Jumanne, 20 Septemba 2022

Ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima !


1Wafalme 12:6-7 “Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani, baba yake, alipokuwa hai, akasema, Mwanipa shauri gani ili niwajibu watu hawa?  Wakamwambia wakasema, Ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa leo, na kuwatumikia, na kuwajibu, na kuwapa maneno mazuri, basi watakuwa watumishi wako daima.”



Utangulizi:

Mojawapo ya maombi yanayompendeza sana Mungu ni pamoja na kuomba Hekima, Mfalme Suleimani mara alipotawazwa kuwa mfalme wa Israel, Mungu alimtokea na kumtaka amuombe lolote alitakalo, katika namna ya kushangaza sana Mfalme Suleimani aliomba Hekima jambo ambalo lilimpendeza sana Mungu hata akamjalia na mambo mengine mengi sana ambayo hakuyaomba ona:-

1Wafalme 3:5-13 “Na huko Gibeoni Bwana akamtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akasema, Umemfanyia mtumwa wako Daudi baba yangu fadhili kuu, kadiri alivyoenenda mbele zako katika kweli, na katika haki, na katika unyofu wa moyo pamoja nawe; nawe umemwekea na fadhili hii kubwa, maana umempa mwana wa kuketi kitini pake kama ilivyo leo. Na sasa, Ee Bwana, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. Na mtumwa wako yu katikati ya watu wako uliowachagua, watu wengi wasioweza kuhesabiwa, wala kufahamiwa idadi yao, kwa kuwa ni wengi. Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi? Neno hili likawa jema machoni pa Bwana, ya kuwa Sulemani ameomba neno hili. Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako; bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe, wala baada yako hatainuka mtu kama wewe. Na mambo yale usiyoyaomba nimekupa, mali na fahari, hata hapatakuwa na mtu katika wafalme kama wewe, siku zako zote.”

Kila siku katika maisha yetu tunakabiliwa na swala la kufanya uamuzi, Hakuna jambo gumu sana duniani kama kufanya uamuzi, maamuzi yetu tunayoyafanya leo yanaweza kuwa na faida kubwa sana katika siku zetu zote za maisha yetu na ya watu wengine, lakini vilevile yanaweza kutugharimu na kusababisha machungu katika maisha yetu au hata na ya wengine kwa hiyo ni muhimu sana kumuomba Mungu atupe Hekima.

Yakobo 1:5 “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.”

Katika kifungu cha maandiko ya msingi, tulichosoma tunamuona Mwana wa mfalme Sulemani aliyeitwa Rehoboamu akiwa anakabiliwa na wakati wa kufanya maamuzi kwa mustakabali wa taifa lake mapema tu katika siku za mwanzoni mwa utawala wake.

1Wafalme 12:1-5 “Rehoboamu akaenda Shekemu; maana Israeli wote walikuwa wamekwenda Shekemu, ili kumfanya mfalme. Ikawa Yeroboamu mwana wa Nebati alipopata habari (maana alikuwa akaliko Misri, huko alikokimbilia awe mbali na mfalme Sulemani; Yeroboamu akakaa huko Misri, wakapeleka watu kwenda kumwita); basi Yeroboamu na jamii yote ya Israeli wakaenda, wakamwambia Rehoboamu, wakasema, Baba yako alilifanya zito kongwa letu; basi sasa utupunguzie utumwa mzito tuliotumikishwa na baba yako, na lile kongwa zito alilotutwika, nasi tutakutumikia. Akawaambia, Enendeni zenu hata siku ya tatu, kisha mnirudie tena. Watu wakaenda zao.”

Wana wa Israel wanaonekana ya kuwa walikuwa tayari kabisa kumtumikia mfalme Rehoboamu baada ya baba yake Suleimani, lakini walikuwa na ombi kwamba wawarahisishie maisha maana wakati wa baba yake hali ilikuwa ngumu sana walielemewa na kodi na utumwa mzito uliowanyima furaha, Suleimani alikuwa amewatumikisha watu sana kwa utumwa mzito na Kodi kwaajili ya fahari ya ufalme wake, Mfalme Rehoboamu aliwapa Muda ili kwamba aweze kulitafakari ombi lao, jambo hili au hatua hii ilikuwa njema kwani hakufanya haraka alikuwa na utulivu na hii ni hatua nzuri kila wakati tunapotaka kufanya maamuzi, hatupaswi kufanya maamuzi kwa kufuata mihemko, ni muhimu kutulia na ikiwezekana kuwa na wakati wa kumuomba Mungu ili kwamba atupe hakima ya kufanya maamuzi mema yanayokusudiwa, Mungu akitupa hekima yake tutakuwa na mafanikio makubwa sana yaani matunda mema kwa sababu hekima ya Mungu ni safi, ya amani, ya upole, na inasikiliza watu hekima hii ina rehema, na ina matunda mema haina fitina wala haina unafiki imetajwa hivyo katika maandiko;-

Yakobo 3:17-18 “Lakini hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki. Na tunda la haki hupandwa katika amani na wale wafanyao amani.”

Tunapotafakari haya tutaliangalia somo hili katika vipengele vitatu vifuatavyo:-

1.       Ushauri wa wazee na ushauri wa vijana

2.       Umuhimu wa kufanya maamuzi yenye busara

3.       Ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima

Ushauri wa wazee na ushauri wa vijana.

Kuna kitu cha kujifunza tunapoangalia maamuzi yaliyofanywa na mfalme Rehoboamu, Maamuzi yake yanaletwa kwetu na neno la Mungu ili tuweze kujifunza maswala halisi yanayoweza kujitokeza kwetu katika maisha  Mfalme Rehoboamu alipotulia ili atake ushauri, alipata ushauri kutoka katika makundi makuu mawili, kundi la kwanza lilikuwa kundi la wazee hawa walikuwa ni watu waliokuwa na uzoefu na ujuzi (Experience) walikuwa wameona utawala uliopita wa wakati wa baba yake walijua mazuri na machungu ya utawala huo, kwa kawaida Biblia inapotaja wazee wakati mwingine huwa inazungumzia UZOEFU hawa walitoa ushauri wao  kama hivi ona

 1Wafalme 12:6-7 Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani, baba yake, alipokuwa hai, akasema, Mwanipa shauri gani ili niwajibu watu hawa? Wakamwambia wakasema, Ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa leo, na kuwatumikia, na kuwajibu, na kuwapa maneno mazuri, basi watakuwa watumishi wako daima.”

Kundi hili ni kundi la watu wanaojua wapi tunatoka na wapi tunakwenda, maandiko yanaonyesha kuwa walikuwa ni washauri pia wa Mfalme Suleimani, maandiko yanasema waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani alipokuwa hai, hawa waliona ukatili aliokuwa nao Sulemani na ukali wake hunda kuna mambo walishauri na Sulemani kwa ubabe wake alikataa, na sasa anapokuja mfalme mpya walimshauri kwamba akubali kuwa mtumwa yaani mtumishi awajali watu awatumie watu lakini vilevile azungumze nao vizuri, awape majibu akutane na haja za mioyo yao, na kuwapa maneno mazuri, walimwambia akifanya hivyo watu hawa watamtumikia daima.  

Kundi la Pili lilikuwa kundi la vijana, vijana katika lugha ya kinabii ni watu wasio na uzoefu, hawana ujuzi wa kutosha wa kupambanua mambo, wao walikuwa ni machipukizi bado hawana mizizi kundi hili wao walimpa mfalme ushauri wa kuongeza ukatili na kutokuwahurumia watu

1Wafalme 12:8-11 “Lakini akaliacha shauri lile la wazee, walilompa, akataka shauri kwa wale vijana waliokua pamoja naye, na kusimama mbele yake. Akawaambia, Mwanipa shauri gani ili tuwajibu watu hawa, waliosema nami, wakinena Utufanyie jepesi kongwa lile alilotutwika baba yako? Na wale vijana waliokua pamoja naye wakamwambia, wakasema, Uwaambie hivi watu wale waliokuambia, wakisema, Baba yako alilifanya zito kongwa letu, bali wewe utufanyie jepesi, uwaambie hivi, Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu. Basi kama vile baba yangu alivyowatwika kongwa zito, mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge.”

Mfalme Rehoboamu kwa bahati mbaya alifuata ushauri wa vijana maana yake alifuata ushauri wa watu wasio na uzoefu, wajanja wajanja ambao kimsingi walikuwa wakitarajia nafasi kadhaa katika utawala mpya hivyo wasingekuwa na jipya zaidi ya kumpamba mfalme na kumpa maneno ambayo walifikiri yangeweza kuwa na tija katika jamii matokeo yake wana wa Israel waligawanyika makundi makundi na inchi ya Israel ikapoteza umoja na kuvunjika katika falme mbili

1Wafalme 12:12-16 “Basi, Yeroboamu na watu wote wakamfikia Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyoamuru, akisema, Mnirudie siku ya tatu. Mfalme akawajibu watu wale kwa ukali, akaliacha shauri lile wazee walilompa; akawajibu kama vile walivyomshauri vijana, akasema, Baba yangu alilifanya zito kongwa lenu, bali mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge. Basi mfalme hakuwasikia wale watu; maana jambo hili lilitoka kwa Bwana, ili alitimize neno lake, Bwana alilomwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kwa kinywa cha Ahiya Mshiloni. Basi Israeli wote walipoona ya kuwa mfalme hakuwasikia, hao watu walimjibu mfalme, wakasema, Tuna sehemu gani katika Daudi? Wala hatuna urithi katika mwana wa Yese. Haya! Nendeni zenu hemani kwenu, enyi Israeli; sasa itunze nyumba yako mwenyewe, Ee Daudi. Hivyo Israeli wakaenda zao hemani kwao.”

Umuhimu wa kufanya maamuzi yenye busara

Ni jambo la kusikitisha sana kuwa Nchi ya Israel iligawanyika na watu walivunjika Moyo, mfalme hakuwajibu watu kwa upole na badala yake aliwajibu watu kwa ukali na watu wakavunjika moyo kila mmoja akarejea nyumbani kwake,  Siku zote katika maisha yetu hatuna budi kuhakikisha ya kuwa tunafanya maamuzi ambayo yanampendeza Mungu maamuzi ambayo kwa namna yoyote ile hayatakuja yawaumize watu na kuwakatisha tamaa, tusifanye uamuzi wowote wenye kuaibisha watu au kudhalilisha, au kuumiza, tusifanye kwa mihemko yetu wala kwa ubinafsi wetu wala kwa kutaka makuu, Mungu anatutaka watu wote tuwe na maamuzi yenye busara, watu wa Mungu hawapaswi kuwa kama watu wa dunia hii, katika kanuni za kimungu kuwatumikia watu ndio hatua ya juu zaidi itakayotupa heshima kwa Mungu, Bwana Yesu ametufundisha kuwa namna hiyo

Mathayo 20:25-28 “Lakini Yesu akawaita, akasema, Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”

Kumbe ni kanuni ya kibiblia kabisa ya kuwa  tunapaswa kuwatumikia watu kwa maana nyingine tuwe wanyenyekevu na jambo hili litatupa faida kubwa sana katika maisha yetu, Wazee walikuwa wamemshauri Rehoboamu namna njema ya kufaulu walimtaka awe mnyenyekevu kwa watu, awe mpole azungumze nao kwa amani awe mtumwa na kuwa watu wangemtumikia daima, kumbe katika maisha yetu tukitaka kufanikiwa tukubali kuwa watumwa, tujinyenyekeze, tutii wazee, tusikilize wakubwa, tusikilize walimu, tusikilize wazazi, na walezi, tusikilize wale wenye uzoefu wanatuambia nini  na wakati wote tukatae hali ya kujifanya mabwana:-

1Petro 5: 1-3 “Nawasihi wazee walio kwenu, mimi niliye mzee, mwenzi wao, na shahidi wa mateso ya Kristo, na mshirika wa utukufu utakaofunuliwa baadaye; lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi.”

Ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima!.

Huu ndio ushauri mwema kutoka katika mapenzi ya Mungu, wazee walimshauri Rehoboamu kwamba ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa watakutumikia daima, hii ndio kanuni ya msingi ya kibiblia na ina faida nyingi sana kwa mujibu wa maandiko;-

1.       Ukijinyenyekesha utainuliwa juu sana, unapokubali kuwa mtumwa Mungu atakuinua juu mno utapanda katika viwango na watu wote watakutumikia ona Wafilipi 2:5-11 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu;  tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba. Hii ni kanuni huru ya kibiblia Zaburi 147:6 “Bwana huwategemeza wenye upole, Huwaangusha chini wenye jeuri.” Bwana wetu Yesu Kristo alikubali kuwa mtumwa, aliwatumikia watu, kumbuka alikuwa sawa na Mungu alikini alijinyenyekeza moyo wake ulijikita katika kumtumikia Mungu na watu wake na hivyi Mungu alimuinua juu sana na kumpa jina lipitalo majina yote na kutukuzwa sana mbinguni na duniani.

2.       Kujinyenyekeza kunaongeza Neema ya Mungu, 1Petro 5:5-6 “Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake;” Hakuna jambo baya duniani kama kupungukiwa neema, Mungu wetu ana upendo mkubwa sana aukipata neema mbele zake utafanikiwa katika maisha yako, lakini kiburi ni sumu ya neema, kama tukishindwa kujinyenyekesha haraka sana Mungu ataondoa neema yake kwetu! Na hivyo tutajisikia vibaya na kupatwa na aibu.

3.       Kujinyenyekeza kunaleta kukubaliwa na kujikweza kunaleta kukataliwa Luka 18:9-14 “Akawaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote. Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.” Yakobo 4:10 “Jidhilini mbele za Bwana, naye atawakuza.” 3Yohana 1:9 “Naliliandikia kanisa neno, lakini Diotrefe, apendaye kuwa wa kwanza kati yao, hatukubali.”

4.       Mungu huwasikiliza wanyenyekevu 2Nyakati 34:27 “kwa kuwa moyo wako ulikuwa mwororo, nawe umejinyenyekeza mbele ya Mungu, uliposikia maneno yake juu ya mahali hapa, na juu ya wakaao, ukajinyenyekeza mbele zangu, na kuyararua mavazi yako, na kulia mbele zangu; mimi nami nimekusikia, asema Bwana.”

5.       Unyenyekevu unaleta hekima na kutufanya tukubali kufundishika ona Zaburi 25:9 “Wenye upole atawaongoza katika hukumu, Wenye upole atawafundisha njia yake”. na Mithali 11:2 “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; Bali hekima hukaa na wanyenyekevu.”

6.       Huepusha hasira ya Mungu na kutupa wokovu ona 2Nyakati 32:26 “Hata hivyo Hezekia akajinyenyekeza kwa ajili ya huku kutukuka kwa moyo wake, yeye na wenyeji wa Yerusalemu, hata haikuwajia hasira ya Bwana siku za Hezekia.” na Zaburi 149:4 “Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake, Huwapamba wenye upole kwa wokovu.

7.       Ukijishusha utakuwa mkubwa katika ufalme wa Mungu Mathayo 18:4 Basi, ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.”    

Kama Rehoboamu angejinyenyekeza angeweza kupata thawabu kubwa na nyingi zinazotajwa katika mandiko, Bwana na ampe neema kila mmoja wetu kujifunza umuhimu wa kunyenyekea na kujishusha ili tuweze kuona faida na uzuri wa kanuni za kimungu sawa na namna Mungu anavyokusudia katika Maisha yetu na tukumbuke siku zote ya kuwa ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima.

Rev. Innocent Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Alhamisi, 15 Septemba 2022

Kuhani mkuu kwa Mfano wa Melkizedek


Zaburi 110:1-4 “Neno la Bwana kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwafanyapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako.  Bwana atainyosha toka Sayuni Fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako; Watu wako wanajitoa kwa hiari, Siku ya uwezo wako; Kwa uzuri wa utakatifu, Tokea tumbo la asubuhi, Unao umande wa ujana wako. Bwana ameapa, Wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, Kwa mfano wa Melkizedeki.”



Utangulizi

Maandiko yanamuonyesha Yesu Kristo kama ni Nabii mkubwa na aliyebora zaidi kuliko Musa, lakini pia ni Kuhani mkuu aliye bora zaidi kwa mfano wa Melkizedeki unaweza kuona poia katika Waebrania 6:20 “alimoingia Yesu kwa ajili yetu, mtangulizi wetu, amekuwa kuhani mkuu hata milele kwa mfano wa Melkizedeki.” Tunapojifunza somo hili kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki tutazingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Tofauti ya nabii na kuhani

·         Wajibu wa kikuhani.

·         Kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki

Tofauti ya Nabii na kuhani

Neno la Mungu linatufundisha tofauti kubwa iliyoko kati ya nabii na kuhani, kwa kawaida hawa wote ni watumishi wa Mungu, na huwa wanaitwa ama kuteuliwa na Mungu mwenyewe ona Kumbukumbu 18:18 “Mimi nitawaondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zao mfano wako wewe, nami nitatia maneno yangu kinywani mwake, naye atawaambia yote nitakayomwamuru.” Unaona ni Mungu ndiye anayeinua nabii na kuweka neno lake ndani yao ili aseme kwa niaba yake na kuwafundisha watu wa Mungu njia zake nan i Mungu mwenyewe anayechagua kuhani ona Waebrania 5:1-4 “Maana kila kuhani mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika mambo yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi; awezaye kuwachukulia kwa upole wao wasiojua na wenye kupotea, kwa kuwa yeye mwenyewe yu katika hali ya udhaifu; na kwa sababu hiyo imempasa, kama kwa ajili ya watu, vivyo hivyo kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi. Na hapana mtu ajitwaliaye mwenyewe heshima hii, ila yeye aitwaye na Mungu, kama vile Haruni.” Unaweza kuona hawa wote huteuliwa au kuitwa na Mungu, Nabii yeye huchaguliwa na Mungu ili awe msemaji kwa niaba ya Mungu Neno nabii katika Lugha ya kiibrania huwakilishwa kwa maneno makuu matatu ambayo ni NABI, ROEH, na HOZEH

Nabi – Maana yake ni Msemaji, au mtangazaji Hawa ni wasemaji au wanenaji wanaosukumwa na Roho wa Mungu kuyasema mapenzi ya Mungu kwa msukumo na wivu mkali wa kiungu, lakini pia ni walimu wa neno la Mungu kwa ufupi ni wasemaji kwa niaba ya Mungu, ni wasemaji wa Mapenzi ya Mungu

Roeh – Maana yake ni waonaji, au wafunuaji wao hitwa na Mungu na kuwawezesha kuona mambo yaliyofichika na kuyasema au kuonya au kutangaza au kufundisha mapenzi ya Mungu baada ya kufunuliwa na Mungu, mwisho wa siku nao ni wasemaji kwa niaba ya Mungu

Hozeh – Ni msahuri au mwenye hekima ambao kazi yao ni kufikiri na kutoa ushauri kwa niaba ya Mungu kwa watu wake ni wenye uwezo wa kutambua kama ujumbe ni wa kiungu au la walitumika sana kuwashauri wafalme ili watende sawasawa na mapenzi ya Mungu

Katika kiyunani Prophet ni mtu anayezungumza jambo kwa niaba ya mwingine kwa hivyo wao husema au kutafasiri jambo kwa niaba ya Mungu, ili watu wa Mungu wajue mapenzi ya Mungu katika maisha yao hivyo kwa vyovyote vile manabii ni walimu wa neno la Mungu, ni walimu kwa niaba ya Mungu ni wajumbe kwa niaba ya Mungu, Mungu anapotaka kuyafunua mapenzi yake kwa wanadamu.

Kuhani kwa upande mwingine ni mwanaume anayechaguliwa na Mungu kuwawakilisha wanadamu kwa Mungu, wao ni wasemaji wa wanadamu kwa Mungu, wana wana kibali maalumu cha kumfikia Mungu, na kuzungumza au kutenda kwa niaba ya wanadamu kwa Mungu , hata hivyo hii haiachi ukweli kuwa nao ni walimu wa nenola Mungu kwa watu wa Mungu, lakini mafundisho yao ni tofauti nay ale ya manabii, wakati manabii wanakazia uadilifu, hali safi ya kiroho na wajibu wetu kwa Mungu, Makuhani wao hushughulika na njia sahihi za kumuendea Mungu.

Wajibu wa kikuhani.

Huduma ya kikuhani kwa kawaida kihistoria ilianzishwa na Mungu kwa wana wa Israel baada ya kutoka katika inchi ya Misri, baada ya maelekezo ya Mungu kwa Musa katika mlima wa Sinai, Kutoka 28:1 “Nawe umlete Haruni ndugu yako karibu nami, na wanawe pamoja naye, miongoni mwa wana wa Israeli, ili anitumikie katika kazi ya ukuhani. Haruni, na Nadabu, na Abihu, na Eleazari, na Ithamari, wana wa Haruni.” Makuhani hawa walichaguliwa kutoka miongoni mwa wanadamu ili waweze kuwawakilisha wanadamu kwa Mungu kwa hiyo sifa zao zilikuwa

1.       Walichaguliwa kutoka miongoni mwa wanadamu ili kuwawakilisha wanadamu

2.       Walichaguliwa na Mungu mwenyewe

3.       Walifanya kazi ya Mungu kwa niaba ya wanadamu, kwa mambo yote ya wanadamu ya kidini ili kumfikia Mungu

4.       Walikuwa na kazi ya kutoa sadaka za kuteketezwa kwaajili ya watu kwa Mungu

5.       Walikuwa na wajibu wa kuwaombea watu kwa Mungu

6.       Walikuwa na wajibu wa kuwabariki watu wa Mungu

Kwa msingi huo katika maandiko iko wazi kabisa kuwa wajibu wa kikuhani ulikuwa ni kutoa sadaka zakuteketezwa, kuwaombea watu, na kuwabariki watu kwa jina la Mungu, hata hivyo kazi zote hizi zilizokuwa zikifanywa na makuhani bado zilikuwa zinaashiria kuwa siku moja atakuja kuhani mkuu aliye bora zaidi huyu ndiye ametabiriwa kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki “Zaburi 110:1-4 “Neno la Bwana kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwafanyapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako.  Bwana atainyosha toka Sayuni Fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako; Watu wako wanajitoa kwa hiari, Siku ya uwezo wako; Kwa uzuri wa utakatifu, Tokea tumbo la asubuhi, Unao umande wa ujana wako. Bwana ameapa, Wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, Kwa mfano wa Melkizedeki.” Huyu atakuwa ni masihi ambaye hangetoka katika ukoo wa kikuhani bali katika kabila nyingine ya Yuda na ukoo wa Daudi ukuhani wake huyu utakuwa wa milele kuhani huyu vilevile ataketi katika kiti cha enzi cha Daudi milele na milele, kuhani huyu atakuwa ni mfalme na wakati huo huo kuhani kama ilivyokuwa kwa Melkizedeki, Kuhani huyu atakuwa bora zaidi ya wale wa agano la kale kutoka kabila ya walawi, Huyu ni Yesu Kristo ambaye anafanya kazi zilezile zilizokuwa zikifanywa na makuhani katika agano lililo bora zaidi Warumi 8:33-34 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Waebrania 7:24-25 “bali yeye, kwa kuwa akaa milele, anao ukuhani wake usioondoka. Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.”  Kwa msingi huo tunaona kwamba Mungu ametupa kuhani aliyebora zaidi kutoka nje ya kabila la walawi, ambaye ni kuhani na mfalme sawa na ilivyokuwa kwa Melkizedeki

Kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki

Yesu kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki ina faida gani kwetu?  Kama wakristo? Yako mambo kadhaa ya muhimu na msingi yenye faida kwetu kwa kristo Yesu kuwa kuhani mkuu kwaajili yetu.

1.       Tunaweza kupatanishwa na Mungu

 

Kwa sababu ya kazi aliyoifanya Yesu Kristo pale msalabani kama Kuhani mkuu ametupatanisha na Mungu 2Wakoritho 5:18-20 “Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo, naye alitupa huduma ya upatanisho; yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho. Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu.”

 

Wakolosai 1:19-20 “Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; kwa yeye, ikiwa ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni.”

 

Dhambi ilisababisha uadui kati yetu na Mungu, sote tulikuwa tumefarakanishwa na Mungu lakini kupitia Kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki Neema ya Mungu imekuwa juu yetu na uadui uliokuweko kati yetu umevunjwa wote tunajua kuwa maovu huwa yanatufarikisha kwa Mungu

 

Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.”

 

Lakini kupitia Mwokozi wetu Yesu Kristo hakuna uadui tena kati yetu na Mungu Warumi 5:8:-11 “Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi. Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye. Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake; zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake. Wala si hivyo tu, ila pia twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho.”            

 

2.       Tunaweza kumfikia Mungu kwa Maombi tukiwa na ujasiri

 

Sasa tunaweza kumuomba Mungu kwa ujasiri kwa sababu ya kazi kubwa ya ukuhani aliyoifanya Bwana wetu Yesu, Mwanzoni ilikuwa ngumu kumfikia Mungu na kumuomba bila kuhani mkuu kutuombea kwanza kwa kutoa sadaka ya dhambi zake na zetu ndio tupate kibali cha kumfikia Mungu na ujasiri wa mioyo yetu, Lakini kupitia ubora wa sadaka aliyoitoa kuhani huyu mkuu kwa mfano wa Melikizedeki sasa tunaweza kabisa kumuendea Mungu kwa ujasiri na kumuomba moja kwa moja ikifahamika ya kuwa tunaye mwombezi na mpatanishi mbinguni Warumi 8:33-34 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Waebrania 7:24-25 “bali yeye, kwa kuwa akaa milele, anao ukuhani wake usioondoka. Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.” Tunaoujasiri ya kuwa Mungu anasikia maombi yetu na kuwa atatujibu sawa na mapenzi yake kwanini kwa sababu mwanzoni ilikuwa ngumu Yohana 9:31 “Twajua ya kuwa Mungu hawasikii wenye dhambi; bali mtu akiwa ni mcha Mungu, na kuyafanya mapenzi yake, humsikia huyo.”

 

3.       Tunapata amani nafsini mwetu

 

Jambo lingine bora zuri na la amani ni kuwa tunapata amani katika dhamiri zetu hii pia ni kutokana na kazi kubwa aliyoifanya Bwana wetu Yesu Kristo pale Msalabani, Waebrania 4:14-16 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi.  Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”

4.       Sisi sasa ni makuhani pia.

 

Moja ya faida kubwa tunayoipata katika ukuhani wa Yesu Kristo, ni pamoja na sisi kuwa tunaushiriki huo ukuhani hivyo kila aaminiye ni kuhani 1Petro 2:9-10 “       Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

 

Ufunuo 1:4-6  Yohana, kwa yale makanisa saba yaliyoko Asia; Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwake yeye aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja; na zitokazo kwa roho saba walioko mbele ya kiti chake cha enzi; tena zitokazo kwa Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa waliokufa, na mkuu wa wafalme wa dunia. Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake, na kutufanya kuwa ufalme, na makuhani kwa Mungu, naye ni Baba yake; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na milele. Amina.”

 

Raha ya aina yake kuwa na kuhani mkuu wa kipekee mwenye Baraka zetu zote za kimwili na kiroho!

 

Rev. Innocent Kamote.

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jiwe la Kukwaza Katika Sayuni !


1Petro 2:6-8 “Kwa kuwa imeandikwa katika maandiko Tazama, naweka katika Sayuni jiwe kuu la pembeni, teule, lenye heshima, Na kila amwaminiye hatatahayarika.  Basi, heshima hii ni kwenu ninyi mnaoamini. Bali kwao wasioamini, Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni. Tena, Jiwe la kujikwaza mguu, na mwamba wa kuangusha, Kwa maana hujikwaza kwa neno lile,wasiliamini,nao waliwekwa kusudi wapate hayo.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa ni kwanini mtume Petro anamtaja Yesu Kristo kama jiwe la kukwaza? (Stumbling block) Hili linaweza kuwa jambo lenye kushangaza sana, kwa sababu kwa lugha rahisi hauwezi kudhani kuwa Mungu angeweza kukusudia Kristo Yesu awe jiwe la Kukwaza pia, Katika hali ya kawaida tunapomuelezea Yesu Kristo kama jiwe la Pembeni na lenye heshima inaweza kueleweka vema zaidi, lakini hata hivyo kama tutaelewa kile kinacho maanishwa katika maandiko tunaweza kutoka tukiwa na amani ya kutosha sana kumuhusu Yesu Kristo na sisi tuliomuamini. Tutajifunza somo hili kwa kuzinagatia vipengele vifuatavyo vikuu viwili vifuatavyo:-

·         Maana ya jiwe la kukwaza.

·         Jiwe la kukwaza katika Sayuni. 

Maana ya jiwe la kukwaza.

Kibiblia neno jiwe la kukwaza au kukwaza maana yake ni kukosesha kwa hila kwa kiingereza ni Stumbling Block yaani ukwazo, au makwazo ambalo kwa kiibrania husomeka kama neno Miksol na kwa kiyunani ni Skandalon ambalo maana yake ni kukosesha au kutegea mtu ili aanguke na kupata madhara au jambo lolote linaloweza kufanyika na kumfanya mtu afanye dhambi au apatikane na madhara na kuhukumiwa sawa na kumuwekea mtu mtego ili aingie hatiani 

Zaburi 140:4-5 “Ee Bwana, unilinde na mikono ya mtu asiye haki; Unihifadhi na mtu wa jeuri; Waliowaza kuzipotosha hatua zangu. Wenye kiburi wamenifichia mtego na kamba; Wametandika wavu kando ya njia; Wameniwekea matanzi.”

Jambo hili kimaandiko sio jambo jema na Katika lugha ya kinabii kukosesha mtu au kumkwaza mtu kulihesabika kuwa ni tukio baya, hasa linapofanyika kwa mtu asiye na hatia, Mungu aliwaagiza makuhani kutokuweka kwazo kwa mtu asiye na ufahamu au asiyeona (kipofu) kwani kufanya hivyo lilionekana kuwa jambo baya na la kikatili sana  

Walawi 19: 14 “Usimlaani kiziwi, wala usitie kwazo mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako; Mimi ndimi BWANA.”

Kimsingi maandiko haya yalikuwa na maana ya kutokusababisha makwazo kwa watu wanaohitaji kuelekezwa au kufahamishwa, kwa hiyo kimsingi maonyo haya yanawahusu walimu wa neno la Mungu kwamba wasitumie ufahamu wao kuwapotosha watu kwa hila kwa kufanya hivyo kungeleta hukumu iliyokubwa sana au ya kutisha ona

 Mathayo 18:6 “bali atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari.

Unaweza kuona maandiko yanatangaza hukumu kubwa sana kwa mtu atakayekosesha wengine au kwa lugha nyingine anayesababisha makwazo au kwa lugha nyingine kufundisha watu uongo au kumtia mwenye haki hatiani

Yakobo 3:1-2 “Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa mtapata hukumu kubwa zaidi. Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”  

Kwa msingi huo unaweza kupata picha ya wazi kuwa kukosesha au kukwaza kamwe kibiblia halikuweza kuhesabiwa kuwa  la jambo zuri bali ni tukio baya na lililoambatana na maonyo makali dhidi ya wale wote wanaosababisha makwazo ya aina yoyote ile :-

Luka 17:1-2 “Akawaambia wanafunzi wake, Makwazo hayana budi kuja, lakini ole wake mtu yule ambaye yaja kwa sababu yake! Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa wadogo hawa.  

Sasa ni katika namna ya kushangaza sana unaweza kustaajabu kuona kuwa ujio wa Masihi Bwana wetu Yesu Kristo unatajwa vilevile kuambatana na Heshima kwa wale watakaomwamini lakini vilevile na kukwaza  kwa wale watakaomkataa au kutokumuelewa na kutokumuamini hii maana yake ni nini hilo sasa linatuleta kutafakari kipengele kinachofuata kama ifuatavyo:-         

Jiwe la kukwaza katika sayuni

Ni muhimu kufahamu kuwa kuja kwa Yesu Kristo duniani, kulitabiriwa na manabii na kuwekwa wazi kuwa Yesu angekuja kwa makusudi makuu mawili, yaani kuokoa wengi  na kuwapa heshima kubwa lakini vilevile kukwaza wengi hasa wale wasiomuamini au wasiomuelewa na kumkubali na kusababisha hukumu kubwa sana kwao, 

Yohana 3:16 -18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Kwa msingi huo ujio wa Yesu Kristo una maswala makubwa mawili ya msingi kwa wanaomuamini na kwa wasiomuamini, wanaomuamini hawatatahayarika lakini kwa wale wasiomuamini watapata hukumu watakutana na mambo magumu sana sawa na alivyotabiri nabii isaya ona.  

Isaya 28:16 “kwa ajili ya hayo Bwana, MUNGU, asema hivi, Tazama, naweka jiwe katika Sayuni, liwe msingi, jiwe lililojaribiwa, jiwe la pembeni lenye thamani, msingi ulio imara; yeye aaminiye hatafanya haraka.”

Swala hili lilielezwa mapema katika maandiko lakini vilevile nabii mwingine alimuelezea Mariamu mama yake Yesu waziwazi mara baada ya kuzaliwa na walipokuwa wamempeleka kijana Yesu Hekaluni kwa kubarikiwa ona katika

Luka 2: 25-34 “Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake. Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, yeye mwenyewe alimpokea mikononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema, Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, Uliouweka tayari machoni pa watu wote; Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.  Na babaye na mamaye walikuwa wakiyastaajabia hayo yaliyonenwa juu yake. Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa.”

Kuna maneno kadhaa ambayo watafasiri wa biblia ya Kiswahili waliyachanganya au kuyanukuu vibaya hasa katika mstari wa 34 hapo ambao katika biblia ya Kiswahili Union Version unasomeka hivi Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa.” Mstari huo katika biblia ya  kiingereza  ya NIV yaani New International version unasomeka hiviThen Simeon blessed them and said to Mary, his mother: This child is destined to cause the Falling and rising of many in Israel, and to be a sign that will be spoken againstkwa hiyo kwa tafasiri yangu mimi kifungu hiki kilitakiwa kusomeka Simeoni akawabarikia na kumwambia Mariam, mama yake, Mtoto huyu hatima yake itasababisha kuanguka (Kujikwaa) na kuinuka (kuokolewa) kwa wengi katika Israel  na kuwa Ishara itakayonenwa kinyume  unaona Kwa msingi huo Petro anamuelezea Yesu katika pande hizo mbili ya kuwa ni jiwe zuri sana la thamani na heshima kwa wale walimuamini lakini vilevile ni jiwe la kukwaza kwa wale waliomkataa na wasiomuelewa, au waliompuuzia, Wakati wote Yesu alipokuwa duniani na kufanya kazi yake  makundi mawili yalitokea wale waliomuamini na wale wasiomuamini na wale wasiomuamini Kristo wamepata hasara kubwa sana Yohana 6:54-62 Petro anatoa ushauri kwa waamini waendelee kumfuata Yesu kwa sababu yeye ni jiwe lililo hai, ni jiwe teule, ni jiwe lenye heshima na kwa kufanya hivyo hakuna mtu atakayetahayari au atakayeaibika kwa kumtegemea Yesu. 

1Petro 2:4-9 “Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima. Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo. Kwa kuwa imeandikwa katika maandiko Tazama, naweka katika Sayuni jiwe kuu la pembeni, teule, lenye heshima, Na kila amwaminiye hatatahayarika. Basi, heshima hii ni kwenu ninyi mnaoamini. Bali kwao wasioamini, Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni.Tena, Jiwe la kujikwaza mguu, na mwamba wa kuangusha, Kwa maana hujikwaza kwa neno lile,wasiliamini,nao waliwekwa kusudi wapate hayo. Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu;    
    

Petro anakazia katika ujumbe wake sawa na neno la Mungu kwa vinywa vya manabii ya kuwa tumchague Yesu, yeye ni jiwe lenye heshima ni teule limendaliwa na Mungu baba kwaajili ya ukombozi wetu na kwamba ni fahari kumuamini Yesu na kumkubali na kuwa yeye hatatukataa na kuwa hatutatahayari, yesu hatamuangusha mtu awaye yote anayemtumaini na kumwendea yeye wakati wowote hata tuwapo majaribuni, hatatuangusha kwa hiyo ukimuamini Yesu na kumtegemea katika maisha yako kutoboa katika jambo lolote kuko nje nje lakini ukimpuuzia Yesu aibu na makwazo na hukumu zinakungoja ona katika maandiko:- 

Warumi 9:33 “kama ilivyoandikwa, Tazama, naweka katika Sayuni jiwe likwazalo, na mwamba uangushao; Na kila amwaminiye hatatahayarika.”  

Kumwamini Yesu kunalipa na kuliwapa faida kubwa wale waliomsadiki, lakini wale wanaojifanya wana hekima na akili na wanaomtambua Yesu kama mtu wa kawaida watajikwaa, watu hawajikwai kwa Yesu tu wanajikwaa hata kwa neno lake na kukataa ujumbe wake hata leo, Yesu hatambuliki kwa historia ya kibinadamu tu na hekima ya kibinadamu tu huwezi kumtambua Yesu kwa hisia tu, au kwa ujuzi wako binafsi, wako watu waliojikwaa kwa sababu walimuona Yesu kuwa ni wa kawaida tu wakitimia akili zao na hekima ya kibinadamu watu wengi wataingia dhambini na hatimaye kuingia mtoni kwa sababu ya kutumia fahamu zao katika maswala ya kiungu, wako watu wenye dharau kubwa sana kuhusu Mungu, na mambo ya Mungu huonekana kama ya kipumbavu kwao, na wengine hulichukulia neno la Mungu kwa mazoea tu  jambo hili litawagharimu gharama kubwa sana kwa sababu watajikwaa na ukijikwaa hukumu itakupasa 

Marko 6:1-3 “Akatoka huko, akafika mpaka nchi ya kwao; wanafunzi wake wakamfuata. Na ilipokuwa sabato, alianza kufundisha katika sinagogi; wengi waliposikia wakashangaa, wakisema, Huyu ameyapata wapi haya? Na, Ni hekima gani hii aliyopewa huyu? Na, Ni nini miujiza hii mikubwa inayotendeka kwa mikono yake? Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake.” 

Hatuwezi kumtambua Yesu kwa akili za kawaida na ujuzi wa kawaida Yesu alikuja ili wanyenyeevu watu waliovunjika moyo waweze kumkubali na watu wenye kiburi waweze kukataliwa Yesu ataendelea kuwa jiwe la kukwaza kwa watu wote wanaojidhani kuwa wana hekima ya mwilini na watu wote wenye kiburi na wale wanaojihesabia haki na ndio maana Yesu alipokuja duniani Mafarisayo ambao  walifikiriwa kuwa ndio wenye Haki waliumbuliwa na kujulikana kama wanafiki, wale waliokuwa wakiitumainia haki yao wenyewe waliumbuka na kujiona kuwa sio kitu kila mtu anayejitumainia na kujiamini mwenyewe Yesu kama jiwe la kukwaza litawasaga tikitiki, watu wasio na akili huitegemea akili yao wenyewe, lakini Yesu ameifanya hekima ya dunia hii kuwa ni upuuzi na kuifanya kuwa si kitu ni kupitia kumwamini Yesu tu tunaweza kuokolewa na kuhesabiwa haki kutoka kwa Mungu, kila anayemuami Yeye hatatahayari wala hatakwazika lakini kila anayejitumainia atakwazika na kukengeuka na kuingia katika hukumu ya Mungu. Mungu hawezi kueleweka kwa hekima ya kibinadamu, wengi waliokosa Baraka za Mungu ni wale waliopuuzia neno la Mungu na kuona kama Yesu hana maana lakini wale wanaomkubali wanazijua nguvu zake na uwezo wake 

1Wakoritho 1:18-19 “Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, Na akili zao wenye akili nitazikataa.”   
              

Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima



Alhamisi, 21 Julai 2022

Waachie watu wangu waende!


Kutoka 3:7-10 “BWANA akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa. Haya, basi, nitakutuma sasa kwa Farao, ili upate kuwatoa watu wangu, hao wana wa Israeli, katika Misri.”



Utangulizi:

Tuwapo Duniani tunapitia changamoto za aina mbalimbali, ikiwa ni pamoja na mikandamizo ya aina mbalimbali kutoka kwa Shetani ambaye ndiye adui mkubwa wa maisha ya wanadamu, Mungu hafurahii uonevu au udhalimu wa aina yoyote ule unaowapata wanadamu, Wana wa Israel kwa Muda mrefu sana walikuwa wakionewa na wamisri na wakikandamizwa ili waendelee kuwa watumwa katika nchi ya Misri, hawakuweza kutoka, na adui hakutaka kuwaachia kwa haraka mpaka Mungu alipoamua kuingilia kati.

Mungu alimtuma Musa kwa mfalme wa Misri yaani Farao ili amuamuru mfalme huyu awaachie wana wa Israel waende zao kwa kusudi alilolikusudia Mungu mwenyewe yaani wakamtumikie Mungu na kutimiza kusudi lake, Ujumbe mkubwa aliopewa Musa ulikuwa ni kumwambia Farao Mungu wa ewaebrania ameamuru uwaachie watu wake waende, WAACHE WATU WANGU WAENDE hii ilikuwa ni Amri na sio ombi ujumbe huu umerudiwa tena na tena kwa farao waachie watu wangu waende ona katika maandiko yafuatayo:-

Kutoka 5:1  Hata baadaye, Musa na Haruni wakaenda wakamwambia Farao, wakasema, BWANA, Mungu wa Israeli, asema hivi, WAPE WATU WANGU RUHUSA WAENDE, ili kunifanyia sikukuu jangwani.”

Unaona sifurahiswi kwa namna fulani na lugha inayotumika katika Kiswahili kwa sababu yenyewe iko katika mfumo wa kiungwana nani kama  ombi WAPE WATU WANGU RUHUSA WAENDE kimsingi Mungu hakuwa anaomba ruhusa Mungu alikuwa anaamuru ni amri kwa Farao WAACHIE WATU WANGU WAENDE, Lugha ya kiingereza katika maeneo yote yanayozungumzia WAPE WATU WANGU RUHUSA WAENDE  inatumia AMRI lugha inayotumika kiingereza ni neno LET MY PEOPLE GO sawa na kuamuru Waachie watu wangu waende ni aina hii ya lugha ndio inayojirudia rudia kila mahali kwenye kitabu cha kutoka  na maeneo mengine na unaweza kuona ;-

Kutoka 8:1 “BWANA akamwambia Musa, Ingia kwa Farao, ukamwambie, BWANA asema hivi, Wape watu wangu ruhusa, ili wapate kunitumikia.”

Kutoka 8:20 “BWANA akamwambia Musa, Inuka asubuhi na mapema usimame mbele ya Farao; angalia! Atoka aende majini; kamwambie, BWANA asema, Wape watu wangu ruhusa waende zao, ili wanitumikie mimi.”

Kutoka 9:1 “Ndipo BWANA akamwambia Musa, Ingia wewe kwa Farao, umwambie, BWANA, Mungu wa Waebrania, yuasema, Wape ruhusa watu wangu ili waende wanitumikie.”

Kutoka 9:16-17 “lakini, nilikusimamisha wewe kwa sababu hii hii, ili nikuonyeshe uweza wangu, tena kwamba jina langu litangazwe katika dunia yote. Nawe, je! Hata sasa wajitukuza juu ya watu wangu, usiwape ruhusa waende zao”?          

Unaona ni kwanini Mungu amerudia mara kwa mara kwa msisitizo waache watu wangu waende? Mungu hafurahii udhalimu, ukandamizaji na mateso ambayo kwaasili watu wake wanayapitia Mungu aliamua kuingilia katika hali ya wana wa Israel kwa kuwa walikuwa wanaonewa na wamisri na wamisri ndio walikuwa wenye nguvu zaidi kuliko Israel, Mungu hakubaliani na uonevu wa aina yoyote ile:-

Uonevu ni nini hasa!

1.       Ni kukandamizwa na kuwekwa chini ya mamlaka ya mtu mwingine mwenye nguvu zaidi yako bila matakwa yako mwenyewe

2.       Ni kuonewa au kuteswa na nguvu Fulani iliyojuu zaidi ya uwezo wako wa kawaida, bila uhuru kamili

3.       Uonevu hauko katika eneo moja tu, unaweza kuweko katika mwili, katika akili, katika nafsi, katika ndoa, katika fedha katika Elimu,Biashara, haki na kadhalika  na pia uko uonevu wa kiroho au tunaweza kusema kuwa asili yauonevu wa aina yoyote unaouona ni kutokea rohoni au katika ulimwengu wa kiroho;

Hatuna budi kugundua na kubaini ni maeneo gani ya uonevu shetani anatuonelea ili tuweze kuliitia jina la Mungu atuokoe, kumbuka Israel waliteseka mpaka pale walipolia na kutafuta msaada wa Mungu ndipo Mungu aliposhuka ili awaokoe ona Zaburi 118:5 “Katika shida yangu nalimwita BWANA; BWANA akanijibu akaniweka panapo nafasi.” Unaona kila shida unayoipitia kama mwanadamu hakikisha ya kuwa unamuita Bwana yaani Mungu naye atakuweka panapo nafasi yaani atakujibu na kutatua tatizo ulilonalo usinyamaze ukafikiri ya kuwa Mungu amekusahau, HAPANA Mungu anakutaka uwajibike na kufanya sehemu yako kwa kukataa hali unayoipitia.

Zaburi 42:9 “Nitamwambia Mungu, mwamba wangu, Kwa nini umenisahau? Kwa nini ninakwenda nikihuzunika, adui wakinionea?

Mwandishi wa zaburi aliamua kuomba Mungu Mwamba wake aliona kama amesahaulika adui alikuwa akimuonea na hakuwa na furaha alikumbuka kumwambia Mungu, ni lazima tumlilie Mungu atutoe katika hali zozote za mikandamizo tunazozipitia duniani kumbuka kuwa ni ahadi ya Mungu kutuweka huru kutoka kwa wale wanaotuonea, Mungu ameahidi kwamba utakuwa mbali na kunewa ona  

Isaya 54:14. “Utathibitika katika haki; utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu, kwa maana haitakukaribia.”

Wakati wowote uonevu sio jambo zuri, maandiko yanasema uonevu humfanya mtu awe kama kichaa, Moja ya sababu ya kuja kwa Yesu Kristo duniani kama Mwokozi ni pamoja na kufanya kazi ya kuwafungua walioonewa ona Matendo 10:38 “habari za Yesu wa Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa Roho Mtakatifu na nguvu naye akazunguka huko na huko, akitenda kazi njema na kuponya wote walioonewa na Ibilisi; kwa maana Mungu alikuwa pamoja naye.” Adui yetu mkuu adui wa wanadamu wote na anayetuonea ni shetani yeye hutuonea katika mazingira mbalimbali na wakati mwingine anawatumia watu kuleta uonevu, shetani na mapepo na maajenti wake wanaweza kumuonea mwanadamu katika maeneo zaidi ya kumi na tano:-

·         Unaweza kuonewa Mwili

·         Unaweza kuonewa kwa asili

·         Unaweza kuonewa kiakili

·         Unaweza kuonewa Kiroho

·         Unaweza kuonewa katika Ndoa yako

·         Unaweza kuonewa kiuchumi

·         Unaweza kuonewa Kazini

·         Unaweza kuonewa katika ndoto

·         Unaweza  kuonewa kwa maneno

·         Unaweza kuonewa kihisia/Kisaikolojia/kijinsia.

·         Unaweza kuonewa kichawi

·         Unaweza kuonewa kwa ukoo mzima mnateswa ukoo wenu wote au familia yenu yote

·         Unaweza kuonewa kwa nguvu na uonevu wa kukandamizwa

·         Unaweza kuonewa katika haki zako makahamani

·         Unaweza kuonewa bila sababu

·         Unaweza kuonewa kwa sababu

·         Unaweza kuonewa kihuduma

Maandiko yanaonyesha kuwa kila aina ya uonevu hutoka kwa shetani Yohana 10:10Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.” Ni kwa sababu ya kuonewa kwa namna mbalimbali Mungu alimpaka Yesu Mafuta ili aweze kuwakomboa wanadamu, na Mungu vilevile huwapaka watumishi wake mafuta ili kuzivunja nira za uonevu ona Luka 4:18-19 “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.” Unaona Lugha inayotumika hapo kusetwa maana yake ni kuonewa huduma ya kimasihi ilitolewa na Mungu kwa wanadamu kwa kusudi la kuwaweka watu huru kutoka katika uonevu wa kila namna, kama Musa ambaye alikuwa na ujumbe waache watu wangu waende, Yesu ana ujumbe ulio bora zaidi katika ufalme wa ibilisi kumuamuru kwa jina lake kukuacha uwe huru kutoka katika aina yako ya mgandamizo uliyo nayo!

Tunawezaje basi kutoka katika migandamizo ya shetani.

1.       Kubali zawadi ya wokovu:

Ni ukweli ulio wazi kuwa wokovu ni msamaha wa dhambi, nani ukweli ulio wazi kuwa Mungu anatuhurumia na mgandamizo mkubwa na wa kwanza alionao mwanadamu ni kuwa katika maisha ya dhambi, dhambi yenyewe ikukutawala inakugeuza kuwa mtumwa inakukandamiza, wanadamu wengi wanakandamizwa na dhambi hivyo ni watumwa wa dhambi hawawezi kuimudu na hawawezi kuishinda ona Yohana 8:34 “Yesu akawajibu, Amin, amin, nawaambia, Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi.” Matatizo mengi ya wanadamu yamesababishwa na dhambi, mtu anayedumu katika dhambi naye ni mtumwa wa dhambi, dhambi ni mlango mkubwa wa mashambulizi mengi ya adui katika maisha yetu na uharibifu wa kila namna,  wakati mwingine utaweza kuona mtu aliposamehewa dhambi hapo hapo alipata na uponyaji wa mwili na akili na roho ona Zaburi 103:3 “Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote,” unaona Mungu anaposamehe dhambi katika kifurushi kimoja hikihiki cha msamaha anatoa na uponyaji kwa hivyo kimaandiko ni dhahiri kwamba dhambi ikiondoka kwetu ni rahisi sana kuwa huru katika maeneo mengine Yohana 5:14 “Baada ya hayo Yesu akamkuta ndani ya hekalu, akamwambia, Angalia, umekuwa mzima; usitende dhambi tena, lisije likakupata jambo lililo baya zaidi.” Unaona yako mateso mengine ambayo yana uhusiano wa moja kwa moja na dhambi japo sio yote hivyo Mungu anapotusamehe dhambi basi moja kwa moja anatuweka huru vile vile na kutupa uzima wa maeneo mengine, unapokuwa kwenye dhambi unapoteza haki zako nyingi ikiwa ni pamoja na ulinzi wa Mungu na hivyo adui anakuwa na mamlaka ya kukuonea lakini wokovu unapokuja kwetu tunapewa haki yetu

 

Warumi 6:16-20 “Hamjui ya kuwa kwake yeye ambaye mnajitoa nafsi zenu kuwa watumwa wake katika kumtii, mmekuwa watumwa wake yule mnayemtii, kwamba ni utumishi wa dhambi uletao mauti, au kwamba ni utumishi wa utii uletao haki. Lakini Mungu na ashukuriwe, kwa maana mlikuwa watumwa wa dhambi, lakini mliitii kwa mioyo yenu ile namna ya elimu ambayo mliwekwa chini yake; na mlipokwisha kuwekwa huru mbali na dhambi, mkawa watumwa wa haki. Nasema kwa jinsi ya kibinadamu kwa sababu ya udhaifu wa miili yenu. Kwa kuwa kama mlivyovitoa viungo vyenu vitumiwe na uchafu na uasi mpate kuasi, vivyo hivyo sasa vitoeni viungo vyenu vitumiwe na haki mpate kutakaswa. Kwa maana mlipokuwa watumwa wa dhambi, mlikuwa huru mbali na haki.”

 

Uko uhusiano mkubwa sana wa mafanikio yetu ya kiroho yaani wokovu na afya yetu Yakobo 5:13-15 “Mtu wa kwenu amepatikana na mabaya? Na aombe. Ana moyo wa kuchangamka? Na aimbe zaburi. Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”


3Yohana 1:2 “Mpenzi naomba ufanikiwe katika mambo yote na kuwa na afya yako kama vile roho yako ifanikiwavyo

 

Unaona kwa hiyo kuipokea zawadi ya wokovu ni kwa Muhimu na msingi wa kufunguliwa kwetu kutoka katika migandamizo ya namna mbalimbali wokovu una uhusiano mkubwa na kusamehewa dhambi Luka 1:77 “Uwajulishe watu wake wokovu, Katika kusamehewa dhambi zao.”  Na Mafanikio yetu katika mambo yote asili yake ni mafanikio ya roho zetu, Ni kwaajili ya ukombozi wa Mwanadamu Mungu alimtuma Yesu duniani ili kila anayemwamini awe na uzima wa milele kwa hivyo tunapata uzima huu na uzima wa milele, Yesu alitolewa pale msalabani na kuteswa na kuuawa ili sisi tuweze kupona katika maeneo yote kama asemavyo nabii Isaya mahali Fulani hivi:-

 

Isaya 53:3-5 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

 

Kumbe ni ukweli ulio wazi kuwa tukimwamini Bwana Yesu kazi yake aliyoifanya pale msalabani na kuikubali kama zawadi tutaokolewa, Na ndani ya wokovu tutapata raha nyingi sana nafsini mwetu wokovu huwa na ukombozi mkubwa na wa aina nyingi. Yesu alikuwa ameahidi tujitie nira yake ili tusilemewe na mizigo yaani utumwa wa namna mbalimbali Mathayo 11:28-29 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;”    

 

2.       Uwe na ufahamu wa neno la Mungu.

 

Ufunuo 12:10-11 “Nikasikia sauti kuu mbinguni, ikisema, Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku. Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa.”

 

Neno la ushuhuda maana yake ni neno la Mungu, neno la Mungu lina nguvu na mamlaka kubwa sana kuliko tunavyodhani lenyewe linafananishwa na nyundo ivunjayo mawe vipande vipande ona Yeremia 23:28-29 “Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema Bwana. Je! Neno langu si kama moto? Asema Bwana; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande?

 

Unaona iwapo unataka ushindi katika maisha yako huna budi kujaa neno, Neno linafananishwa na moto au nyundo ivunjayo mawe vipande vipande, hivyo tukiujaza ufahamu wetu kwa neno la Mungu kila aina ya utumwa itavunjika haijalishi ni utumwa  wa zamani kiasi gani, au ni wenye nguvu kiasi gani wala haijalishi ni nani ametuweka kwenye utumwa huo, au utumwa huo unatokea wapi?, kinga kubwa na ya kipekee na silaha ya kumshambulia adui na kupata ushindi ni neno la Mungu.

 

Waebrania 4:12-13 “Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo. Wala hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake, lakini vitu vyote vi utupu na kufunuliwa machoni pake yeye aliye na mambo yetu.”       

 

Kamwe tusilidharau neno la Mungu wala kulichukulia kama kitu cha kawaida neno la uzima linga nguvu ya kubadili kila kitu katika maisha yetu neno la Mungu linapotamkwa huwa haliendi bure ni lazima litatimiza mapenzi ya Mungu ona

 

Isaya 55:9-11 “Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu. Maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”

 

Neno la Mungu ni roho tena ni uzima Yohana 6:63 “Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima.”               

 

Muda usingeweza kutosha kupitia maeneo kadhaa wa kadhaa yanayotufundisha kuhusu neno la Mungu ni ukweli ulio wazi kuwa Yesu alipopandishwa katika mlima wa majaribu alikutana na shetani na kwa kutumia neno la Mungu aliweza kupata ushindi mkubwa hakuweza kujitia chini ya ushawishi na majaribu ya yule Muovu, tunaweza kushinda hali zozote zile endapo tutakuwa na tabia ya kutafuta neno la Mungu linazungumza nini kutokana na hali yetu na ile hali tunayokumbana nayo na tukajiweka huru!

 

3.       Omba kwaajili ya ukombozi.

 

Mwanadamu anapokuwa anakandamizwa na ibilisi katika maeneo mbalimbali, kumbuka kuwa huwezi kujitoa mwenyewe katika maeneo hayo, ni lazima umuombe Mungu aje akupe msaada wa ukombozi, akukomboe kutoka katika hali unayoipitia, Neno ukombozi limetajwa mara 147 katika maandiko, Yesu ni mwokozi maana yake vilevile ni Mkombozi,  watu waliokuwa wanatazamia kuzaliwa kwa Masihi vilevile wanaitwa watu waliokuwa wakiutazamia ukombozi

 

Luka 2:36-38 “Palikuwa na nabii mke, jina lake Ana, binti Fanueli, wa kabila ya Asheri, na umri wake ulikuwa miaka mingi, alikuwa amekaa na mume miaka saba baada ya uanawali wake. Naye ni mjane wa miaka themanini na minne; haondoki katika hekalu, ila huabudu usiku na mchana kwa kufunga na kuomba.Huyu alitokea saa ile ile akamshukuru Mungu, na wote waliokuwa wakiutarajia ukombozi katika Yerusalemu akawatolea habari zake.”

 

Yesu kwa kuwa ni Mkombozi ni vema tunapopita taabuni ni muhimu kuliitia jina lake kwaajili ya ukombozi, kwanini kwa sababu maandiko yanaonyesha ya kuwa ndani yake yeye tunao ukombozi, Waefeso 1:6-7 “Na usifiwe utukufu wa neema yake, ambayo ametuneemesha katika huyo Mpendwa. Katika yeye huyo, kwa damu yake, tunao ukombozi wetu, masamaha ya dhambi, sawasawa na wingi wa neema yake.” Kwa hiyo tunakubaliana kuwa kuna ukombozi na huu hufanywa na Yesu Kristo kwa neema yake, Yeye alijitoa mwenyewe ili atukomboe sisi

 

Tito 2:13-14 “tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu; ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi yote, na kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema.”

 

1Wakorintho 1:30-31 “Bali kwa yeye ninyi mmepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu hekima itokayo kwa Mungu, na haki, na utakatifu, na ukombozi; kusudi, kama ilivyoandikwa, Yeye aonaye fahari na aone fahari juu ya Bwana.”

 

Yesu kama mkombozi wetu yu aweza kutukomboa nafsi zetu miili yatu na roho zetu, Mungu alimkomboa Daudi katika shida zake zote na hakusahau jambo hili katika maisha yake yote, kumbe tunaweza kupitia shida na mateso ya aina mbalimbali lakini Mungu anaweza kutukomboa na shida zote ona 1Wafalme 1:30 “Naye mfalme akaapa, akasema, Bwana aishivyo, aliyenikomboa roho yangu katika shida zoteKristo Yesu anaweza kutukomboa na shida zetu zote maana yake kila eneo ambalo kwalo adui anakusudia kutukandamiza au anatukandamiza tayari tunaye mkombozi,  tunaweza kukombolewa, familia zetu, maisha yetu, ndoa zetu, uchumi wetu,  na hata kama tunadhani kuwa tuna laana ya aina yoyote laana hizo zinaweza kukombolewa kupitia Jina la Yesu, Lakini vilevile kwa imani katika kazi yake aliyoifanya pale Msalabani

 

Wagalatia 3:13-14 “Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti; ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika Yesu Kristo, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani.”

 

Ni wajibu wetu kama waamini kuutarajia ukombozi Zaburi 130:7-8 “Ee Israeli, umtarajie Bwana; Maana kwa Bwana kuna fadhili, Na kwake kuna ukombozi mwingi.Yeye atamkomboa Israeli na maovu yake yote.”  Mungu ameahidi kuwa tumtarajie yeye, kumtarajia maana yake kumsubiria, kumgojea katika njia ya Maombi, na kumtazamia, tunapaswa kuiamini ahadi hii ya Mungu na kumuomba ukombozi katika maeneo mbalimbali tunayokandamizwa, Yeye ana uwezo wa kutukomboa katika taabu zote, tunapomlilia yeye hutuponya na taabu zetu zote na kutukomboa  Zaburi 107:1-6. “Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, Kwa maana fadhili zake ni za milele. Na waseme hivi waliokombolewa na Bwana, Wale aliowakomboa na mkono wa mtesi. Akawakusanya kutoka nchi zote, Mashariki na magharibi, kaskazini na kusini. Walitanga-tanga jangwani katika njia ya nyika; Hawakuona mji wa kukaa. Waliona njaa, waliona na kiu, Nafsi yao ilikuwa ikizimia ndani yao. Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao.”

 

Tukimlilia Mungu na kumuomba yeye atatuma ukombozi katika maisha yetu Zaburi 111:9 “Amewapelekea watu wake ukombozi, Ameamuru agano lake liwe la milele, Jina lake ni takatifu la kuogopwa.”

 

Hatuna budi kumuomba Mungu na kumlilia ili atukomboe na kutuachia kila mmoja asiwe chini ya uonevu na kukandamizwa na ibilisi, Mungu na amuweke huru kila mmoja na familia yake na ndugu zake na jamaa zake, Mungu atupe kuwa mbali na uonevu, Mungu na atuthibitishe katika haki!, hatuna budi kumuomba Mungu atukomboe na roho zote chafu za uharibifu, kiburi, migawanyiko, woga, uzushi, mikandamizo, rushwa, uchafu, ufisadi, tamaa, mashaka, kutokusamehe, upotoshaji, uvivu, uchawi, utapeli, uasi, hasira, ulevi, Mauti, maluweluwe, uchungu, zinaa na uasherati, ulafi, choyo, ubinafsi,  na mambo yanayofanana na hayo!.

 

4.       Tumia silaha ya kusifu:

 

Moja ya silaha Muhimu ya ukombozi wetu kutoka kwa Mungu kwa mujibu wa maandiko ni pamoja na kumsifu Mungu, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kuanza maombi kwa Msingi wa kumsifia Mungu kumuheshimu na kumtukuza yaani kumsifu Luka 11:1-2 “Ikawa alipokuwa mahali fulani akiomba, alipokwisha, mmoja katika wanafunzi wake alimwambia, Bwana, tufundishe sisi kusali, kama vile Yohana alivyowafundisha wanafunzi wake. Akawaambia, Msalipo, semeni, Baba [yetu uliye mbinguni], Jina lako litakaswe, Ufalme wako uje, [Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.] Kusifu ni mlango au ufunguo wa kuingilia katika nyua yaani katika ukumbi wa Mungu kwaajili ya kupokea huduma na majibu ya mahitaji yetu Zaburi 100:1-5 “Mfanyieni Bwana shangwe, dunia yote; Mtumikieni Bwana kwa furaha; Njoni mbele zake kwa kuimba; Jueni kwamba Bwana ndiye Mungu; Ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake; Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake. Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru; Nyuani mwake kwa kusifu; Mshukuruni, lihimidini jina lake; Kwa kuwa Bwana ndiye mwema; Rehema zake ni za milele; Na uaminifu wake vizazi na vizazi.” Kwa hiyo tunapoenda mbele za Mungu kwa ibada ya aina yoyote ile ikiwa ni pamoja na maombi ni muhimu kuanza na kusifu kwa sababu sifa kwa Mungu inafungua mambo mengi na kumfanya Bwana atujali, na kutusikiliza, Zaburi 29:1-2 “Mpeni Bwana, enyi wana wa Mungu, Mpeni Bwana utukufu na nguvu; Mpeni Bwana utukufu wa jina lake; Mwabuduni Bwana kwa uzuri wa utakatifu.” Kwa nini maandiko yaaagiza kuanza ibada au maombi kwa kumsifu Mungu? Ziko sababu kadhaa wa kadhaaa:-

 

1.       Kusifu kunaandaa mioyo yetu kumwangalia Mungu huku tukiwa tunatambua sifa zake, tunapoaishwa kupelekwa kwenye uwepo wake na kutusaidia kuelewa ukuu wake pale tunapomuendea  lakini sio hivyo tu sifa zina tabia ya kuufanya uwepo wa Mungu kushuka na kutuhudumia 2Nyakati 5:13 “tena Walawi waimbaji, wote pia, yaani Asafu, na Hemani, na Yeduthuni, na wana wao, na ndugu zao, hali wamevaa kitani safi, wenye matoazi na vinanda na vinubi, wamesimama upande wa mashariki wa madhabahu, na pamoja nao makuhani mia na ishirini wakipiga panda;) hata ikawa, wenye panda na waimbaji walipokuwa kama mmoja, wakisikizisha sauti moja ya kumsifu na kumshukuru Bwana nao wakipaza sauti pamoja na panda na matoazi na vinanda, wakimsifu Bwana, wakisema, Kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake ni za milele; ndipo nyumba ikajawa na wingu, naam, nyumba ya Bwana,hata makuhani hawakuweza kusimama ili kufanya huduma yao, kwa sababu ya lile wingu; kwa kuwa nyumba ya Mungu imejaa utukufu wa Bwana.” Kumbuka ya kuwa Mungu anakaa katikati ya sifa Zaburi 22:3 -5 “Na Wewe U Mtakatifu, Uketiye juu ya sifa za Israeli.Baba zetu walikutumaini Wewe, Walitumaini, na Wewe ukawaokoa.Walikulilia Wewe wakaokoka, Walikutumaini wasiaibike.”

2.       Kusifu kunaharibu vifungo vya adui Kila kitu ambacho kinakandamiza maisha ya mwanadamu na kututishia katika uonevu wa aina yoyote ile kimwili na hata kiroho vinaweza kutiishwa na kuharibiwa kupitia Maombi Matendo 16:23-26 “Na walipokwisha kuwapiga mapigo mengi, wakawatupa gerezani, wakamwamuru mlinzi wa gereza awalinde sana. Naye akiisha kupata amri hii akawatupa katika chumba cha ndani, akawafunga miguu kwa mkatale. Lakini panapo usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za kumsifu, na wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza. Ghafula pakawa tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisika, na mara hiyo milango ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa.”

3.       Kusifu na kuabudu kunamfanya adui achanganyikiwe na kupoteana, Hakuna silaha ya ajabu kama kumsifu Mungu na kumuabudu, silaha hii ni ya kipekee inapotumika katika tishio la kivita au uonevu Bila kujali kuwa jeshi lililojipanga ni kubwa kwa kiwango gani kumsifu Mungu kutatuletea ushindi wa kushangaza sana angalia 2Nyakati 20:1-4 “Ikawa baadaye, wana wa Moabu, na wana wa Amoni, na pamoja nao baadhi ya Wameuni, wakaja juu ya Yehoshafati vitani.Wakaja watu waliomwambia Yehoshafati, wakisema, Wanakuja jamii kubwa juu yako watokao Shamu toka ng'ambo ya bahari; na tazama, wako katika Hasason-tamari (ndio En-gedi).Yehoshafati akaogopa, akauelekeza uso wake amtafute Bwana; akatangaza mbiu ya watu kufunga katika Yuda yote.Yuda wakakusanyika pamoja ili wamtafute Bwana; hata kutoka miji yote ya Yuda wakaja kumtafuta Bwana.” Wakati majeshi ya wana wa Moabu na wana wa Amoni na Wameuni walipokuwa wameungana kinyume na mfalme Yeshoshafati, unaweza kuona pamoja na silaha yote ya kufunga na kumuomba Mungu safari hii maelekezo ya Mungu namna ya kupigana na kupata ushindi ilikuwa ni kupanga waimbaji ili wamsifu Mungu ona 2Nyakati 20:14-26 “Ndipo Yahazieli mwana wa Zekaria, mwana wa Benaya, mwana wa Yeieli, mwana wa Matania, Mlawi, wa wana wa Asafu, akajiliwa na roho ya Bwana, katikati ya kusanyiko; akasema, Sikieni, Yuda wote, nanyi mkaao Yerusalemu, na wewe mfalme Yehoshafati; Bwana awaambia hivi, Msiogope, wala msifadhaike kwa ajili ya jeshi kubwa hili; kwani vita si yenu bali ni ya Mungu. Kesho shukeni juu yao; tazameni, wanakwea kwa kupandia Sisi; nanyi mtawapata penye mwisho wa bonde, mbele ya jangwa la Yerueli. Hamtahitaji kupigana vita, jipangeni, simameni, mkauone wokovu wa Bwana ulio pamoja nanyi, enyi Yuda na Yerusalemu; msiogope, wala msifadhaike; kesho tokeni juu yao; kwa kuwa Bwana yu pamoja nanyi. Yehoshafati akainama kichwa, kifulifuli; wakaanguka mbele za Bwana Yuda wote na wakaao Yerusalemu, wakimsujudia Bwana. Na Walawi, wa wana wa Wakohathi na wa wana wa Wakorahi, wakasimama ili wamsifu Bwana, Mungu wa Israeli, kwa sauti kuu sana. Wakaamka asubuhi na mapema, wakaenda nje katika jangwa la Tekoa; nao walipokuwa wakitoka, Yehoshafati akasimama, akasema, Nisikieni, enyi Yuda nanyi wenyeji wa Yerusalemu; mwaminini Bwana, Mungu wenu, ndivyo mtakavyothibitika; waaminini manabii wake, ndivyo mtakavyofanikiwa. Naye alipokwisha kufanya shauri na watu, akawaweka wale watakaomwimbia Bwana, na kumsifu katika uzuri wa utakatifu, wakitoka mbele ya jeshi, na kusema, Mshukuruni Bwana; kwa maana fadhili zake ni za milele. Nao walipoanza kuimba na kusifu, Bwana akaweka waviziao juu ya wana wa Amoni, na Moabu, na wa mlima Seiri, waliokuja juu ya Yuda; nao wakapigwa. Kwani wana wa Amoni na wa Moabu waliwaondokea wenyeji wa mlima Seiri kuwaulia mbali na kuwaharibu; nao walipokwisha kuwakomesha hao wakaao Seiri, wakajitia kuharibu kila mtu mwenziwe. Hata Yuda walipofika mnara wa kulindia wa jangwani, wakalitazama hilo jeshi; nao, angalia, walikuwa maiti walioanguka nchi, wala hapana aliyeokoka. Nao Yehoshafati na watu wake walipokuja kuchukua nyara zao, wakaona kati yao wingi wa mali, na mavazi, na johari za thamani, walivyojivulia, zaidi kuliko wawezavyo kuchukua; wakawa siku tatu katika kuteka nyara, maana zilikuwa nyingi sana.Hata siku ya nne wakakusanyika katika bonde la Baraka; maana ndipo walipombarikia Bwana; kwa hiyo jina lake mahali pale pakaitwa Bonde la Baraka hata leo.”

Unaona kumbe hatupaswi kuwa na hofu iko njia nyepesi sana na silaha nzito ya kutukomboa nayo ni kumsifu Mungu, hii ni silaha kuu ya kiroho hatupaswi kwa namna yoyote kudhani au kufikiri kuwa wakati wa kumsifu Mungu ni wakati wa mzaha hapana ni wakati ambapo Mungu yuko kazini hivyo hatuna budi kumaanisha linapokuja swala la kumsifu Mungu Zaburi 8:2 “Vinywani mwa watoto wachanga na wanyonyao Umeiweka misingi ya nguvu; Kwa sababu yao wanaoshindana nawe; Uwakomeshe adui na mijilipiza kisasi.”  Watu wanapomsifu Mungu hata kama ni watoto kunakuwa na misingi ya nguvu na kukomesha adui na kujilipizia kisasi wote wanaoshindana nasi watatupwa nje kama tutagundua siri iliyoko katika sifa, kusifu kunatoa nguvu na kibali cha kuwafanyika hukumu dhidi ya adui zetu na wafalme wao Zaburi 149:5-9 “Watauwa na waushangilie utukufu, Waimbe kwa sauti kuu vitandani mwao. Sifa kuu za Mungu na ziwe vinywani mwao, Na upanga mkali kuwili mikononi mwao. Ili kufanya kisasi juu ya mataifa, Na adhabu juu ya kabila za watu. Wawafunge wafalme wao kwa minyororo, Na wakuu wao kwa pingu za chuma. Kuwafanyia hukumu iliyoandikwa; Hiyo ndiyo heshima ya watauwa wake wote. Haleluya.”               

 

Unaona kwa msingi huo hatuna budi wakati wote kukumbuka ya kuwa kumsifu Mungu ni silaha yenye nguvu kubwa na ya ajabu sana inayoweza kusukuma nyuma majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho na mwili pia, kumsifu Mungu na kumtukuza hutufanya na kuyanoa mawazo yetu ili yaweze kumuelekea Mungu na kutambua ukuu wake na uweza wake kila siku kama ikiwezekana tuwe na Muda wa kumtukuza Mungu na kumsifu Biblia imeeleza hata vitandani mwetu, unapopita katika wakati Mgumu acha kuogopa mwamini Mungu na hakikisha kuwa unamuelekea yeye na wakati mwingine jaribu tu kumsifu na utaweza kuona Mungu atakuweka huru! Hakuna Jeshi la aina yoyote litakaloweza kushindana nawe kama wewe ni mtu uliyejaa sifa kwa Mungu, Kumsifu Mungu namna hii ndio siri ya ushindi wa Daudi katika maisha yake yote yeye alikuwa mtu aliyejaa zaburi za sifa na hivyo hakuwahi kushindwa vita ya aina yoyote!

 

Zaburi 27:1-6 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini. Neno Moja nimelitaka kwa Bwana, Nalo ndilo nitakalolitafuta, Nikae nyumbani mwa Bwana Siku zote za maisha yangu, Niutazame uzuri wa Bwana, Na kutafakari hekaluni mwake. Mradi atanisitiri bandani mwake siku ya mabaya, Atanisitiri katika sitara ya hema yake, Na kuniinua juu ya mwamba. Na sasa kichwa changu kitainuka Juu ya adui zangu wanaonizunguka. Nami nitatoa dhabihu za shangwe hemani mwake; Nitaimba, naam, nitamhimidi Bwana.”

 

5.       Omba upako wa Roho Mtakatifu.

 

Roho Mtakatifu ni moja ya mwanachama muhimu katika utatu wa Mungu anajihusisha sana na maeneo mengi ya ukombozi wetu, yeye ni chanzo cha ushuhuda na ufunuo, anatuongoza katika maamuzi ya kiulinzi kimwili na kiroho ili tusiiingie hatarini,  yeye ni mfariji pia na hivyo anauwezo wa kutusaidia na kutupa tumaini, Katika nyakati za agano la kale popote pale ambapo palitokea uonevu na ukahitajika msaada wa kiungu basi Roho wa Mungu alikuja kwa nguvu juu ya mmoja wapo ya waamuzi au mfalme na mfalme huyo akawaweka watu huru,  uhuru huu ulitokana na upako wa Roho Mtakatifu, tunaambiwa kuwa Upako unavunja nira  ona Isaya 10:27Tena itakuwa katika siku hiyo mzigo wake utaondoka begani mwako, na nira yake shingoni mwako, nayo nira itaharibiwa, kwa sababu ya kutiwa mafuta.” Maandiko yanaonyesha kuwa Upako yaani mafuta ya Roho Mtakatifu huwa yanafanya kazi ya kuondoa uonevu, Ni kazi ya Roho Mtakatifu kuwatia mafuta watumishi wake ili wafanye kazi ya kuwatoa watu kutoka katika uonevu wa namna mbalimbali ona Luka 4:18-19 “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.” Unaona mafuta yaliyokuwa juu ya Yesu kutokana na Roho Mtakatifu yalifanya kazi mbalimbali ya kuwafungua watu walioonewa na kukandamizwa na shetani, sio hivyo tu lakini na kuwaponya na kuwaweka huru, tunaweza kusoma pia katika Matendo 10:38 “habari za Yesu wa Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa Roho Mtakatifu na nguvu naye akazunguka huko na huko, akitenda kazi njema na kuponya wote walioonewa na Ibilisi; kwa maana Mungu alikuwa pamoja naye.”

 

Nyakati za agano la kale hususani kipindi cha waamuzi na wafalme Mungu Roho Mtakatifu aliwawezesha wakati wote kufanya matendo ya ukombozi baada ya yeye kuja juu ya watumishi wake na kuwatia nguvu iliyowawezesha kuwasaidia ndugu zao wasikandamizwe au waliokuwa wanakandamizwa na maadui na kuwakimbiza adui zao ona maeneo mblimbali:-

 

Waamuzi 3:9-11 “Kisha wana wa Israeli walipomlingana Bwana, Bwana akawainulia wana wa Israeli mwokozi, aliyewaokoa, yaani, Othnieli mwana wa Kenazi, ndugu mdogo wa Kalebu. Roho ya Bwana ikamjilia juu yake, naye akawa mwamuzi wa Israeli; akatoka kwenenda vitani, naye Bwana akamtia huyo Kushan-rishathaimu, mfalme wa Mesopotamia, mkononi mwake; na mkono wake ukamshinda Kushan-rishathaimu. Nayo nchi ikawa na amani muda wa miaka arobaini. Kisha Othnieli, mwana wa Kenazi, akafa.”

 

Waamuzi 13:24-25 “Basi yule mwanamke akamzaa mtoto mwanamume akamwita jina lake Samsoni, mtoto huyu akakua, Bwana akambarikia. Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha katika Mahane-dani, katikati ya Sora na Eshtaoli.”

 

Waamuzi 14:19 “Roho ya Bwana ikamjilia juu yake kwa nguvu, naye akatelemkia Ashkeloni, akapiga watu waume thelathini katika watu hao, na kuzitwaa nyara zao, na kuwapa hao waliokitambua kitendawili mavao hayo. Hasira zake zikamwaka, naye akakwea kwenda nyumbani kwa baba yake.”     

 

Waamuzi 11:28-29. “Lakini mfalme wa wana wa Amoni hakuyasikiza hayo maneno ya Yeftha aliompelekea. Ndipo roho ya Bwana ikamjilia juu yake Yeftha, naye akapita katika Gileadi na Manase, akapita na katika Mispa ya Gileadi, na kutoka hapo Mispa ya Gileadi akapita kuwaendea wana wa Amoni.”

 

Unaona popote pale waaamuzi walipowasaidia watu ili kuwaletea ukombozi utaweza kuona Roho Mtakatifu alikuja juu yao kwanza, Ni Roho huyu huyu Mtakatifu aliyeyainua maisha ya waamuzi ili kuwatetea watu wake dhidi ya migandamizo ya aina mbalimbali anaweza kwa uhalisia kutuwezesha na sisi kuondoka katika migandamizo ya aina mbalimbali, ni mfariji, ni kiongozi kwa awaye yote anayemtegemea atakuonyesha yakupasayo kufanya na kukupa mbinu unazozihitaji,  kila mtu anahitaji, kuwa na maono, hekima, ujasiri na kukabiliana na changamoto za aina mbalimbali unapotaka kulitumikia shauri la Bwana au kutimiza kusudi lake duniani, utakuwa kwenye nafasi nzuri ya kutimiza hilo kama utamruhusu Roho Mtakatifu akutie nguvu, unapojaribu kuongoza bila Roho Mtakatifu utaanguka lakini ili uweze kufanikiwa tunamuhitaji Roho wa Mungu. Matendo 11:22-24 “Habari hizo za watu hao zikafika masikioni mwa kanisa lililokuwako katika Yerusalemu; wakamtuma Barnaba, aende hata Antiokia. Naye, alipokwisha kufika na kuiona neema ya Mungu akafurahi, akawasihi wote waambatane na Bwana kwa kusudi la moyo. Maana alikuwa mtu mwema amejaa Roho Mtakatifu na imani; watu wengi wakaongezeka upande wa Bwana.”

 

6.       Mkemee shetani na majeshi yake yote.

 

Katika maombi yetu ni muhimu kukumbuka kuwa na maombi ya kufanya vita dhidi ya ibilisi, kumshughulikia shetani na majeshi yake na maajenti wake wote ni wajibu pekee tuliopewa na Mungu sio ombi ni amri ona, Mfumo wa kishetani uko katika protokali za kijeshi, hivyo Ndivyo Mungu alivyowaumba, Mungu anaitwa Bwana wa Majeshi, Yeye ndio Amiri Jeshi mkuu ana serikali na ana dola Mbinguni, Malaika waliumbwa kama vyombo vya Dola, hii ikiwa ni pamoja na Malaika walioasi baadaye yaani majeshi ya Pepo wabaya katika ulimwengu war oho, kwa msingi huo wao husikiliza amri na mari haitolewi kama ombi inatolewa kwa mamlaka kwa kuamuru kupitia mairi Jeshi mkuu wa Majeshi ya Bwana yaani Kristo ona Waefeso 6:10-13 “Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake.Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.”

 

Kwa msingi huo unaweza kugundua kuwa shetani na serikali zake wako katika mfumo wa kijeshi na ndio maana Yesu aliamuru tumshughulikie alitupa amri sio ombi la kumshughulikia shetani angalia mfumo wa lugha inayotumika  katika     

 

Luka 10:17-19 “Ndipo wale sabini waliporudi kwa furaha, wakisema, Bwana, hata pepo wanatutii kwa jina lako. Akawaambia, Nilimwona Shetani, akianguka kutoka mbinguni kama umeme. Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu kitakachowadhuru.”

 

Maandiko wakati wote yanaonyesha lugha ya kupinga na kukemea linapokuja swala la maombi yetu dhidi ya kushughulikia kazi za shetani, wakati wote maombi ya kimapambano dhidi ya ibilisi ni kukemea ni kupigana vita ona maagizo ya kimaandiko:-

 

2Wakoritho 10:3-5 “Maana ingawa tunaenenda katika mwili, hatufanyi vita kwa jinsi ya mwili; (maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome;) tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo; tena tukiwa tayari kupatiliza maasi yote, kutii kwenu kutakapotimia

 

1Petro 5: 8-9 “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.”

 

Yakobo 4:7-8 “Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili. 

 

Zekaria 3:2 “Bwana akamwambia Shetani, Bwana na akukemee Ewe Shetani; naam, Bwana, aliyechagua Yerusalemu, na akukemee; je! Hiki si kinga kilichotolewa motoni?

 

Yuda 1:9 “Lakini Mikaeli, malaika mkuu, aliposhindana na Ibilisi, na kuhojiana naye kwa ajili ya mwili wa Musa, hakuthubutu kumshitaki kwa kumlaumu, bali alisema, Bwana na akukemee.”

 

Kwa kuwa shetani anataka kuwakandamiza watu wetu, sisi wenyewe,familia zetu na hata taifa letu linapokuja swala la kumtaka aachie huwa ni amri kali, achiaa, toka, nakuamuru, bwana na akukemee na kadhalika hakuna lugha laini wakati wa kumkemea shetani, ni kumuamuru aachie haraka na taaachialia

 

7.       Vunja madhabahu za uovu

 

Ni muhimu kufahamu kuwa mawasiliano yote ya kiroho kati ya Mungu na wanadamu au miungu na wanadamu hufanyika kupitia madhabahu, kwa msingi huo Mungu aliwaagiza wana wa Israel watakapoingia katika inchi ya kanaani moja ya jambo muhimu wanalopaswa kulifanya ni kuzivunja madhabahu zao agizo hili la kuharibu madhabau za uovu limerudiwa tena na tena katika maandiko ona Kutoka 34:12-13 “Ujihadhari nafsi yako, usije ukafanya agano na wenyeji wa nchi ile unayoiendea, lisiwe mtego katikati yako. Bali utabomoa madhabahu zao, na kuvunja-vunja nguzo zao, na kuyakata-kata maashera yaoUnaona unaweza kuona tena Kumbukumbu la torati 7:1-7 “Bwana, Mungu wako, atakapokutia katika nchi uendayo kuimiliki, atakapoyang'oa mataifa mengi watoke mbele yako, Mhiti, na Mgirgashi, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi, mataifa saba makubwa yenye nguvu kukupita wewe; wakati Bwana, Mungu wako, atakapowatoa mbele yako, nawe utawapiga; wakati huo ndipo uwaondoe kabisa; usifanye agano nao, wala kuwahurumia; wala usioane nao;binti yako usimpe mwanawe mume, wala usimtwalie mwanao mume binti yake.Kwa kuwa atamkengeusha mwanao mume asinifuate, ili wapate kuabudu miungu mingine; ndipo itakapowaka hasira ya Bwana juu yenu, naye atakuangamiza upesi. Lakini watendeni hivi; zivunjeni madhabahu zao zibomosheni nguzo zao, yakateni maashera yao, ziteketezeni kwa moto sanamu zao za kuchonga. Kwa maana wewe u taifa takatifu kwa Bwana, Mungu wako; Bwana Mungu wako, amekuchagua kuwa watu wake hasa, zaidi ya mataifa yote walioko juu ya uso wa nchi.”

Kwa nini Mungu aliamuru Madhabau za mataifa yasiyomcha Mungu yaharibiwe? Hii ni kwa sababu madhabahu ndio ni eneo la kutolea sadaka kwa miungu au kwa shetani ndio eneo la mwasiliano kati ya miungu na wanadamu, kwa hiyo madhabahu ndizo zinaziotumika kufanya mawasiliano ya kipepo na kufanya uchawi, kutengeneza hirizi, kupokea maelekezo ya kipepo, kufanya uaguzi, kufanya utambuzi kwa ramli  na mawasiliano yote kati ya miungu na wanadamu hufanyika kupitia madhabahu, ni madhabahu ndio zinazotumika kuwafunga watu na kuwaweka katika mahusiano ya kipepo na kusababisha mikandamizo, watu wanapotaka kukutana na ulimwengu wa kiroho basi pale wanapokutania kwa ibada ndio maagano ya kipepo yanapofanyika au mahusiano na mapepo ndipo yanapofanyika na ndipo maisha ya watu wengi yanapoharibiwa

 

2Wafalme 3:26-27 “Naye mfalme wa Moabu alipoona ya kwamba ameshindwa vitani, alitwaa pamoja naye watu mia saba wenye kufuta panga ili wapenye hata kwa mfalme wa Edomu; wala hawakudiriki. Ndipo akamtwaa mwanawe wa kwanza, yeye ambaye angetawala mahali pake, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa juu ya ukuta. Kukawa hasira kuu juu ya Israeli; basi wakatoka kwake, wakarudi kwenda nchi yao wenyewe.”               

 

Balaamu alipokodiwa kuja kuwalaani Israel utaweza kuona jambo la kwanza kulifanya ni kutengeneza madhabahu unaweza kuona Hesabu 23:1-5 “Balaamu akamwambia Balaki, Nijengee hapa madhabahu saba, ukaniandalie hapa ng'ombe waume saba, na kondoo waume saba.Balaki akafanya kama Balaamu alivyonena. Balaki na Balaamu wakatoa sadaka, ng'ombe mume mmoja na kondoo mume mmoja juu ya kila madhabahu. Balaamu akamwambia Balaki, Simama karibu na sadaka yako, nami nitakwenda, labda Bwana atakuja kuonana nami; na lo lote atakalonionyesha nitakuambia. Akaenda hata mahali peupe juu ya kilima. Mungu akakutana na Balaamu; naye Balaamu akamwambia, Nimetengeneza madhabahu saba, nami nimetoa sadaka ng'ombe mume mmoja na kondoo mume mmoja juu ya kila madhabahu. Bwana akatia neno katika kinywa chake Balaamu, akasema, Umrudie Balaki; ukaseme maneno haya.”

 

Kabla ya Mungu kumtumia Gideoni kama Mwamuzi wa Israel kwa uwezo wake Gideoni alipoisikia msauti ya Mungu aliye hai aliamua kuivinja kwanza Madhabahu ya baba yake ona Waamuzi 6:24-32 “Ndipo Gideoni akamjengea Bwana madhabahu hapo, akaiita jina lake, Yehova-Shalomu; hata hivi leo iko huko katika Ofra ya Waabiezeri. Ikawa usiku uo huo Bwana akamwambia, Mtwae ng'ombe wa baba yako, yaani ng'ombe wa pili, wa miaka saba, ukaiangushe madhabahu ya Baali, aliyo nayo baba yako, ukaikate Ashera ile iliyo karibu nayo; ukamjengee Bwana, Mungu wako, madhabahu juu ya ngome hii, kwa taratibu zake; ukamtwae yule ng'ombe wa pili na kumtoa awe sadaka ya kuteketezwa, kwa kuni za ile Ashera uliyoikata. Ndipo Gideoni akatwaa watu kumi miongoni mwa watumishi wake, akafanya kama Bwana alivyomwambia; lakini ikawa kwa sababu aliwaogopa watu wa nyumba ya baba yake, na watu wa mji, hakuweza kuyatenda hayo wakati wa mchana, basi aliyatenda usiku. Hata watu wa mji walipoondoka asubuhi na mapema, tazama, madhabahu ya Baali imebomolewa, na ile Ashera iliyokuwa karibu nayo imekatwa, na yule ng'ombe wa pili ametolewa sadaka juu ya ile madhabahu iliyojengwa. Wakaambiana, Ni nani aliyetenda jambo hili? Hata walipotafuta habari na kuuliza, wakasema, Gideoni, mwana wa Yoashi, ndiye aliyetenda jambo hili. Ndipo watu wa mji wakamwambia Yoashi Mlete mwanao, afe; kwa sababu ameibomoa madhabahu ya Baali na kwa sababu ameikata ile Ashera iliyokuwa karibu nayo. Yoashi akawaambia watu wote waliokuwa wakishindana naye, Je! Mtamtetea Baali? Au mtamwokoa ninyi? Yeye atakayemtetea na auawe hivi asubuhi; kama yeye ni Mungu, na ajitetee nafsi yake, kwa sababu mtu mmoja ameibomoa madhabahu yake. Basi akamwita Yerubaali siku hiyo, akisema, Baali na atete naye kwa ajili ya nafsi yake, kwa sababu ameibomoa madhabahu yake.”        

 

Unaona kwa sababu hiyo ni lazima tunapotaka ukombozi kutoka katika maeneo mbalimbali ya maisha yetu hatuna budi kuharibu kila njia za mawasiliano ya kishetani kwani hizo ndio madhabahu zenyewe, haribu, hirizi, pembe au vyungu, vimbo au vifaa vyote vya kiroho ambavyo umepewa na waganga au ambavyo vimezindikwa nyumbani kwenu, kumbuka kuwa Madhabahu ndio njia ya mawasiliano, na ikiwa madhabahu hiyo sio ya kiungu, basi itapingana na sheria za kiungu, za Mungu aliye hai, madhabahu ya miungu migeni itazuia neema ya Mungu wetu kwetu, itaweka mipaka ya utendaji wa kiungu kwetu, itafungua milango ya roho chafu, itasababisha matatizo yasiyoweza kupata ufumbuzi, itachelewesha sana upatikananaji wa Baraka zako, itasababisha matatizo yasiyoisha, inaweza kushababisha talaka, umasikini, kurudi nyuma, utasa, vifo, aibu  na mambo ya ajabu ajabu, madhabahu zina uwezo wa kusababisha laana au Baraka, Madhabahu ni ukumbusho kwa wale walioziinua, ili uweze kupata upenyo katika maisha yako ni lazima uziharibu madhabahu zisizo rasmi na makuhani wake, Madhabahu hugeuka na kuwa njia (Malango) ya kuvutia viumbe wa kiroho kufanya utembeleo aidha awe Mungu au miungu yaani mapepo

 

Mathayo 16:18 . “Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda.”

 

Mwanzo 28:11-19 “Akafika mahali fulani akakaa huko usiku kucha, maana jua lilikuwa limekuchwa; akatwaa jiwe moja la mahali pale akaliweka chini ya kichwa chake, akalala usingizi pale pale.Akaota ndoto; na tazama, ngazi imesimamishwa juu ya nchi, na ncha yake yafika mbinguni. Tena, tazama, malaika wa Mungu wanapanda, na kushuka juu yake. Na tazama, BWANA amesimama juu yake, akasema, Mimi ni BWANA, Mungu wa Ibrahimu baba yako, na Mungu wa Isaka; nchi hii uilalayo nitakupa wewe na uzao wako. Na uzao wako utakuwa kama mavumbi ya nchi, nawe utaenea upande wa magharibi, na mashariki, na kaskazini, na kusini; na katika wewe, na katika uzao wako, jamaa zote za dunia watabarikiwa. Na tazama, mimi nipo pamoja nawe, nitakulinda kila uendako, nami nitakuleta tena mpaka nchi hii, kwa maana sitakuacha, hata nitakapokufanyia hayo niliyokuambia. Yakobo akaamka katika usingizi wake, akasema, Kweli BWANA yupo mahali hapa, wala mimi sikujua. Naye akaogopa akasema, Mahali hapa panatisha kama nini! Bila shaka, hapa ni nyumba ya Mungu, napo ndipo lango la mbinguni. Yakobo akaondoka asubuhi na mapema, akalitwaa lile jiwe aliloliweka chini ya kichwa chake, akalisimamisha kama nguzo, na kumimina mafuta juu yake. Akaita jina la mahali pale Betheli; lakini jina la mji ule hapo kwanza uliitwa Luzu.”

 

Unaona kwa msingi huo hatuna budi kuhakikisha kuwa tunaharibu kila aina ya madhabahu ambayo iko kinyume na Mungu wetu ili kuzuia sisi kuwa chini ya utumwa wa miungu mingine kama haya yakifanyika vema basi Ibilisi atatii na kukuacha uende, waachie watu wangu waende, Wakati wote unapotaka Mungu awe pamoja nawe na kukukomboa unapotaka mpenyo katika maisha yako na unapotaka Mungu atembee nawe ni lazima kuhakikisha kuwa njia zote za mawasiliano na miungu migeni zinahabiwa na kutupwa mbali ili Mungu atembee katikati yako na familia yako haribu miungu migeni iondoe katika nyumba yako ichome moto ifukie baki na Mungu akiye hai na uwepo wa Mungu utakuwa pamoja nawe na hakuna wa kukuonea utaogopwa kila utakakopita

 

Waefeso 19:19 “Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu.”  

 

Mwanzo 35:1-5 “Mungu akamwambia Yakobo, Ondoka, panda uende Betheli, ukakae huko; ukamfanyie Mungu madhabahu huko; yeye aliyekutokea ulipomkimbia Esau, ndugu yako. Yakobo akawaambia watu wa nyumbani mwake, na wote waliokuwa pamoja naye, Ondoeni miungu migeni iliyoko kwenu, mjisafishe mkabadili nguo zenu.Tuondoke, tupande kwenda Betheli, nami nitamfanyia Mungu madhabahu huko; yeye aliyenisikia siku ya shida yangu, akawa pamoja nami katika njia yote niliyoiendea. Nao wakampa Yakobo miungu migeni yote iliyokuwa mikononi mwao, na pete zilizokuwa masikioni mwao, naye Yakobo akazificha chini ya mwaloni ulioko Shekemu. Wakashika njia, hofu ya Mungu ikaishika miji iliyowazunguka, wala hawakuwafuata wana wa Yakobo.”

 

Imani yangu ni kuwa somo hili ukilifanyia kazi na kuweka yote niliyokufundisha kivitendo utashangaa kwa miujiza ya ajabu na mpenyo wa ajabu utakaoambatana na maisha yako kuanzia leo namuomba Mungu kwamba uongezewe neema unapoadhimisha siri za ukombozi wako kupitia somo hili katika jina la Yesu Kristo  wa Nazareth Mwana wa Mungu aliye hai amen.

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima