Jumapili, 18 Februari 2024

Neema ya Mungu na mwaliko wa maadui!


Mwanzo 26:12-16 “Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi.”


 

 

Naliweka wakfu somo hili kwa heshima ya Hayati Edward Ngoyai Lowassa waziri mkuu wa zamani wa Tanzania kwani somo hili liliandaliwa siku ambayo yeye alikuwa anazikwa.

 

Utangulizi:

Ni Muhimu kufahamu kuwa wakati mwingine vita na mapito tunayoyapitia kutoka kwa watu yanatokana na neema ya Mungu iliyoko juu yetu, Mungu anapokupa kibali na baraka mbalimbali Baraka hizo au neema hiyo hualika maadui!

Wakati Isaka alipokaa Gerari kwa sababu ya njaa iliyotokea mashariki ya kati, kwa agizo la Mungu, Mungu alimbariki sana Isaka, Mazao yake na mifugo yake iliongezeka sana kiasi ambacho wafilisti walijawa na wivu wenye uchungu!

Maandiko yanaeleza wazi kwamba wafilisti wakamhusudu! Neno Kuhusudu linalotumika hapo katika kiebrania linatumika neno Qana  mbalo maana yake ni Jealous au Zealous in a bad sense kiswahili fasaha wivu wenye uchungu  

Yakobo 3:14-16 “Lakini, mkiwa na wivu wenye uchungu na ugomvi mioyoni mwenu, msijisifu, wala msiseme uongo juu ya kweli. Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani. Maana hapo palipo wivu na ugomvi ndipo palipo machafuko, na kila tendo baya.”

Kwaajili ya wivu wenye uchungu, waliharibu visima alivyokuwa anatumia Isaka, Visima hivi vilichimbwa na Ibrahimu baba yake miaka ya uhai wake, na visima hivi vilikuwa ndio chanzo cha mfumo wa umwagiliaji na unyweshaji wa mifugo, na pasipo visima hivyo ni ngumu kuendesha shughuli za kilimo na ufugaji hususani wakati wa ukame, kwa hiyo wafilisti walikusudia kumuharibu Isaka na walikusudia kuharibi kabisa vyanzo vya Baraka zake, na walipoona majaribio yao yanashindikana mwisho wakamwambia atoke kwao, na bila aibu walimweleza sababu kwanini aende

Mwanzo 26:16 “Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisikwa nini walifanya hivyo Neema ya Mungu ilikuwa juu ya Isaka, alibarikiwa sana Mungu alimpa akili ya kupata utajiri, familia yao walikuwa na ujuzi wa elimu ya umwagiliaji, na ujuzi wa kuchimba visima hata kujua sehemu zenye maji, Jambo hili liliwapelekea Wafilisti kujawa na wivu wenye uchungu kwaajili ya maisha ya Isaka,  Neema ya Mungu inapokuwa juu yako na akaweka mkono wake kukubariki, ukawa na Nguvu, ukawa na bidii ya kazi, ukawa na fedha, ukawa na ndoa nzuri, ukawa na watoto wenye mafanikio, ukawa na afya nzuri ukastawi pande zote, ukawa na ustawi wa mwili nafsi na roho, hata hali yako ya kiroho ikiwa vizuri, Shetani na majeshi yake ya pepo wabaya pamoja na watu wabaya wataanza kukuonea wivu wenye uchungu, watu wataanza kukuchukia pasipo sababu , kwanini kwa sababu ya neema ya Mungu iliyo juu yako inayokuletea Baraka !

Kwa hiyo ni Lazima uelewe kama wewe ni mtu mkubwa ndani, Mungu ameweka mkono wake juu yako, Mungu amekupa kibali, na Baraka zake zikaanza kumiminika juu yako, Adui hatalala usingizi, hataketi na kukuacha ufurahie Baraka za Mungu kwa Amani, ataanza kuchochea shida na taabu. Leo basi tutachukua muda kujifunza somo hili Neema ya Mungu na Mwaliko wa Maadui kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

 

·         Mifano ya watu waliopata Neema ya Mungu na kusababisha kuwa na Maadui

·         Neema ya Mungu na mwaliko wa maadui

·         Ushauri kutoka kwa Mungu  

 

Mifano ya watu waliopata Neema ya Mungu na kusababisha kuwa na Maadui

Neno la Mungu limejaa mifano ya watu waliopewa neema ya Mungu katika maisha yao na badala ya kupendwa na watu, watu waliwachukia na kuwawashia moto, na kuwategea mitego ya aina mbalimbali kuhakikisha kuwa wanakwama katika kila eneo la Maisha yao na ikiwezekana vyanzo vya Baraka zao kuharibiwa!

1.       Alichukiwa kwa sababu ya ndoto kubwa na maono makubwa aliyokuwa nayo – Yusufu angalia katika Mwanzo 37:2-11 “Hivi ndivyo vizazi vya Yakobo. Yusufu, aliyekuwa mwenye miaka kumi na saba, alikuwa akichunga kondoo pamoja na ndugu zake; naye alikuwa kijana pamoja na wana wa Bilha, na wana wa Zilpa, wake wa baba yake. Yusufu akamletea baba yao habari zao mbaya. Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani. Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”

 

Yusufu alipata neema kutoka kwa Mungu, neema hii ilimfanya apate upendeleo kutoka kwa baba yake, lakini nduguze walimchukia sana na Mungu akasema na Yusufu kwa habari ya Maisha yake ya baadaye kwa njia ya Ndoto, Jambo hili lilipelekea nduguze wamchukie zaidi na hata baadaye walikusudia kumuua,  kumbuka hapo Ndoto zilikuwa hazijatimia, lilikuwa ni ujumbe tu kutoka kwa Mungu, watu wenye maono makubwa huchukiwa, Kimsingi kupitia kisa hiki wako watu wanasema usimweleze mtu maono yako eti ufiche, kutokana na kisa hiki, Lakini, Mungu hanaga tabia ya kuficha maono yake, huwa anaweka wazi, serikali huwa haifichi mipango yake huwa inawekwa wazi, vyama huwa havifichi sera zake huwa wanazinadi, kuficha maono ni woga, Mipango ya Mungu ya kumuokoa mwanadamu, kuja kwa masihi iliwekwa wazi zamani sana Mungu mwenyewe aliiweka wazi, kwa hiyo ukiona mpango umewekwa wazi kisha haukutimia ujue huo haukuwa mpango wa Mungu, Mungu huweka wazi mipango yake na hakuna mtu anayeweza kusimama na kuzuia kusudi lake na ndio maana Ndoto ya Yusufu iliwekwa wazi na Ndugu zake walipigana nayo lakini ilikuja kutimia,.

 

Amosi 3:7 “Hakika Bwana MUNGU hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.”

 

Siri za Mungu huwekwa wazi kwa watumishi wake hata kabla Hazijatimizwa, sijui wanaofundisha ufiche siri zako wana maana gani, wanaogopa vita? wanaogopa maadui,? wanaogopa wachawi?  Mungu hana cha kuogopa yeye anaweka wazi mambo yake na ndivyo alivyofanya kwa Yusufu, Mungu alitangaza atakachomfanyia Yusufu hata kabla havijafanyika ni Mungu Bora anatangaza Mwisho tangu mwanzo !

 

Isaya 46:9-10 “Kumbukeni mambo ya zamani za kale; maana mimi ni Mungu, wala hapana mwingine; mimi ni Mungu, wala hapana aliye kama mimi; nitangazaye mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado; nikisema, Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote

 

Mungu haogopi kutangaza mpango wake, na hakuna anayeweza kuzuia mapenzi yake, yanayoweza kuzuiwa ni mapenzi ya wanadamu tu, lakini ya Mungu hayazuiliki, kusudi la Mungu ni lazima lisimame, kwa hiyo uweke wazi usiweke wazi, Neema ya Mungu ikiwa juu yako ndani yako kukiwa kuna kitu cha ziada ndani yako basi ni lazima kitaalika maadui bila kujali kuwa kimesemwa au hakikusema kitaalika maadui tu na hii ni kwa sababu gani ni kwa sababu ya wivu wenye uchungu! Walionao wanadamu kwa uzito wa maono yako.

 

2.       Alichukiwa kwa sababu ya Upako wa kifalme na uwezo mkubwa aliokuwa nao – Daudi  - angalia katika

1Samuel 18: 6-9 “Hata ikawa, walipokuwa wakienda, hapo Daudi aliporudi baada ya kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka katika miji yote ya Israeli, kwa kuimba na kucheza, ili kumlaki mfalme Sauli; wakatoka na matari, na shangwe, na vinanda. Nao wale wanawake wakaitikiana wakicheza, wakasema, Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake. Basi Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme? Sauli akamwonea Daudi wivu tangu siku ile.”

