi, wana huzuni kwa sababu hawakuzingatia lishe bora, wana huzuni, kwa sababu hawakufanya mapatano, wana huzuni kwa sababu hawakuwa wanalala usingizi wa kutosha afya zimeharibika na sasa wanajuta, wako hata waliokuwa wakifunga kwa kusudi la kuutafuta uso wa Bwana lakini walifunga hovyo hovyo bila kuzingatia kanuni za afya na sasa wana madonda ya tumbo, na hawawezi kufunga tena na wanajuta

Wako watu ambao wanajuta kwa sababu hawakuwekeza, hawakuweka akiba za kutosha hawakufikiri mambo ya baadaye sasa ni masikini, hawana fedha, hawakuwekeza mashamba wala mifugo hawakujali tabia zao zitawaletea matunda gani ya baadaye na sasa wanajuta, hawakupanga wanazaa watoto wangapi na kwa kiasi gani, wao kila kilichotokea kiliwatokea kama bahati tu, wako wanaojuta kwa usaliti, kupigania vyeo wakavipata lakini baadaye wakajuta hata kwanini walipigania vyeo hivyo, kutaka umaarufu, kuoa au kuolewa na watu wasio sahihi na kadhalika na sasa wao wako Jehanamu ya moto wa ndoa zao wakati wengine wako Paradiso umepata lakini unajuta!, wako waliozalishwa wakiwa nyumbani, waliona raha kujirusha lakini sasa wanajuta, wako ambao wameolewa na kuachika, wako waliotoa talaka na wanajuta, wako waliodai talaka na sasa wanajuta  hii ndio hali halisi ya Dunia pale tunapofanya mambo na kuchagua mambo kwa kuyapa uthamani wa kwetu wenyewe machoni petu wenyewe na kufanya mambo ambayo yanaweza kutufurahisha kwa muda mfupi badala ya kuwaza yatakayotufurahisha kwa muda mrefu, chaguzi za namna hiyo ni chaguzi za kiesharati kwa mujibu wa maelekezo ya kimaandiko, mwesharati ni mtu anayewaza kumaliza haja zake za muda mfupi tu na ikamgharimu maisha yake, badala ya kufikiri mbele hii ilikuwa changamoto ya Esau ambaye alijuta sana baadaye baada ya kuuza urithi wake kwa sikumoja.

Waebrania 12:16-17 “Asiwepo mwasherati wala asiyemcha Mungu, kama Esau, aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya chakula kimoja. Maana mwajua ya kuwa hata alipotaka baadaye kuirithi Baraka, alikataliwa (maana hakuona nafasi ya kutubu), ijapokuwa aliitafuta sana kwa machozi.”

Wewe hapo ulipo ulitamani nini na ukakitafuta na kukipigania kwa nguvu zako zote na ukakipata lakini sasa unajuta moyoni, wako watu wengi wenye majuto ya kila aina hapa duniani na wewe sio wa kwanza sisi kama wanadamu tunaweza kufanya maamuzi ambayo baadae yanaweza kutuletea majuto makubwa sana katika mioyo yetu! Tufanyeje tujiue, turudi nyuma hapana tunashauriwa cha kufanya Na maandiko  

Ufanyeje sasa ili usishi kwa majuto?

Mungu wakati mwingine anatutaka tuwe na subira, subira hupita njia ndefu na ngumu sana na ndio maana watu wengi hawaipendi njia hii, ni njia ngumu lakini inaweza kutuletea matokeo mazuri ya kiungu na kuiungwana unajua Mungu hufanya mambo kwa wakati, lakini mwanadamu hutaka matokeo ya haraka na ni vigumu kwetu kuvumilia na kusubiri wakati wa Mungu, kwa haraka zetu.

Muhubiri 3:11 “Kila kitu amekifanya kizuri kwa wakati wake; tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao; ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuivumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho.”

Mungu anatutaka tutangulize faida za kiroho kabla ya zile faida za mwilini, wengi wanaopitia njia za majuto ni wale ambao tunafikiri kwa jinsi ya mwili, kwa kuangalia vinavyoonekana na kupuuzia vile visivyoonekana ambayo kwa asili ni vya milele na hutupa furaha ya kudumu, ni lazima tuutafute kwanza ufalme wa Mungu na haki yake na mengine yote tutazidishiwa

Luka 12:16-21 “Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”

Nadhani kila unapofikia wakati wowote katika maisha mahali ambapo tunataka kufanya uamuzi basi ni vema sana tukatafuta sana mapenzi ya Mungu na uongozi wa Mungu neno linasema usizitegemee akili zako mwenyewe bali katika njia zako zote mtegemee Mungu

Warumi 8:13-16 “kwa maana kama tukiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi. Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu. Kwa kuwa hamkupokea tena roho wa utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba. Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu;”

Mithali 3:5-7 “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako; Mche Bwana, ukajiepushe na uovu.”

Linda dhamiri yako wakati wote unapotaka jambo - unataka hicho unachokitaka kwa sababu gani? Mungu huangalia nia ya moyo na kuhukumu kulingana na nia ya moyo, kama kuna kitu unakihitaji lakini kwa tamaa unaweza usipewe au unaweza ukapewa lakini kikakutokea puani

Hesabu 11:18-20 “Kisha uwaambie watu hawa, Jitakaseni nafsi zenu kabla ya kesho, nanyi mtakula nyama; kwa maana mmelia masikioni mwa Bwana, mkisema, Ni nani atakayetupa nyama, tule? Maana huko Misri tulikuwa na uheri. Basi kwa sababu hiyo Bwana atawapa nyama, nanyi mtakula.Hamtakula siku moja, wala siku mbili, wala siku tano, wala siku kumi, wala siku ishirini; lakini mtakula muda wa mwezi mzima, hata hapo nyama hiyo itakapotoka katika mianzi ya pua zenu, nanyi mtaikinai, kwa sababu mmemkataa Bwana aliye kati yenu, na kulia mbele zake, mkisema, Tulitoka Misri kwa maana gani?

Hata kama tumemkosea Mungu na ikaleta majuto katika maisha yetu, ni Muhimu kwetu tukamrudia Mungu huyo huyo, kwa toba, kukiri, na kuutafuta uso wake tena, Upendo wa Mungu na rehema zake hauna mipaka, tukinyenyekea kwake atatupokea tena kama ilivyokuwa kwa mwana mpotevu, kupoteza kwetu sio mwisho wa maisha, kwani Baba wa rehema anayi nafasi nyingine, ttutafute uwepo wake naye atatutia nguvu na kuturejesha tena

Luka 15:17-20 “Alipozingatia moyoni mwake, alisema, Ni watumishi wangapi wa baba yangu wanaokula chakula na kusaza, na mimi hapa ninakufa kwa njaa. Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena; nifanye kama mmoja wa watumishi wako. Akaondoka, akaenda kwa babaye. Alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu sana.”

Hitimisho:

Mpango wa kamili wa Mungu ni kila mmoja wetu kuyafurahia maisha, Mungu kama Baba aliye mwema anatufikiria mema na yuko kwaajili yetu, lakini pia yule muovu yuko, hata hivyo pamoja na kuweko kwa yule muovu, na majaribu mbalimbali mpango wa Mungu ni kuhakikisha ya kuwa anatubariki na kutupa mambo ya kudumu ambayo kimsingi hatachanganya nayo na huzuni wala majuto. Baraka za kweli kutoka kwa Mungu ni zile zinazokuja kwetu na hazituletei majuto, ukipata katika mpango wa Mungu bila ya hila, utaufurahia uwepo wa Mungu maisha yako yote, Bwana ampe neema kila mmoja wetu kuwa na Baraka za Mungu zisizo changamana na huzuni wala majuto. Amen

Mithali 10:22 “Baraka ya Bwana hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 14 Desemba 2025

Siku za miaka ya kusafiri kwangu!


