Jumatatu, 24 Oktoba 2016

Sisi tutalitaja jina la Bwana Mungu wetu!


Andiko Zaburi 20:7 “ Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja BWANA, Mungu wetu


 Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja BWANA, Mungu wetu

Utangulizi.

Ni muhimu kufahamu kuwa Zaburi hii chimbuko lake ni Mfalme Daudi, kiongozi wa nyimbo au kwaya wa Daudi aliimba wimbo huu, au Daudi alitunga na kuwapa watu wa sifa waimbe hivyo Zaburi hii inahesabika kama moja ya zaburi ya Daudi, Hata hivyo kihistoria Zaburi hii ilitumiwa sana na wafalme waliofuata baada ya Daudi kama njia ya maombi walipokuwa wanakwenda kupigana vita, Mfalme aliomba na kutoa sadaka kisha watu walisindikiza maombi na dua za mfalme wao kwa Zaburi hii, hivyo ni zaburi maarufu kama maombi kwaajili ya kukabiliana na mambo ya kutisha! Ilitumika wakati wa shida na wakati wa kuhitaji msaada.

Kuna mambo mengi sana yaliyomo katika zaburi hii, lakini kubwa likiwa ni Dua ya kumuombea Mfalme, kwa nini mfalme aliomewa sana kwa sababu yeye alitangulia mbele wakati wa vita, alikuwa ndio mpambanaji mkuu na hivyo waimbaji na waombaji walimuombea angalia Mstari wa 1-4 Biblia inasema

1. Bwana akujibu siku ya dhiki, Jina la Mungu wa Yakobo likuinue. 2. Akupelekee msaada toka patakatifu pake, Na kukutegemeza toka Sayuni. 3. Azikumbuke sadaka zako zote, Na kuzitakabali dhabihu zako. 4. Akujalie kwa kadiri ya haja ya moyo wako, Na kuyatimiza mashauri yako yote.”

Baada ya dua na maombi ya kumuombea Mfalme waliweka matumaini yao kuwa Mungu anakwenda kuwapa ushindi hivyo walianza kushangilia ushindi, walilitumia jina la bwana na waliweka bendera tayari kwa imani  na pia walimkumbusha Mungu kwa imani kuwa atamwokoa masihi wake na kumjibu Maombi yake walikuwa na ujasiri kuwa watajibiwa Mstari wa 5-6 na kuwa ni lazima Mungu atafanya mambo makubwa kwa mkono wake 

“5. Na tuushangilie wokovu wako, Kwa jina la Mungu wetu tuzitweke bendera zetu. Bwana akutimizie matakwa yako yote. 6. Sasa najua kuwa Bwana amwokoa masihi wake;Atamjibu kutoka mbingu zake takatifu.”

Katika mstari wa 7 na wa 8 waimbaji hawa walionyesha tofauti iliyoko kati ya wanaoamini na wasioamini lakini pia walionyesha kwamba ndipo mahali pa kuzingatiwa sana katika utendaji wa Mungu, “Hao (wasiamini) au wenye kiburi wanataja Magari na hawa wasiomtegemea Mungu wa kweli wanataja Farasi, Bali sisi tunaoliamini Jina la Mungu tutalitaja jina la bwana Mungu wetu! Ni muhimu kupaangalia mahali hapa kwa makini sana

Mungu alikuwa amewafundisha Isarael siku nyingi sana kumtegemea yeye na kumwangalia kwaajili ya ushindi na dhiki ya aina yoyote, na katika nyakati za vita moja ya vitu vilivyokuwa vinaogopewa sana katika nyakati za vita za zamani ni magari ya vita na magari ya wapiganaji walikuwa wakipigana juu ya farasi, watu hao walikuwa hodari hata kufukuzia na hivyo katika nyakati za biblia watu au mataifa yaliyokuwa na magari ya vita na wapanda farsi hodari waliogopwa zaidi kwani ndio waliokuwa hatari na wenye kutisha sana katika nyakati za leo Magari haya tungeweza kufananisha na tanks au vifaru wakati wa vita wote tunajua namna vinavyotisha sana