 

Daudi alikuwa amepakwa mafuta ya ufalme kichwani pake, lakini Muda wake ulikuwa bado haujawadia, hata hivyo uweza wa kifalme ulitenda kazi ndani yake kwa kiwango kikubwa sana alimpiga mfilisti na kujipatia umaarufu mwingi sana  kwa sababu ya upako na uweza wa Mungu uliokuwa juu yake, Angalia kuwa mfalme aliyekuwepo madarakani alianza kumpiga vita, alitaka kumuua mara kadhaa kwa sababu alijua kuwa bila shaka ndiye atakayekuwa mfalme, Mungu anapoweka ukubwa wowote ndani yako, hata kama wakati wake bado watainuka wenye ukubwa kama wako watakupiga vita, hii ni kwa sababu hawafurahii wewe uwe kama wao, hata unapotenda kwa busara ukiwa chini yao wanaogopa wanadhani ni ile hali yako ya ukubwa inawaelemea, wanaweza kukuwinda, wanaweza kukuwekea sumu, wanaweza kukusudia kukutendea mabaya wanapigwa upofu kwa sababu ya nini Neema ya Mungu ya ukubwa wako inawatesa na kualika uadui, angalia Daudi alikuwa na Adui ambaye ni Mfalme Sauli hivyo Sauli alikusudia kumuua Daudi, Hata hivyo ukubwa wa Daudi usingeweza kuharibiwa kwa sababu Mungu alikusudia lakini wote tunaelewa jinsi Sauli alivyosababisha maisha ya Daudi kuwa magumu sana akikimbia huku na kule katika mapango na majabali na nyika  kujificha na kuhami uhai wake kwaajili ya wivu wenye uchungu wa Sauli.

 

3.       Alichukiwa kwa sababu hawakuweza kushindana na Hekima iliyokuwa juu yake – Stefano angalia katika

 

Matendo 6:8-10 “Na Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu.Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano; lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye.”

 

Roho Mtakatifu alikuwa amempaka mafuta Stefano, uweza wa Mungu ulikuwa juu yake akitumiwa na Mungu kufanya ishara na miujiza mikubwa, lakini sio hivyo tu kichwani alikuwa yuko vizuri, alikuwa na ujuzi wa maandiko na neno la Mungu lilikuwa limejaa, watu wa masinagogi kama matano hivi  walikuja kujadiliana naye lakini hawakumuweza kwa sababu alikuwa na hekima ya kupita kawaida na Roho wa Mungu alisema naye, tunajifunza hapa sio mali tu, sio cheo tu hata hekima na uwepo wa Mungu unaoubeba unavutia maadui, wanachukizwa na hali yako ya kiroho, wanatamani uchafuke, uonekane ulikuwa mtu mbaya hufai, wewe ni kama kirusi tu, unatengenezewa skendo adui zako wanatamani wapate sababu mbaya za kukuharibia walifanya hivyo kwa Stefano watafanya hivyo na kwako bila kujali kuwa ni walokole wenzako au la angalia walitafuta kumchafua Stefano kwa sababu za kizushi

 

Matendo 6:11 - 14 “Hata wakashawishi watu waliosema, Tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu. Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi, wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati; maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahali hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa.”

 

Unaona? Hamkuwahi kuona watu wakichafuliwa, hamkuwahi kuona watu wakizushiwa maneno ya uongo katika jamii? Hamkuwahi kuona wakiitwa mafisadi, kumbe ni kwaajili ya wivu wenye uchungu kutoka kwa maadui, watu wanachukizwa na utajiri ulio nao, wanachukizwa na Neema ya Mungu iliyoko juu yako, wanachukizwa na Mali alizokupa Mungu wanachukizwa na ndoto zako, wanachukizwa na uchungu na uzalendo na msimamo wako wa dhati na uzalendo kwa watu wako lakini pia wanachukizwa na Hekima iliyoko juu yako, akili kubwa uliyo nayo utendaji wako, uwajibikaji wako kazini na kadhalika ndivyo walivyomfanyia Stefano wakampiga kwa mawe na kumuua, wako watu wamedhurika na magonjwa, wamekufa vifo vyenye utata, wameumizwa mioyo si kwa sababu walikuwa na hatia bali kwa sababu ya watu wenye wivu, wivu wenye uchungu.

 

4.       Alichukiwa kwa sababu tu alikuwa mkweli – Mungu anapokupa neema ya kuwa mkweli Neema hiyo pia huwavutia maadui, Yohana mbatizaji alitiwa gerezani na kuuawa kwa sababu Mungu alimpa neema na ujasiri wa kusema kweli!

 

Marko 6:17-28 “Kwa maana Herode mwenyewe alikuwa ametuma watu, akamkamata Yohana, akamfunga gerezani, kwa ajili ya Herodia, mkewe Filipo ndugu yake, kwa kuwa amemwoa; kwa sababu Yohana alimwambia Herode, Si halali kwako kuwa na mke wa nduguyo. Naye yule Herodia akawa akimvizia, akataka kumwua, asipate. Maana Herode alimwogopa Yohana; akimjua kuwa ni mtu wa haki, mtakatifu, akamlinda; na alipokwisha kumsikiliza alifadhaika sana; naye alikuwa akimsikiliza kwa furaha. Hata ilipotokea siku ya kufaa, na Herode, sikukuu ya kuzaliwa kwake, alipowafanyia karamu wakubwa wake, na majemadari, na watu wenye cheo wa Galilaya; ndipo binti yake yule Herodia alipoingia, akacheza, akampendeza Herode na wale walioketi pamoja naye karamuni. Mfalme akamwambia yule kijana, Niombe lo lote utakalo, nitakupa. Akamwapia, Lo lote utakaloniomba nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu. Basi akatoka, akamwuliza mamaye, Niombe nini? Naye akasema, Kichwa cha Yohana Mbatizaji. Mara akaingia kwa haraka mbele ya mfalme, akaomba akisema, Nataka unipe sasa hivi katika kombe kichwa cha Yohana Mbatizaji. Mfalme akafanya huzuni sana, lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya hao walioketi karamuni, hakutaka kumkatalia. Mara mfalme akatuma askari, akaamuru kuleta kichwa chake. Basi akaenda, akamkata kichwa mle gerezani, akakileta kichwa chake katika kombe, akampa yule kijana, naye yule kijana akampa mamaye.”

 

Yohana mbatizaji aliuawa kwa sababu alikuwa Msemakweli, kweli iligharimu maisha yake maandiko yanamtaja kuwa alikuwa mtu wa haki, alimkemea mfalme Herode kwa tendo la kuwa na mke wa ndugu yake, akaamua kumtia gerezani, lakini mwanamke alifanya njama ya kuhakikisha anauawa ili uovu wao uendelee, wakose mtu wa kuwakemea, hivi ndivyo dunia inavyotaka, dunia haitaki watu wa kweli, haitaki watu wa haki, haiitaji watu safi, kuwepo kwako kunawahukumu, hawafaidi maisha yao, ya dhambi, hawataki mtu awe  na kidomo domo watataka wakunyamazishe ili nao wapige, aliyekuambia dunia inataka wasema kweli ni nani hii ilimgharimu maisha ya nabii Yahaya au Yohana mbatizaji kama inenavyo injili

 

5.       Alichukiwa kwa sababu  kwa sababu ya husuda aliwazidi katika kila idara – Yesu alikuwa mwema alifanya kazi njema umati mkubwa wa watu ulimfuata walimuimbia hosanna mwana wa Daudi, ndiye mbarikiwa ajaye kwa jina Bwana

 

Mathayo 27:116-20 “Basi palikuwa na mfungwa mashuhuri siku zile, aitwaye Baraba. Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda. Na alipokuwa ameketi juu ya kiti cha hukumu, mkewe alimpelekea mjumbe, kumwambia, Usiwe na neno na yule mwenye haki; kwa sababu nimeteswa mengi leo katika ndoto kwa ajili yake. Nao wakuu wa makuhani na wazee wakawashawishi makutano ili wamtake Baraba, na kumwangamiza Yesu.”

 

Hivi umewahi kujiuliza kwanini Yesu alichukiwa? Vikao vya siri vikakaliwa na mikakati ya kuhakikisha anashughulikiwa ikafanyika? Sababu kubwa ni kuwa Yesu alikuwa mashuhuri kuliko watu wote, alijizolea sifa zote, kutokana na huduma na utumishi wake kwa kondoo wa Mungu waliotawanyika, alikuwa Mwalimu mwema, alikuwa ni mchungaji mwema, aliponya watu, aliwahurumia, alikuwa na majibu ya shida na matatizo yote ambayo jamii ilikuwa inakutana nayo, alilisha watu wengi, alifufua alifuta misiba ya wengi alafu mshahara wake ni kusulubiwa? Inakuwaje mtu mwema auawe? Inakuwaje watu wachague mtu muovu wamuache Yesu asulubiwe? Maandiko yanasema Pilato alijua kuwa wamemtoa kwa sababu ya husuda yaani wivu wenye uchungu, kila baya unalofanyiwa wakati mwingine ni kwa sababu umewazidi adui zako katika idara zote Neema iliyokuwa juu ya Yesu ilikuwa imewafunika viongozi wa dini, alikuwa akiwaumbua kwa kujawa na unafiki, aliifundisha kweli na kunyosha mstari, aliwakosoa vikali, akiwatendea mema watu na kuwafungua macho, akiruka vikwazo vyao, kwa hiyo walitafuta sababu za kumsulubisha  kwanini kwa sababu Neema ya Mungu iliyokuwa juu yake iliwavutia maadui!, vaa vizuri, kula vizuri, jenga nyumba nzuri, uwe na cheo kizuri utavutia watu wengi sana wawe karibu na wewe lakini wengine ni nyoka ni watu waliojaa wivu wenye uchungu wanaotaka kukuharibia maisha yako, watakuambia twende uwandani kisha huko watakuinukia wakuue  kama Habili kwanini kwa sababu neema ya Mungu iliyoko juu yako inaalika maadui.

Neema ya Mungu na mwaliko wa maadui

Mwanzo 26:12-16 “Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi.”

Tumeona katika utangulizi wa somo letu, namna Isaka alivyochukiwa na wafilisti na sababu kubwa ni kuwa walimuonea wivu, na wakaamua kuziba vyanzo vya Baraka zake yaani vile visima, Wakisahau kuwa chanzo kikuu cha Baraka za Isaka ni neema ya Mungu iliyokuwa juu yake, hata hivyo kama ipoipo tu, Mungu akishakuwa na mpango na mtu hakuna mwanadamu anaweza kuzuia mpango wa Mungu, Ndugu yangu vita yote kubwa uliyo nayo ni kwa sababu wewe u mzuri, unavaa vizuri, una neema ya Mungu juu yako, Mungu amekusudia kukuweka juu na kukubariki, kwa hiyo usifadhaike unapokutana na changamoto mbalimbali jua tu ya kuwa Mungu akiwa na mpango na wewe mipango yote ya wanadamu inafikia ukingoni, na Mungu anakwenda kujitukuza katika maisha yako, Isaka hakushindania visima na badala yake alichimba kingine na kingine na kingine na mwisho wa siku wakaona aibu wakamwacha na Mungu akaweka mkono wake na kuwapatia ahueni au nafasi Rehoboth wakati mwingine tuondoke na kwenda mbali na maadui zetu ili Bwana atupe nafasi ya kupumua maana wanaumwa sana na wivu wanaumwa mno wanadahani wakifukia visima na kudai kuwa ni vyao basi watatoboa lakini ijulikane wazi ya kuwa Mungu ni Mungu na Mungu kwa neema yake ndio chanzo kikuu cha Baraka zetu, Isaka angeweza kupigana vita lakini kwa kuwa alikuwa ni mtu mwema na mpenda Amani aliamua kujiepusha ili kutafuta kwa bidi kuwa na amani na watu wote!

Mwanzo 16:17-22. “Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko. Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye.Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika.Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye.Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna.Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”

Ushauri kutoka kwa Mungu.

Huu ni ushauri ambao Mungu anautoa kwa watu wenye wivu, kwamba ili Mungu akubariki, wewe endelea kufanya mema, basi, ukifanya vema naye atakubariki, Mungu amekusudia kumbariki kila mmoja  Mungu hana upendeleo hivyo jitahidi usimuonee wivu nduguyo, acha kuwafanyia watu mabaya, usiwauwe kwa ushahidi wa uongo, usiwachafue, usiwakasirikie ni neema ya Mungu iko juu yake huwezi kushindana naye ikiwa mkono wa Bwana uko juu yake, Mungu baba alimshauri Kaini ili asiingie dhambini kuwa afanye vema ! Mpango wa Mungu ni kumbariki kila mtu, lakini Mungu anataka usiwe na uchungu anapombariki mwengine hakikisha ya kuwa unakuwa mbali na kuumwa pale Mungu anapotoa kibali na neema yake kwa nduguyo kwani ni swala la zamu tu usitende dhambi, usifanye hila usikasirike, fanya vema nawe utabarikiwa pia usiwe na roho ya kaini aliyemuua nduguye  

Mwanzo 4:2-11 “Akaongeza akamzaa ndugu yake, Habili. Habili alikuwa mchunga kondoo, na Kaini alikuwa mkulima ardhi. Ikawa hatimaye Kaini akaleta mazao ya ardhi, sadaka kwa BWANA. Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama. BWANA akamtakabali Habili na sadaka yake; bali Kaini hakumtakabali, wala sadaka yake. Kaini akaghadhibika sana, uso wake ukakunjamana. BWANA akamwambia Kaini, Kwa nini una ghadhabu? Na kwa nini uso wako umekunjamana? Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde. Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende uwandani]Ikawa walipokuwapo uwandani, Kaini akamwinukia Habili nduguye,akamwua. BWANA akamwambia Kaini, Yuko wapi Habili ndugu yako? Akasema, Sijui, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu? Akasema, Umefanya nini? Sauti ya damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika ardhi. Basi sasa, umelaaniwa wewe katika ardhi, iliyofumbua kinywa chake ipokee damu ya ndugu yako kwa mkono wako;”

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!







Jumapili, 11 Februari 2024

Yule mjanja alisema siku ya tatu nitafufuka


Mathayo 27:62-66 “Hata siku ya pili, ndiyo iliyo baada ya Maandalio, wakuu wa makuhani, na Mafarisayo wakamkusanyikia Pilato, wakasema, Bwana, tumekumbuka kwamba yule mjanja alisema, alipokuwa akali hai, Baada ya siku tatu nitafufuka. Basi amuru kwamba kaburi lilindwe salama hata siku ya tatu; wasije wanafunzi wake wakamwiba, na kuwaambia watu, Amefufuka katika wafu; na udanganyifu wa mwisho utapita ule wa kwanza. Pilato akawaambia, Mna askari; nendeni mkalilinde salama kadiri mjuavyo. Wakaenda, wakalilinda kaburi salama, kwa kulitia lile jiwe muhuri, pamoja na wale askari walinzi.”




Utangulizi:

Moja ya tukio muhimu sana katika Imani ya Ukristo ni pamoja na tukio la Kusulubiwa, kufa na kufufuka kwa Yesu Kristo, tukio hili halikuwa tukio la bahati mbaya na ndio maana Yesu Kristo katika Hekima yake alilirudia tena na tena mara kwa mara alipokuwa pamoja na wanafunzi wake na hii ni kwa sababu Mateso yake na kifo chake ndio kilele cha juu zaidi cha huduma yake ya ukombozi kwa wanadamu, Na ndio maana tunaona Yesu akizungumza juu ya tukio hili mara kadhaa na kila wakati akijitaja kama Mwana wa Adamu ona :-

-          Mathayo 16:21-23 “Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka. Petro akamchukua, akaanza kumkemea, akisema, Hasha, Bwana, hayo hayatakupata. Akageuka, akamwambia Petro, Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.”

 

-          Marko 8:31-32 “Akaanza kuwafundisha kwamba imempasa Mwana wa Adamu kupatikana na mateso mengi, na kukataliwa na wazee, na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na baada ya siku tatu kufufuka. Naye alikuwa akinena neno hilo waziwazi. Petro akamchukua, akaanza kumkemea.”

 

-          Luka 9:21-22 “Akawaonya, akawakataza wasimwambie mtu neno hilo; akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka.”

 

-          Mathayo 17:22-23 “Nao walipokuwa wakikaa Galilaya, Yesu akawaambia, Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua, na siku ya tatu atafufuka. Wakasikitika sana.”

 

-          Marko 9:30-32 “Wakatoka huko, wakapita katikati ya Galilaya; naye hakutaka mtu kujua. Kwa sababu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake, akawaambia, Mwana wa Adamu yuaenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua; hata akiisha kuuawa, baada ya siku tatu atafufuka. Lakini hawakulifahamu neno lile, wakaogopa kumwuliza.          “

 

-          Luka 9:43-45 “Wote wakashangaa, wakiuona ukuu wa Mungu. Nao walipokuwa wakiyastaajabia mambo yote aliyoyafanya, aliwaambia wanafunzi wake, Yashikeni maneno haya masikioni mwenu, kwa kuwa Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa katika mikono ya watu. Lakini hawakulifahamu neno lile, likafichwa kwao wasilitambue; wakaogopa kumwuliza maana yake neno lile.”

 

Unaona Yesu alikuwa na kusudi maalumu la kurejea tena na tena kuhusiana na tukio hili, na anaeleza hivi mbele ya wanafunzi wake ili kwamba wapate kuamini litakapotukia.

Yohana 14: 28-29 “Mlisikia ya kwamba mimi naliwaambia, Naenda zangu, tena naja kwenu. Kama mngalinipenda, mngalifurahi kwa sababu naenda kwa Baba, kwa maana Baba ni mkuu kuliko mimi. Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini.”   

Kwanini Yesu alirejea tena na tena tukio hili sio tu wanafunzi wake wapate kumuamini lakini pia ijulikane wazi kuwa alikuwa akiyatoa maisha yake yawe fidia ya wengi na kuleta ukombozi wa Mwanadamu, kwa Msingi huo kuna uwezekano mkubwa sana maadui wa Yesu Kristo walikuwa wamesikia Yesu akizungumza wazi wazi kuhusiana na swala hili na hivyo alipokufa walitaka kuhakikisha kuwa wanalidhibiti kaburi la Yesu ili wanafunzi wake wasije wakamuiba na kudai kuwa amefufuka kama alivyosema na hapo ndipo kukawa na mikakati ya kuhakikisha Kaburi la Yesu linawekwa muhuri na kuwekwa walinzi kuhakikisha kuwa halibatiliki neno. Kwa Msingi huo leo tutachukua Muda kutafakari kwa kina somo hili lenye kichwa YULE MJANJA ALISEMA SIKU YA TATU NITAFUFUKA. Tutajifunza somo hili muhimu kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:- 


·         Maana ya maneno yule mjanja.

·         Jinsi Kaburi la Yesu lilivyopewa Ulinzi mkali.

·         Yule Mjanja alisema siku ya tatu nitafufuka.  



Maana ya maneno Yule mjanja.

Tunasoma katika kifungu cha Msingi maneno haya Mathayo 27:62-66 “Hata siku ya pili, ndiyo iliyo baada ya Maandalio, wakuu wa makuhani, na Mafarisayo wakamkusanyikia Pilato, wakasema, Bwana, TUMEKUMBUKA KWAMBA YULE MJANJA ALISEMA, ALIPOKUWA AKALI HAI, BAADA YA SIKU TATU NITAFUFUKA. Basi amuru kwamba kaburi lilindwe salama hata siku ya tatu; wasije wanafunzi wake wakamwiba, na kuwaambia watu, Amefufuka katika wafu; na udanganyifu wa mwisho utapita ule wa kwanza. Pilato akawaambia, Mna askari; nendeni mkalilinde salama kadiri mjuavyo. Wakaenda, wakalilinda kaburi salama, kwa kulitia lile jiwe muhuri, pamoja na wale askari walinzi.”

Tunaona Neno yule Mjanja likitumika hapa, kabla ya kuzungumza mambo mengine nataka tuchukue muda mfupi kuangalia neno hili walilolitumia dhidi ya Yesu Kristo kwa kumuita mjanja neno Mjanja linalotumika hapo katika kiingereza linatumika neno DECEIVER  Na katika kiyunani linatumika neno PLANOS ambayo kwa ujumla yana tafasiri mbaya na chafu, kwa kiingereza  linatumika neno Misleader, Seducer,  na Neno hili limetumika kama mara 4 katika biblia ya kiingereza, Kwa ujumla ni neno baya sana lililotumiwa kwa Yesu Kinyume kabisa na Sifa Halisi alizokuwa nazo, Neno Deceiver  ufafanuzi wake katika kiingereza ni a Liar, Fraud, Cheat, fake, betrayer, crook, Pretender na deluder  Kwa ujumla wanazungumza Kwamba Yesu alikuwa ni Tapeli au mtu anayepotosha watu, kwa uwongo, kutunga, kudanganya, kupika majungu, kusaliti, kuigiza, Mwongo, Haya yalikuwa ni maneno ya viongozi waliokuwa wamejawa na uchungu sana na kutoa neno kali sana kwa Yesu licha ya kuwa wakati huu walikuwa wamemuua kwa hila lakini bado waliendelea kuzungumza mambo mabaya kumuhusu kwa kusudi la kuchafua utu wake na tabia yake Yesu anatajwa katika maandiko kama:- 

Yohana 14:6 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na KWELI, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”

Yohana 1:14 “Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na KWELI.”

Yohana 16:13 “Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa KWELI, atawaongoza awatie kwenye KWELI yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake.”

Ufunuo 3:14 “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Laodikia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye Amina, Shahidi aliye MWAMINIFU NA WA KWELI, mwanzo wa kuumba kwa Mungu.”

Muda usingelitosha kuona jinsi maandiko yanavyomtaja Yesu kuwa ni kweli na Mwaminifu, kwa msingi huo wivu na chuki za maadui wa Yesu Kristo, uliwasukuma kushughulika naye wakimuita mjanja kwa kusudi la kumdhalilisha na kumuhakikishia Pilato kuwa Yesu alikuwa Mzushi tu na hakuwa mkweli  wakati Yesu alizaliwa kwa kusudi la kuishuhudia kweli

Yohana 18:37-38 “Yesu akajibu, Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa. Basi Pilato akamwambia, Wewe u mfalme basi? Yesu akajibu, Wewe wasema, kwa kuwa mimi ni mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na KWA AJILI YA HAYA MIMI NALIKUJA ULIMWENGUNI, ILI NIISHUHUDIE KWELI. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu.Pilato akamwambia, Kweli ni nini? Naye akiisha kusema neno hilo akawatokea Wayahudi tena, akawaambia, Mimi sioni hatia yo yote kwake.”

Hata hivyo kutokana na ujinga waliokuwa nao na ufahamu waliokuwa nao Pilato aliwataka walilinde kaburi kwa nguvu zote kwa kadiri wawezavyo na kuliwekea kaburi hilo Muhuri ili huyo wanayedai kuwa ni mjanja yeye au wanafunzi wake wasiweze kufanya jambo lolote kinyume na wanavyofikiri au kinyume na alivyosema !

Jinsi Kaburi la Yesu lilivyopewa Ulinzi mkali

Kutokana na madai ya wazee wa Sanhedrin (Mahakama ya juu ya kiyhahudi) kupeleka madai hayo kwa Pilato tunaona amri ikitolewa kufanyika kwa ulinzi maalumu wa Kaburi la Yesu ili isiwe kama alivyosema. 

Mathayo 27:64-66 “Basi amuru kwamba kaburi lilindwe salama hata siku ya tatu; wasije wanafunzi wake wakamwiba, na kuwaambia watu, Amefufuka katika wafu; na udanganyifu wa mwisho utapita ule wa kwanza.PILATO AKAWAAMBIA, MNA ASKARI; NENDENI MKALILINDE SALAMA KADIRI MJUAVYO. Wakaenda, wakalilinda kaburi salama, kwa kulitia lile jiwe muhuri, pamoja na wale askari walinzi.”

Ni jambo la kusikitisha sana na kushangaza kuwa maadui wa Yesu Kristo hawakuridhika kwamba wamefanya fitina na kuhakikisha kuwa Yesu anakufa Msalabani, wakuu hawa wa makuhani na wazee siku ile ya pili ilikuwa ni sabato, lakini jambo la kusikitisha ni kuwa walikuwa tayari kuongeza dhambi juu ya dhambi siku ambayo walipaswa kuishika sabato na wakati wanafunzi wa Yesu na watu wengine wametulia wao walikuwa na mkakati wa kumdhibiti Yesu zaidi, mioyo yao ilikuwa imejawa na uovu na chuki kubwa sana hata pale ambapo Yesu alikuwa amekufa, Dunia ya leo pia imejawa na watu wanaopingana na maswala ya Mungu na kushindana na watumishi wa Mungu wa kweli na hata pale unapoamua kunyamaza kimya bado wako watu watatafuta kukuchafua, kumekuwako na watu waovu, wasiomcha Mungu, wasiotenda haki, waliojawa na wivu na uovu wa kila aina ambao kazi yao kubwa ni kupingana na Mungu na watumishi wake na wengine wakijifanya ni watumishi wa Mungu, ni jambo la kusikitisha kuona Viongozi wa Dini tena siku ya sabato Yesu akiwa kaburini bado wanaendelea kumfuatilia na kushitaki kwa Pilato na Pilato aliamuru Kaburi lilindwe kwa kadiri iwezekanavyo, Ukiona bado watu wanakusema vibaya hata baada ya wewe kuondoka au kufa ujue wewe umeacha historia ya kuigwa aidha kwa wema au kwa ubaya, tunaweza kumkumbuka Hitler kwa sababu ya ukatili wake wa kuua watu wengi, tunaweza pia kumkumbuka Idd Amin kwa ukatili wake lakini vilevile tunaweza kuwakumbuka watu wema kupitia wema wao, lakini ukiona mtu mwema anachafuliwa hata baada ya kifo chake au yeye mwenyewe akiwa hayupo ujue mtu huyo ameacha rekodi (legacy) isiyokuwa ya kawaida na hata ingawa hayupo bado ni tishio,

1.       Kaburi liliwekwa Muhuri – “Seal” – Ni muhimu kufahamu hapa tunapozungumza kuhusu Muhuri hatuzungumzii ule muhuri ambao watu wamezoea, kizazi cha leo kinajua Muhuri ule waliozoea kuiona ikiwepo Ofisini, na wino wake, Muhuri hii inayotajwa katika Biblia ikiwepo kule katika kitabu cha Ufunuo ni aina ya Kamba maalumu au nyororo maalumu inayofungwa na chuma katika kitu kinachomilikiwa na Serikali ikiwa na alama ya marufuku kufunguliwa na mtu mwingine, Muhuri hiyo ni alama ya ulinzi na usalama mfano serikali inapoweka umeme katika nyumba Mita ya umeme  ni mali ya shirika na hivyo hufungwa na Kamba au waya maalumu na kubanwa ili kwamba mtu mwingine asiweze kufungua, hali kadhalika mita ya maji, na ikiwa muhuri itaharibiwa maana yake amri halali ya kiulinzi imehalifiwa, na hatua kali za kisheria zinaweza kuchukuliwa dhidi ya mtu aliyevunja muhuri hiyo, wanaoweza kufungua Muhuri hiyo ni wale tu waliofunga,  kwa kiyunani Muhuri hiyo huitwa SPHRAGIZO. Kwa hiyo unaposikia kuwa Kaburi liliwekwa Muhuri maana yake kuna aidha kuna Kamba maalumu zilihusika kulifunga kabisa kaburi, ili isitokee mtu akasogeza lile jiwe na au lilisilibwa kwa simenti ili kuliunga kaburi hilo kusipatikane upenyo wowote wa kitu kupita,  au alama inayowekwa kuthibitisha kuwa hakuna uharibifu wowote unaoweza kufanyika ni tukio kama hili lilifanywa kwa nabii Daniel kuhakikisha kuwa anabaki katika tundu la Simba ona

 

Daniel 6:15-17“Ndipo watu wale wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia mfalme, Ee mfalme, ujue ya kuwa ni sheria ya Wamedi na Waajemi, lisibadilike neno lo lote lililo marufuku, wala amri yo yote iliyowekwa na mfalme. Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danieli.”               