Mwanzo 47:7-9 “Yusufu akamleta Yakobo babaye ndani akamweka mbele ya Farao. Yakobo akambariki Farao. Farao akamwuliza Yakobo, Je! Siku za miaka ya maisha yako ni ngapi? Yakobo akamjibu Farao, Siku za miaka ya kusafiri kwangu ni mia na thelathini; siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu, wala hazikufikilia siku za miaka ya maisha ya baba zangu katika siku za kusafiri kwao.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa maisha yetu hapa duniani yanafananishwa na safari, siku zetu za kuishi ni chache na tena zimejaa taabu sana, Maisha yetu yamejaa mabadiliko mengi sana na changamoto nyingi sana za kimwili na kiroho, kwa ujumla maisha yetu duniani ni ya kitambo kifupi sana ingawaje yana kusudi kubwa la Mungu na maana kubwa sana ya kiroho, Na ndio maana Yakobo alielewa wazi kuwa maisha yake duniani ni kama safari, anapita katika hii dunia kama mgeni na mpitaji tu, Yakobo alikuwa na ufahamu kuwa dunia hii sio nyumbani kwetu na kwamba hata kama ataishi maisha merefu kiasi gani bado miaka hiyo itakuwa ni miaka ya kusafiri kwake tu. Hivi ndivyo maandiko yanavyotukumbusha hata leo ili tuishi vizuri tukiwa na uhusiano mzuri na Amani kwa Mungu na wanadamu wote!

1 Petro 2:11-12 “Wapenzi, nawasihi kama wapitaji na wasafiri, ziepukeni tamaa za mwili zipiganazo na roho. Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”

Miaka ya kusafiri ni usemi (Metaphor) unaokazia kuwa maisha ni safari ya mchakato wenye kutupa uzoefu, mafunzo, kukua, kuelewa, kukomaa, kuongeza ufahamu na maarifa na kukutana na mambo chanya na mambo hasi, kutuchonga, kuuelewa ulimwengu na zaidi sana kuelewa kusudi la kuwepo kwetu, kwa utukufu wa Mungu Baba, hata hivyo maisha ni ya kitambo/yaani ni ya muda mfupi, sana na kwa sababu hiyo tunatiwa moyo kukabiliana na changamoto zote na kuzihesabu kuwa ni nafasi ya kipekee ya kutuandaa kwaajili ya maisha yajayo, Maisha ni safari kwa sababu hapa duniani sio mwisho na hatujafika na badala yake tunapita tu. Leo tutachukua muda basi kutafakari somo hili muhimu kwetu “Siku za miaka ya kusafiri kwangu” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Siku za miaka ya kusafiri kwangu.

·         Siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu.

·         Wakristo kama wasafiri  
              

Siku za miaka ya kusafiri kwangu

Mwanzo 47:7-9 “Yusufu akamleta Yakobo babaye ndani akamweka mbele ya Farao. Yakobo akambariki Farao. Farao akamwuliza Yakobo, Je! Siku za miaka ya maisha yako ni ngapi? Yakobo akamjibu Farao, Siku za miaka ya kusafiri kwangu ni mia na thelathini; siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu, wala hazikufikilia siku za miaka ya maisha ya baba zangu katika siku za kusafiri kwao.”

Ni muhimu kujifunza na kutafakari jinsi ambavyo Yakobo anayachukulia maisha kama safari, Maisha ni safari kweli ya kimwili na kiroho, Safari hii inakabiliwa na maswala mengi chanya na hasi lakini zaidi sana nyakati muhimu za kufanya maamuzi ambayo yataamua hatima yetu ya baadaye, ndani ya maisha tutapimwa imani, utii, na changamoto za kimaisha zitakazolazimisha maisha yetu yawe na mabadiliko kadhaa na kuzaa uvumilivu utakaotusaidia kuwa na uwepo wa Mungu na ukomavu.

Yakobo anaonyesha kuwa sio yeye tu alikuwa katika safari ya maisha lakini hata baba zake yaani Ibrahimu na Isaka nao walikuwa katika kusafiri kwao, hivyo Ibrahimu, na Isaka na Yakobo waliishi duniani kama wasafiri na wapitaji duniani, hawakuwa na makazi ya kudumu, waliishi kwa Imani, walijitambua kuwa hapa duniani wao ni wapitaji tu.

Waebrania 11:13-16 “Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi. Maana hao wasemao maneno kama hayo waonyesha wazi kwamba wanatafuta nchi yao wenyewe. Na kama wangaliikumbuka nchi ile waliyotoka, wangalipata nafasi ya kurejea. Lakini sasa waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni. Kwa hiyo Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao; maana amewatengenezea mji.”

Yakobo anahesabu miaka ya kukaa duniani kama miaka ya safari tu, Yeye na wazazi wake waliishi hivyo, hii ni kwa sababu hawakuishi katika nyumba za kudumu kama tunavyoishi leo, maisha yao yalikuwa ya kutanga tanga na kuhama hama (Nomads), kwa hiyo hawakuwa na makazi ya kudumu, waliishi duniani kama wapitaji wakiashiria ukweli halisi wa maisha ya kuwa maisha ni safari, na imejaa mabadiliko ya iana mbalimbali kimwili na kiroho, wakipitia changamoto nyingi na majaribu mengi, pamoja na baraka za Mungu, lakini maisha ya kawaida ya kibinadamu yana changamoto nyingi wao walikuwa ni mfano tu wa kutukumbusha sisi tunaoishi leo kwamba tuko safarini, na kuwa duniani tunapita tu, tuko hapa katika hali ya ugeni tu na dunia sio nyumbani kwetu kwa kudumu, maisha ya mwanadamu ni ya muda tu, ujumbe wake Yakobo na majibu yake kwa Farao yalikuwa  ni  mauhubiri tosha kumjulisha Farao kuwa wanadamu wote hapa dunia ni wanasafiri akiwepo yeye aliyekuwa na madaraka makubwa duniani kwa wakati ule, Yakobo alitaka hili lifike akilini kwa mtu huyu mkubwa kumkumbusha kuwa Pamoja na mamlaka yake kubwa na nguvu alizo nazo anapaswa kukumbuka kuwa siku za miaka yetu ni siku za miaka ya kusafiri kwetu tu na hakuna cha kudumu duniani!

Waebrania 11:8-9.“Kwa imani Ibrahimu alipoitwa aliitika, atoke aende mahali pale atakapopapata kuwa urithi; akatoka asijue aendako. Kwa imani alikaa ugenini katika ile nchi ya ahadi, kama katika nchi isiyo yake, akikaa katika hema pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ile ile.”

Kila mwanadamu mwenye akili timamu anapaswa kukumbuka kuwa maisha haya ni “temporally” ni ya muda tu tunapita kwa kasi sana na kwa sababu hiyo hatuna budi kuishi kwa Amani na wenzetu na kuwafanyia watu mambo mema, tusiwafanyie watu ubaya, wala tusiwawekee watu kinyongo, na kujilimbikizia mali na madaraka kana kwamba sisi ni watawala wa kifalme, watu wengi hujisahau katika hili, Yakobo alikuwa amebarikiwa sana lakini hakusahau kuwa yeye ni msafiri, tuishi na watu vizuri, isifikie wakati watu wakafurahia kufa kwetu au kuugua kwetu, badala yake watuombolezee, siku hizi linaanza kuwa jambo la kawaida watu kufurahia kifo cha watu wengine kana kwamba wao hawatakufa, lakini sababu kubwa ni kuwa watu hao waliishi bila ya kujali wengine, au waliumiza wengine kwaajili ya ubinafsi na mafanikio yao, na wengine, walijisahau kuwa wao wanapita tu, kila kitu duniani ni cha muda tu na maisha kwa ujumla yana masomo mengi ya kutufunza! Na la muhimu sisi ni wasafiri na tuko duniani kwa muda!, acha kinyongo, acha kuhukumu wengine, acha ubinafsi, acha kinyongo, tafuta kwa bidi Amani na wote

Siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu.