Mungu aliwaonya mapema Israel kutokuogopa Kumbukumbu la taorati 20: 1Utokapo kwenda vitani kupigana na adui zako na kuona farasi na magari na watu wengi sana kuliko wewe usiwaogope, kwa kuwa Bwana Mungu wako yu pamoja nawe aliyekukweza kutoka nchi ya Misri” pia Yoshua 17:16

Nchi ya Misri na Syria ndio zilikuwa hatari zaidi kwa aina hii ya vita katika nyakati hizo na makabila mengine pia Israel hawakuwa na aina hiyo ya silaha wakati huo, wala hawakuwa na jeshi kubwa sana, hivyo wale wasiomuamini Mungu waliweka tumainilao katika hayo magari ya chuma nay a farasi na wapanda farasi, Israel walikuwa wamekwisha kupata somo kubwa kwamba Misri ilifanywa nini pamoja na kuwa na Magari ya farasi na wapanda farasi Kutoka 15:1-4, Mungu alikwisha kuwafundisha kutokuyategemea magari na wapanda farasi, Mungu aliwajulisha kuwa hufanya mambo kwaajili ya jina lake na kwaajili ya utukufu wake, Mungu hatakuinamisha bali Mungu atakusimamisha mungu hatakuaibisha bali Mungu atakuokoa Mstari 8-9 waimbaji wanaonyesha kuwa hawataaibika na kuwa adui zao watainama

Ndugu yangu haijalishi ni hila kiasi gani adui anazo,

Haijalishi watakuwa na nguvu kiasi gani

Haijalishi magonjwa yamekutesa kiasi gani, yamekuandama na kukukandamiza kwa kiwango gani mtegemee Mungu tu

Haijalishi watakuwa na mbinu  za kibinadamu kiasi gani, wana silaha na magari ya chuma kiasi gani, wana watetezi kiasi gani, wana uzoefu kiasi gani, wana akili kiasi gani, wana mitego kiasi gani, wana nguvu kiasi gani tunachokiangalia wanatumainia nini, je wanatumainia fedha, majeshi, nguvu waimbaji wakasema wao wanataja Farasi namagari sisi tutalitaja jina la Bwana Mungu wetu, wapendwa na tuchangamke, tunaye Mungu, tunaye shujaa, anauwezo, ana nguvu, ni hodari wa vita atatupigania anakwenda kutupa ushindi anza kuufurahia ushidni wako leo yuko Mungu wa Yakobo atatuokoa na ataisikia sauti yetu,

Bwana Mungu nimekutegemea wewe, tumaini langu si kwa wanadamu Bali ni katika jina lako
Sasa najua kuwa Bwana amwokoa masihi wake*

Na. Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Hapana mfalme aokokaye kwa wingi wa uwezo!



Andiko la Msingi: Zaburi 33: 16—19 Biblia inasema “16. Hapana mfalme aokokaye kwa wingi wa uwezo, Wala shujaa haokoki kwa wingi wa nguvu. 17. Farasi hafai kitu kwa wokovu, Wala hamponyi mtu kwa wingi wa nguvu zake. 18. Tazama, jicho la Bwana li kwao wamchao, Wazingojeao fadhili zake. 19. Yeye huwaponya nafsi zao na mauti, Na kuwahuisha wakati wa njaa. 20. Nafsi zetu zinamngoja Bwana; Yeye ndiye msaada wetu na ngao yetu.”