 

Muhuri huu ulikuwa ni alama ya kuhakikisha kuwa hakuna mabadiliko yoyote yanayoweza kufanyika kinyume na kile ambacho serikali imekiamua na kuwa hakuna kutoka ndani ya kaburi au pango kwa msaada wa kibinadamu isipokuwa kama mfalme au aliyetoa amri atabatilisha, kwa hiyo kitu kilipowekwa muhuri ilimaanisha lisibatilike neno katika jambo lolote ambalo limeamuriwa labda Mungu aingilie kati.

 

2.       Kaburi liliwekewa ulinzi mkali sana – Utafiti wa kibiblia na kihistoria unakubaliana na ukweli kuwa hakuna askari walikuwa na utii kama askari wa Kirumi, na katika tamaduni za kirumi kama askari waliagizwa kulinda kitu na kitu hicho kikabainika kuwa hakikulindwa ipaswavyo hukumu yake ilikuwa ni kifo tu na kwa sababu hiyo wakati mwingine askari waliweza kuamua kujiua wenyewe kuliko kushughulikiwa na serikali angalia

 

-          Matendo ya Mitume 12:4-19 “Alipokwisha kumkamata, akamweka gerezani akamtia mikononi mwa vikosi vinne vya askari wanne wanne, wamlinde, akitaka baada ya Pasaka kumtoa na kumweka mbele ya watu. Basi Petro akalindwa gerezani, nalo kanisa likamwomba Mungu kwa juhudi kwa ajili yake. Hata wakati Herode alipotaka kumtoa, usiku ule ule Petro alikuwa analala katikati ya askari wawili, amefungwa minyororo miwili; walinzi mbele ya mlango wakailinda gereza. Mara malaika wa Bwana akasimama karibu naye, nuru ikamulika mle chumbani, akampiga Petro ubavuni, akamwamsha, akisema, Ondoka upesi. Minyororo yake ikamwanguka mikononi. Malaika akamwambia, Jifunge, kavae viatu vyako. Akafanya hivyo. Kisha akamwambia, Jivike nguo yako, ukanifuate. Akatoka nje, akamfuata; wala hakujua ya kuwa ni kweli yaliyofanywa na malaika; bali alidhani kwamba anaona maono. Na walipopita lindo la kwanza na la pili, wakaja hata mlango wa chuma wa kuingilia mjini, ukawafungukia wenyewe. Wakatoka nje, wakapita katika njia moja; mara malaika akamwacha. Hata Petro alipopata fahamu akasema, Sasa nimejua yakini ya kuwa Bwana amempeleka malaika wake na kunitoa katika mkono wa Herode na katika kutazamia kote kwa taifa la Wayahudi. Na alipokuwa akifikiri haya akafika nyumbani kwa Mariamu, mamaye Yohana, ambaye jina lake la pili ni Marko; na watu wengi walikuwa wamekutana humo wakiomba. Naye alipobisha kilango cha lango, kijakazi, jina lake Roda, akaja kusikiliza.  Alipoitambua sauti ya Petro, hakukifungua lango, kwa ajili ya furaha, bali alipiga mbio, akaingia ndani akawaambia kwamba Petro anasimama mbele ya lango. Wakamwambia, Una wazimu. Lakini yeye akakaza sana, akasema ya kwamba ndivyo hivyo. Wakanena, Ni malaika wake. Petro akafuliza kugonga, hata walipokwisha kumfungulia wakamwona, wakastaajabu. Naye akawapungia mkono wanyamaze, akawaeleza jinsi Bwana alivyomtoa katika gereza. Akasema, Kampasheni Yakobo na wale ndugu habari hizi. Akaondoka, akaenda mahali pengine. Hata kulipopambauka askari wakaingiwa na fadhaa nyingi, amekuwaje Petro. Na Herode alipomtafuta, asimwone, aliwauliza-uliza wale walinzi, akaamuru wauawe. Kisha akatelemkia kutoka Uyahudi kwenda Kaisaria, akakaa huko.”                

 

-          Matendo ya Mitume 16:25-27 “Lakini panapo usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za kumsifu, na wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza. Ghafula pakawa tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisika, na mara hiyo milango ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa.Yule mlinzi wa gereza akaamka, naye alipoona ya kuwa milango ya gereza imefunguka, alifuta upanga, akataka kujiua, akidhani ya kuwa wafungwa wamekimbia.”

Kwa msingi huo unaweza kupata picha kuwa licha ya kuwepo kwa Muhuri lakini vile vile kaburi la Yesu lilikuwa na ulinzi mkali sana, kuna uwezekano walikuwepo askari zaidi ya 16 na kwa taratibu za kirumi askari asipotimiza wajibu alitakuwa kuuawa na ndio maana unaona hata mkuu wa gereza aliyekuwa akiwashikilia Paulo na Sila alitaka kujiua yeye mwenyewe kwa sababu ilieleweka wazi kuwa kama ameshindwa kutimiza wajibu katika kulinda kile alichotakiwa kukilinda basi hukumu yake ni kifo, kwa msingi huo tamaduni hii inatuhakikishia kuwa Kaburi la Yesu lililindwa bara bara na ilipaswa kuwa hivyo maana wao waliona Yesu kuwa ni Mjanja, mwongo, tapeli na mzushi kwa hiyo ulinzi wao ulikuwa ni wa kuhakikisha kuwa huyo mjanja hatoki! 

Yule Mjanja alisema siku ya tatu nitafufuka 

Ukweli ni kuwa wazee wale walikuwa wanafanya ujinga, Mungu alikuwa anataka wao wenyewe ndio wawe mashahidi wa Kwanza wa kufufuka kwake Kristo, Kumbuka pamoja na Yesu kurudia rudia kuwa atasulubiwa na kuuawa na siku ya tatu atafufuka jambo hili lilikuwa zito kueleweka kwa wanafunzi wa Yesu, lakini maadui wa Yesu walikuwa wanakumbuka na sasa wanafanya makakati wa kulilinda kaburi kama tulivyoona lilikuwa jambo jema kwao.

Hawakuwa wanajua kuwa wanashughulika na mtu ambaye Kifo hakiwezi kumzuia, walikuwa wakishughulika na Mwenyewe ambaye ni ufufuo na uzima, mwenye mamlaka ya mauti na uzima! Na ambaye makusudi yake hayawezi kuzuiliwa kamwe

Yohana 11:24-25 “Martha akamwambia, Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho. Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi;”

Huwezi kumuwekea mipaka mwanaume mwenye funguo/Mamlaka ya mauti na uzima Ufunuo 1:17-18 “Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.”

Yesu alifufuka, kufufuka kwake kunatoa ujumbe kuwa hakuna kitu wala mtu anaweza kuzuia kusudi la Mungu katika maisha yako, kama jinsi ambavyo hawakuweza kuzuia kusudi la Mungu kumfufua Yesu Kristo, Mungu ni mwenye nguvu ya kufufua anauwezo wa kuondoa lolote lililokufa na kulirudishia uhai, anauwezo wa kubadilisha huzuni kuwa furaha, anauwezo wa kubadilisha maombolezo kuwa machezo, kama jinsi ambavyo viongozi wa dini na askari na wazushi walishindwa kuzuia Yesu asifufuke nataka nikutangazie kuwa Roho Mtakatifu amenituma nikutangazie kuwa haijalishi wachawi wameweka muhuri ya namna gani, haijalishi kuwa wapiga majungu wamepiga kwa kiasi gani, hauijalishi kuwa wafitini wamefitinisha kwa kiwango gani, hajalishi kuwa umekandamizwa kwa kiasi gani, Mungu atamtuma malaika wake aliyezivunja zile muhuri na kudongolosha lile jiwe linalosimama kama kizuizi katika maisha yako na utatoka tena nasema utatoka tena nasema utainuka, adui zako wanataka kuhakikisha ya kuwa unalala, wanataka kuharibu sifa na wema wako uonekane kuwa wewe ni mjanja mjanja tu, wanatangaza mwisho wako na kudhani ya kuwa wamekudhibiti na kuwa huwezekani kuinuka tena Lakini  Roho Mtakatifu anatangaza mwanzo wako leo katika jina la Yesu Kristo wa Nazareth aliye hai, hakuna jini, hakuna maimuna, hakuna makata wala kinyamkera, hakuna pepo, hakuna mganga, hakuna mchawi, hakuna hirizi, hakuna pembe, hakuna zindiko, hakuna uchawi, hakuna mamlaka, hakuna jeshi, hakuna askari hakuna, hakuna hakuna kizuizi chochote kitakachozuia kusudi la Mungu katika maisha yako, wakati ambapo ujanja ulitumika kama neno la kejeli leo tunaligeuza kuwa sisi tulio ndani ya Yesu ni wajanja kweli kweli, sisi sio wa kawaida, tumewekwa katika ulimwengu wa roho pamoja na Kristo, tumekufa pamoja naye, tumefufuka pamoja naye, tunatawala pamoja naye hivyo ndivyo neno la Mungu linavyotuambia:-  