Yakobo wakati anashuka Misri na kuonana na Farao wakati huu alikuwa na miaka 130 na mpaka anafariki alikuwa na umri wa miaka 147 tu, kwa msingi huo aliishi Misri kwa muda wa miaka kama  17 hivi, Yakobo anaziona siku hizi kuwa ni chache sana, Ibrahimu aliishi miaka 175, wakati Isaka aliishi miaka 180. Kwa hiyo Yakobo anayaona maisha yake kuwa mafupi na yaliyojaa taabu sana kuliko maisha ya baba zake, na pia ingawa hakuwa anajua ataishi umri gani lakini alijitabiria kuwa siku zake ni chache na zilizojaa taabu sana kuliko siku za baba zake, yaani Isaka na Ibrahimu, Yakobo alipanda milima na mabonde akipambana na maisha yaliyojaa ugumu wa maswala mbalimbali kama:

1.       Migogoro ya kifamilia – Yakobo alilazimika kukimbia nyumbani siku za maisha ya ujana wake na kuishi mbali na baba na mama kwaajili ya kumkimbia kaka yake, Esau, hayakuwa maisha ya kawaida, tabia yake ya hila na kuutumia upole wa kaka yake kwa faida zake mwenyewe uliweza kuongeza ugumu wa maisha na kumfanya kuwa mbali na wapendwa wake wa karibu uko uwezekano kuwa Yakobo Hakuonana na Rebeka tena mpaka kifo kwajili ya tukio hili.

 

Mwanzo 27:41-45 “Esau akamchukia Yakobo kwa ajili ya ule mbaraka babaye aliombarikia. Esau akasema moyoni mwake, Siku za kumlilia baba yangu zinakaribia, ndipo nitakapomwua ndugu yangu Yakobo. Rebeka akaarifiwa maneno ya Esau, mwanawe mkubwa. Akapeleka mtu kumwita Yakobo, mwanawe mdogo, akamwambia, Tazama, katika habari zako Esau, ndugu yako, anajifariji moyo wake, maana anakusudia kukuua. Na sasa, mwanangu, sikia sauti yangu, uondoke, ukimbilie kwa Labani, ndugu yangu huko Harani; ukae kwake siku chache, hata ghadhabu ya ndugu yako igeuke; hata ikuondokee ghadhabu ya ndugu yako, akasahau uliyomtenda. Ndipo nitakapopeleka watu kukuchukua kutoka huko. Kwa nini nifiwe nanyi nyote wawili siku moja?”             

 

2.       Dhuluma na ukatili kutoka kwa mjomba – Yakobo alipokuwa akifanya kazi kwa mjomba wake, ni ukweli usiopingika kuwa Yakobo alikuwa na mjomba aliyejaa hila zaidi kuliko yeye, aliishi na mjomba katili, alimdanganya katika maswala ya ndoa na kuishia kumtumikisha, lakini alibadili-badili maswala ya mkataba wa mshahara wake zaidi ya mara kumi, siku chache zilizokadiriwa na kudhaniwa na Rebeka, zikawa ni miaka mingi ya kitumwa uko uwezekano kuwa alikaa ugenini kwa mjomba wake kwa miaka 20 akidhulumiwa tu

 

Mwanzo 29:18-27 “Yakobo akampenda Raheli akasema, Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo. Labani akasema, Afadhali nikupe wewe kuliko mtu mwingine; kaa kwangu. Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda. Yakobo akamwambia Labani, Nipe mke wangu, maana siku zangu zimetimia; niingie kwake. Labani akakusanya watu wote wa mahali pale, akafanya karamu. Ikawa wakati wa jioni akamtwaa Lea, binti yake, akamletea Yakobo, naye akaingia kwake. Labani akampa Lea mjakazi wake Zilpa, awe mjakazi wake. Ikawa, kulipokuwa asubuhi, kumbe! Ni Lea. Akamwambia Labani, Nini hii uliyonitenda? Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya? Labani akasema, Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa; timiza siku zake saba, nasi tutakupa huyu naye kwa utumishi utakaonitumikia, miaka saba mingine.”

 

Mwanzo 31:1-9 “Basi Yakobo akasikia maneno ya wana wa Labani, wakisema, Yakobo amechukua mali yote ya baba yetu; na kwa mali ya baba yetu amepata fahari hii yote. Yakobo akaona uso wa Labani, ya kuwa hakumtazama vema kama jana na juzi.  BWANA akamwambia Yakobo, Urudi mpaka nchi ya baba zako na kwa jamaa zako, nami nitakuwa pamoja nawe. Yakobo akatuma watu, akawaita Raheli na Lea waje nyikani kwenye wanyama wake. Akawaambia, Naona uso wa baba yenu, kwamba hanitazami vema kama jana na juzi. Lakini Mungu wa baba yangu amekuwa pamoja nami. Nanyi mmejua ya kwamba kwa nguvu zangu zote nimemtumikia baba yenu. Na baba yenu amenidanganya, akabadili mshahara wangu mara kumi; lakini Mungu hakumwacha kunidhuru. Aliposema, Walio na madoadoa watakuwa mshahara wako, wanyama wote wakazaa madoadoa. Aliposema, Walio na milia watakuwa mshahara wako, ndipo wanyama wote wakazaa wenye milia. Hivi Mungu akamnyang'anya mali yake baba yenu, na kunipa mimi.”

 

3.       Mateso katika familia yake – Yakobo alikutana na changamoto kutoka katika familia yake mwenyewe, watoto wake waliokuwa wakichukiana wao kwa wao, walimuuza ndugu yao Yusufu kijana wake mpendwa na kumdanganya kuwa amefariki, Yakobo aliomboleza sana akijua kuwa mwanae atakuwa amefariki, hii ilizidisha shida na huzuni kubwa katika maisha yake, nadhani walifanya msiba na kuzika nguo lakini kumbe alikuwa amedanganywa tena!

 

Mwanzo 37:31-35 “Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi. Wanawe wote, na binti zake wote, wakaondoka wamtulize, lakini akakataa kutulizwa, akasema, La! Nitamshukia mwanangu, nikisikitika, hata kuzimu. Baba yake akamlilia.”

 

4.       Njaa iliyosababisha safari Misri – Pamoja na mapito kadhaa wa kadhaa ilimlazimu kusafiri na kuiacha nchi ya ahadi akiwa na umri mkubwa 130, anakumbwa na njaa inayowalazimisha kushuka Misri kwaajili ya chakula na wito wa mwanaye Yusufu, Ingawa Abrahamu na Isaka walikutana na changamoto mbalimbali katika maisha, Yakobo anahisi maisha yake yalikuwa magumu zaidi kuliko wao  kwa sababu ya wingi wa mateso na maumivu na migogoro ya kifamilia aliyoipitia, Hata hivyo katika hali isiyokuwa ya kawaida Mungu alimtia moyo kushuka Misri na aliambiwa na Mungu kuwa atakuwa pamoja naye, atafia huko mikononi mwa Yusufu

 

Mwanzo 46:2-4 “Mungu akanena na Israeli katika ndoto ya usiku, akasema, Yakobo, Yakobo. Akasema, Mimi hapa. Akasema, Mimi ni Mungu, Mungu wa baba yako, usiogope kushuka mpaka Misri; maana nitakufanya uwe taifa kubwa huko. Mimi nitashuka pamoja nawe mpaka Misri; nami nitakupandisha tena bila shaka; na Yusufu ataweka mkono wake juu ya macho yako.”

Wakristo kama wasafiri               

Kimsingi yako maswala mengi ya kujifunza kutoka kwa Yakobo na mtazamo wake wa maisha kama safari

1.       Tunajifunza kuwa maisha yetu ni ya muda – Haijalishi utaishi duniani kwa muda gani lakini vyovyote iwavyo maisha ni ya muda mfupi sana na maandiko yako wazi kuhusiana na jambo hili, na kuonyesha ufupi wa maisha ikionyesha mifano ya maua, mvuke, majani, usingizi na kadhalika

 

Zaburi 90:5-6 “Wawagharikisha, huwa kama usingizi, Asubuhi huwa kama majani yameayo. Asubuhi yachipuka na kumea, Jioni yakatika na kukauka.”