 Hapana mfalme aokokaye kwa wingi wa uwezo, Wala shujaa hamponyi mtu kwa wingi wa nguvu zake
 
Utangulizi:

Zaburi hii ni zaburi inayokazia katika tabia ya kumtegemea Mungu na kupata Ushindi katika maisha yetu, ni zaburi ambayo haithibitiki kuwa ilikuwa ya Mfalme Daudi kama ilivyo kwa zaburi nyingine, lakini Zaburi hii inawezekana kabisa ni zaburi iliyoimbwa na kwaya ya Walawi, waliokuwa wakimsifu Mungu kwa Amri ya Daudi miaka mingi nyuma alimchagua kiongozi mkuu wa sifa aliyeitwa Asafuhuyu  alikuwa kiongozi wa sifa na nduguze na baadaye wana wa Asafu walirithi kazi hii ya kuimba na kumsifu Mungu

 1Nyakati 16:7-8, Ndipo siku hiyo Daudi alipoagiza kwanza kumshukuru Bwana, kwa mkono wa Asafu na nduguze. Mshukuruni Bwana, liitieni jina lake; Wajulisheni watu matendo yake.” 

Na pia 1Nyakati 25:1  Tena Daudi na maakida wa jeshi wakatenga kwa utumishi baadhi ya wana wa Asafu, na wa Hemani, na wa Yeduthuni, watakaotabiri kwa vinubi na vinanda, na matoazi; hii ndiyo hesabu ya wafanya kazi sawasawa na utumishi wao;”

Hivyo wana wa Asafu ndio waliimba Zaburi hii na ni wazi kuwa Kiongozi wa ibada ya sifa aliimbisha kuanzia mstari wa 1-3 na kisha waimbaji wengine waliitikia katika mistari yote inayofuata, kwa vyoyote vile wimbo huu unaonekana kuitwa wimbo mpya na huenda ulizungumzia tukio la kuokolewa kwa taifa hususani ufalme wa Yuda

Wimbo unaonekana kudhihirisha tukio la ushindi wa kitaifa lililotokea wakati wa utawala wa Yehoshafati au wakati wa utawala wa Hezekia, Pia kidogo Ushindi wa Daudi dhidi ya Goliath, Nyakati za utawala wa wafalme hao Mungu alikwisha dhihirisha kuwa haokoi kwa wingi wa jeshi, wala shujaa hapati ushindi kwa wingi wa nguvu zake!

·         2Nyakati 20:1-30 Mungu alisambaratisha combine ya majeshi yote yaliyoinuka juu ya Yehoshafati na Yuda bila kupigana “mwaminini Mungu mtathibitika waaminini manabii wake mtafanikiwa”

·         2Wafalme 19:1-35 Malaika wa Bwana alipiga watu 185,000 mst 35 huu ulikuwa wakati wa Hezekia
Mungu alikuwa amekwisha wafundisha Israel kivitendo kuwa wokovu wake hautegemei wingi wa nguvu alizonazo mtu au wingi wa jeshi lake bali mtu akimtegemea Mungu na kumcha Mungu, Mungu huleta wokovu mkuu

Zaburi 33:16-19
1.       Inatoa somo kuu sana Mungu anaokoa kwa uweza wake si katika njia zinazotegemewa na wanadamu
2.       Yeye ndiye mlinzi mkuu sana wa maisha yetu na kuwa tusipomuhusisha yeye katika maisha yetu uwezekano wa kujilinda wenyewe ni hafifu

3.       Jeshi hata liwe kubwa kiasi gani na liwe na akili kiasi gani na vifaa kiasi gani, Mungu anaweza kuleta ugonjwa ukawapiga jeshi zima, anaweza kuwatia hofu wakaogopa wote na kutwawanyika kwa hofu

4.       Rehema zake zinao wamchao siku zote Muhubiri 9:11 si wenye mbio washindao, wala sio waliohodari washidao vita, wala sio wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo

5.       Goliath alikuwa na nguvu na uzoefu wa vita lakini alishindwa na Daudi kijana mororo.
Mafanikio yetu hayako katika ujanja na uweza wa kibinadamu yako katika kumtanguliza Mungu na kumtegemea, uwezo wetu wa kufaulu katika Mitihani utategemea na namna tunavyomtegemea Mungu na kujinyenyekeza kwake, Ufanisi wa kweli uko katika kumtegemea Mungu, kumfanya yeye kuwa kinga yetu, kumtanguliza Yesu mbele, kuhakikisha tunafanya mambo kwa utukufu wake, kuhakikisha kuwa hatutafuti utukufu wetu wenyewe bali tunatafauta utukufu wa Mungu, Daudi hakuwa anatafuta utukufu wake, alitaka Mungu ainuliwe, Tazama jicho la Bwana li kwao wamchao , wazingojeao fadhili zake’ huwaponya wakati wa mauti na kuwahuisha wakati wa njaa.