Waefeso 2:6 “Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho”, 

Katika Kristo Yesu; kila anayemuamini Yesu yuko juu, ameinuliwa amefufuka pamoja naye sisi sio wa kawaida, hakuna anayeweza kushindana na mapenzi ya Mungu katika maisha yetu, hakuna anayeweza kuhakikisha kuwa tunabaki kaburini, hakuna wa kutuzuia, hakuna wa kutuzibia, hakuna wa kulinda na kumzuia  Mungu mwenye nguvu, Mungu wa baba zetu anayahuisha tena maisha yetu na kutuweka mahali salama Kristo alitoka kwa mkwara kaburi lilitetemeka muhuri zikavunjwa na malaika akalivingirisha jiwe na akalikalia jiwe, walinzi wakawa kama wafu kiwewe kiliwashika, Yesu ni aliye hai katika wafu, wewe na mimi tu hai leo haleluyaaa! Wakati adui zetu wakikesha kuhakikisha hatuamki ni wao ndio watakaokuwa wafu wakati sisi tunafufuka!, Maandiko yanaonyesha kuwa walinzi wa kirumi safari hii hawakuweza kutimiza wajibu wao malaika wa Bwana alilivingirisha jiwe akalikalia, alivunja mihuri yao, alibatilisha matakwa yao Yesu alifufuka na hakuibiwa mwanaume wa wanaume kaburi halikumuweza, Alifufuka kwelikweli!, Nampenda Mungu nampenda Yesu mipango yao huiweka wazi kabisa kwa sababu hakuna anayeweza kuzuia mpango wa Mungu, Mtu mmoja aliniambia usiweke wazi mipango yako wala usimwambie mtu ndoto zako kwa sababu wanadamu ni waovu wanaweza kwenda kuzuia mipango yako au kupigana nayo, sielewi anatumia andiko gani lakini Tabia ya Mungu huweka wazi mipango yake hueleza mapema siku ya tatu nitafufuka na hakuna wa kuzuia, Kama ndoto zangu ni mpango wa Mungu hata nikiweka wazi hakuna wa kuzuia, kama mipango yangu ni mipango ya Bwana hakuna wa kuzuia, mbona walijaribu kumuua mwenye ndoto Yusufu ili kuua ndoto zake na Je ziliztimizwa hazikutimizwa? Hekima ya Mungu sio kama hekima ya wapuuzi wa dunia hii, Mungu akiwa na mpango na jambo lake hata mroge kwa ramba ramba, chaumbeya au tekelo, au uende kwa waganga kule Pemba, au Newala kule Nchedebwa, au Nachingwea, au Lamu, au Kwasemangube, au Kwamsisi huko Handeni, au Sumbawanga kokote unakoweza kwenda huwezi kuzuia makusudi na mpango wa Mungu, Mungu ni mwenye nguvu angalia walipozuia na kulilinda kaburi kwa ulinzi wao wote maandiko yanasema kulitoka tetemeko kubwa la nchi, malaika alishuka akalivingirisha jiwe na kulikalia, wapinzani wakawa kama wafu hivi ndivyo Mungu wentu anavyofanya mambo yake !

Mathayo 28:2-4 “Na tazama, palikuwa na tetemeko kubwa la nchi; kwa sababu malaika wa Bwana alishuka kutoka mbinguni, akaja akalivingirisha lile jiwe akalikalia. Na sura yake ilikuwa kama umeme, na mavazi yake meupe kama theluji. Na kwa kumwogopa, wale walinzi wakatetemeka, wakawa kama wafu.” 
    

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 4 Februari 2024

Kuponywa kwa mtu mwenye kibiongo!


Luka 13:10-13 “Siku ya sabato alikuwa akifundisha katika sinagogi mojawapo. Na tazama, palikuwa na mwanamke aliyekuwa na pepo wa udhaifu muda wa miaka kumi na minane, naye amepindana, hawezi kujinyosha kabisa.Yesu alipomwona alimwita, akamwambia, Mama, umefunguliwa katika udhaifu wako.  Akaweka mikono yake juu yake, naye akanyoka mara hiyo, akamtukuza Mungu.”




Utangulizi:

Katika moja ya miujiza kadhaa mikubwa aliyoifanya Bwana Yesu, Moja ya muujiza wa muhimu sana ni pamoja na huu wa kuponywa kwa mtu mwenye kibiongo.(Ugonjwa wa kupindana kwa mgongo) Luka 13:10-13 “Siku ya sabato alikuwa akifundisha katika sinagogi mojawapo. Na tazama, palikuwa na mwanamke aliyekuwa na pepo wa udhaifu muda wa miaka kumi na minane, naye amepindana, hawezi kujinyosha kabisa. Yesu alipomwona alimwita, akamwambia, Mama, umefunguliwa katika udhaifu wako.  Akaweka mikono yake juu yake, naye akanyoka mara hiyo, akamtukuza Mungu.”

Ugonjwa huu wa kibiongo au ugonjwa wa kupindana mgongo ni moja ya ugonjwa mbaya sana sana katika historia ya  magonjwa duniani, na kwa bahati nzuri Yesu Kristo alikuwa haponyi ilimradi tu, utaweza kuona miujiza mingi aliyoifanya Kristo aliifanya kimkakati, aidha kwa watu walioteseka sana na kupoteza matumaini ili awasaidie, au kwa kusudi Mungu atukuzwe na watu wapate kumuamini, na pia kwaajili ya kutufundisha!, Muujiza huu wa kuponywa kwa mtu mwenye kibiongo, una maswala kadhaa ya kutufundisha yanayoonyesha namna Mungu anavyoshughulika na watu wake hasa ambao wanapitia hali ngumu sana, leo tutachukua Muda kuuangalia muujiza huu, kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-  


·         Ufahamu kuhusu ugonjwa wa kupindana mgongo (Kibiongo)

·         Kuponywa kwa mtu mwenye kibiongo

·         Mambo ya kujifunza kupitia muujiza huu


Ufahamu kuhusu ugonjwa wa kupindana mgongo (Kibiongo)

Ugonjwa wa kupinda mgongo (kibiongo) ni mojawapo ya magonjwa mabaya sana duniani, ugonjwa huu kitaalamu unaitwa CAMPTOCORMIA ambapo kwa kawaida wanaopatwa na ugonjwa huu huwa na muonekano wa kupinda usiokuwa wa kawaida anaposimama, na unaweza kuonekana zaidi anapotembea, ni ugonjwa unaotokana na muundo mmbaya unaojitokeza kutokana na kupinda kwa mbele au kwa nyuma kwa uti wa mgongo,  Neno hilo CAMPTOCORMIA  limetokana na neno la Kiyunani KAMPTOS  ambalo maana yake ni BENT FORWARD au BENT BACKWARD  kwa kawaida jina la kawaida kwa kiingereza ni “Bent spine syndrome” kupinda kwa mgongo. Ni ugonjwa mbaya na unapoteza kabisa “shape”  muonekano wa mtu, Ugonjwa huu sio tu kuwa haujulikani sababu zake lakini pia hauna matibabu maalumu zaidi ya kuwaona wataalamu wa mifupa (Physiotherapy) ambao watakuwa wakimpatia mgonjwa matibabu ya kimazoezi tu, ugonjwa huu sio tu unaweza kujitokeza kwa mtu kufutukia kifuani na kudidimia sehemu ya nyuma ya mgongo, au kuwa na umbile kama la upinde mgongoni unaofikia nyuzi 45  na kumfanya mtu huyo kuinama hata asiweze kuiona mbingu au kumchungulia mtu usoni, kwa ujumla ukiacha kuwa mtu mwenye ugonjwa huu hapandezi unapomuona, lakini vilevile unaweza kuhisi maumivu anayoyapata mtu aliyepindana wakati mwingine uti wa mgongo wa mtu mwenye ugonjwa huu unaweza kujichora kama umbo la S na  na wakati mwingine unaweza kusababisha bega moja la mtu huyo likawa juu na lingine chini, au mbavu zake zikaonekana zimeinama upande mmoja, Nguo za kawaida hazimkai vizuri mtu wa jinsi hiyo kwa ujumla ni ugonjwa wa kusikitisha, madaktari wanasema ugonjwa huu unaweza kujitokeza kwa mtu anapoanza kubalehe hasa wanawake na kwa sababu hiyo wanaoshambuliwa sana ni wanawake kwa wingi na wanaume wa uchache, kwa kuwa mpaka sasa hakuna anayejua sababu za ugonjwa huu, Lakini Luka kwa vile alikuwa ni tabibu anaelezea kuwa ugonjwa huu unatokana na UDHAIFU lakini Luka anaelezea wazi kuwa ni udhaifu uliosababishwa na shetani  na tunaelezwa kuwa alikuwa katika hali hiyo kwa miaka 18, Ugonjwa huu unaambatana kwa mbali na hali ya udumavu kwa ujumla wake ni ugonjwa mmbaya sana ona:-  

Luka 13:10-13 “Siku ya sabato alikuwa akifundisha katika sinagogi mojawapo. Na tazama, palikuwa na mwanamke aliyekuwa na pepo wa udhaifu muda wa miaka kumi na minane, naye amepindana, hawezi kujinyosha kabisa. Yesu alipomwona alimwita, akamwambia, Mama, umefunguliwa katika udhaifu wako.  Akaweka mikono yake juu yake, naye akanyoka mara hiyo, akamtukuza Mungu.”