 

Yakobo 4:13-15 “Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida; walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.”

 

2.       Tunajifunza kumtegemea Mungu na neno lake – Wakati wote wa mahangaiko yake Yakobo pamoja na safari zake alizokuwa akizunguka duniani Mungu alimtokea mara kwa mara na kumuonyesha dhahiri kuwa atakuwa pamoja naye, wakati mwingine katika maisha yako utahangaika huku na huko na unaweza ukafikiri kuwa labda Mungu hako pamoja nawe lakini nataka nikudhihirishie kuwa yuko pamoja nawe, haijalishi ulikoenda ni utumwani au unakutana na shida gani kama Mungu alivyomuongoza Yakobo atakuongoza na wewe pia katika safari yako ya maisha, changamoto za maisha na ugumu wake ni jambo la kawaida.

 

Mwanzo 28:10-15 “Yakobo akatoka Beer-sheba, kwenda Harani. Akafika mahali fulani akakaa huko usiku kucha, maana jua lilikuwa limekuchwa; akatwaa jiwe moja la mahali pale akaliweka chini ya kichwa chake, akalala usingizi pale pale. Akaota ndoto; na tazama, ngazi imesimamishwa juu ya nchi, na ncha yake yafika mbinguni. Tena, tazama, malaika wa Mungu wanapanda, na kushuka juu yake. Na tazama, BWANA amesimama juu yake, akasema, Mimi ni BWANA, Mungu wa Ibrahimu baba yako, na Mungu wa Isaka; nchi hii uilalayo nitakupa wewe na uzao wako. Na uzao wako utakuwa kama mavumbi ya nchi, nawe utaenea upande wa magharibi, na mashariki, na kaskazini, na kusini; na katika wewe, na katika uzao wako, jamaa zote za dunia watabarikiwa. Na tazama, mimi nipo pamoja nawe, nitakulinda kila uendako, nami nitakuleta tena mpaka nchi hii, kwa maana sitakuacha, hata nitakapokufanyia hayo niliyokuambia.”              

Mwanzo 46:2-4 “Mungu akanena na Israeli katika ndoto ya usiku, akasema, Yakobo, Yakobo. Akasema, Mimi hapa. Akasema, Mimi ni Mungu, Mungu wa baba yako, usiogope kushuka mpaka Misri; maana nitakufanya uwe taifa kubwa huko. Mimi nitashuka pamoja nawe mpaka Misri; nami nitakupandisha tena bila shaka; na Yusufu ataweka mkono wake juu ya macho yako.”

 

Zaburi 119:105 “Neno lako ni taa ya miguu yangu, Na mwanga wa njia yangu.”

 

3.       Tunajifunza kujitayarisha kwa Mungu – Kwa kuwa maisha ni ya muda tu maana yake pamoja na kupanga na kuweka maono na mikakati ya kibinadamu, kamwe tusiache kujitayarisha kwa Mungu, maandiko yanamuita mtun anayejiwekea mikakati ya kidunia na kuacha kujitayarisha kwa Mungu kama mtu mpumbavu, kwa sababu hiyo Mungu atupe moyo wa hekima ili tujue itupasavyo kuhesabu siku zetu.

 

Luka 12:16-21 “Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”

 

4.       Tunajifunza kuwa tayari kukabiliana na magumu – Kuwa mtu wa Mungu kamwe hakukufanyi wewe usikutane na magumu hapa duniani, Yakobo alikuwa mtu wa Mungu na Mungu alimbariki sana lakini hata hivyo maisha yake au miaka ya kusafiri kwake duniani ilijaa taabu kuliko ya siku za baba zake kama anavyosema, hii inatufundisha na kutuimarisha kuwa, kuwa mtu wa Mungu hakutazuia wewe kukutana na magumu, lakini pamoja na hayo tusiache kumcha Mungu na kuwa na uhusiano naye, Yakobo alikutana na changamoto nyingi lakini aliendelea kuwa na uhusiano na Mungu na kuwa mvumilivu na mwenye subira na Mungu akawa pamoja naye.  

 

Waebrania 13:5-6 “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. Hata twathubutu kusema, Bwana ndiye anisaidiaye, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini?

 

5.       Tunajifunza kuishi kwa viwango – Wasafiri na wapitaji hawaishi kwa viwango vya ugenini na badala yake huishi kwa viwango vya nchi zao, sisi wenyeji wetu uko mbinguni na kwasababu hiyo kamwe hatupaswi kuishi sawa na watu wa dunia hii, wala kufungwa na mambo ya dunia hii, badala yake tuishi sawa na viwango vya kule tunakokwenda.

 

Warumi 12:1-2 “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”        

 

Mathayo 6:19-21 “Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.”              

 

Hitimisho

Maisha ya Yakobo yanatufundisha kuwa safari ya maisha yetu duniani inaweza kugubikwa na changamoto nyingi sana lakini hata hivyo, Bado Mungu atakuwa pamoja nasi, kwa msingi huo sisi kama wakristo hatupaswi kujisahau  na badala yake tuendelee kutumaini na kuwa na imani, uvumilivu, saburi na kuwa tayari kuongozwa na Mungu na neno lake ili kufikia malengo ya kuwa pamoja naye mbinguni, na hata kama maisha yatajaa taabu kama yale ya Yakobo, Neno la Mungu lina ahidi kuwa Mungu atakuwa pamoja nasi atatushika mkono na kututia nguvu hadi mwisho wa safari yetu, Siku za miaka ya kusafiri kwetu ni chache nazo imejaa taabu. Ilikuwa ushuhuda kwa Farao pia

Ayubu 14:1-2 “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke Siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu. Yeye huchanua kama vile ua, kisha hukatwa; Hukimbia kama kivuli, wala hakai kamwe.”

Isaya 41:8-10 “Nawe, Israeli, mtumishi wangu; Yakobo, niliyekuchagua; mzao wa Ibrahimu, rafiki yangu; wewe niliyekushika toka miisho ya dunia, na kukuita toka pembe zake, nikikuambia, Wewe u mtumishi wangu; nimekuchagua wala sikukutupa; usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Muungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima!.

Jumapili, 7 Desemba 2025

Nafsi yangu inakuonea kiu kama Ayala!


Zaburi 42:1-4 “Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji. Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. Nafsi yangu inamwonea kiu MUNGU, Mungu aliye hai, Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu? Machozi yangu yamekuwa chakula changu mchana na usiku, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi Mungu wako. Nayakumbuka hayo nikiweka wazi nafsi yangu ndani yangu, Jinsi nilivyokuwa nikienda na mkutano, Na kuwaongoza nyumbani kwa Mungu, Kwa sauti ya furaha na kusifu, mkutano wa sikukuu.”




Utangulizi:

Kila mwanadamu aliyeumbwa na Mungu katika roho yake ameumbiwa kiu, njaa, hamu na shauku ya kutaka kuwa na uhusiano na Mungu, kimsingi mwanadamu aliumbwa ili awe na ushirika au uhusiano na Mungu, ushirika huo au uhusiano huo unafananishwa na kiu ya maji aliyonayo Ayala, hii ni kiu ya uhitaji wa uwepo wa Mungu, kiu ya kutaka kumsikia Mungu, kiu ya kutaka kumuabudu, kiu ya kutaka kumtumikia Mungu katika viwango vyenye kuleta utoshelevu, kiu ya kutaka kuongozwa na yeye na kumuona Mungu akitembea katika utukufu wake, Kama kuna jambo linaumiza moyo wa mtu aliyezoea kuwa na ushirika na Mungu ni pamoja na kutokuhisi ule uwepo wake, Musa alikuwa na kiu na shauku ya kutaka uwepo wa Mungu uwe pamoja naye kiasi kwamba alimwambia Mungu uso wako usipokwenda pamoja nasi usituchukue kutoka hapa, hii ilikuwa ni shauku ya kuhitaji uwepo wa Mungu kama jambo la lazima, aliona bila uwepo wa Mungu yeye na wana wa Israel hawawezi lolote.