Wana wa Asafu walihitimisha kwa kusema nafsi zetu zinamngoja Bwana, yeye ndiye Msaada wetu na ngao yetu, mioyo yetu itanfurahia kwa kuwa tumelitumainia jina lake ee bwana fadhili zako zikae nasi kama vile tulivyokungoja wewe” 

16-17 hatuwezi kufanyo lolote bila Mungu
18 –19 Mungu mwenyewe huwaangalia wamchao na kuwasaidia wanaongoja msaada wake
20- wana wa Asafu na Israel wote waliamua kuwa watamngoja Bwana na kumtegemea yeye
21, walijua kuwa watafurahi walijitolea unabii kwa sababu wamelitumainia Jina lake
22 walijiombe fadhili za Mungu zikae nao milele.

Wema wako nimeungoja ee Bwana!

Na Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 16 Oktoba 2016

“Kama utakuwa mtumwa wa watu hawa leo, watakuwa watumwa wako siku zote”


“If today you will be a servant to these People, they will always be your servants” 

Lengo: kufanya maamuzi yenye Busara.

Andiko: 1Wafalme 12:1-15 “1. Rehoboamu akaenda Shekemu; maana Israeli wote walikuwa wamekwenda Shekemu, ili kumfanya mfalme. 2. Ikawa Yeroboamu mwana wa Nebati alipopata habari (maana alikuwa akaliko Misri, huko alikokimbilia awe mbali na mfalme Sulemani; Yeroboamu akakaa huko Misri, 3. wakapeleka watu kwenda kumwita); basi Yeroboamu na jamii yote ya Israeli wakaenda, wakamwambia Rehoboamu, wakasema, 4. Baba yako alilifanya zito kongwa letu; basi sasa utupunguzie utumwa mzito tuliotumikishwa na baba yako, na lile kongwa zito alilotutwika, nasi tutakutumikia. 5. Akawaambia, Enendeni zenu hata siku ya tatu, kisha mnirudie tena. Watu wakaenda zao. 6. Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani, baba yake, alipokuwa hai, akasema, Mwanipa shauri gani ili niwajibu watu hawa? 7. Wakamwambia wakasema, Ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa leo, na kuwatumikia, na kuwajibu, na kuwapa maneno mazuri, basi watakuwa watumishi wako daima.   8. Lakini akaliacha shauri lile la wazee, walilompa, akataka shauri kwa wale vijana waliokua pamoja naye, na kusimama mbele yake. 9. Akawaambia, Mwanipa shauri gani ili tuwajibu watu hawa, waliosema nami, wakinena Utufanyie jepesi kongwa lile alilotutwika baba yako? 10. Na wale vijana waliokua pamoja naye wakamwambia, wakasema, Uwaambie hivi watu wale waliokuambia, wakisema, Baba yako alilifanya zito kongwa letu, bali wewe utufanyie jepesi, uwaambie hivi, Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu. 11. Basi kama vile baba yangu alivyowatwika kongwa zito, mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge. 12. Basi, Yeroboamu na watu wote wakamfikia Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyoamuru, akisema, Mnirudie siku ya tatu. 13. Mfalme akawajibu watu wale kwa ukali, akaliacha shauri lile wazee walilompa; 14. akawajibu kama vile walivyomshauri vijana, akasema, Baba yangu alilifanya zito kongwa lenu, bali mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge. 15. Basi mfalme hakuwasikia wale watu; maana jambo hili lilitoka kwa Bwana, ili alitimize neno lake, Bwana alilomwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kwa kinywa cha Ahiya Mshiloni.



Utangulizi.