Luka ni tabibu, ni Daktari wa binadamu aliyeokoka hivyo anaelewa wazi kuwa kuna udhaifu wa kawaida na udhaifu unaosababishwa na Shetani, au mapepo, na Luka aliweza kujua udhaifu ule kitabibu hauwezi kuponyeka wala kuutibika lakini kujua kuwa ni Pepo inawezekana ni kutokana na Tabibu mkuu Yesu Mwenyewe kuwafunulia watu kuwa mateso ya mama yule yalitokana na kifungo cha shetani  kumbuika maneno yale “Na huyu mwanamke, aliye wa uzao wa Ibrahimu, ambaye Shetani amemfunga miaka kumi na minane” ona

Luka 13:11-17 “Na tazama, palikuwa na mwanamke aliyekuwa na pepo wa udhaifu muda wa miaka kumi na minane, naye amepindana, hawezi kujinyosha kabisa. Yesu alipomwona alimwita, akamwambia, Mama, umefunguliwa katika udhaifu wako. Akaweka mikono yake juu yake, naye akanyoka mara hiyo, akamtukuza Mungu. Basi mkuu wa sinagogi alikasirika kwa sababu Yesu amemponya mtu siku ya sabato, akajibu, akawaambia mkutano, Kuna siku sita zifaazo kufanya kazi, basi njoni mponywe katika siku hizo, wala si katika siku ya sabato. Lakini Bwana akajibu akasema, Enyi wanafiki, kila mmoja wenu, je! Hamfungui ng'ombe wake au punda wake siku ya sabato katika zizi, aende naye kumnywesha? Na huyu mwanamke, aliye wa uzao wa Ibrahimu, ambaye Shetani amemfunga miaka kumi na minane hii, haikupasa afunguliwe kifungo hiki siku ya sabato? Aliposema haya wakatahayari wote walioshindana naye; mkutano wote wakafurahi kwa sababu ya mambo matukufu yaliyotendwa na yeye.”   

Unaona maelezo ya Luka ya awali yametokana na maelezo ya Yesu mwenyewe Kwamba mwanamke yule alikuwa amefungwa na Shetani kwa miaka 18, tena Yesu anamtaja kuwa mwanamke wa Uzao wa Ibrahimu, hii inaonyesha wazi kuwa kulikuwa na uonevu wa Ibilisi, tena bila kujali kuwa huyu binti ni wa uzao wa Ibrahimu, maana yake nini unaweza kuwa Mkristo na bado ukafungwa katika vifungo na uonevu wa ibilisi, unaweza kuwa wa uzao wa Ibrahimu yaani mtu wa Imani, Binti huyu alikuwa na imani, angalia kuwa alikuwa anahudhuria ibada alifika kwenye Sinagogi, siku ya sabato, lakini alikuwa anaonewa, viongozi wake wa dini hawakuweza kumsaidia, Ashukuriwe Mungu kwamba Mgeni rasmi alikuweko kwenye ibada siku ile, Yesu Kristo mtenda miujiza alikuwepo kwenye singagogi, kuhudhuria ibada pekee hakutoshi, kuwa wa uzao wa Ibrahimu pekee hakutoshi, kuwa na imani ya Ibrahimu pekee hakutoshi, tunamuhitaji Yesu Kristo aliye hai, Tunamtaka Bwana na nguvu zake, yako mambo kibinadamu sio ya kawaida hata kama tunayaona ya kawaida, yako mambo ambayo yako juu ya uwezo wetu ni Yesu pekee ndiye anayeweza kujua sababu ya mambo hayo kumbe mengine ni uonevu wa ibilisi unadhani nani angelijua, yako mambo hata madaktari hawajui ni kwanini, Lakini maandiko yanatukumbusha kuwa Yuko Yesu ambaye maalumu sana anaweza kuyachukua madhaifu yetu na kujitwika na kutupa unafuu bila kujali wataalamu wanasemaje.

Mathayo 8:16-16 “Hata kulipokuwa jioni, wakamletea wengi wenye pepo; akawatoa pepo kwa neno lake, akawaponya wote waliokuwa hawawezi, ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu.” 
            

Haijalishi una udhaifu wa namna gani na umeteseka kwa miaka mingapi, lakini maandiko yanaonyesha kuwa ni kazi yake Yesu kuponya madhaifu na magonjwa yetu, kwa hiyo kila mwanadamu bila kujali historia yake, kabila lake, ana uzuri kiasi gani ana ubaya kiasi gani maandiko yanatukumbusha leo kumwangalia Yesu kwa mambo ambayo madaktari na matabibu wa kawaida wameshindwa, Yeye atakuweka huru na kukufungua kutoka katika udhaifu wako

Kuponywa kwa mtu mwenye kibiongo:

Nadhani baada ya kuelezea ugonjwa aliokuwa nao mwanamke huyu wewe mwenyewe unaweza kupata hisia za mateso yake, kwamba alikuwa anateseka kiasi gani, na chukulia kama mwanamke wa aina hii ni binti yako! Au dada yako au mama yako! Au mkeo? Ungejisikiaje? Mateso haya sio tu yalikuwa ya mwilini lakini vilevile na kisaikolojia huenda alichekwa na watu, na sio hivyo tu hata familia yake huenda ilichekwa, au watu walimkwepa, au sio rahisi kuchumbiwa na kuolewa kulikuwa na ndoto nyingi ambazo zilikufa kutokana na maisha ya mateso aliyokuwa nayo mwanamke huyu, Ashukuriwe Mungu Yesu ni mwenye huruma sana, Mwanamke huyu aliyekuwa amepindana na hawezi kuinuka Biblia inasema Yesu alipomuona alimuita mbele, na akamwambia mama umefunguliwa katika udhaifu wako, na kama haitoshi Yesu akamwekea mikono yake na mara moja mwanamke yule aliponywa na akanyooka mara moja nakuanza kumtukuza Mungu, kulikuwa na namna nyingi tu ambazo Yesu angeweza kufanya angelituma neno, angekemea pepo, lakini Yesu akiwa amejawa na huruma, alimuita kitendo cha kuitwa mbele kilimfanya mwanamke yule ajue wazi kuwa ile ilikuwa ni siku yake,  na kuwa Yesu alionyesha kuwa anamjali, labda alisikia habari za Yesu na matendo yake makuu, aliwaza ni lini na mimi nitakuja kukutana na mtu huyo na aniponye? hakua na matumaini, lakini Hakuna jambo zuri duniani kama kuitwa na mtu mkubwa wa kiwango cha Kristo na sio hivyo tu Yesu alitamka neno na mwisho akaweka mikono yake juu yake, Mwanamke huyu aliponywa kwa heshima kubwa sana sio lazima wakati wote muhubiri akuwekee mikono, lakini Yesu alitaka kumuonyesha upendo wake mtu huyu alitaka kuponya na nafsi yake iliyoumizwa, alitaka kuinyesha kuwa yuko mmoja anayemjali, unaposoma juu juu utaweza kudhani kuwa Labda Yesu alifanya muujiza huu kuonyesha nguvu yake juu ya sabato, au juu ya viongozi wa dini, au kuonyesha nguvu yake juu ya shetani lakini stori hii ni kwajili ya upendo, kwaajili ya mateso, kwaajili ya kumuhurumia mtu mwenye fadhaa kubwa na nzito isiyo na tabibu kumtoa katika kifungo cha ibilisi angalia maneno yale UMEFUNGULIWA KATIKA UDHAIFU WAKO!, You are set Free from your infirmity !  Kusudi letu kubwa au langu kubwa kubwa ni kuonyesha kuwa ibada za maombezi haziko kwaajili ya kuonyesha nguvu za Mungu au nguvu za Muhubiri, au kuonyesha kuwa ninasikiwa na Yesu kwa kiwango gani, ua ninatymiwa na Mungu, au kujitafutia umaarufu, nataka watu wawe huru kwa sababu sifurahii kuona mateso, Huu ndio ulikuwa moyo wa Yesu Kristo, Roho Mtakatifu alikuwa amempaka mafuta na kumtumia kwa kusudia la kuwafungua watu wanaoonewa!

Luka 4:18-19 “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.”

Matendo 10:38 “habari za Yesu wa Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa Roho Mtakatifu na nguvu naye akazunguka huko na huko, akitenda kazi njema na kuponya wote walioonewa na Ibilisi; kwa maana Mungu alikuwa pamoja naye.”

Nia kubwa ya Yesu Kristo ni kuwasaidia watu, hakufurahi Mwalimu kuona watu wanaoonewa na Ibilisi, watu wa Mungu tumtafute Mungu, tutafute nguvu zake ili watu wanaoonewa kila mahali na hata makanisani mwetu na katika masinagogi, wapate kutoka katika uonevu wa ibilisi, haiwezekani watu wa Mungu wawe wanadhalilika na sisi tupo na Mungu ametuweka kwaajili ya kuwasaidia. Kristo Yesu alisikitishwa sana na viongozi wa dini na sinagogi ambao hata ibada ya uponyaji wa mwanamke huyu kwao ilikuwa kama kwazo ona

Luka 13:14-17 “Basi mkuu wa sinagogi alikasirika kwa sababu Yesu amemponya mtu siku ya sabato, akajibu, akawaambia mkutano, Kuna siku sita zifaazo kufanya kazi, basi njoni mponywe katika siku hizo, wala si katika siku ya sabato. Lakini Bwana akajibu akasema, Enyi wanafiki, kila mmoja wenu, je! Hamfungui ng'ombe wake au punda wake siku ya sabato katika zizi, aende naye kumnywesha? Na huyu mwanamke, aliye wa uzao wa Ibrahimu, ambaye Shetani amemfunga miaka kumi na minane hii, haikupasa afunguliwe kifungo hiki siku ya sabato? Aliposema haya wakatahayari wote walioshindana naye; mkutano wote wakafurahi kwa sababu ya mambo matukufu yaliyotendwa na yeye.”

Unaweza kuona nia ya Yesu hapa wala haikuwa shindano la sabato, Yesu alitaka kuonyesha uchungu aliokuwa nao kwa mwanamke aliyekuwa amefungwa, siku sita za kufanya kazi sio siku za ibada ni siku za watu kujitafutia mahitaji yao, na sabato ndio siku ya ibada watu wanajihudhurisha nyumbani kwa Bwana, nadhani  Yesu anatuonyesha siku ya bwana inavyopaswa kutumika, siku ya ibada yako, Leo hii unaweza kwenda kanisani na sio kibiongo, lakini ukawa tu umevunjika moyo na unakutana na watumishi wa Mungu waliojaa hasira, wanafokea watu, wanashushua watu, unatoka katika ibada ulikuja na majanga yako na badala ya kugangwa unatoka ukiwa umeumizwa moyo, watumishi wa Mungu ni lazima tuchague maneno ya kusema siku za ibada, kama unaona moyo wako hauko vizuri basi afadhali uache kuhudumu, wazee mnaotangaza matangazo, hakikisha kuwa mnazungumza kwa busara msiwaharibie watu ibada, Mwanamke huyu ilikuwa ni siku yake ya furaha na hata watu wa kawaida walifurahi na kumtukuza Mungu anakuja mtu kufunga ibada anabwatuka NABANA PUA HAPA “Kuna siku sita zifaazo kufanya kazi, basi njoni mponywe katika siku hizo, wala si katika siku ya sabato.” MWISHO WA KUBANA PUA. Ashukuriwe Yesu ni kiongozi mzuri wa ibada alihakikisha watu wanatoka ibadani wakimtukuza Mungu! Siku ya ibada ni lazima itumike kwa busara kunganga mioyo ya watu na sio kuwakwaza, kuwainua walioinama na sio kuwainamisha, Yesu alikuwa akionyesha matumizi sahihi ya siku ya Bwana, haipaswi kuwa siku ya kukandamiza watu na tafasiri mbaya za sharia bali ni siku ya kuweka watu huru kutoka katika majanga ya maisha yanayowasibu sikuhadi siku!

Mambo ya kujifunza kupitia muujiza huu

1.       Tunajifunza kwamba Yesu Kristo aliongozwa na upendo katika kila jambo alilolifanya, Yesu hakuwahi kufurahi hata siku moja lolote lile lisimame kinyume na msukumo wake wa upendo, ni kupitia upendo Karama na utumishi wetu kwa Mungu na kwa watu unapaswa kujengwa katika msingi huo. 1Wakorintho 13:1-8 “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi.Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu. Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni;haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote. Upendo haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika.” 

 

2.       Ugonjwa huu ulikuwa ni mbaya sana na uliambatana na ubaguzi wa hali ya juu watu wa jinsi hii kama walikuwa wanaume tena wa kabila la lawi hawakuruhusiwa kuwa makuhani kwani Torati iliwatenga na ilionekana ni kama watu waliokataliwa na Mungu ona Walawi 21:17-20 “Nena na Haruni, umwambie, Mtu awaye yote wa kizazi chako wewe katika vizazi vyao, aliye na kilema, asikaribie kusongeza chakula cha Mungu wake. Kwa kuwa mtu awaye yote aliye na kilema hatakaribia; mtu kipofu, au kiwete, au mtu aliye na pua iliyoharibika, au aliye na kitu kilichozidi vimpasavyo mwili, au mtu aliyevunjika mguu, au aliyevunjika mkono, au aliye na kijongo, au aliye kibeti, au aliye na kilema cha jichoni, au aliye na upele, au mwenye buba, au aliyevunjika mapumbu;” Yesu alithibitisha kuwa yuko kwaajili ya watu wa namna hii, alikuwa anafunua wazi kuwa hali ile kamwe sio kazi za Mungu bali ni uonevu wa shetani na kuwa Mungu yuko kinyume na aina zote za uonevu, Kristo alichukizwa na aina hii ya uonevu na akamfungua

 

3.       Kiongozi wa Sinagogi mwenye roho mbaya – kutokana na Yesu kutenda mema yeye alikasirika ndivyo maandiko yanavyotuambia, mtazamo wake kuhusu uponyaji na utendaji wa miujiza anaona kama ni kazi inayotakiwa kufanyika siku za kawaida na sio siku ya sabato, haishangazi kuwa na watu wenye ufahamu finyu kuhusu namna na jinsi Mungu anavyofanya kazi, ni hao hao ambao walikuwa wakifungulia punda kunywa maji au kuokoa mnyama asidumbukie shimoni siku ya sabato, lakini wanaona mtu kuponywa siku ya sabato ni ishu, Yesu alikemea tabia hii mbaya, watumishi wa Mungu wanapaswa kuwa na roho nzuri, huruma na upendo na ufahamu mkubwa kuliko hata wanaowaongoza, wakati watu wanafurahia matendo makuu ya Mungu inashangaza kuona mkuu wa sinagogi anakasirika, washirika wa siku hizi wana ufahamu mkubwa sana wa neno la Mungu hivyo viongozi hawana budi kujiongeza, na kuwa makini kwa wanachokiongea na hija wanayoijenga kuhusu utendaji wa Mungu na matendo yake ya huruma kwa watu

 

4.       Shetani anahusika kuwafunga watu ni kazi ya watumishi wa Mungu kuutafuta uso wa Bwana na karama za rohoni kwa kusudi la kuwasaidia watu kwa upendo, aidha katika upendo wake Yesu anaonyesha kuwa anaweza kuponya changamoto yoyote hata kama ni ya Muda mrefu, kumbuka mwanamke yule alionewa na ibilisi kwa miaka 18 lakini alipokutana na Yesu ukawa mwisho wa changamoto zake! Changamoto zako zitafikia mwisho hata bila kujali imechukua muda mrefu kwa kiasi gani!

 

5.       Wako watu ambao katika hali ya kawaida wamenyooka lakini roho zao zimepindana wana kibiongo nao wanahitaji kuhudumiwa roho zao, Kristo Yesu yupo tayari kuwahudumia watu wake leo, yeye hajabadilika yeye ni yeye yule jana leo na hata milele, kama moyo wako na roho yako imeinama huwezi hata kuangalia mbinguni leo kwa mamlaka niliyopewa kama mtumishi wa Mungu nakutangazia uzima katika jina la Yesu Kristo wa Nazareth aliye hai Bwana akutane na wewe katika kila eneo la maisha yako, bwana akuinue kutoka katika kupindana kwako.Bwana akuinue kutoka katika hali ya kuinama kwako kwa namna yoyote ile Katika jina la Yesu!

 

6.       Hakuna ugonjwa usiotibika kwa Yesu!, kama jinsi ambavyo tumejifunza kuhusu ugonjwa wa kibiongo au kupindana kwa mgongo ni ugonjwa mbaya haujulikani Dhahiri sababu zake na pia hauna tiba, Lakini kufumba na kufumbua Yesu alipomuombea mwanamke huyu Mwenye kibiongo alisimama pale pale, hii inatufundisha na kutufunulia kuwa hakuna uogonjwa wwowote ambao unaweza kusimama mbele za Yesu, uwe unaeleweka kitaalamu, au uwe haueleweki, uwe una tiba au hauna tiba, linapokuja swala la Yesu kujihusisha na tatizo lako hakuna linaloshindikana, Yote yawezekana kwa Mungu, Katika jina la Yesu Kristo tatizo lako leo kwa mamlaka niliyopewa kama Mtumishi wake nakutangaza kuwa umefunguliwa kutoka katika udhaifu wako kwa jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai Ameeeen!

 

Na Rev. Innocent Samuel Bin Hamza Bina Jumaa, Bin bin Athuman Sekivunga Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.