Kutoka 33:13-15 “Basi, sasa nakuomba, ikiwa nimepata neema mbele zako, unionyeshe njia zako, nipate kukujua, ili nipate neema mbele zako; ukakumbuke ya kuwa taifa hilo ndilo watu wako. Akasema, Uso wangu utakwenda pamoja nawe, nami nitakupa raha. Naye akamwambia, Uso wako usipokwenda pamoja nami, usituchukue kutoka hapa.”

Mwandishi wa zaburi hii ya “42” ambaye kitaalamu ni wana wa Kora waliitumia zaburi hii ambayo iko katika kundi la zaburi za Kuomboleza, yaani za mwandishi anaomboleza kwamba hawezi tena kwenda Hekaluni nyakati za sikukuu mbalimbali, kutokana na mazingira kumtenga asikaribie uwepo wa Mungu, Mwandishi anatumia hapo mfano wa Ayala (Kulungu) kuonyesha jinsi ambayo nasfi yao ilivyo na shauku na kiu ya kutaka maji, Nao wana wa Kora wana kiu ya kuona uwepo wa Mungu, yaani wana kiu na shauku ya uwepo wa Mungu. Lakini wako katika mazingira magumu ambapo kuabudu kwao sio kwa furaha na uhuru kama vile kwenda Hekaluni, kiu hii ya kuutafuta uwepo wa Mungu hekaluni mwake inatupa fursa ya kuitafakari zaburi hii chini ya kichwa Nafsi yangu inakuonea kiu kama Ayala! Na tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Kwa nini kiu kama Ayala?.

·         Nafsi yangu inakuonea kiu kama Ayala.

·         Umuhimu wa kuwa na kiu kama Ayala.

 

Kwa nini kiu kama Ayala?

Zaburi 42:1-2 “Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji. Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. Nafsi yangu inamwonea kiu MUNGU, Mungu aliye hai, lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu?

Mwandishi yaani wana wa Kora wakiimba kwa niaba ya Daudi, wanaonyesha kiu kubwa sana ya kutamani kwenda nyumbani mwa Bwana ili kujihudhurisha mbele za Mungu, akitaka kuielezea kiu yake na hamu na shauku ya kutaka kuutafuta uwepo wa Mungu mwandishi anatumia mfano wa Ayala atamanivyo maji ya mto sawa na kiu yake ya kumtafuta Mungu, Mwandihi hakuchagua mfano huu kwa bahati tu lakini bila shaka alikuwa na ujuzi mkubwa kuhusu mnyama huyu Ayala au (Kulungu) Katika lugha ya Kiebrania mnyama huyu anaitwa ‘ayâl sawa na neno Ayala la Kiswahili na Deer la kiingereza jina lingine la Kiswahili ni Kulungu, au paa, ingawa paa wako wa aina nyingi sana!

Ayala au Paa ni mnyama anayejulikana  sana kuwa ni rahisi sana kushambuliwa na wanyama wakali, na kwa sababu hiyo kwaajili ya kujilinda wao huishi katika maeneo ya milimani hasa katika mbuga za wanyama jangwani au nyikani na pia wana uwezo wa kukimbia kwa umbali mrefu kwa kasi, kutokana na uwezo wake wa kukimbia kwa kasi kati ya 35-40 mph huku akiruka ruka uwezo wake wa kuruka ruka ni kati ya 8-10 futi sana yeye hutumia nguvu ambazo zinapoteza maji mwilini mwake kwa haraka, kwa hiyo hujikuta akisumbuliwa sana na kiu, na kwa sababu hiyo hawezi kutulia ni lazima atafute maji bila kuacha,Mwili wa Ayala umeumbwa kwa maji kwa asilimia 65% kwa hivyo hata kama kuna chakula cha kutosha Maji yana umuhimu mkubwa sana kwake vinginevyo hataweza kuwa na nguvu za kukimbia maadui zake, lakini pia hawezi kuishi muda mrefu bila maji kwa hiyo uhai wake unategemeana sana na kunywa maji, sio hivyo tu maisha yake juani na jangwani na kwenye joto huchangia kuifanya kiu yake kuwa kali kuliko wanyama wa kawaida, kwa hiyo hawezi kuishi bila maji, maji kwake ni hitaji lisilozuilika, maji kwake ni uhai, maji kwake ni ya lazima, maji kwake ni swala la dharula kwa hiyo wana wa Kora wanatumia mfano wa Ayala kuonyesha kuwa wao nao uwepo wa Mungu una umuhimu mkubwa sana sawa tu na Ayala anavyohitaji maji ya mito kwa kunywa!

Zaburi 63:1-3 “Ee MUNGU, Mungu wangu, nitakutafuta mapema, Nafsi yangu inakuonea kiu, Mwili wangu wakuonea shauku, Katika nchi kame na uchovu, isiyo na maji.Ndivyo nilivyokutazama katika patakatifu, Nizione nguvu zako na utukufu wako. Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai; Midomo yangu itakusifu.”

Nafsi yangu inakuonea kiu kama Ayala.

Kwa nini Mwandishi alikuwa na kiu hii inayofananishwa na kiu ya Ayala? Mwandishi anaonekana kuwa alikuwa katika kipindi cha shida na taabu, alikuwa amefukuzwa mbali na nyumba ya Bwana, kwa hiyo hakuwa na Muda wa kujiudhurisha mbele za Mungu na badala yake alikuwa akikimbia kutoka nyika moja kwenda nyika nyingine, alikuwa katika mashambulizi makali, hali ngumu na kipindi cha giza la kiroho, kwa hiyo alihisi maisha yake yako hatarini na uwepo wa Mungu pekee ndio ulinzi wake na hata ingawa alimtegema Mungu adui zake waliohoji yuko wapi Mungu wake, mwandishi alikuwa akitoa machozi usiku na mchana na machozi yakawa kama chakula chake!

Zaburi 42:3-6 “Machozi yangu yamekuwa chakula changu mchana na usiku, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi Mungu wako. Nayakumbuka hayo nikiweka wazi nafsi yangu ndani yangu, Jinsi nilivyokuwa nikienda na mkutano, Na kuwaongoza nyumbani kwa Mungu, Kwa sauti ya furaha na kusifu, mkutano wa sikukuu. Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu. Nafsi yangu imeinama ndani yangu, kwa hiyo nitakukumbuka, Toka nchi ya Yordani, na Mahermoni, na toka kilima cha Mizari.”

Unaona anakumbuka alivyokuwa akiongoza watu kwenda nyumbani mwa Bwana kwa furaha, lakini siku hizo zimetoweka, yuko mbali na uwepo wa Mungu anakaukiwa kwa hiyo kiu yake kwa Mungu iliongezeka kwa sababu ya mazingira magumu aliyokuwa anayapitia, sasa hafurahii uwepo wa Mungu kama zamani kwa sababu yuko mbali, yuko mbali na madhabahu ya Bwana, na Hekaluni, anaukosa uwepo wa Mungu na uwepo wa Mungu unaibuka kuwa kiu yake kubwa, Yeye kimsingi hakuwa analenga Baraka au uhitaji mwingine lakini yeye alikuwa na hamu au kiu ya ushirika na Mungu yeye mwenyewe, kiu ya aina hii ni kiu yenye Baraka kubwa sana kama watu watakuwa nayo