Somo letu leo linahusu tukio hili kubwa kabisa la kusikitisha ambalo lilitokea mapema sana mara baada ya utawala wa Rehoboamu mwana wa Sulemani kuingia Madarakani!
Jina Rehoboamu maana yake “Mwenye kuwaongeza watu” Lakini hata hivyo maisha yake yalijawa na wingi wa majanga yenye kuhuzunisha na kusikitisha sana, na Moja ya janga kubwa ni kugawanyika kwa Ufalme wa Israel na kujitenga kutoka kabila la Yuda, jambo hili linatupelekea leo kuchukua Muda mfupi ili kujifunza mengi kutoka kwa Rehoboamu.

Katika kujifunza somo hili tutaangalia mambo muhimu yafuatayo:-

1.       Ushauri kutoka kwa wazee 1Falme 12:6-7
2.       Ushauri kutoka kwa vijana 1Falme 12:8-11
3.       Muitikio wa watu baada ya Uamuzi 1Falme 12:13-14a, 16

Ushauri kutoka kwa wazee IFalme 12:6-7

Inaonekana mfalme Rehoboamu alisikiliza ombi la watu, na jamii kubwa ya watu waliomshauri katika kundi la Kwanza walikuwa ni wazee, hawa walikuwa ni Makuhani, makamanda, washauri na magavana, hawa walikuwa ni watu wenye ujuzi na ufahamu kuhusu utaratibu wa Israel na tamaduni zake. Lakini pia walifahamu athari za utawala wa kifalme hasa wakati wa Sulemani na jinsi utawala wake ulivyoacha athari mbaya kwa raia wake.

Wazee hawa walichokifanya kwa Rehoboamu ilikuwa ni kuweka wazi udhaifu wa Mfalme aliyetangulia, Ufalme wa Sulemani ambaye aliitwa mwenye hekima kubwa kuliko watu wote Duniani katika nyakati zile, ulikuwa umeacha athari kubwa na makovu makubwa sana kwa watu wake na hata kwa Mungu pia, Sulemani alikosa muda wa kushughulika hata na familia yake, alikuwa akishughulika na mambo ya watu wengine Wimbo uliobora 1:5-6, Sulemani katika utawala wake alijishughulisha kushauri wafalme wa maytaifa mengine, alijishughulisha kujenga utukufu wake na sifa zake, aliiigeuza jamii yote kuwa watumwa wake, alisahau hata kumuweka Mungu mbele, alioa wanawake wengi ambao waliingiza ibada za miungu katika Israel, Mahitaji ya Sulemani yalikuwa makubwa sana kiasi ambacho aliongeza kodi kwa raia wake na kila mmoja alijihisi kuwa ni mtumwa, watu walikaa kimya, waliojaribu kumpinga walitaka kuuawa na hivyo walikimbia uhamishoni, Mungu alikwisha kukusudia mapema kuwa atausambaratisha utawala wa Sulemani na kuugawa na atabakiza kabila moja tu kwaajili ya Daudi mtumishi wake, Mungu alikwishakuupima moyo wa Sulemani nakuona kuwa ameshindwa kuiendea njia ya Daudi baba yake.

Wazee waliona nafasi ya magezi ilikuwa moja tu, ni Mara alipotawazwa Rehoboamu kuwa mfalme, hapo ndipo walipojua kuwa watapata Nafuu hivyo walimsihi mfalme.

1.       Utupunguzie utumwa mzito tuliotumikishwa na baba yako
2.       Kubali kuwa mtumwa wa watu hawa ( hapa wazee walikuwa wanamaanisha Unyenyekevu,Utu, Huruma na kujali)
3.       Wape maneno mazuri (Jibu watu vizuri, jali watu ona watu kuwa wathamani, kuwa mwema kwao na wakati mwingine wasikilize na kuwajibu watu vizuri) “Mithali 15:1-4
4.       Watu watakutumikia daima, walikuwa tayari kumtumikia mfalme anayejali
Rehoboamu alifanya maamuzi ya busara, alitulia na alitoa siku tatu kuwa atatoa jibu ni maamuzi gani atafanya.

Ushauri kutoka kwa vijana 1Falme 12:8-11.

Hata hivyo ilikuweko nafasi nyingine, hii ilikuwa ni kuwasikiliza vijana wanasema nini? Na hata hivyo hakuweza kuukubali ushauri wa wazee mapema kwani aliona hawezi kuwa mnyenyekevu na kuwatumikia watu wanaostahili kutawaliwa tu majibu ya Rehoboamu yalikuwa ya Ujeuri zaidi
1.       “Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu” “loins – sex organ
Haya yalikuwa ni majivuno na kiburi cha hali ya juu, Rehoboamu alitaka kuonyesha kuwa ana nguvu kuliko aliyemtangulia, utawala wake ni superior kuliko ule wa Sulemani yeye ni super power
2.       Rehoboamu alishauriwa kuongeza utumwa na kodi na kuifanya nzito zaidi, alisema kama Baba aliwapiga kwa mijeledi mimi nitawapiga kwa nge (Scorpion) hiki ni chombo chenye vipande vya chuma vyenye uwezo wa kukatakata, ujumbe aliokuwa akiutoa hapa ni wazi kuwa nitaongeza machungu yenu hasa kuliko ilivyokuwa kwa Sulemani
3.        Alizungumza na watu kwa ukali sana Mstari 13. Hakuna kubembeleza mtu,Hakuna maneno mazuri wala ya Heshima
4.       Watu wakaasi na kumuacha Rehoboamu.

Muitikio wa watu baada ya Uamuzi 1Falme 12:13-14a, 16

1.       Watu waliona kuwa hawana urithi wowote katika Yuda waliamua kujitenga 15-16
2.       Watu waliamua kuangalia maisha yao wenyewe na nyumba zao wenyewe 16
3.       Watu waliingiwa na roho ya ukatili, walimuuamsimamizi wa utumwa 18
4.       Na Israel waliasi 19. Sio tu waliasi ufalme wa Yuda bali pia walimchukia Mungu wa Israel na katika utawala wao waliona waabudu miungu mingine (watu wakikasirishwa nawe hata Mungu unayemuamini hawatamuamini)
5.       Rehoboamu alitaka kupigana na Ndugu zake Mungu akamkemea 1Wafalme 12:21-24

Hitimisho.

Nini cha kujifunza kutoka katika somo hili.

1.       Kuzaliwa na mwenye Hekima hakukufanyi uwe na Hekima, wengine wameshindwa kupata japo nusu ya akili za Baba zao
2.       Tukiisha kumuacha Mungu na kumdaharu utukufu wake unaondoka
3.       Namna yoyote ile ya kutaka kuwa na nguvu na utukufu bila kutanguliza Mungu na utu utatupa kuishia kwenye wakati mgumu
4.       Bila uongozi wa kiroho au wa Roho wa Mungu hatuwezi kufanya maamuzi ya Busara
5.       Ni lazima tuwe na huruma kwa wanadamu, na kuonyesha kujali ubinadamu kwanza kabla ya mambo mengine
6.       Manabii walikuweko na makuhani, ambao waliweza hata kuepusha vita kati ya ndugu na ndugu, walitakiwa kusikilizwa kwanza
7.       Rehoboamu alilijua wazi kabisa tatizo lakini, alikataa kabisa kulishughulikia na hivyo watu walimuasi na Mungu aliruhusu
8.       Mgawanyiko na udhaifu huu uliwapa nguvu maadui wa Israel kuwamaliza na kupelekwa utumwani
9.       Lazima wakati wote tufanye maamuzi yenye busara na kukataa ushauri mbaya, lakini pia kama wazazi wetu hawakufanya vema tusiiifuate njia yao.

Mkiyajua hayo Heri ninyi mkiyatenda! Yohana 13:17

Na mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Rev. Innocent Kamote.

Alhamisi, 6 Oktoba 2016

Nabii Malaki



MALACHI: NABII WA SIKU ZA UAMSHO
A.       Mwandishi


-          Malaki aliishi katika nusu ya pili ya karne ya tano Kabla ya Kristo, baada ya ujenzi wa hekalu kumalizika. Malaki ambalo ni neno la Kiebrania ‘‘Malaki’’ kama lilivyo kwenye Kiswahili, maana yake ‘‘Mjumbe wangu.’’. Jina hili ni kifupi cha ‘‘Malakia’’ ambalo maana yake ni ‘‘Mjumbe wa Bwana‘’ (1:1).
-          Jina hili la kitabu limetumika vivyo hivyo kwenye maandiko ya Kiebrania na Kiyunani likionyesha kwamba hili likuwa jina la nabii ambaye ujumbe wake umenukuliwa humu. Hakuna habari nyingine zo zote za kibinafsi zinazofahamika za huyu nabii. Maisha ya kidini ya Wayahudi yalikuwa mabaya :
-           Walikuwa wamekengeuka, wakawa wameoa wanawake wa mataifa mengine, wakaacha kutoa zaka (fungu la kumi) na dhabihu ambayo na sehemu ya Mungu, hata wakawa wamemwacha Mungu, hali ambayo ilifanana sana na ile iliyokuwepo wakati wa Nehemia (444-432 K.K.). 

B.      Kiini cha ujumbe wa kitabu cha Malaki

-          Masikitiko makubwa ya Malaki ni uhusiano kati ya Waisraeli na Mungu haukuwa kama ulivyopaswa uwe. Walimwacha Mungu na kumdharau, wala hawakumheshimu inavyostahili, wakashindwa kufuata yale Mungu aliyowaagiza. Matokeo yake hukumu ikawa inawangoja, lakini watu wanaomcha Mungu wamehakikishiwa kuwa wameandikwa kwenye kitabu cha Mungu, nao watafuhia wokovu wa Mungu milele. 

C.      Kusudi
-          Kuwahimiza watu wafanye mabadiliko thabiti ya kimsingi katika maisha yao, kwa kuwakumbusha upendo wa Mungu (1:1-5) na pia kwamba adhabu yake iko karibu (2:17; 3:13)

D.      Mchanganuo wa kitabu cha malaki

-          Kitabu hiki kinaonyesha kuwa:(1)Hekalu lilijengwa tena (516/515 K.K.), dhabihu na sikukuu zilirudishwa. (2)Ufahamu wa jumla wa sheria ulirudishwa tena na Ezra (kama 457-455 K.K. ; tazama Ezra 7 :10, 14, 25-26) na (3).Kurudi nyuma kimaadili kulikofuatia kulitokea miongoni mwa makuhani na mwa watu pia (kama mwaka 433K.K.). Kutokana na hali hii hali ya kiroho na upuzi Malaki anaouzungumzia kwa karibu vilifanana sana n aile hali aliyoikuta Nehemia aliporudi kutoka uhamishoni Uajemi (kama 433-425 K.K.) ili kuwa mtawala wa Yerusalemu (ling. 13 :4-30).
E.       Mahali
-          Yerusalemu. Malaki, Hagai na Zekaria walikuwa manabii katika Yuda (Ufalme wa kusini) baada ya watu kurudi kutoka uhamishoni.. Hagai na Zakaria waliwakemea watu kwa kutokumalizia ujenzi wa hekalu. Malaki alipambana nao kwa sababu walipuuzia hekalu na kutokumjali Mungu.
F.       Tarehe
-          Yale yaliyomo kwenye kitabu hiki yanaonyesha kwamba huduma ya Malaki ilikuwa kwenye utendaji mnamo sehemu ya pili ya karne ya tano Kabla ya Kristo. Hekalu lilikuwa tayari limeshajengwa tena upya. Kutokana na wakati alioishi Malaki na yale yaliyomo kwenye kitabu hiki, inawezekana kiliandikwa 557- 525 K.K.
G.      Wahusika wakuu
-          Malaki na makuhani
H.       Mgawanyo
-          Upendo wa Mungu kwa Israeli. (1:1-5)
-          Israeli yamtukana Mungu. (1:6-2:16)
-          Hukumu ya Mungu na ahadi yake. (2:17-4:6)