Mathayo 5:6  Heri wenye njaa na kiu ya haki; Maana hao watashibishwa.” Mwandishi alikuwa na kiu ya kusikia kutoka kwa Mungu, kiu ya neno la Mungu, alikuwa na kiu ya kutaka kuabudu na kufurahia uwepo wake na ukaribu wake na Mungu, Kumkosa Mungu kwake ilikuwa ni sawa na kuwa katika nyika au katika nchi ya ukame, uhai wake ulikuwa unahitaji sana vitu hivi, alikuwa anatambua kuwa ushirika kati yake na Mungu ndio chanzo cha Baraka nyinginezo zote, alitambua kuwa ulinzi wake na usalama wake unategemeana sana na ukaribu wake na Mungu, Maneno ya Mwandishi wa zaburi hii ni ya muhimu na ya msingi kwa kila mwanadamu duniani, Unaishije bila kuabudu, unaishishe bila maombi, unaishije? Unategemea nini na usalama wako ni nini Maisha yetu bila uwepo wa Mungu ni kujihatarisha ni lazima tuwe na kiu na hamu na shauku ya mambo ya Mungu wetu, ziko nyakati katika maisha tunaweza kukosa kabisa nafasi ya kuufurahia uwepo wa Mungu, Ayala bila kunywa maji hata kama kuna chakula uwezo wake wa kuishi unapungua sana na uwezo wake wa kujihami unapungua mno na mauti inakuwa karibu, uhai wake unategemea sana maji na sisi nasi uhai wetu unamtegemea sana Mungu, mwandishi wa zaburi alimtegemea sana Mungu sisi nasi hatuna budi kumtegemea sana Mungu na kuona ya kuwa bila yeye sisi hatuwezi kuishi, Ayala hukimbia anakokimbia lakini lazima atafute vijito vya maji ili maisha yaweze kuendelea, wewe na mimi tunawezaje kuishi bila Mungu na bila kuwa na uhusiano naye? Ni lazima kuwa na kiu kwa maswala ya Mungu, kiu ya kuabudu, kiu ya kujazwa na Roho wake Mtakatifu, na kiu ya kumuabudu

Amosi 8:11-12 “Angalia, siku zinakuja, asema Bwana MUNGU, ambazo nitaleta njaa katika nchi; si njaa ya kukosa chakula, wala kiu ya kukosa maji, bali ya kukosa kuyasikia maneno ya Bwana.Nao watatanga-tanga toka bahari hata bahari; na toka upande wa kaskazi hata upande wa mashariki; watapiga mbio, wakienda huko na huko, kulitafuta neno la Bwana, wasilione.”       

Umuhimu wa kuwa na kiu kama Ayala.

Tunaona mwandishi akiomboleza kwa sabahu alikuwa katika kipindi ha mateso na majaribu, na alikuwa na uhakika kuwa Mungu ndiye msaada wake mkubwa, kwa hiyo kiu yake sio ya maji na chakula, ni kiu ya uwepo wa Mungu kama zamani, ni kiu yanafasi ya kumuabudu Mungu, inaonekana mwandishi aliwahi kuwa Hekaluni na aliwahi pia kuongoza ibada, au kuongoza watu kuelekea ibadani lakini sasa anakosa jambo hili muhimu, na anateseka, jambo hili linaibua kiu ya kumuhitaji Mungu kwa wingi zaidi, Uhai wetu wa kiroho unategemea sana na uhusiano wetu wa amani na Mungu, kila mwanadamu anahitaji hili, ni kiu hii ya ndani ya kuhitaji ushirika na Mungu ndiyo inayotufanya tuwe na uwezo wa kumtafuta Mungu, kiu hii husababishwa na Roho wa Mungu ndani

Yeremia 29:11-13 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho. Nanyi mtaniita, mtakwenda na kuniomba, nami nitawasikiliza. Nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu wote.”

Ayala anategemea sana Maji pia sio kwaajili ya kunyumbulika kwa misuli yake lakini maji pia humfanya akue na kuongezeka hatua kwa hatua, kiu ya uwepo wa Mungu hutusaidia katika ukuaji wetu wa kiroho, Mtu aliyeokoka karibuni anaitwa mtoto mchanga wa kiroho, kama mtu atakosa kiu ya neno la Mungu, na kiu ya ibada, na kiu ya kuutafuta uwepo wa Mungu ni dhahiri kuwa ukuaji wake wa kiroho utaathiriwa anaweza kudumaa au kuwa na miaka mingi katika wokovu lakini akiwa amebaki vile vile tu, kama kiu hii itaondoka kwa kweli tunaweza kusema kuwa uhai nwako wa kiroho umeondoka! Kifo cha kiroho kimetokea, Kama uzima wa kiroho uko ndani yako tamaa au kiu ya kumtafuta Mungu itakuweko ndani yako nah ii ndio dalili ya uhai wako wa kiroho.

1 Petro 2:2 “Kama watoto wachanga waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate kuukulia wokovu;”

Waebrania 5:11-14 “Ambaye tuna maneno mengi ya kunena katika habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa kusikia. Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu.Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.”

Moja ya changamoto kubwa inayolikabili Kanisa katika nyakati za leo, sio tu kukosa uamsho pekee lakini pia kanisa limejawa na wakristo na hata watumishi waliodumaa kiroho, wako vile vile miaka yote matendo ya mwilini yanaonekana wazi wazi, mafarakano na fitina zinazonekana wazi wazi na hii ni dalili ya kuwa watu wamedumaa kiroho au wamebaki katika hali ya uchanga ni kiu ya neno la Mungu na uwepo wake pekee utakaotusaidia kukua kiroho siku hadi siku na kuondoka mwilini ona:-

1Wakorintho 3:1-3 “Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo. Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi,kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?

Ni kiu ya aina kama ile ya Ayala ambayo kimsingi pia inaleta uamsho na uwepo wa Roho Mtakatifu unapohisi kukaukiwa kiroho basi unayo kiu hii na Mungu ametoa wito kumpa maji ya uzima kila mwenye kiu

Isaya 44:1-3 “Lakini sikia sasa, Ee Yakobo, mtumishi wangu; na Israeli, niliyekuchagua; Bwana, aliyekufanya, na kukuumba toka tumboni, yeye atakayekusaidia, asema hivi; Usiogope, Ee Yakobo, mtumishi wangu; na wewe, Yeshuruni, niliyekuchagua. Kwa maana nitamimina maji juu yake aliye na kiu, na vijito vya maji juu ya mahali pakavu; nitamwaga roho yangu juu ya wazao wako, na baraka yangu juu yao utakaowazaa;”              

Yohana 7:37-38 “Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.”     

Huduma za kiroho zinatolewa kwa watu wenye kiu, kama mtu akipoteza kiu amepoteza uhai wa kiroho, Roho Mtakatifu anatolewa kwa watu wenye kiu, kama huna kiu huwezi kupokea mito ya maji hai inayoahidiwa na Neno la Mungu, Mungu anamtarajia kila mwanadamu awe na kiu hii, sio wakati wa mapito na shida tu lakini kila siku kama tunavyohitaji maji katika maisha yetu tunamuhitaji na Mungu pia, Mtu wa rohoni aliye hai ni yule mwenye kiu, kiu yake inamlazimisha kufika katika ibada za mafundisho katikati ya wiki, na siku za ibada kuu kila jumapili, na kumtafuta Mungu sisi wenyewe binafsi,tukiwa na kiu hii Mungu hutujalia neema na utoshelevu wa kiroho, Ayala huyatafuta maji kwa gharama yoyote hata kama yako mbali anajua uhai wake umeungamanishwa na maji, sisi nasi tunapaswa kumtafuta Mungu kwa bidii kama Ayala ayatafutavyo maji ya mto, Mwandishi ameonyesha wazi kuwa kama Ayala asivyoweza kustahimili maisha bila maji, sisi nasi hatuwezi kustahimili maisha bila uwepo wa Mungu, ni kiu yetu ndiyo inatayotupeleka katika vyanzo ma maji ya uzima na kutupa wakati wa kuburudishwa na Roho Mtakatifu jambo litakalofungua baraka kubwa za kiroho katika maisha yetu ya kila siku na kuchochea ukuaji wa kiroho na ukomavu wake!

“Nafsi yangu yakutamani, Nafsi yangu yaona kiu, Kama Ayala atafutavyo maji ya mto, Bwana nafsi yangu yakutamani, Nijaze Roho Mtakatifu, niweke karibu na wewe, Kama Ayala atafutavyo maji ya mto Bwana nafsi yangu yakutamani”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 30 Novemba 2025

Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale!


Maombolezo 5:19-21. “Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi. Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”


Utangulizi:

Je? umewahi kufikiri kuwa siku kadhaa au miaka kadhaa huko nyuma ilikuwa bora katika maisha yako kuliko ilivyo sasa? Siku ambazo furaha yako ilikuwa timilifu, siku ambazo afya yako ilikuwa njema, siku ambazo uhusiano wako na Mungu ulikuwa mzuri sana, siku ambazo ulikuwa mwombaji sana, siku ambazo ulikuwa hukosi mikesha, huachi kufunga, siku ambazo hata upitie taabu gani hukuona shida, siku ambazo ni kama zilikuwa siku za ushindi wako, siku ambazo familia ziliishi kijamaa, tuliwatembelea Babu na Bibi zetu vijijini, tulikutana na ndugu wengi, ulikuwa na marafiki wengi, watu walikaa pamoja kwa umoja na upendo ulikuwa ni kama umefikia kilele cha hali ya juu cha furaha ya maisha, unazikumbuka siku zile na unatamani kama zingerudia tena upya! Hali kama hii ndiyo iliyomkuta nabii Yeremia alikumbuka siku za utukufu mkubwa wa Mungu katika Uyahudi, wakati Hekalu la Yerusalem lililojengwa na Suleimani bado halijatiwa moto na kubomolewa zilikuwa siku njema, lakini Mungu alikuwa ameziondoa na sasa anaona uharibifu na mambo hayako kama siku zile, anaona ni kama Mungu amewaacha na kuwasahau kwa muda mrefu na kwa siku nyingi sana.

Maombolezo 5:19-21. “Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi. Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Hali hii ni hali ya kuhuzunisha sana ni hali yenye mchanganyiko wa majonzi na kukata tamaa ni wakati ambapo maisha ya mwanadamu yanakuwa yamezidiwa na kumbukumbu ya mambo mabaya yaliyotokea na yanayoendelea katika wakati ulioko, huku ukikumbuka siku zile za utukufu ambazo sasa unatamani ungezirudisha siku nyuma, uweze kuzifurahia na kupata Amani, Kisaikolojia hili tukio linaitwa “Nostalgia”.  Nostalgia is a state of being sick emotional for the past period or homesick, university days etc. Hali ya kuumwa kihisia kwaajili ya kukumbuka mambo mazuri ya zamani au kukumbuka nyumbani au siku zako za chuoni na kadhalika, Yeremia sasa anaumwa ugonjwa huu na anamuomba Mungu kwamba asikawie anamuomba Mungu awageuze nao watageuka na azifanye mpya siku zao kama siku za zamani!, ilikuwa ni sauti ya kuomboleza iliyojaa uchungu hasa baada ya Hekalu la Yerusalem kutiwa moto na kubomolewa na mfalme wa Babeli mwaka 586 KK Yeye alikuwa ameshuhudia siku nzuri za utukufu wa Hekalu hilo na siku mbaya za uharibifu mkubwa Hekalu likiwa limebomolewa, watu wamechukuliwa kwenda uhamishoni, taifa limepoteza fahari yake, na Mungu anaonekana kuwa kimya kwa hiyo moyo wake umejaa ombi lenye huzuni, toba na matumaini. Wewe je unapitia hali ya namna gani hapo ulipo? Familia yako je? Umri wako je? Ndoa yako Je? Hali yako ya kiuchumi, hali yako ya kiroho? Uhusiano wako je? Kanisa lako je kuna uamsho? Watu wanampenda Mungu kama zamani? Uzuri wako? kazini kwako je zipi siku bora katika maisha yako? Leo tutachukua muda kujifunza kwa undani somo hili muhimu lenye kichwa Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale! Na tutajifunza somo hili litakalo kurejeshea matumaini kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vufuatavyo;-

·         Kilio cha kukumbuka siku za kale

·         Sababu za kukumbuka siku za kale  

·         Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale!

Kilio cha kukumbuka siku za kale

Maombolezo 5:19-21. “Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi. Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Kimsingi kifungu hiki yalikuwa ni maombolezo au kilio ya Nabii Yeremia ambaye alikuwa akiomboleza baada ya mashambulizi mazito na hali mbaya ambayo watu wake na yeye mwenyewe walikuwa wameishuhudia, uharibifu mkubwa uliofanywa na majeshi ya Wakaldayo chini ya utawala wa Nebukadreza mfalme wa Babeli, Yeremia alikuwa anaona uchungu na sasa anaomboleza juu ya mateso ya taifa huku akiona kana kwamba Mungu amewasahau na kuwaacha kwa hiyo Yeremia alikuwa akimlilia Mungu na kumtaka awarejeze katika hali yao waliyokuwa nayo mwanzo.

Kisaikolojia hisia hizi zinaitwa “Nostalgic feelings” yaani hii ni tabia ya mwanadamu kukumbuka siku nzuri za utukufu za zamani zilizokuwa za furaha kwaajili ya kufidia hali ngumu anayokutana nayo katika wakati ulioko, akili haitaki kuona mambo mabaya inataka mambo mazuri, akili haitaki nyakati ngumu inataka amani raha na utulivu tu kwa hiyo kwa mfano umri unapokuwa unaenda mtu anaanza kukumbuka enzi za ujana wake, anakumbuka siku za zamani shuleni, chuoni na kadhalika, katika mahusiano anaanza kukumbuka siku nzuri ambazo alikuwa na soko, anapendwa na kila mtu, unapokuwa mpweke unakumbuka zamani familia zilipokuwa zinakaa pamoja na kula na pamoja na sikukuu tulizokuwa tunaenda kwa Babu na Bibi na kujumuika pamoja, unapokuwa na afya mbaya unakumbuka siku zako ulizokuwa na uzima ukiwa na nguvu, ulipokuwa na uwezo wa kula nyama na mahindi ya kuchoma na sasa meno hayana uwezo huo tena, unakumbuka siku za kale mlivyokuwa mkihubiri injili, unakumbuka wahubiri wakubwa wa zamani, miujiza mikubwa iliyokuwa ikifanyika, unakumbuka nyakati ambazo ulikuwa maarufu, na wakati wa mafanikio, unakumbuka nyimbo za zamani, wachezaji wazuri wa timu yako uliyoipenda ilipokuwa ikitwaa ubingwa, unakumbuka vipindi maalumu ambavyo sasa ni kama vimepita na haviwezi kurudi tena, unakumbuka kipindi chako kiitwacho “the golden age” hii ni hali ya kawaida wakati mwanadamu anapopitia magumu, Israel walikumbuka chakula walichokuwa wanakula Misri japo walikuwa utumwani na waliteswa

Hesabu 11:4-6 “Kisha mkutano wa wafuasi waliokuwa kati yao, wakashikwa na tamaa; wana wa Israeli nao wakalia tena, wakasema, N'nani atakayetupa nyama tule? Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu.”

Hali kama hii inamkuta nabii Yeremia anakumbuka jinsi Wayahudi walivyokuwa na amani katika taifa lao, walivyokuwa wakipanda kwenda Hekaluni, anakumbuka Mungu alivyokuwa mtetezi wao na jinsi Mungu aliyokuwa akisema nao na kuwapa wafalme na mahitaji yao, sasa kila kitu kimebakia historia mambo yameharibika, watu wamechukuliwa uhamishoni Babeli, Taifa limepoteza matumaini hakuna uhai tena, watu wako utumwani Mungu yuko kimya amegeuza uso wake Yeremia anamlilia Mungu anamuomba kwa unyenyekevu, anamuuliza mbona umetuacha, umetuacha muda mwingi, yaani unakawia, utugeuze kwako nasi tutageuka, lakini zaidi ya yote zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.

Yeremia 5:20-21 “Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Sababu za kukumbuka siku za kale.

Maombolezo 5:19-21. “Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi. Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Kwa nini Yeremia anakumbuka siku za kale? Kwa nini wewe na mimi tunazikumbuka siku zile? Siku za kale ulikuwa ni wakati wa utukufu, ulikuwa ni wakati watu wamejitoa kwa uaminifu, ulikuwa wakati wa uhusiano mzuri na Mungu, ulikuwa ni wakati watu waliabudu na kutembea na uwepo wa Mungu na miujiza mingi ilifanyika, ulikuwa ni wakati wa uhusiano mzuri, urafiki mwema wakati wa kuoneana shauku, wakati ambapo kila unaloliomba linajibiwa ulikuwa ni wakati wa Baraka, akitokea adui watu walijaa Roho Mtakatifu na maadui walikimbizwa, taifa lilikuwa na heshima, watu walikuja kutafuta Hekima na kumuabudu Mungu wa Yakobo, watu walivyotoa sadaka kwa unyoofu wa moyo, katika mahusiano watu walipendana, sasa nyakati hizo haziko tena, majumba yamekuwa magofu, upako haupo, miujiza imepotea, watu hawana mikesha tena, hekalu limechomwa moto Yeremia analia anaomboleza anamwambia Mungu zifanye upya siku zetu kama siku za kale, msikilizaji wangu na msomaji wangu wewe u hali gani sasa? Uko wapi, familia yako iko wapi, ndoa yako iko wapi, malezi yako yako wapi, furaha yako iko wapi, utukufu wako uko wapi, u hali gani, kanisa lako li hali gani na wewe mwenyewe hali yako ya kiroho ikoje?  Je unaugua kama Yeremia? Asante Mungu kwaajili ya nabii Yeremia alimfahamu Mungu alijua ya kuwa Mungu anauwezo wa kuzifanya upya ziku zetu na kuzirejeza zikawa kama siku za kale, leo ni siku yako ambayo Bwana atazifanya upya siku zako Mungu wetu anauwezo wa kurejesha, neno la Mungu linatueleza hivyo ana uwezo wa kututia nguvu

Zaburi 103:1-5 “Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana. Naam, vyote vilivyo ndani yangu Vilihimidi jina lake takatifu. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana, Wala usizisahau fadhili zake zote. Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, Aukomboa uhai wako na kaburi, Akutia taji ya fadhili na rehema, Aushibisha mema uzee wako, Ujana wako ukarejezwa kama tai;”

Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale!

Mungu anawezaje kuzifanya upya siku zetu kama siku za kale? Yeremia alikuwa amegundua siri mojawapo muhimu katika dua yake ambayo inatufunulia maswala muhimu sana yanayoweza kutuasaidia na sisi katika Maisha yetu ili tusiweze kumezwa na huzuni kutokana na hali unayoipitia!

Maombolezo 5:21 “Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.”

Katika lugha ya Kiebrania kifungu hiki muhimu kinasomeka hivi “Hashivenoo ADONAI elecha venashuvah, chadash yamenu ke’kedem” Kwa kiingereza maneno hayo yanasomeka hivi “turn us back Adonai and we will come back, renew our days, as they were in the past”

Hashivenoo (shuv)  - Uturudishe nyuma, utugeuze, uturejeshe, tugeuze, tubadilishe, ni neno linalotumika katika lugha ya Kiebrania mara nyingi likimaanisha kutubu, kubadilika moyo, kutoka dhambini, kumrudia Mungu, Yeremia hasemi tunageuka anasema utugeuze, akimaanisha Mungu ndiye chanzo cha toba ya kweli, hii inamaanisha toba ya kweli sio matokeo ya hisia zetu  na matakwa yetu wanadamu tu bali ni neema ya Mungu inayoufanya moyo wa mwanadamu ulainike na kumgeukia Mungu na kuamua kufuata njia za Mungu, kwa hiyo Yeremia anajua ya kuwa siku njema kama za zamani haziwezi kurejea hivi hivi bila ya msaada wa Mungu, ni lazima Mungu atuamshe tena na kuwasha upya moto ndani yetu utakaotusaidia kurudi kwake na sio maamuzi ya kibinadamu.

Warumi 9:15-16 “Maana amwambia Musa, Nitamrehemu yeye nimrehemuye, nitamhurumia yeye nimhurumiaye. Basi, kama ni hivyo, si katika uwezo wa yule atakaye, wala wa yule apigaye mbio; bali wa yule arehemuye, yaani, Mungu.”

Venashuvah – Tutageuka, tutaitikia, tutakubali, yaani tutakubali mabadiliko tutatii, Yeremia anatambua kuwa ili siku njema ziweze kurejeshwa ni lazima Mungu mwenyewe awashe moto wa mawasiliano na kugeuza mioyo yetu na kuturehemu na sisi nasi tuitikie kwa kutii kwa hiyo hapa tunajifunza kwamba uamsho ni ushirikiano kati ya Mungu na Mwanadamu, Mungu anapoanza kwa rehema zake sisi ni wajibu wetu kuitikia kwa toba na utii kwa uaminifu na moto ule utawaka.

Chadash (Chadesh) – Kufanywa upya kurejesha, kuhuhisha kujenga hari mpya, neno Chadash linatokana na neno Chodesh ambalo maana yake ni mwezi mpya mwenzi mchanga, mwezi unaochomoza kwa upya kutoka gizani, Yeremia anamsihi Mungu aanzishe jambo jipya katika mioyo yetu alete uhai katika mambo yote yalitopotea atupe mwanzo mpya arejeshe hali ya kiroho, kiuchumi na kimaisha aturejeshee furaha, atupe nuru hii pia ni kazi ya Mungu ndani yetu kutuhuisha

Zaburi 51:10-12 “Ee Mungu, uniumbie moyo safi, Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu Usinitenge na uso wako, Wala roho yako Mtakatifu usiniondolee. Unirudishie furaha ya wokovu wako; Unitegemeze kwa roho ya wepesi.”

Maombi ya Yeremia yalikuwa yamejaa ujuzi na hekima ya kuwa ni Mungu mwenyewe peke yake na mwitikio wetu kwa rehema zake unaoweza kusababisha mabadiliko na kurejeswa kwa siku zetu kama siku za kale, Kama watu wa Mungu wanataka kurejeshewa siku za furaha na amani basi ni lazima tumsihi Mungu kama Yeremia alivyoomba kwamba Mungu aturejeshe na sisi tukubali kurejea tukatae kupoa kiroho, tukatae ubaridi katika uhusiano wetu na Mungu ambaye ndiye chanzo cha Baraka, tumsihi Mungu afufue mambo yote yaliyokufa ndani yetu, aiponye mioyo iliyovunjika atupe uwezo wa kusamehe, atupe nguvu ya kuomba, atupe kuliheshimu neno lake, atupe ile hali ya kumuhofu, atupe kuihubiri injili ya kweli na Mungu ataturudishia siku zetu zilizopotea hii haimaanishi kuwa ataturudisha tulikotoka au kwenye miaka ile ya zamani, lakini maana yake zitakuja nyakati za kuburudishwa ambazo roho zetu zitafurahi tena na tutasahu maumivu yetu, Mungu yuko tayari kuzifanya upya siku zetu yuko tayari kuziburudisha siku zetu na kuyafutilia mbali machozi yetu yote badala ya kukumbuka mambo ya zamani yeye ameahidi kufanya mambo mapya katika maisha yetu.

Matendo 3:19-21 “Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu zamani; ambaye ilimpasa kupokewa mbinguni hata zije zamani za kufanywa upya vitu vyote, zilizonenwa na Mungu kwa kinywa cha manabii wake watakatifu tokea mwanzo wa ulimwengu.”

Isaya 43:18-19    “Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani. Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima